Mwenendo Unaomtukuza Mungu
1. Kwa nini watu wengi hutambua kwa urahisi Mashahidi wa Yehova wanapohudhuria makusanyiko ya wilaya?
1 Watu wengi hutambua kwa urahisi tunapohudhuria makusanyiko ya wilaya. Katika majiji mengi ambapo makusanyiko hufanywa, vyombo vingi vya habari hujulisha watu kuhusu kuwepo kwetu. Kwa kawaida hoteli na mikahawa hujaa wajumbe wanaohudhuria kusanyiko, na watu kwenye eneo la kusanyiko huwaona wageni hao ambao wamevaa beji za kusanyiko. Vifuatavyo ni baadhi ya vikumbusho vitakavyotusaidia kumtukuza Mungu kupitia mwenendo wetu mzuri tunapokuwa kwenye mji ambapo kusanyiko litafanywa.—1 Pet. 2:12.
2. Mavazi yetu yenye kiasi tunapokuwa kwenye mji wa kusanyiko yanawezaje kumletea Mungu utukufu?
2 Mavazi Yenye Kiasi: Kwa kawaida, tunapohudhuria kusanyiko watu huvutiwa na mavazi yetu yenye kiasi. Hata hivyo, nyakati nyingine mtindo wetu wa mavazi—tunapofika hotelini, tunapokula kwenye mikahawa iliyo katika eneo la kusanyiko, tunaponunua vitu madukani, na kadhalika—huenda ukaathiri sana maoni ya wale wanaotutazama. Ingawa si lazima tuvae nguo rasmi katika pindi hizo, mavazi yetu yanapaswa kuwa yenye kiasi, heshima, na yasiwe ya kizembe. Watu wanapaswa kuona tofauti kati yetu na wasioamini. (Rom. 12:2) Kwa kuongezea, tunapaswa kuvaa beji zetu za kusanyiko, kwa kuwa hilo litawafanya wengine wajue kwamba kuna kusanyiko, litatupa fursa za kutoa ushahidi, na litatuwezesha kuwatambua wenzetu.
3. Tunawezaje kuonyesha subira na adabu?
3 Subira na Adabu: Katika wakati ambapo watu wengi ulimwenguni ni wenye ubinafsi na hawana shukrani, watu wengine kama vile wafanyakazi hotelini na mikahawani watavutiwa sana tunapoonyesha subira na adabu! (2 Tim. 3:1-5) Tunapowahifadhia wengine viti au tunapopanga foleni ili kupokea machapisho yaliyotolewa kusanyikoni, tunapaswa kutafuta, si faida yetu wenyewe, bali ya wengine. (1 Kor. 10:23, 24) Baada ya kuhudhuria kusanyiko kwa mara ya kwanza, mwanamume mmoja mwenye kupendezwa alisema hivi: “Sikumbuki hotuba hata moja iliyotolewa siku hiyo, lakini siwezi kamwe kusahau mwenendo wa Mashahidi.”
4. Kwa nini tunapaswa kufikiria kujitolea kusanyikoni ikiwa hali zetu zinaturuhusu?
4 Wajitoleaji: Wakristo wa kweli wanajulikana kwa kujitolea kwa hiari. (Zab. 110:3) Je, unaweza kujitolea ili usaidie wakati wa kusanyiko? Katika kusanyiko moja, ndugu na dada 600 hivi walijitolea kufanya usafi kabla ya kusanyiko kuanza. Wafanyakazi walisema hivi kwa mshangao: “Hili ni jambo lenye kupendeza sana ambalo hatujawahi kuona! Ni vigumu kuwazia kuwa watu hawa wote ni wajitoleaji.” Tunatazamia kwa hamu makusanyiko ya wilaya ya mwaka wa 2013 na fursa tutakazopata si za kusikiliza na kujifunza tu bali pia za kumtukuza Mungu.
[Sanduku katika ukurasa wa 2]
Vikumbusho vya Kusanyiko la Wilaya—2013
◼ Saa za Programu: Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Kipindi cha muziki kitaanza saa 3:20 asubuhi siku zote tatu. Wakati huo, sote tunapaswa kuketi ili programu ianze kwa utaratibu na heshima. Wimbo na sala ya kumalizia itatolewa saa 10:50 jioni siku ya Ijumaa na Jumamosi, na saa 9:35 alasiri siku ya Jumapili.
◼ Maegesho: Katika sehemu zote za makusanyiko ambapo tumeruhusiwa kuegesha magari, sehemu za kuegesha zitapatikana bila malipo, lakini wale watakaofika kwanza ndio watakaopata mahali pa kuegesha kwanza. Kwa kawaida sehemu za kuegesha ni chache, hivyo ingefaa sana watu wasafiri pamoja kwa gari moja, badala ya kila mmoja kuja na gari lake.
◼ Viti: Unaweza kuhifadhi viti kwa ajili tu ya wale unaoishi nao, au unaosafiri nao katika gari moja au wanafunzi wako wa Biblia. Kuna viti vichache kwa ajili ya wale waliozeeka na walio dhaifu, kwa hiyo huenda wasiweze kuketi pamoja na watu wao wa familia. Tafadhali waachieni viti hivyo wale waliozeeka na walio dhaifu na wale wanaowatunza.—1 Kor. 13:5.
◼ Chakula cha Mchana: Tafadhali beba chakula chepesi cha mchana badala ya kuondoka mahali pa kusanyiko wakati wa mapumziko ili kwenda kutafuta chakula. Mfuko au sanduku dogo la kuhifadhia vyakula vikiwa baridi linaweza kuwekwa chini ya kiti. Mifuko au masanduku makubwa ya kuhifadhia vyakula vikiwa baridi na vyombo vya glasi haviruhusiwi kusanyikoni.
◼ Michango: Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mipango ya kusanyiko kwa kutoa michango ya hiari kusanyikoni kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Cheki au hundi zozote zinazotolewa zinapaswa kuandikwa zilipwe kwa IBSA au jina la shirika la kisheria linalotumiwa nchini kwenu.
◼ Aksidenti na Hali za Dharura: Hali ya dharura ya kimatibabu ikitokea kusanyikoni, tafadhali wasiliana na mkaribishaji aliye karibu, ambaye ataijulisha mara moja Idara ya Huduma ya Kwanza ili mtu anayestahili kutoa huduma ya kwanza achunguze hali hiyo na kutoa msaada unaohitajika. Ikihitajika, ndugu katika idara hii watatafuta gari la kubebea wagonjwa. Jambo hili litapunguza idadi ya simu zinazopokewa na kitengo cha huduma za dharura.
◼ Dawa: Ikiwa unatumia dawa ulizoagizwa na daktari, tafadhali hakikisha umebeba za kutosha, kwa kuwa hazitapatikana kusanyikoni. Mabomba ya sindano au sirinji na sindano zinazotumiwa na wagonjwa wa kisukari hazipaswi kutupwa ovyoovyo kwani ni takataka hatari, wala zisitupwe pamoja na takataka zilizo katika eneo la kusanyiko au hotelini.
◼ Viatu: Kila mwaka watu kadhaa hujeruhiwa kwa sababu ya viatu, hasa viatu vyenye kisigino kirefu. Itafaa sana kuvaa viatu vinavyofaa, vinavyokutoshea vizuri na vinavyokuwezesha kutembea vizuri kwenye sehemu zilizoinuka, ngazi, vifuniko vyenye matundu vinavyofunika mashimo ya maji machafu na sehemu nyinginezo.
◼ Marashi: Makusanyiko mengine hufanyiwa ndani ya majumba. Kwa hiyo, litakuwa jambo la fadhili kuepuka kutumia marashi yenye harufu kali ambayo huenda yakawaathiri wale walio na matatizo ya kupumua au matatizo mengine kama hayo.—1 Kor. 10:24.
◼ Fomu za Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43): Fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi inapaswa kutumiwa kutoa habari kuhusu mtu yeyote mwenye kupendezwa ambaye ulimpata ulipokuwa ukihubiri isivyo rasmi wakati wa kusanyiko. Fomu zilizojazwa zinaweza kuachwa kwenye Idara ya Vitabu au unaweza kumpa mwandishi wa kutaniko lenu utakaporudi nyumbani.
◼ Mikahawa: Liheshimu jina la Yehova kupitia mwenendo wako mzuri kwenye mikahawa. Mavazi yetu yaonyeshe kwamba sisi ni wahudumu Wakristo. Toa bakshishi ikiwa kufanya hivyo ni desturi katika eneo lenu.
◼ Hoteli:
(1) Tafadhali usihifadhi vyumba vingi kuliko utakavyohitaji, wala chumba kisikaliwe na watu wanaozidi idadi ya watu inayoruhusiwa.
(2) Usivunje mipango uliyofanya mapema ya kuwa na chumba isipokuwa hali ya dharura itokee, na unapaswa kuwajulisha wasimamizi wa hoteli mara moja unapogundua kwamba hutatumia chumba kilichokuwa kimehifadhiwa ili wengine wenye uhitaji huo waweze kukitumia. (Mt. 5:37) Ikiwa utahitaji kuvunja mipango ya kuwa na chumba, hakikisha umepata nambari inayoonyesha kwamba umevunja mipango hiyo. Ikiwa utavunja mipango ya kuwa na chumba chini ya saa 48 kabla ya kutumia chumba hicho, hutarudishiwa pesa ulizotoa ili kuhifadhi chumba hicho.
(3) Tafadhali zingatia kwamba ikiwa utatumia kadi ya mkopo kulipia gharama unapojiandikisha kwenye hoteli, ni zoea la kawaida kwa wasimamizi wa hoteli “kuweka kando” kiasi fulani cha pesa zako ambazo zitatoshea kulipia gharama zako zote za chumba, kutia ndani uharibifu au matukio yasiyotazamiwa ambayo huenda yakatukia unapokuwa hotelini. Baada ya kuondoka hotelini, hutaweza kutumia pesa hizo zilizowekwa kando mpaka siku kadhaa za kushughulikia akaunti yako zipite.
(4) Chukua kigari cha kubebea mizigo wakati unapokuwa tayari kukitumia, na ukirudishe mara moja ili wengine waweze kukitumia.
(5) Ikiwa ni desturi katika eneo lenu, wape bakshishi kila siku wafanyakazi wa hoteli wanapokubebea mizigo, na pia yule anayekusafishia chumba.
(6) Pika tu katika vyumba ambavyo upishi umeruhusiwa.
(7) Fuata vizuri utaratibu uliowekwa hotelini kuhusu kiamsha-kinywa, kahawa, au barafu ambazo huandaliwa kwa ajili ya wageni.
(8) Nyakati zote onyesha tunda la roho unaposhughulika na wafanyakazi hotelini. Wanawahudumia watu wengi, nao wanathamini tunapokuwa wenye fadhili, subira, na kiasi.
(9) Wazazi wanapaswa kuwasimamia watoto wao nyakati zote wanapokuwa kwenye hoteli, kutia ndani wanapopanda lifti, wanapotumia kidimbwi cha kuogelea, wanapokuwa sebuleni, katika chumba cha mazoezi, na kadhalika.
(10) Kukiwa na shida kuhusiana na chumba chako hotelini, julisha Idara ya Mahali pa Kulala ukiwa ungali kusanyikoni ili ndugu waweze kukusaidia.
◼ Kazi ya Kujitolea: Yeyote ambaye angependa kujitolea anapaswa kwenda kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kusanyikoni. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kutoa mchango mkubwa kwa kufanya kazi chini ya usimamizi wa mzazi, mtunzaji wao, au mtu mzima mwingine ambaye amekabidhiwa daraka hilo na mzazi au mtunzaji wao.