-
Kutahini na Kupepeta Kuanzia NdaniMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Maoni ya Mafundisho Yaliyohitaji Kurekebishwa
Mashahidi wa Yehova hukubali waziwazi kwamba uelewevu wao wa kusudi la Mungu umepata marekebisho mengi kwa muda wa miaka. Jambo la kwamba ujuzi wa kusudi la Mungu ni wenye kuendelea lamaanisha kwamba ni lazima kuwe na badiliko. Si kwamba kusudi la Mungu hubadilika, lakini nuru ya elimu anayowapa watumishi wake kila wakati hutaka kuwe na marekebisho katika maoni yao.
Kutoka kwa Biblia Mashahidi huonyesha kwamba hilo lilikuwa kweli pia kuhusu watumishi waaminifu wa Mungu wakati uliopita. Abrahamu alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova; lakini alipoondoka Uru, mwanamume huyo wa imani hakujua nchi ambayo Mungu alikuwa akimwelekeza, na kwa miaka mingi hakuwa na uhakika kabisa jinsi Mungu angetimiza ahadi yake ya kufanyiza taifa kubwa kutoka kwake. (Mwa. 12:1-3; 15:3; 17:15-21; Ebr. 11:8) Mungu alifunua kweli nyingi kwa manabii, lakini kulikuwa na mambo mengine ambayo hawakuelewa wakati huo. (Dan. 12:8, 9; 1 Pet. 1:10-12) Vivyo hivyo, Yesu aliwaeleza mitume wake mambo mengi, lakini hata mwishoni mwa maisha yake ya kidunia aliwaambia kwamba bado kulikuwa na mambo mengi ya wao kujifunza. (Yn. 16:12) Baadhi ya mambo hayo, kama vile kusudi la Mungu kuwaleta Watu wa Mataifa katika kutaniko, hayakueleweka hadi mitume walipoona yale yaliyokuwa yakitukia hasa katika kutimiza unabii.—Mdo. 11:1-18.
Kama vile inavyoweza kutazamiwa, wakati mabadiliko yametaka kutupilia mbali maoni yaliyopendelewa hapo kwanza, hilo limetahini wengine. Isitoshe, si marekebisho yote katika uelewevu yamekuja mara moja tu. Kwa sababu ya kutokamilika, nyakati nyingine kuna mwelekeo wa kupita kiasi kabla ya msimamo sahihi kujulikana. Hilo laweza kuchukua wakati. Wengine walio na mbetuko wa kuwa wachambuzi wamejikwaa juu ya hilo. Fikiria kielelezo kimoja:
Mapema kama 1880, vichapo vya Watch Tower vilizungumzia mambo mbalimbali yanayohusiana na agano la Kiabrahamu, agano la Sheria, na agano jipya. Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imesahau ahadi ya Mungu kwamba kupitia mbegu ya Abrahamu familia zote za dunia kwa kweli zingejibarikia zenyewe. (Mwa. 22:18) Lakini Ndugu Russell alipendezwa sana na kujua jinsi Mungu angelitimiza hilo. Alidhani aliona katika maelezo ya Biblia ya Siku ya Ufuniko ya Wayahudi juu ya jinsi hilo lingetimizwa kuhusiana na agano jipya. Katika 1907, wakati maagano hayohayo yalipozungumzwa tena, mkazo wa pekee ukiwekwa kwenye jukumu la warithi-washirika wa Kristo katika kuletea wanadamu baraka zilizotabiriwa katika agano la Kiabrahamu, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia waliteta vikali.
Wakati huo kulikuwa na vipingamizi fulani kuhusiana na uelewevu mzuri wa mambo. Wanafunzi wa Biblia bado hawakuona kwa usahihi msimamo ambao Israeli wa asili alikuwa nao kuhusiana na kusudi la Mungu. Kizuizi hicho hakikuondolewa hadi ilipodhihirika waziwazi kwamba Wayahudi wakiwa watu hawakupendezwa kutumiwa na Mungu katika kutimiza neno lake la unabii. Kizuizi kingine kilikuwa kule kutoweza kwa Wanafunzi wa Biblia kutambulisha kwa usahihi “umati mkubwa” wa Ufunuo 7:9, 10. (NW) Utambulisho huo haukuwa wazi hadi umati mkubwa ulipoanza hasa kujidhihirisha wenyewe katika kutimiza unabii. Wale waliomchambua sana Ndugu Russell hawakuelewa mambo hayo pia.
Hata hivyo, kwa uwongo, wale waliodai kuwa ndugu Wakristo walishtaki kwamba The Watch Tower lilikuwa limekana kwamba Yesu siye Mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu, kwamba lilikuwa limeikataa katakata fidia na kukana uhitaji na uhakika wa kulipia (kufunika) dhambi. Hakuna lolote la mambo hayo lililokuwa la kweli. Lakini baadhi ya wale walioyasema walikuwa watu mashuhuri, na wakawavuta wengine baada yao kuwa wanafunzi. Huenda hawakukosea katika baadhi ya mambo waliyofundisha kuhusiana na agano jipya, lakini je, Bwana alibariki yale waliyokuwa wakifanya? Kwa wakati fulani, baadhi yao walifanya mikutano, lakini vikundi vyao vikatokomea mbali.
Kwa kutofautisha, Wanafunzi wa Biblia waliendelea kushiriki katika kuhubiri habari njema, kama vile Yesu alivyowaamuru wanafunzi wake. Wakati huohuo, waliendelea kujifunza Neno la Mungu na kutazama kuona matukio ambayo yangetia nuru juu ya maana yalo. Hatimaye, wakati wa miaka ya 1930, vizuizi vikuu vya uelewevu mzuri wa maagano viliondolewa, na taarifa zilizosahihishwa juu ya jambo hilo zilitokea kwenye Mnara wa Mlinzi na vichapo vilivyohusiana.d Hiyo ilileta shangwe iliyoje kwa wale waliokuwa wamengoja kwa subira!
Je, Matarajio Yao Yalikuwa Sahihi?
Nyakati nyingine Wanafunzi wa Biblia walikuwa na matumaini na matarajio ambayo yamedhihakiwa na wachambuzi. Na bado, shina la matumaini na matarajio hayo yote lilikuwa tamaa kubwa ya kuona kutimizwa kwa yale ambayo Wakristo hao wenye bidii walitambua kuwa ahadi zisizoshindwa za Mungu.
Kutokana na funzo lao la Maandiko yaliyopuliziwa, walijua kwamba Yehova alikuwa ameahidi baraka nyingi kwa mataifa yote ya dunia kupitia mbegu ya Abrahamu. (Mwa. 12:1-3; 22:15-18) Waliona ahadi katika Neno la Mungu kwamba Mwana wa binadamu angetawala akiwa Mfalme wa kimbingu juu ya dunia yote, kwamba kundi dogo la wale waaminifu lingechukuliwa kutoka duniani ili kushiriki naye katika Ufalme wake, na kwamba hao wangetawala wakiwa wafalme kwa miaka elfu. (Dan. 7:13, 14; Luka 12:32; Ufu. 5:9, 10; 14:1-5; 20:6) Walijua ahadi ya Yesu kwamba angerudi na kuwachukua wale ambao alikuwa amewatayarishia mahali mbinguni. (Yn. 14:1-3) Walijua ile ahadi kwamba Mesiya angechagua pia baadhi ya mababu walio waaminifu wawe wakuu duniani pote. (Zab. 45:16) Walitambua kwamba Maandiko yalitabiri juu ya mwisho wa mfumo wa mambo wa kale ulio mwovu na wakang’amua kwamba hilo lilishirikishwa na vita ya siku ile kuu ya Mungu Mweza Yote kwenye Har–Magedoni. (Mt. 24:3; Ufu. 16:14, 16) Walivutiwa sana na maandiko yaliyoonyesha kwamba dunia iliumbwa ili ikaliwe milele, kwamba wale walioishi juu yayo wangekuwa na amani ya kweli, na kwamba wote ambao wangedhihirisha imani katika dhabihu ya kibinadamu ya Yesu iliyo kamilifu wangefurahia uhai wa milele katika Paradiso.—Isa. 2:4; 45:18; Luka 23:42, 43; Yn. 3:16.
Ingetazamiwa kwamba wangejiuliza ni lini na jinsi gani mambo hayo yangetukia. Je, Maandiko yaliyopuliziwa yaliandaa dalili zozote?
