Vikumbusho vya Kusanyiko la Eneo
Saa za Programu: Milango itafunguliwa saa 2:00 asubuhi. Kipindi cha muziki kitaanza saa 3:20 asubuhi siku zote tatu. Wakati huo, sote tunapaswa kuketi ili programu ianze kwa utaratibu na heshima. Programu itamalizika saa 11:00 jioni siku ya Ijumaa na Jumamosi, na saa 10:00 alasiri siku ya Jumapili.
‘Msifu Yehova kwa Nyimbo’: Watu wa Mungu wa kale walimsifu Yehova kwa nyimbo, na muziki ni sehemu muhimu sana ya ibada ya kweli leo. (Zab. 28:7) Kila kipindi cha programu ya kusanyiko letu la eneo huanza kwa kipindi cha muziki. Huu si muziki wa kuchezwa kwa sauti ya chini tu bali umetayarishwa ili kutusaidia tuwe tayari kujifunza kumhusu Yehova na kumwabudu. Hivyo basi, mwenyekiti anapotangaza kwamba kipindi cha muziki kitaanza baada ya muda mfupi, tunapaswa kuketi na kusikiliza kwa uthamini muziki huo, badala ya kuanza mazungumzo na wengine. Kufanya hivyo kunaonyesha kwamba tunathamini jitihada za kikundi cha wanamuziki cha Watchtower. Mara mbili kila mwaka, ndugu na dada hao husafiri kwa gharama zao wenyewe hadi Patterson, New York, na kutayarisha muziki mtamu ili tuufurahie. Baada ya kusikiliza kwa makini muziki huo, sote tunapaswa kumsifu Yehova pamoja kwa kuimba nyimbo zetu za Ufalme.
Maegesho: Katika makusanyiko yote ambapo kuna sehemu za kuegesha zilizo chini ya usimamizi wetu, magari yataegeshwa bila malipo, lakini wale watakaofika kwanza ndio watakaokuwa wa kwanza kupata mahali pa kuegesha. Mara nyingi sehemu za kuegesha ni chache, hivyo ingefaa sana watu wasafiri pamoja kwa gari moja, badala ya kila mmoja kutumia gari lake. Ni wale tu waliobandika ishara ya walemavu kwenye magari yao ndio watakaoruhusiwa kuegesha magari katika eneo lililotengwa kwa ajili ya walemavu.
Viti: Kila asubuhi milango inapofunguliwa, tafadhali usikimbilie kuhifadhi viti kana kwamba unashindana na wahudhuriaji wengine. Tafadhali wafikirie wengine, na uwe tayari kutanguliza mapendezi yao. Roho ya kujidhabihu hututambulisha sisi kuwa Wakristo wa kweli na huwachochea wanaotutazama wamtukuze Mungu. (Yoh. 13:34, 35; 1 Kor. 13:5; 1 Pet. 2:12) Unaweza kuhifadhi viti kwa ajili tu ya wale unaoishi nao, au unaosafiri nao katika gari moja au wale unaojifunza nao Biblia. Tafadhali usiweke chochote kwenye viti ambavyo hujahifadhi. Hilo litawasaidia wengine kujua kwamba hakuna mtu aliyehifadhiwa viti hivyo. Viti vimehifadhiwa kwa ajili ya wazee wa umri na walio dhaifu. Kwa kuwa viti hivyo ni vichache, ni mtu mmoja tu au wawili wanaomtunza mtu mzee au aliye dhaifu, wanaoruhusiwa kuketi naye.
Mavazi ya Heshima: Tunapohudhuria kusanyiko tunapaswa kuvalia kwa njia ya heshima na inayofaa, bila kuiga mitindo ya ulimwengu yenye kupita kiasi. (1 Tim. 2:9) Hata tunapowasili na kuondoka hotelini, wakati wa mapumziko, au kabla na baada ya programu, ni vizuri kuepuka kuvalia kizembe. Tukifanya hivyo tutafurahia kuvaa beji zetu za kusanyiko na hatutaogopa kutoa ushahidi tunapopata fursa. Tunapohudhuria kusanyiko, mwenendo wetu mzuri na mavazi yetu yatawavutia watu wanyoofu wajifunze Biblia, na vilevile tutamletea Yehova shangwe.—Sef. 3:17.
