KAMAL VIRDEE | SIMULIZI LA MAISHA
“Nilitamani Sana Kuona Haki Ikitendeka”
Agosti 1973, mimi na dada zangu wawili tulihudhuria Kusanyiko la Kimataifa la “Ushindi wa Kimungu” huko Twickenham, Uingereza. Tukiwa huko tulikutana na Ndugu Edwin Skinner, aliyekuwa ametumikia akiwa mmishonari nchini India tangu 1926. Alipogundua kwamba tunazungumza Kipunjabi, alituuliza, “Mnafanya nini hapa? Njooni India!” Tulienda India na hapo ndipo nilipoanza kufanya kazi ya Ufalme katika eneo la Kipunjabi. Lakini acha kwanza niwasimulie kilichokuwa kimetokea kabla ya kukutana na Ndugu Skinner.
Nilizaliwa Aprili 1951, jijini Nairobi, Kenya. Wazazi wangu walikuwa wametoka India na walikuwa Wakalasinga. Kaka ya Baba yangu alipokufa, Baba alimwoa mke wake, hivyo akawa na wake wawili. Ingawa mama yangu alikuwa mke wa kwanza, hangeweza kufanya chochote kuhusu uamuzi huo. Mara nyingi, mama yangu mzazi na mama yangu wa kambo walipata watoto karibu wakati uleule. Kwa hiyo, nilikuwa na ndugu na dada kadhaa na sote tulilelewa pamoja kutia ndani binamu yetu mmoja—kwa ujumla tulikuwa watoto saba. Mwaka wa 1964, nilipokuwa tu nimefikisha umri wa miaka 13, baba yangu alikufa.
Kutafuta Haki
Nilipokuwa nikikua nilijionea ugomvi mwingi na upendeleo. Baadaye nilipojifunza Biblia niligundua kwamba maisha ya familia yetu yalikuwa kama tu ya Lea na Raheli katika Biblia. Niliona jinsi watu wa familia yangu walivyowatendea vibaya wafanyakazi wetu ambao walikuwa wa asili ya Kenya na kuwaona kuwa duni. Baba yangu alitaka tuwe marafiki na jirani zetu waliokuwa wametoka Ulaya na alidai kwamba tungeweza kujifunza kutoka kwao. Lakini alituambia tusishirikiane na Waafrika kwa sababu hawangetufundisha chochote. Alituambia pia tusiwe na urafiki na watu wa Pakistan na tuwaone kuwa maadui. Nilipenda haki sana na sikukubaliana na njia ya Baba yangu ya kuona mambo.
Dini ya Wakalasinga ilianzishwa mwishoni mwa karne ya 15 na Guru Nānak. Nilikubaliana na mafundisho ya Nānak kutia ndani wazo la kwamba kuna Mungu mmoja. Hata hivyo, nilipojionea jinsi Wakalasinga walivyotendeana isivyo haki, nilianza kujiuliza ikiwa dini hiyo ilikuwa ya kweli.
Hilo halikuwa jambo pekee lililonihangaisha. Dini ya Wakalasinga imekuwepo kwa karne kadhaa tu. Kwa hiyo, mara nyingi nilijiuliza: ‘Mambo yalikuwaje kabla ya hapo? Ni ipi iliyokuwa njia ya kwanza ya kumwabudu Mungu iliyokubalika kwake?’ Familia yetu ilikuwa na kalenda zenye picha za maguru 10 maarufu wa Wakalasinga. Lakini nilijiuliza: ‘Tunajuaje jinsi walivyoonekana? Kwa nini watu, kutia ndani familia yetu, wanainamia picha za maguru ilhali maguru wenyewe walifundisha kwamba tunapaswa kumwabudu Mungu mmoja wa kweli?’
Mwaka wa 1965, nikiwa na umri wa miaka 14, familia yetu ilihamia India. Maisha huko yalikuwa magumu kwa sababu hatukuwa na pesa nyingi. Mwaka mmoja baadaye, familia yetu ilianza kuhamia Uingereza hatua kwa hatua. Tulihama wawili-wawili na tukaanza kuishi katika jiji la Leicester.
Nikiwa na umri wa miaka 16, nilianza kufanya kazi mbalimbali za mkono mchana, na usiku nilienda shule ili kuendeleza masomo yangu ambayo yalikuwa yamesimama kwa muda. Lakini nilijionea ubaguzi kazini. Kwa mfano, wenyeji walilipwa vizuri zaidi kuliko wahamiaji. Kwa sababu nilitaka kila mtu atendewe kwa haki, niliamua kuwa mwanaharakati wa kutetea haki za wafanyakazi. Niliwachochea wafanyakazi wanawake ambao ni wahamiaji waandamane wakidai malipo sawa na wenyeji. Nilitamani sana kuona haki ikitendeka.
Kupata Suluhisho
Nilikutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza mwaka wa 1968. Mashahidi wawili wanaume walibisha mlango wetu na kuzungumza nami kuhusu ahadi ya Biblia ya kwamba Ufalme utaleta usawa kwa wote, jambo ambalo lilinivutia sana. Mmoja wa Mashahidi hao, alinitembelea tena akiwa na mke wake. Basi mimi, dada yangu Jaswinder, na dada yangu wa kambo Chani, tukaanza kujifunza Biblia. Baada ya kujifunza sura sita tu, tulisadiki kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli, kwamba Biblia ni neno lake, na kwamba Ufalme tu ndio utakaoleta haki ya kweli kwa wote.
Hata hivyo, familia yetu ilitupinga sana. Baba yangu alipokufa, ndugu yangu wa kambo akawa kichwa cha familia. Mama yetu wa kambo alianza kumchochea atupinge. Hivyo, ndugu yetu alianza kuwapiga dada zangu wadogo, Jaswinder na Chani, na hata nyakati nyingine aliwapiga mateke kwa viatu vyenye ncha ya chuma. Hata hivyo, hakuthubutu kunipiga kwa sababu nilikuwa na umri wa miaka 18 na alijua kwamba nina haki za kisheria, lakini aliwaonea dada zangu kwa sababu walikuwa wadogo. Siku moja alichukua Biblia, akaifungua, na kuiwasha moto, kisha akaisukuma usoni mwao na kuwaambia, “Mwambieni huyo Yehova wenu azime moto huu!” Kufikia wakati huo, tulikuwa tumehudhuria mikutano michache tu. Na tulifanya hivyo kisiri. Lakini tulitamani sana kumtumikia Mungu wa pekee wa kweli, Yehova. Hata hivyo, ilikuwa vigumu kumtumikia Yehova chini ya hali hizo. Kwa hiyo, tulianza kufanya mipango ya kutoroka nyumbani ili twende mahali salama. Tungefanya hivyo jinsi gani?
Tulianza kuhifadhi pesa kisiri. Tulichukua pesa za chakula cha mchana, za nauli, na pia sehemu ndogo ya mshahara wangu na tukaanza kuzihifadhi. Tulihifadhi sehemu ndogo ya mshahara wangu kwa sababu mama yangu wa kambo alinilazimisha nimpe mshahara wangu. Tulinunua masanduku matatu ya nguo na tukayaficha sehemu fulani mbali na nyumbani. Tulianza kuhifadhi nguo zetu hapo pole kwa pole. Mei 1972, Jaswinder alikuwa akikaribia umri wa miaka 18. Wakati huo, tulikuwa tumekusanya pauni 100 (dola 260 za Marekani). Hivyo, tulipanda treni na kwenda Penzance, kusini-magharibi mwa Uingereza. Baada ya kuwasili Penzance, tulitumia simu ya umma kuwapigia Mashahidi. Na walitukaribisha kwa uchangamfu. Kwa kuwa tulikusudia kuendelea kukaa katika eneo hilo, tulifanya kazi mbalimbali, kutia ndani kazi ya kusafisha samaki, ili tupate pesa za kulipia nyumba.
Tuliendelea kujifunza Biblia. Walimu wetu walikuwa Harry na Betty Briggs, wenzi wa ndoa waliokuwa na umri mkubwa. Septemba 1972, tulibatizwa katika kidimbwi kidogo kilichokuwa kwenye jukwaa la Jumba la Ufalme la Truro. Wakati huo bado tulikuwa mbali na nyumbani. Chani alianza upainia, na mimi na Jaswinder tulimtegemeza kifedha.
Kutumikia Eneo Lenye Uhitaji Mkubwa
Ingawa Harry na Betty walikuwa wanakaribia umri wa miaka 90, walikuwa wakienda kuhubiri kwa ukawaida kwenye Visiwa vya Scilly, karibu na pwani ya kusini-magharibi ya Uingereza. Mfano wao ulituchochea kuwaiga. Hivyo, baada ya kuzungumza na Ndugu Skinner mwaka wa 1973, kama nilivyosimulia hapo mwanzoni, tulijua jambo tulilopaswa kufanya.
Januari 1974, tuliamua kwenda New Delhi, India. Hivyo, tulinunua tiketi za ndege kwa ajili ya safari ya kwenda tu. Tulipofika, tulikutana na Ndugu Dick Cotterill aliyeturuhusu kuishi kwenye makao ya wamishonari kama wageni. Chani aliendelea na upainia, na mimi na Jaswinder tukaongeza muda tuliotumia katika utumishi.
Hatimaye, tuliombwa tutumikie kwenye jimbo la Punjab, lililo kaskazini-magharibi mwa India. Tulikaa kwa muda kwenye makao ya wamishonari yaliyokuwa katika jiji la Chandigarh, kisha tukakodi nyumba. Nilianza kutumikia nikiwa painia wa kawaida Septemba 1974, na mwaka wa 1975, nikaalikwa kutumikia nikiwa painia wa pekee. Kuhubiri kulinisaidia kutambua kwamba kulikuwa na uhitaji mkubwa wa machapisho ya Kipunjabi ambayo yangewasaidia watu wengi zaidi kujifunza kuhusu upendo na haki ya Yehova. Mwaka wa 1976, ofisi ya tawi ya India ilitualika sote watatu tusaidie katika kazi ya kutafsiri machapisho katika Kipunjabi. Kazi hiyo ilikuwa ngumu sana kwa sababu hatukuwa na kompyuta au taipureta. Tuliandika tafsiri yetu kwa mkono, kisha tulikagua kila sentensi, na kusoma tena tafsiri yenyewe ili kuhakikisha hakuna makosa. Baada ya hapo, tulipeleka makala zilizotafsiriwa kwenye duka la kuchapisha. Duka hilo lilitumia mashine za zamani, na tulihitaji kupanga herufi mojamoja kwa mkono ili kutokeza nakala ya mwisho.
Kutaniko letu huko Chandigarh, Punjab, India
Kuendelea Kuwa na Shangwe Licha ya Matatizo ya Kiafya
Hali zetu zilibadilika haraka sana. Jaswinder alikutana na ndugu fulani, na baadaye wakafunga ndoa na kuhamia nchini Kanada. Naye Chani alifunga ndoa na ndugu Mjerumani kutoka Marekani aliyekuwa ametembelea India, na wakahamia Marekani. Nami nilikuwa mgonjwa sana na nikarudi Uingereza Oktoba 1976. Mama yangu mzazi na ndugu yangu walikuwa wakiishi jijini Leicester. Ingawa hawakuwa Mashahidi, hawakupinga kweli, na kwa fadhili walikubali kunitunza. Iligunduliwa kwamba nina ugonjwa wa Evans. Ugonjwa huo hauwapati watu wengi na unasababisha kinga ya mwili kushambulia kimakosa chembe za damu na kuziharibu. Ugonjwa huo unahitaji matibabu mbalimbali, kutia ndani kuondoa bandama (wengu). Hivyo, nililazimika kuacha upainia.
Nilisali kwa Yehova kwa bidii na nikamwahidi kwamba nikipona, nitarudia utumishi wa wakati wote. Na nilifanya hivyo! Licha ya kwamba nilikabili matatizo ya kiafya mara kwa mara, nilihamia Wolverhampton mwaka wa 1978, na nikaendelea kufanya upainia katika eneo lililokuwa na watu wengi wanaozungumza Kipunjabi. Tuliandika kwa mkono mialiko ya kuwakaribisha watu mkutanoni, kisha tukaipeleka itolewe fotokopi. Tuliwapa watu wanaozungumza Kipunjabi, na tukawaalika wasikilize hotuba ya watu wote. Sasa kuna makutaniko matano na vikundi vitatu vya Kipunjabi nchini Uingereza.
