Ijumaa, Julai 18
Alitufanya tuwe ufalme, makuhani kwa Mungu na Baba yake.—Ufu. 1:6.
Idadi hususa ya wanafunzi wa Kristo wametiwa mafuta kwa roho takatifu, nao wana uhusiano wa pekee pamoja na Yehova. Wakristo hao 144,000 watatumikia wakiwa makuhani mbinguni pamoja na Yesu. (Ufu. 14:1) Patakatifu pa hema la ibada panafananisha hali yao ya kuzaliwa kwa roho na kuwa wana wa Mungu wakiwa bado duniani. (Rom. 8:15-17) Patakatifu Zaidi pa hema la ibada panafananisha mbinguni, ambako Yehova anaishi. “Pazia” lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi lilifananisha mwili wa kibinadamu wa Yesu ambao ulikuwa kizuizi cha kuingia mbinguni akiwa Kuhani Mkuu sana wa hekalu la kiroho. Kwa kuutoa uhai wake wa kibinadamu uwe dhabihu kwa ajili ya wanadamu, Yesu alifungua njia ya uhai wa mbinguni kwa ajili ya Wakristo watiwa-mafuta. Ili wapokee thawabu yao ya mbinguni, ni lazima wao pia wavue miili yao ya kibinadamu.—Ebr. 10:19, 20; 1 Kor. 15:50. w23.10 28 ¶13
Jumamosi, Julai 19
Nitakosa wakati nikiendelea kusimulia kuhusu Gideoni.—Ebr. 11:32.
Gideoni alijibu kwa upole Waefraimu walipomkosoa. (Amu. 8:1-3) Hakujibu kwa hasira. Alionyesha unyenyekevu wa akili kwa kusikiliza mahangaiko yao, na kwa busara alifaulu kutuliza hali hiyo. Wazee wenye hekima wanamwiga Gideoni kwa kusikiliza kwa makini na kujibu kwa upole wanapokosolewa. (Yak. 3:13) Wanapofanya hivyo, wanachangia amani kutanikoni. Gideoni aliposifiwa kwa kuwashinda Wamidiani, alimwelekezea Yehova sifa. (Amu. 8:22, 23) Wazee wanawezaje kumwiga Gideoni? Wanapaswa kumsifu Yehova kwa mambo wanayotimiza. (1 Kor. 4:6, 7) Kwa mfano, mzee anaposifiwa kwa sababu ya uwezo wake wa kufundisha, anaweza kusema kwamba chanzo cha mwongozo huo ni Neno la Mungu, na sisi sote tunapata mazoezi katika tengenezo la Yehova. Nyakati nyingine, wazee wanaweza kujichunguza ili kuona kama wanajielekezea fikira. w23.06 4 ¶7-8
Jumapili, Julai 20
Mawazo yangu si mawazo yenu.—Isa. 55:8.
Ikiwa sala yetu haijibiwi, huenda tukahitaji kujiuliza, ‘Je, ninasali kuhusu jambo linalofaa?’ Mara nyingi, huenda tukafikiri kwamba tunajua jambo ambalo linatufaa zaidi. Lakini inawezekana mambo tunayoomba hata yasitunufaishe. Ikiwa tunasali kuhusu tatizo fulani, huenda kukawa na suluhisho bora zaidi kuliko lile tunaloomba. Na labda baadhi ya mambo tunayoomba hayapatani na mapenzi ya Yehova. (1 Yoh. 5:14) Kwa mfano, fikiria mfano wa wazazi ambao walimwomba Yehova amsaidie mtoto wao abaki katika kweli. Hilo linaonekana kuwa ombi linalofaa. Hata hivyo, Yehova hamlazimishi yeyote kati yetu amtumikie. Anataka kila mmoja wetu, kutia ndani watoto wetu, wachague kumwabudu yeye. (Kum. 10:12, 13; 30:19, 20) Hivyo, wazazi wanaweza kumwomba Yehova awasaidie kugusa moyo wa mtoto wao ili aweze kuchochewa kumpenda Yehova na kuwa rafiki Yake.—Met. 22:6; Efe. 6:4. w23.11 21 ¶5; 23 ¶12