Jumapili, Oktoba 26
Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.—Yak. 4:6.
Biblia inawataja wanawake wengi wa pekee waliompenda Yehova na kumtumikia. Wanawake hao walikuwa “wenye kiasi katika mazoea” na “waaminifu katika mambo yote.” (1 Tim. 3:11) Kwa kuongezea, akina dada vijana wanaweza kupata katika kutaniko lao wanawake Wakristo wakomavu ambao ni mfano mzuri wa kuigwa. Akina dada vijana, je, mnaweza kutafuta kutanikoni wanawake Wakristo wakomavu ambao mnaweza kuiga mfano wao? Chunguzeni sifa zao zinazovutia; kisha mfikirie jinsi mnavyoweza kuonyesha sifa hizo. Sifa muhimu ya kuwa Mkristo mkomavu ni unyenyekevu. Ikiwa mwanamke ni mnyenyekevu, atafurahia uhusiano mzuri na Yehova na watu wengine pia. Kwa mfano, mwanamke anayempenda Yehova, kwa unyenyekevu anachagua kuunga mkono kanuni ya ukichwa ambayo Baba yake wa mbinguni alianzisha. (1 Kor. 11:3) Kanuni hiyo inatumika kwa njia hususa katika kutaniko na katika familia pia. w23.12 18-19 ¶3-5
Jumatatu, Oktoba 27
Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.—Efe. 5:28.
Yehova anatarajia mume ampende mke wake na kumtunza kimwili, kihisia, na kiroho. Kusitawisha uwezo wa kufikiri, kuwaheshimu wanawake, na kuwa mwenye kutegemeka, kutakusaidia ukiwa mwenzi wa ndoa. Baada ya kufunga ndoa, unaweza kuwa baba. Unaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kuwa baba mzuri? (Efe. 6:4) Yehova alimwambia waziwazi Mwana wake, Yesu, kwamba anampenda na kumkubali. (Mt. 3:17) Ikiwa utakuwa baba, hakikisha kuwa unawahakikishia kwa ukawaida watoto wako kwamba unawapenda. Wapongeze mara kwa mara kwa mambo mazuri wanayofanya. Akina baba wanaoiga mfano wa Yehova wanawasaidia watoto wao kuwa wanaume na wanawake Wakristo wakomavu. Unaweza kujitayarisha sasa kwa ajili ya jukumu hilo kwa kuwajali kwa upendo watu katika familia yenu na katika kutaniko na kwa kujifunza kuwaambia kwamba unawapenda na unawathamini.—Yoh. 15:9. w23.12 28-29 ¶17-18
Jumanne, Oktoba 28
[Yehova] ndiye tegemeo imara la nyakati zako.—Isa. 33:6.
Ingawa sisi ni watumishi waaminifu wa Yehova, tunakabili hali ngumu na magonjwa kama watu wengine. Huenda pia tukahitaji kuvumilia upinzani au mateso kutoka kwa watu wanaowachukia watu wa Mungu. Ingawa Yehova hatukingi tusipatwe na hali hizo ngumu, anaahidi kutusaidia. (Isa. 41:10) Kwa msaada wake, tunaweza kudumisha shangwe yetu, kufanya maamuzi mazuri, na kuendelea kuwa waaminifu licha ya kukabili hali ngumu. Yehova anaahidi kutupatia kile ambacho Biblia inakiita “amani ya Mungu.” (Flp. 4:6, 7) Amani ya Mungu inarejelea utulivu na amani ya akilini na moyoni tunayopata kwa sababu ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Amani hiyo ‘inazidi uelewaji wote’; inastaajabisha sana kuliko tunavyoweza kuwazia. Kwa mfano, umewahi kuhisi umepata utulivu sana baada ya kusali kwa bidii kwa Yehova? Utulivu huo ni “amani ya Mungu.” w24.01 20 ¶2; 21 ¶4