MAKALA YA 22
WIMBO 15 Msifuni Mzaliwa wa Kwanza wa Yehova!
Jina la Yehova Lina Umuhimu Gani kwa Yesu?
“Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha.”—YOH. 17:26.
JAMBO KUU
Jinsi Yesu alivyowajulisha wengine jina la Yehova na jinsi ambavyo amelitakasa na kulitetea.
1-2. (a) Yesu alifanya nini usiku kabla ya kuuawa? (b) Tutazungumzia maswali gani katika makala hii?
ILIKUWA Alhamisi jioni, Nisani 14, 33 W.K., na Yesu alikuwa karibu kusalitiwa, kuhukumiwa, kuteswa, na kuuawa. Alikuwa amemaliza tu kula mlo wa pekee pamoja na mitume wake waaminifu katika chumba cha juu. Baada ya mlo huo, Yesu aliwapatia mitume wake maneno ya mwisho ya kuwatia moyo. Na muda mfupi kabla ya kuondoka kwenye chumba hicho cha juu, Yesu alitoa sala ya muhimu sana. Mtume Yohana aliandika sala hiyo; inayopatikana katika Yohana sura ya 17.
2 Sala ya Yesu inafunua nini kuhusu mahangaiko yake wakati huo? Sala hiyo inaonyeshaje jambo lililokuwa muhimu kwake wakati wote wa huduma yake akiwa hapa duniani? Acheni tuzungumzie maswali hayo.
“NIMEWAJULISHA JINA LAKO”
3. Yesu alisema nini kuhusu jina la Yehova, na alimaanisha nini? (Yohana 17:6, 26)
3 Yesu alisema hivi katika sala yake: “Nimewajulisha jina lako.” Kwa kweli, alitaja mara mbili kwamba alikuwa amewajulisha wanafunzi wake jina la Yehova. (Soma Yohana 17:6, 26.) Alimaanisha nini? Je, alikuwa amewajulisha jina ambalo hawalijui? Wanafunzi wa Yesu walikuwa Wayahudi, hivyo tayari walilijua jina la Mungu, Yehova. Jina hilo linapatikana karibu mara 7,000 katika Maandiko ya Kiebrania. Basi, Yesu aliposema, “Nimewajulisha jina lako,” hakumaanisha kwamba aliwafundisha kuwa Mungu anaitwa Yehova. Badala yake, alimaanisha kwamba aliwafundisha Yehova ni Mungu wa aina gani. Yesu aliwasaidia wanafunzi wake wamjue Yehova vizuri zaidi. Hilo lilitia ndani kuwafundisha kuhusu kusudi, matendo, na sifa Zake, kwa njia ambayo hakuna mtu mwingine yeyote angeweza.
4-5. (a) Jina la mtu linawezaje kuwa na maana zaidi? Toa mfano. (b) Wanafunzi wa Yesu walimjuaje Yehova vizuri zaidi?
4 Kwa mfano, wazia kwamba kuna mzee mmoja katika kutaniko lako anayeitwa David na ambaye ni daktari wa upasuaji. Umemjua ndugu huyo kwa miaka mingi. Lakini siku moja unahitaji matibabu ya dharura. Hivyo, haraka unapelekwa kwenye hospitali anayofanya kazi ndugu huyo, naye anatumia ustadi wake akiwa daktari kuokoa uhai wako. Sasa unampenda ndugu huyo hata zaidi, na unaposikia jina lake, unakumbuka jambo alilokufanyia. David si tu yule mzee wa kutaniko unayemjua, bali pia ni daktari wa upasuaji aliyeokoa uhai wako.
5 Vivyo hivyo, wanafunzi wa Yesu tayari walilijua jina la Yehova. Lakini jina hilo lilikuwa na maana zaidi kwao baada ya Yesu kuwasaidia wamjue Yehova vizuri zaidi. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Kwa sababu Yesu aliiga utu wa Baba yake katika kila jambo alilosema na kutenda. Hivyo, mitume wake ‘walimjua’ Yehova vizuri zaidi kwa kukazia fikira njia ya Yesu ya kufundisha na kwa kuchunguza jinsi alivyowatendea watu.—Yoh. 14:9; 17:3.
“JINA LAKO AMBALO UMENIPA”
6. Ni katika maana gani Yehova alimpa Yesu jina Lake? (Yohana 17:11, 12)
6 Katika sala yake, Yesu alisali hivi kwa ajili ya wanafunzi wake: “Walinde kwa sababu ya jina lako ambalo umenipa.” (Soma Yohana 17:11, 12.) Je, hilo lilimaanisha kwamba sasa Yesu angeitwa Yehova? Hapana. Ona kwamba katika sala hiyo Yesu alipomrejelea Yehova alitumia maneno, “jina lako.” Hivyo, jina la Yehova halikuja kuwa jina la kibinafsi la Yesu. Basi, Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba alikuwa amepewa jina la Mungu? Kwanza, Yesu alikuwa mwakilishi na Msemaji wa Yehova. Alikuja katika jina la Baba yake na alifanya matendo mengi yenye nguvu katika jina hilo. (Yoh. 5:43; 10:25) Zaidi ya hilo, jina la Yesu linamaanisha “Yehova Ni Wokovu.” Naam, maana ya jina la Yesu inatia ndani jina la Yehova.
7. Toa mfano unaoonyesha jinsi ambavyo Yesu angeweza kuzungumza katika jina la Yehova.
7 Kwa mfano, kwa kuwa balozi anamwakilisha mtawala fulani, anaweza kuzungumza kwa niaba ya mtawala huyo. Hivyo, maneno ya balozi huyo yana mamlaka sawa na maneno ya mtawala huyo. Vivyo hivyo, Yesu alimwakilisha Yehova na alizungumza na watu katika jina Lake.—Mt. 21:9; Luka 13:35.
8. Jina la Yehova lilikuwaje “ndani” ya Yesu kabla ya kuja kwake duniani? (Kutoka 23:20, 21)
8 Katika jukumu lake akiwa Neno, Yesu ametumikia akiwa Msemaji wa Yehova kwa kuwasilisha habari na miongozo kwa malaika na wanadamu pia. (Yoh. 1:1-3) Inaelekea Yesu ndiye malaika aliyetumwa na Yehova kuwatunza Waisraeli walipokuwa nyikani. Alipowaambia Waisraeli wamtii malaika huyo, Yehova aliwaambia sababu ya kufanya hivyo, alisema hivi: “Kwa sababu jina langu limo ndani yake.”a (Soma Kutoka 23:20, 21.) Jina la Yehova lilikuwa “ndani” ya Yesu katika maana ya kwamba alimwakilisha Yehova, na Yesu ndiye hasa anayelitetea na kulitakasa jina la Baba yake.
“BABA, LITUKUZE JINA LAKO”
9. Jina la Yehova lilikuwa muhimu kadiri gani kwa Yesu? Eleza.
9 Kama ambavyo tumeona, jina la Yehova lilikuwa muhimu sana kwa Yesu hata kabla ya kuja duniani. Hivyo, haishangazi kwamba alipokuwa duniani alilihusisha jina hilo katika kila jambo alilofanya! Mwishoni mwa huduma yake, Yesu alimwambia hivi Yehova: “Baba, litukuze jina lako.” Bila kukawia, Baba yake alimjibu hivi kwa sauti kubwa kutoka mbinguni: “Nimelitukuza nami nitalitukuza tena.”—Yoh. 12:28.
10-11. (a) Yesu alilitukuzaje jina la Yehova? (Tazama pia picha.) (b) Kwa nini jina la Yehova linahitaji kutakaswa na kutetewa?
10 Yesu pia alilitukuza jina la Yehova. Jinsi gani? Njia moja ni kwa kuwaambia wengine kuhusu sifa zenye kustaajabisha za Baba yake na matendo yake. Hata hivyo, mengi zaidi yalihusika katika kulitukuza jina hilo. Jina la Yehova lilihitaji kutakaswa na sifa yake kutetewa.b Yesu alionyesha umuhimu wa jambo hilo alipowafundisha wafuasi wake sala ya mfano. Alisema hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.”—Mt. 6:9.
11 Kwa nini jina la Yehova linahitaji kutakaswa na kutetewa? Kwa sababu katika bustani ya Edeni, Shetani Ibilisi alimchongea na kumvunjia heshima Yehova Mungu. Shetani alidai kwamba Yehova ni mwongo na alikuwa anawanyima Adamu na Hawa jambo fulani zuri. (Mwa. 3:1-5) Pia, Shetani alidai kwamba njia ya Yehova ya kufanya mambo haikuwa sawa. Mashtaka ya uwongo ya Shetani yalishambulia moja kwa moja sifa, au jina la Yehova. Baadaye, katika siku za Ayubu, Shetani alidai kwamba wale wanaomtumikia Yehova wanafanya hivyo kwa sababu tu ya vitu wanavyopata kutoka Kwake. Mchongezi huyo aliendelea kushtaki kwamba hakuna mwanadamu anayempenda kikweli Yehova hivi kwamba aendelee kumtumikia akiwa chini ya jaribu. (Ayu. 1:9-11; 2:4) Wakati ulihitajika ili kuthibitisha ni nani aliyekuwa mwongo, Yehova au Shetani.
Yesu aliwafundisha wafuasi wake umuhimu wa kulitakasa jina la Mungu (Tazama fungu la 10)
“NINAUTOA UHAI WANGU”
12. Yesu alikuwa tayari kufanya nini kwa sababu ya upendo wake kwa ajili ya jina la Yehova?
12 Kwa sababu ya upendo wake kwa Yehova, Yesu alitaka kufanya yote aliyoweza kulitakasa na kulitetea jina la Yehova. Yesu alisema hivi: “Ninautoa uhai wangu.” (Yoh. 10:17, 18) Naam, alikuwa tayari hata kufa kwa ajili ya jina la Yehova.c Wanadamu wawili wa kwanza wakamilifu, Adamu na Hawa, hawakumtii Yehova na badala yake walimfuata Shetani. Tofauti na hilo, Yesu alikuwa tayari kuja duniani na kuthibitisha upendo wake kwa Yehova. Yesu alifanya hivyo kwa kudumisha utimilifu kikamilifu. (Ebr. 4:15; 5:7-10) Alidumisha utimilifu wake mpaka alipokufa katika mti wa mateso. (Ebr. 12:2) Kwa njia hiyo, alithibitisha upendo wake kwa Yehova na kwa jina Lake.
13. Kwa nini Yesu alikuwa na nafasi ya pekee ya kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo? (Tazama pia picha.)
13 Kupitia maisha yake, Yesu alithibitisha bila shaka yoyote kwamba Shetani ndiye mwongo, na si Yehova! (Yoh. 8:44) Yesu alimjua Yehova vizuri zaidi kuliko mtu mwingine yeyote aliyewahi kuishi. Yesu angejua ikiwa kulikuwa na ukweli wowote kuhusu mashtaka ambayo Shetani alitoa dhidi ya Yehova. Lakini Yesu aliendelea kutetea kwa uthabiti sifa, au jina la Yehova. Hata ilipoonekana kana kwamba Yehova amemwacha, Yesu alikuwa tayari kufa badala ya kukosa kumtii Baba yake mpendwa.—Mt. 27:46.d
Kupitia maisha yake, Yesu alithibitisha bila shaka yoyote kwamba Shetani ndiye mwongo, na si Yehova! (Tazama fungu la 13)
“NIMEMALIZA KAZI ULIYONIPA NIFANYE”
14. Yehova alimthawabishaje Yesu kwa sababu ya uaminifu wake?
14 Katika sala aliyotoa usiku kabla ya kifo chake, Yesu aliweza kusema hivi: “Nimemaliza kazi uliyonipa nifanye.” Alikuwa na uhakika kwamba Yehova angemthawabisha kwa sababu ya uaminifu wake. (Yoh. 17:4, 5) Yesu alikuwa na sababu nzuri ya kumtumaini Baba yake. Yehova hakuruhusu aendelee kubaki kaburini. (Mdo. 2:23, 24) Alimfufua Yesu na kumpa cheo cha juu zaidi mbinguni. (Flp. 2:8, 9) Hatimaye, Yesu alianza kutawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Ufalme huo ungetimiza nini? Sehemu ya pili ya sala ya mfano inatuambia hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi [ya Yehova] na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mt. 6:10.
15. Yesu atatimiza mambo gani mengine?
15 Hivi karibuni, Yesu atapigana vita dhidi ya maadui wa Mungu na kuwaangamiza waovu katika Har–Magedoni. (Ufu. 16:14, 16; 19:11-16) Muda mfupi baada ya vita hivyo, atamtupa Shetani kwenye “shimo refu lisilo na mwisho,” yaani, hali ya kutotenda kama ya wafu. (Ufu. 20:1-3) Yesu atarudisha amani na ukamilifu kwa wanadamu wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja. Atawafufua wafu. Ataifanya dunia nzima iwe paradiso. Kusudi la Yehova litatimizwa!—Ufu. 21:1-4.
16. Ni mambo gani yatakayotimizwa mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja?
16 Tunaweza kutarajia mambo gani mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja? Dhambi na kutokamilika kwa wanadamu hakutakuwapo. Wanadamu hawatahitaji kuomba msamaha wa dhambi zao kwa msingi wa fidia; wala hawatahitaji mpatanishi au ukuhani. Na “adui wa mwisho [atakayekuwa ameangamizwa] ni kifo [kilichotokana na Adamu].” Makaburi yatakuwa matupu. Wafu watakuwa wamefufuliwa. Kila mtu atakuwa mkamilifu.—1 Kor. 15:25, 26.
17-18. (a) Ni nini kitakachotokea mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja? (b) Yesu atafanya nini kipindi chake cha kutawala kitakapokwisha? (1 Wakorintho 15:24, 28) (Tazama pia picha.)
17 Ni jambo gani lingine linalotokea mwishoni mwa Utawala huo wa Miaka Elfu Moja? Wakati huo, jambo la pekee sana litatukia. Suala linalohusu kutakaswa kwa jina la Yehova litatatuliwa. Jinsi gani? Kwenye bustani ya Edeni, Shetani alidai kuwa Yehova ni mwongo, naye hawatawali wanadamu kwa upendo. Tangu wakati huo, jina lake limetakaswa tena na tena na wale wanaomheshimu. Hivyo, kufikia mwishoni mwa Utawala wa Miaka Elfu Moja, sifa ya Yehova itakuwa imetetewa kikamili. Atakuwa amethibitisha bila shaka yoyote kwamba yeye ni Baba wa mbinguni mwenye upendo.
18 Hatimaye, madai ya Shetani yatathibitika kwa watu wote kuwa ya uwongo. Yesu atafanya nini kipindi chake cha kutawala kitakapokwisha? Je, atafuata mfano wa Shetani na kumwasi Yehova? Hapana! (Soma 1 Wakorintho 15:24, 28.) Yesu ataukabidhi Ufalme kwa Baba yake. Atajitiisha chini ya utawala wa Yehova. Naam, tofauti na Shetani, Yesu yuko tayari kukabidhi mamlaka yake yote kwa Yehova kwa sababu anampenda.
Kwa hiari, Yesu anamkabidhi Yehova Ufalme mwishoni mwa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja (Tazama fungu la 18)
19. Jina la Yehova lina umuhimu gani kwa Yesu?
19 Haishangazi kwamba Yehova alikuwa tayari kumpa Yesu jina Lake! Yesu amethibitika kuwa mwakilishi mkamilifu wa Baba Yake. Hivyo, jina la Yehova lina umuhimu gani kwa Yesu? Ni la muhimu sana kwa Yesu kuliko kitu kingine chochote. Alikuwa tayari kufa kwa ajili ya jina hilo, na atakuwa tayari kumkabidhi Yehova kila kitu mwishoni mwa Utawala wake wa Miaka Elfu Moja. Tunawezaje kuiga mfano wa Yesu? Tutazungumzia jibu la swali hilo katika makala inayofuata.
WIMBO 16 Msifuni Yah kwa Mwana Wake Mtiwa Mafuta
a Pindi fulani, malaika pia walimwakilisha Yehova walipowasilisha jumbe mbalimbali katika jina lake. Hiyo ndiyo sababu kuna sehemu katika Biblia ambazo malaika anatajwa au anarejelewa kana kwamba ni Yehova mwenyewe. (Mwa. 18:1-33) Ingawa Maandiko yanasema kwamba Musa alipokea Sheria kutoka kwa Yehova, mistari mingine inaonyesha kwamba alipokea Sheria hiyo kupitia malaika.—Law. 27:34; Mdo. 7:38, 53; Gal. 3:19; Ebr. 2:2-4.
b UFAFANUZI WA MANENO: “Kutakasa” kunamaanisha kuheshimu, kuona kitu kuwa kitakatifu, au kuonyesha staha. “Kutetea” kunamaanisha kumweka mtu huru kutokana na mashtaka ya uwongo dhidi ya sifa yake, au kuthibitisha kwamba hana hatia dhidi ya mashtaka ya uwongo au uchongezi.
c Kifo cha Yesu kiliandaa pia njia kwa wanadamu kupata uzima wa milele.
d Tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 2021, uku. 30-31.