-
Kwa Nini Unaweza Kuamini Vitabu vya Injili vya Biblia?Mnara wa Mlinzi—2010 | Machi 1
-
-
“Vimefanikiwa sana. Sinema zinazogharimu mamilioni ya pesa zimetayarishwa . . . na vitabu vinavyonunuliwa kwa wingi vimeandikwa kwa kutegemea vitabu hivyo vya Injili . . . madhehebu ya Kikristo yamekubali vitabu hivyo. Dini nyingi na mawazo mengi ya uwongo yameanzishwa kwa msingi wa vitabu hivyo vya Injili.”—SUPER INTERESSANTE, GAZETI LA BRAZILI.
NI NINI kilichochochea msisimuko huo wote? Gazeti hilo lilikuwa likizungumza kuhusu ongezeko la hivi karibuni la watu wanaopendezwa na kujishughulisha na vitabu vya uwongo vya injili, barua, na maandishi mengine ya uwongo yaliyogunduliwa katikati ya karne ya 20 huko Nag Hammadi na maeneo mengine ya Misri. Kwa ujumla, maandishi hayo na mengine ya aina hiyo yameitwa maandishi ya Kignosti au ya Kiapokrifa.a
Je, Kulikuwa na Mpango wa Siri?
Katika nyakati ambazo kwa ujumla watu hawaamini Biblia na dini kuu za kiothodoksi, inaonekana kwamba maandishi ya Kignosti au ya Kiapokrifa yamewavutia wengi. Maandishi hayo yamebadili sana maoni ya wengi kuhusu mafundisho ya Yesu Kristo na Ukristo wenyewe. Kama gazeti moja lilivyosema: “Injili ya Tomasi na [vitabu vingine vya] kiapokrifa vinagusa mioyo ya watu wengi zaidi leo: watu ambao wana njaa ya kujua mambo ya kiroho lakini hawaamini dini.” Imekadiriwa kwamba katika nchi ya Brazili peke yake “kuna angalau vikundi 30 ambavyo imani yao inategemea vitabu vya Apokrifa.”
Kugunduliwa kwa maandishi hayo kumeeneza maoni ya kwamba katika karne ya nne W.K., Kanisa Katoliki lilifanya mpango wa siri wa kuficha ukweli kumhusu Yesu, na kwamba masimulizi fulani ya maisha yake yaliyokuwa katika maandishi ya Kiapokrifa yalifichwa, na kwamba vile vitabu vinne vya Injili ambavyo viko katika Biblia za leo vilibadilishwa. Elaine Pagels, profesa wa dini, alisema hivi: “Sasa tumeanza kuona kwamba ule ambao tunauita Ukristo na desturi ya Kikristo, kwa kweli ni sehemu ndogo sana iliyochaguliwa kutoka katika vyanzo fulani vichache kati ya vyanzo vingine vingi.”
Kulingana na maoni ya wasomi kama Pagels, Biblia si chanzo pekee cha imani ya Kikristo; kuna vyanzo vingine, kama vile maandishi ya Kiapokrifa. Kwa mfano, kipindi kimoja katika stesheni ya BBC kinachoitwa Mafumbo ya Biblia, kilichozungumza kuhusu “Maria Magdalene wa Kweli,” kilisema kwamba maandishi ya Kiapokrifa yanafundisha kwamba Maria Magdalene alikuwa “mwalimu na kiongozi wa kiroho wa wanafunzi wengine. Yeye si mwanafunzi tu; yeye ni mtume aliyetumwa kwa mitume.” Akitoa maelezo kuhusu daraka hilo la Maria Magdalene, Juan Arias, anaandika hivi katika gazeti O Estado de S. Paulo la Brazili: “Leo tuna kila sababu ya kuamini kwamba kikundi cha kwanza cha Kikristo, kilichoanzishwa na Yesu, kilisimamiwa kabisa na ‘wanawake,’ kwa kuwa makanisa ya kwanza yalikuwa katika nyumba za wanawake, ambamo walitumika wakiwa makasisi na maaskofu.”
Watu wengi wanaona kwamba maandishi ya Kiapokrifa yana uzito zaidi kuliko Biblia. Hata hivyo, maoni hayo yanatokeza maswali fulani ya maana: Je, maandishi ya Kiapokrifa ni msingi unaofaa wa imani ya Kikristo? Maoni hayo yanapopinga mafundisho yaliyo wazi ya Biblia, tunapaswa kuamini nini, Biblia au vitabu vya Apokrifa? Je, kweli kulikuwa na mpango wa siri katika karne ya nne wa kuficha vitabu hivyo na kubadili vile vitabu vinne vya Injili ili kuondoa habari ya maana kumhusu Yesu, Maria Magdalene, na wengine? Ili tupate majibu kwa maswali hayo, acheni tuchunguze Injili moja kati ya zile Injili nne za Biblia, Injili ya Yohana.
Uthibitisho Kutoka Katika Injili ya Yohana
Kipande cha maana sana cha kitabu cha Injili ya Yohana kilipatikana huko Misri mwanzoni mwa karne ya 20 na sasa kinaitwa Papyrus Rylands 457 (P52). Kipande hicho kina kitabu cha Yohana 18:31-33, 37, 38 ambacho kinapatikana katika Biblia za leo na kimewekwa katika Maktaba ya John Rylands, huko Manchester, Uingereza. Hicho ndicho kipande cha zamani zaidi kilichopo cha hati ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Wasomi wengi wanaamini kwamba kiliandikwa karibu mwaka wa 125 W.K., robo karne hivi baada ya kifo cha Yohana. Jambo la kushangaza ni kwamba maandishi ya kipande hicho yanalingana sana na maandishi ya hati za baadaye. Uhakika wa kwamba nakala ya zamani sana ya Injili ya Yohana ilikuwa tayari imefika nchini Misri, ambako kipande hicho kilipatikana, unaunga mkono maoni ya kwamba habari njema kulingana na Yohana kwa kweli iliandikwa na Yohana mwenyewe katika karne ya kwanza W.K., kama Biblia inavyoonyesha. Kwa hiyo, kitabu cha Yohana kiliandikwa na mtu aliyejionea matukio hayo.
Kwa upande mwingine, maandishi yote ya Kiapokrifa yaliandikwa katika karne ya pili na kuendelea, miaka 100 au zaidi baada ya mambo yaliyomo kutukia. Wataalamu fulani wanadai kwamba maandishi ya Kiapokrifa yanategemea maandishi au mapokeo ya zamani, lakini hakuna uthibitisho wa jambo hilo. Kwa hiyo, swali hili linafaa, Ungeamini nini, ushahidi wa watu waliojionea matukio hayo au wa watu walioishi miaka 100 baadaye? Jibu ni wazi.b
-
-
Kwa Nini Unaweza Kuamini Vitabu vya Injili vya Biblia?Mnara wa Mlinzi—2010 | Machi 1
-
-
a Neno “Kignosti” linatokana na neno la Kigiriki ambalo linaweza kumaanisha “ujuzi wa kisiri” na neno “Apokrifa” linaloweza kumaanisha “habari iliyofichwa kwa uangalifu.” Maneno hayo yanatumiwa kuhusu maandishi ya uwongo au yasiyokubaliwa ambayo yanajaribu kuiga vitabu vya Injili, Matendo, barua, na mafunuo katika vitabu vinavyokubaliwa vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.
-