Kuwajali Wengine Tunapotumia Vifaa vya Kielektroniki: Tunaonyesha tabia nzuri wakati wa programu kwa kuhakikisha kwamba simu au vifaa vyetu vingine vya kielektroniki haviwakengeushi wengine. Iwapo tunatumia kamera, mashine ya kurekodia video, kompyuta ndogo, au vifaa vingine kama hivyo, tungependa kuwajali wengine kwa kutowasumbua au kuwazuia. Pia, tunaonyesha adabu kwa kutotuma ujumbe mfupi au barua pepe isivyo lazima wakati wa programu.
Chakula cha Mchana: Tafadhali beba chakula chepesi cha mchana badala ya kuondoka mahali pa kusanyiko wakati wa mapumziko ili kutafuta chakula. Unaweza kubeba mfuko au sanduku dogo la kuhifadhia vyakula linaloweza kuwekwa chini ya kiti. Masanduku makubwa ya kuhifadhia vyakula na vyombo vya glasi haviruhusiwi kusanyikoni.
Michango: Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mipango ya kusanyiko kwa kutoa michango ya hiari kusanyikoni kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Cheki au hundi zozote zinazotolewa zinapaswa kuandikwa zilipwe kwa shirika la kisheria linalotumiwa nchini kwenu. Pia, michango inaweza kutolewa kwa kutumia kadi ya benki.
Dawa: Ikiwa unatumia dawa ulizoagizwa na daktari, tafadhali hakikisha umebeba za kutosha, kwa sababu hazitapatikana kusanyikoni. Mabomba ya sindano au sirinji na sindano zinazotumiwa na wagonjwa wa kisukari hazipaswi kutupwa ovyoovyo kwani ni takataka hatari, wala zisitupwe pamoja na takataka zilizo katika eneo la kusanyiko au hotelini.
Tahadhari za Usalama: Tafadhali uwe mwangalifu ili kuzuia uwezekano wa kupata majeraha ambayo huenda yakasababishwa na kuteleza au kujikwaa. Kila mwaka watu kadhaa hujeruhiwa kwa sababu ya viatu, hasa viatu vyenye visigino virefu. Ni vizuri kuvaa viatu vinavyofaa, vinavyokutosha vizuri na vinavyokuwezesha kutembea vizuri kwenye sehemu zilizoinuka, ngazi, vifuniko vyenye matundu vinavyofunika mashimo ya maji machafu, na sehemu nyinginezo.
Wenye Matatizo ya Kusikia: Katika nchi nyingine, programu inaweza kusikilizwa kupitia mawimbi ya FM. Ili kusikiliza programu, utahitaji kubeba mashine ya kupokea mawimbi ya FM inayotumia betri ndogo, na vilevile kifaa cha kusikilizia sikioni.
Vigari vya Kuwabebea Watoto na Viti vya Bustanini: Vigari vya kuwabebea watoto na viti vya bustanini havipaswi kuletwa kusanyikoni. Hata hivyo, viti vya watoto vinavyoweza kufungwa kwenye kiti karibu na wazazi vinakubalika.
Marashi: Makusanyiko mengine hufanywa ndani ya majumba. Kwa hiyo, litakuwa jambo la fadhili kuepuka kutumia marashi yenye harufu kali ambayo huenda yakawaathiri wale walio na matatizo ya kupumua au matatizo mengine kama hayo.—1 Kor. 10:24.
Fomu za Tafadhali Fuatia Upendezi (S-43): Fomu ya Tafadhali Fuatia Upendezi inapaswa kutumiwa kutoa habari kuhusu mtu yeyote mwenye kupendezwa ambaye ulimpata ulipokuwa ukihubiri isivyo rasmi wakati wa kusanyiko. Fomu zilizojazwa zinaweza kuachwa kwenye Idara ya Vitabu au unaweza kumpa mwandishi wa kutaniko lenu utakaporudi nyumbani.
Mikahawa: Liheshimu jina la Yehova kupitia mwenendo wako mzuri kwenye mikahawa. Valia kwa njia inayowafaa wahudumu Wakristo. Toa bakshishi ikiwa kufanya hivyo ni desturi katika eneo lenu.
Hoteli:
Tafadhali usihifadhi vyumba vingi kuliko utakavyohitaji, wala chumba kisikaliwe na watu wanaozidi idadi inayoruhusiwa.
Usivunje mipango uliyofanya mapema ya kuwa na chumba isipokuwa hali ya dharura itokee, na unapaswa kuwajulisha wasimamizi wa hoteli mara moja unapogundua kwamba hutatumia chumba kilichokuwa kimehifadhiwa ili wengine wenye uhitaji huo waweze kukitumia. (Mt. 5:37) Ikiwa utahitaji kuvunja mipango ya kuwa na chumba, hakikisha umepata nambari inayoonyesha kwamba umevunja mipango hiyo. Ikiwa utavunja mipango ya kuwa na chumba chini ya saa 48 kabla ya kutumia chumba hicho, hutarudishiwa pesa ulizotoa ili kuhifadhi chumba hicho.
Tafadhali zingatia kwamba ikiwa utatumia kadi ya benki kulipia gharama unapojiandikisha kwenye hoteli, ni zoea la kawaida kwa wasimamizi wa hoteli kuweka kando kiasi fulani cha pesa zako ambazo zitatosha kulipia gharama zako zote za chumba, kutia ndani uharibifu au matukio yasiyotazamiwa ambayo huenda yakatukia unapokuwa hotelini. Baada ya kuondoka hotelini, hutaweza kutumia pesa hizo zilizowekwa kando mpaka siku kadhaa za kushughulikia akaunti yako zipite.
Chukua kigari cha kubebea mizigo wakati unapokuwa tayari kukitumia, na ukirudishe mara moja ili wengine waweze kukitumia.
Ikiwa ni desturi katika eneo lenu, wape bakshishi wafanyakazi wa hoteli wanapokubebea mizigo, na pia yule anayekusafishia chumba.
Pika tu katika vyumba ambavyo idhini ya kupika imetolewa.
Fuata vizuri utaratibu uliowekwa hotelini kuhusu kiamsha-kinywa, kahawa, au barafu ambazo huandaliwa kwa ajili ya wageni.
Nyakati zote, onyesha sifa za tunda la roho unaposhughulika na wafanyakazi hotelini. Wanawahudumia watu wengi, kwa hiyo, wanathamini tunapokuwa wenye fadhili, subira, na kiasi.
Wazazi wanapaswa kuwasimamia watoto wao nyakati zote wanapokuwa kwenye hoteli, kutia ndani wanapopanda lifti, wanapotumia dimbwi la kuogelea, wanapokuwa sebuleni, katika chumba cha mazoezi, na kadhalika.
Bei ya chumba iliyoonyeshwa katika Orodha ya Mahali pa Kulala Palipopendekezwa ni ya siku moja bila kutia ndani kodi. Ikiwa umetozwa gharama kubwa zaidi kuliko ile uliyopaswa kulipa, usikubali kulipa gharama hizo na uwajulishe mara moja ndugu katika Idara ya Mahali pa Kulala.
Ukipata tatizo kuhusiana na chumba chako hotelini, julisha Idara ya Mahali pa Kulala kabla ya kuondoka kusanyikoni ili ndugu waweze kukusaidia.
Utumishi wa Kujitolea: Yeyote ambaye angependa kujitolea kufanya kazi fulani anapaswa kwenda kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea. Watoto walio chini ya umri wa miaka 16 wanaweza kutimiza mengi kwa kufanya kazi chini ya usimamizi wa mzazi, mtunzaji wao, au mtu mzima mwingine ambaye amekabidhiwa daraka hilo na mzazi au mtunzaji wao.