IBOLYA BARTHA | SIMULIZI LA MAISHA
Nilimvuta Mume Wangu “Bila Neno”
Kuna mambo mengi mazuri yaliyofanya nimpende Yehova. Niliguswa moyo na upendo na uchangamfu wa Mashahidi wake na pia nilivutiwa na jinsi walivyofundisha kweli za Biblia. Nilipojifunza kwamba Mungu anawajali watu kikweli na kwamba atawapa maisha mazuri wakati ujao, nilifurahi sana. Hata hivyo, mume wangu hakupenda mambo niliyokuwa nikijifunza na hilo lilikuwa changamoto.
Siku ya harusi yetu
Nilizaliwa mwaka wa 1952 nchini Romania. Ingawa mama yangu alikuwa Shahidi aliyebatizwa, alikuwa asiyetenda. Kwa hiyo, sikuwahi kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Isitoshe, Romania ilikuwa chini ya utawala wa Kikomunisti. Hivyo, Mashahidi hawakuruhusiwa kuhubiri au kufanya kazi ya kuchapisha machapisho. Kwa hiyo, kufikia wakati nilipokuwa na miaka 36, sikumjua Yehova na sikujua Biblia inafundisha nini. Hata hivyo, mwaka wa 1988, mimi na István, mume wangu, tulipokuwa tukiishi katika jiji la Satu-Mare, jambo fulani lilitendeka na likabadili maisha yangu.
Mwaliko Ambao Singeweza Kukataa
Siku moja, mama yangu alinitembelea. Aliniambia hivi: “Ninaenda kumwona shangazi yako. Tunaweza kwenda sote? Baadaye tunaweza kwenda kufanya manunuzi pamoja.” Sikuwa na kazi nyingi, basi nikakubali twende.
Tulipofika nyumbani kwa shangazi niligundua kwamba kulikuwa na mkutano wa Mashahidi wa Yehova uliokuwa ukiendelea na kulikuwa na watu wengine tisa ambao walikuwa wakihudhuria. Tulipokuwa huko nikajua kwamba Mama alikuwa ameanza tena kutenda na kuwa Shahidi mwenye bidii. Mambo niliyosikia asubuhi hiyo kwenye mkutano yalinigusa moyo sana.
Mkutano ulipokwisha ndugu aliyekuwa akiongoza alinifikia na kujitambulisha. “Ninaitwa János. Niliona ulikuwa ukisikiliza kwa makini. Ulifurahia mambo uliyosikia?” Nilimwambia kwamba sijawahi kuhudhuria mkutano kama huo na ningependa kurudi tena. Akaniuliza, “Ungependa kujifunza Biblia?” Huo ulikuwa mwaliko ambao singeweza kukataa. Nilihisi kwamba Mungu alikuwa amenivuta kwa watu hawa.
Siku iliyofuata, János alinitambulisha kwa Ida, ambaye alianza kunifundisha Biblia. Hata hivyo, nilihofia jinsi István atakavyoitikia akigundua ninajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Nilijaribu mara kadhaa kumweleza kuhusu mambo niliyokuwa nikijifunza, lakini hakutaka kusikia. Nilijua hakuwa akifurahia mambo niliyokuwa nikifanya.
Licha ya hayo, niliendelea kujifunza Biblia na nikabatizwa Agosti 1989. Miezi minne baadaye, serikali ya Kikomunisti ilianguka nchini Romania na kiongozi wake akauawa.
Upinzani Waongezeka
Utawala ulipobadilika, kukawa na uhuru mwingi. Sasa, Mashahidi wa Yehova wangeweza kukutana na kuhubiri kwa uhuru. Hata hivyo, katika kisa changu, uhuru huu ulitokeza upinzani zaidi. István aliniambia, “Kile unachoamini hakinihusu, lakini sitaki kukuona ukihubiri nyumba kwa nyumba.”
Kwa kweli, singeacha kuhubiri. (Matendo 4:20) Hata hivyo, nilijaribu kufanya hivyo kwa busara. Lakini siku moja marafiki wa István waliniona nikihubiri nyumba kwa nyumba na wakamwambia. Nilipofika nyumbani, mume wangu alinifokea, “Unanidhalilisha mimi na familia yetu!” Kisha akaweka kisu shingoni mwangu akitishia kwamba ataniua ikiwa sitaacha kuhubiri.
Nilijaribu kuongea na István, na kumhakikishia kwamba ninampenda. Maneno yangu yalimtuliza kwa muda. Hata hivyo, nilipokataa kuhudhuria harusi ya mtu wa ukoo kwa sababu ingehusisha mambo ya kidini, alikasirika sana. Aliendelea kunitukana hata zaidi.
Kwa kusikitisha, nilihitaji kuvumilia hasira ya István kwa miaka 13. Katika kipindi hicho, alitishia kwamba atanipa talaka. Wakati mwingine angefunga nyumba na hangeniruhusu kuingia. Isitoshe, wakati mwingine angeniambia nichukue vitu vyangu niondoke.