Kwa kutumia kronolojia ya Biblia ambayo ilikuwa imeelezwa kwanza na Christopher Bowen wa Uingereza, walifikiri kwamba miaka 6,000 ya historia ya kibinadamu ilikwisha katika 1873, kwamba baada ya hapo walikuwa katika kipindi cha saba cha miaka elfu ya historia ya kibinadamu, na kwamba kwa hakika walikuwa wamekaribia mpambazuko wa ile Mileani iliyotabiriwa. Mfululizo wa vitabu uitwao Millennial Dawn (na baadaye uliitwa Studies in the Scriptures), ulioandikwa na C. T. Russell, ulivuta fikira kwenye maana ya hayo kulingana na yale ambayo Wanafunzi wa Biblia walielewa kutoka kwa Maandiko.
Jambo jingine lililoonwa kuwa laweza kuwa ishara nyingine ya wakati lilihusu mpango ambao Mungu alianzisha katika Israeli wa kale kwa ajili ya Yubile, mwaka wa kuachiliwa huru, kila mwaka wa 50. Huo ulikuja baada ya mfululizo wa vipindi saba vya miaka 7, kila kimoja chavyo kikiishia na mwaka wa sabato. Wakati wa mwaka wa Yubile, watumwa Waebrania waliwekwa huru na mashamba ya urithi yaliyokuwa yameuzwa yalirudishwa. (Law. 25:8-10) Hesabu zilizotegemea kipindi hiki cha miaka ziliongoza kwenye mkataa wa kwamba labda Yubile kubwa zaidi kwa dunia yote ilikuwa imeanza katika vuli ya 1874, kwamba ilionekana Bwana alikuwa amerudi katika mwaka huo na alikuwapo bila kuonekana, na kwamba “wakati wa urudisho wa vitu vyote” ulikuwa umefika.—Mdo. 3:19-21, KJ.
Wakitegemea wazo la kwamba labda matukio ya karne ya kwanza yangepata ufanani katika matukio mengine baadaye, walifanya mkataa pia kwamba ikiwa kubatizwa na kutiwa mafuta kwa Yesu katika vuli ya 29 W.K. kulifanana na mwanzo wa kuwapo kwake kusikoonekana katika 1874, basi kupanda kwake punda kuingia Yerusalemu akiwa Mfalme katika masika ya 33 W.K. kungeelekeza kwenye masika ya 1878 kuwa wakati ambao angepata uwezo wake akiwa Mfalme wa kimbingu.e Wao walifikiri pia kwamba wangepewa zawadi yao ya kimbingu wakati huo. Hilo lilipokosa kutukia, walifanya mkataa kwamba kwa kuwa wafuasi wa Yesu watiwa-mafuta wangeshiriki naye katika Ufalme, ufufuo kwenye uhai wa roho wa wale ambao tayari wanalala katika kifo ulianza wakati huo. Pia sababu zilitolewa kwamba mwisho wa upendeleo wa pekee wa Mungu kuelekea Israeli wa asili hadi kufikia 36 W.K. labda ulielekeza kwenye 1881 ukiwa wakati ambapo fursa ya pekee ya kuwa sehemu ya Israeli wa kiroho ingekoma.f
Katika hotuba “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe,” iliyotolewa na J. F. Rutherford mnamo Machi 21, 1920, katika jumba la Hippodrome katika New York City, fikira zilielekezwa kwenye mwaka 1925. Mwaka huo ulifikiriwa kuwa wa maana kwa msingi gani? Katika kijitabu kilichotangazwa mwaka huohuo, 1920, ilionyeshwa kwamba ikiwa Yubile kamili 70 zingehesabiwa kuanzia tarehe iliyofikiriwa kuwa ndiyo Waisraeli waliingia Bara Lililoahidiwa (badala ya kuanzia baada ya Yubile halisi ya mwisho kabla ya kuhamishiwa Babiloni na kisha kuhesabu hadi mwanzo wa mwaka wa Yubile mwishoni mwa kipindi cha miaka 50), hicho kingeweza kuelekeza kwenye mwaka 1925. Kwa msingi wa yale yaliyosemwa huko, wengi walitumaini kwamba labda waliobaki wa kundi dogo wangepokea zawadi yao ya kimbingu kufikia 1925. Mwaka huo pia ulihusishwa na matarajio ya ufufuo wa watumishi wa Mungu waaminifu wa kabla ya Ukristo kwa kusudi la kutumikia duniani wakiwa wawakilishi wakiwa na cheo cha wakuu wa Ufalme wa kimbingu. Ikiwa hilo lingetukia kikweli, lingemaanisha kwamba wanadamu walikuwa wameingia katika muhula ambao kifo kingekoma kuwa bwana mkubwa, na mamilioni wanaoishi wakati huo wangekuwa na tumaini la kutokufa kamwe duniani. Ni taraja la kupendeza kama nini! Ingawa walikosea, walishiriki taraja lao na wengine.
Baadaye, wakati wa miaka ya kuanzia 1935 hadi 1944, pitio la muundo wote wa kronolojia ya Biblia lilifunua kwamba kutafsiriwa vibaya kwa Matendo 13:19, 20 katika King James Version,g pamoja na mambo fulani mengineyo, kulikuwa kumesababisha kosa la kronolojia kwa zaidi ya karne moja.h Hilo liliongoza baadaye kwenye wazo—nyakati nyingine likisemwa kwa shaka, nyakati nyingine kwa uhakika—la kwamba mileani ya saba ya historia ya kibinadamu ingeanza katika 1975, matukio yanayoshirikishwa na kuanza kwa Utawala wa Mileani wa Kristo labda yangeanza kutukia wakati huo.
Je, imani za Mashahidi wa Yehova katika mambo hayo zilithibitika kuwa sahihi? Kwa kweli hawakukosea katika kuamini kwamba Mungu bila shaka angefanya yale aliyoahidi. Lakini baadhi ya hesabu zao za wakati na matarajio waliyoshirikisha pamoja nayo yalisababisha kuvunjika moyo sana.
Kufuatia 1925, hudhurio la mikutano lilishuka kwa kutazamisha katika makutaniko mengine katika Ufaransa na Uswisi. Tena, katika 1975, ilivunja moyo wakati matarajio yaliyohusu kuanza kwa Mileani yalipokosa kutokea. Kama tokeo, wengine waliacha tengenezo. Wengine walitengwa, kwa sababu walitaka kupotosha imani ya washiriki. Bila shaka, kuvunjika moyo kwa sababu ya tarehe kulisababisha hayo, lakini katika pindi nyingine kulikuwa na sababu za ndani zaidi. Baadhi ya watu pia walibisha dhidi ya uhitaji wa kushiriki katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Wengine wao hawakuchagua tu kuacha tengenezo; walikuwa wagomvi katika kupinga tengenezo ambalo walikuwa wameshirikiana nalo, na walitumia magazeti ya habari na televisheni ili kujulisha maoni yao. Hata hivyo, idadi ya waliokengeuka ilikuwa ndogo kwa kulinganisha.
Ingawa mitihani hiyo ilifanya wengine wakapepetwa na kupeperushwa mbali kama makapi wakati ngano inapopurwa, wengine walibaki imara. Kwa nini? Kuhusu ono lake mwenyewe na maono ya wengine katika 1925, Jules Feller alieleza: “Wale walioweka tumaini lao katika Yehova walibaki imara na wakaendelea na utendaji wao wa kuhubiri.” Walitambua kwamba kosa lilikuwa limefanywa lakini kwamba Neno la Mungu halikuwa limeshindwa hata kidogo, na kwa hiyo hakukuwa na sababu ya ama kuacha tumaini lao wenyewe lididimie ama kupunguza mwendo wa kazi ya kuelekeza watu kwenye Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la wanadamu.
Baadhi ya matarajio hayakutimizwa, lakini hilo halikumaanisha kwamba kronolojia ya Biblia haikuwa na thamani yoyote. Unabii uliorekodiwa na Danieli kuhusu kutokea kwa Mesiya majuma 69 ya miaka baada ya “kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu” ulitimizwa kwa wakati barabara, katika 29 W.K.i (Dan. 9:24-27) Mwaka 1914 pia ulitiwa alama na unabii wa Biblia.
1914—Matarajio na Uhalisi
Katika 1876, C. T. Russell aliandika makala ya kwanza kati ya nyingine ambamo alionyesha mwaka 1914 kuwa mwisho wa Nyakati za Mataifa zilizorejezewa na Yesu Kristo. (Luka 21:24, KJ) Katika buku la pili la Millennial Dawn, lililotangazwa katika 1889, Ndugu Russell alionyesha mambo mengi ya kutoa sababu ambayo yangewezesha wasomaji kuona msingi wa Kimaandiko wa yale yaliyosemwa na kujichunguzia wenyewe. Katika kipindi cha karibu karne nne kilichoongoza hadi 1914, Wanafunzi wa Biblia waligawanya mamilioni ya nakala za vichapo vilivyokazia fikira kwenye mwisho wa Nyakati za Mataifa. Vichapo vingine vichache vya kidini vilitambua kronolojia ya Biblia iliyoelekeza kwenye mwaka 1914, lakini ni kikundi gani isipokuwa kile cha Wanafunzi wa Biblia kilichoendelea kuitangaza kimataifa na kuishi katika njia iliyoonyesha kwamba waliamini kwamba Nyakati za Mataifa zingeisha mwaka huo?
Mwaka 1914 ulipokaribia, matarajio yalipanda. Ungeleta nini? Katika The Bible Students Monthly (Buku 6, Na. 1, lililotangazwa mapema katika 1914), Ndugu Russell aliandika: “Ikiwa tuna tarehe na kronolojia sahihi, Nyakati za Mataifa zitakwisha mwaka huu—1914. Maana yake nini? Hatujui kwa uhakika. Tarajio letu ni kwamba utawala wenye utendaji wa Mesiya utaanza karibu na wakati wa mwisho wa kipindi cha utawala cha Mataifa. Tarajio letu, liwe kweli au si kweli, ni kwamba kutakuwako madhihirisho ya ajabu ya hukumu ya Kimungu dhidi ya ukosefu wote wa haki, na kwamba hilo litamaanisha kuvunjwa kwa mifumo mingi ya wakati huu, ikiwa si yote.” Alikazia kwamba hakutazamia “mwisho wa ulimwengu” katika 1914 na kwamba dunia yadumu milele, lakini kwamba utaratibu wa mambo wa sasa, ambao Shetani ndiye mtawala, utapitilia mbali.
Katika toleo lalo la Oktoba 15, 1913, The Watch Tower lilikuwa limesema: “Kulingana na ufahamu bora zaidi wa kronolojia tuwezao, ni karibu wakati huo—iwe ni Oktoba 1914, au baadaye. Bila kushikilia kauli, tunatazamia matukio fulani: (1) Mwisho wa Nyakati za Mataifa—utawala wa Mataifa ulimwenguni—na (2) Kuanzishwa kwa Ufalme wa Mesiya ulimwenguni.”
Hilo lingetukiaje? Ilionekana kuwa yafaa kwa Wanafunzi wa Biblia wakati huo kwamba huko kungetia ndani utukuzo wa wowote walio duniani bado ambao walikuwa wamechaguliwa na Mungu kushiriki katika Ufalme wa kimbingu pamoja na Kristo. Lakini walihisije wakati hilo lilipokosa kutukia katika 1914? The Watch Tower la Aprili 15, 1916, lilisema: “Tunaamini kwamba tarehe zimethibitika kuwa sahihi kikweli. Tunaamini kwamba Nyakati za Mataifa zimekwisha.” Hata hivyo, uliongezea hivi waziwazi: “Bwana hakusema kwamba Kanisa lote lingetukuzwa kufikia 1914. Tulifanya mkataa huo tu na, bila shaka tukakosea.”
Katika jambo hilo walikuwa kama mitume wa Yesu. Mitume walijua na walifikiri waliamini unabii mbalimbali kuhusu Ufalme wa Mungu. Lakini katika nyakati mbalimbali walikuwa na matarajio yenye makosa kuhusu ni jinsi gani na lini hayo yangetimizwa. Hilo lilifanya wengine wakate tamaa.—Luka 19:11; 24:19-24; Mdo. 1:6.
Wakati Oktoba 1914 ulipopita bila badiliko lililotazamiwa la uhai wa kimbingu, Ndugu Russell alijua kwamba kungekuwako kujipekuapekua sana moyo. Katika The Watch Tower la Novemba 1, 1914, aliandika: “Acheni tukumbuke kwamba sisi tumo katika majira ya kutahini. Mitume walikuwa na majira kama hayo wakati wa muda wa kati ya kifo cha Bwana na Pentekoste. Baada ya kufufuliwa kwa Bwana, Yeye alitokea wanafunzi Wake mara chache, na hawakumwona Yeye kwa siku nyingi. Kisha wakakata tamaa na kusema, ‘Hakuna haja ya kungoja’; ‘Ninaenda kuvua samaki,’ mmoja akasema. Wengine wawili wakasema, ‘Tutaenda nawe.’ Walitaka kwenda kwenye biashara ya uvuvi na kuacha kazi ya kuvua watu. Huo ulikuwa wakati wenye kutahini kwa wanafunzi. Vivyo hivyo wakati huo upo sasa. Ikiwa kuna sababu yoyote ambayo ingeongoza yeyote kuacha Bwana na Kweli Yake na kuacha kutoa dhabihu kwa ajili ya Kusudi la Bwana, basi si upendo wa Mungu tu ndani ya moyo ambao umesukuma kupendezwa katika Bwana, bali jambo jingine; labda kutumaini kwamba wakati ulikuwa mfupi; kujitakasa kulikuwa kwa wakati fulani tu.”
Mambo yalionekana kuwa hivyo kwa watu fulani. Fikira na tamaa zao zilikuwa zimekazwa hasa juu ya taraja la kuweza kubadilishwa kwenye uhai wa kimbingu. Hilo lilipokosa kutukia katika wakati uliotarajiwa, walikosa kuona maana ya mambo yenye kushangaza yaliyotukia katika 1914. Walikosa kutambua kweli zote zenye thamani ambazo walikuwa wamejifunza kutoka kwa Neno la Mungu, na wakaanza kuwadhihaki watu ambao walikuwa wamewasaidia kujifunza hizo.
Kwa unyenyekevu, Wanafunzi wa Biblia walichunguza Maandiko tena, ili waache Neno la Mungu libadilishe mtazamo wao. Usadikisho wao kwamba Nyakati za Mataifa zilikuwa zimekwisha mwaka 1914 haukubadilika. Hatua kwa hatua walikuja kuona waziwazi zaidi jinsi Ufalme wa Kimesiya ulivyokuwa umeanza—kwamba ulisimamishwa mbinguni wakati Yehova alipokabidhi mamlaka kwa Yesu Kristo, Mwanae; pia, kwamba hilo halikuhitaji kungojea hadi warithi-washiriki wa Yesu wainuliwe kwenye uhai wa kimbingu bali kwamba wangetukuzwa naye baadaye. Kwa kuongezea, walikuja kuona kwamba kuenezwa kwa uvutano wa Ufalme hakukuhitaji kwanza manabii waaminifu wa zamani wafufuliwe, bali Mfalme angetumia Wakristo waaminifu-washikamanifu wanaoishi sasa kuwa wawakilishi wake kuwatolea watu wa mataifa yote fursa ya kuishi milele wakiwa raia wa kidunia wa Ufalme.
Mwono huo mtukufu ulipofunuka machoni pao, walitahiniwa na kupepetwa zaidi. Lakini wale waliompenda Yehova kikweli na wakafurahi kumtumikia walikuwa wenye shukrani kwa mapendeleo ya utumishi yaliyofunguka kwa ajili yao.—Ufu. 3:7, 8.
Mmoja wao alikuwa A. H. Macmillan. Baadaye aliandika: “Ingawa mataraja yetu kuhusu kuchukuliwa hadi mbinguni hayakutimizwa katika 1914, mwaka huo ndio uliokuwa mwisho wa Nyakati za Mataifa . . . Hatukusikitika sana hasa kwamba kila kitu hakikutukia kama vile tulivyokuwa tumetazamia, kwa sababu tulikuwa wenye shughuli mno na kazi ya Photo-Drama na matatizo yaliyoletwa na vita.” Yeye aliendelea kuwa mwenye shughuli katika utumishi wa Yehova na alisisimuliwa kuona idadi ya wapiga-mbiu wa Ufalme ikiongezeka kufikia zaidi ya milioni moja wakati wa maisha yake.
Akitazama nyuma kwenye mambo aliyoona wakati wa miaka 66 katika tengenezo, yeye alisema: “Nimeona majaribu mengi makali yakikumba tengenezo na kutahiniwa kwa imani ya wale waliomo. Kwa msaada wa roho ya Mungu tengenezo liliokoka na likaendelea kusitawi.” Kuhusu marekebisho ya uelewevu kadiri wakati ulivyopita, yeye aliongeza: “Kweli za msingi tulizojifunza kutoka kwa Maandiko zilibaki vilevile. Kwa hiyo nilijifunza kwamba tunapaswa kukubali makosa yetu na kuendelea kutafuta katika Neno la Mungu ili kupata nuru zaidi. Hata iwe ni mabadiliko gani ambayo tungelazimika kufanya wakati mmoja au mwingine katika maoni yetu, hilo halingebadili uandalizi wa fadhili wa fidia na ahadi ya Mungu ya uhai wa milele.”
-
-
Kutahini na Kupepeta Kuanzia NdaniMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 634]
C. J. Woodworth
Akiandikia mmoja aliyeacha utumishi wa Yehova kwa sababu wafuasi wa Yesu Kristo watiwa-mafuta hawakuchukuliwa hadi mbinguni katika 1914, C. J. Woodworth alisema:
“Miaka 20 iliyopita wewe na mimi tuliamini katika ubatizo wa vitoto; katika haki ya Kimungu ya makasisi kutoa ubatizo huo; kwamba ubatizo ulikuwa wa lazima ili kuepuka mateso ya milele; kwamba Mungu ni upendo; kwamba Mungu aliumba na aendelea kuumba mabilioni ya viumbe katika mfano Wake ambao kwa mihula ya umilele watakuwa kwenye mioto yenye kusonga ya kiberiti chenye kuwaka, wakiomba tone moja la maji lipunguze uchungu wao bila kufanikiwa . . .
“Tuliamini kwamba baada ya mtu kufa, yeye yuko hai; tuliamini kwamba Yesu Kristo hakufa kamwe; kwamba Yeye hangeweza kufa; kwamba hakuna Fidia iliyopata kulipwa au itapata kulipwa; kwamba Yehova Mungu na Kristo Yesu Mwana Wake ni mtu yuleyule mmoja; kwamba Kristo alikuwa ndiye Baba Yake mwenyewe; kwamba Yesu alikuwa ndiye Mwana Wake mwenyewe; kwamba Roho Takatifu ni mtu; kwamba moja kuongeza moja, kuongeza moja, tokeo ni moja; kwamba wakati Yesu alipotundikwa kwenye msalaba na kusema, ‘Mungu Wangu, Mungu Wangu, mbona Umeniacha,’ Yeye alikuwa tu akijisemeza; . . . kwamba falme za sasa ni sehemu ya Ufalme wa Kristo; kwamba Ibilisi amekuwa mbali mahali fulani katika Helo isiyojulikana mahali ipo, badala ya kuwa na umiliki juu ya falme za dunia hii . . .
“Ninamsifu Mungu kwa siku ambayo alileta Kweli ya Sasa mlangoni pangu. Ilikuwa yenye kufaa sana, yenye kuburudisha akili na moyo sana, hivi kwamba niliacha upesi uwongo na mambo ya upuuzi ya zamani na nikatumiwa na Mungu kufungua pia macho yako yaliyopofushwa. Tulishangilia pamoja katika Kweli, tukifanya kazi pamoja kwa miaka kumi na mitano. Bwana alikustahi sana ukiwa msemaji; Sikupata kamwe kumjua mtu ambaye angeweza kufunua uwongo wa Babiloni kama wewe. Katika barua yako unauliza, ‘Ni nini kinachofuata?’ Lo! sasa ndiyo sehemu yenye kuhuzunisha! Kitu kinachofuata ni kwamba unaruhusu moyo wako umchukie yule ambaye kazi zake za upendo na baraka zake kutoka Juu zilileta Kweli kwa mioyo yetu sote wawili. Uliacha tengenezo, na kuchukua kondoo kadhaa pamoja nawe. . . .
“Labda ninaonekana kuwa mpuuzi kwako kwa sababu sikuenda Mbinguni, Oktoba 1, 1914, lakini wewe huonekani kuwa mpuuzi kwangu—la hasha!
“Wakati huu ambapo mataifa kumi makubwa kati ya mataifa ya dunia yanafurukuta katika uchungu mkali wa kifo chayo, kwangu inaonekana kuwa wakati usiofaa hasa kumdhihaki mtu huyo, na mtu pekee, ambaye kwa miaka arobaini amefundisha kwamba Nyakati za Mataifa zingekoma katika 1914.”
Imani ya Ndugu Woodworth haikutikisika wakati matukio ya 1914 yalipokosa kutimiza yale yaliyotarajiwa. Yeye aling’amua tu kwamba kulikuwa na mengi zaidi ya kujifunza. Kwa sababu ya tumaini lake katika kusudi la Mungu, alifungwa miezi tisa gerezani katika 1918-1919. Baadaye alitumikia akiwa mhariri wa magazeti “The Golden Age” na “Consolation.” Alibaki imara katika imani na mwaminifu-mshikamanifu kwa tengenezo la Yehova hadi kufikia kifo chake katika 1951, akiwa mwenye umri wa miaka 81.
-