Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Hatari Inayowahangaisha Wazazi Wote
    Amkeni!—2007 | Oktoba
    • Hatari Inayowahangaisha Wazazi Wote

      HEATHER na Scott ni wenzi wa ndoa wachangamfu walio na mtoto mwenye umri wa miaka mitatu aliye na afya nzuri.a Wanamtunza mwana wao vizuri. Kwenye ulimwengu wa leo hilo si jambo rahisi, linatia ndani mahangaiko na majukumu mengi. Watoto wanahitaji kufundishwa mambo mengi sana. Heather na Scott wanahisi kwamba wana daraka zito hasa kuhusu jambo moja: Wanataka kumlinda mtoto wao asitendewe vibaya kingono. Kwa nini?

      “Baba yangu hakuwa mwenye urafiki, alikuwa mwenye hasira na mlevi,” anasema Heather. “Alinipiga sana na kunitendea mimi na dada zangu vibaya kingono.”b Watu wengi wanakubali kwamba kutendewa hivyo kunaweza kumfanya mtu awe na matatizo makubwa sana ya kihisia. Si ajabu kwamba Heather ameazimia kumlinda mwana wake! Scott naye ameazimia kufanya vivyo hivyo.

      Wazazi wengi wanahangaishwa sana na suala la watoto kutendewa vibaya. Labda wewe pia unahangaishwa na jambo hilo. Tofauti na Scott na Heather huenda usiwe umekumbwa moja kwa moja na mambo kama hayo, lakini bila shaka umesikia ripoti zenye kushtua kuhusu kuenea kwa zoea hilo lenye kuchukiza. Ulimwenguni pote wazazi wazuri wanaogopa wanaposikia kuhusu mambo yanayowapata watoto katika maeneo yao.

      Haishangazi kuwa mtafiti mmoja anayechunguza masuala ya watu kutendewa vibaya kingono alisema kwamba kuenea kwa visa vya kutendea watoto vibaya ni “moja kati ya ugunduzi wenye kuvunja moyo wa enzi yetu.” Habari hizo ni zenye kuhuzunisha, lakini je, inashangaza kwamba mambo kama hayo yanazidi kuenea? Wanafunzi wa Biblia hawashangazwi na mambo hayo. Neno la Mungu linaeleza kwamba tunaishi katika wakati wenye taabu unaoitwa “siku za mwisho,” wakati ambapo watu wangekuwa “wakali,” na pia wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe” na “wasio na upendo wa asili.”—2 Timotheo 3:1-5.

      Kuwatendea watoto vibaya kingono ni suala lenye kuogopesha. Kwa kweli, wazazi fulani huchukizwa wanapowaza kuhusu uovu wa watu wanaowatendea watoto vibaya kingono. Lakini, je, wazazi wanaweza kukabiliana na tatizo hilo? Au je, kuna hatua zinazofaa ambazo wazazi wanaweza kuchukua ili kuwalinda watoto wao? Makala zinazofuata zitazungumzia maswali haya.

  • Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako
    Amkeni!—2007 | Oktoba
    • Jinsi ya Kuwalinda Watoto Wako

      WATU wengi hawapendi kuzungumza kuhusu suala la kuwatendea watoto vibaya. Kufikiria tu kuhusu jambo hilo huwaogopesha wazazi wengi! Hata hivyo, hayo ni mambo yenye kuogopesha na yasiyopendeza katika ulimwengu wa leo, na watoto huathiriwa sana nayo. Je, inafaa kufikiria kuhusu jambo hilo? Ungetoa kitu gani ili kumlinda mtoto wako? Haigharimu chochote kujifunza kuhusu athari za kutendewa vibaya kingono. Kujua mambo hayo kunaweza kukusaidia kuwalinda watoto wako.

      Usiache tatizo hilo likulemee na ukose ujasiri wa kukabiliana nalo. Hata ukihisi umelemewa, una nguvu ambazo mtoto wako hana, kwani mtoto wako anahitaji miaka mingi au hata makumi ya miaka ili awe na uwezo kama huo. Umepata ujuzi, uzoefu, na hekima kadiri ambavyo miaka imepita. Ili ufaulu unapaswa kutumia uwezo huo kumlinda mtoto wako. Tutazungumzia hatua tatu za msingi ambazo kila mzazi anaweza kuchukua. Hatua hizo ni: (1) Uwe ngao ya mtoto wako dhidi ya kutendewa vibaya, (2) mfundishe mtoto wako mambo yanayohitajika, na (3) mfundishe mtoto wako hatua za kuchukua anapokabiliwa na mambo hayo.

      Je, Wewe Ni Ngao?

      Wazazi ndio wenye daraka la kuwalinda watoto wao dhidi ya kutendewa vibaya kingono, si watoto. Hivyo, wazazi wanapaswa kuelimishwa kabla ya watoto. Ikiwa wewe ni mzazi, kuna mambo machache unayopaswa kujua kuhusu suala la kuwatendea watoto vibaya kingono. Unahitaji kujua ni watu wa aina gani wanaowatendea watoto vibaya na mbinu wanazotumia. Mara nyingi wazazi hufikiri kwamba watu wanaowatendea watoto vibaya kingono ni watu wasiojulikana ambao huvizia gizani, wakitafuta njia za kuwateka nyara au kuwalala kwa nguvu watoto wao. Ni kweli kwamba kuna watu kama hao. Mara nyingi tunasikia kuwahusu katika vyombo vya habari. Hata hivyo, watu kama hao ni wachache. Asilimia 90 hivi ya visa vya watoto kutendewa vibaya kingono, hufanywa na mtu ambaye tayari mtoto anamfahamu na kumtumaini.

      Kiasili hupendi kuamini kwamba jirani mzuri, mwalimu, mfanyakazi wa huduma za afya, kocha, au mtu wa ukoo anaweza kuwa na uchu kumwelekea mtoto wako. Ni kweli, watu wengi hawako hivyo. Hakuna sababu ya kumtilia shaka kila mtu aliye karibu nawe. Hata hivyo, unaweza kumlinda mtoto wako kwa kujifunza jinsi watu wanaowatendea watoto vibaya kingono wanavyotenda.—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 6.

      Kujua mbinu hizo kunaweza kukusaidia wewe mzazi, uwe tayari kuwa ngao kwa ajili ya mtoto wako. Kwa mfano, mtu fulani anayependezwa sana na watoto kuliko watu wazima akianza kumkazia uangalifu mtoto wako na kumpa zawadi au akijitolea kubaki nyumbani na mtoto wako au kwenda matembezi na mtoto wako, utafanya nini? Je, utafikiri kwamba mtu huyo anataka kumtendea mtoto wako vibaya kingono? La. Usikate kauli haraka. Si lazima tabia kama hiyo iwe na dosari. Hata hivyo, inaweza kukusaidia kuwa macho. Biblia inasema: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

      Kumbuka kwamba mtu akikuambia atakufanyia mengi kuliko ilivyo kawaida, kuna uwezekano mkubwa kwamba hana nia nzuri. Mchunguze kwa uangalifu mtu yeyote anayejitolea kutumia wakati akiwa peke yake na mtoto wako. Mjulishe mtu kama huyo kwamba utakuwa ukienda kumwona mtoto wako wakati wowote. Melissa na Brad, wazazi walio na wavulana watatu, ni waangalifu sana kuhusu kumwacha mtoto peke yake na mtu mzima. Mtoto wao mmoja alipotaka kujifunza muziki nyumbani, Melissa alimwambia mwalimu huyo: “Nitakuwa nikiingia mara kwa mara katika chumba hiki muda wote utakapokuwa hapa.” Huenda kufanya hivyo kukaonekana kuwa ulinzi unaopita kiasi, lakini wazazi hao wanaona inafaa kufanya hivyo kuliko kujuta baadaye.

      Jihusishe sana katika utendaji wa mtoto wako, wafahamu rafiki zake, na upendezwe na kazi zake za shuleni. Anapoenda matembezi na mtu mwingine fahamu mambo yote watakayofanya. Mtaalamu mmoja wa afya ya akili ambaye ametumia miaka 33 akichunguza visa vya watu kutendewa vibaya kingono anasema kwamba ameona visa vingi ambavyo vingeweza kuzuiwa ikiwa tu wazazi wangekuwa macho. Anamnukuu mtu mmoja ambaye alihukumiwa kwa kuwatendea watoto vibaya kingono aliyesema: “Ni kana kwamba wazazi wenyewe hutuletea watoto wao. . . . Kwa kweli walifanya iwe rahisi sana kwangu.” Kumbuka, watu wengi wanaowatendea watoto vibaya kingono hutafuta mawindo rahisi. Wazazi wanaojihusisha sana katika maisha ya watoto wao hufanya iwe vigumu watoto wao kushambuliwa.

      Kuwa msikilizaji mzuri ni njia nyingine unayoweza kuwa ngao ya mtoto wako. Si rahisi kwa mtoto kueleza waziwazi kwamba ametendewa vibaya kingono. Mara nyingi wao huaibika sana na kuhangaishwa na jinsi utakavyoitikia. Hivyo, sikiliza kwa makini uone kama kuna ujumbe fulani uliofichika.a Kama mtoto wako anakueleza jambo linalokuhangaisha, kwa utulivu uliza maswali ili kuufikia moyo wake. Ikiwa mtoto anakueleza kwamba hamtaki mlezi fulani, muulize ni kwa nini. Iwapo atakuambia ya kwamba mtu mzima fulani anacheza naye michezo ya ajabu-ajabu, muulize: “Hiyo ni michezo ya aina gani? Anafanya nini?” Akilalamika kwamba mtu fulani alimtekenya, muulize, “Alikutekenya sehemu gani?” Usipuuze majibu ya mtoto wako. Watu wanaowatendea vibaya watoto wanawaambia kwamba hakuna mtu atakayewaamini, na kwa kusikitisha mara nyingi hilo ndilo hutukia. Ili mtoto aliyetendewa vibaya kingono apone haraka anahitaji kuhisi kwamba anaaminiwa na ana utegemezo wa mzazi.

      Uwe ngao ya mtoto wako

      Wafundishe Watoto Wako Mambo Yanayohitajika

      Kitabu fulani kinachozungumzia watoto kutendewa vibaya kilimnukuu mtu mmoja aliyehukumiwa kwa kuwatendea watoto vibaya akisema: “Ukinipa mtoto ambaye hajui chochote kuhusu ngono, utakuwa umenipa mtoto mwingine wa kumtendea vibaya.” Maneno hayo yanayotia hofu ni kikumbusha kinachofaa kwa wazazi. Inakuwa rahisi zaidi kuwadanganya watoto ambao hawajui chochote kuhusu ngono. Biblia inasema kwamba mtu anapokuwa na ujuzi na hekima anaweza kulindwa “kutoka kwa mtu anayesema mambo mapotovu.” (Methali 2:10-12) Bila shaka hilo ndilo jambo unalotaka kwa ajili ya mtoto wako. Jambo la pili muhimu katika kumlinda mtoto wako, ni kumweleza waziwazi kuhusu suala hilo muhimu.

      Unaweza kuwaelezaje mambo hayo? Wazazi wengi huaibika kuzungumza na watoto wao kuhusu ngono. Huenda mtoto wako akaaibika zaidi na hivyo huenda asije kuzungumza nawe kuhusu jambo hilo. Kwa hiyo, chukua hatua ya kwanza. Melissa anasema: “Tulianza mapema, kwa kuwafundisha majina ya viungo vya mwili. Tulitumia majina halisi, si majina ya badala, ili kuwaonyesha hakuna jambo la kuchekesha au la kuaibisha kuhusu viungo vyovyote vya miili yao.” Baada ya kufanya hivyo ni rahisi kuzungumza kuhusu kutendewa vibaya kingono. Wazazi wengi huwaeleza watoto wao kwamba viungo ambavyo hufichwa na chupi ni vya siri na vya pekee.

      Heather aliyetajwa katika makala inayotangulia anasema: “Mimi na Scott tulimweleza mwana wetu kwamba uume wake ni kiungo cha siri na si kitu cha kuchezewa. Hakuna mtu anayepaswa kukichezea, iwe ni Mama, au Baba, au hata daktari. Tunapompeleka kwa daktari, mimi humweleza kwamba daktari atachunguza ikiwa ana ugonjwa wowote na hiyo ndiyo sababu huenda atakigusa kiungo hicho.” Wazazi wote wawili hushiriki katika mazungumzo hayo mara kwa mara, nao humhakikishia kwamba anaweza kuwaendea wakati wowote iwapo mtu yeyote atamgusa kwa njia isiyo sawa au kwa njia itakayomfanya ajihisi vibaya. Wataalamu wa kutunza watoto na kuzuia kutendewa vibaya kingono wanapendekeza kwamba wazazi wote wawe na mazungumzo kama hayo na watoto wao.

      Watu wengi wameona kwamba kitabu Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuub kimewasaidia sana wanapowafundisha watoto jambo hilo. Sura ya 32, “Jinsi Yesu Alivyolindwa,” kina mashauri ya moja kwa moja lakini yanayofariji kwa ajili ya watoto kuhusu hatari za kutendewa vibaya na umuhimu wa kujilinda. Melissa anasema: “Kitabu hicho kimetusaidia kukazia mambo ambayo tayari tumewaeleza watoto wetu.”

      Katika ulimwengu wa leo, watoto wanahitaji kujua kwamba kuna watu ambao wanapenda kuwashika-shika watoto au kuwafanya watoto wawashike katika njia zisizofaa. Maonyo hayo hayapaswi kuwajaza hofu watoto au kuwafanya wasiwaamini watu wazima wote. “Ni ujumbe tu wa tahadhari,” anasema Heather. “Hilo ni onyo moja kati ya maonyo mengi ambayo watoto wanapewa, mengi kati ya maonyo hayo hayahusiani na kutendewa vibaya kingono. Hayajafanya mtoto wangu awe na hofu.”

      Mafunzo unayompa mtoto wako yanapaswa kutia ndani maoni yaliyosawazika kuhusu utii. Ni jambo muhimu na gumu kumfundisha mtoto kutii. (Wakolosai 3:20) Hata hivyo, mafundisho hayo hayapaswi kupita mpaka. Ikiwa mtoto atafundishwa kwamba wakati wote anapaswa kumtii mtu mzima yeyote, hata hali iweje, ni rahisi kwake kutendewa vibaya. Watu wanaowatendea watoto vibaya kingono hugundua haraka watoto wanaotii kila jambo. Wazazi wenye busara wanawafundisha watoto wao kwamba utii unapaswa kuwa wa kadiri. Hilo si jambo gumu kwa Wakristo. Wao huwaambia tu watoto: “Mtu yeyote akikuambia ufanye jambo ambalo Yehova Mungu anasema ni kosa, hupaswi kulifanya. Hata Mama au Baba hapaswi kukuambia ufanye jambo ambalo Yehova anasema ni kosa. Nawe unapaswa kumwambia Mama au Baba wakati wowote ambapo mtu atajaribu kukulazimisha ufanye jambo baya.”

      Mwishowe, hakikisha kwamba mtoto wako anaelewa kuwa hakuna mtu anayepaswa kumwambia akufiche jambo lolote. Mwambie kwamba ikiwa mtu yeyote anamwambia akufiche jambo lolote, anapaswa kuja na kukujulisha. Haidhuru aambiwe nini, hata ikiwa atatishwa sana au ikiwa yeye wenyewe amefanya kosa fulani, sikuzote ni sawa kumwendea Mama au Baba na kumwambia jambo hilo. Mafundisho haya hayapaswi kumwogopesha mtoto wako. Unaweza kumhakikishia kwamba watu wengi hawafanyi mambo kama hayo, yaani, kumshika-shika sehemu asizopaswa, kumwambia asimtii Mungu, au kumwambia afiche jambo fulani. Kama tu mtu anayepanga njia ambayo atatumia ili kukimbilia moto unapozuka, mafundisho hayo kuhusu kutendewa vibaya kingono ni tahadhari tu ambazo huenda hazitahitajika.

      Mfundishe mtoto wako mambo yanayohitajika

      Mfundishe Mtoto Wako Hatua za Kujilinda

      Hatua ya tatu ambayo tutazungumzia ni kumfundisha mtoto mambo rahisi ya kufanya mtu anapojaribu kumtumia vibaya wakati ambapo haupo. Njia moja ambayo hupendekezwa mara nyingi ni kama mchezo. Wazazi huuliza “Vipi ikiwa . . . ?” kisha mtoto anajibu. Unaweza kumwuliza, “Vipi ikiwa tulikuwa sokoni kisha tupoteane? Ungenitafutaje?” Huenda jibu la mtoto lisiwe lile ulilotazamia, lakini unaweza kumwelekeza kwa kutumia maswali ya ziada, kama vile “Je, unaweza kufikiria njia salama zaidi?”

      Unaweza kutumia maswali kama hayo kumwuliza mtoto njia salama zaidi anayoweza kutumia mtu akijaribu kumshika-shika sehemu isiyofaa. Ikiwa mtoto anashtushwa na maswali kama hayo, unaweza kusimulia hadithi inayomhusu mtoto mwingine. Kwa mfano: “Msichana fulani ana mtu wa ukoo ambaye anampenda, lakini mtu huyo anajaribu kumshika-shika sehemu isiyofaa. Unafikiri anapaswa kufanya nini ili awe salama?”

      Mfundishe mtoto wako hatua za kujilinda

      Unapaswa kumfundisha mtoto wako afanye nini katika hali kama hiyo iliyotajwa? Mwandishi mmoja anasema hivi: “Kusema ‘Sitaki!’ kwa ujasiri au ‘Usifanye hivyo!’ au ‘Niache!’ humwogopesha sana mtu anayejaribu kumshawishi na kumfanya aache kumlazimisha.” Msaidie mtoto wako aonyeshe kwa ufupi jinsi atakavyofanya ili awe na ujasiri wa kukataa kwa sauti, kukimbia, na kukueleza yaliyotukia. Mtoto ambaye anaonekana ameelewa mazoezi hayo anaweza kusahau baada ya majuma au miezi michache. Kwa hiyo uwe na kawaida ya kurudia mazoezi hayo.

      Watu wote wanaomlea mtoto huyo, kutia ndani wa kiume, iwe ni baba, baba wa kambo, au wanaume wengine wa ukoo, wanapaswa kuhusishwa katika mazungumzo hayo. Kwa nini? Kwa sababu ni kama wote wanaohusika katika mafundisho hayo wanamwahidi mtoto kwamba hawatawahi kumtendea vibaya kwa njia hiyo. Kwa kusikitisha, mara nyingi watu wanaowatendea watoto vibaya kingono huwa watu wa familia. Makala inayofuata itazungumzia jinsi unavyoweza kuifanya familia yako iwe salama katika ulimwengu uliopotoka.

      a Wataalamu wanasema kwamba watoto wengi ambao wanatendewa vibaya kingono, hutoa ishara zinazoonyesha kwamba kuna tatizo bila kuzungumza. Kwa mfano, mtoto akianza kurudia tabia alizokuwa ameacha kama vile, kukojoa kitandani, kila wakati kutaka kuwa karibu na wazazi wake, au kuogopa anapoachwa peke yake, anaweza kuwa akitoa ishara ya kwamba ana tatizo kubwa. Dalili kama hizo si uthibitisho wa kwamba anatendewa vibaya kingono. Kwa utulivu muulize mtoto wako ikiwa kuna tatizo linalomsumbua ili uweze kumfariji, kumhakikishia kwamba utamtegemeza, na kumlinda.

      b Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

  • Ilinde Familia Yako
    Amkeni!—2007 | Oktoba
    • Ilinde Familia Yako

      “WASIO na upendo wa asili.” Biblia inatumia maneno hayo yenye kusikitisha kuwafafanua watu wengi wa siku zetu, kipindi kinachoitwa “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1, 3, 4) Kuenea kwa visa vya kuwatendea watoto vibaya kingono katika familia hutoa uthibitisho wa wazi kwamba unabii huo ni wa kweli. Kwa kweli, neno la awali la Kigiriki aʹstor·gos, linalotafsiriwa katika Kiswahili “wasio na upendo wa asili,” linadokeza kutokuwa na upendo ambao unapaswa kuwa kati ya washiriki wa familia, hasa upendo kati ya wazazi na watoto.a Na mara nyingi visa vya watoto kutendewa vibaya kingono hutukia ndani ya familia.

      Watafiti fulani wanasema kwamba mtu anayewatendea watoto vibaya kingono mara nyingi ni baba au baba wa kambo. Pia, wanaume wengine wa ukoo huwatendea watoto vibaya mara nyingi. Ingawa wengi wa wanaotendewa vibaya ni wasichana, wavulana wengi pia hutendewa hivyo. Lakini wanawake wanaowatendea watoto vibaya si wachache kama unavyofikiri. Huenda visa vya kutendewa vibaya kingono ambavyo haviripotiwi mara nyingi ni vile vinavyofanywa kati ya kaka na dada, ambapo mtoto mkubwa au mwenye nguvu zaidi anamwonea au kumshawishi ndugu au dada yake mdogo afanye vitendo vya ngono naye. Ukiwa mzazi, bila shaka matendo yote kama hayo ni yenye kuchukiza.

      Unaweza kufanya nini ili matatizo kama hayo yasitokee katika familia yako? Kwa wazi, kila mtu katika kila familia anapaswa kujifunza na kuthamini kanuni fulani zinazopaswa kuzuia mwenendo wa kuwatendea wengine vibaya. Mahali panapofaa zaidi pa kupata mwongozo kama huo ni katika Neno la Mungu, Biblia.

      Neno la Mungu na Uhusiano wa Kimwili

      Ili kuwa salama, kila familia inahitaji kukubali viwango vya Biblia vinavyohusu maadili. Biblia inataja mambo wazi inapozungumza kuhusu ngono. Inataja mambo kwa njia ya heshima lakini bila kuficha. Inaonyesha kwamba Mungu alipanga uhusiano wa kingono uwe baraka kwa mume na mke. (Methali 5:15-20) Hata hivyo, inashutumu mahusiano ya kingono nje ya mpango wa ndoa. Kwa mfano, Biblia inapinga waziwazi mahusiano ya kingono kati ya watu wa ukoo. Katika Mambo ya Walawi sura ya 18, kuna orodha inayokataza mahusiano mbalimbali ya kingono kati ya watu wa ukoo. Ona maneno haya: “Yeyote kati yenu asimkaribie mtu yeyote wa jamaa yake, wa kimwili, wa karibu ili kufunua uchi [kufanya ngono]. Mimi ni Yehova.”—Mambo ya Walawi 18:6.

      Yehova aliorodhesha matendo hayo kati ya “mambo . . . yenye kuchukiza” ambayo mtu alipaswa kuhukumiwa kifo kwa sababu ya kuyafanya. (Mambo ya Walawi 18:26, 29) Ni wazi kwamba Muumba ana viwango vya juu sana kuhusiana na mambo hayo. Leo, serikali nyingi zimechukua hatua kama hiyo kwa kutunga sheria dhidi ya kuwatendea watoto vibaya kingono katika familia. Mara nyingi, sheria husema kwamba mtoto anayeshiriki katika kitendo cha ngono na mtu mzima amelalwa kwa nguvu. Kwa nini isemwe hivyo ikiwa nguvu haikutumiwa?

      Serikali nyingi zimekuja kutambua kile ambacho Biblia imesema kwa muda mrefu kuwahusu watoto, kwamba hawawezi kufikiri kama watu wazima. Kwa mfano, andiko la Methali 22:15 linasema: “Ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana.” Na mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika: “Nilipokuwa mtoto, nilikuwa . . . nikifikiri kama mtoto, nikiwaza kama mtoto; lakini kwa kuwa sasa nimekuwa mtu mzima, nimeziondolea mbali tabia za mtoto.”—1 Wakorintho 13:11.

      Mtoto hawezi kuelewa maana halisi ya vitendo vya ngono, wala hawezi kuwazia madhara yatakayotukia kadiri miaka inavyopita. Hivyo, inakubalika kwamba watoto hawana uwezo wa kufanya maamuzi yanayopatana na akili kuhusu ngono. Kwa maneno mengine, mtu mzima (au kijana mwenye umri mkubwa kiasi) akifanya ngono na mtoto, mtu huyo hawezi kusema kwamba mtoto huyo hakukataa au kwamba mtoto huyo alikubali. Mtu huyo amemlala mtoto huyo kwa nguvu. Huo ni uhalifu ambao mara nyingi adhabu yake ni kifungo. Lawama humwangukia anayemlala mtoto kwa nguvu, si mtoto ambaye hakukubali.

      Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba wahalifu wengi hawapewi adhabu yoyote na wenye mamlaka. Kwa mfano, nchini Australia inakadiriwa kwamba asilimia 10 pekee ya watu wanaofanya matendo hayo ndiyo wanaoshtakiwa, na ni wachache tu wanaoadhibiwa. Mambo yako hivyohivyo katika nchi nyingine. Ingawa serikali haziwezi kufanya mengi ili kuilinda familia ya Kikristo, kutumia kanuni za Biblia kunaweza kusaidia sana.

      Wakristo wa kweli wanatambua kwamba Mungu aliyeagiza kanuni hizo ziandikwe katika Neno lake hajabadilika. Yeye huona mambo yote tunayofanya kutia ndani yale yasiyoonwa na wanadamu wengine. Biblia inasema: “Vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.”—Waebrania 4:13.

      Mungu atatutoza hesabu ikiwa tutavunja sheria zake na kuwaumiza wengine. Kwa upande mwingine, anatubariki tukitii sheria zake zinazohusiana na maisha ya familia. Ni zipi baadhi ya sheria hizo?

      Familia Iliyounganishwa na Upendo

      Biblia inasema, “Upendo . . . ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Biblia haifafanui upendo kama hisia tu. Inafafanua sifa hiyo kwa njia ambayo inawachochea watu, yaani, upendo unachochea matendo mazuri na kuwafanya watu waepuke matendo ambayo Biblia inakataza. (1 Wakorintho 13:4-8) Katika familia, kuonyesha upendo humaanisha kumtendea kila mshiriki kwa staha, heshima, na fadhili. Inamaanisha kuishi kulingana na jinsi Mungu anavyomtaka kila mshiriki wa familia aishi. Mungu anampa kila mmoja jukumu muhimu na lenye heshima.

      Akiwa kichwa cha familia, baba anapaswa kuchukua hatua ya kwanza kuonyesha upendo. Anaelewa kwamba baba Mkristo hajapewa ruhusa ya kuwa dikteta, akitumia mamlaka vibaya dhidi ya mke au watoto. Badala yake, anaiga mfano wa Kristo akiwa kichwa chake. (Waefeso 5:23, 25) Kwa hiyo, yeye humtendea mke wake kwa wororo na upendo naye huwa mwenye subira na wororo anaposhughulika na watoto wake. Yeye huwalinda na kujitoa ili kuzuia chochote kinachoweza kuharibu amani, kujiheshimu, kutumainiana, au hali ya kujihisi salama katika familia.

      Vivyo hivyo, mke ambaye pia ni mama ana jukumu muhimu lenye kuheshimika. Biblia inatumia hisi ya mama katika jamii ya wanyama kufananisha ulinzi ambao Yehova na Yesu wanaweza kutoa. (Mathayo 23:37) Pia, mama wa kibinadamu anapaswa kuwalinda sana watoto wake. Kwa upendo, anapaswa kutanguliza usalama na hali njema ya watoto wake. Hakuna mzazi anayepaswa kutumia mamlaka vibaya, kuonea, au kutisha anaposhughulika na mwenzake au watoto, wala hawapaswi kuwaruhusu watoto watumie mbinu kama hizo kati yao.

      Kadiri kila mshiriki wa familia anavyomtendea mwingine kwa heshima na staha, ndivyo kunavyozidi kuwa na mawasiliano mazuri. Mwandishi William Prendergast anasema: “Wazazi wote wanapaswa kuwa na mawasiliano ya karibu, ya kila siku kwa kawaida na watoto au vijana wao.” Anaongezea: “Inaonekana kwamba hilo ndilo suluhisho bora zaidi kwa tatizo la kuwatendea watoto vibaya kingono.” Kwa kweli, Biblia inapendekeza aina hiyo ya mawasiliano ya kawaida na ya upendo. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Mwongozo huo unapotumiwa, nyumbani panakuwa pahali ambapo kila mshiriki wa familia anaweza kuzungumza kutoka moyoni kwa uhuru na kwa usalama.

      Ni kweli kwamba tunaishi katika ulimwengu mwovu na hatuwezi kuzuia mambo yote mabaya. Lakini familia yenye usalama inaweza kusaidia sana. Mtu yeyote katika familia anapoumizwa, anajua mahali anapoweza kukimbilia ili afarijiwe na kuhurumiwa. Nyumba kama hiyo ni kama ngome, mahali salama katika ulimwengu huu wenye taabu. Mungu na abariki jitihada zako za kuhakikisha kwamba kuna usalama katika familia yako!

      a Neno hilo la Kigiriki limefafanuliwa kuwa: “Moyo mgumu kuelekea watu wa familia.” Hivyo, tafsiri moja ya Biblia inatafsiri mstari huo hivi: “Hawatakuwa na upendo wa kawaida kuelekea familia zao.”

      MADOKEZO YA KUWA NA FAMILIA SALAMA

      Intaneti: Ikiwa watoto wako wanatumia Intaneti, wanahitaji maagizo ya jinsi ya kuitumia kwa njia ambayo ni salama. Kuna vituo vingi vya ponografia kutia ndani vituo vya maongezi na vingine vya kuwasiliana ambavyo watu wanaowatendea watoto vibaya kingono wanavitumia kuwashawishi watoto. Ni jambo la hekima kuweka kompyuta mahali palipo wazi ambapo wazazi wanaweza kuchunguza kile ambacho watoto wao wanafanya. Watoto hawapaswi kutoa habari za kibinafsi au kupanga kukutana na mtu wasiyemjua ambaye wamekutana naye kwenye Intaneti.—Zaburi 26:4.

      Vileo: Katika visa vingi ambapo mtoto ametendewa vibaya kingono, kileo kimechangia jambo hilo. Visa vingi vinaonyesha kwamba watu wazima ambao hunywa kileo kupita kiasi hawawezi kujizuia; chini ya hali hiyo wengine hawawezi kukinza tamaa ambazo wangeweza kuzidhibiti. Vyovyote vile, hatari hiyo ni sababu nyingine kwa nini tunapaswa kutii shauri la Biblia kuhusu ulevi na kunywa kupita kiasi.—Methali 20:1; 23:20, 31-33; 1 Petro 4:3.

      Faragha: Mwanamke mmoja anasema hivi: “Baada ya Mama kufa, baba yangu tu ndiye aliyekuwa na pazia katika madirisha yake na mlango katika chumba chake cha kulala. Hatukuwa na faragha, hata tulipokuwa ndani ya bafu.” Mwa- namume huyo aliwatendea vibaya kingono mabinti wake wote. Kila mshiriki wa familia anahitaji kuelewa umuhimu wa faragha. Kama vile wazazi wanavyohitaji faragha kutoka kwa watoto wao nyakati fulani, vivyo hivyo watoto wanahitaji faragha ya kadiri fulani wanapokua. Wazazi wenye hekima wanawatendea wengine kama wanavyotaka watendewe.—Mathayo 7:12.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki