Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Aprili kur. 2-7
  • “Chagueni . . . Yule Mtakayemtumikia”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Chagueni . . . Yule Mtakayemtumikia”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KWA NINI YESU ALICHAGUA KUMTUMIKIA YEHOVA?
  • KWA NINI YEHOVA ANASTAHILI IBADA YETU?
  • KWA NINI TUNACHAGUA KUMTUMIKIA YEHOVA?
  • ENDELEA KUMTUMIKIA YEHOVA
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Maamuzi Yanayoonyesha Unamtegemea Yehova
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
  • Kumbuka Kwamba Yehova Ndiye “Mungu Aliye Hai”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Yehova “Huwaponya Waliovunjika Moyo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Aprili kur. 2-7

MAKALA YA 14

WIMBO 8 Yehova Ni Kimbilio Letu

“Chagueni . . . Yule Mtakayemtumikia”

“Mimi na familia yangu, tutamtumikia Yehova.”—YOS. 24:15.

JAMBO KUU

Kutukumbusha sababu zilizofanya tuchague kumtumikia Yehova.

1. Ili tuwe na furaha ya kweli ni lazima tufanye nini, na kwa nini? (Isaya 48:​17, 18)

BABA yetu wa mbinguni anatupenda sana, na anataka tufurahie maisha sasa na wakati ujao. (Mhu. 3:​12, 13) Alituumba tukiwa na vipawa vya pekee, hata hivyo hakutupatia uwezo wa kujitawala au kujiwekea viwango vyetu wenyewe vya mema na mabaya. (Mhu. 8:9; Yer. 10:23) Anajua kwamba ili tuwe na furaha ya kweli, ni lazima tumtumikie na kuishi kulingana na viwango vyake.—Soma Isaya 48:​17, 18.

2. Shetani angependa tuamini nini, na Yehova ameshughulikiaje dai hilo la uwongo?

2 Shetani angependa tuamini kwamba tunaweza kuwa na furaha bila kumtegemea Yehova, na kwamba wanadamu wanaweza kujitawala wenyewe kwa mafanikio. (Mwa. 3:​4, 5) Yehova alijibu dai hilo la uwongo kwa kuwaruhusu wanadamu waasi wajitawale wenyewe kwa kipindi fulani cha wakati. Kwa kweli, tunajionea wazi matokeo yenye kuhuzunisha ya utawala wa wanadamu. Kwa upande mwingine, Biblia ina mifano mingi ya wanaume na wanawake walioishi maisha yenye kuridhisha katika utumishi wa Yehova. Mfano bora zaidi ni Yesu Kristo. Kwanza, acheni tuchunguze sababu zilizomfanya achague kumtumikia Yehova. Kisha, tutachunguza kwa nini Baba yetu wa mbinguni anastahili ibada yetu. Mwishowe, tutachunguza baadhi ya sababu zinazofanya tuchague kumtumikia Yehova.

KWA NINI YESU ALICHAGUA KUMTUMIKIA YEHOVA?

3. Yesu aliahidiwa nini, naye alifanya uamuzi gani?

3 Yesu alipokuwa duniani alihitaji kuchagua atamtumikia nani. Muda mfupi baada ya Yesu kubatizwa, Shetani aliahidi kumpatia falme zote za ulimwengu ikiwa atamfanyia tendo moja tu la ibada. Yesu alijibu hivi: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa: ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’” (Mt. 4:​8-10) Kwa nini Yesu alifanya uamuzi huo? Fikiria sababu kadhaa.

4-5. Taja baadhi ya sababu zilizomfanya Yesu achague kumtumikia Yehova.

4 Sababu kuu iliyomfanya Yesu achague kumtumikia Yehova ni upendo. Yesu anampenda sana Baba yake na upendo huo hauwezi kuvunjwa. (Yoh. 14:31) Zaidi ya hilo, Yesu anamtumikia Yehova kwa sababu hilo ndilo jambo sahihi la kufanya. (Yoh. 8:​28, 29; Ufu. 4:11) Anajua kwamba Yehova ndiye Chanzo cha uhai, anategemeka, na ni mkarimu. (Zab. 33:4; 36:9; Yak. 1:17) Sikuzote Yehova amemweleza Yesu ukweli na alikuwa amempatia kila kitu alichokuwa nacho. (Yoh. 1:14) Kinyume na hilo, Shetani amesababisha kifo. Yeye ni mwongo anayechochewa na pupa na ubinafsi. (Yoh. 8:44) Akijua kweli hizo, Yesu hakufikiria kamwe kumwiga Shetani kwa kumwasi Yehova.—Flp. 2:​5-8.