Ofisi ya tawi ya Uingereza ilijua kwamba nilikuwa nimetumikia nikiwa mtafsiri wa Kipunjabi nchini India. Kwa hiyo, ofisi hiyo ya tawi ikawasiliana nami mwishoni mwa miaka ya 1980. Nilianza kujitolea kwenye Betheli ya London ili kusaidia kazi ya kutengeneza herufi na programu za kompyuta na pia kusaidia kuweka sheria kwa ajili ya uchapishaji wa machapisho yaliyofuata herufi za Gurmukhi. Nilikuwa na ratiba yenye mambo mengi. Nilifanya kazi ili kujiruzuku, nilimtunza mama yangu ambaye aliishi mbali kidogo nami, na pia nilijitolea Betheli. Lakini nilifurahia sana kufanya kazi Betheli.
Nikizoezwa kwenye Betheli ya London, mwishoni mwa miaka ya 1980
Septemba 1991, nilialikwa kuwa mshiriki wa familia ya Betheli, na nikapewa mgawo wa kutafsiri machapisho ya Biblia katika Kipunjabi. Sikutarajia kamwe kupata mgawo huo. Kwanza, nilihisi sina ustadi, pia nilikuwa nimepita umri ambao watu wangealikwa Betheli, na zaidi ya hayo nilikuwa na ugonjwa. Lakini Yehova alinipatia pendeleo hili la pekee. Ingawa nilifurahia kutumikia Betheli, matatizo ya kiafya yaliendelea kunisumbua. Mara nyingi nilikabiliana na suala la damu, na pia nilikuwa nikipata matibabu ya kemikali (chemotherapy) pamoja na matibabu mengine. Madaktari waliokuwa wakinitibu walivutiwa na maendeleo yangu ya kiafya hivi kwamba wakanialika kwenye semina iliyokuwa na madaktari wengine 40 katika hospitali kubwa jijini London. Nilizungumza kwa dakika 10 hivi kuhusu msimamo wangu wa kukataa kutiwa damu, kisha ndugu kutoka Dawati la Habari za Hospitali akajibu maswali ambayo yaliulizwa.
Dada zangu Jaswinder na Chani walinitegemeza katika kipindi hicho kigumu. Pia, ninathamini sana jinsi familia ya Betheli na marafiki wangu walivyonitunza na kunionyesha fadhili. Katika majaribu yangu yote, Yehova ameniimarisha na kuniwezesha kuendelea na mgawo wangu.—Zaburi 73:26.
Baraka ya Yehova Humtajirisha Mtu
Miaka 33 ambayo nimetumikia Betheli imeniwezesha ‘kuonja na kuona kwamba Yehova ni mwema.’ (Zaburi 34:8; Methali 10:22) Watu wenye umri mkubwa ambao wamedumisha uaminifu wananitia moyo sana. Nimefurahia sana kuona wengi kati ya wanafunzi wangu wa Biblia wanaozungumza Kipunjabi wakifanya maendeleo na kuwa watumishi washikamanifu wa Yehova. Nina uhusiano mzuri pamoja na washiriki wa karibu wa familia yangu. Mama yangu na ndugu yangu bado si Mashahidi, lakini mara nyingi mama yangu husema, “Unampenda sana Mungu.” Na nilipotaka kuondoka Betheli ili nimtunze mama yangu ambaye sasa amezeeka, ndugu yangu aliniambia, “Unafanya kazi muhimu. Baki huko.” Mama yangu anaishi katika nyumba ya kuwatunza wazee ambayo iko mbali na Betheli, lakini ninamtembelea mara nyingi niwezavyo.
Wakati wowote ninapokabili majaribu maishani, mimi hujiambia: ‘Usiogope, Kamal. Yehova ni ngao yako. Thawabu yako itakuwa kubwa sana.’ (Mwanzo 15:1) Ninamshukuru sana Yehova, “Mungu wa haki,” kwa kunisaidia kumjua tangu nikiwa msichana mdogo, na kunipatia kazi ambayo imefanya maisha yangu yawe yenye kuridhisha. (Isaya 30:18) Na ninatazamia kwa hamu wakati ambapo, “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24.
Nikiwa kwenye Betheli ya Chelmsford