SIMULIZI LA MAISHA
“Vita Ni vya Yehova”
JANUARI 28, 2010, ilikuwa siku yenye baridi nilipokuwa katika jiji maridadi la Strasbourg, nchini Ufaransa. Lakini sikuwa katika jiji hilo ili kutalii. Nilikuwa katika timu ya wanasheria waliopewa mgawo wa kutetea haki za Mashahidi wa Yehova mbele ya Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu (ECHR). Serikali ya Ufaransa ilisema kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa na deni la kodi la kiasi cha Euro 64,000,000 hivi (Dola 89,000,000 za Marekani), nasi tulikuwa hapo ili kuthibitisha kwamba jambo hilo halikuwa la kweli. Hata hivyo, pesa hizo hazikuwa sababu ya msingi kwa nini tulihitaji kushinda kesi hiyo. Ikiwa tungeshinda, jina la Yehova lingetukuzwa, watu wake wangedumisha sifa yao nzuri, na tungeweza kuendelea kumwabudu Yehova kwa uhuru nchini humo. Mambo yaliyotokea katika kesi hiyo yalithibitisha kwamba “vita ni vya Yehova.” (1 Sam. 17:47) Acheni niwaeleze.
Katika mwaka wa 1999, serikali ya Ufaransa ilisema kwamba ofisi yetu ya tawi ya Ufaransa ilihitaji kulipa kodi ya michango iliyopokea kati ya mwaka wa 1993 na 1996. Hatukupata hukumu ya haki katika mahakama za Ufaransa. Baada ya kushindwa katika mahakama ya rufaa, serikali ilichukua zaidi ya Euro 4,500,000 (Dola 6,300,000 za Marekani) kutoka katika akaunti ya benki ya ofisi ya tawi. Tegemeo letu la mwisho lilikuwa Mahakama ya ECHR. Hata hivyo, kabla ya kusikiliza kesi yetu, Mahakama ya ECHR, ilitaka sisi na timu ya mawakili wa serikali ya Ufaransa na wawakilishi kutoka katika Mahakama ya Ulaya, tukutane ili tuone ikiwa tunaweza kufikia makubaliano kabla ya kesi hiyo kusikilizwa.
Tulitazamia kwamba msajili angetushinikiza tusuluhishe jambo hilo kwa kukubali kulipa kiasi fulani cha pesa kilichodaiwa. Lakini tulitambua wazi kwamba tungevunja kanuni za Biblia ikiwa tungelipa kiasi chochote cha pesa. Ndugu na dada walitoa michango ili kuunga mkono masilahi ya Ufalme, hivyo michango hiyo haikuwa mali ya serikali. (Mt. 22:21) Hata hivyo, tulihudhuria mkutano huo ili kuonyesha kwamba tunaheshimu utaratibu wa Mahakama hiyo.
Timu yetu ya wanasheria mbele ya mahakama ya ECHR, mwaka wa 2010
Tulikutana kwa ajili ya kesi hiyo katika chumba maridadi cha mkutano katika Mahakama hiyo. Kesi hiyo haikuanza vizuri. Katika maneno yake ya mwanzoni, msajili alisema kwamba alitazamia Mashahidi wa Yehova nchini Ufaransa walipe kiasi fulani cha kodi wanayodaiwa. Ghafla tukachochewa kumuuliza hivi, “Je, unajua kwamba tayari serikali imechukua zaidi ya Euro 4,500,000 kutoka katika akaunti yetu ya benki?”
Alishtuka kusikia hilo. Timu ya wanasheria wa serikali walipothibitisha jambo hilo, mtazamo wake kuelekea kesi hiyo ulibadilika kabisa. Aliwakemea na akasitisha kwa ghafla mkutano huo. Kisha nilitambua kwamba kwa njia fulani ambayo hatukutarajia, Yehova alikuwa amebadilisha kabisa mwelekeo wa kesi hiyo. Tulitoka katika mkutano huo tukiwa na furaha na tukiwa tumeshangazwa na kilichotokea.
Mnamo Juni 30, 2011, Mahakama ya ECHR ilifikia uamuzi wa pamoja uliotuunga mkono. Iliamua kwamba kulazimishwa kulipa kodi hiyo kulikuwa kinyume cha sheria, na ikaiamuru serikali irudishe pesa ilizochukua pamoja na riba! Uamuzi huo wa kihistoria umelinda ibada safi nchini Ufaransa mpaka leo. Swali hilo ambalo mapema hatukuwa tumepanga kuliuliza, lilikuwa kama jiwe lililomuua Goliathi. Lilibadilisha matokeo ya kesi hiyo. Kwa nini tulishinda? Kwa sababu kama tu Daudi alivyomwambia Goliathi, “vita ni vya Yehova.”—1 Sam. 17:45-47.
Tumeshinda kesi katika nyakati nyingine pia. Kufikia sasa, licha ya upinzani mkali kutoka kwa viongozi wa kisiasa na kidini, mahakama kuu katika nchi mbalimbali 70 na mahakama nyingine za kimataifa, zimetoa maamuzi yanayounga mkono Mashahidi wa Yehova katika kesi 1,225. Ushindi huo wa kisheria unalinda haki zetu za msingi kama vile, haki yetu ya kutambuliwa kisheria kuwa ni dini, kuhubiri hadharani, kukataa kushiriki katika maadhimisho ya kizalendo, na kukataa damu.
Ilikuwaje kwamba nilihusika katika kesi huko bara la Ulaya ijapokuwa ninatumikia katika Makao Makuu ya Ulimwenguni Pote ya Mashahidi wa Yehova, yaliyo New York, Marekani?
NILILELEWA NA WAZAZI WALIOKUWA NA BIDII
Wazazi wangu, George na Lucille, walihitimu darasa la 12 la Shule ya Gileadi na walikuwa wanatumikia nchini Ethiopia nilipozaliwa mwaka wa 1956. Waliniita Philip, (Filipo kwa Kiswahili) aliyekuwa mweneza-injili katika karne ya kwanza. (Mdo. 21:8) Mwaka uliofuata, serikali ilipiga marufuku ibada yetu. Ingawa nilikuwa mdogo sana, bado ninakumbuka vizuri familia yetu ikiabudu kwa siri. Nikiwa mtoto, nilifurahishwa sana na jambo hilo! Kwa kusikitisha, katika mwaka wa 1960, maofisa wa serikali walitulazimisha tuondoke nchini humo.
Nathan H. Knorr (kushoto kabisa) alipotembelea familia yetu Addis Ababa, Ethiopia, mwaka wa 1959
Familia yetu ilihamia Wichita, Kansas, Marekani, licha ya hilo, wazazi wangu hawakupoteza bidii waliyokuwa nayo katika huduma walipokuwa wamishonari. Walinifundisha mimi, dada yangu mkubwa, Judy, na ndugu yangu mdogo, Leslie, waliozaliwa pia Ethiopia, kumpenda na kumtumikia Yehova kwa moyo wetu wote. Nilibatizwa nilipokuwa na umri wa miaka 13. Baada ya miaka mitatu, familia yetu ilihamia katika eneo lenye uhitaji mkubwa la Arequipa, nchini Peru.
Mwaka wa 1974 nilipokuwa na umri wa miaka 18 tu, ofisi ya tawi ya Peru ilinituma mimi na ndugu wengine wanne kutumikia tukiwa mapainia wa pekee. Tulitumwa tukahubiri katika Eneo la Kati la Milima ya Andes ambapo hakuna mhubiri aliyewahi kuhubiri katika maeneo hayo. Mgawo wetu ulitia ndani kuwahubiria wenyeji wanaozungumza Kikwechua na Kiaymara. Tulisafiri kwa kutumia gari tulilotumia kama nyumba na tulilipatia jina la Safina kwa sababu lilifanana na sanduku kubwa. Bado ninafurahi ninapokumbuka nikitumia Biblia kuwaonyesha wenyeji katika maeneo hayo kwamba hivi karibuni Yehova ataondoa umaskini, magonjwa, na kifo. (Ufu. 21:3, 4) Wengi walikubali ujumbe wa Ufalme.
“Safina,” mwaka wa 1974
NINAANZA KAZI MAKAO MAKUU
Alipotembelea nchini Peru mwaka wa 1977, Albert Schroeder, aliyekuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alinitia moyo nijaze fomu ya utumishi wa Betheli ili niweze kutumikia katika makao makuu. Nilifanya hivyo. Muda mfupi baadaye, mnamo Juni 17, 1977, nilianza kutumikia katika Betheli ya Brooklyn. Katika kipindi cha miaka minne iliyofuata, nilifanya kazi katika idara ya Usafi na Udumishaji.
Siku yetu ya harusi, mwaka wa 1979
Nilikutana na Elizabeth Avallone mnamo Juni 1978, katika kusanyiko la kimataifa lililofanyika New Orleans, Louisiana. Yeye pia alikuwa amelelewa na wazazi waliomtumikia Yehova kwa moyo wao wote. Tayari Elizabeth alikuwa ametumikia akiwa painia wa kawaida kwa miaka minne, na aliuona utumishi wa wakati wote kuwa njia yake ya maisha. Tuliendelea kuwasiliana. Baada ya muda, tulifahamiana vizuri na tukapendana sana. Tulifunga ndoa Oktoba 20, 1979, na tukiwa wenzi wa ndoa, tukaanza utumishi wa Betheli.
Ndugu na dada katika kutaniko letu la kwanza la Brooklyn Spanish, walitupenda sana. Kwa miaka mingi, tumeshirikiana pia na makutaniko mengine matatu yenye upendo ambamo ndugu na dada wametukaribisha na kututia moyo tuendelee na utumishi wetu wa Betheli. Tunathamini sana msaada kutoka kwao na kutoka kwa marafiki na watu wa familia waliotusaidia kuwatunza wazazi wetu walipozeeka.
Wanabetheli walioshirikiana na Kutaniko la Brooklyn Spanish, mwaka wa 1986
NAJIUNGA NA IDARA YA SHERIA
Kwa kushangaza, Januari 1982, nilipewa mgawo wa kutumikia katika Idara ya Sheria katika Betheli. Miaka mitatu baadaye, niliambiwa nisome chuo kikuu ili niwe mwanasheria. Nilishangaa sana nilipojifunza katika masomo yangu kwamba watu nchini Marekani na nchi nyingine, wana uhuru wa kufanya mambo mengi kwa sababu ya ushindi wa kisheria waliopata Mashahidi wa Yehova. Kesi hizo muhimu zilizungumziwa kwa undani darasani.
Mwaka wa 1986, nilipokuwa na umri wa miaka 30, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa Idara ya Sheria. Kwa sababu nilikuwa kijana sana na sikuwa nimejua mengi yatakayohusika wakati ujao, nilihisi hilo ni pendeleo na pia nililemewa na mgawo huo.
Nilikuwa wakili mwaka wa 1988, lakini sikuwa nimetambua ni kwa kiasi gani masomo hayo yaliniathiri mimi na uhusiano wangu na Yehova. Elimu ya juu inaweza kumfanya mtu awe na kiburi na ahisi kwamba kuwa na ujuzi huo wa pekee kunamfanya awe bora kuliko wengine ambao hawana elimu hiyo. Elizabeth alinisaidia. Alinisaidia nirudie tena ratiba yangu ya kiroho niliyokuwa nayo kabla ya kwenda chuo kikuu. Ilichukua muda, lakini hatua kwa hatua nilirudia hali yangu ya kiroho. Ninaweza kusema kwa uhakika kwamba, kuwa na ujuzi mwingi wa pekee si jambo la muhimu maishani. Jambo la muhimu maishani ni kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova na kumpenda sana Yeye na watu wake.
KUITETEA NA KUITHIBITISHA KISHERIA HABARI NJEMA
Baada ya kumaliza masomo ya sheria, nilikazia fikira kupanga huduma za kisheria zilizohitajiwa Betheli na kutetea masilahi ya Ufalme mahakamani. Kazi yangu ilinisisimua sana lakini ilikuwa na changamoto kwa sababu, mambo katika tengenezo letu yalikuwa yakibadilika haraka. Kwa mfano, mwanzoni mwa mwaka wa 1991, Idara ya Sheria iliombwa isaidie kutoa mwongozo wa jinsi ya kusitisha kuomba michango kwa ajili ya machapisho, jambo ambalo tulikuwa tumelifanya kwa muda mrefu. Baada ya muda, Mashahidi wa Yehova walianza kutoa machapisho bila gharama yoyote. Jambo hilo lilirahisisha kazi ya Betheli na shambani, na mpaka leo inalinda utendaji wetu dhidi ya matatizo yanayotokana na kulipa kodi. Wengine walifikiri kwamba badiliko hilo lingemaliza pesa zetu na kuzuia huduma yetu ya hadharani. Mambo yamekuwa tofauti. Idadi ya wale wanaomtumikia Yehova tangu mwaka wa 1990 imeongezeka mara mbili, na leo watu wanaweza kupata chakula cha kiroho kinachookoa uhai bila malipo. Nimejionea kibinafsi kuwa ni kupitia nguvu anayotoa Yehova na mwongozo anaotoa kupitia mtumwa mwaminifu, kwamba jambo hilo na mabadiliko mengine mengi ambayo tengenezo limefanya yanaweza kufanikiwa.—Kut. 15:2; Mt. 24:45.
Hatushindi kesi mahakamani kwa sababu tu ya kuwa na mawakili wazuri. Mara nyingi, mwenendo mzuri wa watu wa Yehova ndio unaowachochea wenye mamlaka kutusaidia. Nilijionea jambo hilo mwaka wa 1998 wakati ambapo washiriki watatu wa Baraza Linaloongoza na wake zao, walipohudhuria makusanyiko ya pekee nchini Kuba. Walikuwa wenye fadhili na heshima, na mwenendo wao ulitoa ushahidi wa kutosha kwa maofisa wa serikali kwamba hatukujihusisha na siasa.
Hata hivyo, nyakati nyingine, njia pekee ya kushughulikia ukosefu wa haki ni kwa ‘kuitetea na kuithibitisha kisheria habari njema’ mahakamani. (Flp. 1:7) Kwa mfano, kwa miaka mingi, wenye mamlaka katika bara la Ulaya na nchini Korea Kusini, hawakutambua haki yetu ya kukataa kutumikia jeshini na badala yake kufanya utumishi wa badala wa kiraia. Matokeo ni kwamba akina ndugu 18,000 hivi katika bara la Ulaya na ndugu zaidi ya 19,000 nchini Korea Kusini, walifungwa gerezani kwa kuwa walikataa utumishi wa kijeshi kwa sababu ya dhamiri zao.
Hatimaye, mnamo Julai 7, 2011, mahakama ya ECHR ilitoa uamuzi wa kihistoria katika kesi ya Bayatyan dhidi ya serikali ya Armenia uliotaka kuwepo kwa utumishi wa badala wa kiraia katika bara lote la Ulaya. Uamuzi huo ulifuatiwa na uamuzi kama huo uliofanywa na Mahakama ya Katiba ya Korea Kusini mnamo Juni 28, 2018. Hatungepata ushindi huo ikiwa baadhi ya ndugu zetu vijana wangevunja msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote.
Idara ya Sheria katika makao makuu na idara za sheria katika ofisi za tawi ulimwenguni, zinafanya kazi kwa bidii ili kutetea masilahi ya Ufalme. Tunahisi kuwa ni pendeleo kuwatetea ndugu na dada zetu wanaokabili upinzani kutoka kwa serikali. Hata tukishindwa kesi mahakamani, bado tunatoa ushahidi kwa magavana na wafalme na kwa mataifa. (Mt. 10:18) Mahakimu, wawakilishi wa serikali, vyombo vya habari, na watu wote kwa ujumla, lazima wafikirie maandiko tunayoweka katika hati za kisheria na hoja tunazotoa. Watu wanyoofu hupata nafasi ya kuwajua Mashahidi wa Yehova na msingi wa mambo wanayoamini. Baadhi yao wamekuja kuwa ndugu na dada zetu.
ASANTE YEHOVA!
Kwa zaidi ya miaka 40, nimekuwa na pendeleo la kufanya kazi za kisheria na ofisi za tawi ulimwenguni pote, kwenda katika mahakama kuu, na kuzungumza na maofisa wengi wenye mamlaka. Ninawapenda na ninawathamini wafanyakazi wenzangu katika Idara ya Sheria ya makao makuu na idara za sheria ulimwenguni pote. Nimepata baraka na uradhi mwingi maishani.
Elizabeth amenitegemeza kwa ushikamanifu na upendo kwa miaka 45 katika pindi nzuri na pindi ngumu. Ninampenda sana kwa hilo kwa sababu anafanya hivyo licha ya kuugua ugonjwa unaomfanya asiwe na nguvu za kutosha.
Tumejionea kibinafsi kwamba nguvu na ushindi havitokani na uwezo wetu wenyewe. Daudi alisema hivi: “Yehova ni nguvu kwa watu wake.” (Zab. 28:8) Naam, “vita ni vya Yehova.”