Vifaa Vyetu vya Kufundishia
1. Wahubiri Wakristo ni kama mafundi katika njia gani?
1 Mafundi hutumia vifaa mbalimbali wanapofanya kazi. Ingawa baadhi ya vifaa havitumiwi sana, kuna vifaa vingine vinavyotumiwa mara nyingi. Kwa kawaida mafundi wenye uzoefu huwa na vifaa vya msingi, na huvitumia vifaa hivyo kwa ustadi mkubwa sana. Biblia inawatia moyo Wakristo wote washiriki katika huduma kwa bidii na wawe ‘wafanyakazi wasio na lolote la kuonea aibu.’ (2 Tim. 2:15) Ni kifaa gani kilicho muhimu zaidi kati ya vyote tulivyo navyo? Ni Neno la Mungu, Biblia. Hicho ndicho kifaa kikuu tunachotumia ‘kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kwa hiyo, tunapaswa kujitahidi kuwa na ustadi wa ‘kulitumia sawasawa neno la kweli.’ Hata hivyo, pia kuna vifaa vingine tunavyotumia mara nyingi tunapofundisha watu kweli, ambavyo tunapaswa kujifunza kuvitumia kwa ustadi.—Met. 22:29.
2. Ni vifaa gani vya msingi tunavyotumia kufundisha?
2 Vifaa Vyetu vya Msingi: Mbali na Biblia, ni vifaa gani vingine tunavyopaswa kutumia? Kifaa cha msingi tunachotumia kufundisha kweli za Biblia ni kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Baada ya kumaliza kujifunza kitabu hicho, tunatumia kitabu“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu” ili kumsaidia mwanafunzi kutumia kanuni za Biblia katika maisha ya kila siku. Kwa hiyo, tunapaswa kuwa na ustadi wa kutumia machapisho hayo vizuri. Pia, kuna broshua ambazo tunapaswa kutumia. Broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu! ni mojawapo ya kifaa kikuu tunachotumia kuanzisha mafunzo ya Biblia. Ikiwa eneo tunalohubiri lina watu wenye uwezo mdogo wa kusoma au ikiwa kuna machapisho machache tu yanayopatikana katika lugha yao, tunaweza kutumia broshua Msikilize Mungu au Msikilize Mungu Uishi Milele. Broshua Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?, ndicho kifaa kikuu tunachotumia kuwaelekeza wanafunzi kwenye tengenezo. Video Kwa Nini Ujifunze Biblia?, Ni Nini Hutendeka Katika Jumba la Ufalme?, na Je, Mungu Ana Jina? zinatusaidia kufanya wanafunzi, na tunapaswa kujua jinsi ya kuzitumia kwa njia nzuri.
3. Makala za Huduma Yetu ya Ufalme zitakazofuata zitatusaidia kufanya nini?
3 Makala za Huduma Yetu ya Ufalme zitakazofuata zitatusaidia kuwa na ustadi wa kutumia machapisho yetu tunapofundisha. Kadiri tunavyojitahidi kutumia vifaa hivi kwa ustadi, ndivyo tutakavyotii shauri hili lililoongozwa na roho: “Jiangalie daima wewe mwenyewe na kufundisha kwako. Kaa katika mambo haya, kwa maana kwa kufanya hivyo utajiokoa wewe mwenyewe na wale wanaokusikiliza pia.”—1 Tim. 4:16.