Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Makasisi Waomba Kuwe na Mjadala wa Hadhara

      Mwenezo wa maandishi ya C. T. Russell ulipoongezeka upesi kufikia makumi ya mamilioni ya nakala katika lugha nyingi, makasisi Wakatoliki na Waprotestanti hawangeweza kupuuza kwa urahisi yale aliyokuwa akisema. Wakighadhibishwa na kule kufunuliwa kwa mafundisho yao kuwa yasiyo ya Kimaandiko, na wakifadhaishwa kwa kuwapoteza washiriki, makasisi wengi walitumia mimbari yao ili kushutumu maandishi ya Russell. Waliwaamuru makundi yao yasikubali fasihi zinazogawanywa na Wanafunzi wa Biblia. Idadi fulani yao walijaribu kuwachochea maofisa wa umma wakomeshe kazi hiyo. Katika sehemu nyingine katika Marekani—miongoni mwazo Tampa, Florida; Rock Island, Illinois; Winston-Salem, North Carolina; na Scranton, Pennsylvania—walisimamia kuchomwa hadharani kwa vitabu vilivyoandikwa na Russell.

      Baadhi ya makasisi walihisi uhitaji wa kuangamiza uvutano wa Russell kwa kumfunua katika mjadala wa hadhara. Karibu na makao makuu ya utendaji wake, kikundi cha makasisi kilipendekeza Dakt. E. L. Eaton, pasta wa Kanisa la Methodisti ya Kiepiskopali ya North Avenue katika Allegheny, Pennsylvania, awe msemaji wacho. Katika 1903 yeye alidokeza kuwe na mjadala wa hadhara, na Ndugu Russell alikubali huo mwaliko.

      Mambo sita ya kujadiliwa yalijulishwa kama ifuatavyo: Ndugu Russell alithibitisha, lakini Dakt. Eaton akakana, kwamba nafsi za wafu hazitambui lolote; kwamba “kuja kwa pili” kwa Kristo kunatangulia Mileani na kwamba kusudi la “kuja [kwake] kwa pili” na Mileani pia ni kubarikiwa kwa familia zote za dunia; pia kwamba ni watakatifu wa “kipindi cha Gospeli” tu wanaoshiriki katika ufufuo wa kwanza lakini kwamba halaiki kubwa watakuwa na fursa ya kuokoka kwa ufufuo unaofuata. Dakt. Eaton alithibitisha, lakini Ndugu Russell akakana, kwamba mtu yeyote hangejaribiwa baada ya kufa; kwamba wote wanaookolewa wataenda mbinguni; na kwamba waovu watundu watateswa milele. Mfululizo wa mijadala sita juu ya mambo hayo ulifanywa, kila mjadala mbele ya umati uliojaza Jumba la Carnegie katika Allegheny mwaka 1903.

      Ni nini kilichochochea mwito huo wa kuwa na mjadala? Akitazama jambo hilo katika mwono wa kihistoria, Albert Vandenberg aliandika hivi baadaye: “Mijadala iliongozwa na mhubiri kutoka dhehebu tofauti la Protestanti akiwa msimamizi wakati wa kila kikao cha mazungumzo. Kwa kuongezea, wahubiri kutoka makanisa mbalimbali ya karibu waliketi kwenye jukwaa la msemaji pamoja na Mwadhama Eaton, inasemekana ili kumpa utegemezo wa kimaandiko na kumuunga mkono. . . . Jambo la kwamba muungano wa makasisi Waprotestanti usio rasmi ungeweza kufanyizwa lilionyesha kwamba waliogopa uwezo wa Russell wa kuwaongoa washiriki wa madhehebu yao.”—“Charles Taze Russell: Nabii wa Pittsburgh, 1879-1909,” iliyochapwa katika The Western Pennsylvania Historical Magazine, Januari 1986, uku. 14.

      Mijadala kama hiyo kidogo ilikuwa michache. Haikuwa na matokeo yaliyotakwa na muungano wa makasisi. Baadhi ya watu wa kutaniko la Dakt. Eaton walivutiwa na yale waliyosikia wakati wa mfululizo wa mihadhara katika 1903, wakaacha kanisa lake na kuchagua kushirikiana na Wanafunzi wa Biblia. Hata kasisi mmoja aliyekuwako alikiri kwamba Russell alikuwa ‘ameelekeza bomba la maji kwenye helo na kuuzima moto huo.’ Hata hivyo, Ndugu Russell mwenyewe alihisi kwamba kusudi la ile kweli lingeweza kutimizwa vema zaidi kwa kutumia wakati na jitihada katika utendaji mwingineo badala ya mijadala.

      Makasisi hawakuacha mashambulizi yao. Ndugu Russell alipozungumza katika Dublin, Ireland, na Otley, Yorkshire, Uingereza, waliweka wanaume miongoni mwa wasikilizaji ili wapaaze sauti wakipinga na kutoa mashtaka bandia dhidi ya Russell mwenyewe. Ndugu Russell alishughulikia hali hizo kwa ustadi, wakati wote akitegemea Biblia kuwa mamlaka kwa majibu yake.

      Bila kujali dhehebu, makasisi Waprotestanti walishirikiana katika ule ulioitwa Muungano wa Kievanjeli. Wawakilishi wao katika nchi nyingi walikuwa wachochezi dhidi ya Russell na wale waliogawanya fasihi zake. Katika Texas (Marekani), kwa kielelezo, Wanafunzi wa Biblia walipata kwamba kila kasisi, hata katika miji na wilaya za mashambani zilizo ndogo zaidi, alikuwa na aina ileile ya mashtaka bandia dhidi ya Russell na upotovu uleule wa yale aliyofundisha.

      Hata hivyo, nyakati nyingine mashambulizi dhidi ya Russell yalikuwa na matokeo ambayo makasisi hawakutarajia. Katika New Brunswick, Kanada, wakati mhubiri alipotumia mimbari yake ili kutoa hotuba yenye kuvunjia heshima Russell, miongoni mwa wasikilizaji kulikuwa na mtu aliyekuwa amesoma binafsi fasihi zilizoandikwa na Ndugu Russell. Aliudhika wakati mhubiri alipotumia uwongo wa kukusudia. Karibu na katikati ya hotuba, mtu huyo alisimama, akamshika mke wake kwa mkono, na kuwaita mabinti wake saba walioimba katika kwaya: “Njooni wasichana, tunaenda nyumbani.” Wote tisa walitoka nje, na mhubiri akatazama huku yule mtu aliyekuwa amejenga kanisa na alikuwa mwandalizi mkuu wa fedha za kutaniko alipoondoka. Upesi kutaniko likatokomea, na mhubiri huyo akaenda zake.

      Kutumia Dhihaka na Uchongezi

      Katika jitihada zao nyingi za kuangamiza uvutano wa C. T. Russell na washiriki wake, makasisi walipuuza dai kwamba yeye alikuwa mhudumu Mkristo. Kwa sababu hizohizo, viongozi wa kidini Wayahudi katika karne ya kwanza waliwatendea mitume Petro na Yohana kama “watu wasio na elimu na wa kawaida tu.”—Mdo. 4:13, NW.

      Ndugu Russell hakuwa amehitimu kutoka mojawapo shule za kitheolojia za Jumuiya ya Wakristo. Lakini alisema hivi kwa ujasiri: “Tunawatolea [makasisi] mwito wa ushindani wathibitishe kwamba walikuwa wametawazwa Kimungu au kwamba wamepata kufikiri juu yalo. Wao hufikiri tu juu ya kutawazwa kimafarakano, au kuagizwa, kila mmoja kutoka kwa farakano au kikundi chake. . . . Kutawazwa au kuagizwa na Mungu kwa mtu yeyote ili ahubiri ni kwa kupewa Roho Takatifu. Mtu yeyote ambaye amepokea Roho Takatifu amepokea uwezo na mamlaka ya kufundisha na kuhubiri katika jina la Mungu. Mtu yeyote ambaye hajapokea Roho Takatifu hana mamlaka au idhini ya Kimungu ya kuhubiri kwake.”—Isa. 61:1, 2.

      Ili kutilia shaka sifa yake, baadhi ya makasisi walihubiri na kuchapisha uwongo mbaya juu yake. Mojawapo waliyotumia mara nyingi—na bado hutumia—linahusu hali ya ndoa ya Ndugu Russell. Maoni ambayo wamejaribu kuonyesha ni kwamba Russell alikosa maadili. Mambo hakika ni yapi?

      Katika 1879, Charles Taze Russell alioa Maria Frances Ackley. Walikuwa na uhusiano mzuri kwa miaka 13. Kisha, wengine walipombembeleza Maria na kwa vile yeye alikuwa na mwelekeo wa kiburi, uhusiano huo ulianza kudhoofika; lakini kusudi lao lilipojulikana, ni kama alipata usawaziko wake tena. Baada ya mtu aliyekuwa mshiriki kueneza mambo ya uwongo kuhusu Ndugu Russell, yeye hata alimwuliza ruhusa mume wake ili azuru makutaniko kadhaa ili akanushe mashtaka hayo, kwa kuwa ilikuwa imesemekana kuwa Ndugu Russell alimkandamiza. Hata hivyo, inaonekana kwamba upokezi mwema aliopata kwenye safari hiyo katika 1894 ulisababisha badiliko la hatua kwa hatua la jinsi alivyojiona. Alijaribu kupata uwezo zaidi katika kuelekeza yale ambayo yangewekwa katika Watch Tower.a Alipong’amua kwamba hakuna chochote alichoandika ambacho kingechapwa isipokuwa mume wake, aliye mhariri wa gazeti hilo, akubaliane na yaliyomo (kwa msingi wa upatano wayo na Maandiko), aliudhika sana. Russell alitia jitihada nyingi ili kumsaidia, lakini katika Novemba 1897 Maria alimwacha. Hata hivyo, alimwandalia mahali pa kuishi na utegemezo mwingineo. Miaka mingi baadaye, baada ya mashtaka ya mahakamani aliyokuwa amepeleka katika 1903, Maria alipata uamuzi katika 1908, si wa talaka kamili, bali wa haki ya kisheria ya kutoishi na Russell, huku Maria akipokea malipo kutoka kwake.

      Baada ya kushindwa kumlazimisha mume wake akubaliane na matakwa yake, alitia jitihada nyingi baada ya yeye kumwacha ili kuharibu sifa ya jina lake. Katika 1903 alichapisha trakti iliyojaa, si kweli za Kimaandiko, bali masingizio mabaya juu ya Ndugu Russell. Alijaribu kuwatumia wahubiri wa madhehebu mbalimbali ili wazigawanye mahali ambapo Wanafunzi wa Biblia walikuwa wakifanya mikutano ya pekee. Wahubiri hao wanastahili kupewa sifa kwa sababu si wengi wakati huo waliotaka kutumiwa kwa njia hiyo. Hata hivyo, tangu wakati huo makasisi wengine wameonyesha roho tofauti.

