Kwa Nini Vita na Ukatili Vinaendelea?
Biblia inafunua mambo yanayosababisha vita na ukatili na sababu zinazofanya matukio hayo yenye kuhuzunisha yaendelee kutukia.
DHAMBI
Mungu aliwaumba wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, kwa mfano wake. (Mwanzo 1:27) Hilo linamaanisha kwamba wangeonyesha sifa za Mungu kama vile amani na upendo. (1 Wakorintho 14:33; 1 Yohana 4:8) Hata hivyo, Adamu na Hawa walikosa kumtii Mungu na kutenda dhambi. Na matokeo ni kwamba sisi sote tumerithi dhambi na kifo. (Waroma 5:12) Dhambi tuliyorithi hutuchochea kuwa na mawazo na matendo ya kikatili.—Mwanzo 6:5; Marko 7:21, 22.
SERIKALI ZA WANADAMU
Mungu hakutuumba ili tujitawale sisi wenyewe. Biblia inasema hivi: “Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Kwa sababu hiyo, serikali za wanadamu haziwezi kuondoa kabisa vita na ukatili.
SHETANI NA ROHO WAKE WAOVU
Biblia inafunua kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) “Yule mwovu” anaitwa Shetani Ibilisi, naye ni muuaji mwenye ukatili. (Yohana 8:44) Yeye pamoja na roho wake waovu, ndio wanaowachochea watu wapigane na wawe wakatili.—Ufunuo 12:9, 12.
Hatuwezi kuondoa mambo yanayosababisha vita na ukatili, lakini Mungu anaweza.