-
Kuwasiliana na Makao ya RohoAmkeni!—1996 | Novemba 22
-
-
Kuwasiliana na Makao ya Roho
KATIKATI ya mji wa kawaida wa Afrika Magharibi pamesimama jengo linalovutia lenye orofa moja, lililopakwa rangi nyeupe na kijani. Katika chumba cha mapokezi, makarani wawili walifanya kazi katika mashine zao za kupiga taipu. Watu kadhaa waliketi vitini, wakingoja kumwona babaláwo, yule mwaguzi.
Nyuma ya dawati katika ofisi inayopakana, kando ya mashine ya faksi, alikaa babaláwo mwenyewe. Akiwa pandikizi la mtu, mwenye mvi, alivalia majoho marefu meupe—yaliyo ghali, yaliyotariziwa. “Baba yangu alikuwa mwaguzi,” akasema. “Nilipangiwa kuwa katika desturi hiyo. Nililelewa katika hiyo. Nilipofika umri wa miaka mitano, wakati baba yangu alipokwenda kuagua, nilikwenda naye. Nilitazama jinsi alivyofanya, nami nikaiga alivyofanya hadi ilipokuwa sehemu yangu muhimu.”
Huyo babaláwo alionyesha ishara kuelekea ubao mkubwa ulioorodhesha mfumo ulio tata wa kuagua ambao watu wake walikuwa wameutumia kwa vizazi visivyohesabika. Ukitegemea kurusha mbegu 16 za mawese, huo ni mfumo ambao umeenea kotekote katika Afrika Magharibi na ng’ambo ya hapo. “Watu hunijia wakiwa na matatizo ya aina zote,” akasema. “Matatizo na wanawake, utasa, ukosefu wa kazi, kurukwa kichwa, afya, na kadhalika. Ikitegemea matokeo ya uaguzi, ombi linafanywa kwa ama wazazi wa kale ama watu wa kimbingu [miungu]. Vyovyote vile, ni lazima aina fulani ya dhabihu itolewe.”
Mazoea ya kidesturi ya kidini, kutia ndani uaguzi, yamesitawi sana katika eneo hilo, lakini ndivyo ilivyo pia na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Karibu tu na ofisi za babaláwo kuna majengo yaliyopakwa chokaa yenye ishara mbele yayo: Kanisa la Mfalme Sulemani 2, Kerubimu na Serafimu, Kanisa la Kimbingu la Kristo, Kanisa la Kristo la Kimitume, Kanisa la Wapiga Tarumbeta wa Kristo. Makanisa haya yapo pamoja na nyakati fulani hukubali mazoea ya dini ya kimapokeo. Akasema babaláwo: “Hivi majuzi nilikuwa nikiongea na askofu. Alikuja hapa. Baada ya kuzungumza mambo kwa dakika 30 hivi, yeye alisema kwamba alitaka tufanye mpango wa mazungumzo fulani ambamo Wakristo na wanamapokeo wanaweza kukutana na kujadiliana na kuondosha ukosefu wa uelewevu.”
Milango ya Ulimwengu wa Roho
Ukosefu huo wa uelewevu mara nyingi huhusisha utambulisho wa wale wakaao katika makao ya roho. Kotekote katika Afrika iliyo kusini ya Sahara, kuna itikadi iliyoenea sana kwamba kuna vikundi viwili vya viumbe ambao hukaa katika ulimwengu wa roho. Kikundi cha kwanza ni cha watu wa kimungu, au miungu, ambao hawajapata kuwa binadamu. Cha pili ni cha wazazi wa kale, au roho za wafu, ambao daraka lao ni kuhakikisha kusalimika na ufanisi wa familia zao duniani. Wote miungu na wazazi wa kale inaaminika kuwa wana uwezo wa ama kusaidia ama kudhuru wale walio duniani. Hivyo basi, ni lazima wote waonyeshwe staha na heshima ifaayo.