      Hapo awali, Maria Russell alikuwa ameshutumu, kwa mdomo na kwa maandishi, wale waliomshtaki Ndugu Russell na aina ya ukosefu wa adili ambao yeye mwenyewe alimshtaki nao. Wakitumia taarifa fulani zisizothibitishwa zilizofanywa wakati wa mashtaka ya mahakamani katika 1906 (taarifa ambazo zilifutwa katika rekodi kwa amri ya mahakama), baadhi ya wapinzani wa kidini wa Ndugu Russell wamechapisha mashtaka yaliyofanywa yaonekane kana kwamba alikuwa mtu asiye na maadili na hivyo hafai kuwa mhudumu wa Mungu. Hata hivyo, rekodi ya mahakama iko wazi kwamba mashtaka kama hayo si ya kweli. Wakili wake mwenyewe alimuuliza Bi. Russell kama aliamini mume wake alikuwa na hatia ya uzinzi. Yeye alijibu: “La.” Pia ni jambo linalostahili kuangaliwa kwamba wakati halmashauri ya wazee Wakristo iliposikiliza mashtaka ya Bi. Russell dhidi ya mume wake katika 1897, hakutaja yoyote ya mambo aliyosema baadaye mahakamani ili kusadikisha wasaidizi wa hakimu kwamba talaka yapaswa itolewe, ingawa matukio hayo yaliyosingiziwa yalitukia kabla ya mkutano huo.

      Miaka tisa baada ya Bi. Russell kuwasilisha kesi hiyo mahakamani kwa mara ya kwanza, Hakimu James Macfarlane aliandika barua ya majibu kwa mtu aliyekuwa akitafuta nakala ya rekodi ya mahakama ili mmoja wa washiriki wake amfunue Russell. Hakimu alimwambia waziwazi kwamba kile alichotaka kingekuwa ni kupoteza wakati na pesa. Barua yake ilisema: “Msingi wa mashtaka yake na wa amri iliyotolewa baada ya uamuzi wa wasaidizi wa hakimu ulikuwa ‘ufidhuli’ na si uzinzi na kama ninavyoelewa, ushuhuda hauonyeshi kwamba Russell alikuwa akiishi ‘maisha ya uzinzi na mwenzi mwingine.’ Kwa kweli hakukuwa na mwenzi mwingine.”

      Ungamo lililochelewa la Maria Russell mwenyewe lilikuja wakati wa maziko ya Ndugu Russell kwenye Jumba la Carnegie katika Pittsburgh mwaka 1916. Akiwa amevaa utaji, alitembea katika kijia kilicho kati ya viti hadi kwenye jeneza na kuweka hapo furushi la maua-lili ya bondeni. Kulikuwa na utepe uliofungishwa wenye maneno, “Kwa Mume Wangu Mpendwa.”

      Ni wazi kwamba makasisi wametumia aina ileile ya mbinu zilizotumiwa na wenzao wa karne ya kwanza. Wakati ule, walijaribu kuharibu sifa ya Yesu kwa kushtaki kwamba alikuwa pamoja na watenda dhambi na kwamba yeye mwenyewe alikuwa mtenda dhambi na mkufuru. (Mt. 9:11; Yn. 9:16-24; 10:33-37) Mashtaka ya aina hiyo hayakubadili kweli kuhusu Yesu, lakini yalifunua wale walioamua kutumia uchongezi huo—na yanafunua wale wanaoamua kutumia mbinu hizohizo leo—kuwa baba yao wa kiroho ni Ibilisi, jina linalomaanisha “Mchongezi.”—Yn. 8:44.

      Kutumia Harara ya Wakati wa Vita ili Kutimiza Malengo Yao

      Huku kukiwa na harara ya utukuzo wa taifa uliokumba ulimwengu wakati wa vita ya ulimwengu ya kwanza, silaha mpya ilipatikana ili itumiwe dhidi ya Wanafunzi wa Biblia. Uadui wa viongozi wa kidini wa Protestanti na Katoliki ya Roma ungeweza kuonyeshwa kwa kutumia kisitiri cha uzalendo. Walitumia msisimko wa wakati wa vita kwa faida yao ili kuwashtaki Wanafunzi wa Biblia kuwa wachochezi—shtaka lilelile ambalo lilielekezwa kwa Yesu Kristo na mtume Paulo na viongozi wa kidini wa Yerusalemu wa karne ya kwanza. (Luka 23:2, 4; Mdo. 24:1, 5) Bila shaka, ili makasisi wafanye shtaka hilo, wao wenyewe wangelazimika kuwa waungaji mkono walio watendaji wa vita, lakini hilo halikuonekana kuwa likiwasumbua wengi wao, hata ingawa lilimaanisha kutuma vijana wakawaue washiriki wa dini yao wenyewe katika nchi nyingine.

      Ilikuwa katika Julai 1917, baada ya kifo cha Russell, kwamba Watch Tower Society ilitoa kitabu The Finished Mystery, ufafanuzi juu ya Ufunuo na Ezekieli pamoja na Wimbo Ulio Bora. Kitabu hicho kilifunua waziwazi unafiki wa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo! Kiligawanywa sana kwa wakati mfupi. Mwishoni mwa Desemba 1917 na mapema katika 1918, Wanafunzi wa Biblia katika Marekani na Kanada pia walianza kugawanya nakala 10,000,000 za ujumbe wenye kuchoma katika trakti The Bible Students Monthly. Trakti hiyo ya kurasa nne yenye ukubwa wa kiasi ilikuwa na kichwa “Kuanguka kwa Babiloni,” na ilikuwa na kichwa kidogo “Sababu Kwa Nini Ni Lazima Jumuiya ya Wakristo Iteseke Sasa—Tokeo la Mwisho.” Ilitambulisha matengenezo ya kidini ya Katoliki na Protestanti yakiwa pamoja kuwa Babiloni ya kisasa, ambayo lazima ianguke hivi karibuni. Katika kuunga mkono yale yaliyosemwa, ilitokeza tena kutoka kitabu The Finished Mystery mafafanuzi juu ya unabii mbalimbali unaoonyesha hukumu ya kimungu dhidi ya “Babiloni wa Kifumbo.” Kwenye ukurasa wa nyuma kulikuwa na katuni iliyochorwa kuonyesha ukuta ukiporomoka. Mawe makubwa kutoka kwenye ukuta huo yalikuwa na vibandiko kama vile “Fundisho la Utatu (‘3 X 1 = 1’),” “Kutokufa kwa Nafsi,” “Nadharia ya Mateso ya Milele,” “Uprotestanti—mafundisho, makasisi, n.k.,” “Uroma—mapapa, makadinali, n.k., n.k.”—na mawe hayo yote yalikuwa yakianguka.

      Makasisi walighadhibishwa na kufunuliwa huko, kama vile makasisi wa Kiyahudi walivyoghadhibika wakati Yesu alipofunua unafiki wao. (Mt. 23:1-39; 26:3, 4) Katika Kanada makasisi walitenda upesi. Katika Januari 1918, makasisi zaidi ya 600 wa Kanada walitia sahihi ombi lenye kusihi serikali izuie vichapo vya Shirika la Kimataifa la Wanafunzi wa Biblia. Kama ilivyoripotiwa katika Winnipeg Evening Tribune, baada ya Charles G. Paterson, pasta wa Kanisa la St. Stephen katika Winnipeg, kushutumu kutoka kwenye mimbari The Bible Students Monthly, iliyokuwa na makala “Kuanguka kwa Babiloni,” Mkuu wa Sheria Johnson aliwasiliana naye ili apate nakala. Punde baadaye, Februari 12, 1918, amri ya serikali ya Kanada ilifanya liwe kosa linalostahili adhabu ya kutozwa faini na kufungwa gerezani, mtu akipatikana ana ama kitabu The Finished Mystery ama trakti inayoonyeshwa juu.

      Mwezi huohuo, mnamo Februari 24, Ndugu Rutherford, msimamizi mpya aliyechaguliwa wa Watch Tower Society, alihutubu katika Marekani kwenye Jumba la Temple jijini Los Angeles, California. Kichwa cha habari yake kilishtusha: “Ulimwengu Umekwisha—Mamilioni Wanaoishi Sasa Huenda Wasife Kamwe.” Katika kutoa ithibati kwamba ulimwengu kama ulivyojulikana kufikia wakati huo kwa kweli ulikuwa umekwisha katika 1914, alielekeza kwenye vita iliyokuwa ikiendelea, pamoja na njaa yenye kuandamana, na kuitambulisha kuwa sehemu ya ishara iliyotabiriwa na Yesu. (Mt. 24:3-8) Kisha alielekeza fikira kwa makasisi, akisema:

      “Wakiwa jamii, kulingana na maandiko, makasisi ndio watu wenye kulaumika zaidi duniani kwa sababu ya vita kuu inayokumba wanadamu sasa. Kwa miaka 1,500 wamefundisha watu fundisho la kishetani la haki ya kimungu ya watawala kuweza kumiliki. Wamechanganya siasa na dini, kanisa na taifa; wamethibitika kuwa wasio waaminifu-washikamanifu kwa pendeleo lao walilopewa na Mungu la kupiga mbiu ya ujumbe wa ufalme wa Mesiya, na wamejitoa wenyewe ili kuwatia moyo watawala waamini kwamba mtawala humiliki kwa haki ya kimungu, na kwa hiyo lolote afanyalo linafaa.” Akionyesha tokeo la hilo, yeye alisema: “Wafalme wa Ulaya wenye tamaa ya kibinafsi walijihami tayari kwa vita, kwa sababu walitamani kunyakua maeneo ya watu wengineo; na makasisi waliwapongeza na kusema: ‘Fanyeni mtakalo, hamwezi kukosea; lolote mfanyalo lafaa.’” Lakini si makasisi wa Ulaya tu waliokuwa wakifanya hivyo, wahubiri katika Amerika walifanya ivyo hivyo.

      Ripoti ndefu ya mhadhara huo ilichapwa siku iliyofuata katika gazeti Morning Tribune la Los Angeles. Makasisi walighadhibishwa sana hivi kwamba shirika la wahudumu lilifanya mkutano siku iyo hiyo na likamtuma msimamizi walo kwa mameneja wa gazeti hilo ili kuwajulisha juu ya kuudhika kwao kwingi. Kufuatia hilo, kulikuwa na kipindi cha kupekuliwapekuliwa kwa ofisi za Watch Tower Society na washiriki wa idara ya upelelezi ya serikali.

      Wakati wa kipindi hicho cha harara ya utukuzo wa taifa, kongamano la makasisi lilifanywa jijini Philadelphia, katika Marekani, ambamo azimio lilipitishwa likiomba Sheria ya Ujasusi ipitiwe tena ili wakiukaji wanaoshtakiwa wajaribiwe katika mahakama ya kijeshi na kupewa adhabu ya kifo. John Lord O’Brian katibu wa pekee wa mkuu wa sheria kwa kazi ya vita, aliteuliwa kuwasilisha jambo hilo katika Bunge. Rais wa Marekani hakuruhusu mswada huo uwe sheria. Lakini Meja-Jenerali James Franklin Bell, wa jeshi la Marekani, akiwa ameghadhibika sana aliwaambia J. F. Rutherford na W. E. Van Amburgh yale yaliyokuwa yametukia kwenye kongamano hilo na kusudi la kutumia mswada huo dhidi ya maofisa wa Watch Tower Society.

      Faili rasmi za serikali ya Marekani zinaonyesha kwamba angalau kuanzia Februari 21, 1918, na kuendelea, John Lord O’Brian, alihusika binafsi katika jitihada za kufanya mashtaka dhidi ya Wanafunzi wa Biblia. Rekodi ya Bunge ya Aprili 24 na Mei 4 ina hati kutoka kwa John Lord O’Brian ambayo alitoa hoja kwa nguvu kwamba ikiwa sheria iliruhusu kusemwa kwa “yale yaliyo ya kweli, kwa makusudi mema, na kwa njia zinazofaa,” kama ilivyosemwa katika ile iliyoitwa eti Sahihisho la Sheria ya Ujasusi ya Ufaransa na kama vile ilivyokuwa imekubaliwa na Bunge la Marekani, hangeweza kuwashtaki Wanafunzi wa Biblia kwa kufanikiwa.

      Katika Worcester, Massachusetts, “Mwadhama” B. F. Wyland alitumia harara ya vita kwa faida yake kwa kudai kwamba Wanafunzi wa Biblia walikuwa wakiendeleza propaganda ya adui. Alichapa makala moja katika Daily Telegram ambayo alijulisha: “Mojawapo kazi za uzalendo zinazowakabili nyinyi mkiwa wananchi ni kulikandamiza Shirika la Kimataifa la Wanafunzi wa Biblia, lenye makao makuu katika Brooklyn. Chini ya kisitiri cha dini, wamekuwa wakiendeleza propaganda ya Ujerumani katika Worcester kwa kuuza kitabu chao, ‘The Finished Mystery.’” Aliwaambia wenye mamlaka waziwazi kwamba ilikuwa kazi yao kuwakamata Wanafunzi wa Biblia na kuwazuia wasifanye mikutano zaidi.

      Kulikuwa na mnyanyaso wenye kuenea wa Wanafunzi wa Biblia katika masika na kiangazi cha 1918, katika Amerika Kaskazini na Ulaya pia. Miongoni mwa wachochezi mlikuwamo makasisi wa Baptisti, Methodisti, Episkopali, Luther, Katoliki ya Roma, na makanisa mengineyo. Fasihi za Biblia zilitwaliwa na maofisa bila hati ya upekuzi, na Wanafunzi wa Biblia wengi wakatiwa gerezani. Wengine walifukuzwa na wafanyaghasia, wakapigwa, wakachapwa mijeledi, wakamwagiwa lami na manyoya, au wakavunjwa mbavu au kukatwa vichwa. Wengine walilemazwa kabisa. Wanaume na wanawake Wakristo walitiwa gerezani bila kushtakiwa au bila kuhukumiwa. Visa hususa zaidi ya mia moja vya kutendwa kikatili viliripotiwa katika The Golden Age la Septemba 29, 1920.

      Washtakiwa kwa Ujasusi

      Kilele kilifikiwa Mei 7, 1918, wakati waranti za serikali zilipotolewa katika Marekani za kumkamata J. F. Rutherford, msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society, na washiriki wake wa karibu.

      Siku iliyotangulia, mashtaka mawili yalikuwa yamefanywa dhidi ya Ndugu Rutherford na washiriki wake, katika Brooklyn, New York. Kama matokeo yaliyotakwa hayakupatikana katika kesi moja, shtaka lile jingine lingefuatiliwa. Shtaka la kwanza, lililofanywa dhidi ya idadi kubwa zaidi ya watu, lilitia ndani mashtaka manne: Mawili yaliwashtaki kwa kufanya shauri ili kukiuka Sheria ya Ujasusi ya Juni 15, 1917; na mengine mawili yaliwashtaki kwa kujaribu kufanya mipango isiyo halali au kufanya hivyo hasa. Ilidaiwa kwamba walikuwa wanafanya shauri ili kuleta maasi na kukataa kazi ya uanajeshi katika Marekani na kwamba walikuwa wanafanya shauri kuzuia kusajiliwa na kuandikishwa kwa watu kwa ajili ya utumishi huo taifa lilipokuwa vitani, pia kwamba walikuwa wamejaribu kufanya au walikuwa hasa wamefanya mambo hayo yote mawili. Shtaka lilitaja kihususa kuchapwa na kugawanywa kwa kitabu The Finished Mystery. Shtaka la pili lilionyesha kwamba kule kupelekwa kwa hundi hadi Ulaya (ambayo ingetumiwa kwa kazi ya elimu ya Biblia katika Ujerumani) kuwa ni tisho kwa masilahi ya Marekani. Wakati washtakiwa walipopelekwa mahakamani, lile shtaka la kwanza, lenye mashtaka manne, ndilo lilifuatiwa.

      Shtaka jingine la C. J. Woodworth na J. F. Rutherford chini ya Sheria ya Ujasusi lilikuwako katika Scranton, Pennsylvania. Lakini, kulingana na barua kutoka kwa John Lord O’Brian ya tarehe Mei 20, 1918, washiriki wa Idara ya Sheria walihofu kwamba Hakimu Witmer wa Wilaya ya Marekani, ambaye angeamua mashtaka, hangekubali utumizi wao wa Sheria ya Ujasusi ili kukandamiza utendaji wa watu ambao, kwa sababu ya masadikisho ya kidini yaliyo manyoofu, walisema mambo ambayo wengine wangeyaona kuwa propaganda ya kupinga vita. Kwa hiyo Idara ya Sheria iliikawiza kesi ya Scranton, ikingoja matokeo ya kesi ya Brooklyn. Serikali pia iliongoza mambo hivi kwamba Hakimu Harland B. Howe, kutoka Vermont, ambaye John Lord O’Brian alijua alikubaliana na maoni yake katika mambo kama hayo, angekuwa mwamuzi wa kesi katika Mahakama ya Wilaya ya Marekani kwa Wilaya ya Mashariki ya New York. Kesi ilianza Juni 5, washtaki wakiwa Isaac R. Oeland na Charles J. Buchner wa Katoliki ya Roma. Wakati kesi ilipokuwa ikiendelea, kama vile Ndugu Rutherford alivyoona, mapadri Wakatoliki walishauriana mara kwa mara na Buchner na Oeland.

      Kadiri kesi ilivyoendelea, ilionyeshwa kwamba maofisa wa Sosaiti na watungaji wa kile kitabu hawakuwa na madhumuni ya kuingilia shughuli za vita za nchi. Ushahidi uliotolewa wakati wa mashtaka ulionyesha kwamba mipango kwa ajili ya kuandikwa kwa kitabu hicho—kwa kweli, uandishi wa sehemu kubwa ya kitabu hicho—ulikuwa umefanywa kabla ya Marekani kutangaza vita (Aprili 6, 1917) na kwamba maafikiano ya kwanza ya kukichapa yalikuwa yametiwa sahihi kabla ya Marekani kupitisha sheria (mnamo Juni 15) ambayo ilisemwa walikuwa wamekiuka.

      Mashtaka yalikazia nyongeza kwenye kitabu hicho iliyofanywa wakati wa Aprili na Juni wa 1917, katika shughuli za kutayarisha nakala na kusoma zile zilizokamilishwa. Hiyo ilitia ndani nukuu kutoka kwa John Haynes Holmes, kasisi aliyekuwa amejulisha kwa nguvu kwamba vita ilikuwa kukiuka Ukristo. Kama ilivyoonyeshwa na mmojawapo mawakili watetezi, maelezo hayo ya kasisi, yaliyochapwa katika kitabu chenye kichwa A Statement to My People on the Eve of War, kilikuwa bado kikiuzwa katika Marekani wakati wa kesi hiyo. Wala kasisi huyo wala mchapaji wacho hawakushtakiwa. Lakini Wanafunzi wa Biblia waliorejezea hotuba yake ndio walioshtakiwa kwa mambo yaliyosemwa ndani yacho.

      Kitabu The Finished Mystery hakikuwaambia watu wa ulimwengu kwamba hawakuwa na haki ya kushiriki vitani. Lakini, katika kueleza unabii, kilinukuu madondoo kutoka matoleo ya The Watch Tower la 1915 ili kuonyesha kutopatana kwa makasisi waliodai kuwa wahudumu wa Kristo lakini walikuwa wakitenda wakiwa wajumbe wa kuandikisha majeshi ya mataifa yaliyo vitani.

      Ilipofahamika kwamba serikali ilipinga kitabu hicho, Ndugu Rutherford alikuwa amepeleka telegramu mara hiyo kwa mchapaji ili aache kukitokeza, na wakati uleule, mwakilishi wa Sosaiti alikuwa ametumwa kwenye idara ya upelelezi ya Jeshi la Marekani ili kujua sababu ya wao kukipinga. Ilipojulikana kwamba kwa sababu ya vita iliyokuwa ikiendelea, kurasa 247-253 za kitabu hicho zilionwa kuwa zisizofaa, Sosaiti ilielekeza kwamba kurasa hizo ziondolewe katika nakala zote za kitabu hicho kabla ya umma kupewa. Na wakati serikali ilipojulisha mawakili wa wilaya kwamba kugawanywa kwacho zaidi kungekuwa ni kukiuka Sheria ya Ujasusi (ingawa serikali ilikataa kutoa maoni kwa Sosaiti juu ya kitabu hicho kikiwa kimebadilishwa), Sosaiti ilielekeza kwamba kugawanywa kote kwa kitabu hicho kwa umma kukomeshwe.

      Kwa Nini Hukumu Kali Jinsi Hiyo?

      Kujapokuwa na yote hayo, katika Juni 20, 1918, wasaidizi wa hakimu walifanya uamuzi na wakampata kila mshtakiwa kuwa na kosa kwa kila shtaka. Siku iliyofuata, sabab kati yao walihukumiwa vifungo vinne vya miaka 20 kila moja, vinavyotumika pamoja. Julai 10, yule wa nanec alihukumiwa vipindi vinne vyenye kutumika pamoja vya miaka 10. Hukumu hiyo ilikuwa kali jinsi gani? Katika barua kwa mkuu wa sheria katika Machi 12, 1919, rais wa Marekani Woodrow Wilson alikiri kwamba “vifungo hivyo kwa wazi vinapita kiasi.” Kwa kweli, yule mtu aliyefyatua risasi katika Sarajevo ambazo zilimwua maliki mwana-mfalme wa Milki ya Austria na Hungaria—jambo lililochochea matukio yaliyoingiza mataifa katika Vita ya Ulimwengu 1—hakuwa amepata hukumu kali jinsi hiyo. Hukumu yake ilikuwa miaka 20 gerezani—si vifungo vinne vya miaka 20, kama ilivyokuwa kwa Wanafunzi wa Biblia!

      Ni nini kilichochea kuwekwa kwa vifungo hivyo vikali vya Wanafunzi wa Biblia? Hakimu Harland B. Howe alijulisha: “Kwa maoni ya Mahakama, propaganda ya kidini ambayo washtakiwa hawa wametetea kwa bidii na kuieneza kotekote katika taifa na miongoni mwa mataifa rafiki, ni hatari kubwa zaidi ya kikosi kimoja cha Jeshi la Ujerumani. . . . Mtu anayehubiri dini mara nyingi huwa na uvutano mwingi, na ikiwa ni mnyoofu, yeye ni mwenye matokeo hata zaidi. Hilo linazidisha badala ya kupunguza kosa walilofanya. Kwa hiyo, likiwa jambo lifaalo zaidi kufanyia watu kama hao, Mahakama imekata kauli kwamba hukumu lazima iwe kali.” Hata hivyo, inastahili kuangaliwa pia kwamba kabla ya kupitisha hukumu, Hakimu Howe alisema kwamba taarifa zilizotolewa na mawakili wa washtakiwa zilikuwa zimetia shuku na kutendea isivyofaa si maofisa wa sheria wa serikali tu bali pia “wahudumu wote wa kidini kotekote nchini.”

      Baada ya uamuzi huo, rufani ilikatwa mara hiyo kwa mahakama ya mzunguko ya rufani ya Marekani. Lakini Hakimu Howe alikataa kuwaachilia kwa dhamana wakisubiri kusikizwa kwa rufani hiyo,d na katika Julai 4, kabla ya rufani ya tatu iliyokuwa ya mwisho ya kupata dhamana kusikizwa, ndugu saba wa kwanza walihamishwa upesi wakapelekwa kwenye gereza la kitaifa la Atlanta, Georgia. Baada ya hapo, ilidhihirishwa kwamba kulikuwa na makosa 130 ya kimahakama katika hukumu hiyo yenye kupendelea upande mmoja sana. Kazi ya miezi mingi ilifanywa ili kutayarisha karatasi zilizotakikana katika kusikizwa kwa rufani. Wakati uo huo, vita ilikwisha. Mnamo Februari 19, 1919, ndugu wanane walio gerezani walipeleka rufani ili wahurumiwe rasmi na rais wa Marekani, Woodrow Wilson. Barua nyinginezo zilizohimiza kuachiliwa kwa ndugu hao zilipelekwa na wananchi wengi kwa mkuu wa sheria mpya. Kisha, mnamo Machi 1, 1919, katika kujibu maulizo ya mkuu wa sheria, Hakimu Howe alipendekeza “kubadilishwa mara hiyo” kwa hukumu hiyo. Ingawa hilo lingepunguza hukumu, pia lingethibitisha kosa la washtakiwa. Kabla ya hilo kufanywa, mawakili wa akina ndugu walimpelekea wakili mkuu wa Marekani agizo la mahakama lililoleta kesi hiyo mbele ya mahakama ya rufani.

      Miezi tisa baada ya Rutherford na washiriki wake kuhukumiwa—na vita ikiwa imekwisha—Machi 21, 1919, mahakama ya rufani iliagiza washtakiwa wote wanane wapate dhamana, na Machi 26, waliachiliwa katika Brooklyn kwa dhamana ya dola 10,000 kila mmoja. Katika Mei 14, 1919, mahakama ya mzunguko ya Marekani ya rufani katika New York ilikata kauli: “Washtakiwa katika kesi hii hawakupewa hukumu ya kiasi na isiyopendelea upande wowote ambayo walistahili kupewa, na kwa sababu hiyo hukumu hiyo imebatilishwa.” Kesi hiyo iliahirishwa ili ifanywe upya. Hata hivyo, Mei 5, 1920, baada ya washtakiwa kuja mahakamani, baada ya kupewa samansi, wakili wa serikali katika mahakama ya wazi katika Brooklyn, alitangaza mara tano kuondolewa kwa mashtaka.e Kwa nini? Kama ilivyofunuliwa na barua zilizohifadhiwa katika Jumba la Hati za Kitaifa la Marekani, Idara ya Sheria ilihofu kwamba ikiwa masuala hayo yangepelekwa mbele ya wasaidizi wa hakimu wasiopendelea upande wowote, huku harara ya vita ikiwa imekwisha, wangeshindwa kesi hiyo. Wakili wa Marekani aitwaye L. W. Ross alisema katika barua kwa mkuu wa sheria: “Ninafikiri ingekuwa afadhali, kwa uhusiano wetu na umma, ikiwa kwa hiari yetu wenyewe” tungesema kwamba kesi imefungwa.

      Siku iyo hiyo, Mei 5, 1920, shtaka lile jingine lililokuwa limefanywa katika Mei 1918 dhidi ya J. F. Rutherford na wanne kati ya washirika wake lilifutiliwa mbali pia.

      Ni Nani kwa Kweli Aliyeyachochea?

      Je, yote hayo kwa kweli yalichochewa na makasisi? John Lord O’Brian alikana hilo. Lakini mambo ya hakika yalijulikana vema na wale walioishi wakati huo. Katika Machi 22, 1919, gazeti lililochapwa katika Girard, Kansas liitwalo Appeal to Reason, liliteta hivi: “Wafuasi wa Pasta Russell, Wakifuatiwa na Ukorofi wa Makasisi wa ‘Orthodoksi,’ Walihukumiwa na Kufungwa Bila Dhamana, Ingawa Walifanya Kila Jitihada Iliyowezekana ili Kushikamana na Masharti ya Sheria ya Ujasusi. . . . Tunajulisha kwamba, hata iwe au isiwe kwamba Sheria ya Ujasusi ilikuwa ya kikatiba kikweli au inayofaa kiadili, wafuasi hao wa Pasta Russell walihukumiwa isivyo haki chini ya masharti yayo. Uchunguzi wa akili iliyofunguka wa ithibati utamsadikisha yeyote upesi kwamba watu hao si kwamba tu hawakuwa na kusudi la kukiuka sheria, bali pia hawakuikiuka.”

      Miaka mingi baadaye, katika kitabu Preachers Present Arms, Dakt. Ray Abrams alionelea hivi: “Ni jambo lenye kutokeza kwamba makasisi wengi walishiriki sehemu ya uchochezi katika kujaribu kuwaondolea mbali Warusselli [kama vile Wanafunzi wa Biblia walivyoitwa kwa dharau]. Mizozo ya kidini na chuki za muda mrefu, ambazo hazikushughulikiwa kwa vyovyote mahakamani katika wakati wa amani, sasa zilifika mahakamani chini ya uvutano wa harara ya wakati wa vita.” Yeye pia alisema: “Uchanganuzi wa kesi yote huongoza kwenye mkataa kwamba hapo awali makanisa na makasisi walichochea harakati ya kuwafutilia mbali Warusselli.”—Kur. 183-185.

      Hata hivyo, mwisho wa vita haukuleta mwisho wa mnyanyaso wa Wanafunzi wa Biblia. Kipindi kipya cha mnyanyaso ndicho kilichoanza.

      Mapadri Wawachochea Polisi

      Vita ikiwa imekwisha, masuala mengine yalichochewa na makasisi ili kukomesha utendaji wa Wanafunzi wa Biblia, ikiwa ingewezekana. Katika Bavaria ya Katoliki na sehemu nyingine za Ujerumani, wengi walikamatwa katika miaka ya 1920 chini ya sheria za uchuuzi. Lakini wakati kesi hizo zilipokuja kwenye mahakama za rufani, mara nyingi mahakimu waliwaunga mkono Wanafunzi wa Biblia. Hatimaye, baada ya mahakama kugharikishwa kwa maelfu ya kesi kama hizo, Wizara ya Mambo ya Ndani ilitoa agizo katika 1930 kwa maofisa wote wa polisi ikiwaagiza waache kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Wanafunzi wa Biblia chini ya sheria za uchuuzi. Hivyo, kwa muda mfupi, msongo kutoka kwa chanzo hicho ulikoma, na Mashahidi wa Yehova wakaendelea na utendaji wao kwa kiwango kisicho cha kawaida katika shamba la Ujerumani.

  • “Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku katika ukurasa wa 655]

      Makasisi Waonyesha Hisia Zao

      Maitikio ya magazeti ya kidini baada ya kuhukumiwa kwa J. F. Rutherford na washiriki wake mwaka 1918 yanastahili kuangaliwa:

      ◆ “The Christian Register”: “Kile ambacho Serikali hapa inashambulia moja kwa moja kwa njia ya kufisha ni ile dhana kwamba mawazo ya kidini, hata yawe ya kichaa na yenye kudhuru jinsi gani, yanaweza kuenezwa bila hofu ya kuadhibiwa. Dhana hiyo ni uwongo wa kale, na kufikia sasa hatujakuwa waangalifu sana kulihusu. . . . Hukumu hiyo inaonekana kuwa ndiyo mwisho wa Urusselli.”

      ◆ “The Western Recorder,” kichapo cha Baptisti, kilisema: “Haishangazi kwamba kiongozi wa kidhehebu hicho chenye ukaidi amefungiwa katika mojawapo ya vituo vya watu wakaidi. . . . Tatizo lenye kutatanisha kwelikweli kuhusiana na jambo hilo ni ikiwa washtakiwa wangepaswa wapelekwe kwenye makao ya wenye kichaa au kwenye gereza.”

      ◆ “The Fortnightly Review” lilielekeza fikira kwenye maelezo katika gazeti la New York “Evening Post,” ambalo lilisema: “Tunatumaini kwamba walimu wa dini kila mahali wataona maoni ya hakimu huyu kwamba kufunza dini yoyote isipokuwa ile ambayo inapatana kabisa na sheria zilizowekwa ni hatia kubwa ambayo inafanywa kuwa kubwa zaidi, ikiwa wewe ukiwa mhudumu wa gospeli, ungali mnyoofu.”

      ◆ “The Continent” kwa kuwashushia heshima liliwaonyesha washtakiwa kuwa “wafuasi wa ‘Pasta’ Russell aliyekufa” na likapotoa imani zao kwa kusema kwamba waliunga mkono “kwamba watu wote wanapaswa wasipelekwe kupigana na kaiser wa Ujerumani isipokuwa wale wenye dhambi.” Lilidai kwamba kulingana na wakili mkuu katika Washington, “muda fulani uliopita serikali ya Italia ililalamikia Marekani kwamba Rutherford na washiriki wake . . . walikuwa wameeneza kiasi fulani cha propaganda ya kupinga vita katika majeshi ya Italia.”

      ◆ Juma moja baadaye, “The Christian Century” lilichapa sehemu kubwa ya habari iliyo juu neno kwa neno, ikionyesha kwamba walikubaliana nayo kabisa.

      ◆ Gazeti la Katoliki “Truth” liliripoti kifupi ile hukumu waliyopewa na kisha likaeleza hisi za wahariri walo, likisema: “Fasihi za shirika hilo zimejaa mashambulizi makali sana juu ya Kanisa Katoliki na upadri walo.” Ili kujaribu kuweka kibandiko cha “uasi” juu ya yeyote ambaye huenda akapinga hadharani maoni ya Kanisa Katoliki, liliongezea hivi: “Inazidi kuwa wazi kwamba roho ya kutovumilia inafungamanishwa kwa ukaribu na ile ya uasi.”

      ◆ Dakt. Ray Abrams, katika kitabu chake “Preachers Present Arms,” alionelea hivi: “Wakati habari za hukumu ya vifungo hivyo vya miaka ishirini zilipofikia wahariri wa magazeti ya kidini, karibu kila kimoja cha ­vichapo hivyo, kikubwa na kidogo, kilishangilia tukio hilo. Mimi nimeshindwa kupata maneno yoyote ya masikitiko katika yoyote ya majarida ya kidini yanayokubaliwa.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki