Jumatatu, Oktoba 27
Waume wanapaswa kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.—Efe. 5:28.
Yehova anatarajia mume ampende mke wake na kumtunza kimwili, kihisia, na kiroho. Kusitawisha uwezo wa kufikiri, kuwaheshimu wanawake, na kuwa mwenye kutegemeka, kutakusaidia ukiwa mwenzi wa ndoa. Baada ya kufunga ndoa, unaweza kuwa baba. Unaweza kujifunza nini kutoka kwa Yehova kuhusu kuwa baba mzuri? (Efe. 6:4) Yehova alimwambia waziwazi Mwana wake, Yesu, kwamba anampenda na kumkubali. (Mt. 3:17) Ikiwa utakuwa baba, hakikisha kuwa unawahakikishia kwa ukawaida watoto wako kwamba unawapenda. Wapongeze mara kwa mara kwa mambo mazuri wanayofanya. Akina baba wanaoiga mfano wa Yehova wanawasaidia watoto wao kuwa wanaume na wanawake Wakristo wakomavu. Unaweza kujitayarisha sasa kwa ajili ya jukumu hilo kwa kuwajali kwa upendo watu katika familia yenu na katika kutaniko na kwa kujifunza kuwaambia kwamba unawapenda na unawathamini.—Yoh. 15:9. w23.12 28-29 ¶17-18
Jumanne, Oktoba 28
[Yehova] ndiye tegemeo imara la nyakati zako.—Isa. 33:6.
Ingawa sisi ni watumishi waaminifu wa Yehova, tunakabili hali ngumu na magonjwa kama watu wengine. Huenda pia tukahitaji kuvumilia upinzani au mateso kutoka kwa watu wanaowachukia watu wa Mungu. Ingawa Yehova hatukingi tusipatwe na hali hizo ngumu, anaahidi kutusaidia. (Isa. 41:10) Kwa msaada wake, tunaweza kudumisha shangwe yetu, kufanya maamuzi mazuri, na kuendelea kuwa waaminifu licha ya kukabili hali ngumu. Yehova anaahidi kutupatia kile ambacho Biblia inakiita “amani ya Mungu.” (Flp. 4:6, 7) Amani ya Mungu inarejelea utulivu na amani ya akilini na moyoni tunayopata kwa sababu ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Amani hiyo ‘inazidi uelewaji wote’; inastaajabisha sana kuliko tunavyoweza kuwazia. Kwa mfano, umewahi kuhisi umepata utulivu sana baada ya kusali kwa bidii kwa Yehova? Utulivu huo ni “amani ya Mungu.” w24.01 20 ¶2; 21 ¶4
Jumatano, Oktoba 29
Nafsi yangu na imsifu Yehova; kila kitu kilicho ndani yangu na kilisifu jina lake takatifu.—Zab. 103:1.
Kwa kuwa wanampenda Mungu, watu waaminifu wanachochewa kulisifu jina lake kwa moyo wote. Mfalme Daudi alielewa kwamba kulisifu jina la Yehova ni sawa na kumsifu Yehova mwenyewe. Jina la Yehova linahusisha sifa yake nzuri, hivyo linatukumbusha sifa zake zote maridadi na matendo yake yenye kustaajabisha. Daudi aliliona jina la Baba yake kuwa takatifu na alitamani kulisifu. Alitaka kufanya hivyo na “kila kitu kilicho ndani” yake—yaani, kwa moyo wote. Vivyo hivyo, Walawi waliongoza katika kumsifu Yehova. Kwa unyenyekevu, walikubali kwamba maneno yao hayangeweza kamwe kueleza kikamili sifa ambayo jina hilo takatifu linastahili. (Neh. 9:5) Hapana shaka kwamba sifa hizo za kutoka moyoni zilimletea shangwe Yehova. w24.02 9 ¶6