Wachukueni Manabii Kuwa Kielelezo—Mika
1. Mika alijiuliza swali gani, lakini kwa nini kazi yake ya kuhubiri haikuwa ya bure?
1 ‘Mwisho wa mfumo huu mbovu wa mambo utakuja lini?’ Huenda nabii Mika alifikiria swali kama hilo alipokuwa akitangaza ujumbe wa hukumu ya Yehova dhidi ya ufalme wa Israeli na Yuda. Hata hivyo, imani yake ilithawabishwa. Wakati wa maisha ya Mika, mwaka wa 740 K.W.K., maneno ya Yehova kuhusu Samaria yalitimia. (Mika 1:6, 7) Baadaye, Yerusalemu liliharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. (Mika 3:12) Tunaweza kumwiga Mika katika njia gani tunaposubiri kutimizwa kwa hukumu za Yehova katika siku zetu?
2. Tunaonyeshaje subira tunapoitazamia siku ya Yehova? Na kwa nini?
2 Uwe na Subira: Mika aliandika hivi: “Mimi, nitaendelea kumtazamia Yehova. Nitaonyesha mtazamo wa kumngojea Mungu wa wokovu wangu.” (Mika 7:7) Bila shaka, Mika hakukaa tu kitako akisubiri mwisho uje. Aliendelea kutangaza kwa bidii unabii wa Yehova. Tunaposubiri siku ya Yehova, tunapaswa pia kujihusisha katika “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.” (2 Pet. 3:11, 12) Subira ya Yehova inawapa watu mmoja-mmoja nafasi ya kutubu. (2 Pet. 3:9) Kwa hiyo, tunatii ushauri wa Biblia tunapowaiga manabii kwa kuwa na sifa ya subira.—Yak. 5:10.
3. Kwa nini tunapaswa kumwomba Yehova atupatie roho yake takatifu?
3 Tegemea Nguvu za Yehova: Ingawa, mgawo wa Mika ulikuwa na changamoto nyingi, alimtegemea Yehova ampe nguvu za kuutimiza. (Mika 3:8) Yehova anajua kwamba tunahitaji nguvu zake na ndiyo sababu katika Neno Lake tunatiwa moyo tumtegemee. Kwa ukarimu Yehova huwapa nguvu waliochoka ili watimize majukumu yao ya kitheokrasi. (Zab. 84:5, 7; Isa. 40:28-31) Je, wewe mwenyewe umejionea jambo hilo katika utumishi wako mtakatifu? Je, una kawaida ya kumwomba Yehova ili akusaidie na roho yake takatifu yenye nguvu?—Luka 11:13.
4. Tunajifunza nini kutokana na maisha ya Mika?
4 Mika alitanguliza kufanya mapenzi ya Mungu maishani mwake. Aliazimia kubaki mwaminifu licha ya kuzungukwa na upotovu mwingi wa maadili. Vivyo hivyo, uaminifu wetu unajaribiwa kila siku. Hivyo basi, na tuimarishe azimio letu la ‘kutembea katika jina la Yehova Mungu wetu mpaka wakati usio na kipimo, naam, milele.’—Mika 4:5.