Jumatano, Oktoba 29
Nafsi yangu na imsifu Yehova; kila kitu kilicho ndani yangu na kilisifu jina lake takatifu.—Zab. 103:1.
Kwa kuwa wanampenda Mungu, watu waaminifu wanachochewa kulisifu jina lake kwa moyo wote. Mfalme Daudi alielewa kwamba kulisifu jina la Yehova ni sawa na kumsifu Yehova mwenyewe. Jina la Yehova linahusisha sifa yake nzuri, hivyo linatukumbusha sifa zake zote maridadi na matendo yake yenye kustaajabisha. Daudi aliliona jina la Baba yake kuwa takatifu na alitamani kulisifu. Alitaka kufanya hivyo na “kila kitu kilicho ndani” yake—yaani, kwa moyo wote. Vivyo hivyo, Walawi waliongoza katika kumsifu Yehova. Kwa unyenyekevu, walikubali kwamba maneno yao hayangeweza kamwe kueleza kikamili sifa ambayo jina hilo takatifu linastahili. (Neh. 9:5) Hapana shaka kwamba sifa hizo za kutoka moyoni zilimletea shangwe Yehova. w24.02 9 ¶6
Alhamisi, Oktoba 30
Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika mwendo huohuo.—Flp. 3:16.
Yehova hataona kwamba umeshindwa kwa kukosa kutimiza lengo ambalo linapita uwezo wako. (2 Kor. 8:12) Ona kipingamizi hicho kuwa fursa ya kujifunza. Kumbuka mambo ambayo tayari umetimiza. Biblia inasema hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi [yako].” (Ebr. 6:10) Basi wewe pia hupaswi kusahau. Fikiria kuhusu mambo ambayo tayari umetimiza—iwe ni kusitawisha urafiki pamoja na Yehova, kuwaambia wengine kumhusu, au kubatizwa. Kama vile ulivyofanya maendeleo na kutimiza malengo ya kiroho wakati uliopita, unaweza kuendelea kufanya maendeleo ili kutimiza lengo lako sasa. Kwa msaada wa Yehova, unaweza kutimiza lengo lako. Unapoendelea kufanyia kazi lengo lako la kiroho, usisahau kufurahia kuona jinsi Yehova anavyokusaidia na kukubariki unapojitahidi kutimiza lengo lako. (2 Kor. 4:7) Usipokufa moyo, utapata baraka kubwa hata zaidi.—Gal. 6:9. w23.05 31 ¶16-18
Ijumaa, Oktoba 31
Baba mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu mmenipenda na mmeamini kwamba nilikuja nikiwa mwakilishi wa Mungu.—Yoh. 16:27.
Yehova anafurahi kuwaonyesha kibali chake wale anaowapenda. Maandiko yanataja pindi mbili ambapo Yehova alimwambia Yesu kwamba yeye ni Mwana wake mpendwa, anayemkubali. (Mt. 3:17; 17:5) Je, ungependa kumsikia Yehova akikuhakikishia kwamba una kibali chake? Yehova hazungumzi nasi moja kwa moja, lakini anazungumza nasi kupitia Neno lake. Tunaposoma katika vitabu vya Injili maneno yenye upendo ya Yesu aliyowaambia wanafunzi wake, ni kana kwamba tunamsikia Yehova akizungumza nasi. Yesu aliiga kikamilifu utu wa Baba yake. Hivyo, tunaposoma kwamba Yesu aliwaambia wafuasi wake waaminifu ambao si wakamilifu kwamba amewakubali, tunaweza kuwazia Yehova akituambia maneno hayohayo. (Yoh. 15:9, 15) Majaribu yanapotokea, hayamaanishi kwamba tumepoteza kibali cha Mungu. Badala yake, yanatupatia fursa ya kuthibitisha kina cha upendo wetu kwa Mungu na kwamba tunamtumaini.—Yak. 1:12. w24.03 28 ¶10-11