Itikadi kama hizo zapatikana katika sehemu nyingi za ulimwengu. Wakitumia njia tofauti-tofauti watu kila mahali hufikia kani za viumbe wapitao uwezo wa kibinadamu, wakitafuta ujuzi juu ya wakati ujao na msaada na mwongozo katika matatizo ya kila siku ya maisha. Je, inawezekana kweli kupata msaada kutoka kwa makao ya roho? Yesu Kristo, ambaye aliishi huko, alionyesha kwamba inawezekana. Yeye alisema hivi: “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa.” (Mathayo 7:7) Lakini ili kupata msaada huo, ni lazima tumwombe mtu afaaye, tutafute katika njia ifaayo, na kubisha kwenye mlango ufaao. Ikiwa tutabisha kwenye mlango usiofaa, huenda ukafunguliwa na mtu ambaye atatudhuru, badala ya kutufaidi.
Kwa hiyo, ni jambo la muhimu sana kujua ni nani anayeishi katika makao ya roho na asiyeishi huko. Twahitaji kujua pia tofauti kati ya wale watakaotusaidia na wale watakaotudhuru. Hatimaye, twahitaji kujua tutakacholazimika kufanya ili kupata msaada kutoka kwa wale wawezao kutupatia msaada huo. Makala zifuatazo zitachunguza mambo haya.
-
-
Ni Nani Wanaoishi Katika Makao ya Roho?Amkeni!—1996 | Novemba 22
-
-
Ni Nani Wanaoishi Katika Makao ya Roho?
ULIMWENGU umekuwa kama “duka kubwa” la itikadi na imani za kidini. Katika Afrika pekee kuna maelfu ya vikundi vya kidini, kila kimoja kikiwa na maoni yacho chenyewe kuhusu kile kinachoendelea katika makao ya roho. Lakini ili kupata habari ya wazi na ya kweli, twahitaji kuelekeza uangalifu wetu kwenye Biblia. Hiyo hutambulisha viumbe wa roho—wote wema na wabaya—ambao hukaa katika makao ya roho. Hiyo pia huonyesha ni nani tuwezaye kwa mafanikio kumwomba msaada na ulinzi.
Yehova, Mungu Mweza Yote
Dini ya kimapokeo katika Afrika hufundisha kwamba anayeongoza wazazi wa kale na miungu ni Mungu mweza yote. Chataarifu kitabu African Mythology: “Hakuna shaka kwamba karibu Waafrika wote, ikiwa si wote, huamini katika Mtu Mkuu Zaidi, muumba wa vitu vyote.” Chasema kitabu African Religion in African Scholarship: “Kwa kuwa Mungu ndiye mwenye mamlaka kamili juu ya ulimwengu wote mzima, viumbe wengine wote na uwezo wote unatokana Naye. Yeye ndiye mwenye mamlaka kamili na uwezo.”
Biblia hukubali kwamba kuna Mmoja ambaye hutawala akiwa mkuu zaidi katika makao ya roho. Hiyo humfafanua kuwa “Mungu wa miungu, na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu, mwenye kuogofya, asiyependelea nyuso za watu, wala hakubali rushwa.”—Kumbukumbu la Torati 10:17.
Kotekote katika Afrika kuna mamia ya majina na vyeo kwa yule aonwaye kuwa mkuu zaidi. Hata hivyo, Neno la Mungu husema nini kuhusu jina la kimungu? Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Wewe, uitwaye jina lako YEHOVA, ndiwe peke yako Uliye juu, juu ya nchi yote.” (Zaburi 83:18) Jina hili takatifu hupatikana zaidi ya mara 7,000 katika rekodi ya Biblia, ingawa watafsiri fulani wamelibadili na vyeo kama vile “Mungu” au “Bwana.”
Kwa sababu Yehova ni Mweza Yote, yeye aweza kutusaidia. Yeye hujifafanua kuwa “Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa si mwenye hatia kamwe.”—Kutoka 34:6, 7; 1 Samweli 2:6, 7.
Malaika, Wahudumu Wenye Uwezo wa Mungu
Muda mrefu kabla ya Yehova kuumba wanadamu au hata dunia yenyewe, aliumba watu wa roho mbinguni. Biblia husema kwamba katika wakati ambao Mungu ‘alipoiweka misingi ya nchi . . . , wana wote wa kimalaika wa Mungu walipiga kelele kwa furaha.’ (Ayubu 38:4-7) Kuna mamilioni ya malaika. Mtumishi wa Yehova Danieli aliandika juu ya ono la vitu vya kimbingu ambamo aliona “maelfu elfu wa[ki]mtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi wa[ki]simama mbele zake.”—Danieli 7:10.
Mtu wa kwanza wa roho ambaye Yehova alimuumba alikuwa yule aliyekuja kuitwa Yesu Kristo. (Yohana 17:5; Wakolosai 1:15) Kabla ya kuishi akiwa mwanadamu duniani, Yesu aliishi mbinguni akiwa kiumbe wa roho mwenye uweza. Baada ya kifo chake akiwa binadamu, Yesu alifufuliwa kwenda mbinguni, ambapo aliendelea na maisha yake akiwa kiumbe wa roho mwenye uweza.—Matendo 2:32, 33.
Yesu ana uwezo mwingi mbinguni. Kwenye Yuda 9, Yesu, aitwaye pia Mikaeli, huitwa “malaika mkuu,” kumaanisha kwamba yeye ndiye mkubwa wa malaika. (1 Wathesalonike 4:16) Yeye pia ana mamlaka juu ya dunia. Yehova amempa “mamlaka na utukufu, na ufalme ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie.” (Danieli 7:13, 14) Licha ya mamlaka yake kuu, Yesu abaki akiwa chini ya Baba yake, Yehova.—1 Wakorintho 11:3.
Ingawa malaika waaminifu wanamhudumia Yehova, wao pia huhudumia watumishi wa Mungu duniani. Mtume Paulo aliandika hivi: “Je, hao [malaika] wote si roho watumikiao, wakitumwa kuwahudumu wale watakaourithi wokovu?” (Waebrania 1:14) Hangaiko lao hasa ni kwamba watu wajifunze kweli kuhusu Yehova. Mtume Yohana aliona katika ono ‘malaika akiruka katikati ya mbingu, mwenye Injili ya milele, awahubiri hao wakaao juu ya nchi, na kila taifa na kabila na lugha na jamaa, akasema kwa sauti kuu, Mcheni Mungu na kumtukuza.’—Ufunuo 14:6, 7.
Shetani na Roho Waovu, Maadui wa Mungu na Mwanadamu
Kwa kuhuzunisha, si malaika wote wamekuwa waaminifu kwa Mungu. Wengine waliasi dhidi yake, wakawa maadui wa Mungu na wanadamu. Mwasi mkuu ni Shetani Ibilisi.
Ingawa wengi leo hukana kuwapo kwa Shetani, hakuna mtu akataaye kwamba uovu upo. Kuamini kwamba uovu upo na wakati uleule kutoamini kwamba uovu una kisababishi huongoza kwenye “tatizo lisiloweza kuepukika,” chaonelea kitabu The Death of Satan. “Twatambua kitu fulani ambacho utamaduni wetu hautupatii tena msamiati wa kukieleza.”
Kinyume cha hilo, Biblia ina msamiati na hueleza waziwazi kweli kuhusu chanzo cha uovu. Hiyo hueleza kwamba viumbe wa kimalaika ambao Yehova aliumba walikuwa waadilifu na wema; yeye hakuumba malaika wowote waovu. (Kumbukumbu la Torati 32:4; Zaburi 5:4) Hata hivyo, malaika, kama vile wanadamu, walipewa uwezo wa kuchagua kati ya lililo jema na baya. Mmoja wa hawa wana wakamilifu wa roho alisitawisha tamaa ya ubinafsi ya kujipatia ibada ambayo ni ya Yehova kihalali. Hivyo akapata jina Shetani, ambalo humaanisha “Mkinzani.” (Linganisha Yakobo 1:14, 15.) Shetani si mwenye hila tu, kama vile dini fulani za Kiafrika zifundishavyo; wala si “mlinzi” ambaye hulinda wale wamtoleao dhabihu kwa ukawaida. Biblia huonyesha kwamba yeye ni mwovu na mkatili kabisa.
Malaika wengine walijiunga na Shetani katika uasi dhidi ya Mungu. Malaika hawa walio roho waovu pia ni maadui wa watu duniani. Wao pia ni wenye nia mbaya na waovu. Katika nyakati zilizopita, walifanya wanadamu fulani wawe mabubu na vipofu. (Mathayo 9:32, 33; 12:22) Waliwatesa wengine, kutia ndani watoto kwa ugonjwa au kichaa. (Mathayo 17:15, 18; Marko 5:2-5) Kwa wazi, hakuna mtu yeyote mwenye busara ambaye angetaka kujishughulisha na Shetani au hao roho waovu.
Wazazi wa Kale Wako Wapi?
Mamilioni ya watu katika Afrika na kwingineko huamini kwamba kifo si mwisho wa uhai bali ni mgeuko tu, au kupita kuelekea uhai katika makao ya roho, mahali wanapokaa miungu na vilevile wazazi wa kale. Msomi John Mbiti, mtaalamu wa dini za Kiafrika, aandika juu ya itikadi katika wazazi wa kale, ambao awaita “wafu-wanaoishi”: “Hawa ndio ‘roho’ ambazo watu wa Afrika wanahangaikia . . . Wao wanajua na wana upendezi katika kile kinachoendelea katika familia zao [duniani]. . . . Wao ndio watunzaji wa mambo ya familia, mapokeo, maadili na utendaji wa familia. Makosa katika mambo haya kimsingi ni makosa dhidi ya mababu wa kale ambao, katika kiwango hicho, hutenda wakiwa viongozi wasioonekana wa familia na jumuiya. Kwa kuwa bado wanaonwa kuwa ‘watu,’ kwa hiyo wafu-wanaoishi ndio kikundi bora zaidi cha wapatanishi kati ya wanadamu na Mungu: wao wanajua mahitaji ya wanadamu, ‘majuzi’ walikuwa hapa pamoja na wanadamu, na kwa wakati huohuo wanaweza kufikia kikamili njia za kuwasiliana na Mungu.”
Ingawa hivyo, Biblia husema nini kuhusu hali ya wafu? Hiyo huonyesha kwamba hakuna kitu kama “wafu-wanaoishi.” Watu ama wako hai ama wamekufa—hawawezi kuwa katika hali zote mbili. Neno la Mungu hufundisha kwamba wafu hawawezi kusikia, kuona, kusema, au kufikiri. Wafu hawako katika hali yoyote ya kuweza kuongoza walio hai. Biblia husema: “Wafu hawajui neno lo lote . . . Mapenzi yao na machukio yao, na husuda yao, imepotea yote pamoja . . . Hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu [kaburini], uendako wewe.” (Mhubiri 9:5, 6, 10) “[Mwanadamu] huurudia udongo wake; siku hiyo mawazo yake yapotea.”—Zaburi 146:4.
Kurudi Mavumbini
Ikiwa waona hilo likiwa gumu kukubali, fikiria kile kilichompata mwanadamu wa kwanza, Adamu. Yehova alimfanya Adamu “kwa mavumbi ya ardhi.” (Mwanzo 2:7) Wakati Adamu alipokosa kutii amri ya Yehova, adhabu ilikuwa kifo. Mungu alimwambia: ‘Utairudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.’—Mwanzo 3:19.
Kabla ya Yehova kumuumba Adamu kutoka mavumbi, Adamu hakuwapo. Kwa hiyo wakati ‘aliporudi ardhini,’ akawa tena bila uhai, kama mavumbi. Yeye hakuvuka kuingia katika makao ya roho za wazazi wa kale. Yeye hakuenda mbinguni au helo. Alipokufa, huo ndio ulikuwa mwisho wake.
Je, jambo lilo hilo hupata wanadamu wengine wakati wa kifo? Ndivyo. Biblia hutaarifu: “Wote [wanadamu na wanyama] huendea mahali pamoja. Wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.” (Mhubiri 3:20) Biblia huahidi kwamba Mungu atawaamsha wanadamu waliokufa warudi kwenye uhai katika dunia iliyo paradiso, lakini wakati huo bado utakuja. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Kwa wakati uliopo, hatupaswi kuhofu wafu au kuwatolea dhabihu, kwa kuwa hawawezi kutusaidia wala kutudhuru.
Shetani na roho waovu wake wanataka kuongoza watu vibaya kuhusu hali ya wazazi wa kale waliokufa, kwa hiyo wanaendeleza uwongo kwamba watu huishi baada ya kifo. Njia moja wanayofanya hivyo ni kupitia hadithi zisizo za kweli. (1 Timotheo 4:1) Wao pia hutumia maono, ndoto, na wawasiliani-roho ili kudanganya watu wafikiri kwamba wamewasiliana na waliokufa. Lakini watu hawawasiliani na waliokufa. Badala ya hivyo, ni roho waovu ambao hujidai kuwa watu ambao wamekufa. Hiyo ndiyo sababu Yehova hushutumu sana wale wanaoulizia habari kutoka kwa wafu, ama moja kwa moja ama kwa njia isiyo ya moja kwa moja, kupitia njia nyinginezo, kama vile uaguzi.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.
-
-
Rafiki Yetu Bora Zaidi Yuko Katika Makao ya RohoAmkeni!—1996 | Novemba 22
-
-
Rafiki Yetu Bora Zaidi Yuko Katika Makao ya Roho
BIBLIA hutupatia ufafanuzi ulio wazi wa wale wanaoishi katika makao ya roho. Yehova Mungu ndiye mkuu kuliko wote mbinguni. Yesu Kristo anamfuata Yehova katika uwezo na mamlaka. Malaika walio waaminifu kwa Mungu hutumikia wakiwa wahudumu wa Mungu na wa watu wake duniani. Shetani na roho wake waovu humpinga Mungu na kuongoza wanadamu vibaya. Wafu wamelala katika kifo hadi wakati ambapo Mungu atawafufua.
Roho Waovu Wanataka Tuwaabudu
Kwa kuwa wafu hawana uhai, hakuna faida yoyote iwezayo kupatikana kwa kuwaabudu. Kuwatolea wafu dhabihu huendeleza tu uwongo wa Shetani na roho waovu.
Je, malaika wa Mungu wanatamani tuwaabudu? Sivyo hata kidogo! Malaika waaminifu humpa Mungu utukufu na kuwatia moyo wanadamu wafanye vivyo hivyo. Mara mbili, Yohana alijaribu kuabudu malaika, lakini walimkemea, wakisema: “Angalia, usifanye hivi. . . . Msujudie Mungu.”—Ufunuo 19:10; 22:8, 9.
Shetani na roho waovu wake, tofauti na malaika waaminifu, hutaka waabudiwe na kupewa utukufu. Hili lilikuwa wazi wakati Shetani alipomjaribu Yesu akiwa mwanadamu duniani. Biblia husimulia: “Ibilisi akamchukua [Yesu] mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia.”—Mathayo 4:8, 9.
Yesu alijibu: “Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.” (Mathayo 4:10) Yesu alijua Sheria ya Yehova, naye akakataa kuivunja.—Kumbukumbu la Torati 6:13.
Ingawa Shetani hakuweza kumfanya Yesu amwabudu, amefaulu na wengine. Bila shaka, ni watu wachache wanaomwabudu Shetani kwa kutaka kwao wenyewe. Hata hivyo, kwa njia ya werevu, hila, uwongo, na hofu, Shetani na roho waovu wamepotosha watu wengi sana kutoka kwa ibada ya Yehova hivi kwamba mtume Yohana akaandika: “Dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Wale wanaoabudu katika njia zilizo kinyume cha Neno la Mungu humheshimu Shetani, si Yehova. Biblia huonya: “Vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu.”—1 Wakorintho 10:20.
Yehova Ndiye Apaswaye Kuabudiwa
Ibada yetu yapasa kuelekezwa kwa Mungu pekee. Yehova alimwambia Musa hivi: “Usiwe na miungu mingine ila mimi. Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, BWANA, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu [“anayedai ujitoaji usiohusisha wengine,” NW].”—Kutoka 20:3-5.
Ingawa Yehova ni mwenye kutisha katika fahari, yeye anaweza kufikiwa. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Mtume Paulo alisema hivi: “[Mungu] hawi mbali na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Na mtume Yohana aliandika: “Huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia. Na kama tukijua kwamba atusikia, tuombacho chote, twajua kwamba tunazo zile haja tulizomwomba.”—1 Yohana 5:14, 15.
Ona kwamba Yohana aliandika kwamba Yehova atatutimizia maombi yetu ikiwa twaomba “sawasawa na mapenzi yake.” Ili kujua mapenzi ya Mungu ni nini, ni lazima tujifunze kile inachofundisha Biblia. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kuifahamu Biblia.
Unapojifunza zaidi kuhusu Yehova, utapata ujuzi kuhusu wale ambao huishi katika makao ya roho. Ujuzi huu huleta uhuru kutokana na ushirikina, itikadi, na mapokeo ambayo Shetani hutumia ili kushika watu katika hofu na utumwa. Kupitia ujuzi sahihi juu ya Mungu, utajifunza jinsi ya kumtumaini akusaidie kuepuka au kushinda matatizo ya kila siku ya maisha. Wewe waweza kuwa rafiki ya Mungu. Naye Mungu atathibitika kuwa kwako “kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.”—Zaburi 46:1.
Kani Zilizo Ovu Zitaondoshwa
Usitie shaka kamwe kwamba kani za roho za wema zitashinda kani za roho za uovu. Tayari vita vimepiganwa katika makao ya roho ambavyo vimesafisha mbingu na kumwondoa Shetani na waandamani wake waovu. Kitabu cha Ufunuo hutaarifu: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli [Yesu Kristo aliyefufuliwa] na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.”—Ufunuo 12:7-9.
Matokeo ya vita hiyo yalikuwa nini? Ripoti hiyo huendelea hivi: “Kwa hiyo, shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:12) Wale walio mbinguni waliweza kushangilia, kwa kuwa Shetani na roho wake waovu hawakuwa tena huko ili kusababisha taabu. Hata hivyo, kutupwa kwake kutoka mbinguni kumeleta ole mwingi, taabu kuu, kwa wale walio duniani. Twaishi katika wakati huo wa ole sasa.—2 Timotheo 3:1-5.
Wakati Ujao Usio na Uovu
Hata hivyo, Biblia pia huandaa tumaini. Hiyo hutuhakikishia kwamba Ibilisi ana “wakati mchache” kabla ya kuwekwa katika hali ya kutotenda. Hilo litakapotukia, Yehova ataleta baraka nzuri ajabu kwa wote duniani ambao hutafuta urafiki wake. Fikiria baadhi ya ahadi zake za wakati ujao:
“Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zaburi 72:16.
“Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure.”—Isaya 65:22, 23.
“Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.
“Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6.
“Naye [Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4.
“Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.
Ni Yehova tu, Mungu wa kweli, awezaye kutimiza ahadi hizo tukufu. Hakuna kitu kitakachomzuia kutimiza kusudi lake. “Hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.”—Luka 1:37.
-