-
Tii kwa Uaminifu Mamlaka ya KimunguMnara wa Mlinzi—2002 | Agosti 1
-
-
“Je! Mwataka na Ukuhani Pia?”
8. (a) Kora alikuwa nani? (b) Ni nini ambacho huenda kilifanya Kora aanze kuwa na maoni ya kibinadamu kuelekea makuhani?
8 Kora hakuwa mkuu wa kichwa cha nyumba ya Lawi, wala hakuwa kichwa cha familia za Wakohathi. (Hesabu 3:30, 32) Hata hivyo, alikuwa mkuu aliyeheshimiwa Israeli. Huenda ikawa kazi ambazo Kora alifanya zilimwezesha kushirikiana kwa ukaribu na Aroni na wanawe. (Hesabu 4:18, 19) Baada ya kuona udhaifu wa watu hao, huenda Kora aliwaza hivi: ‘Bila shaka makuhani hawa si wakamilifu, na bado ninatazamiwa niwatii! Aroni alikuwa ametengeneza ndama ya dhahabu muda mfupi tu uliopita. Watu wetu walishiriki ibada ya sanamu kwa kuabudu ndama hiyo. Sasa Aroni, nduguye Musa anatumikia akiwa kuhani mkuu! Huo ni upendeleo ulioje! Namna gani wana wa Aroni, Nadabu na Abihu? Kwa kweli, walidharau kabisa migawo yao hivi kwamba ilimbidi Yehova awaue!’a (Kutoka 32:1-5; Mambo ya Walawi 10:1, 2) Hata iwe Kora alikuwa akiwaza nini, ni wazi kwamba alianza kuwa na maoni ya kibinadamu kuelekea ukuhani. Jambo hilo lilifanya aasi Musa na Aroni, na hatimaye akamwasi Yehova.—1 Samweli 15:23; Yakobo 1:14, 15.
9, 10. Kora na waasi wenzake walimlaumu Musa kwa jambo gani, na kwa nini hawakupaswa kufanya hivyo?
9 Kwa kuwa Kora alikuwa mashuhuri, haikuwa vigumu kutafuta watu waliokuwa na mtazamo kama wake ili wamwunge mkono. Yeye, pamoja na Dathani na Abiramu, walipata watu 250 waliokuwa na maoni kama yake na wote walikuwa wakuu wa mkutano. Wote pamoja walimwendea Musa na Aroni na kusema: “Mkutano wote ni mtakatifu, kila mmoja miongoni mwao, BWANA naye yu kati yao; n’ nini basi kujitukuza juu ya mkutano wa BWANA?”—Hesabu 16:1-3.
10 Waasi hao hawakupaswa kukaidi mamlaka ya Musa kwa kuzingatia yale ambayo walijua tayari. Muda mfupi kabla ya hapo, Aroni na Miriamu walikuwa wamekaidi mamlaka ya Musa. Kwa kweli, walikuwa wamesababu kama Kora! Kulingana na andiko la Hesabu 12:1, 2, Aroni na Miriamu waliuliza hivi: “Je! ni kweli BWANA amenena na Musa tu? hakunena na sisi pia?” Yehova alikuwa akisikiliza. Hivyo akawaamuru Musa, Aroni, na Miriamu wakutanike kwenye lango la hema la kukutania ili aonyeshe amechagua nani awe kiongozi. Kisha Yehova akasema hivi waziwazi: “Akiwapo nabii kati yenu, mimi, BWANA, nitajifunua kwake katika maono, nitasema naye katika ndoto. Sivyo ilivyo kwa mtumishi wangu, Musa; yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote.” Baada ya hapo, Yehova alimpiga Miriamu kwa ukoma kwa muda mfupi.—Hesabu 12:4-7, 10.
11. Musa alishughulikaje na uasi wa Kora?
11 Lazima iwe Kora pamoja na watu waliomwunga mkono walijua kisa hicho. Hawakuwa na sababu ya kuasi. Hata hivyo, Musa alijaribu kusababu nao kwa subira. Aliwasihi wathamini mapendeleo yao hata zaidi, akisema: “Je! mwaona kuwa ni jambo dogo kwenu, kuwa Mungu wa Israeli amewatenga ninyi na mkutano wa Israeli, ili apate kuwakaribisha kwake?” La, halikuwa “jambo dogo”! Tayari Walawi walikuwa na mapendeleo mengi. Wangetamani nini zaidi? Maneno ya Musa yanayofuata yalifunua jinsi walivyokuwa wakisababu mioyoni mwao: “Je! mwataka na ukuhani pia?”b (Hesabu 12:3; 16:9, 10) Hata hivyo, Yehova alitendaje baada ya watu hao kuasi mamlaka yake?
Mwamuzi wa Israeli Aingilia Kati
12. Waisraeli walipaswa kufanya nini ili waendelee kuwa na uhusiano mzuri na Mungu?
12 Yehova alipowapa Waisraeli Sheria, aliwaambia watu kwamba iwapo wangetii, wangekuwa “taifa takatifu” na kwamba taifa hilo lingeendelea kuwa takatifu mradi lingekubali mpango wa Yehova. (Kutoka 19:5, 6) Sasa kwa kuwa walionyesha uasi waziwazi, Mwamuzi na Mfanya Sheria wa Israeli alilazimika kuingilia kati! Musa alimwambia Kora: “Wewe na mkutano wako wote iweni hapa mbele ya BWANA kesho, wewe, na wao, na Haruni; mkatwae kila mtu chetezo chake, na kutia uvumba juu yake, mkavilete mbele za BWANA, vyetezo mia mbili na hamsini; wewe pia, na Haruni, kila mtu na awe na chetezo chake.”—Hesabu 16:16, 17.
13. (a) Kwa nini waasi hao walionyesha kimbelembele kwa kufukiza uvumba mbele za Yehova? (b) Yehova aliwatendeaje waasi hao?
13 Kulingana na Sheria ya Mungu, makuhani peke yao ndio waliopaswa kufukiza uvumba. Waasi hao walipaswa kushtuka kwa kukumbuka kwamba Mlawi asiye kuhani hapaswi kufukiza uvumba mbele za Yehova. (Kutoka 30:7; Hesabu 4:16) Kora na watu waliokuwa wakimwunga mkono hawakushtuka! Siku iliyofuata ‘alikutanisha mkutano wote kinyume chao Musa na Aroni mlangoni pa hema ya kukutania.’ Simulizi hilo linatuambia: “Kisha BWANA akanena na Musa na Haruni, na kuwaambia, Jitengeni ninyi mkaondoke kati ya mkutano huu, ili nipate kuwaangamiza mara moja.” Lakini Musa na Aroni walimsihi Yehova asiangamize mkutano huo. Yehova alisikiliza maombi yao. Lakini kuhusu Kora na watu waliomwunga mkono, ‘moto ulitoka kwa BWANA, ukawateketeza hao watu mia mbili hamsini waliofukiza uvumba.’—Hesabu 16:19-22, 35.c
14. Kwa nini Yehova alichukua hatua thabiti dhidi ya mkutano wa Israeli?
14 Jambo la kushangaza ni kwamba hata Waisraeli walioona jinsi Yehova alivyoshughulika na waasi hao hawakujifunza somo lolote. “Siku ya pili yake mkutano wote wa wana wa Israeli wakamnung’unikia Musa, na Haruni, wakasema, Ninyi mmewaua watu wa BWANA.” Waisraeli waliwaunga mkono watu hao waliokula njama! Hatimaye, subira ya Yehova ilikoma. Hakuna mtu ambaye angeweza kuwatetea watu hao, wala Musa wala Aroni. Yehova alileta tauni juu ya watu wasiotii, ‘na wale waliokufa kwa tauni walikuwa kumi na nne elfu na mia saba, zaidi ya wale waliokufa kwa jambo la Kora.’—Hesabu 16:41-49.
15. (a) Kwa nini Waisraeli hawakupaswa kusitasita kukubali uongozi wa Musa na Aroni? (b) Simulizi hili limekufundisha nini kuhusu Yehova?
15 Watu hao wote hawangekufa iwapo wangetumia uwezo wao wa kufikiri kuhusiana na mambo hayo ya uongozi. Wangejiuliza maswali kama vile: ‘Ni nani walioenda mbele ya Farao na kuhatarisha maisha yao? Ni nani waliodai Waisraeli waachiliwe? Ni nani pekee aliyealikwa kwenye Mlima Horebu ili kuzungumza na malaika wa Mungu uso kwa uso baada ya Waisraeli kukombolewa?’ Bila shaka Musa na Aroni walithibitisha kwamba walikuwa waaminifu kwa Yehova na kwamba waliwapenda watu. (Kutoka 10:28; 19:24; 24:12-15) Yehova hakufurahia kuwaua waasi hao. Hata hivyo, ilipoonekana wazi kwamba watu hao wangeendelea na uasi wao, Yehova alichukua hatua ya kukata maneno. (Ezekieli 33:11)
-
-
Tii kwa Uaminifu Mamlaka ya KimunguMnara wa Mlinzi—2002 | Agosti 1
-
-
b Dathani na Abiramu ambao walikula njama pamoja na Kora walikuwa wana wa Reubeni. Kwa hiyo, inaonekana hawakutamani ukuhani. Wao walichukia tu uongozi wa Musa, na kwamba kufikia wakati huo taraja lao la kuingia katika Bara Lililoahidiwa halikuwa limetimizwa.—Hesabu 16:12-14.
c Nyakati za wazee wa ukoo, kila kichwa cha familia aliwakilisha mke na watoto wake mbele za Mungu, na hata kutoa dhabihu kwa niaba yao. (Mwanzo 8:20; 46:1; Ayubu 1:5) Hata hivyo, Sheria ilipotolewa, Yehova alichagua wanaume kutoka familia ya Aroni kuwa makuhani ambao wangewatolea watu dhabihu. Yaonekana waasi hao 250 hawakutaka kukubali badiliko lililofanywa katika mpango huo.
-