-
Unapokumbwa na UgonjwaAmkeni!—2001 | Januari 22
-
-
Unapokumbwa na Ugonjwa
John, baada ya kugundua kwamba alikuwa na ugonjwa wenye kudhoofisha—“Nilishtuka sana.”
Beth, baada ya kufahamu hatari ya ugonjwa wake.—“Nilihofu sana.”
KUFAHAMU kwamba una ugonjwa wa kudumu au wa kulemaza au kufahamu kwamba utalemaa kabisa kwa sababu ya majeraha uliyoyapata katika aksidenti ni mojawapo ya mambo yenye kuhuzunisha zaidi maishani. Iwe utapokea habari za ugonjwa wako katika ofisi tulivu ya daktari au utagundua ulemavu wako katika chumba cha tiba ya dharura chenye hekaheka, yamkini utapigwa na bumbuazi. Maisha hayakutayarishi kukabiliana na hisia-moyo kali zinazokukumba wakati unaposhikwa na tatizo baya sana la kiafya.
Ili kukusanya habari ambazo zaweza kuwasaidia wale ambao afya yao imezorota vibaya hivi karibuni, Amkeni! liliwahoji watu kadhaa kutoka nchi mbalimbali ambao wamekabiliana kwa mafanikio na ugonjwa wa kudumu wenye kulemaza kwa miaka mingi. Waliombwa watoe maoni yao kwa maswali kama vile: Ulihisije? Ni nini kilichokusaidia ustahimili tatizo hilo na kupata usawaziko tena? Ulichukua hatua gani ili kudhibiti tena maisha yako kwa njia fulani? Habari yenye kuarifu kutoka kwa mahoji hayo ya moja kwa moja na vilevile matokeo ya watafiti ambao wanachunguza athari za magonjwa ya kudumu yameandikwa ili kuwanufaisha wale wanaokabili ugonjwa hivi sasa.a
[Maelezo ya Chini]
a Ingawa mfululizo huu unaelekezwa hasa kwa wale walio wagonjwa au walemavu, mfululizo “Ugonjwa wa Kudumu—Kukabiliana Nao Mkiwa Familia” (Gazeti la Amkeni! la Mei 22, 2000) ulikuwa na habari iliyoelekezwa hasa kwa wale ambao wanawatunza wagonjwa.
-
-
Kufadhaishwa na Hisia-MoyoAmkeni!—2001 | Januari 22
-
-
Kufadhaishwa na Hisia-Moyo
“BAADA ya kuambiwa kwamba nilikuwa na ugonjwa wenye kufisha,” akumbuka mwanamume mmoja mzeemzee, “nilijaribu kushinda hofu yangu, lakini hisia za shaka zilinilemea.” Maneno yake yakazia uhakika wa kwamba ugonjwa mbaya haumlemazi mtu kimwili tu bali pia humwumiza kihisia. Hata hivyo, kuna watu ambao wanakabiliana kwa mafanikio na hali hizo. Wengi wao wangependa kukuhakikishia kwamba kuna njia za kukabiliana kwa mafanikio na ugonjwa wenye kudumu. Lakini kabla ya kuzungumzia unaloweza kufanya, acheni kwanza tuchunguze kinagaubaga baadhi ya hisia ambazo yaelekea zitakupata mwanzoni.
Kutoamini, Kutokubali, Kuhuzunika
Waweza kuwa na hisia-moyo tofauti sana na za wengine. Hata hivyo, wataalamu wa afya na watu wanaougua wanasema kwamba watu wanaokumbwa na ugonjwa huwa na hisia-moyo mbalimbali za kawaida. Mwanzoni wao hushtuka na kutoamini kisha wanakuwa na hisia za kutokubali: ‘Haiwezi kuwa kweli.’ ‘Lazima wawe wamekosea.’ ‘Labda walichanganya matokeo ya upimaji kwenye maabara.’ Mwanamke mmoja alieleza alivyohisi alipoambiwa ana kansa: “Unataka tu kujifunika kichwa kwa blanketi, na unatumaini kwamba ukijifunua itakuwa imetokomea.”
Lakini unapoanza kung’amua kuwa ni kweli, unahuzunika sana kwa sababu ya mabaya yatakayokupata. ‘Nitaishi muda mrefu kadiri gani?’ ‘Je, nitaishi kwa maumivu hadi nifapo?’ na maswali mengine kama hayo yaweza kukusumbua. Huenda ukatamani kuishi jinsi ulivyoishi kabla ya kugunduliwa kwa ugonjwa wako, lakini huwezi. Punde si punde waweza kujikuta umelemewa sana na hisia nyingine kali na zenye kuumiza. Hisia kama zipi?
Kukosa Uhakika, Kufadhaika, Hofu
Ugonjwa mbaya sana hukufanya ukose uhakika kabisa na ufadhaike. “Nyakati nyingine, hali yangu isiyojulikana hufanya maisha yawe yenye kutamausha sana,” asema mwanamume mwenye ugonjwa wa kutetemeka. “Kila siku, nina wasiwasi kuhusu hali yangu.” Ugonjwa wako waweza pia kukuogopesha. Endapo utazuka ghafula, waweza kulemewa mno na hofu. Hata hivyo, ikiwa ugonjwa wako umegunduliwa baada ya kusumbuliwa kwa miaka mingi sana na dalili ambazo hazikupimwa vizuri, huenda hofu hiyo isiwe dhahiri. Mwanzoni, huenda hata ukatulia kwa kuhisi kwamba hatimaye watu wataamini kwamba kwa kweli wewe ni mgonjwa na wala si kisingizio. Lakini, baada ya muda utulivu huo waweza kufuatwa na hofu kuu unapogundua matokeo ya ugonjwa wako.
Hofu ya kushindwa kudhibiti maisha yako yaweza pia kukutia wasiwasi. Hasa ikiwa unapenda kujitegemea, huenda ukahofu ufikiripo uwezekano wa kuwategemea wengine zaidi na zaidi. Huenda ukahangaika kwamba ugonjwa wako unaanza kudhibiti maisha yako na kukuwekea mipaka.
Hasira, Aibu, Upweke
Waweza pia kushikwa na hasira unapong’amua kwamba huwezi kudhibiti maisha yako. ‘Mbona iwe mimi? Kwani nilifanya nini ili nistahili hali hii?’ huenda ukajiuliza. Pigo hilo kwa afya yako huonekana kuwa lisilo la haki na lisilofaa. Aibu na kukata tamaa kwaweza kukupata ghafula. Mtu mmoja aliyepooza akumbuka hivi: “Niliaibika sana kwamba nilipatwa na hali hiyo kwa sababu ya aksidenti moja ya kipumbavu!”
Huenda ukaanza kujitenga na wengine. Kujitenga na wengine kwaweza kusababisha upweke kwa urahisi. Iwapo ugonjwa wako wakuzuilia nyumbani, huenda usiweze tena kushirikiana na marafiki wa zamani. Lakini, huo ndio wakati unapotamani sana ushirika wa wengine kuliko wakati mwingine wowote. Baada ya kukutembelea na kukupigia simu kwa bidii sana mwanzoni, sasa ni watu wachache zaidi na zaidi wanaokutembelea au kukupigia simu.
Kwa kuwa inaumiza kuona marafiki wakijitenga nawe, huenda hali hiyo yenye kutia uchungu ikakufanya ujitenge kabisa na wengine. Bila shaka, inaeleweka kwamba waweza kuhitaji kuwa peke yako kabla ya kushirikiana na wengine tena. Lakini ikiwa utajitenga na wengine zaidi wakati huu, huenda hali yako ya kukosa marafiki (ambapo wengine hawakutembelei) ikutumbukize katika upweke wa kihisia-moyo (ambapo hutaki kuwaona wengine). Vyovyote vile, yaelekea unapambana na hisia kali mno za upweke.a Nyakati nyingine, huenda ukawa na tashwishi iwapo utaendelea kuishi.
Kujifunza Kutokana na Wengine
Hata hivyo, kuna tumaini. Iwapo umekumbwa na ugonjwa hivi karibuni, kuna hatua madhubuti unazoweza kuchukua ambazo zitakusaidia kudhibiti tena maisha yako kwa kadiri fulani.
Bila shaka, mfululizo huu wa makala hautasuluhisha ugonjwa wowote ule wa kudumu ulio nao. Lakini, habari iliyotolewa yaweza kukusaidia kujua jinsi ya kukabiliana na ugonjwa wako. Mwanamke mmoja mwenye kansa alisema hivi kwa ufupi kuhusu mawazo na hisia zake: “Baada ya kutokubali hali yangu nilishikwa na hasira kali kisha nikaanza kutafuta msaada.” Wewe pia waweza kutafuta msaada, kwa kuzungumza na watu ambao wamepatwa na hali hiyohiyo na ujifunze kutokana nao jinsi unavyoweza kunufaika na msaada wa wengine walio karibu nawe.
[Maelezo ya Chini]
a Bila shaka, watu wengi hupatwa na hisia hizo mbalimbali kwa njia na hali mbalimbali.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
‘Mbona iwe mimi? Kwani nilifanya nini ili nistahili hali hii?’ huenda ukajiuliza
-
-
Kuishi kwa Mafanikio na Ugonjwa Wako—Jinsi Gani?Amkeni!—2001 | Januari 22
-
-
Kuishi kwa Mafanikio na Ugonjwa Wako—Jinsi Gani?
UWE na hakika kwamba hisia ambazo yaelekea zinakukumba zinatarajiwa kuwapo. Ijapokuwa huenda ukawa mgonjwa au ukawa umelemaa kimwili, akili yako hukinza mabadiliko ambayo yamesababishwa na ugonjwa wako. Huenda ikaonekana kana kwamba unapambana kufa kupona na ugonjwa wako, huku ukifikiria sana hali yako ya awali na hali yako ya baadaye. Na hivi sasa huenda ikaonekana kana kwamba ugonjwa wako unakulemea. Lakini unaweza kubadili hali hiyo. Jinsi gani?
“Ugonjwa unapomwathiri mtu vibaya,” asema Dakt. Kitty Stein, “anahisi ni kama amefiwa.” Hivyo basi, afya yako ambayo ni ya thamani sana inapozorota, ni kawaida kuomboleza na kulia kwa muda fulani, kama vile ambavyo ungefanya endapo ungefiwa na mpendwa wako. Kwa kweli, huenda ukaathiriwa kwa njia nyingine mbali na afya yako. Ni kama mwanamke mmoja anavyoeleza, “Ilinibidi kuacha kazi yangu. . . . Ilinibidi kupoteza uhuru ambao nilikuwa nikifurahia daima.” Hata hivyo, uwe na maoni yaliyosawazika kuhusu matokeo hayo yote. “Omboleza kuhusu hali uliyopoteza,” aongezea Dakt. Stein, ambaye ana ugonjwa wa kukakamaa kwa tishu (multiple sclerosis), “lakini wahitaji pia kufahamu uwezo ambao ungali nao.” Kwa kweli, baada ya kupambana na kilio chako mwanzoni, utagundua kwamba ungali na uwezo muhimu sana. Kwanza, una uwezo wa kunyumbulika.
Baharia hawezi kudhibiti dhoruba, bali anaweza kustahimili dhoruba kwa kurekebisha matanga ya merikebu yake. Vivyo hivyo, huenda usiweze kudhibiti ugonjwa ambao umekukumba kama dhoruba, lakini unaweza kukabiliana nao kwa kurekebisha “matanga” yako, yaani, uwezo wako wa kimwili, kiakili, na kihisia-moyo. Nini kimewasaidia watu wengine wenye ugonjwa wa kudumu kufanya hivyo?
Jifunze Kuhusu Ugonjwa Wako
Baada ya kustahimili uchungu wanaohisi ugonjwa wao unapogunduliwa, watu wengi huhisi kwamba kujua ukweli huo mchungu ni bora kuliko kuhofu bila msingi. Hofu yaweza kukuzuia kutenda, ilhali kujua hali yako kwaweza kukusaidia kufikiria hatua unayoweza kuchukua—na kufanya hivyo tu hunufaisha. “Fikiria furaha unayokuwa nayo unapobuni mbinu ya kusuluhisha tatizo linalokuhangaisha,” asema Dakt. David Spiegel wa Chuo Kikuu cha Stanford. “Kabla hujafanya lolote, punguza wasiwasi wako kwa kupanga hatua ya kuchukua.”
Huenda ukaona uhitaji wa kujifunza mengi kuhusu hali yako. Ni kama tu mithali moja ya Biblia inavyosema, “mtu mwenye maarifa huongeza uwezo.” (Mithali 24:5) “Azima vitabu kutoka kwenye maktaba. Jifunze mengi kadiri uwezavyo kuhusu ugonjwa wako,” ashauri mwanamume mmoja aliye mgonjwa kitandani. Kadiri unavyojifunza kuhusu matibabu yaliyopo na mbinu za kukabiliana na ugonjwa, huenda ukaona kwamba hali yako labda si mbaya kama ulivyohofia. Huenda hata ukapata sababu za kutarajia mema.
Hata hivyo, lengo lako kuu si kuwa tu na maarifa ya ugonjwa wako. Dakt. Spiegel aeleza hivi: “Ukusanyaji huo wa habari ni sehemu muhimu ya kukabiliana na ugonjwa, kuuelewa, na kuwa na maoni yanayofaa kuuhusu.” Kukubali kwamba maisha yako yamebadilika ujapokuwa hai si jambo rahisi na kwa kawaida huchukua muda. Lakini hatua hii ya ziada—ya kutokuwa tu na maarifa ya ugonjwa wako bali kuukubali kihisia—ni hatua unayoweza kuchukua. Vipi?
Kupata Usawaziko Unaofaa
Huenda ukalazimika kurekebisha maoni yako kuhusu maana ya kukubali ugonjwa wako. Kwani, kukubali kwamba wewe ni mgonjwa hakumaanishi umeshindwa, kama vile tu haimaanishi baharia ameshindwa kwa kukubali uhakika wa kwamba yuko katika dhoruba. Badala yake, kukubali kwamba anakabili dhoruba humchochea kutenda. Hali kadhalika, kukubali kwamba wewe ni mgonjwa hakumaanishi umeshindwa, lakini humaanisha “kupiga hatua kuelekea upande mwingine,” ndivyo alivyosema mwanamke mmoja mwenye ugonjwa wa kudumu.
Hata ingawa uwezo wako wa kimwili umedidimia, yamkini utahitaji kujikumbusha kwamba sifa zako za kiakili, kihisia-moyo, na kiroho hazihitaji kuathiriwa. Mathalani, je, uwezo wako wa kufikiri na wa kupanga mambo na kusababu ungalipo? Labda ungali unatabasamu kwa uchangamfu, ungali unawajali wengine, ungali na uwezo wako wa kusikiliza wengine kwa makini na kuwa rafiki wa kweli. Na la muhimu zaidi ni kwamba ungali na imani katika Mungu.
Zaidi ya hayo, kumbuka kwamba ijapokuwa huwezi kubadili hali yako, bado unaweza kuamua jinsi ya kuitikia hali hiyo. Irene Pollin wa Taasisi ya Taifa ya Kansa asema: “Ni jukumu lako kuamua utakavyoitikia ugonjwa wako. Unaweza kufanya hivyo haidhuru athari ya ugonjwa wako.” Helen, mwanamke mwenye umri wa miaka 70 aliyedhoofishwa sana na ugonjwa wa kukakamaa kwa tishu, athibitisha hilo: “Kuwa tena na usawaziko wa kiakili na kihisia-moyo hakutegemei ugonjwa wako bali jinsi unavyoitikia ugonjwa huo.” Mtu mmoja ambaye amekabiliana na ulemavu kwa miaka kadhaa asema hivi: “Mtazamo chanya ni kama mkuku unaosawazisha merikebu.” Kwa kweli, Mithali 18:14 yasema hivi: “Roho ya mtu itastahimili udhaifu wake; bali roho iliyovunjika nani awezaye kuistahimili?”
Kupata Tena Usawaziko
Unapopata tena usawaziko wa kihisia-moyo, maswali kama vile, ‘Mbona nikapatwa na hali hii?’ yaweza kukufanya ujiulize ‘Kwa kuwa hali hii imenipata, nifanye nini kuihusu?’ Wakati huo waweza kuamua kuchukua hatua zaidi za kuboresha hali yako ya sasa. Acheni tuchunguze baadhi ya hatua hizo.
Changanua hali yako, fikiria mambo unayoweza kurekebisha, kisha jitahidi kubadili yale yanayoweza kubadilishwa. “Ugonjwa wako unakupa fursa yakuchunguza upya maisha yako—ni mwito wa kukuamsha, si wa kushindwa kabisa,” asema Dakt. Spiegel. Jiulize hivi, ‘Ni nini kilichokuwa muhimu kwangu kabla sijawa mgonjwa? Hilo limebadilikaje?’ Jiulize maswali hayo, si kwa madhumuni ya kujua mambo usiyoweza kufanya, bali kujua yale unayoweza kufanya, labda kwa kutumia njia nyingine. Kwa mfano, mfikirie Helen, aliyetajwa awali.
Kwa miaka 25 iliyopita, ugonjwa wa kukakamaa kwa tishu umedhoofisha misuli yake. Mwanzoni, alikuwa akitembea kwa msaada wa kifaa cha matembezi. Baadaye, aliposhindwa kutumia mkono wake wa kulia, alianza kutumia wa kushoto. Halafu, mkono wake wa kushoto ukadhoofika kabisa. Hatimaye, miaka minane iliyopita, alishindwa kabisa kutembea. Sasa anahitaji kuoshwa, kulishwa, na kuvishwa mavazi na wengine. Hilo humhuzunisha sana, hata hivyo, yeye asema: “Mwito wangu ungali, ‘Fikiria mambo unayoweza kufanya wala si yale uliyokuwa ukifanya.’” Na kwa msaada wa mumewe na wauguzi wanaomtembelea vilevile ubunifu wake mwenyewe, yeye huweza kufanya kazi fulani ambazo amekuwa akifurahia. Kwa mfano, kuwaeleza wengine ahadi ya Biblia ya ulimwengu wenye amani unaokuja kumekuwa sehemu muhimu sana ya maisha yake tangu alipokuwa na umri wa miaka 11, na leo bado anafanya hivyo kila juma. (Mathayo 28:19, 20) Helen aeleza anavyofanya:
“Mimi humwomba muuguzi anayenitembelea anishikie gazeti. Tunasoma pamoja matangazo ya vifo na kuteua kadhaa. Kisha mimi humwambia muuguzi huyo mambo ninayotaka yaandikwe kwenye barua nitakayowatumia watu wa ukoo wa yule aliyekufa, halafu muuguzi huyo hupiga chapa barua hiyo. Mimi huambatanisha barua hiyo na broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa,a ambayo inaeleza tumaini la Biblia la ufufuo lenye kufariji. Mimi hufanya hivyo kila Jumapili alasiri. Mimi hufurahi kwa sababu bado naweza kujulisha wengine habari njema za Ufalme wa Mungu.”
Weka miradi inayofaa na unayoweza kutimiza. Sababu moja inayomfanya Helen ajaribu kubadili mambo yanayoweza kubadilishwa ni kwamba kufanya hivyo humwezesha kuweka na kutimiza miradi. Hilo ni muhimu kwako pia. Kwa nini? Kwa sababu kuweka miradi hukufanya ukazie akili wakati ujao, na kutimiza miradi hukufanya uhisi unafaulu. Huenda pia ikahuisha tena hali yako ya kujiamini. Hata hivyo, hakikisha kwamba unaweka mradi hususa. Mathalani, unaweza kuazimia hivi: ‘Nitasoma sura moja ya Biblia leo.’ Weka pia miradi ambayo ni halisi kwako. Kwa kuwa hali yako ya kimwili na ya kihisia-moyo ni tofauti na ya watu wengine wenye magonjwa ya kudumu, huenda usiweze kutimiza miradi sawa na yao.—Wagalatia 6:4.
“Haidhuru mradi waonekana mdogo kadiri gani, kuutimiza hukuchochea kufanya zaidi,” asema Lex, mkazi wa Uholanzi. Zaidi ya miaka 20 iliyopita, alipokuwa na umri wa miaka 23, alihusika katika aksidenti iliyomfanya apooze. Wakati wa vipindi vingi vya matibabu ya maungo vilivyofuata, alitiwa moyo ajiwekee miradi, kama vile kunawa uso kwa kitambaa. Ilikuwa kazi ya kuchosha sana, lakini alifaulu. Alipoona kwamba alikuwa amefaulu kutimiza mradi huo, aliweka mradi mwingine—kufunua na kufunika tyubu ya dawa ya meno bila msaada. Alifaulu tena. “Ijapokuwa haikuwa rahisi,” asema Lex, “niligundua kwamba ningeweza kufanya mengi zaidi ya vile nilivyofikiri.”
Kwa kweli, Lex alitimiza miradi mikubwa zaidi kwa msaada wa mke wake. Kwa mfano, sasa yeye huandamana na Tineke, kwenda nyumba kwa nyumba kwa kiti cha magurudumu ili kushiriki na wengine ujuzi wa Biblia. Kila juma yeye pia humtembelea na kumtia moyo mtu mmoja aliyelemaa kabisa ambaye anajifunza naye Biblia. “Kuwasaidia wengine,” asema Lex, “hunipa uradhi mkubwa.” Kama Biblia inavyothibitisha, “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.
Je, waweza pia kuweka miradi ya kuwasaidia wengine? Kuugua au kulemaa kwaweza kukusaidia kuwa mfariji stadi sana kwa sababu matatizo yako hukufanya uwe na hisia kuelekea maumivu ya wengine.
Shirikiana na wengine. Uchunguzi wa kitiba waonyesha kwamba kushirikiana na wengine huboresha afya yako. Kwa upande mwingine, kutoshirikiana na wengine ni hatari. “Uhusiano baina ya kujitenga na wengine na kifo ni . . . mkubwa sana kama uhusiano baina ya kuvuta sigareti . . . na kifo,” asema mtafiti mmoja. Aongezea hivi: “Kuboresha uhusiano wako na wengine ni muhimu kwa afya yako kama vile kuacha kuvuta sigareti kulivyo muhimu.” Si ajabu yeye afikia mkataa wa kwamba ustadi wetu katika kudumisha uhusiano na wengine “ni muhimu sana kwa maisha”!—Mithali 18:1.
Lakini, kama ilivyoelezwa katika makala inayotangulia, huenda tatizo likawa kwamba baadhi ya marafiki wako wameacha kukutembelea. Kwa manufaa yako unahitaji kuepuka mwelekeo wa kujitenga na wengine. Jinsi gani? Unaweza kuanza kwa kuwaalika marafiki wako wakutembelee.
Starehesha wageni.b Unaweza kufanya hivyo kwa kuepuka kuzungumza mno kuhusu ugonjwa wako ili wageni wako wasije wakachoshwa na habari hizo. Mwanamke mmoja mwenye ugonjwa wa kudumu alisuluhisha tatizo hilo kwa kuweka mipaka ya wakati aliotumia akizungumza na mumewe kuhusu ugonjwa wake. “Hatukuwa na budi kuweka mipaka ya mazungumzo hayo,” yeye asema. Kwa kweli, ugonjwa wako hauhitaji kuzuia mambo mengineyo unayoweza kushiriki. Mgeni mmoja, baada ya kuongea na rafikiye aliye kitandani kuhusu sanaa, historia, na sababu zinazomfanya awe na imani katika Yehova Mungu, alisema: “Yeye hajaruhusu ugonjwa wake uathiri utu wake. Nilifurahi mno kuongea naye.”
Kuwa mcheshi daima kutawafanya marafiki wako wafurahie kukutembelea. Mbali na hayo, kicheko hukunufaisha wewe binafsi. “Ucheshi hukusaidia kukabiliana na hali mbalimbali zinazosababishwa na mambo tofauti-tofauti,” asema mwanamume mmoja mwenye maradhi ya kutetemeka. Kwa kweli, kicheko chaweza kuwa dawa bora. Mithali 17:22 yasema: “Moyo uliochangamka ni dawa nzuri.” Hata kucheka kwa dakika chache kwaweza kuboresha afya yako. Isitoshe, “tofauti na matibabu mengine tunayojaribu, kicheko ni salama kabisa, hakina madhara, na kinaburudisha,” asema mtungaji Susan Milstrey Wells, ambaye pia ana ugonjwa wa kudumu. “Tunapocheka tunaepuka msononeko.”
Tafuta njia za kupunguza mkazo. Uchunguzi wathibitisha kwamba mkazo waweza kuzidisha dalili za ugonjwa, ilhali kupunguza mkazo huzifanya zistahimilike. Hivyo basi, pumzika mara kwa mara. (Mhubiri 3:1, 4) Usifanye ugonjwa wako uwe jambo kuu maishani. Unapokuwa nyumbani, waweza kujaribu kupunguza mkazo wa hisia-moyo zako kwa kusikiliza muziki taratibu, kusoma kitabu, kuoga mwili pasina haraka, kuandika barua au mashairi, kuchora picha, kucheza ala ya muziki, kuzungumza na rafiki unayemtumaini, au kufanya mambo mengine kama hayo. Kufanya hivyo hakutasuluhisha kabisa tatizo lako, lakini kwaweza kukutuliza kwa kitambo.
Ikiwa unaweza kutembea, fanya matembezi, nenda dukani, tunza bustani, endesha gari au, ikiwezekana, chukua likizo. Kwa wazi, kusafiri kwaweza kuchosha sana kwa sababu ya ugonjwa wako, lakini ukipanga mapema na ukiwa mbunifu, waweza kushinda vikwazo vilivyopo. Mathalani, Lex na Tineke, waliotajwa awali, walifaulu kusafiri ng’ambo. “Mwanzoni, tulikuwa na wasiwasi kidogo,” asema Lex, “lakini tulikuwa na likizo ya kupendeza sana!” Kwa kweli, huenda ukaishi na ugonjwa wako, lakini si lazima ugonjwa huo udhibiti maisha yako.
Pata nguvu kwa kuwa na imani. Wakristo wa kweli ambao wamefaulu kukabiliana na ulemavu mbaya wanasema kwamba imani yao kwa Yehova Mungu na pia ushirika wao na kutaniko la Kikristo ni vyanzo vya faraja na nguvu daima.c Yafuatayo ni baadhi ya maelezo yao kuhusu umuhimu wa kusali, kujifunza Biblia, kutafakari kuhusu wakati ujao, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme.
● “Bado mimi hushuka moyo mara kwa mara. Hilo linapotukia, mimi husali kwa Yehova, naye huimarisha tena azimio langu la kuendelea kufanya yote niwezayo.”—Zaburi 55:22; Luka 11:13.
● “Kusoma Biblia na kutafakari yale ninayosoma hunisaidia sana kudumisha amani yangu ya akili.”—Zaburi 63:6; 77:11, 12.
● “Funzo la Biblia hunikumbusha kwamba uhai halisi utakuja wakati ujao na kwamba sitakuwa kilema milele.”—Isaya 35:5, 6; Ufunuo 21:3, 4.
● “Kuwa na imani katika wakati ujao ulioahidiwa katika Biblia hunitia nguvu kushughulika na maisha siku kwa siku.”—Mathayo 6:33, 34; Waroma 12:12.
● “Kuhudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme hunisaidia nikazie akili mambo yajengayo wala si ugonjwa wangu.”—Zaburi 26:12; 27:4.
● “Ushirika wenye kutia moyo na washiriki wa kutaniko huuchangamsha moyo wangu.”—Matendo 28:15.
Biblia hutuhakikishia hivi: “BWANA ni mwema, ni ngome siku ya taabu; naye huwajua hao wamkimbiliao.” (Nahumu 1:7) Kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu na kushirikiana na kutaniko la Kikristo ni vyanzo vya faraja na nguvu.—Waroma 1:11, 12; 2 Wakorintho 1:3; 4:7.
Jipe Muda
Kuishi kwa mafanikio na ugonjwa wako mbaya au ulemavu ni hali “inayotukia baada ya muda mrefu wala si siku moja tu,” asema mfanyakazi mmoja wa jamii ambaye huwasaidia watu wamudu athari za ugonjwa wa kudumu. Jipe muda, ashauri mtaalamu mwingine, kwa kuwa unajifunza “ustadi mpya kabisa: kushughulika na ugonjwa mbaya.” Ng’amua kwamba hata ukiwa na mtazamo chanya, unaweza kuwa na siku mbaya au majuma ambayo athari za ugonjwa wako hukulemea sana. Hata hivyo, yaelekea utaona maendeleo baada ya muda. Ndivyo ilivyokuwa kwa mwanamke mmoja, aliyesema hivi: “Nilisisimuka sana nilipotambua kwamba kwa siku nzima sikuwa nimefikiria kansa yangu. . . . Muda fulani uliopita, singeweza kamwe kudhani kwamba hilo lingewezekana.”
Kwa kweli, mara tu ukisha shinda hofu ya mwanzoni na kuweka miradi mipya, utashangaa kujikuta ukikabiliana na hali kwa njia bora sana—kama makala ifuatayo inavyoonyesha.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Madokezo hayo kuhusu jinsi ya kuwatendea wageni, bila shaka, yanahusu hata zaidi jinsi unavyomtendea mwenzi wako, watoto wako, au yule anayekutunza.
c Jambo la kupendeza ni kwamba, uchunguzi mwingi sana wa kitiba umeonyesha kwamba imani huboresha afya na hali njema ya mtu. Profesa Dale Matthews wa Kitivo cha Kitiba cha Chuo Kikuu cha Georgetown asema kwamba, “imani imethibitishwa kuwa muhimu sana.”
[Picha katika ukurasa 7]
Kujifunza kuhusu ugonjwa wako kwaweza kukusaidia ukabiliane nao
[Picha katika ukurasa 8]
Kwa msaada wa wengine, Helen huandika barua zenye kutia moyo
[Picha katika ukurasa 8]
“Mimi hufurahi kujulisha wengine habari njema za Ufalme wa Mungu”
[Picha katika ukurasa 9]
“Niligundua kwamba, ijapokuwa nimepooza, ningeweza kufanya mengi zaidi ya vile nilivyofikiri.”—Lex
-
-
Kushinda Vipingamizi kwa Kuweka MiradiAmkeni!—2001 | Januari 22
-
-
Kushinda Vipingamizi kwa Kuweka Miradi
WILLIAM (Bill) Meiners na mkewe, Rose, wanaishi katika chumba kimoja karibu na Uwanja wa Ndege wa LaGuardia huko New York. Humo Rose, mkaribishaji mwenye haiba aliye na umri wa kati ya miaka ya 70, amkaribisha mgeni wake kwa uchangamfu. Mtu aingiapo chumbani anaona mara moja kwamba sebule yenye kustarehesha inapendeza na kulandana na uchangamfu wa Rose. Mpangilio maridadi wa maua karibu mlangoni na picha zenye kuvutia zilizo ukutani huleta hisia ya shangwe na shauku kubwa ya kuishi.
Kuna chumba chenye kuvutia sana karibu na sebule ambamo Bill, mwenye umri wa miaka 77, amelala kitandani, mgongo wake ukiwa umetegemezwa na godoro linalorekebishika. Mara tu anapomwona mgeni wake, macho yake ya fadhili yanang’aa naye anatabasamu kwa shauku. Angependa kuinuka, kumsalimu kwa mikono, na kumkumbatia, lakini hawezi. Bill amepooza mwili wote ila mkono wake wa kushoto.
Kwa kuwa Bill amekuwa na matatizo ya afya tangu alipokuwa na umri wa miaka 26, yeye aulizwa kile ambacho kimemsaidia kukabiliana na ugonjwa wake kwa zaidi ya miaka 50. Bill na Rose waangaliana kwa kicheko. “Hatumjui mgonjwa yeyote!” asema Rose, huku kicheko chake cha kutoka moyoni kikisambaa chumbani. Macho ya Bill yang’aa kwa furaha; acheka-cheka na kutikisa kichwa chake kwa kuitikia. “Hakuna mgonjwa hapa,” yeye asema kwa kusitasita kwa sauti nzito yenye kukwaruza. Rose na Bill wataniana kwa mchezo, na punde si punde, kicheko chazagaa chumbani. Ni dhahiri kwamba Bill na Rose wangali na upendo waliokuwa nao walipokutana mara ya kwanza mnamo Septemba 1945. Bill aulizwa tena: “Lakini bila utani wowote, umekabili vipingamizi gani? Ni nini ambacho kimekusaidia kukabiliana navyo na kudumisha mtazamo chanya maishani?” Baada ya kumsihi, Bill akubali kusimulia yaliyompata. Yafuatayo ni madondoo ya mazungumzo kadhaa kati ya Amkeni!, Bill na mkewe.
Vipingamizi Vyaanza
Mnamo Oktoba 1949—miaka mitatu baada ya kumwoa Rose na miezi mitatu baada ya kuzaliwa kwa binti yao, Vicki—Bill alijulishwa kwamba ana uvimbe wenye kusababisha kansa katika moja ya nyuzi zake za sauti, uvimbe huo uliondolewa. Miezi michache baadaye, daktari wa Bill alimjulisha kipingamizi kingine—kansa hiyo ilikuwa imeathiri zoloto yote. “Niliambiwa kwamba bila kupasuliwa na kuondolewa zoloto yote, ningekufa baada ya miaka miwili tu.”
Bill na Rose walielezwa matokeo ambayo yangesababishwa na upasuaji huo. Zoloto huanzia kwenye shina la ulimi hadi kwenye mwingilio wa koromeo. Ndani ya zoloto mna nyuzi mbili za sauti. Hewa inayotoka mapafuni inapopita kwenye nyuzi hizo, zinatikisika na kutoa sauti za usemi. Zoloto inapoondolewa, sehemu ya juu ya koromeo huunganishwa na shimo lililotobolewa upande wa mbele wa shingo. Baada ya upasuaji, mgonjwa hupumua kupitia kwa shimo hilo—lakini huwa amepoteza sauti yake.
“Niliposikia maelezo hayo, nilikasirika sana,” asema Bill. “Tulikuwa na binti mchanga, nilikuwa na kazi nzuri, tulikuwa na mataraja bora maishani, na sasa matumaini yangu yote yalididimia kabisa.” Lakini kwa kuwa kuondolewa zoloto kungeokoa uhai wake, Bill alikubali kufanyiwa upasuaji huo. “Baada ya upasuaji,” asema Bill, “singemeza kitu chochote. Singesema hata neno moja. Nilikuwa bubu.” Rose alipomtembelea Bill, aliweza kuwasiliana naye kwa kuandika maneno kwenye kijitabu. Ulikuwa wakati mgumu sana. Ili kushinda kipingamizi hicho, walihitaji kuweka miradi mipya.
