Jumamosi, Julai 19
Nitakosa wakati nikiendelea kusimulia kuhusu Gideoni.—Ebr. 11:32.
Gideoni alijibu kwa upole Waefraimu walipomkosoa. (Amu. 8:1-3) Hakujibu kwa hasira. Alionyesha unyenyekevu wa akili kwa kusikiliza mahangaiko yao, na kwa busara alifaulu kutuliza hali hiyo. Wazee wenye hekima wanamwiga Gideoni kwa kusikiliza kwa makini na kujibu kwa upole wanapokosolewa. (Yak. 3:13) Wanapofanya hivyo, wanachangia amani kutanikoni. Gideoni aliposifiwa kwa kuwashinda Wamidiani, alimwelekezea Yehova sifa. (Amu. 8:22, 23) Wazee wanawezaje kumwiga Gideoni? Wanapaswa kumsifu Yehova kwa mambo wanayotimiza. (1 Kor. 4:6, 7) Kwa mfano, mzee anaposifiwa kwa sababu ya uwezo wake wa kufundisha, anaweza kusema kwamba chanzo cha mwongozo huo ni Neno la Mungu, na sisi sote tunapata mazoezi katika tengenezo la Yehova. Nyakati nyingine, wazee wanaweza kujichunguza ili kuona kama wanajielekezea fikira. w23.06 4 ¶7-8
Jumapili, Julai 20
Mawazo yangu si mawazo yenu.—Isa. 55:8.
Ikiwa sala yetu haijibiwi, huenda tukahitaji kujiuliza, ‘Je, ninasali kuhusu jambo linalofaa?’ Mara nyingi, huenda tukafikiri kwamba tunajua jambo ambalo linatufaa zaidi. Lakini inawezekana mambo tunayoomba hata yasitunufaishe. Ikiwa tunasali kuhusu tatizo fulani, huenda kukawa na suluhisho bora zaidi kuliko lile tunaloomba. Na labda baadhi ya mambo tunayoomba hayapatani na mapenzi ya Yehova. (1 Yoh. 5:14) Kwa mfano, fikiria mfano wa wazazi ambao walimwomba Yehova amsaidie mtoto wao abaki katika kweli. Hilo linaonekana kuwa ombi linalofaa. Hata hivyo, Yehova hamlazimishi yeyote kati yetu amtumikie. Anataka kila mmoja wetu, kutia ndani watoto wetu, wachague kumwabudu yeye. (Kum. 10:12, 13; 30:19, 20) Hivyo, wazazi wanaweza kumwomba Yehova awasaidie kugusa moyo wa mtoto wao ili aweze kuchochewa kumpenda Yehova na kuwa rafiki Yake.—Met. 22:6; Efe. 6:4. w23.11 21 ¶5; 23 ¶12
Jumatatu, Julai 21
Endeleeni kufarijiana.—1 The. 4:18.
Kwa nini kuwafariji wengine ni njia muhimu ya kuwaonyesha kwamba tunawapenda? Kulingana na rejeo fulani la Biblia, neno “kufarijiana” ambalo Paulo alitumia linamaanisha “kusimama kando ya mtu na kumtia moyo anapopata majaribu makali.” Hivyo, tunapotoa faraja tunamsaidia mwabudu mwenzetu anayekabili hali ngumu, asimame na kuendelea kutembea katika barabara ya uzima. Kila mara tunapomfariji ndugu au dada yetu, tunamwonyesha upendo mwabudu mwenzetu. (2 Kor. 7:6, 7, 13) Kuonyesha huruma na kufariji ni sifa zinazohusiana kwa ukaribu. Kwa njia gani? Mtu mwenye huruma huchochewa kuwafariji wengine na kujitahidi kuwapunguzia mateso yao. Hivyo, kwanza tunaonyesha huruma; kisha tunawafariji wengine. Ona jinsi Paulo anavyohusianisha huruma ya Yehova na faraja anayotoa. Paulo anamfafanua Yehova kuwa “Baba wa rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.”—2 Kor. 1:3. w23.11 9-10 ¶8-10