Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Ndevu za Yesu Katika mfululizo wenu “Yesu—Kwa Kweli Alifananaje? Yeye Ni Nani Sasa?” (Desemba 8, 1998), picha zenu zadokeza kwamba Yesu hakutii sheria iliyoandikwa kwenye Mambo ya Walawi 19:27: “Msinyoe denge pembe za vichwani, wala msiharibu pembe za ndevu zenu.” Kwa nini picha zenu hazimwonyeshi akiwa na denge zisizonyolewa?
C. S., Uingereza
Sheria hiyo kwa wazi ilitolewa ili kuzuia Wayahudi wasikate ndevu au nywele zao kwa mtindo ambao ungeiga tabia fulani za kipagani. Hata hivyo, sheria ya Mungu haikumaanisha kwamba Wayahudi hawangeweza kukata ndevu zao au nywele zao za usoni kamwe. Simulizi kwenye 2 Samweli 19:24 laonyesha kwamba wanaume Wayahudi kwa kawaida ‘walikata’ au kupunguza, nywele zao za usoni. Walifanya hivyo kutegemea desturi zilizokuwa za kawaida wakati huo. Uthibitisho wa kiakiolojia waonyesha kwamba Wayahudi walikuwa na mitindo tofauti-tofauti ya ndevu karne baada ya karne. Kwa hiyo uchoraji wetu wa Yesu akiwa na ndevu fupi, zilizokatwa vizuri na denge zilizopunguzwa zapatana na uthibitisho huo.—Mhariri.
Mgongano wa Sayari Ndogo Katika toleo la Januari 22, 1999, kulikuwa na makala yenye kichwa “Sayari Ndogo, Nyotamkia, na Dunia—Je, Ziko Katika Mwendo wa Kugongana?” Asanteni sana kwa makala hii. Ilitoa maelezo ya kusadikisha ya mambo yanayoweza kupata dunia. Kwa sababu ya Yehova, hakuna misiba imetokea. Nilithamini jinsi makala hiyo ilivyosema mambo moja kwa moja na kwa njia ya unyoofu.
O. R., Finland
Matatizo ya Kula Mliokoa maisha yangu kihalisi kwa mfululizo wa Januari 22, 1999, “Ni Nini Kinachosababisha Matatizo ya Kula?” Nilikuwa na tatizo baya sana kuhusu hilo miaka 20 iliyopita. Kisha kwa miaka kumi hivi iliyopita, nilidumisha uzito wa kawaida. Ingawa hivyo, hivi majuzi nilipatwa na mshuko wa moyo na kupoteza kilogramu 5 kwa siku 16. Nilikuwa nimeanza kukabwa kooni kila mara nilipoanza kula chakula. Nikahofia sana hali yangu ya baadaye. Makala hizo zilinisaidia nifikirie tena hali yangu na kunifanya niazimie kupata lishe bora. Nashukuru sana kwa moyo wangu wote kwa makala zenu zenye kujali na zenye upendo.
P. M., Marekani
Niliposoma makala hizi, nilibubujika machozi. Zilionekana kama kwamba ziliandikwa tu kwa ajili yangu. Zilinigusa moyo na kunisaidia kuelewa kwamba nikiendelea kumtegemea Yehova, nitapata nafuu kutokana na ugonjwa huu.
G. G., Puerto Riko
Nina umri wa miaka 14 na nataka kuwashukuru sana kwa makala zilizohusu matatizo ya kula. Tatizo la bulimia lilikuwa limenianza. Sikujua la kufanya, kwa kuwa hata vitabu vilivyoshughulika na tatizo hilo havikunisaidia. Wazazi wangu walitambua hali yangu na kuongea nami kuhusu makala hizo. Asanteni sana.
N. H., Ujerumani
Karibu mwaka moja na nusu uliopita, nilikuwa na tatizo la bulimia. Nilifikiri kwamba nilikuwa mnene, hata ingawa sikuwa mwenye uzani wa kupita kiasi kamwe. Nilijua kwamba ni vibaya kula kupita kiasi kisha kusafisha tumbo, lakini nilishindwa kuacha. Kwa msaada wa Yehova na kitia-moyo kutoka kwa marafiki wa karibu, nilipata nafuu. Makala hizo zimenisaidia sana. Naona kwamba si mimi peke yangu ambaye nimekuwa na matatizo hayo.
M. R., Uingereza
Nilijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova kwa miaka miwili lakini nikaacha kwa sababu ya mshuko wa moyo. Nina tatizo la bulimia. Kwa kuwa sikuzote natibiwa, nakusudia kuwapa madaktari na wagonjwa wenzangu gazeti hili. Natazamia kuanza kujifunza Biblia tena.
V. K., Jamhuri ya Cheki