Alhamisi, Julai 10
Mjulisheni Mungu maombi yenu.—Flp. 4:6.
Tunaweza kusitawisha sifa ya uvumilivu kwa kuzungumza na Yehova kwa ukawaida kuhusu mambo yanayotuhangaisha. (1 The. 5:17) Labda sasa hukabiliani na jaribu kali. Hata hivyo, je, wewe hutafuta mwongozo wa Yehova kila mara unapokasirika, unapochanganyikiwa, au kulemewa na hisia? Ikiwa sasa unamwomba Mungu msaada kwa ukawaida unapokabiliana na changamoto za kila siku, hutasita kufanya hivyo utakapokabili changamoto kubwa zaidi wakati ujao. Utakuwa na uhakika kwamba Yehova anajua kihususa wakati na jinsi ya kukusaidia. (Zab. 27:1, 3) Itakuwa rahisi zaidi kwetu kuvumilia dhiki kuu wakati ujao ikiwa sasa tunavumilia majaribu. (Rom. 5:3) Kwa nini tunasema hivyo? Ndugu wengi wametambua kwamba kila jaribu la imani walilovumilia liliwasaidia kuvumilia jaribu lililofuata. Uvumilivu uliwasaidia kuimarisha imani yao kwamba Yehova yuko tayari na anataka kuwasaidia. Kisha imani yao iliwasaidia kuvumilia jaribu lililofuata.—Yak. 1:2-4. w23.07 3 ¶7-8
Ijumaa, Julai 11
Nitakutendea . . . kwa fadhili.—Mwa. 19:21.
Unyenyekevu na huruma ya Yehova humchochea kuwa mwenye usawaziko. Kwa mfano, Yehova alionyesha unyenyekevu kabla ya kuharibu watu waovu huko Sodoma. Kupitia malaika wake, Yehova alimwagiza Loti mwadilifu akimbilie kwenye eneo lenye milima. Loti aliogopa kwenda huko. Basi, akaomba kwamba yeye na familia yake waruhusiwe kukimbilia huko Soari, mji mdogo ambao ulipaswa kuharibiwa. Yehova angeweza kusisitiza kwamba Loti anapaswa kufuata kikamili maagizo yaliyotolewa. Badala yake, alikubali ombi la Loti, ingawa hilo lilimaanisha kwamba mji wa Soari haungeharibiwa. (Mwa. 19:18-22) Karne nyingi baadaye, Yehova aliwaonyesha huruma wakaaji wa Ninawi. Alimtuma nabii Yona atangaze kuhusu uharibifu ambao ungelipata jiji hilo na wakaaji wake waovu. Lakini Waninawi walipotubu, Yehova aliwahurumia, naye hakuharibu jiji hilo.—Yona 3:1, 10; 4:10, 11. w23.07 21 ¶5
Jumamosi, Julai 12
Walimuua [Yehoashi] . . . , lakini hawakumzika katika makaburi ya wafalme.—2 Nya. 24:25.
Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Yehoashi? Alikuwa kama mti wenye mizizi mifupi ambao ulitegemezwa na nguzo, nguzo hiyo ilipoondolewa, yaani, Yehoyada alipokufa, upepo wa uasi-imani ulivuma na kumwangusha Yehoashi. Hilo ni somo lenye nguvu kwamba hatupaswi kumwogopa Mungu kwa sababu tu ya kuchochewa na Wakristo wenzetu, kutia ndani watu wa familia yetu. Ili tuendelee kuwa wenye nguvu kiroho, ni lazima tuimarishe ujitoaji wetu kimungu na woga wetu kumwelekea Mungu kwa kujifunza kwa ukawaida, kutafakari, na kusali. (Yer. 17:7, 8; Kol. 2:6, 7) Yehova hadai mengi kutoka kwetu. Jambo ambalo anataka tufanye linatajwa kwenye andiko la Mhubiri 12:13, linalosema: “Mwogope Mungu wa kweli na ushike amri zake, kwa maana huu ndio wajibu wote wa mwanadamu.” Ikiwa tutamwogopa Mungu, tutafaulu kukabiliana na majaribu ya wakati ujao na kusimama imara. Hakuna kitu chochote kitakachoharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. w23.06 19 ¶17-19