Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w23 Novemba kur. 20-25
  • Je, Yehova Atajibu Sala Zangu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, Yehova Atajibu Sala Zangu?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • TUNAWEZA KUTARAJIA NINI KUTOKA KWA YEHOVA?
  • YEHOVA ANATARAJIA NINI KUTOKA KWETU?
  • KWA NINI HUENDA TUKAHITAJI KUREKEBISHA BAADHI YA MAOMBI YETU?
  • Jinsi Yehova Anavyojibu Sala Zetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Mkaribie Mungu Katika Sala
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Kwa Nini Mungu Hasikilizi Baadhi ya Sala?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2021
  • Ni Sala za Nani Hujibiwa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
w23 Novemba kur. 20-25

MAKALA YA 49

Je, Yehova Atajibu Sala Zangu?

“Mtaniita na kuja na kusali kwangu, nami nitawasikiliza.”—YER. 29:12.

WIMBO 41 Tafadhali Sikiliza Sala Yangu

MUHTASARIa

1-2. Kwa nini huenda tukahisi kwamba Yehova hajibu sala zetu?

“PATA furaha tele katika Yehova, naye atatosheleza tamaa za moyo wako.” (Zab. 37:4) Hiyo ni ahadi nzuri sana! Lakini je, tutarajie Yehova atupatie kila kitu tunachoomba papo hapo? Kwa nini ni muhimu kujiuliza swali hilo? Fikiria hali zifuatazo. Dada mseja anasali akiomba aalikwe kwenye Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Lakini miaka kadhaa inapita, na bado hajaalikwa. Ndugu kijana anamwomba Yehova amponye ugonjwa wake mbaya sana ili aweze kutumikia zaidi kutanikoni. Lakini bado anaendelea kuugua. Wazazi Wakristo wanasali kwamba mtoto wao abaki katika kweli. Lakini mtoto wao anaamua kuacha kumtumikia Yehova.

2 Labda wewe pia umemwomba Yehova kitu fulani lakini bado hujakipata. Hivyo, huenda ukahisi kwamba Yehova anajibu sala za wengine lakini hajibu sala zako. Au unaweza kufikiri kwamba umefanya jambo fulani baya. Dada anayeitwa Janiceb alihisi hivyo. Yeye na mume wake walisali kuhusu tamaa yao ya kutumikia Betheli. Anasema hivi: “Niliamini kwamba tungealikwa Betheli baada ya muda mfupi.” Lakini miaka mingi ikapita, na hawakualikwa Betheli. Janice anasema: “Nilihuzunika na sikuelewa. Nilijiuliza nimemkosea nini Yehova. Nilikuwa nimesali kihususa anipatie mwongozo. Kwa nini hakujibu sala yangu?”

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Wakati mwingine, huenda tukajiuliza ikiwa Yehova anasikiliza sala zetu. Baadhi ya wanaume waaminifu wa zamani walijiuliza swali hilo pia. (Ayu. 30:20; Zab. 22:2; Hab. 1:2) Ni nini kinachoweza kukusadikisha kwamba Yehova atajibu sala zako? (Zab. 65:2) Ili kupata jibu la swali hilo, kwanza tunahitaji kujibu maswali yafuatayo: (1) Tunaweza kutarajia nini kutoka kwa Yehova? (2) Yehova anatarajia nini kutoka kwetu? (3) Kwa nini huenda tukahitaji kurekebisha baadhi ya maombi yetu?

TUNAWEZA KUTARAJIA NINI KUTOKA KWA YEHOVA?

4. Kulingana na Yeremia 29:​12, Yehova anaahidi kufanya nini?

4 Yehova anaahidi kusikiliza sala zetu. (Soma Yeremia 29:12.) Mungu wetu anawapenda waabudu wake waaminifu, hivyo hatapuuza kamwe sala zao. (Zab. 10:17; 37:28) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba atatupatia kila kitu tunachomwomba. Huenda tukapata baadhi ya mambo tunayoomba katika ulimwengu mpya.

5. Yehova anazingatia nini anaposikiliza sala zetu? Eleza.

5 Yehova anazingatia jinsi maombi yetu yanavyohusiana na kusudi lake. (Isa. 55:​8, 9) Mojawapo ya mambo anayotaka ni kwamba dunia ijae watu wanaomtii yeye kwa shangwe akiwa Mtawala wao. Lakini Shetani alidai kwamba wanadamu wangekuwa na maisha mazuri zaidi ikiwa wangejitawala. (Mwa. 3:​1-5) Yehova aliwaruhusu wanadamu wajitawale ili kuthibitisha kwamba madai ya Ibilisi ni ya uwongo. Hata hivyo, serikali za wanadamu zimesababisha matatizo mengi ambayo tunakabili leo. (Mhu. 8:9) Tunajua kwamba Yehova hataondoa sasa matatizo haya yote. Ikiwa angeyaondoa, huenda baadhi ya watu wangefikiri kwamba utawala wa wanadamu umefanikiwa kuondoa matatizo ya wanadamu.

6. Kwa nini tunahitaji kuwa na uhakika kwamba sikuzote Yehova atatenda kwa upendo na haki?

6 Huenda Yehova akajibu maombi yanayofanana kwa njia tofauti. Kwa mfano, Mfalme Hezekia alipokuwa mgonjwa sana, alimsihi Yehova amponye. Yehova alijibu sala yake kwa kumponya. (2 Fal. 20:​1-6) Kwa upande mwingine, mtume Paulo alipomsihi Yehova amwondolee “mwiba katika mwili,” ambao huenda ulikuwa tatizo la afya, Yehova hakuondoa tatizo hilo. (2 Kor. 12:​7-9) Fikiria pia mfano wa mtume Yakobo na Petro. Mfalme Herode alitaka kuwaua wote wawili. Kutaniko lilisali kwa ajili ya Petro na inawezekana kwa ajili ya Yakobo pia. Hata hivyo, Yakobo aliuawa, lakini Petro aliokolewa kimuujiza. (Mdo. 12:​1-11) Huenda tukajiuliza, ‘Kwa nini Yehova alimwokoa Petro na hakumwokoa Yakobo?’ Biblia haielezi jambo hilo.c Jambo tunaloweza kuwa na uhakika nalo ni kwamba njia za Yehova ‘kamwe hazina ukosefu wa haki.’ (Kum. 32:4) Na tunajua kwamba wote wawili, Petro na Yakobo, walikuwa na kibali cha Yehova. (Ufu. 21:14) Wakati mwingine, huenda Yehova asijibu sala zetu kwa njia tunayotarajia. Lakini kwa kuwa tunaamini kwamba sikuzote jibu la Yehova litakuwa la upendo na la haki, hatutilii shaka njia anayochagua kujibu sala zetu.—Ayu. 33:13.

7. Tunajitahidi kuepuka nini, na kwa nini?

7 Tunajitahidi kuepuka kulinganisha hali zetu na za watu wengine. Kwa mfano, huenda tukamwomba Yehova jambo fulani hususa, lakini sala yetu haijibiwi. Baadaye, huenda tunagundua kwamba mtu mwingine amesali kuhusu jambo hilohilo, na inaonekana Yehova amejibu sala yake. Dada anayeitwa Anna alijionea jambo hilo. Alimwomba Yehova amsaidie Matthew, mume wake, apone ugonjwa wa kansa. Wakati huohuo dada wawili Wakristo wenye umri mkubwa walikuwa pia wakiugua kansa. Anna alisali kwa bidii kwa ajili ya Matthew na dada hao wawili. Dada hao walipona, lakini Matthew alikufa. Mwanzoni, Anna alikuwa akijiuliza ikiwa dada hao walipona kwa sababu Yehova aliingilia kati. Na ikiwa Yehova aliwasaidia, kwa nini hakujibu sala yake ya kumsaidia mume wake apate nafuu? Bila shaka, hatujui jinsi dada hao walivyopona. Tunachojua ni kwamba Yehova ana suluhisho la kudumu la mateso yetu yote, na anatamani kuwafufua rafiki zake waliokufa.—Ayu. 14:15.

8. (a) Kulingana na Isaya 43:​2, Yehova anatutegemezaje? (b) Sala inawezaje kutusaidia tunapokabili majaribu makali? (Tazama video Sala Hutusaidia Kukabiliana na Matatizo.)

8 Yehova atatutegemeza sikuzote. Akiwa Baba yetu mwenye upendo, Yehova hapendi kuona tukiteseka. (Isa. 63:9) Hata hivyo, hazuii majaribu yetu yote, ambayo yanaweza kulinganishwa na mito au miali ya moto. (Soma Isaya 43:2.) Lakini anaahidi atatusaidia ‘tunapopita katika’ majaribu hayo. Na hataruhusu majaribu yetu yatusababishie madhara ya kudumu. Pia, Yehova anatupatia roho yake takatifu yenye nguvu ili itusaidie kuvumilia. (Luka 11:13; Flp. 4:13) Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote atatupatia mambo tunayohitaji ili tuvumilie na kuendelea kuwa waaminifu kwake.d

YEHOVA ANATARAJIA NINI KUTOKA KWETU?

9. Kulingana na Yakobo 1:​6, 7, kwa nini tunapaswa kuamini kwamba Yehova atatusaidia?

9 Yehova anatarajia tumtumaini. (Ebr. 11:6) Wakati mwingine, tunaweza kulemewa na majaribu yetu. Huenda hata tukawa na shaka ikiwa Yehova atatusaidia. Lakini Biblia inatuhakikishia kwamba kwa nguvu za Mungu tunaweza “kuupanda ukuta.” (Zab. 18:29) Hivyo, badala ya kuwa na shaka, tunapaswa kusali tukiwa na imani kamili, tukiamini kwamba Yehova atajibu sala zetu.—Soma Yakobo 1:​6, 7.

10. Toa mfano wa jinsi tunavyoweza kutenda kulingana na sala zetu.

10 Yehova anatarajia tutende kulingana na sala zetu. Kwa mfano, ndugu anaweza kumwomba Yehova amsaidie kupata ruhusa kazini ili aweze kuhudhuria kusanyiko la eneo. Yehova anaweza kujibuje sala hiyo? Huenda akampa ndugu huyo ujasiri anaohitaji ili aweze kuzungumza na mwajiri wake. Lakini ndugu huyo bado anahitaji kutenda kulingana na sala yake kwa kwenda kuomba ruhusa. Huenda akahitaji kwenda kwa mwajiri tena na tena ili kuomba ruhusa. Hata anaweza kuomba kubadilishana zamu na mfanyakazi mwenzake. Na, ikilazimu, huenda akachukua likizo ya bila malipo.

11. Kwa nini tunapaswa kusali tena na tena kuhusu mahangaiko yetu?

11 Yehova anatarajia tusali tena na tena kuhusu mahangaiko yetu. (1 The. 5:17) Kulingana na maneno ya Yesu, baadhi ya maombi yetu hayatajibiwa papo hapo. (Luka 11:9) Hivyo usife moyo! Sali tena na tena na kwa bidii. (Luka 18:​1-7) Tunapoendelea kusali kuhusu jambo fulani, tunamwonyesha Yehova kwamba jambo hilo ni muhimu kwetu. Pia, tunaonyesha kwamba tuna imani katika uwezo wake wa kutusaidia.

KWA NINI HUENDA TUKAHITAJI KUREKEBISHA BAADHI YA MAOMBI YETU?

12. (a) Ni swali gani ambalo tunapaswa kujiuliza kuhusu maombi yetu, na kwa nini? (b) Tunawezaje kuhakikisha kwamba sala zetu zinaonyesha tunamheshimu Yehova? (Tazama sanduku “Je, Maombi Yangu Yanaonyesha Kwamba Ninamheshimu Yehova?”)

12 Ikiwa sala yetu haijibiwi, huenda tukahitaji kujiuliza maswali matatu yafuatayo. Swali la kwanza ni, ‘Je, ninasali kuhusu jambo linalofaa?’ Mara nyingi, huenda tukafikiri kwamba tunajua jambo ambalo linatufaa zaidi. Lakini inawezekana mambo tunayoomba hata yasitunufaishe. Ikiwa tunasali kuhusu tatizo fulani, huenda kukawa na suluhisho bora zaidi kuliko lile tunaloomba. Na labda baadhi ya mambo tunayoomba hayapatani na mapenzi ya Yehova. (1 Yoh. 5:14) Kwa mfano, fikiria mfano wa wazazi waliotajwa awali. Walikuwa wamemwomba Yehova amsaidie mtoto wao abaki katika kweli. Hilo linaonekana kuwa ombi linalofaa. Hata hivyo, Yehova hamlazimishi yeyote kati yetu amtumikie. Anataka kila mmoja wetu, kutia ndani watoto wetu, wachague kumwabudu yeye. (Kum. 10:​12, 13; 30:​19, 20) Hivyo, wazazi wanaweza kumwomba Yehova awasaidie kugusa moyo wa mtoto wao ili aweze kuchochewa kumpenda Yehova na kuwa rafiki Yake.—Met. 22:6; Efe. 6:4.

Je, Maombi Yangu Yanaonyesha Kwamba Ninamheshimu Yehova?

Yehova ni Baba mwenye upendo anayetaka kujibu maombi yetu. Lakini pia ni Muumba wetu na anastahili kuheshimiwa. (Ufu. 4:11) Unawezaje kuonyesha unamheshimu Baba yako wa mbinguni unaposali?

  • Hakikisha kwamba mambo unayoomba yanapatana na mapenzi ya Mungu na kwamba una nia inayofaa. (1 Yoh. 5:14) Sala zetu hazipaswi kuwa za ubinafsi, tukikazia tu mahitaji na tamaa zetu. Yakobo aliwaonya Wakristo wa karne ya kwanza kwamba sala zao zisingejibiwa ikiwa wangeomba wakiwa na “kusudi baya,” yaani, kwa kuchochewa na ubinafsi.—Yak. 4:3.

  • Usilazimishe Yehova akujibu kwa njia unayotaka. (Mt. 4:7) Amini kwamba Yehova anajua njia bora ya kujibu sala zako. Na wakati mwingine anaweza kujibu kwa njia tofauti na ile unayotarajia.—Efe. 3:20.

  • Kumbuka kumshukuru kwa sababu ya vitu anavyokupatia kila siku. Wazia furaha anayokuwa nayo unapomweleza jinsi unavyomshukuru kwa msaada wake.—Kol. 3:15; 1 The. 5:​17, 18.

13. Kulingana na Waebrania 4:16 na maelezo ya chini, Yehova atatusaidia wakati gani? Eleza.

13 Swali la pili ni, ‘Je, huu ni wakati wa Yehova kujibu ombi langu?’ Huenda tukahisi kwamba tunahitaji kupata jibu la sala zetu papo hapo. Lakini ukweli ni kwamba Yehova anajua wakati unaofaa wa kutusaidia. (Soma Waebrania 4:​16, maelezo ya chini.) Sala yetu isipojibiwa papo hapo, huenda tukahisi kwamba jibu la Yehova ni ‘Hapana.’ Lakini jibu la Yehova linaweza kuwa ‘Bado wakati haujafika.’ Kwa mfano, mfikirie yule ndugu kijana aliyeomba aponywe ugonjwa wake mbaya. Ikiwa Yehova angemponya kimuujiza, Shetani angeweza kudai kwamba ndugu huyo anaendelea kumtumikia Yehova kwa sababu tu ameponywa. (Ayu. 1:​9-11; 2:4) Isitoshe, tayari Yehova amepanga wakati wa kuponya magonjwa yote. (Isa. 33:24; Ufu. 21:​3, 4) Na mpaka wakati huo ufike, hatuwezi kutarajia kuponywa kimuujiza. Hivyo, ndugu huyo anaweza kumwomba Yehova ampatie nguvu na amani ya akili ili avumilie ugonjwa wake na kuendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu.—Zab. 29:11.

14. Unajifunza nini kutokana na jambo ambalo Janice alijionea?

14 Je, unamkumbuka Janice, aliyesali ili aalikwe Betheli? Baada ya miaka mitano kupita, ndipo alipotambua jinsi Yehova alivyokuwa amejibu sala yake. Anasema hivi: “Yehova alitumia wakati huo kunifundisha na kunifinyanga. Nilihitaji kumtumaini zaidi. Nilihitaji kuboresha mazoea yangu ya kujifunza kibinafsi. Na nilihitaji kuwa na shangwe ambayo haitegemei hali zangu.” Baadaye, Janice na mume wake walialikwa kutumikia katika kazi ya kuzungukia makutaniko. Anapotafakari mambo aliyopitia, Janice anasema: “Yehova alijibu sala zangu, ingawa katika njia ambayo sikutarajia. Ilinichukua muda kutambua kwamba jibu la Yehova lilikuwa zawadi nzuri, lakini ninamshukuru sana kwa upendo na fadhili alizonionyesha.”

Mkusanyo wa picha: 1. Dada wawili wakijaza fomu ya kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Kila dada anasali kabla ya kutuma fomu yake. 2. Dada mmoja akiwa katika Jumba la Ufalme, akiwaonyesha kwa shangwe rafiki zake, kutia ndani yule dada mwingine aliyetuma ombi, mwaliko wake wa kuhudhuria shule. 3. Dada ambaye hakualikwa katika shule akisali kwa Yehova na kisha kuandika barua. Baadaye anahubiri katika nchi ya kigeni na kufanya kazi katika mradi wa ujenzi.

Ikiwa unahisi kwamba Yehova hajajibu sala yako, fikiria kusali kuhusu mambo mengine (Tazama fungu la 15)f

15. Kwa nini nyakati nyingine tunapaswa kutosali kuhusu mambo hususa tu? (Tazama pia picha.)

15 Swali la tatu ni, ‘Je, ninapaswa kusali kuhusu jambo lingine?’ Ni vizuri kumwomba Yehova jambo hususa katika sala. Lakini huenda wakati mwingine tukahitaji kumwomba Yehova mambo yasiyo hususa ili tuweze kutambua mapenzi yake kwetu. Fikiria mfano wa yule dada mseja ambaye amekuwa akisali ili ahudhurie Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Anataka kuhudhuria shule ili aweze kutumikia kwenye eneo lenye uhitaji mkubwa. Hivyo, anapoendelea kusali ili ahudhurie shule, anaweza pia kumwomba Yehova amsaidie kutambua fursa nyingine za kupanua huduma yake. (Mdo. 16:​9, 10) Kisha anaweza kutenda kulingana na sala yake kwa kumwomba mwangalizi wa mzunguko amweleze kuhusu kutaniko la karibu lililo na uhitaji wa mapainia zaidi. Au anaweza kuiandikia barua ofisi ya tawi na kuuliza kuhusu eneo ambalo lina uhitaji wa wahubiri zaidi wa Ufalme.e

16. Tunaweza kuwa na uhakika gani?

16 Kama tulivyojifunza, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atajibu sala zetu kwa njia ya upendo na ya haki. (Zab. 4:3; Isa. 30:18) Wakati mwingine huenda tusipate jibu tunalotarajia. Lakini Yehova hawezi kamwe kupuuza sala zetu. Anatupenda sana. Na hatatuacha kamwe. (Zab. 9:10) Hivyo, endelea ‘kumtumaini nyakati zote,’ na kumwagia moyo wako katika sala.—Zab. 62:8.

INAPOHUSU SALA ZETU, . . .

  • tunaweza kutarajia nini kutoka kwa Yehova?

  • Yehova anatarajia nini kutoka kwetu?

  • kwa nini huenda tukahitaji kurekebisha baadhi ya maombi yetu?

WIMBO 43 Sala ya Shukrani

a Makala hii inaeleza kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote Yehova atajibu sala zetu kwa njia ya upendo na haki.

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.

c Tazama makala “Je, Unaamini Kwamba Njia ya Yehova ya Kufanya Mambo Ndiyo Bora?” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 2022, uku. 3-6.

d Ili kupata habari zaidi kuhusu jinsi Yehova anavyotusaidia kuvumilia majaribu makali, tazama video Sala Hutusaidia Kukabiliana na Matatizo kwenye jw.org.

e Ili kupata mwongozo wa jinsi ya kutumikia katika eneo la ofisi nyingine ya tawi, tazama kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, sura ya 10, uku. 6-9.

f MAELEZO YA PICHA: Dada wawili wakisali kabla ya kujaza fomu ya Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Baada ya muda, mmoja anaalikwa, lakini mwingine haalikwi. Badala ya kuvunjika moyo, dada ambaye hakualikwa anasali kwa Yehova amsaidie kutambua fursa nyingine za kupanua huduma yake. Kisha anaiandikia barua ofisi ya tawi, akiomba kujitolea katika eneo lenye uhitaji mkubwa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki