Jumanne, Oktoba 28
[Yehova] ndiye tegemeo imara la nyakati zako.—Isa. 33:6.
Ingawa sisi ni watumishi waaminifu wa Yehova, tunakabili hali ngumu na magonjwa kama watu wengine. Huenda pia tukahitaji kuvumilia upinzani au mateso kutoka kwa watu wanaowachukia watu wa Mungu. Ingawa Yehova hatukingi tusipatwe na hali hizo ngumu, anaahidi kutusaidia. (Isa. 41:10) Kwa msaada wake, tunaweza kudumisha shangwe yetu, kufanya maamuzi mazuri, na kuendelea kuwa waaminifu licha ya kukabili hali ngumu. Yehova anaahidi kutupatia kile ambacho Biblia inakiita “amani ya Mungu.” (Flp. 4:6, 7) Amani ya Mungu inarejelea utulivu na amani ya akilini na moyoni tunayopata kwa sababu ya kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Amani hiyo ‘inazidi uelewaji wote’; inastaajabisha sana kuliko tunavyoweza kuwazia. Kwa mfano, umewahi kuhisi umepata utulivu sana baada ya kusali kwa bidii kwa Yehova? Utulivu huo ni “amani ya Mungu.” w24.01 20 ¶2; 21 ¶4
Jumatano, Oktoba 29
Nafsi yangu na imsifu Yehova; kila kitu kilicho ndani yangu na kilisifu jina lake takatifu.—Zab. 103:1.
Kwa kuwa wanampenda Mungu, watu waaminifu wanachochewa kulisifu jina lake kwa moyo wote. Mfalme Daudi alielewa kwamba kulisifu jina la Yehova ni sawa na kumsifu Yehova mwenyewe. Jina la Yehova linahusisha sifa yake nzuri, hivyo linatukumbusha sifa zake zote maridadi na matendo yake yenye kustaajabisha. Daudi aliliona jina la Baba yake kuwa takatifu na alitamani kulisifu. Alitaka kufanya hivyo na “kila kitu kilicho ndani” yake—yaani, kwa moyo wote. Vivyo hivyo, Walawi waliongoza katika kumsifu Yehova. Kwa unyenyekevu, walikubali kwamba maneno yao hayangeweza kamwe kueleza kikamili sifa ambayo jina hilo takatifu linastahili. (Neh. 9:5) Hapana shaka kwamba sifa hizo za kutoka moyoni zilimletea shangwe Yehova. w24.02 9 ¶6
Alhamisi, Oktoba 30
Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika mwendo huohuo.—Flp. 3:16.
Yehova hataona kwamba umeshindwa kwa kukosa kutimiza lengo ambalo linapita uwezo wako. (2 Kor. 8:12) Ona kipingamizi hicho kuwa fursa ya kujifunza. Kumbuka mambo ambayo tayari umetimiza. Biblia inasema hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi [yako].” (Ebr. 6:10) Basi wewe pia hupaswi kusahau. Fikiria kuhusu mambo ambayo tayari umetimiza—iwe ni kusitawisha urafiki pamoja na Yehova, kuwaambia wengine kumhusu, au kubatizwa. Kama vile ulivyofanya maendeleo na kutimiza malengo ya kiroho wakati uliopita, unaweza kuendelea kufanya maendeleo ili kutimiza lengo lako sasa. Kwa msaada wa Yehova, unaweza kutimiza lengo lako. Unapoendelea kufanyia kazi lengo lako la kiroho, usisahau kufurahia kuona jinsi Yehova anavyokusaidia na kukubariki unapojitahidi kutimiza lengo lako. (2 Kor. 4:7) Usipokufa moyo, utapata baraka kubwa hata zaidi.—Gal. 6:9. w23.05 31 ¶16-18