Ni nini kilichonisaidia kuvumilia hali hiyo ngumu? Nilisali kwa Yehova na nikamwomba anisaidie niendelee kuwa mtulivu na kwa kweli nilihisi akinitegemeza. (Zaburi 55:22) Kutaniko pia lilinitegemeza sana. Wazee na dada wakomavu walinitia moyo nisikate tamaa na kuacha kumtumikia Yehova. Walinikumbusha Biblia inasema kwamba wake wanaweza kuwavuta waume zao “bila neno” kwa kuendelea kubaki imara na kuwa washikamanifu kwa Yehova. (1 Petro 3:1) Baada ya muda, nilijionea ukweli wa maneno hayo.
Mambo Yabadilika
Mwaka wa 2001, István alipatwa na ugonjwa wa kiharusi na hivyo hakuweza kutembea tena. Alilazwa hospitalini kwa zaidi ya mwezi mmoja kisha akaendelea na matibabu mengine kwa majuma kadhaa. Nilikuwa kando yake katika kipindi hicho chote. Nilimlisha, nikazungumza naye, na pia nikahakikisha alikuwa na kila kitu alichohitaji.
Ndugu na dada kutanikoni walikuja kumwona pia. István alijionea moja kwa moja jinsi ndugu na dada wanavyowaonyesha wengine upendo na kuwajali. Wengi walijitolea kutusaidia kazi nyumbani. Wazee pia waliendelea kutufariji na kututegemeza.
István aliguswa moyo alipoona ndugu na dada wakimtembelea na akaanza kujutia jinsi alivyokuwa amenitendea. Vilevile, aliona kwamba hakuna rafiki yake aliyekuja kumwona. Kwa hiyo, István aliporuhusiwa kutoka hospitalini alisema, “Ninataka kujifunza Biblia na kuwa Shahidi wa Yehova.” Nilitokwa na machozi ya furaha!
István alibatizwa Mei 2005. Kwa kuwa hangeweza kutembea, akina ndugu walimpeleka karibu na kidimbwi cha ubatizo kwa kiti cha magurudumu, kisha wakambeba na kumwingiza kwenye maji na kumbatiza. István alikuwa mwenye bidii sana katika kazi ya kuhubiri. Ninakumbuka jinsi tulivyofurahia kuhubiri pamoja. Hilo lilikuwa jambo la pekee. Hebu wazia, mwanamume ambaye alikuwa akinipinga kwa sababu ya kuhubiri kweli za Neno la Mungu, sasa alikuwa kando yangu akiwatangazia wengine habari njema kwa furaha!
István alimpenda sana Yehova na alitumia muda wake kujifunza na pia kukariri mistari ya Biblia. Alipenda kuzungumzia mistari hiyo pamoja na ndugu na dada kutanikoni. Alitumia fursa hizo kuwatia moyo.
Tukiwa pamoja na marafiki kwenye kusanyiko la eneo
Afya ya István iliendelea kuzorota. Ugonjwa wa kiharusi ulimpiga mara kadhaa na hatimaye akapoteza uwezo wake wa kuongea. Hali ilizidi kuwa mbaya na akawa hawezi kutoka kitandani. Je, hali hiyo ilimzuia kumtumikia Yehova? La hasha! Aliendelea kusoma na kujifunza kadiri ya uwezo wake. Ndugu na dada walipomtembelea, aliwasiliana nao kupitia kifaa cha kielektroni kilichokuwa na skrini. Kwa kweli, aliimarisha imani yao. Ndugu mmoja alisema hivi: “Ninapenda kumtembelea István. Sikuzote mimi hurudi nyumbani nikiwa na nguvu na nikiwa nimeburudishwa.”
Kwa kusikitisha, István alikufa Desemba 2015. Kumpoteza István kulinihuzunisha sana. Hata hivyo, pia nilihisi amani moyoni. Hii ni kwa sababu muda mrefu kabla ya kifo chake, István alikuwa amesitawisha uhusiano mzuri na Yehova. Jambo hilo linaniletea shangwe nyingi. István na mama yangu wako katika kumbukumbu ya Yehova. Ninatazamia kwa hamu kuwakumbatia tena na kuwakaribisha katika ulimwengu mpya wa Yehova wenye uadilifu.
Zaidi ya miaka 35 imepita tangu mimi na mama yangu tulipomtembelea shangazi na sitawahi kamwe kusahau siku hiyo. Sasa nina zaidi ya miaka 70 na ninatumikia nikiwa painia wa kawaida. Ninahisi hiyo ndiyo njia bora zaidi ya kumshukuru Yehova kwa yote aliyonitendea. (Zaburi 116:12) Alinisaidia niendelee kuwa mshikamanifu na mtulivu nilipokabili upinzani. Na ingawa nilikabili upinzani, nilijifunza kwamba hali zinaweza kubadilika. Nilifaulu kumvuta mume wangu bila neno ingawa sikutarajia mambo yatakuwa hivyo.