◼ Saa za Programu: Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Kipindi cha muziki kitaanza saa 3:20 asubuhi siku zote tatu. Wakati huo, sote tunapaswa kuketi ili programu ianze kwa utaratibu na heshima. Wimbo na sala ya kumalizia itatolewa saa 10:55 jioni siku ya Ijumaa na Jumamosi, na saa 9:50 alasiri siku ya Jumapili.
◼ Makusanyiko ya Kimataifa: Kuna maeneo yatakayokuwa na makusanyiko ya kimataifa. Kumbuka kwamba ofisi ya tawi imealika makutaniko hususa na wajumbe wa nchi nyingine baada ya kufanya mahesabu kwa uangalifu ili kulinganisha idadi ya wahudhuriaji na idadi ya viti katika mahali pa kusanyiko, nafasi za kuegesha magari, na vyumba vya hoteli vinavyoweza kupatikana. Msongamano unaweza kutokea ikiwa wahubiri watahudhuria kusanyiko la kimataifa ambalo hawakukaribishwa wahudhurie. Ikiwa hali zinakulazimu uende kwenye kusanyiko tofauti na lile ulilopangiwa, usiende kwenye kusanyiko la kimataifa.
◼ Maegesho ya Magari: Katika sehemu zote za makusanyiko ambapo tumeruhusiwa kuegesha magari, sehemu za kuegesha zitapatikana bila malipo, lakini wale watakaofika kwanza ndio watakaopata mahali pa kuegesha kwanza. Kwa kawaida sehemu za kuegesha ni chache, hivyo ingefaa sana watu wasafiri pamoja kwa gari moja, badala ya kila mmoja kutumia gari lake. Ni wale tu walioweka ishara ya walemavu ndio watakaoruhusiwa kuegesha magari katika eneo kwa ajili ya walemavu.
◼ Viti: Kila asubuhi milango inapofunguliwa, tafadhali usikimbilie sehemu yenye viti unayopendelea, kana kwamba unashindana na wahudhuriaji wengine. Roho ya kujidhabihu ambayo hutuchochea kuwatendea wengine mema hututambulisha sisi kuwa Wakristo wa kweli na hivyo kuwachochea wanaotutazama wamtukuze Mungu. (Yoh. 13:34, 35; 1 Kor. 13:4, 5; 1 Pet. 2:12) Unaweza kuhifadhi viti kwa ajili tu ya wale unaoishi nao, au unaosafiri nao katika gari moja au wanafunzi wako wa Biblia. Viti vimehifadhiwa kwa ajili ya wazee wa umri na walio dhaifu. Kwa sababu viti hivyo ni vichache, ni mtu mmoja au wawili tu wanaowatunza moja kwa moja, ndio wanaoruhusiwa kuketi pamoja nao.
◼ Chakula cha Mchana: Tafadhali beba chakula chepesi cha mchana badala ya kuondoka mahali pa kusanyiko wakati wa mapumziko ili kutafuta chakula. Unaweza kubeba mfuko au sanduku dogo la kuhifadhia vyakula linaloweza kuwekwa chini ya kiti. Masanduku makubwa ya kuhifadhia vyakula na vyombo vya glasi haviruhusiwi kusanyikoni.
◼ Michango: Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mipango ya kusanyiko kwa kutoa michango ya hiari kusanyikoni kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Cheki au hundi zozote zinazotolewa zinapaswa kuandikwa zilipwe kwa IBSA au jina la shirika la kisheria linalotumiwa nchini kwenu. Michango pia inaweza kutolewa kwa kutumia kadi ya benki.
◼ Dawa: Ikiwa unatumia dawa ulizoagizwa na daktari, tafadhali hakikisha umebeba za kutosha, kwa sababu hazitapatikana kusanyikoni. Mabomba ya sindano au sirinji na sindano zinazotumiwa na wagonjwa wa kisukari hazipaswi kutupwa ovyoovyo kwani ni takataka hatari, wala zisitupwe pamoja na takataka zilizo katika eneo la kusanyiko au hotelini.
◼ Kanuni za Usalama: Tafadhali uwe mwangalifu ili kuzuia uwezekano wa kupata majeraha ambayo huenda yakasababishwa na kuteleza au kujikwaa. Kila mwaka watu kadhaa hujeruhiwa kwa sababu ya viatu, hasa viatu vyenye visigino virefu. Ni vizuri kuvaa viatu vinavyofaa, vinavyokutosha vizuri na vinavyokuwezesha kutembea vizuri kwenye sehemu zilizoinuka, ngazi, vifuniko vyenye matundu vinavyofunika mashimo ya maji machafu, na sehemu nyinginezo.
◼ Marashi: Makusanyiko mengine hufanywa ndani ya majumba. Kwa hiyo, litakuwa jambo la fadhili kuepuka kutumia marashi yenye harufu kali ambayo huenda yakawaathiri wale walio na matatizo ya kupumua au matatizo mengine kama hayo.—1 Kor. 10:24.
◼ Fomu za Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43): Fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi inapaswa kutumiwa kutoa habari kuhusu mtu yeyote mwenye kupendezwa ambaye ulimpata ulipokuwa ukihubiri isivyo rasmi wakati wa kusanyiko. Fomu zilizojazwa zinaweza kuachwa kwenye Idara ya Vitabu au unaweza kumpa mwandishi wa kutaniko lenu utakaporudi nyumbani.
◼ Mikahawa: Liheshimu jina la Yehova kupitia mwenendo wako mzuri kwenye mikahawa. Mavazi yetu yaonyeshe kwamba sisi ni wahudumu Wakristo. Toa bakshishi ikiwa kufanya hivyo ni desturi katika eneo lenu.
◼ Hoteli:
Tafadhali usihifadhi vyumba vingi kuliko utakavyohitaji, wala chumba kisikaliwe na watu wanaozidi idadi ya watu inayoruhusiwa.
Usivunje mipango uliyofanya mapema ya kuwa na chumba isipokuwa hali ya dharura itokee, na unapaswa kuwajulisha wasimamizi wa hoteli mara moja unapogundua kwamba hutatumia chumba kilichokuwa kimehifadhiwa ili wengine wenye uhitaji huo waweze kukitumia. (Mt. 5:37) Ikiwa utahitaji kuvunja mipango ya kuwa na chumba, hakikisha umepata nambari inayoonyesha kwamba umevunja mipango hiyo. Ikiwa utavunja mipango ya kuwa na chumba chini ya saa 48 kabla ya kutumia chumba hicho, hutarudishiwa pesa ulizotoa ili kuhifadhi chumba hicho.
Tafadhali zingatia kwamba ikiwa utatumia kadi ya mkopo kulipia gharama unapojiandikisha kwenye hoteli, ni zoea la kawaida kwa wasimamizi wa hoteli “kuweka kando” kiasi fulani cha pesa zako ambazo zitatosha kulipia gharama zako zote za chumba, kutia ndani uharibifu au matukio yasiyotazamiwa ambayo huenda yakatukia unapokuwa hotelini. Baada ya kuondoka hotelini, hutaweza kutumia pesa hizo zilizowekwa kando mpaka siku kadhaa za kushughulikia akaunti yako zipite.
Chukua kigari cha kubebea mizigo wakati unapokuwa tayari kukitumia, na ukirudishe mara moja ili wengine waweze kukitumia.
Ikiwa ni desturi katika eneo lenu, wape bakshishi kila siku wafanyakazi wa hoteli wanapokubebea mizigo, na pia yule anayekusafishia chumba.
Pika tu katika vyumba ambavyo idhini ya kupika imetolewa.
Fuata vizuri utaratibu uliowekwa hotelini kuhusu kiamsha-kinywa, kahawa, au barafu ambazo huandaliwa kwa ajili ya wageni.
Nyakati zote onyesha tunda la roho unaposhughulika na wafanyakazi hotelini. Wanawahudumia watu wengi, kwa hiyo, wanathamini tunapokuwa wenye fadhili, subira, na kiasi.
Wazazi wanapaswa kuwasimamia watoto wao nyakati zote wanapokuwa kwenye hoteli, kutia ndani wanapopanda lifti, wanapotumia dimbwi la kuogelea, wanapokuwa sebuleni, katika chumba cha mazoezi, na kadhalika.
Bei ya chumba iliyoonyeshwa katika Orodha ya Mahali pa Kulala Palipopendekezwa ni ya siku moja bila kutia ndani kodi. Ukiambiwa bei ya juu kuliko bei iliyoorodheshwa, au utozwe gharama ya vitu ambavyo hukuviagiza wala kuvitumia, usikubali kulipa gharama hizo na uwajulishe ndugu katika Idara ya Mahali pa Kulala kusanyikoni upesi iwezekanavyo.
Kukiwa na shida kuhusiana na chumba chako hotelini, julisha Idara ya Mahali pa Kulala ukiwa ungali kusanyikoni ili ndugu waweze kukusaidia.
◼ Utumishi wa Kujitolea: Yeyote ambaye angependa kujitolea anapaswa kwenda kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea kusanyikoni. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kutoa mchango mkubwa kwa kufanya kazi chini ya usimamizi wa mzazi, mtunzaji wao, au mtu mzima mwingine ambaye amekabidhiwa daraka hilo na mzazi au mtunzaji wao.