Je, Wajua?
Muziki ulikuwa na umuhimu gani katika Israeli la kale?
MUZIKI ulikuwa sehemu muhimu sana ya utamaduni wa Israeli la kale. Biblia inarejelea mara kadhaa watu wanaocheza ala za muziki na kuimba nyimbo. Isitoshe, karibu moja ya kumi ya Maandiko ni nyimbo. Kwa mfano, maneno ya kitabu cha Zaburi, Wimbo wa Sulemani, na Maombolezo yaliandikwa kwa kusudi la kuimbwa. Kitabu Music in Biblical Life kinasema kwamba Biblia “inaonyesha picha nzuri ya jamii ambayo muziki ulihusika katika utendaji mbalimbali maishani mwao, hata ambao haukuhusisha muziki.”
Muziki katika maisha ya kila siku. Waisraeli walipiga ala za muziki na kuimba ili kuonyesha hisia zao. (Isa. 30:29) Wanawake walipiga matari, waliimba kwa shangwe na kucheza dansi wakati wa kutawazwa kwa mfalme, kwenye sherehe mbalimbali, na waliposhinda vita. (Amu. 11:34; 1 Sam. 18:6, 7; 1 Fal. 1:39, 40) Pia, Waisraeli waliimba nyimbo za kuonyesha hisia zao za huzuni mtu fulani alipokufa. (2 Nya. 35:25) Kitabu McClintock and Strong’s Cyclopedia kinasema, bila shaka, “Waebrania walipenda sana muziki.”
Muziki katika makao ya kifalme. Wafalme wa Israeli walifurahia muziki. Mfalme Sauli alimwalika Daudi katika makao yake ya kifalme ili ampigie kinubi. (1 Sam. 16:18, 23) Baadaye, Daudi alipokuwa mfalme, alibuni vifaa vya muziki, alitunga nyimbo maridadi, na kupanga kikundi cha waimbaji kilichoimba nyimbo kwenye hekalu la Yehova. (2 Nya. 7:6; Amo. 6:5) Mfalme Sulemani alikuwa na waimbaji wa kiume na wa kike katika makao yake ya kifalme.—Mhu. 2:8.
Muziki katika ibada. Jambo muhimu zaidi ni kwamba Waisraeli walitumia muziki kumwabudu Yehova. Kwa kweli, wanamuziki 4,000 walipiga ala za muziki kwenye hekalu jijini Yerusalemu. (1 Nya. 23:5) Walicheza matoazi, vinanda, vinubi, na tarumbeta. (2 Nya. 5:12) Lakini si wapiga muziki stadi tu waliotumia muziki kumwabudu Yehova. Inaelekea Waisraeli wengi waliimba Nyimbo za Mipando walipokuwa safarini kuelekea jijini Yerusalemu kwenye sherehe za kila mwaka. (Zab. 120-134) Na kulingana na maandishi ya Kiyahudi, Waisraeli waliimba Zaburi za Halelia wakati wa mlo wa Pasaka.
Bado muziki ni muhimu kwa watu wa Mungu. (Yak. 5:13) Kuimba ni sehemu ya ibada yetu. (Efe. 5:19) Muziki unatuunganisha na Wakristo wenzetu. (Kol. 3:16) Na unatuimarisha tunapokabili hali ngumu. (Mdo. 16:25) Muziki ni njia nzuri sana ya kuonyesha imani na upendo wetu kwa Yehova.
a Wayahudi hurejelea Zaburi ya 113 hadi 118 kuwa Zaburi za Haleli, ambazo ziliimbwa ili kumsifu Yehova.