-
Wageni Wakusanywa Kwenye Nyumba ya Mungu ya SalaUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Faraja kwa Mgeni na Towashi
6. Sasa fikira zinaelekezwa kwenye vikundi gani viwili?
6 Sasa Yehova anahutubia vikundi viwili vinavyotaka kumtumikia, lakini vikundi hivyo vinahesabiwa kuwa havistahili kuingia katika kutaniko la Kiyahudi chini ya Sheria ya Kimusa. Tunasoma hivi: “Mgeni, aambatanaye na BWANA, asiseme hivi, Hakika yake BWANA atanitenga na watu wake; wala towashi asiseme, Mimi ni mti mkavu.” (Isaya 56:3) Hofu ya mgeni ni kwamba uhusiano wake na Israeli utakatiliwa mbali. Naye towashi ana wasiwasi kwamba hatapata kamwe watoto wa kuendeleza jina lake. Vikundi vyote viwili vinapaswa kuwa na moyo mkuu. Kabla hatujaona sababu, acheni tuchunguze vikundi hivyo vina msimamo gani chini ya Sheria kuhusiana na taifa la Israeli.
7. Sheria inawawekea mipaka gani wageni walio katika Israeli?
7 Wageni wasiotahiriwa hawakubaliwi kushiriki katika ibada pamoja na Israeli. Kwa mfano, hawaruhusiwi kushiriki kula sikukuu ya Kupitwa. (Kutoka 12:43) Wageni ambao hawavunji sheria za nchi kwa kuzipuuza wanafurahia kutendewa haki na kuonyeshwa ukaribishaji, lakini uhusiano wao na taifa hilo si wa kudumu. Ni kweli kwamba wengine wao wanaikubali Sheria kabisa, na wale ambao ni wanaume wanaonyesha hivyo kwa kutahiriwa. Ndipo sasa wanakuwa waongofu wenye pendeleo la kuabudu katika ua wa nyumba ya Yehova, na wanaonwa kuwa sehemu ya kutaniko la Israeli. (Mambo ya Walawi 17:10-14; 20:2; 24:22) Ingawa hivyo, hata waongofu si washiriki kamili katika agano la Yehova pamoja na Israeli, na hawapewi urithi wa ardhi katika Nchi ya Ahadi. Wageni wengine wanaweza kusali kwa kulielekea hekalu, na inaonekana kwamba wanaweza kutoa dhabihu kupitia makuhani, mradi tu dhabihu hizo zinapatana na Sheria. (Mambo ya Walawi 22:25; 1 Wafalme 8:41-43) Lakini Waisraeli hawapaswi kuwa na ushirika wa karibu pamoja na wageni hao.
Matowashi Wanapokea Jina la Kudumu Milele
8. (a) Matowashi walionwaje chini ya Sheria? (b) Matowashi walitumiwaje katika mataifa ya kipagani, na nyakati nyingine neno “towashi” linaweza kuwa na maana gani?
8 Matowashi wanakatazwa kuwa washirika kamili wa taifa la Israeli, hata ikiwa wamezaliwa na wazazi Wayahudi.a (Kumbukumbu la Torati 23:1) Nyakati za Biblia, matowashi katika mataifa fulani ya kipagani walitumiwa kwa makusudi ya pekee. Kulikuwako desturi ya kukomesha nguvu za uzazi katika baadhi ya wana waliotekwa vitani. Matowashi waliwekwa kuwa maofisa katika maeneo ya mabaraza ya kifalme. Towashi angeweza kuwa ‘mlinzi wa wanawake,’ ‘mlinzi wa masuria,’ au mtumishi wa malkia. (Esta 2:3, 12-15; 4:4-6, 9) Hakuna ushuhuda wa kuonyesha kwamba Waisraeli walifuata mazoea hayo wala wa kuonyesha kwamba matowashi walitafutwa sana ili waandikwe kazi ya kuwatumikia wafalme Waisraeli.b
9. Yehova anawaambia matowashi halisi maneno gani ya kutuliza moyo?
9 Matowashi halisi katika Israeli wanawekewa mipaka ya kushiriki katika ibada ya yule Mungu wa kweli. Isitoshe, wanashushiwa sana heshima kwa sababu hawawezi kuzaa watoto wa kuendeleza jina la familia yao.
-
-
Wageni Wakusanywa Kwenye Nyumba ya Mungu ya SalaUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
a Baadaye, neno “towashi” lilimaanisha pia kuhusu ofisa aliyetumika eneo la barazani, bila kumaanisha kukatwa kiungo cha uzazi. Bila shaka yule Mwethiopia aliyebatizwa na Filipo alikuwa towashi katika maana hiyo. Sababu ni kwamba, inaonekana towashi huyo alikuwa mwongofu kwa sababu alibatizwa kabla njia haijafunguliwa ya kuingia kwa watu wasiotahiriwa, wasio Wayahudi.—Matendo 8:27-39.
b Ebed-meleki, ambaye alimwokoa Yeremia, na angeweza kwenda kwa Mfalme Sedekia bila kuzuiwa na mtu yeyote, anaitwa towashi. Inaonekana kwamba anatajwa kuwa towashi katika maana ya kuwa ofisa wa eneo la barazani, wala si katika maana ya kukatwa kiungo.—Yeremia 38:7-13.
-