Mwaliko wa Moja kwa Moja
1. Kampeni ya kuwaalika watu kwenye kusanyiko itaanza lini?
1 Ikiwa unapanga kutayarisha mlo maalumu kwa ajili ya familia au marafiki, na utatumia gharama na jitihada nyingi, bila shaka utawakaribisha wageni wako kwa shauku. Vivyo hivyo, kazi nyingi zimefanywa ili kuandaa karamu ya kiroho kwenye kusanyiko lijalo la eneo. Majuma matatu kabla ya kusanyiko letu, tutakuwa na pendeleo la kuwaalika wengine wahudhurie. Ni nini kitakachotusaidia kuwaalika watu kwa shauku?
2. Ni nini kitakachotuchochea kushiriki katika kampeni kwa bidii?
2 Tukithamini jinsi tunavyofaidika kibinafsi kutokana na ufundishaji wenye kuburudisha ambao Yehova anatuandalia kwenye makusanyiko yetu, tutachochewa kushiriki katika kampeni hiyo kwa bidii. (Isa. 65:13, 14) Pia, tunapaswa kukumbuka kwamba kushiriki katika kampeni hiyo ya kila mwaka huleta matokeo mazuri. (Ona sanduku “Kampeni Huwa na Matokeo Mazuri.”) Baadhi ya wale ambao tutawakaribisha watahudhuria, ilhali wengine hawatahudhuria. Jitihada zetu wakati wa kampeni zitamletea Yehova sifa na kuonyesha jinsi alivyo mkarimu, haidhuru ni watu wangapi watahudhuria.—Zab. 145:3, 7; Ufu. 22:17.
3. Mialiko itasambazwaje?
3 Kila baraza la wazee linapaswa kuamua jinsi wahubiri katika makutaniko yao watakavyosambaza mialiko kwa watu wengi iwezekanavyo, kutia ndani iwapo wataacha mialiko hiyo katika nyumba ambazo wanawakosa watu au wataitoa wanapohubiri hadharani. Iwapo inafaa, mwisho-juma tunapaswa kutoa magazeti pamoja na mialiko. Mwishoni mwa kampeni hiyo tutafurahi sana kujua kwamba tulishiriki kwa bidii na shauku kuwaalika watu wengi iwezekanavyo ili wajiunge nasi katika karamu ya kiroho ambayo Yehova ametuandalia!