-
Mwisho Wenye Kutazamisha wa Dini ya Uwongo Waonekana KimbeleUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Babiloni Yashushwa Chini Kwenye Vumbi
3. Fafanua ukuu wa Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Babiloni.
3 Ebu lisikilize tangazo hili rasmi la kimungu linalosisimua: “Haya, shuka, keti mavumbini, ewe bikira, binti Babeli; keti chini pasipo kiti cha enzi, ewe binti wa Wakaldayo; maana hutaitwa tena mwororo, mpenda anasa.” (Isaya 47:1) Kwa miaka mingi, Babiloni amekalia kiti cha ufalme akiwa serikali kubwa ya ulimwengu yenye mamlaka. Amekuwa “utukufu wa falme”—kitovu chenye usitawi wa kidini, wa kibiashara na wa kijeshi. (Isaya 13:19) Babiloni anapofikia upeo, milki yake imetandaa hadi mbali kusini kwenye mpaka wa Misri. Kisha, anapomshinda Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., inaonekana ni kama Mungu mwenyewe hawezi kumzuia kupata-pata ushindi! Basi, Babiloni anajiona kuwa ‘binti bikira,’ ambaye hataingiliwa kamwe na mvamizi wa kigeni.b
4. Babiloni atapatwa na nini?
4 Hata hivyo, “bikira” huyo kichwa kikubwa atadondoshwa kutoka kwenye kiti chake cha kifalme asiwe tena serikali kubwa ya ulimwengu isiyoweza kubishaniwa, ‘aketishwe mavumbini’ kwa kutiwa aibu. (Isaya 26:5) Hataonwa tena kuwa “mwororo, mpenda anasa,” mfano wa malkia wa kubembelezwa-bembelezwa. Hivyo basi, Yehova anaamuru hivi: “Twaa mawe ya kusagia, usage unga; vua utaji wako, ondoa mavazi yako [“rinda lako refu,” “NW”], funua mguu wako, pita katika mito ya maji.” (Isaya 47:2) Baada ya Babiloni kulitia utumwani taifa zima la Yuda, sasa yeye mwenyewe atatendwa kama mtumwa! Wamedi na Waajemi, wanaomwondoa katika kiti chake cha mamlaka, watamfanyisha kazi ngumu ya kumwaibisha.
5. (a) Babiloni atavuliwaje ‘utaji na rinda lake refu’? (b) Amri inayotolewa kwamba Babiloni ‘apite katika mito ya maji’ huenda ikawa inaonyesha nini?
5 Hivyo Babiloni atavuliwa ‘utaji na rinda lake refu,’ hata masazo ya ukuu na fahari yake ya zamani yakung’utwe fyuu. “Pita katika mito ya maji,” mabwana wake wa kazi watamwamuru. Labda Wababiloni fulani wataagizwa hasa kufanya kazi ngumu ya mtumwa kule nje. Au pengine unabii unamaanisha kwamba watu fulani wataburutwa wavuke mito wanapopelekwa uhamishoni. Vyovyote vile, Babiloni hatasafiri tena kwa madaha ya malkia anayesafirishwa na kuvushwa kijito akiwa amekalia kiti au akiwa katika kigari. Bali atakuwa kama mtumwa anayelazimika kuachilia mbali uungwana kwa kuinua rinda lake juu na kufichua miguu yake ili aweze kuvuka mto. Ni aibu iliyoje!
6. (a) Uchi wa Babiloni utafunuliwa katika maana gani? (b) Ni jinsi gani Mungu ‘hamkubali mtu ye yote’? (Ona kielezi-chini.)
6 Yehova anaendeleza shutuma yake: “Uchi wako utafunuliwa, naam, aibu yako itaonekana. Nitalipa kisasi; simkubali mtu ye yote.” (Isaya 47:3)c Naam, Babiloni ataaibishwa na kuvunjiwa heshima. Uovu na ukatili anaowafanyia watu wa Mungu utafichuliwa peupe. Hakuna binadamu anayeweza kuzuia kisasi cha Mungu!
7. (a) Wahamishwa Wayahudi wataitikiaje habari za anguko la Babiloni? (b) Yehova atawakomboa watu wake kwa njia gani?
7 Baada ya watu wa Mungu kuwa wameshikwa mateka muda wa miaka 70 katika Babiloni lililo hodari, watashangilia sana anguko lake. Watapaza sauti kusema: “Mkombozi wetu, BWANA wa majeshi ndilo jina lake, Mtakatifu wa Israeli.” (Isaya 47:4) Chini ya Sheria ya Kimusa, iwapo Mwisraeli alijiuza utumwani kulipia madeni yake, mkombozi (mtu wa damu yake) angeweza kumnunua, au kumkomboa, kutoka utumwani. (Mambo ya Walawi 25:47-54) Kwa kuwa Wayahudi watakuwa wameuzwa utumwani Babiloni, watahitaji kukombolewa, au kuwekwa huru. Nchi moja inaposhindwa na nyingine, watumwa hawafaidiki sana ila huhamishwa tu kutoka kwa bwana-mkubwa mmoja kupelekwa kwa mwingine. Lakini Yehova atamwongoza Mfalme Koreshi mshindi awafungue Wayahudi kutoka utumwani. Koreshi atapewa Misri, Kushi (Ethiopia), na Seba ziwe “ukombozi,” ili naye awaachilie Wayahudi. (Isaya 43:3) Basi ni vizuri kwamba Mwokozi wa Israeli anaitwa “BWANA wa majeshi.” Jeshi la Babiloni linaloonekana kuwa hodari sana si kitu mbele ya vikosi vya Yehova vya malaika wasioonekana.
Malipo ya Ukatili
8. Babiloni ‘ataingia gizani’ kwa maana gani?
8 Yehova anairudia shutuma yake ya kiunabii kuhusu Babiloni: “Kaa kimya, ingia gizani, Ee binti wa Wakaldayo; maana hutaitwa tena Malkia [“Bi-Mkubwa,” “NW”] wa falme.” (Isaya 47:5) Babiloni ataona giza tupu, giza tititi. Hatatawala tena falme nyinginezo akiwa bi-mkubwa mkatili.—Isaya 14:4.
9. Kwa nini Yehova anawakasirikia Wayahudi kwa haki?
9 Kwanza hata imekuwaje Babiloni akaruhusiwa kuwadhuru watu wa Mungu? Yehova anaeleza hivi: “Nalikuwa nimekasirika na watu wangu, naliutia unajisi urithi wangu, nikawatia mkononi mwako.” (Isaya 47:6a) Yehova ana sababu nzuri ya kuwakasirikia Wayahudi. Zamani zile, aliwaonya kwamba wasipoitii Sheria yake wangefukuzwa nchini. (Kumbukumbu la Torati 28:64) Walipotumbukia katika ibada ya sanamu na ukosefu wa adili kingono, Yehova alionyesha upendo kwa kutuma manabii wakawasaidie kuirudia ibada safi. “Lakini waliwadhihaki wajumbe wa Mungu, na kuyadharau maneno yake, na kuwacheka manabii wake, hata ilipozidi ghadhabu ya BWANA juu ya watu wake, hata kusiwe na kuponya.” (2 Mambo ya Nyakati 36:16) Basi, wakati Babiloni anapovamia Yuda na kuchafua hekalu Lake takatifu, Mungu anaruhusu nchi hiyo, iliyo urithi wake, itiwe unajisi.—Zaburi 79:1; Ezekieli 24:21.
10, 11. Kwa nini Yehova anakasirikia Babiloni, hata ingawa ni mapenzi yake kwamba Babiloni awashinde watu wake?
10 Basi, je, Babiloni anapowatumikisha Wayahudi, hafanyi hivyo ili kutimiza mapenzi ya Mungu tu? Sivyo, kwani Mungu anasema hivi: “Wewe hukuwatendea rehema; uliwatia wazee nira yako, nayo nzito sana. Ukasema, Mimi nitakuwa bibi [“Bi-Mkubwa,” “NW”] milele; hata hukuyatia hayo moyoni mwako, wala hukukumbuka mwisho wa mambo hayo.” (Isaya 47:6b, 7) Mungu hajampa Babiloni amri ya kuwa mkatili mno, hivi kwamba hata hawawaonyeshi “wazee” hisani. (Maombolezo 4:16; 5:12) Wala hajawahimiza wajifurahishe kinyama kwa kuwadhihaki mateka Wayahudi.—Zaburi 137:3.
11 Babiloni hatambui kwamba amewashika Wayahudi kwa muda tu. Ameyapuuza maonyo ya Isaya yasemayo kuwa wakati utawadia Yehova awaweke huru watu wake. Babiloni anatenda kana kwamba ni haki yake kuwatawala Wayahudi daima na kubakia milele akiwa bi-mkubwa anayesimamia mataifa yaliyo vibaraka vyake. Anakataa kuusikiza ujumbe wa kwamba utawala wake mwonevu utafika “mwisho”!
Anguko la Babiloni Latabiriwa
12. Kwa nini Babiloni anaitwa ‘mwanamke apendaye anasa’?
12 Yehova anatangaza rasmi hivi: “Sasa, basi, sikia haya, wewe [“mwanamke,” “NW”] upendaye anasa, ukaaye na kujiona salama, wewe usemaye moyoni mwako, Mimi ndiye, wala hapana mwingine zaidi yangu mimi; sitaketi mfano wa mjane, wala sitajua kufiwa na watoto.” (Isaya 47:8) Babiloni amevuma sana kwa kutafuta anasa. Mwanahistoria Herodotus wa karne ya tano K.W.K. anaelezea “desturi ya aibu sana” ya Wababiloni, ya kwamba wanawake wote walitakiwa kufanya umalaya ili kuonyesha kwamba wanamheshimu sana mungu wao wa kike wa mapenzi. Naye Curtius, mwanahistoria wa kale, alisema hivi: “Uchafu wa jiji hilo hauna kifani; hakuna zoea la ufisadi liwezalo kuwachochea watu na kuamsha tamaa zao za uasherati kwa kiwango kile.”
13. Mwelekeo wa Babiloni wa kutafuta anasa utaharakishaje anguko lake?
13 Mwelekeo wa Babiloni wa kutafuta anasa utaharakisha anguko lake. Muda mfupi kabla ya anguko lake, mfalme wa Babiloni na watu wenye vyeo watakula karamu, wanywe walewe chakari. Hivyo, hawatayajali hata kidogo majeshi ya Umedi-Uajemi yanayolivamia jiji. (Danieli 5:1-4) ‘Akiwa amekaa kwa kujiona salama,’ Babiloni atawaza kwamba hawezi kuvamiwa kwani kuta zake na handaki lake lenye maji zinampa himaya inayoonekana kuwa isiyopenyeka. Anajiambia kwamba “hapana mwingine” kamwe wa kutwaa cheo chake cha ukuu. Hafikiri kwamba angeweza kuwa “mjane,” afiwe na maliki wake, na vilevile “watoto” au wananchi wake. Vyovyote vile, hakuna ukuta uwezao kumhami kutokana na mkono wa Yehova Mungu wa kulipiza kisasi! Yehova atasema hivi baadaye: “Babeli ujapopanda mbinguni, na ujapopafanya mahali pa juu penye nguvu zake kuwa ngome, hata hivyo toka kwangu wenye kuangamiza watamwendea.”—Yeremia 51:53.
14. Babiloni ‘atafiwa na watoto na kuwa mjane’ kwa njia zipi?
14 Ni matokeo gani yatakayompata Babiloni? Yehova anaendelea kusema hivi: “Lakini mambo haya mawili yatakupata katika dakika moja siku moja, kufiwa na watoto, na ujane; yatakupata kiasi kitimilifu, uchawi wako ujapokuwa mwingi, na uganga wako mwingi mno.” (Isaya 47:9) Naam, ukuu wa Babiloni akiwa serikali kubwa ya ulimwengu utakoma ghafula. Katika nchi za kale za Mashariki, kuwa mjane na kufiwa na watoto ndiyo maafa makubwa zaidi ambayo yangeweza kumpata mwanamke. Hatujui Babiloni anafiwa na “watoto” wangapi usiku wa anguko lake.d Ingawa hivyo, wakati utawadia jiji hilo liwe mahame kabisa. (Yeremia 51:29) Pia, ujane utamfika Babiloni kwa kuwa wafalme wake watang’olewa.
15. Licha ya Babiloni kuwatenda Wayahudi ukatili, ni sababu gani zaidi inayomfanya Yehova amghadhibikie?
15 Hata hivyo, hasira kali ya Yehova haiji kwa sababu tu ya dhuluma ambazo Babiloni anawatenda Wayahudi. Pia ‘uchawi wake mwingi’ unaichochea hasira ya Yehova. Sheria ya Mungu kwa Israeli hushutumu zoea la kuwasiliana na roho waovu; ingawa hivyo, Babiloni huyafuatia sana mafumbo ya roho. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Ezekieli 21:21) Kitabu Social Life Among the Assyrians and Babylonians kinasema kwamba Wababiloni waliishi ‘wakiwahofu daima roho wengi sana waovu ambao waliamini kuwa wamewazunguka.’
Kutumaini Ubaya
16, 17. (a) Babiloni ‘anautumainia ubaya wake’ jinsi gani? (b) Kwa nini mwisho wa Babiloni hauwezi kuepukwa?
16 Je, wabashiri wa Babiloni watamwokoa? Yehova anajibu hivi: “Umeutumainia ubaya wako; umesema, Hapana anionaye; hekima yako, na maarifa yako yamekupotosha, nawe umesema moyoni mwako, Mimi ndiye, wala hapana mwingine zaidi yangu mimi.” (Isaya 47:10) Babiloni anafikiri kwamba kupitia hekima yake ya kilimwengu na ya kidini, pamoja na uhodari wake wa kijeshi na ukatili wake wenye ujanja, anaweza kudumisha cheo chake akiwa serikali kubwa ya ulimwengu. Anahisi kwamba hakuna awezaye ‘kumwona,’ yaani kumtoza hesabu kwa maovu anayoyatenda. Haoni mtu atakayeweza kupimana nguvu naye hivi karibuni. “Mimi ndiye, wala hapana mwingine,” anajiambia.
17 Lakini Yehova anaonya hivi kupitia mwingine wa manabii wake: “Je, mtu ye yote aweza kujificha mahali pa siri, nisimwone?” (Yeremia 23:24; Waebrania 4:13) Basi Yehova anatangaza hivi: “Ubaya utakupata; wala hutajua kutopoa kwake; na msiba utakuangukia; hutaweza kuuondoa; na ukiwa utakupata kwa ghafula, usioujua.” (Isaya 47:11) Miungu ya Babiloni wala ‘utopozi’ wa waganga wake wanaowasiliana na roho waovu haiwezi kuepusha maafa yanayokuja—maafa ambayo Babiloni hajawahi kuona kifani chake!
Washauri wa Babiloni Washindwa
18, 19. Babiloni atapatwaje na msiba kwa kuwategemea washauri wake?
18 Yehova anaamuru hivi kwa kejeli kali: “Simama sasa na uganga wako, na wingi wa uchawi wako, uliojitaabisha nao tangu ujana wako; labda utaweza kupata faida, labda utaweza kushinda.” (Isaya 47:12) Babiloni anaambiwa ajitokeze ‘asimame,’ au aendelee kutegemea uganga bila kujirekebisha. Basi na asimame, kwani si muda wote tangu “ujana” wake akiwa taifa amekazana kuendeleza sanaa za mafumbo ya roho.
19 Lakini Yehova anamdhihaki, akisema: “Umechoka kwa wingi wa mashauri yako [“washauri wako,” “NW”]; basi, na wasimame hao wajuao falaki [“waabudu wa mbingu,” “NW”], wazitazamao nyota, watabirio kila mwezi mambo ya mwezi huo, wakakuokoe na mambo yatakayokupata.” (Isaya 47:13)e Babiloni ataona wazi washauri wake wakishindwa vibaya sana. Ni kweli kwamba uchunguzi mwingi wa nyota utakuwa umefanywa kwa muda wa karne nyingi ili kusitawisha unajimu wa Babiloni. Lakini katika ule usiku wa anguko lake, wanajimu wake watakuwa hoi, ionekane wazi kwamba uaguzi ni kitu cha bure.—Danieli 5:7, 8.
20. Washauri wa Babiloni watapatwa na msiba gani?
20 Yehova anamalizia sehemu hii ya unabii kwa kusema hivi: “Tazama, watakuwa kama mabua makavu; moto utawateketeza; hawatajiokoa na nguvu za mwali wa moto; hautakuwa kaa la kukota moto, wala moto wa kukaa karibu nao. Ndivyo yatakavyokuwa mambo hayo uliyojitaabisha nayo; wale waliofanya biashara nawe tangu ujana wako watatanga-tanga mbali nawe, kila mtu akienda zake; hapatakuwa na mtu wa kukuokoa.” (Isaya 47:14, 15) Naam, hivi karibuni washauri hao waongo wataona mambo motomoto. Moto wenyewe si moto mtamu wa kuotwa na watu, bali utakuwa moto wa uharibifu na uteketezaji, utakaowafichua washauri hao waongo kuwa mabua ovyo. Basi si ajabu kwamba washauri wa Babiloni watatimua mbio za hofu ya kubabaika! Tegemeo la mwisho la Babiloni likiisha kutokomea, atakosa wa kumwokoa. Ataupata msiba ule ule atakaokuwa ameiletea Yerusalemu.—Yeremia 11:12.
21. Maneno ya unabii wa Isaya yanatimia jinsi gani na wakati gani?
21 Mwaka wa 539 K.W.K., maneno haya yaliyopuliziwa yanaanza kutimizwa. Majeshi ya Wamedi na Waajemi yanaongozwa na Koreshi kuliteka jiji na kumwua mfalme mkazi, Belshaza. (Danieli 5:1-4, 30) Kwa usiku mmoja, Babiloni kapinduliwa kutoka cheo chake cha kuutawala ulimwengu. Hivyo zinakoma karne nyingi za ukuu wa Washemu, na sasa ulimwengu unadhibitiwa na Waarya. Babiloni yenyewe inaanza kipindi cha karne nyingi za kuzorota. Kufikia karne ya nne W.K., Babiloni ni rundo la “magofu.” (Yeremia 51:37) Hivyo unabii wa Isaya umetimizwa kabisa.
-
-
Mwisho Wenye Kutazamisha wa Dini ya Uwongo Waonekana KimbeleUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Picha katika ukurasa wa 111]
Babiloni mtafuta-anasa atashushwa chini kwenye vumbi
[Picha katika ukurasa wa 114]
Wanajimu wa Babiloni watashindwa kutabiri anguko lake
-