-
Usitawi wa Muundo wa TengenezoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Yeye alijua sana kwamba mitume wa Kristo walikuwa wamefanyiza makutaniko na kuweka wazee katika kila moja. Lakini aliamini kwamba Kristo alikuwapo tena, ingawa ni kwa kutoonekana, na yeye binafsi alikuwa akitoa mwelekezo wa kuvunwa kwa mwisho kwa wale ambao wangekuwa warithi pamoja naye. Kwa sababu ya hali hizo, Ndugu Russell mwanzoni alihisi kwamba wakati wa pindi ya mavuno mpango wa wazee uliokuwa katika makutaniko ya Kikristo ya karne ya kwanza haukuhitajiwa.
Hata hivyo, kadiri Wanafunzi wa Biblia walivyoongezeka idadi, Ndugu Russell alipata kujua kwamba Bwana alikuwa akielekeza mambo kwa njia tofauti na ile ambayo yeye mwenyewe alikuwa ametarajia. Rekebisho katika maoni lilihitajiwa. Lakini kwa msingi gani?
Kutimiza Mahitaji ya Mapema ya Ushirika Wenye Kukua
Toleo la Watch Tower la Novemba 15, 1895, karibu lote lilizungumzia habari “Kwa Uzuri na kwa Utaratibu.” Kwa unyoofu, Ndugu Russell alikiri humo hivi: “Mitume walikuwa na mengi ya kusema kwa Kanisa la mapema kuhusu utaratibu katika makusanyiko ya watakatifu; na kwa wazi tumekuwa kidogo wenye kupuuza shauri hilo la hekima, tukihisi kidogo kuwa la umaana mdogo, kwa sababu Kanisa liko karibu sana na mwisho wa mwendo walo na mavuno ni wakati wa kutenganisha.” Ni kitu gani kilichowasukuma kulifikiria tena shauri hilo?
Makala hiyo iliorodhesha hali nne: (1) Ilikuwa wazi kwamba ukuzi wa kiroho wa watu mmoja-mmoja ulitofautiana na ule wa mwingine. Kulikuwa vishawishi, majaribu, magumu, na hatari ambazo wote hawakuwa tayari kwa kiwango kilekile kuyakabili. Hivyo, kulikuwa uhitaji wa waangalizi wenye hekima na wenye busara, wanaume wenye uzoefu na uwezo, wenye kupendezwa sana na kutunza masilahi ya kiroho ya wote na wenye uwezo wa kuwafundisha katika kweli. (2) Ilikuwa imeonwa kwamba kundi lilihitaji kulindwa na ‘mbwa-mwitu wenye kuvaa mavazi ya kondoo.’ (Mt. 7:15, KJ) Walihitaji kuimarishwa kwa kusaidiwa wapate maarifa kamili ya kweli. (3) Mambo yaliyoonwa yalikuwa yameonyesha kwamba kusipokuwa na mpango wa kuweka wazee kulinda kundi, wengine wangechukua cheo hicho waje kuona kundi kuwa lao wenyewe. (4) Bila mpango wenye utaratibu, watu mmoja-mmoja wenye uaminifu-mshikamanifu kuelekea kweli huenda wakaona utumishi wao mbalimbali kuwa usiotakwa kwa sababu ya uvutano wa wachache wasiokubaliana nao.
Kwa kufikiria hayo, Watch Tower lilitaarifu hivi: “Hatusiti kupendekeza kwa Makanisac kila mahali, iwe idadi yao ni kubwa au ndogo, shauri hilo la Kimitume, kwamba, katika kila kampuni, wazee wachaguliwe kutoka miongoni mwa idadi yao ‘kulisha’ na ‘kuangalia’ kundi.” (Mdo. 14:21-23; 20:17, 28) Makutaniko ya mahali yalifuata shauri hilo timamu la Kimaandiko. Hiyo ilikuwa hatua ya maana katika kuanzisha muundo wa kutaniko kupatana na yale yaliyokuwako katika siku za mitume.
Hata hivyo, kulingana na njia waliyoelewa mambo wakati ule, kuteuliwa kwa wazee, na mashemasi ili kuwasaidia, kulifanywa kwa kura ya kutaniko. Kila mwaka, au mara nyingi zaidi ikihitajiwa, sifa za wale wawezao kutumikia zilifikiriwa, na kura ikapigwa. Kwa msingi ulikuwa utaratibu wa kidemokrasi, lakini ambao ulibanwa na mipaka iliyokusudiwa kutenda kuwa ulinzi salama. Wote katika kutaniko walihimizwa wapitie kwa uangalifu sifa za Kibiblia na kuonyesha kwa kura, si maoni yao wenyewe, bali yale ambayo waliamini kuwa mapenzi ya Bwana. Kwa kuwa ni wale tu “waliojitakasa kabisa” waliokuwa na haki ya kupiga kura, kura yao ya umoja, ikiongozwa na Neno na roho ya Bwana, ilionwa kuwa yaonyesha mapenzi ya Bwana katika jambo hilo. Ijapokuwa huenda ikawa Ndugu Russell hakujua kabisa, pendekezo lake la mpango huo labda lilivutwa kwa kadiri fulani na azimio lake la kuepuka mfano wowote wa jamii ya makasisi iliyokwezwa na pia malezi yake mwenyewe akiwa tineja katika Congregational Church.
Buku la Millennial Dawn liitwalo The New Creation (lililotangazwa katika 1904) lilipozungumza tena kirefu juu ya fungu la wazee na njia ambayo walipaswa kuteuliwa, uangalifu wa pekee ulielekezwa kwenye Matendo 14:23. Konkodansi zilizotungwa na James Strong na Robert Young zilitajwa kuwa mamlaka kwa maoni ya kwamba ile taarifa “walikuwa wamewaweka rasmi kuwa wazee” (KJ) yapasa kutafsiriwa “walikuwa wamewateua kuwa wazee kwa wonyesho wa mikono.”d Baadhi ya tafsiri za Biblia hata husema kwamba wazee ‘waliwekwa kwa kura.’ (Literal Translation of the Holy Bible ya Young; Emphasised Bible ya Rotherham) Lakini ni nani aliyepaswa kupiga kura hiyo?
Kuchukua maoni ya kwamba kupiga kura kulipasa kufanywe na kutaniko lote hakukuleta matokeo yaliyotumainiwa sikuzote. Wale waliopiga kura walipaswa kuwa watu “waliojitakasa kabisa,” na baadhi ya wale waliochaguliwa walitimiza kikweli sifa za Kimaandiko nao walitumikia ndugu zao kwa unyenyekevu. Lakini kupiga kura mara nyingi kulionyesha upendeleo wa kibinafsi badala ya Neno na roho ya Mungu. Hivyo, katika Halle, Ujerumani, wakati wengine waliofikiri kwamba walipaswa kuwa wazee hawakupata vyeo walivyotaka, walisababisha migawanyiko mibaya. Katika Barmen, Ujerumani, miongoni mwa wale waliokuwa wachaguliwa katika 1927 mlikuwa wanaume waliopinga kazi ya Sosaiti, na kelele nyingi ilipigwa wakati wa kuonyesha mikono kwenye uchaguzi. Hivyo ilikuwa lazima kugeukia njia ya kupiga kura kwa siri.
Huko nyuma katika 1916, miaka mingi kabla ya visa hivyo, Ndugu Russell, akiwa na hangaiko kubwa, alikuwa ameandika: “Hali mbaya sana ya mambo huwa katika Madarasa fulani wakati wa kufanywa uchaguzi. Watumishi wa Kanisa hujaribu kuwa watawala, madikteta—nyakati nyingine hata wakishika uenyekiti wa mkutano yaonekana kwa lengo la kuona kwamba wao na marafiki wao wa pekee watachaguliwa kuwa Wazee na Mashemasi. . . . Baadhi yao hujaribu kutumia Darasa kwa faida yao kwa siri kwa kuwa na uchaguzi wakati fulani unaowafaa hasa wao na marafiki wao. Wengine hutafuta kujaza mkutano marafiki wao, wakileta watu walio wageni, ambao hawana wazo la kuhudhuria kwa ukawaida kwenye Darasa, bali huja tu kwa sababu ya urafiki ili kupigia kura mmoja wa marafiki wao.”
-
-
Usitawi wa Muundo wa TengenezoMashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 207]
Kwa Nini Badiliko?
Alipoulizwa swali juu ya badiliko lake la maoni kuhusu kuteuliwa kwa wazee katika vile vikundi mbalimbali vya watu wa Bwana, C. T. Russell alijibu hivi:
“Kwanza kabisa nafanya haraka kuwahakikishia kwamba mimi sijadai kamwe kuwa asiyeweza kufanya kosa. . . . Sisi hatukani kukua katika ujuzi, na kwamba twaona sasa kwa nuru iliyo tofauti kidogo mapenzi ya Bwana kwa habari ya Wazee au viongozi katika vile vikundi vidogo mbalimbali vya watu wake. Kosa letu katika uamuzi lilikuwa katika kutazamia mengi mno kutoka kwa ndugu zetu wapendwa ambao, wakija mapema katika Kweli, walipata kiasili kuwa viongozi wa makampuni haya madogo. Maoni ya kuwaziawazia tuliyokuwa nayo kuwahusu yalikuwa, kwamba ujuzi juu ya Kweli ungekuwa na matokeo ya kuwanyenyekeza sana, ukiwafanya wafahamu hali yao ya kutokuwa wa maana, na kwamba lolote walilojua na waliloweza kutolea wengine lilikuwa wakiwa vinywa vya Mungu na kwa sababu watumiwa naye. Matumaini yetu ya kuwaziawazia yalikuwa kwamba hao wangekuwa katika kila maana ya hilo neno vielelezo kwa kundi; na kwamba mwelekezo wa Bwana ukileta katika kampuni dogo mmoja au zaidi wenye uhodari wa kadiri hiyohiyo, au hodari zaidi, wa kuitoa Kweli, kwamba roho ya upendo ingewaongoza kustahiana kwa heshima mmoja na mwenzake, na hivyo kusaidiana na kuhimizana mmoja na mwenzake kushiriki katika utumishi wa Kanisa, mwili wa Kristo.
“Tukiwa na wazo hilo akilini tulikata kauli kwamba vile vipimo vikubwa vya neema na kweli vilivyopo sasa na vinavyothaminiwa na watu wa Bwana waliojitakasa vingefanya isihitajiwe kwao kufuata mwendo ulioonyeshwa na mitume katika Kanisa la mapema. Kosa letu lilikuwa kushindwa kujua kwamba mipango iliyoonyeshwa na mitume chini ya usimamizi wa kimungu ni bora kuliko chochote ambacho wengine wangeweza kutunga, na kwamba Kanisa kwa ujumla litahitaji kuwa na kanuni hizo zilizoanzishwa na mitume mpaka sisi sote tuwe tumefanywa watimilifu na wakamilifu kwa kubadilishwa kwetu katika ufufuo, tuwe na ushirika wa moja kwa moja na Bwana-Mkubwa.
“Kosa letu tulilifahamu hatua kwa hatua tulipoona miongoni mwa ndugu wapendwa kadiri fulani ya roho ya ushindani, na kwa upande wa wengi tamaa ya kushika uongozi wa mikutano kuwa cheo badala ya kuwa utumishi, na kutohusisha na kuzuia ndugu wengine wasisitawi wakiwa viongozi wenye uwezo uleule kiasili na wenye ujuzi uleule juu ya Kweli na uhodari katika kutumia upanga wa Roho.”—“Zion’s Watch Tower,” Machi 15, 1906, uku. 90.
-