Rafiki Yetu Bora Zaidi Yuko Katika Makao ya Roho
BIBLIA hutupatia ufafanuzi ulio wazi wa wale wanaoishi katika makao ya roho. Yehova Mungu ndiye mkuu kuliko wote mbinguni. Yesu Kristo anamfuata Yehova katika uwezo na mamlaka. Malaika walio waaminifu kwa Mungu hutumikia wakiwa wahudumu wa Mungu na wa watu wake duniani. Shetani na roho wake waovu humpinga Mungu na kuongoza wanadamu vibaya. Wafu wamelala katika kifo hadi wakati ambapo Mungu atawafufua.
Roho Waovu Wanataka Tuwaabudu
Kwa kuwa wafu hawana uhai, hakuna faida yoyote iwezayo kupatikana kwa kuwaabudu. Kuwatolea wafu dhabihu huendeleza tu uwongo wa Shetani na roho waovu.
Je, malaika wa Mungu wanatamani tuwaabudu? Sivyo hata kidogo! Malaika waaminifu humpa Mungu utukufu na kuwatia moyo wanadamu wafanye vivyo hivyo. Mara mbili, Yohana alijaribu kuabudu malaika, lakini walimkemea, wakisema: “Angalia, usifanye hivi. . . . Msujudie Mungu.”—Ufunuo 19:10; 22:8, 9.
Shetani na roho waovu wake, tofauti na malaika waaminifu, hutaka waabudiwe na kupewa utukufu. Hili lilikuwa wazi wakati Shetani alipomjaribu Yesu akiwa mwanadamu duniani. Biblia husimulia: “Ibilisi akamchukua [Yesu] mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia.”—Mathayo 4:8, 9.
Yesu alijibu: “Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake.” (Mathayo 4:10) Yesu alijua Sheria ya Yehova, naye akakataa kuivunja.—Kumbukumbu la Torati 6:13.
Ingawa Shetani hakuweza kumfanya Yesu amwabudu, amefaulu na wengine. Bila shaka, ni watu wachache wanaomwabudu Shetani kwa kutaka kwao wenyewe. Hata hivyo, kwa njia ya werevu, hila, uwongo, na hofu, Shetani na roho waovu wamepotosha watu wengi sana kutoka kwa ibada ya Yehova hivi kwamba mtume Yohana akaandika: “Dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Wale wanaoabudu katika njia zilizo kinyume cha Neno la Mungu humheshimu Shetani, si Yehova. Biblia huonya: “Vitu vile wavitoavyo sadaka wavitoa kwa mashetani, wala si kwa Mungu.”—1 Wakorintho 10:20.
Yehova Ndiye Apaswaye Kuabudiwa
Ibada yetu yapasa kuelekezwa kwa Mungu pekee. Yehova alimwambia Musa hivi: “Usiwe na miungu mingine ila mimi. Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia; kwa kuwa mimi, BWANA, Mungu wako, ni Mungu mwenye wivu [“anayedai ujitoaji usiohusisha wengine,” NW].”—Kutoka 20:3-5.
Ingawa Yehova ni mwenye kutisha katika fahari, yeye anaweza kufikiwa. Mwanafunzi Yakobo aliandika: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Mtume Paulo alisema hivi: “[Mungu] hawi mbali na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Na mtume Yohana aliandika: “Huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake, atusikia. Na kama tukijua kwamba atusikia, tuombacho chote, twajua kwamba tunazo zile haja tulizomwomba.”—1 Yohana 5:14, 15.
Ona kwamba Yohana aliandika kwamba Yehova atatutimizia maombi yetu ikiwa twaomba “sawasawa na mapenzi yake.” Ili kujua mapenzi ya Mungu ni nini, ni lazima tujifunze kile inachofundisha Biblia. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kuifahamu Biblia.
Unapojifunza zaidi kuhusu Yehova, utapata ujuzi kuhusu wale ambao huishi katika makao ya roho. Ujuzi huu huleta uhuru kutokana na ushirikina, itikadi, na mapokeo ambayo Shetani hutumia ili kushika watu katika hofu na utumwa. Kupitia ujuzi sahihi juu ya Mungu, utajifunza jinsi ya kumtumaini akusaidie kuepuka au kushinda matatizo ya kila siku ya maisha. Wewe waweza kuwa rafiki ya Mungu. Naye Mungu atathibitika kuwa kwako “kimbilio na nguvu, msaada utakaoonekana tele wakati wa mateso.”—Zaburi 46:1.
Kani Zilizo Ovu Zitaondoshwa
Usitie shaka kamwe kwamba kani za roho za wema zitashinda kani za roho za uovu. Tayari vita vimepiganwa katika makao ya roho ambavyo vimesafisha mbingu na kumwondoa Shetani na waandamani wake waovu. Kitabu cha Ufunuo hutaarifu: “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli [Yesu Kristo aliyefufuliwa] na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake; nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni. Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.”—Ufunuo 12:7-9.
Matokeo ya vita hiyo yalikuwa nini? Ripoti hiyo huendelea hivi: “Kwa hiyo, shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! kwa maana yule Ibilisi ameshuka kwenu mwenye ghadhabu nyingi, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu.” (Ufunuo 12:12) Wale walio mbinguni waliweza kushangilia, kwa kuwa Shetani na roho wake waovu hawakuwa tena huko ili kusababisha taabu. Hata hivyo, kutupwa kwake kutoka mbinguni kumeleta ole mwingi, taabu kuu, kwa wale walio duniani. Twaishi katika wakati huo wa ole sasa.—2 Timotheo 3:1-5.
Wakati Ujao Usio na Uovu
Hata hivyo, Biblia pia huandaa tumaini. Hiyo hutuhakikishia kwamba Ibilisi ana “wakati mchache” kabla ya kuwekwa katika hali ya kutotenda. Hilo litakapotukia, Yehova ataleta baraka nzuri ajabu kwa wote duniani ambao hutafuta urafiki wake. Fikiria baadhi ya ahadi zake za wakati ujao:
“Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zaburi 72:16.
“Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure.”—Isaya 65:22, 23.
“Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.
“Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6.
“Naye [Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4.
“Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.
Ni Yehova tu, Mungu wa kweli, awezaye kutimiza ahadi hizo tukufu. Hakuna kitu kitakachomzuia kutimiza kusudi lake. “Hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.”—Luka 1:37.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Mara tu unapokuwa rafiki ya Mungu, yeye atakusaidia kushughulika na matatizo ya maisha