Jumatano, Julai 9
Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, nikumbuke, tafadhali, na kunitia nguvu.—Amu. 16:28.
Unafikiria kuhusu nini unaposikia jina Samsoni? Inawezekana kwamba unamfikiria mwanamume aliyekuwa na nguvu sana. Hilo ni kweli. Lakini Samsoni alifanya uamuzi mbaya uliomsababishia mateso mengi. Hata hivyo, Yehova alikazia fikira mambo yote ambayo Samsoni alikuwa amefanya ili kumtumikia kwa uaminifu, na alitia ndani mfano wa Samsoni katika Biblia ili kutunufaisha. Yehova alimtumia Samsoni kutimiza mambo yenye kustaajabisha ili kuwasaidia watu aliowachagua, Waisraeli. Karne nyingi baada ya kifo cha Samsoni, Yehova alimwongoza mtume Paulo kutia ndani jina la Samsoni kwenye orodha ya wanaume waliokuwa na imani ya pekee. (Ebr. 11:32-34) Mfano wa Samsoni unaweza kututia moyo. Alimtegemea Yehova, hata alipokabili hali ngumu. Tunaweza kutiwa moyo na pia kujifunza masomo fulani kutokana na mfano wake. w23.09 2 ¶1-2
Alhamisi, Julai 10
Mjulisheni Mungu maombi yenu.—Flp. 4:6.
Tunaweza kusitawisha sifa ya uvumilivu kwa kuzungumza na Yehova kwa ukawaida kuhusu mambo yanayotuhangaisha. (1 The. 5:17) Labda sasa hukabiliani na jaribu kali. Hata hivyo, je, wewe hutafuta mwongozo wa Yehova kila mara unapokasirika, unapochanganyikiwa, au kulemewa na hisia? Ikiwa sasa unamwomba Mungu msaada kwa ukawaida unapokabiliana na changamoto za kila siku, hutasita kufanya hivyo utakapokabili changamoto kubwa zaidi wakati ujao. Utakuwa na uhakika kwamba Yehova anajua kihususa wakati na jinsi ya kukusaidia. (Zab. 27:1, 3) Itakuwa rahisi zaidi kwetu kuvumilia dhiki kuu wakati ujao ikiwa sasa tunavumilia majaribu. (Rom. 5:3) Kwa nini tunasema hivyo? Ndugu wengi wametambua kwamba kila jaribu la imani walilovumilia liliwasaidia kuvumilia jaribu lililofuata. Uvumilivu uliwasaidia kuimarisha imani yao kwamba Yehova yuko tayari na anataka kuwasaidia. Kisha imani yao iliwasaidia kuvumilia jaribu lililofuata.—Yak. 1:2-4. w23.07 3 ¶7-8
Ijumaa, Julai 11
Nitakutendea . . . kwa fadhili.—Mwa. 19:21.
Unyenyekevu na huruma ya Yehova humchochea kuwa mwenye usawaziko. Kwa mfano, Yehova alionyesha unyenyekevu kabla ya kuharibu watu waovu huko Sodoma. Kupitia malaika wake, Yehova alimwagiza Loti mwadilifu akimbilie kwenye eneo lenye milima. Loti aliogopa kwenda huko. Basi, akaomba kwamba yeye na familia yake waruhusiwe kukimbilia huko Soari, mji mdogo ambao ulipaswa kuharibiwa. Yehova angeweza kusisitiza kwamba Loti anapaswa kufuata kikamili maagizo yaliyotolewa. Badala yake, alikubali ombi la Loti, ingawa hilo lilimaanisha kwamba mji wa Soari haungeharibiwa. (Mwa. 19:18-22) Karne nyingi baadaye, Yehova aliwaonyesha huruma wakaaji wa Ninawi. Alimtuma nabii Yona atangaze kuhusu uharibifu ambao ungelipata jiji hilo na wakaaji wake waovu. Lakini Waninawi walipotubu, Yehova aliwahurumia, naye hakuharibu jiji hilo.—Yona 3:1, 10; 4:10, 11. w23.07 21 ¶5