MAKALA YA 23
WIMBO 2 Jina Lako Ni Yehova
Jina la Yehova Linapaswa Kuwa na Umuhimu Gani Kwetu?
“‘Ninyi ni mashahidi wangu,’ asema Yehova.”—ISA. 43:10.
JAMBO KUU
Kuonyesha jukumu letu katika kulitakasa na kulitetea jina la Yehova.
1-2. Tunajuaje kwamba jina la Yehova ni la muhimu kwa Yesu?
JINA la Yehova ni la muhimu sana kwa Yesu. Yesu ndiye hasa anayelitetea jina la Baba yake. Kama tulivyoona katika makala iliyopita, Yesu alikuwa tayari kufa kwa ajili ya jina la Yehova na mambo yote ambayo jina hilo linawakilisha. (Marko 14:36; Ebr. 10:7-9) Na baada ya Utawala wake wa Miaka Elfu Moja, kwa hiari Yesu atakabidhi mamlaka yake yote ili kulitakasa jina la Yehova. (1 Kor. 15:26-28) Upendo wa Yesu kuelekea jina la Mungu unafunua pia mengi kuhusu uhusiano wake na Baba yake. Unathibitisha bila shaka yoyote kwamba Yesu anampenda Yule anayewakilishwa na jina hilo.
2 Yesu alikuja duniani katika jina la Baba yake. (Yoh. 5:43; 12:13) Alilijulisha jina la Baba yake kwa wafuasi wake. (Yoh. 17:6, 26) Alifundisha katika jina la Yehova na kufanya miujiza katika jina hilo. (Yoh. 10:25) Isitoshe, Yesu alimwomba Yehova awalinde wanafunzi wake “kwa sababu ya jina [lake].” (Yoh. 17:11) Basi, ikiwa Yesu alihisi hivyo kuhusu jina la Yehova, mtu anawezaje kudai kwamba ni mfuasi wa Kristo na halijui jina la Baba yake au kulitumia?
3. Tutachunguza nini katika makala hii?
3 Tukiwa Wakristo tunaojitahidi kufuata hatua za Yesu, tunalipenda na kuliheshimu jina la Baba yake. (1 Pet. 2:21) Katika makala hii, tutaona jinsi jina la Yehova linavyowatambulisha wale wanaotangaza “habari njema ya Ufalme.” (Mt. 24:14) Pia, tutachunguza jinsi jina la Yehova linavyopaswa kuwa la muhimu kwa kila mmoja wetu.
“WATU KWA AJILI YA JINA LAKE”
4. (a) Yesu aliwaagiza nini wanafunzi wake kabla ya kurudi mbinguni? (b) Agizo hilo linatokeza swali gani?
4 Kabla tu ya kurudi mbinguni, Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Hivyo, habari njema ingehubiriwa nje ya mipaka ya Israeli. Hatimaye, watu wa mataifa yote wangepata nafasi ya kuwa wafuasi wa Yesu. (Mt. 28:19, 20) Lakini Yesu alisema hivi: “Mtakuwa mashahidi wangu.” Je, wanafunzi hao wapya wangehitaji kujua jina la Yehova, au wangekuwa tu mashahidi wa Yesu? Matukio yanayotajwa katika kitabu cha Matendo sura ya 15 yanatusaidia kujibu swali hilo.
5. Mitume na wanaume wazee katika jiji la Yerusalemu walionyeshaje kwamba watu wote walihitaji kulijua jina la Yehova? (Tazama pia picha.)
5 Mwaka wa 49 W.K., mitume na wanaume wazee walikutana Yerusalemu ili kuzungumzia mambo ambayo Watu wa Mataifa wasiotahiriwa walihitaji kufanya ili wastahili kuwa Wakristo. Mwishoni mwa mazungumzo hayo, Yakobo, ndugu nusu ya Yesu, alisema hivi: “[Petro] amesimulia kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake.” Yakobo alikuwa akirejelea jina la nani? Akimnukuu nabii Amosi, aliongezea hivi: “Ili watu wanaobaki wamtafute Yehova kwa bidii, pamoja na watu wa mataifa yote, watu wanaoitwa kwa jina langu, asema Yehova.” (Mdo. 15:14-18) Wanafunzi hao wapya wangejifunza kumhusu Yehova, na pia ‘wangeitwa kwa jina lake.’ Hilo lilimaanisha kwamba wangelitangaza jina la Mungu na kutambulishwa kwa jina hilo.
Katika mkutano wa baraza linaloongoza la karne ya kwanza, wanaume hao waaminifu walitambua wazi kwamba Wakristo walipaswa kuwa watu kwa ajili ya jina la Mungu (Tazama fungu la 5)
6-7. (a) Kwa nini Yesu alikuja duniani? (b) Ni sababu gani nyingine muhimu iliyohusika?
6 Jina la Yesu linamaanisha “Yehova ni Wokovu,” naye alithibitika kuwa njia ya Yehova ya kuleta wokovu kwa wale wanaoonyesha imani. Yesu alikuja duniani ili kutoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu. (Mt. 20:28) Kwa kulipa fidia, alifanya iwezekane kwa wanadamu kuokolewa na kupata uzima wa milele.—Yoh. 3:16.
7 Lakini kwa nini wanadamu walihitaji kuokolewa? Kwa sababu ya mambo ambayo yalitokea katika bustani ya Edeni. Kama ilivyotajwa katika makala iliyopita, wazazi wa kwanza wa wanadamu, Adamu na Hawa, walimwasi Yehova na hivyo wakapoteza nafasi ya kuishi milele. (Mwa. 3:6, 24) Hata hivyo, jambo lingine la muhimu hata zaidi ya kuokolewa kwa wanadamu watenda dhambi lilihusika. Jina la Yehova lilichongewa. (Mwa. 3:4, 5) Hivyo, wokovu wa wazao wa Adamu na Hawa ulihusiana na suala kuu zaidi—kutakaswa kwa jina la Yehova. Kwa sababu Yesu alimwakilisha Yehova na alitangaza jina Lake, alikuwa na jukumu muhimu katika kulitakasa jina la Yehova.
Mtu anawezaje kudai kwamba ni mfuasi wa Kristo na halijui jina la Baba yake au kulitumia?
8. Wale wote ambao wangeonyesha imani katika Yesu wangehitaji kutambua nini?
8 Wale wote ambao wangeonyesha imani katika Yesu, yaani, Wayahudi na Watu wa Mataifa, wangehitaji kutambua Chanzo cha wokovu wao, Baba ya Yesu, Yehova Mungu. (Yoh. 17:3) Kwa kuongezea, kama Yesu, wangetambuliwa kwa jina la Yehova. Pia, wangehitaji kutambua umuhimu wa kutakaswa kwa jina hilo. Wokovu wao ulitegemea jambo hilo. (Mdo. 2:21, 22) Hivyo, wafuasi wote waaminifu wa Yesu walihitaji kujifunza kumhusu Yehova na pia Yesu. Ndiyo maana Yesu alimalizia sala yake inayopatikana katika Yohana sura ya 17 kwa maneno haya: “Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha, ili upendo ulionipenda uwe ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”—Yoh. 17:26.
“NINYI NI MASHAHIDI WANGU”
9. Tunawezaje kuonyesha kwamba jina la Yehova ni muhimu kwetu?
9 Hivyo, wafuasi wote wa kweli wa Yesu, wanahitaji kupendezwa na kutakaswa kwa jina la Yehova. (Mt. 6:9, 10) Ni lazima walione jina la Yehova kuwa la muhimu zaidi kuliko jina lingine lolote. Hilo linahusisha matendo yao. Lakini tunawezaje kuwa na sehemu katika kulitakasa jina la Yehova, au kuthibitisha kwamba mambo aliyosema Shetani kumhusu Yehova ni uwongo?
10. Ni kesi gani katika mahakama ya mfano inayotajwa kwenye sura ya 42 hadi 44 ya kitabu cha Isaya? (Isaya 43:9; 44:7-9) (Tazama pia picha.)
10 Umuhimu wa sehemu yetu katika kulitakasa jina la Yehova unatajwa kwenye kitabu cha Isaya sura ya 42 hadi 44. Sura hizo zinazungumzia kesi katika mahakama ya mfano ambayo inajadili nani ni mungu wa kweli. Yehova anawaambia wote wanaodai kuwa miungu wathibitishe ikiwa kweli wao ni miungu. Anawaita pia mashahidi waje kuthibitisha madai ya miungu hiyo. Lakini hakuna aliyeweza kufanya hivyo!—Soma Isaya 43:9; 44:7-9.
Tunahusika kwa njia mbalimbali katika kesi kwenye mahakama ya mfano (Tazama fungu la 10-11)
11. Kulingana na Isaya 43:10-12 Yehova anawatangazia nini watu wake?
11 Soma Isaya 43:10-12. Yehova anasema hivi kuhusu watu wake: “Ninyi ni mashahidi wangu, . . . nami ni Mungu.” Yehova anawaomba wajibu swali hili: “Je, kuna Mungu zaidi yangu?” (Isa. 44:8) Hivyo, tuna pendeleo la kujibu swali hilo. Kupitia maneno na matendo yetu, tunatoa ushahidi kwamba Yehova ndiye Mungu wa pekee wa kweli. Jina lake liko juu zaidi ya majina mengine yote. Kupitia njia yetu ya maisha tunathibitisha kwamba tunampenda Yehova kikweli na kwamba sisi ni washikamanifu kwake—hata Shetani atuletee jaribu gani. Kwa njia hiyo, tunakuwa na fursa ya kusaidia katika kulitakasa jina Lake.
12. Unabii unaopatikana kwenye Isaya 40:3, 5 ulitimizwaje?
12 Tunapounga mkono jina la Yehova, au sifa yake, tunamwiga Yesu Kristo. Isaya pia alitabiri kwamba mtangulizi ‘angefungua [au, ‘angetayarisha,’ maelezo ya chini] njia ya Yehova.’ (Isa. 40:3) Jambo hilo lilitimizwaje? Yohana Mbatizaji alitayarisha njia kwa ajili ya Yesu, aliyekuja katika jina la Yehova na kuzungumza katika jina la Yehova. (Mt. 3:3; Marko 1:2-4; Luka 3:3-6) Unabii huo pia ulisema: “Utukufu wa Yehova utafunuliwa.” (Isa. 40:5) Jinsi gani? Yesu alipokuja duniani, alimwakilisha Yehova kikamilifu hivi kwamba ilikuwa ni kama Yehova mwenyewe alikuja duniani.—Yoh. 12:45.
13. Tunawezaje kumwiga Yesu?
13 Kama Yesu, sisi pia ni mashahidi wa Yehova. Tunaitwa kwa jina la Yehova na tunamwambia kila mtu tunayekutana naye kuhusu matendo yake yenye kustaajabisha. Hata hivyo, ili tufanye hivyo kwa njia yenye matokeo, ni lazima pia tuwajulishe watu jukumu muhimu la Yesu katika kulitakasa jina la Yehova. (Mdo. 1:8) Yesu ndiye Shahidi mkuu wa Yehova, na tunafuata mfano wake. (Ufu. 1:5) Ni katika njia gani nyingine tunaonyesha kwamba jina la Yehova ni la muhimu kwa kila mmoja wetu?
NJIA NYINGINE TUNAZOONYESHA KWAMBA JINA LA YEHOVA NI MUHIMU KWETU
14. Kulingana na Zaburi 105:3, tunahisije kuhusu jina la Yehova?
14 Tunajivunia jina la Yehova. (Soma Zaburi 105:3.) Yehova anafurahi sana tunapojigamba au tunapojisifu kwa sababu ya jina lake. (Yer. 9:23, 24; 1 Kor. 1:31; 2 Kor. 10:17) ‘Kujisifu katika Yehova’ kunamaanisha tunajivunia kwamba Yehova ni Mungu wetu. Tunaliona kuwa pendeleo kuliheshimu jina lake na kuunga mkono sifa yake. Hatupaswi kamwe kuona aibu kuwaambia wafanyakazi, wanafunzi, majirani wetu, na watu wengine kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova! Ibilisi anataka tuache kuwaambia wengine kuhusu jina la Yehova. (Yer. 11:21; Ufu 12:17) Kwa kweli, Shetani na manabii wake wa uwongo wanataka kuwafanya watu walisahau jina la Yehova. (Yer. 23:26, 27) Lakini upendo wetu kwa ajili ya jina la Yehova unatufanya tuendelee kushangilia katika jina hilo “mchana kutwa.”—Zab. 5:11; 89:16.
15. Kuliitia jina la Yehova kunamaanisha nini?
15 Tunaendelea kuliitia jina la Yehova. (Yoe. 2:32; Rom. 10:13, 14) Kuliitia jina la Yehova kunahusisha mengi zaidi ya kulijua na kulitumia tu jina la kibinafsi la Mungu. Kunahusisha kuujua utu wa Mungu, kumtumaini, na kumtafuta ili atupatie msaada na mwongozo. (Zab. 20:7; 99:6; 116:4; 145:18) Tunalitangaza pia jina lake na sifa zake kwa wengine, na tunawahimiza watubu na kuchukua hatua ili waweze kupata kibali cha Yehova.—Isa. 12:4; Mdo. 2:21, 38.
16. Tunawezaje kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo?
16 Tuko tayari kuteseka kwa ajili ya jina la Yehova. (Yak. 5:10, 11) Tunapoendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova licha ya kuteseka, tunathibitisha kwamba Shetani ni mwongo. Katika siku za Ayubu, Shetani alitoa shtaka hili kuhusu wale wanaomtumikia Yehova: “Mtu atatoa kila kitu alicho nacho ili aokoe uhai wake.” (Ayu. 2:4) Shetani alidai kwamba watu wangemtumikia Yehova wakati tu mambo ni mazuri, na kwamba wangemwacha Yehova ikiwa wangekabili hali ngumu. Ayubu mwaminifu alithibitisha kwamba dai hilo ni la uwongo. Sisi pia tuna pendeleo la kuthibitisha kwamba hatutamwacha Yehova kamwe, haidhuru Shetani atatusababishia matatizo gani. Tunaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba Yehova atatulinda kwa sababu ya jina lake.—Yoh. 17:11.
17. Kama ilivyotajwa kwenye 1 Petro 2:12, ni katika njia gani nyingine tunaweza kuliletea utukufu jina la Yehova?
17 Tunaliheshimu jina la Yehova. (Met. 30:9; Yer. 7:8-11) Kwa sababu tunamwakilisha Yehova na tunaitwa kwa jina lake, mambo tunayofanya yanaweza kuliletea sifa au kulivunjia heshima jina lake. (Soma 1 Petro 2:12.) Hivyo, tunataka kufanya yote tuwezayo ili kulisifu jina la Yehova kupitia maneno na matendo yetu. Kwa kufanya hivyo, tutaliletea utukufu jina lake kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasio wakamilifu.
18. Ni kwa njia gani nyingine tunaweza kuthibitisha kwamba jina la Yehova ni muhimu kwetu? (Tazama pia maelezo ya chini.)
18 Tunahangaikia zaidi jina la Yehova kuliko sifa yetu wenyewe. (Zab. 138:2) Kwa nini jambo hilo ni la muhimu sana? Kwa sababu huenda upendo wetu kwa ajili ya jina la Yehova ukaharibu sifa yetu machoni pa wengine.a Yesu alikuwa tayari kufa kifo cha aibu kama mhalifu aliyehukumiwa ili kuliheshimu jina la Yehova. Yesu ‘aliidharau aibu’ katika maana ya kwamba hakuhangaishwa au kuwa na wasiwasi kupita kiasi kuhusu maoni ya wengine kumwelekea. (Ebr. 12:2-4) Alikazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu.—Mt. 26:39.
19. Unahisije kuhusu jina la Yehova, na kwa nini?
19 Tunajivunia jina la Yehova na tunahisi ni pendeleo kuitwa Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu hiyo, tuko tayari kuvumilia shutuma zozote ambazo huenda tukakabili. Jina la Yehova ni la muhimu zaidi kwetu kuliko sifa yetu wenyewe. Hivyo, acheni tuazimie kuendelea kulisifu jina la Yehova hata Shetani atuletee jaribu gani. Kwa njia hiyo, tutathibitisha kwamba jina la Yehova ni la muhimu sana kwetu, kama tu lilivyo kwa Yesu Kristo.
WIMBO 10 Msifuni Yehova Mungu Wetu!
a Hata mwanamume mwaminifu Ayubu alikengeuka sifa yake iliposhambuliwa na marafiki wake watatu. Mwanzoni, alipopoteza watoto wake na mali zake zote, “Ayubu hakutenda dhambi wala hakumlaumu Mungu kwa kutenda jambo lolote baya.” (Ayu. 1:22; 2:10) Hata hivyo, Ayubu aliposhtakiwa kwamba alikuwa ametenda dhambi, alianza ‘kuzungumza ovyoovyo.’ Alikazia fikira kutetea sifa yake mwenyewe badala ya kulitakasa jina la Mungu au sifa yake.—Ayu. 6:3; 13:4, 5; 32:2; 34:5.