Asiyeweza Kusema na Asiye na Kazi
Upasuaji wa kuondoa zoloto mbali na kumwacha Bill akiwa bubu, ulimwacha bila kazi. Awali alikuwa akifanya kazi kwenye karakana ya mashine, lakini sasa kwa kuwa alipumua kupitia tu kwa shimo lililo shingoni, vumbi na moshi vingeweza kuhatarisha mapafu yake. Alihitaji kutafuta kazi nyingine. Huku akiwa hawezi kusema, alijiandikisha katika shule moja ili ajifunze kutengeneza saa. “Ilikuwa kama kazi yangu ya awali,” asema Bill. “Nilijua jinsi ya kuunganisha sehemu za mashine, na unapotengeneza saa, unaunganisha pia visehemu pamoja. Tofauti ni kwamba visehemu hivyo havikuwa na uzito wa kilogramu 23!” Mara tu baada ya kukamilisha masomo ya kutengeneza saa, aliajiriwa kazi ya kutengeneza saa. Alikuwa ametimiza mradi wa kwanza.
Wakati huohuo, Bill alikuwa ameanza kuhudhuria masomo ya kusema kwa umio. Katika usemi wa umio, sauti haitokezwi na nyuzi za sauti bali na mitetemo katika umio, njia ya chakula kutoka shingoni hadi tumboni. Kwanza, mtu hujifunza kumeza hewa na kuilazimisha kuingia kwenye umio. Halafu, mtu huteuka hewa hiyo kwa njia fulani maalum. Hewa inapotoka, inasababisha kuta za umio zitetemeke. Mtetemo huo hutokeza sauti nzito inayokwaruza, ambayo inaweza kudhibitiwa kwa mdomo na kuwa usemi.
“Hapo awali, niliteua tu baada ya kula sana,” asema Bill kwa tabasamu, “lakini sasa nilihitaji kujifunza kuteua kwa kawaida. Mwanzoni, niliweza kusema neno moja tu kwa wakati, kwa njia hii: ‘[Pumua, meza, teua] Habari [pumua, meza, teua] yako?’ Haikuwa rahisi. Kisha, mwalimu wangu akaniambia ninywe kinywaji kingi cha tangawizi kwa sababu gesi iliyomo ingenisaidia kuteua. Kwa hivyo wakati wowote Rose alipoenda matembezini na Vicki, nilikunywa na kuteua, kunywa na kuteua. Nilijitahidi mno!”
Ijapokuwa asilimia 60 ya wagonjwa wote wasio na zoloto hushindwa kusema kwa kutumia umio, Bill alifanya maendeleo. Vicki, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka miwili hivi, alimshurutisha pasipo kujua. Bill aeleza: “Vicki angeongea nami kisha angenitazama, akisubiri jibu. Lakini singeweza kumjibu hata kwa neno moja. Alizidi kuongea, lakini kwa mara nyingine sikujibu. Kwa hamaki, Vicki alimgeukia mke wangu na kusema: ‘Mfanye Baba aongee nami!’ Maneno yake yalinichoma sana na kunifanya niazimie kuongea tena.” Vicki, Rose, na wengineo walifurahi sana Bill alipofaulu. Alitimiza mradi mmoja zaidi.
Akumbwa na Pigo Jingine
Kufikia mwishoni mwa mwaka wa 1951, Bill na Rose walikabili tatizo jipya. Madaktari, huku wakihofia kwamba kansa ingeibuka tena, walimshauri Bill apate matibabu ya mnururisho. Bill akakubali. Matibabu yalipokamilika, alikuwa na hamu ya kurejelea maisha ya kawaida. Hakutambua kamwe kwamba pigo jingine kwa afya yake lilikuwa likija!
Mwaka mmoja hivi ulipita. Halafu, siku moja vidole vya Bill vikafa ganzi. Kisha, akashindwa kupanda ngazi. Muda mfupi baadaye, alianguka alipokuwa akitembea na hangeweza kunyanyuka tena. Uchunguzi ulionyesha kwamba matibabu ya mnururisho ambayo Bill alikuwa amepokea (ambayo, wakati huo, hayakuwa sahihi kama yalivyo leo) yalikuwa yameharibu uti wake wa mgongo. Alielezwa kwamba hali yake ingezidi kuzorota. Daktari mmoja hata alimwambia kwamba hakuwa na tumaini “lolote” la kupona. Hilo lilikuwa pigo kubwa sana kwa Bill na Rose.
Hata hivyo, katika jitihada za kushinda kipingamizi hicho, Bill alilazwa hospitalini kwa miezi sita ili kupata matibabu ya maungo. Ingawa matibabu hayo hayakubadili hali ya mwili wake, kulazwa hospitalini kulibadili maisha yake—badiliko ambalo hatimaye lilimwezesha amjue Yehova. Hilo lilitukiaje?
Atiwa Nguvu Baada ya Kuelewa Chanzo cha Vipingamizi
Kwa hiyo miezi sita, Bill alikaa katika chumba kimoja katika hospitali moja ya Kiyahudi na wanaume 19 waliopooza—wote walikuwa Wayahudi Waothodoksi. Kila alasiri wanaume hao walikuwa wakizungumzia Biblia. Bill, mhudhuriaji wa kanisa la Baptisti, alisikiliza tu. Lakini wakati wa kuondoka hospitalini ulipofika, aliyosikia yalimsaidia afikie mkataa wa kwamba Mungu Mweza Yote ni mtu mmoja tu na kwamba fundisho la Utatu hupingana na Biblia. Kama tokeo, Bill hakurudi tena kanisani. Hata hivyo, aliona uhitaji wa kupata mwelekezo wa kiroho ili kukabiliana na vipingamizi maishani. “Nilizidi kumwomba Mungu msaada,” asema Bill, “na sala zangu zilijibiwa.”
Jumamosi moja mnamo mwaka wa 1953, Roy Douglas, mwanamume mzeemzee aliyewahi kuwa jirani yake alimtembelea Bill baada ya kuelezwa hali yake. Roy, mmoja wa Mashahidi wa Yehova, alimwomba Bill ajifunze Biblia naye, Bill akakubali. Mambo ambayo Bill alisoma kwenye Biblia na katika kitabu “Let God Be True”a yalimshangaza sana. Alimwambia Rose mambo ambayo yeye alijifunza, naye akajiunga na funzo hilo. Rose akumbuka hivi: “Kanisani tulielezwa kwamba ugonjwa ni adhabu kutoka kwa Mungu, lakini katika funzo letu la Biblia tulijifunza kwamba huo ni uwongo. Hilo lilitutuliza sana.” Bill aongezea: “Kujifunza kutoka kwa Biblia kisababishi cha matatizo yote, kutia ndani ugonjwa wangu, na kujua kwamba kutakuwa na wakati ujao mzuri kulitusaidia kukabili hali yangu.” Mwaka wa 1954, Bill na Rose walitimiza mradi mwingine. Wote wawili walibatizwa kuwa Mashahidi wa Yehova.
Kufanya Marekebisho Zaidi
Wakati huo, Bill alikuwa amepooza kiasi cha kutoweza kuendelea na kazi yake ya kuajiriwa. Ili kujiruzuku, Bill na Rose walibadilishana mafungu yao: Bill alibaki nyumbani na Vicki, naye Rose akaanza kufanya kazi kwenye kampuni ya kutengeneza saa—alifanya kazi hiyo kwa miaka 35!
“Kumtunza binti yetu kuliniletea shangwe sana,” asema Bill. “Vicki aliye mchanga alifurahia pia. Kwa fahari, alikuwa akimweleza hivi kila mtu aliyekutana naye: ‘Mimi humtunza Baba!’ Baadaye, alipokuwa akienda shuleni, nilimsaidia kufanya mazoezi yake ya shuleni, na mara kwa mara tulicheza michezo. Isitoshe, nilikuwa na fursa nzuri ya kumfundisha Biblia.”
Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwenye Jumba la Ufalme pia kulimletea Bill na familia yake shangwe. Alichechemea kwa saa nzima kutoka nyumbani kwake hadi kwenye Jumba la Ufalme, lakini hakukosa mikutano. Baadaye, baada ya kuhamia eneo jingine jijini, Bill na Rose walinunua gari dogo, na Rose alipeleka familia kwenye jumba. Hata ingawa Bill angeweza kuongea kwa vipindi vifupi tu, alijiandikisha kuwa mwanafunzi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Bill aeleza: “Niliandika hotuba yangu, na ndugu mwingine aliitoa. Baada ya hotuba, mwangalizi wa shule alinishauri kuhusiana na muhtasari huo.”
Watu mbalimbali kutanikoni walimsaidia pia Bill kushiriki kikawaida katika kazi ya kuhubiri. Na wale waliokuwa wakiona ujitoaji wake hawakushangaa wakati Bill aliwekwa rasmi baadaye kuwa mtumishi wa huduma kutanikoni. Halafu, miguu yake ilipodhoofika kabisa naye akazidi kupooza, alikaa tu kwenye chumba chake na hatimaye akawa habanduki kitandani. Je, angeweza kushinda kipingamizi hicho?
Burudani Yenye Kuridhisha
“Nilitafuta burudani kwa sababu ya kushinda nyumbani siku nzima,” asema Bill. “Kabla ya kupooza nilikuwa nikifurahia kupiga picha. Kwa hiyo nilifikiria kujaribu kuchora picha, hata ingawa sikuwahi kuchora picha maishani mwangu. Awali niliandika kwa mkono wa kulia, lakini sasa mkono huo wote na vidole viwili vya mkono wangu wa kushoto vilikuwa vimepooza. Haidhuru, Rose alinunua vitabu vingi kuhusu mbinu za uchoraji. Nilivisoma na nikaamua kuchora kwa mkono wangu wa kushoto. Picha zangu nyingi ziliishia kwenye moto, lakini hatimaye nikaanza kuwa stadi.”
Picha maridadi chungu nzima zilizochorwa kwa rangi ya maji ambazo sasa zinaremba chumba cha Bill na Rose zathibitisha kwamba Bill alifanikiwa zaidi ya alivyotarajia. “Miaka mitano hivi iliyopita,” aongezea Bill, “mkono wangu wa kushoto ulianza kutetemeka sana hivi kwamba ilinibidi kuacha kabisa kuchora, lakini kwa miaka mingi burudani hiyo iliniridhisha sana.”
Mradi Unaosalia
Bill akumbuka: “Zaidi ya miaka 50 imepita sasa tangu nilipoanza kukumbwa na matatizo ya afya. Usomaji wa Biblia ungali unanifariji, hasa ninaposoma Zaburi na kitabu cha Ayubu. Nami hufurahia kusoma vichapo vya Watch Tower Society. Mimi pia hutiwa moyo sana wakati washiriki wa kutaniko letu na waangalizi wasafirio wanaponitembelea na kushiriki nami mambo yaliyoonwa yenye kuchangamsha. Zaidi ya hayo, simu iliyounganishwa kwenye Jumba la Ufalme huniwezesha kusikiliza mikutano, na hata mimi hupokea kanda za vidio za programu za mikusanyiko.
“Ninashukuru sana kwa kuwa nimebarikiwa kuwa na mke mwenye upendo. Kwa miaka mingi, amekuwa mwandamani wangu wa karibu. Pia, binti yetu, ambaye leo anamtumikia Yehova pamoja na familia yake mwenyewe, angali anatuletea shangwe sana. Namshukuru hasa Yehova kwa kunisaidia niwe karibu naye. Hivi leo, kadiri sauti yangu na mwili wangu unavyodhoofika zaidi na zaidi, mara nyingi mimi hufikiria maneno haya ya mtume Paulo: ‘Hatufi moyo, lakini hata ikiwa mtu tuliye kwa nje anachakaa, hakika mtu tuliye kwa ndani anafanywa upya siku kwa siku.’ (2 Wakorintho 4:16) Naam, kudumu nikiwa macho kiroho maadamu ninaishi—ungali mradi wangu.”
-