5 Sababu nyingine iliyomfanya Yesu achague kumtumikia Yehova ni kwamba alitazamia kwa hamu kuona mambo ambayo utumishi wake mshikamanifu ungetimiza. (Ebr. 12:2) Alijua kwamba ikiwa angeendelea kuwa mwaminifu, angelitakasa jina la Baba yake na kutokeza njia ya kuondoa mateso yote yaliyosababishwa na Ibilisi.

KWA NINI YEHOVA ANASTAHILI IBADA YETU?

6-7. Kwa nini watu wengi leo hawamtumikii Yehova, lakini kwa nini anastahili ibada yetu?

6 Leo, watu wengi hawamtumikii Yehova kwa sababu bado hawajajua sifa zake zenye kuvutia na mambo yote mazuri ambayo amewafanyia. Ilikuwa hivyo pia kwa watu wa Athene ambao mtume Paulo aliwahubiria.—Mdo. 17:​19, 20, 30, 34.

7 Paulo aliwaeleza wasikilizaji wake kwamba Mungu wa kweli “huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” Akaongezea hivi: “Kupitia kwake tuko hai, tunatembea, na tunaishi.” Mungu ndiye Muumba ambaye “alifanyiza kila taifa la watu kutoka kwa mtu mmoja,” hivyo anastahili ibada yetu.—Mdo. 17:​25, 26, 28.

8. Yehova hawezi kamwe kufanya nini? Eleza.

8 Akiwa Muumba na Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, Yehova angeweza kuwalazimisha watu wamtumikie. Hata hivyo, Yehova hawezi kamwe kufanya hivyo. Badala yake, anatupatia uthibitisho kwamba yeye yuko na anampenda sana kila mmoja wetu. Anataka watu wengi kadiri iwezekanavyo wawe marafiki wake milele. (1 Tim. 2:​3, 4) Kwa sababu hiyo, Yehova ametuzoeza ili tuwafundishe wengine kuhusu makusudi yake na kuwaambia kuhusu mambo mazuri atakayowafanyia wanadamu. (Mt. 10:​11-13; 28:​19, 20) Yehova ametupanga katika makutaniko na kuwaweka waangalizi wenye upendo ili watutunze.—Mdo. 20:28.

9. Yehova ameonyeshaje upendo kwa watu wote?

9 Upendo wa Yehova wenye kustaajabisha unaonekana wazi kupitia jinsi anavyowatendea wale ambao hawataki kuamini kwamba yeye yuko. Fikiria mambo haya: Katika historia yote, mabilioni ya watu wamechagua kuishi kulingana na viwango vyao wenyewe vya mema na mabaya. Ingawa hivyo, kwa fadhili Yehova amewapatia mambo wanayohitaji ili waendeleze na kufurahia uhai. (Mt. 5:​44, 45; Mdo. 14:​16, 17) Amewapatia uwezo wa kuwa na marafiki na watu wa familia wanaowapenda, kuwa na watoto, na kufurahia kazi yao ngumu. (Zab. 127:3; Mhu. 2:24) Uthibitisho unaonyesha wazi kwamba Baba yetu wa mbinguni anawapenda wanadamu wote. (Kut. 34:6) Acheni sasa tujikumbushe baadhi ya sababu zinazotufanya tuchague kumtumikia Yehova na jinsi anavyotubariki.

KWA NINI TUNACHAGUA KUMTUMIKIA YEHOVA?

10. (a) Taja sababu kuu inayofanya tumtumikie Yehova. (Mathayo 22:37) (b) Umenufaikaje na subira ya Yehova? (Zaburi 103:​13, 14)

10 Kama Yesu, sababu kuu inayofanya tumtumikie Yehova ni kwamba tunampenda sana. (Soma Mathayo 22:37.) Tunamkaribia zaidi Yehova tunapojifunza kuhusu sifa zake. Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova anavyotuonyesha subira. Waisraeli walipokosa kumtii, aliwasihi hivi: “Geukeni, tafadhali, kutoka kwenye njia zenu mbaya.” (Yer. 18:11) Yehova anakumbuka kwamba sisi si wakamilifu na ni mavumbi. (Soma Zaburi 103:​13, 14.) Unapotafakari kuhusu subira ya Yehova na sifa zake nyingine zenye kuvutia, je, huchochewi kumtumikia milele?

11. Taja sababu nyingine zinazofanya tuchague kumtumikia Baba yetu wa mbinguni.

11 Sisi pia tunachochewa kumtumikia Yehova kwa sababu hilo ndilo jambo sahihi la kufanya. (Mt. 4:10) Zaidi ya hilo, tunajua mambo ambayo utumishi wetu mtakatifu utatimiza. Uaminifu wetu utasaidia kulitakasa jina la Yehova, kuthibitisha kwamba Ibilisi ni mwongo, na kuufurahisha moyo wa Baba yetu. Na ikiwa tutachagua kumtumikia Yehova leo, tuna tumaini la kumtumikia milele!—Yoh. 17:3.

12-13. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Jane na Pam?

12 Tukiwa bado vijana, tunaweza kusitawisha upendo wenye kina kwa Yehova, upendo ambao utaendelea kuimarika kadiri tunavyozeeka. Fikiria mfano wa Jane na Pam,a dada wawili wa kimwili. Walipoanza kujifunza Biblia, Jane alikuwa na umri wa miaka 11 na Pam alikuwa na umri wa miaka 10. Ingawa wazazi wao hawakutaka kujifunza Biblia, walimruhusu Jane na Pam kushirikiana na Mashahidi maadamu mwisho juma wangehudhuria ibada kanisani pamoja na familia yao. Jane anasema hivi: “Mambo ambayo Mashahidi walinifundisha kutoka katika Biblia, yalinisaidia kukataa kushinikizwa na vijana wenzangu kutumia dawa za kulevya na kufanya uasherati.”

13 Walipofikia miaka ya mwishoni ya utineja, wote wawili wakawa wahubiri ambao bado hawajabatizwa. Baadaye, walianza utumishi wa upainia huku wakiwatunza wazazi wao waliozeeka. Anapokumbuka mambo waliyopitia, Jane anasema hivi: “Nimejionea kwamba Yehova anawatunza rafiki zake kwa uaminifu, na kama 2 Timotheo 2:19 inavyosema, ‘Yehova anawajua walio wake.’” Hapana shaka kwamba Yehova anawatunza wale wanaochagua kumpenda na kumtumikia!

14. Maneno na matendo yetu yanasaidiaje kuliondolea suto jina la Yehova? (Tazama pia picha.)

14 Tunataka kusaidia kuliondolea suto jina la Yehova. Fikiria hali hii: Una rafiki wa karibu ambaye ni mwenye fadhili, mkarimu, na anayesamehe. Siku moja, unasikia mtu akidai kwamba rafiki yako ni mkatili na si mnyoofu. Utatendaje? Utamtetea. Vivyo hivyo, Shetani na wale walio chini ya uvutano wake wanapojaribu kuharibu sifa nzuri ya Yehova kwa kueneza uwongo kumhusu, tunajibu kwa kusema ukweli kumhusu Yehova na kutetea jina Lake kwa bidii. (Zab. 34:1; Isa. 43:10) Tunaonyesha kwamba tumechagua kumtumikia Yehova kwa nafsi yetu yote, kupitia maneno na matendo yetu.

Mkusanyo wa picha: 1. Mwanamke  akikitazama kikundi cha waasi-imani kinachoandamana nje ya eneo la kusanyiko. 2. Baadaye, mwanamke huyo anazungumza na wenzi wa ndoa walio karibu na kigari cha machapisho.

Je, utasaidia kulitetea jina la Yehova? (Tazama fungu la 14)b


15. Mtume Paulo alinufaikaje kwa kubadili malengo yake? (Wafilipi 3:​7, 8)

15 Tunabadili kwa hiari malengo yetu maishani ili tuweze kumtumikia Yehova kwa njia anayoikubali au kikamili zaidi. Kwa mfano, mtume Paulo alichagua kutokuwa mashuhuri katika jamii ili amfuate Kristo na kumtumikia Yehova. (Gal. 1:14) Matokeo ni kwamba aliishi maisha yenye kuthawabisha na alipata fursa ya kutawala pamoja na Kristo mbinguni. Hakujutia kamwe uamuzi wake wa kumtumikia Yehova, na sisi pia hatutajutia.—Soma Wafilipi 3:​7, 8.

16. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Julia? (Tazama pia picha.)

16 Ikiwa tutatanguliza maishani utumishi wetu kwa Yehova, tutakuwa na maisha yenye kuthawabisha sasa na wakati ujao. Fikiria mfano wa dada anayeitwa Julia. Kabla ya kujifunza kweli, Julia alikuwa mwimbaji katika kwaya ya kanisa tangu alipokuwa na msichana mdogo. Mwimbaji bora wa muziki aina ya opera alitambua kipaji chake na kumzoeza. Baada ya muda mfupi, Julia alipata umaarufu na aliimba katika kumbi maarufu za muziki. Alipokuwa akisoma katika shule maarufu ya muziki, mwanafunzi mwenzake alianza kuzungumza naye kumhusu Mungu na akamwambia kwamba Mungu anaitwa Yehova. Punde si punde, Julia akaanza kujifunza Biblia mara mbili kila juma. Hatimaye, aliamua kukazia fikira kumtumikia Yehova maishani, badala ya kuwa mwimbaji wa opera. Uamuzi huo haukuwa rahisi. Anasema hivi: “Watu wengi waliniambia kwamba ninapoteza kipaji changu, lakini nilitaka kutumia maisha yangu kikamili kumtumikia Yehova.” Leo, anahisije kuhusu uamuzi huo aliofanya zaidi ya miaka 30 iliyopita? Anasema hivi: “Nina amani ya akili na nina uhakika kwamba wakati ujao, Yehova atatosheleza tamaa zote za moyo wangu.”—Zab. 145:16.

Mkusanyo wa picha: Igizo linaloonyesha uamuzi aliofanya Julia. 1. Akiimba jukwaani mbele ya umati. 2. Akiimba pamoja na mume wake kwenye mkutano wa kutaniko.

Ikiwa tutatanguliza maishani utumishi wetu kwa Yehova, tutakuwa na maisha yenye kuthawabisha zaidi (Tazama fungu la 16)c


ENDELEA KUMTUMIKIA YEHOVA

17. Kujua kwamba tunaishi mwishoni kabisa mwa mfumo huu kumekuwa na matokeo gani kwa wale waliochagua kumtumikia Mungu na kwa wale ambao hawajafanya hivyo?

17 Tunaishi mwishoni kabisa mwa mfumo huu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa maana bado ‘muda kidogo sana,’ na ‘yule anayekuja atafika naye hatakawia.’” (Ebr. 10:37) Hilo linamaanisha nini? Jambo moja ni kwamba muda uliobaki kwa wale ambao hawajachagua kumtumikia Yehova umepungua, hivyo wanahitaji kuchukua hatua haraka iwezekanavyo. (1 Kor. 7:29) Na ikiwa tayari tumechagua kumtumikia Mungu tunajua kwamba ingawa tutahitaji kuvumilia majaribu, tutafanya hivyo kwa “muda kidogo sana.”

18. Yesu na Yehova wanataka tufanye nini?

18 Yesu aliwatia moyo wanafunzi wake, si tu waanze kumfuata, bali pia waendelee kumfuata. (Mt. 16:24) Hivyo, ikiwa tumekuwa tukimtumikia Yehova kwa miaka mingi, acheni tuazimie kuendelea kumtumikia. Tunahitaji kujitahidi sana ili tuishi kulingana na uamuzi wetu wa kumtumikia Yehova. Huenda isiwe rahisi, lakini tutakuwa na furaha na tutapata baraka nyingi hata sasa!—Zab. 35:27.

19. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Gene?

19 Baadhi ya watu wanahisi kwamba kumtumikia Yehova kunahusisha kujidhabihu kwa njia kubwa. Ikiwa wewe ni kijana, je, unahisi kwamba utakosa jambo fulani ukichagua kumtumikia Yehova? Ndugu mmoja kijana anayeitwa Gene, anasema hivi: “Nilihisi kwamba kuwa Shahidi wa Yehova kungeninyima uhuru. Ilionekana kwamba watoto wengi wa rika langu walifurahia mambo kama vile tafrija, kuwa na marafiki wa kimapenzi, au kucheza michezo ya video yenye ukatili, huku mimi nilipaswa kutumia wakati wangu katika mikutano na huduma.” Mtazamo huo ulimwathirije Gene? Anasema hivi: “Nilianza kuishi maisha maradufu, na kwa muda fulani niliyafurahia. Lakini sikupata furaha ya kudumu. Nilianza kufikiria kuhusu kweli za Biblia ambazo nilikuwa nimechagua kuzipuuza, na nikaamua kumtumikia Yehova kwa moyo wote. Tangu wakati huo, ninaona kwamba Yehova amejibu kila moja ya sala zangu.”

20. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Mtunga zaburi alimwimbia hivi Yehova: “Mwenye furaha ni yule unayemchagua na kumleta karibu ili akae katika nyua zako.” (Zab. 65:4) Acheni tuendelee kuwa na azimio kama la Yoshua aliposema hivi: “Mimi na nyumba yangu, tutamtumikia Yehova.”—Yos. 24:15.

UNGEJIBUJE?

  • Kwa nini Yesu alichagua kumtumikia Yehova?

  • Kwa nini Yehova anastahili ibada yetu?

  • Kwa nini umechagua kumtumikia Yehova?

WIMBO 28 Kuwa Rafiki ya Yehova

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

b MAELEZO YA PICHA: Baada ya mwanamke mmoja kuwasikia wapinzani wetu nje ya eneo la kusanyiko, anaenda katika kigari cha machapisho na kusikia maneno ya kweli.

c MAELEZO YA PICHA: Igizo linaloonyesha uamuzi aliofanya Julia ili akazie fikira kumtumikia Yehova maishani.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki