Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Agosti kur. 20-25
  • Jinsi ya Kushinda Pambano Dhidi ya Tamaa Mbaya

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi ya Kushinda Pambano Dhidi ya Tamaa Mbaya
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINSI “YULE MWOVU” ANAVYOTAKA TUHISI
  • JINSI HALI YETU YA DHAMBI INAVYOWEZA KUTUFANYA TUHISI
  • JINSI YA KUSHINDA PAMBANO
  • “ENDELEENI KUJIJARIBU”
  • Endelea Kujilinda Dhidi ya Majaribu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • ‘Endelea Kumfuata’ Yesu Baada ya Ubatizo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Yehova Amefanya Nini Ili Kuwakomboa Wanadamu Wenye Dhambi?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Maamuzi Yanayoonyesha Unamtegemea Yehova
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Agosti kur. 20-25

MAKALA YA 35

WIMBO 121 Tunahitaji Sifa ya Kujizuia

Jinsi ya Kushinda Pambano Dhidi ya Tamaa Mbaya

“Msiruhusu dhambi iendelee kutawala kama mfalme katika miili yenu inayoweza kufa hivi kwamba mzitii tamaa zake.”—ROM. 6:12.

JAMBO KUU

Kutusaidia (1) kushinda hali ya kuvunjika moyo na (2) kujifunza jinsi ya kushinda vishawishi.

1. Sisi sote tunakabili hali gani kwa sababu ya kutokuwa wakamilifu?

JE, UMEWAHI kuwa na tamaa yenye nguvu ya kufanya jambo lisilompendeza Yehova? Ikiwa ndivyo, usifikie mkataa kwamba jaribu lako ni kubwa zaidi kuliko majaribu ya wengine. Biblia inasema hivi: “Hakuna majaribu ambayo yamewapata ninyi ila yale yaliyo ya kawaida kwa watu.” (1 Kor. 10:13)a Hilo linamaanisha kwamba tamaa yoyote mbaya unayopambana nayo, wengine pia wanapambana nayo. Hauko peke yako, na kwa msaada wa Yehova, unaweza kushinda pambano hilo.

2. Baadhi ya Wakristo na wanafunzi wa Biblia wanapambana na vishawishi gani? (Tazama pia picha.)

2 Biblia inasema pia hivi: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe.” (Yak. 1:14) Jambo linalomshawishi mtu mmoja linaweza kutofautiana na jambo linalomshawishi mtu mwingine. Kwa mfano, baadhi ya Wakristo huenda wakashawishiwa kujihusisha katika mwenendo mpotovu pamoja na mtu wa jinsia tofauti; ilhali wengine wakashawishiwa kufanya hivyo na watu wa jinsia yao. Wale ambao wameacha kutazama ponografia huenda wakawa na tamaa yenye nguvu ya kurudia zoea hilo. Watu wengi ambao wameacha kutumia dawa za kulevya na kileo wanakabili pia changamoto hiyo. Hizo ni baadhi ya tamaa ambazo Wakristo na wanafunzi wa Biblia wanapambana nazo. Pindi fulani, huenda sisi sote tumehisi kama mtume Paulo aliyeandika hivi: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.”—Rom. 7:21.

Tunaweza kushawishiwa ghafla bila kutarajia—wakati na mahali popote (Tazama fungu la 2)d


3. Mtu anaweza kuhisije anapopambana kwa muda mrefu na tamaa mbaya?

3 Ikiwa unapambana kwa muda mrefu na tamaa mbaya yenye nguvu, huenda ukahisi huna nguvu za kushinda tamaa hiyo, kana kwamba huna uwezo wa kujizuia kunaswa na kishawishi hicho. Pia, huenda ukahisi hauna tumaini, kana kwamba Yehova atakuhukumu kwa sababu tu ya kuwa na tamaa mbaya. Uwe na uhakika kwamba mawazo hayo yote si sahihi! Ili kufafanua jambo hilo, makala hii itazungumzia maswali haya mawili: (1) Hisia za kwamba hatuna nguvu za kushinda tamaa mbaya na hatuna tumaini zinatoka wapi? (2) Unawezaje kushinda pambano dhidi ya tamaa mbaya?

JINSI “YULE MWOVU” ANAVYOTAKA TUHISI

4. (a) Kwa nini Shetani anataka tuhisi hatuna nguvu za kushinda tamaa mbaya? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba tuna nguvu za kushinda vishawishi?

4 Shetani anataka tuhisi kwamba hatuna nguvu za kushinda tamaa mbaya tunaposhawishiwa. Yesu alisema hivi alipowafundisha wafuasi wake kusali: “Usituingize katika majaribu, bali utukomboe kutoka kwa yule mwovu.” (Mt. 6:13) Shetani anatilia shaka utayari wa mtu kumtii Yehova anapokabili kishawishi. (Ayu. 2:​4, 5) Inashangaza kwamba anadai hivyo! Shetani ndiye aliyeshawishiwa na tamaa yake mwenyewe, na hakuwa tayari kuendelea kuwa mwaminifu kwa Yehova. Inaelekea anaamini kwamba sisi tuko kama yeye, yaani, tuko tayari kumwacha Yehova tunapokabili kishawishi. Shetani hata alifikiri kwamba Mwana mkamilifu wa Mungu angenaswa na vishawishi! (Mt. 4:​8, 9) Lakini fikiria jambo hili: Je, kweli hatuna nguvu za kupambana dhidi ya tamaa mbaya? La hasha! Tunakubaliana na mtume Paulo, aliyeandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.”—Flp. 4:13.

5. Tunajuaje kwamba Yehova ana uhakika kwamba tunaweza kushinda pambano letu dhidi ya tamaa mbaya?

5 Tofauti kabisa na Shetani, Yehova ana uhakika kwamba tunaweza kupinga tamaa mbaya. Tunajuaje? Kwa sababu Yehova alitabiri kwamba umati mkubwa wa watu watimilifu wangeokoka dhiki kuu. Hilo linamaanisha nini? Yehova, ambaye hawezi kusema uwongo, anasema kwamba idadi kubwa—si tu watu wachache—wataingia katika ulimwengu wake mpya wakiwa na msimamo safi, wakiwa “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwanakondoo.” (Ufu. 7:​9, 13, 14) Ni wazi kwamba Yehova anajua tuna nguvu za kushinda pambano letu dhidi ya tamaa mbaya.

6-7. Kwa nini Shetani anataka tuhisi kwamba hatuna tumaini katika pambano letu dhidi ya vishawishi?

6 Shetani angependa tuhisi, si tu kwamba hatuna nguvu za kushinda kishawishi, bali pia hatuna tumaini—kana kwamba Yehova atatuhukumu kwa sababu tu ya kuwa na tamaa mbaya. Lakini fikiria hili, Shetani ndiye ambaye hana tumaini, amehukumiwa na Yehova kuwa hastahili uzima wa milele. (Mwa. 3:15; Ufu. 20:10) Bila shaka, Shetani anataka tuhisi kwamba sisi pia hatuna tumaini—hasa kwa sababu tuna tumaini la kupata baraka ileile ya kuishi milele ambayo yeye amenyimwa. Hata hivyo, sisi tuna tumaini. Isitoshe, Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova anataka kutusaidia, na si kutuhukumu. Yehova “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—2 Pet. 3:9.

7 Basi, ikiwa tunaamini kwamba hatuna nguvu za kushinda vishawishi au hatuna tumaini katika pambano letu dhidi ya tamaa mbaya, tunafikiri kwa njia ambayo Shetani anataka. Kutambua jambo hilo kunaweza kuimarisha azimio letu la kuchukua msimamo imara dhidi yake.—1 Pet. 5:​8, 9.

JINSI HALI YETU YA DHAMBI INAVYOWEZA KUTUFANYA TUHISI

8. Mbali na kutenda mabaya, dhambi inahusisha nini? (Zaburi 51:5) (Tazama pia “Ufafanuzi wa Maneno.”)

8 Mbali na Shetani, kuna jambo lingine linaloweza kutufanya tuhisi kwamba hatuna nguvu za kushinda vishawishi na hatuna tumaini katika pambano letu dhidi ya tamaa mbaya. Ni jambo gani hilo? Hali yetu ya dhambi tuliyorithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza.b—Ayu. 14:4; soma Zaburi 51:5.

9-10. (a) Hali ya dhambi iliwaathirije Adamu na Hawa? (Tazama pia picha.) (b) Hali ya dhambi inatuathirije?

9 Fikiria jinsi hali ya dhambi ilivyowaathiri Adamu na Hawa. Baada ya kutomtii Yehova, walijificha na kujaribu kufunika miili yao. Kikizungumzia tendo hilo, kitabu Insight on the Scriptures, kinasema hivi: “Dhambi iliwafanya wahisi wana hatia, hangaiko, ukosefu wa usalama, aibu.” Ilikuwa kana kwamba Adamu na Hawa walikuwa wamefungiwa katika nyumba iliyokuwa na vyumba hivyo vinne tu. Adamu na Hawa wangeweza kutoka chumba kimoja na kuingia kingine, lakini hawangeweza kutoka nje ya nyumba hiyo. Hawangeweza kuepuka hali yao ya dhambi.

10 Bila shaka, hatuko katika hali ileile ambayo Adamu na Hawa walikuwa nayo. Fidia—ambayo haiwahusu wenzi hao wa kwanza wa ndoa—inaweza kusafisha dhambi zetu na kutupatia dhamiri safi. (1 Kor. 6:11) Hata hivyo, tulirithi hali ya dhambi. Hivyo, haishangazi kwamba sisi pia huhisi tukiwa na hatia, hangaiko, ukosefu wa usalama, na aibu. Isitoshe, Biblia inasema kwamba dhambi inaendelea kuwashika wanadamu kwa nguvu. Imefanya hivyo “hata juu ya wale ambao [hawajafanya] dhambi kama vile Adamu alivyofanya kosa.” (Rom. 5:14) Ukweli huo haupaswi kutuvunja moyo na kutufanya tuhisi kwamba hatuna nguvu za kushinda tamaa mbaya na hatuna tumaini katika pambano letu. Tunaweza kukataa hisia hizo zisizofaa. Jinsi gani?

Wakiwa wamevaa ngozi ya mnyama, kwa aibu Adamu na Hawa wanaondoka kutoka katika bustani ya Edeni.

Dhambi ilifanya Adamu na Hawa wahisi wakiwa na hatia, hangaiko, ukosefu wa usalama, na aibu (Tazama fungu la 9)


11. Tunapaswa kutendaje tunapohisi kwamba hatuna nguvu za kushinda tamaa mbaya, na kwa nini? (Waroma 6:12)

11 Tunapohisi hatuna nguvu za kushinda vishawishi—kana kwamba hatuwezi kufanikiwa kushinda pambano letu dhidi ya tamaa mbaya—tunaweza kuona hilo kuwa hali yetu ya dhambi “ikizungumza,” nasi hatupaswi kuisikiliza. Kwa nini? Kwa sababu Biblia inatufundisha kwamba hatupaswi kuruhusu dhambi iendelee ‘kututawala kama mfalme.’ (Soma Waroma 6:12.) Hilo linamaanisha kwamba tunaweza kuchagua kutotenda kulingana na tamaa mbaya. (Gal. 5:16) Yehova ana uhakika kwamba tunaweza kupinga kishawishi; la sivyo, hangetuambia tufanye hivyo. (Kum. 30:​11-14; Rom. 6:6; 1 The. 4:3) Ni wazi kwamba tuna nguvu za kushinda katika pambano letu dhidi ya tamaa mbaya.

12. Tunapaswa kutendaje tunapohisi kwamba hatuna tumaini, na kwa nini?

12 Vivyo hivyo, tunapohisi hatuna tumaini—kana kwamba Yehova atatuhukumu kwa sababu tu ya kuwa na tamaa mbaya—tunaweza kuona hilo kuwa hali yetu ya dhambi “ikizungumza,” nasi hatupaswi kuisikiliza. Kwa nini? Kwa sababu Biblia inatufundisha kwamba Yehova anaelewa hali yetu ya dhambi. (Zab. 103:​13, 14) “Anajua mambo yote” kutuhusu, kutia ndani njia mbalimbali ambazo hali yetu ya dhambi tuliyorithi imechangia katika mielekeo yetu isiyofaa. (1 Yoh. 3:​19, 20) Maadamu hatutendi kulingana na mielekeo yetu ya dhambi na tunaepuka kushawishiwa na tamaa zetu mbaya, tunaweza kuwa na msimamo safi mbele za Yehova. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika na jambo hilo?

13-14. Je, kuwa tu na tamaa mbaya kunamaanisha kwamba hatuwezi kukubaliwa na Yehova? Eleza.

13 Biblia inatofautisha kati ya zoea la kufanya mambo mabaya (jambo ambalo tunaweza kudhibiti) na tamaa ya kufanya mambo mabaya (hali ambayo inaweza kujitokeza ghafla). Kwa mfano, baadhi ya Wakristo katika karne ya kwanza huko Korintho, zamani walikuwa na zoea la kufanya ngono ya jinsia moja. Paulo aliandika hivi: “Baadhi yenu mlikuwa hivyo.” Je, hilo lilimaanisha kwamba hawakuwa tena na tamaa yoyote ya kufanya ngono ya jinsia moja? Huenda hapana, kwa sababu mara nyingi tamaa hizo zinakuwa zimekita mizizi. Lakini Wakristo ambao walionyesha sifa ya kujizuia na kuepuka kutenda kulingana na tamaa zao walikubaliwa na Yehova. Aliwaona kuwa ‘wameoshwa na kuwa safi.’ (1 Kor. 6:​9-11) Inaweza kuwa hivyo kwako pia.

14 Hata iwe unapambana na tamaa gani mbaya, unaweza kufanikiwa kuzishinda. Hata ikiwa huwezi kuziondoa kabisa, unaweza kuonyesha sifa ya kujizuia na kuepuka ‘kufanya mapenzi ya mwili na ya fikira zako.’ (Efe. 2:3) Unawezaje kufanya hivyo na kushinda pambano dhidi ya tamaa mbaya?

JINSI YA KUSHINDA PAMBANO

15. Ili kushinda pambano dhidi ya tamaa mbaya, kwa nini tunahitaji kukubali kwa unyoofu udhaifu tulio nao?

15 Ili kushinda pambano dhidi ya tamaa mbaya, utahitaji kukubali kwa unyoofu udhaifu ulio nao. Uwe mwangalifu ili usijidanganye mwenyewe kwa “mawazo ya uwongo.” (Yak. 1:22) Kupunguza uzito wa tatizo lako—kwa kujiambia hivi: ‘Wengine wanakunywa kileo zaidi yangu,’ au kwa kuwalaumu wengine kwa kusema hivi: ‘Nisingeshawishika kutazama ponografia ikiwa mke wangu angenionyesha upendo zaidi’—kutafanya iwe rahisi zaidi kunaswa na kishawishi. Hivyo, usijaribu kutetea mwenendo usiofaa, hata katika mawazo yako. Wajibika kwa sababu ya matendo yako.—Gal. 6:7.

16. Unawezaje kuimarisha azimio lako la kufanya lililo sawa?

16 Mbali na kuwa mnyoofu kuhusu udhaifu wako mbalimbali, utahitaji kuimarisha azimio lako la kutotenda mambo hayo. (1 Kor. 9:​26, 27; 1 The. 4:4; 1 Pet. 1:​15, 16) Fikiria kuhusu jambo linalokushawishi zaidi na wakati gani unashawishika. Huenda ni aina fulani ya kishawishi au wakati fulani katika siku ambapo huenda ikawa rahisi zaidi kwako kushawishika. Kwa mfano, je, unashawishika kwa urahisi zaidi unapokuwa umechoka au inapokuwa usiku sana? Tarajia kishawishi hicho, na ujiandae kiakili ili ujue jinsi ya kutenda kitakapotokea. Muda mzuri zaidi wa kufanya hivyo ni kabla ya kishawishi kutokea.—Met. 22:3.

17. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Yosefu? (Mwanzo 39:​7-9) (Tazama pia picha.)

17 Fikiria jinsi Yosefu alivyotenda mke wa Potifa alipojaribu kumshawishi. Bila kukawia, alikataa mara moja ushawishi wake. (Soma Mwanzo 39:​7-9.) Hilo linaonyesha nini? Yosefu alijua kihususa jinsi alivyohisi kuhusu kumchukua mke wa mtu mwingine, kabla ya kushawishiwa na mke wa Potifa. Kwa njia hiyohiyo, unaweza kuimarisha azimio lako la kufanya lililo sawa kabla ya kishawishi kutokea. Hivyo, utakaposhawishiwa, itakuwa rahisi zaidi kwako kutenda yaliyo sawa kulingana na uamuzi ambao tayari ulifanya.

Mkusanyo wa picha: 1. Yosefu anamkimbia mke wa Potifa aliyeshika vazi lake. 2. Ndugu tineja anakataa kutongozwa na msichana shuleni.

Kama Yosefu, pinga kishawishi bila kukawia! (Tazama fungu la 17)


“ENDELEENI KUJIJARIBU”

18. Unawezaje kushinda pambano dhidi ya tamaa mbaya? (2 Wakorintho 13:5)

18 Ili kushinda pambano dhidi ya tamaa mbaya, utahitaji ‘kuendelea kujijaribu,’ yaani, kuendelea kujichunguza kwa ukawaida ili uone maendeleo yako. (Soma 2 Wakorintho 13:5.) Pindi kwa pindi, chunguza mawazo na matendo yako na ikihitajika fanya marekebisho. Kwa mfano, hata ikiwa umefanikiwa kupinga kishawishi fulani, jiulize hivi: ‘Ilinichukua muda mrefu kadiri gani kabla ya kusema hapana?’ Ukigundua kwamba ulichukua muda mrefu, usijihukumu. Badala yake, chukua hatua ili kujilinda. Jiulize maswali haya: ‘Je, ninaweza kuondoa mawazo yasiyofaa haraka zaidi? Je, burudani ninayochagua inafanya iwe vigumu zaidi kwangu kupinga vishawishi? Je, ninaacha mara moja kutazama picha zisizofaa? Je, ninaelewa kwa nini viwango vya Yehova sikuzote ni bora zaidi hata ikiwa ninahitaji kujitahidi kuonyesha sifa ya kujizuia ili kuvitii?’—Zab. 101:3.

19. Maamuzi yasiyo na hekima yanayoonekana kuwa madogo yanawezaje kufanya iwe vigumu zaidi kwetu kupambana dhidi ya tamaa mbaya?

19 Unapaswa kuepuka pia kutoa visingizio. Biblia inasema hivi: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yer. 17:9) Yesu alisema kwamba moyo unatokeza “mawazo mabaya.” (Mt. 15:19) Kwa mfano, huenda baada ya muda, mtu ambaye ameacha kutazama ponografia akafikiri kwamba ni “salama” kutazama picha zinazoamsha hamu ya ngono kwa sababu hazionyeshi watu wakiwa uchi. Au huenda akajiambia hivi: ‘Si kosa kuwaza kuhusu tamaa zisizofaa, maadamu sifanyi mambo hayo.’ Kwa maneno mengine, moyo wenye hila wa mtu huyo “[unapanga] mapema kwa ajili ya tamaa za mwili.” (Rom. 13:14) Unawezaje kuepuka kufanya hivyo? Uwe mwenye utambuzi na epuka kufanya maamuzi madogo yasiyo na hekima yatakayokuongoza kufanya uamuzi mkubwa usiofaa, kama vile kutenda mambo mabaya.c Pia, kataa “mawazo mabaya,” yanayotetea mwenendo usiofaa.

20. Tuna tumaini gani la wakati ujao, na leo tuna msaada gani?

20 Kama tulivyojifunza, kwa msaada wa Yehova, tuna nguvu za kushinda vishawishi. Pia, kwa sababu ya rehema zake, tuna tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya. Tutafurahi sana kumtumikia Yehova tukiwa na akili na moyo safi! Kabla ya wakati huo kufika, tunaweza kuwa na uhakika kwamba tuna nguvu za kushinda vishawishi na tunaweza kuwa na tumaini katika pambano letu dhidi ya tamaa mbaya. Tunaweza kushinda, kwa sababu Yehova anabariki jitihada zetu!

UNGEJIBUJE?

  • Tunawezaje kushinda hisia za kwamba hatuna nguvu za kushinda tamaa mbaya na hatuna tumaini?

  • Tunawezaje kutoruhusu dhambi ‘itutawale kama mfalme’?

  • Tunawezaje ‘kuendelea kujijaribu’ wenyewe?

WIMBO 122 Iweni Imara, Thabiti!

a Tafsiri ya Biblia International Standard Version inasema hivi kwenye mstari huo: “Hakuna jaribu lililowapata ninyi ambalo si la kawaida kwa wanadamu.”

b UFAFANUZI WA MANENO: Katika Biblia, mara nyingi neno “dhambi” linarejelea tendo fulani, kama vile kuiba, uzinzi, au kuua. (Kut. 20:​13-15; 1 Kor. 6:18) Hata hivyo, katika baadhi ya maandiko, “dhambi” inarejelea hali ambayo tumerithi tulipozaliwa, hata ingawa bado hatujafanya tendo lolote la dhambi.

c Ona kwamba kijana mwanamume anayetajwa katika Methali 7:​7-23 alifanya maamuzi madogo-madogo yasiyo ya hekima kabla ya kufanya uamuzi mkubwa usio na hekima uliosababisha afanye uasherati.

d MAELEZO YA PICHA: Kushoto: Akiwa ameketi kwenye mkahawa, ndugu kijana anawaona wanaume wawili wakionyeshana upendo. Kulia: Dada anaona watu wawili wakivuta sigara.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki