Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je! Ni Kawaida Kuhisi Hivi?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • Je! Ni Kawaida Kuhisi Hivi?

      MTU fulani aliyefiwa aandika hivi: “Nilipokuwa mtoto katika Uingereza, nilifunzwa nisionyeshe hisia zangu hadharani. Naweza kukumbuka babangu, aliyekuwa mwanajeshi hapo awali, akiniambia hivi akiwa ameyakaza sana meno yake kwa ukali, ‘Usilie!’ wakati jambo fulani lilipokuwa limeniumiza. Siwezi kukumbuka kama mamangu alipata wakati wowote kubusu au kukumbatia yeyote kati ya sisi watoto (tulikuwa wanne). Nilikuwa na miaka 56 nilipomwona babangu akifa. Nilihisi nimepatwa na hasara kubwa mno. Hata hivyo, mwanzoni, sikuweza kutoa machozi.”

      Katika tamaduni fulani-fulani, watu huonyesha hisia zao waziwazi. Iwe wana furaha au huzuni, wengine wanajua jinsi wanavyohisi. Kwa upande mwingine, katika sehemu nyinginezo za ulimwengu, hasa katika kaskazini mwa Ulaya na Uingereza, watu, hasa wanaume, wamezoezwa kuficha hisia zao, kuzuia hisiamoyo zao, kubaki watulivu bila kuonyesha hisia zao waziwazi. Lakini wakati umefiwa na mpendwa, je, ni vibaya kwa njia fulani kuonyesha huzuni yako? Biblia husema nini?

      Wale Katika Biblia Waliotoa Machozi

      Biblia iliandikwa na Waebrania wa mkoa wa mashariki mwa Mediterania, waliokuwa watu walioonyesha hisia zao waziwazi. Hutoa vielelezo vingi vya watu mmoja-mmoja walioonyesha huzuni yao waziwazi. Mfalme Daudi aliomboleza kifo cha mwana wake Amnoni aliyeuawa kimakusudi. Kwa kweli, alitoa machozi kwa “kilio kikubwa mno.” (2 Samweli 13:28-39) Yeye hata alihuzunika alipofiwa na mwana wake mwenye hila Absalomu, aliyekuwa amejaribu kutwaa utawala kwa nguvu. Simulizi la Biblia latuambia hivi: “Naye mfalme [Daudi] akataabika sana, akapanda juu, akaingia kile chumba kilichokuwa juu ya lango, akalia; na katika kwenda kwake alisema hivi, Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! mwanangu Absalomu! laiti ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu, mwanangu!” (2 Samweli 18:33) Daudi aliomboleza sawa na baba yeyote wa kawaida. Na ni mara nyingi jinsi gani wazazi wametamani wangalikufa badala ya watoto wao! Laonekana kutokuwa jambo la asili hata kidogo kwa mtoto kufa kabla ya mzazi.

      Yesu aliitikiaje kifo cha rafiki yake Lazaro? Yeye alitoa machozi alipokaribia kaburi lake. (Yohana 11:30-38) Baadaye, Maria Magdalene alitoa machozi alipokaribia kaburi la Yesu. (Yohana 20:11-16) Ni kweli, Mkristo mwenye uelewevu wa tumaini la ufufuo la Biblia hahuzuniki bila kufarijika, kama vile wengine hufanya ambao imani zao kuhusu hali ya wafu hazina msingi wa Biblia ulio dhahiri. Lakini akiwa binadamu mwenye hisia za kawaida, Mkristo wa kweli, hata aliye na tumaini la ufufuo, huhuzunikia na kuombolezea kifo cha mpendwa yeyote.—1 Wathesalonike 4:13, 14.

      Kutoa Machozi au Kutotoa Machozi

      Namna gani maitikio yetu leo? Je! wewe waona kwamba kuonyesha hisia zako ni jambo gumu au linaloaibisha? Washauri hupendekeza nini? Mara nyingi maoni yao ya kisasa hurudia tu ile hekima ya kale ya Biblia iliyopuliziwa. Wao husema kwamba twapaswa kuonyesha huzuni yetu, si kuizuia. Hili latukumbusha wanaume waaminifu wa kale, kama vile Ayubu, Daudi, na Yeremia, ambao maneno yao ya huzuni yanapatikana katika Biblia. Kwa hakika hawakuzizuia hisia zao. Kwa hiyo, si jambo la hekima kujitenga na watu. (Mithali 18:1) Bila shaka, kuomboleza kunaonyeshwa kwa njia tofauti-tofauti katika tamaduni tofauti-tofauti, pia kunategemea imani za kidini zilizoenea.a

      Namna gani ikiwa wahisi kutaka kutoa machozi? Kutoa machozi ni sehemu ya asili ya binadamu. Kumbuka tena ile pindi ya kifo cha Lazaro, wakati Yesu ‘alipopiga kite katika roho na kutokwa na machozi.’ (Yohana 11:33, 35, NW) Hivyo akaonyesha kwamba kutoa machozi ni itikio la kawaida kwa kifo cha mpendwa.

      Hili laungwa mkono na kisa cha mama fulani, Anne, aliyekuwa amefiwa na mtoto wake mchanga Rachel kutokana na SIDS (Ugonjwa wa Kifo cha Ghafula cha Kitoto). Mume wake alieleza hivi: “Jambo la kushangaza ni kwamba wala Anne wala mimi hatukulia kwenye maziko. Wengine wote walikuwa wakitoa machozi.” Anne aliitikia hilo hivi: “Ndiyo, lakini nimelia vya kutosha sana kwa ajili ya sote wawili. Nafikiri niliathiriwa kwelikweli majuma machache baada ya msiba huo, siku moja nilipokuwa peke yangu nyumbani hatimaye. Nililia siku nzima. Lakini naamini hilo lilinisaidia. Nilisikia nafuu kwa kufanya hivyo. Nililazimika kuomboleza kifo cha mtoto wangu mchanga. Naamimi kwelikweli kwamba wapaswa kuacha watu wanaohuzunika watoe machozi. Ingawa ni itikio la asili kwa wengine kusema, ‘Usilie,’ kwa kweli hilo halisaidii.”

      Jinsi Wengine Huitikia

      Wengine wameitikiaje wanapohuzunishwa na kifo cha mpendwa? Kwa kielelezo, fikiria Juanita. Yeye ajua zinavyokuwa hisia wakati wa kufiwa na mtoto mchanga. Yeye alikuwa ameharibikiwa mimba mara tano. Sasa akawa mjamzito tena. Basi wakati aksidenti ya gari ilipomlazimisha alazwe hospitalini, ni wazi yeye alikuwa na wasiwasi. Majuma mawili baadaye alipatwa na utungu wa kuzaa—kabla ya wakati wake. Muda mfupi baadaye Vanessa mdogo akazaliwa—mwenye uzani zaidi kidogo ya gramu mia tisa. “Nilisisimuka sana,” Juanita akumbuka. “Hatimaye nikawa mama!”

      Lakini furaha yake ilikuwa ya muda mfupi tu. Siku nne baadaye Vanessa alikufa. Juanita akumbuka hivi: “Nilihisi utupu sana. Nilitwaliwa hali yangu ya kuwa mama. Nilihisi kutokuwa kamili. Iliumiza sana kuja nyumbani kwenye chumba tulichokuwa tumemtayarishia Vanessa na kuona zile shati ndogo za kuvaliwa ndani nilizokuwa nimemnunulia. Kwa miezi kadhaa iliyofuata, nilikumbuka upya ile siku ya kuzaliwa kwake. Sikutaka kushirikiana na yeyote yule.”

      Je! hilo ni itikio la kupita kiasi? Huenda ikawa vigumu kwa wengine kuelewa, lakini wale ambao, kama vile Juanita, wamepitia hali hiyo wanaeleza kwamba walihuzunikia mtoto wao mchanga sawa na vile ambavyo wangehuzunikia mtu fulani aliyekuwa ameishi kwa muda fulani. Wanasema kwamba, muda mrefu kabla ya mtoto kuzaliwa, huyo huwa anapendwa na wazazi wake. Kuna kifungo cha pekee pamoja na mama. Mtoto huyo mchanga anapokufa, mama huhisi kwamba mtu halisi amekufa. Na hilo ndilo jambo ambalo wengine wanahitaji kuelewa.

      Jinsi Kasirani na Kuhisi Una Hatia Kwaweza Kukuathiri

      Mama mwingine alionyesha hisia zake alipoambiwa kwamba mwana wake wa miaka sita alikuwa amekufa ghafula kwa sababu ya tatizo la moyo alilozaliwa nalo. “Nilipatwa na mfululizo wa maitikio—ganzi, kutoamini, kuhisi una hatia, na kasirani kuelekea mume wangu na daktari kwa ajili ya kutong’amua jinsi hali yake ilivyokuwa mbaya sana.”

      Kasirani yaweza kuwa dalili nyingine ya huzuni. Huenda ikawa ni kasirani kuelekea madaktari na wauguzi, ukihisi kwamba wangalipaswa kufanya zaidi ili wamshughulikie yule mfu. Au huenda ikawa ni kasirani kuelekea marafiki na watu wa ukoo ambao, yaonekana, wanasema au kufanya jambo lisilofaa. Wengine humkasirikia yule mfu kwa sababu ya kupuuza afya yake. Stella akumbuka hivi: “Nakumbuka nikiwa nimemkasirikia mume wangu kwa sababu nilijua hali ingalikuwa tofauti. Yeye alikuwa amekuwa mgonjwa sana, lakini alikuwa amepuuza maonyo ya madaktari.” Na nyakati nyingine kuna kasirani kuelekea yule mfu kwa sababu ya mizigo yenye kulemea ambayo kifo chake chamletea yule anayebaki.

      Wengine wanahisi wana hatia kwa sababu ya kuwa na kasirani—yaani, huenda wakajilaumu kwa sababu wanahisi kasirani. Wengine wanajilaumu kwa ajili ya kifo cha mpendwa wao. “Yeye asingalikufa,” wao wanajisadikisha, “laiti tu ningalimfanya aende kwa daktari mapema zaidi” au “ningalimfanya amwone daktari mwingine” au “ningalimfanya atunze afya yake vema zaidi.”

      Kwa wengine kuhisi wana hatia kunafikia hatua nyingine zaidi, hasa ikiwa mpendwa wao alikufa ghafula, bila kutazamiwa. Wanaanza kukumbuka nyakati walizokuwa wamemkasirikia yule mfu au walikuwa wamebishana naye. Au huenda wakahisi kwamba kwa kweli hawakuwa kabisa vile wangalipaswa kuwa kuelekea yule mfu.

      Ile kawaida ya kuhuzunika kwa muda mrefu ya akina mama wengi huunga mkono yale ambayo wastadi wengi husema, kwamba kifo cha mtoto huacha pengo la daima maishani mwa wazazi, hasa mama.

      Unapofiwa na Mwenzi wa Ndoa

      Kufiwa na mwenzi wa ndoa ni aina nyingine ya umivu kali la kimoyoni, hasa ikiwa wote wawili waliishi maisha yenye utendaji mwingi wakiwa pamoja. Hilo laweza kumaanisha mwisho wa mtindo-maisha mzima walioshiriki pamoja, mwisho wa kusafiri, wa kufanya kazi, wa kuwa na vitumbuizo, na wa kutegemeana.

      Eunice aeleza yale yaliyotendeka wakati mume wake alipokufa ghafula kutokana na ugonjwa wa moyo. “Kwa juma la kwanza, nilikuwa katika hali ya kutohisi lolote kihisiamoyo, kana kwamba mwili wangu haukuwa ukifanya kazi tena. Hata sikuweza kuonja wala kunusa. Hata hivyo, hisi yangu ya kufikiri vizuri iliendelea ikiwa imejitenga. Kwa sababu nilikuwa nimekuwa na mume wangu walipokuwa wakijaribu kusawazisha hali yake kwa kutumia CPR (utaratibu wa kumhuisha mtu ili aanze kupumua kikawaida) pamoja na madawa, sikupatwa na zile dalili za kawaida za kukana. Hata hivyo, nilihisi kukata tamaa sana, kana kwamba nilikuwa nikitazama gari likianguka kutoka gengeni (mteremko wa ghafula) nami singeweza kufanya lolote juu yalo.”

      Je! alitoa machozi? “Bila shaka nilifanya hivyo, hasa niliposoma yale mamia ya kadi za kusikitikia nilizokuwa nimepokea. Nililia kwa kila moja. Hilo lilinisaidia kujiweza hadi sehemu iliyobaki ya siku. Lakini hakuna chochote ambacho kingeweza kusaidia nilipoulizwa mara kwa mara jinsi nilivyohisi. Bila shaka, nilikuwa katika hali ya kuhuzunika sana.”

      Ni nini kilichomsaidia Eunice avumilie huzuni yake? “Bila kung’amua, niliamua kuendelea na maisha yangu bila kujua,” yeye asema. “Hata hivyo, jambo liniumizalo bado ni wakati nikumbukapo kwamba mume wangu, aliyependa uhai sana, hayupo hapa kuufurahia.”

      “Usiruhusu Wengine Wakuamulie . . . ”

      Watunga-vitabu wa Leavetaking—When and How to Say Goodbye washauri hivi: “Usiruhusu wengine wakuamulie jinsi upaswavyo kutenda au kuhisi. Kawaida ya kuhuzunika huwa tofauti kwa kila mtu. Huenda wengine wakafikiri—na wakakujulisha kwamba wao wanafikiri—una huzuni nyingi mno au huna huzuni ya kutosha. Wasamehe na usahau hilo. Kwa kujaribu kujilazimisha kuwa jinsi wengine watakavyo au jamii ya watu kwa ujumla itakavyo, unazuia ukuzi wako wa kurudia afya nzuri ya kihisiamoyo.”

      Bila shaka, watu tofauti hushughulikia huzuni yao kwa njia tofauti-tofauti. Sisi hatujaribu kudokeza kwamba njia moja kwa lazima ndiyo iliyo bora zaidi ya nyingine kwa kila mtu. Hata hivyo, hatari hutokea wakati mtu aliye na huzuni akwamapo katika hali fulani, wakati hawezi kujipatanisha na uhalisi wa hali. Hapo ndipo huenda msaada ukahitajika kutoka kwa marafiki wenye huruma. Biblia husema: “Rafiki [“wa kweli,” NW] hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Kwa hiyo usiogope kutafuta msaada, kuongea, na kutoa machozi.—Mithali 17:17.

      Huzuni ni itikio la kawaida la kufiwa, na si vibaya huzuni yako kuonekana waziwazi kwa wengine. Lakini maswali mengine yahitaji majibu: ‘Naweza kuishije nikiwa na huzuni yangu? Je! ni kawaida kupatwa na hisia za kuwa na hatia na kasirani? Napaswa kushughulikaje kwa kufaa na maitikio hayo? Ni nini kiwezacho kunisaidia nivumilie kifo na huzuni hii?’ Sehemu ifuatayo itajibu maswali hayo na mengine.

  • Je! Ni Kawaida Kuhisi Hivi?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • Kawaida ya Kuhuzunika

      Neno “kawaida” halidokezi kwamba huzuni ina ratiba au programu yoyote iliyo imara. Maitikio ya huzuni yaweza kupitana na kuchukua urefu mbalimbali wa wakati, ikitegemea mtu mmoja-mmoja. Orodha hii si kamili. Maitikio mengine yaweza kudhihirishwa pia. Zifuatazo ni baadhi ya dalili za huzuni ambazo huenda mtu akapatwa nazo.

      Maitikio ya mapema: Mshtuko wa kwanza; kutoamini, kukana; ganzi ya kihisiamoyo; hisia za kuwa na hatia; kasirani.

      Huzuni nyingi sana yaweza kutia ndani: Kusahau-sahau na kutoweza kulala usingizi; uchovu wa kupita kiasi; mabadiliko ya ghafula ya hali ya moyoni; kuamua na kufikiri kwa njia isiyofaa; vipindi vya kulia-lia; mabadiliko katika hamu ya kula chakula, kukiwa na matokeo ya kupoteza uzani na kuongeza uzani; ishara mbalimbali za afya iliyoathiriwa; kusinzia-sinzia isivyo kawaida; uwezo uliopungua wa kufanya kazi; kuona-ona njozi—kuhisi, kusikia, kumwona yule mfu; katika hali ya kufiwa na mtoto, kuchukizwa na mwenzi wako wa ndoa bila sababu nzuri.

      Kipindi cha kupata usawaziko: Huzuni pamoja na kukumbuka kwa kutamani sana wakati uliopita; kukumbuka mambo yenye kupendeza zaidi juu ya yule mfu, hata kutia ndani yale yenye kuchekesha.

  • Je! Ni Kawaida Kuhisi Hivi?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • Kuharibikiwa Mimba na Kuzaa Mtoto Mfu—Huzuni ya Mama

      Ingawa alikuwa na watoto wengine tayari, Monna alikuwa akitazamia kwa hamu kuzaliwa kwa mtoto wake mwingine. Hata kabla ya yeye kuzaliwa, alikuwa mtoto mchanga “aliyecheza naye, kuongea naye, na kuotea ndoto.”

      Ile kawaida ya kupata kifungo kati ya mama na mtoto asiyezaliwa ilikuwa yenye nguvu. Yeye aendelea hivi: “Rachel Anne alikuwa mtoto mchanga aliyepiga teke vitabu kutoka tumboni pangu [akiwa bado hajazaliwa], alifanya nikose usingizi usiku. Ningali naweza kukumbuka yale mateke madogo ya kwanza, kama vile midukuo ya upendo, yenye uanana. Kila wakati aliposonga, nilijawa na upendo mwingi. Nilimjua vizuri sana hivi kwamba nilijua alipokuwa akiumwa, alipokuwa mgonjwa.”

      Monna aendelea na simulizi lake hivi: “Daktari hakuniamini mpaka kulipokuwa kumechelewa mno. Aliniambia niache kuwa na wasiwasi. Naamini nilihisi alipokufa. Yeye aligeuka tu ghafula na kwa nguvu. Siku iliyofuata alikuwa amekufa.”

      Ono la Monna si tukio lisilo la kawaida. Kulingana na watunga-vitabu Friedman na Gradstein, katika kitabu chao Surviving Pregnancy Loss, karibu wanawake milioni moja kwa mwaka katika Marekani pekee huharibikiwa mimba. Bila shaka, hesabu ya ulimwenguni pote ni wengi zaidi.

      Mara nyingi watu hukosa kung’amua kwamba kuharibikiwa mimba au kuzaa mtoto mfu ni msiba kwa mwanamke na ni mmoja akumbukao—labda muda wote wa maisha yake. Kwa kielelezo, Veronica, ambaye amezeeka sasa, akumbuka kuharibikiwa kwake mimba mara kadhaa na hasa akumbuka yule mtoto mchanga mfu aliyemzaa, aliyekuwa hai hadi mwezi wa tisa na kuzaliwa akiwa na uzani wa kilo sita. Alimbeba akiwa amekufa ndani yake kwa yale majuma mawili ya mwisho. Alisema hivi: “Kumzaa mtoto mfu ni jambo mbaya sana kwa mama.”

      Maitikio ya akina mama hawa waliokata tamaa hayaeleweki sikuzote, hata na wanawake wengine. Mwanamke fulani aliyekuwa amepoteza mtoto wake kupitia mimba iliyoharibika aliandika hivi: “Yale ambayo nimejifunza kwa njia yenye maumivu sana ni kwamba kabla ya hilo kunipata, kwa kweli sikuwa na wazo lolote kuhusu yale ambayo marafiki zangu walilazimika kuvumilia. Sikugusika moyo upesi wala kuelewa vema hali yao kama vile nionavyo kwamba watu hawagusiki moyo wala kuelewa vema hali yangu.”

      Tatizo jingine kwa mama anayehuzunika ni kuona kwamba mume wake hahisi jinsi yeye anavyohisi juu ya hasara hiyo. Mke mmoja alieleza jambo hilo hivi: “Nilikatishwa tamaa kabisa na mume wangu wakati huo. Kulingana na maoni yake, kwa kweli hakukuwa na mimba yoyote. Hakuweza kuhisi ile huzuni niliyokuwa nikihisi. Alikuwa mwenye kusikitikia sana hofu zangu lakini si mwenye kusikitikia huzuni yangu.”

      Labda itikio hilo ni la asili kwa mume—yeye hawi na kifungo kilekile cha kimwili na cha kihisiamoyo (pamoja na kijusi) kama vile mke wake mjamzito huwa nacho. Hata hivyo, anahisi hasara fulani. Na ni muhimu kwamba mume na mke wang’amue kwamba wanateseka pamoja, ingawa ni kwa njia tofauti-tofauti. Wao wapaswa washiriki huzuni yao pamoja. Mume akificha huzuni yake, huenda mke wake akafikiri kwamba yeye hakugusika moyo upesi na hali hiyo. Kwa hiyo shirikini pamoja machozi, mawazo, na makumbatio yenu. Onyesheni kwamba mnahitajiana zaidi ya wakati mwingine wowote. Ndiyo, waume, onyesheni hisia-mwenzi yenu.

  • Je! Ni Kawaida Kuhisi Hivi?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • Ugonjwa wa Kifo cha Ghafula cha Kitoto—Kukabili Hiyo Huzuni

      Kifo cha ghafula cha mtoto mchanga ni msiba wenye kufadhaisha. Siku moja mtoto mchanga aonekanaye kuwa wa kawaida, mwenye afya nzuri ashindwa kuamka. Hilo halitazamiwi hata kidogo, kwani ni nani awaziaye kwamba kitoto au mtoto yeyote atakufa kabla ya wazazi wake? Mtoto mchanga ambaye amekuja kupendwa sana na mamake kwa ghafula awa chanzo cha huzuni kubwa.

      Hisia za kuwa na hatia zaanza kuja kwa wingi. Huenda wazazi wakahisi wao ndio wa kulaumiwa kwa ajili ya kifo hicho, kana kwamba kilisababishwa na uzembe fulani. Wanajiuliza, ‘Tungaliweza kufanya nini ili kukizuia?’b Katika hali nyingine, huenda mume, bila msingi wowote, akamlaumu mke wake bila kujua. Alipoenda kazini, yule mtoto mchanga alikuwa hai na mwenye afya nzuri. Alipofika nyumbani, mtoto huyo mchanga alikuwa amekufa kitandani mwake! Mke wake alikuwa akifanya nini? Yeye alikuwa wapi wakati huo? Ni lazima maswali hayo yenye kusumbua yajibiwe ili yasisababishe mkazo juu ya ndoa.

      Hali zisizotazamiwa na zisizoweza kuonwa kimbele zilisababisha msiba huo. Biblia husema: “Nikarudi, na kuona chini ya jua, ya kwamba si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” NW] huwapata wote.”—Mhubiri 9:11.

      Wengine wanaweza kusaidiaje wakati familia inapofiwa na mtoto mchanga? Mama mmoja aliyefiwa aliitikia hivi: “Rafiki mmoja alikuja akaisafisha nyumba bila mimi kusema neno lolote. Wengine walitupikia chakula. Baadhi yao walisaidia kwa kunikumbatia tu—bila kusema maneno yoyote, kumbatio tu. Sikutaka kuongea juu yalo. Sikutaka kueleza tena na tena juu ya kile kilichotendeka. Sikuhitaji maswali ya kupeleleza, kana kwamba nilikuwa nimekosa kufanya jambo fulani. Nilikuwa ndiye mama [yake]; ningalifanya jambo lolote lile kumwokoa mtoto wangu mchanga.”

  • Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?

      “NILIHISI kusongwa sana nizuie hisia zangu,” aeleza Mike alipokumbuka kifo cha baba yake. Kwa Mike, kuzuia huzuni yake lilikuwa jambo la kiume kufanya. Hata hivyo baadaye aling’amua kwamba alikuwa amekosea. Kwa hiyo rafikiye Mike alipofiwa na babu yake, Mike alijua jambo la kufanya. Yeye asema hivi: “Miaka michache iliyopita, ningalimpigapiga begani na kusema ‘Uwe mwanamume.’ Sasa niligusa mkono wake na kusema, ‘Hisi vile utakavyo kuhisi. Hilo litakusaidia ushughulike vya kufaa na hali hii. Ikiwa wataka niende, nitaenda. Ikiwa wataka nikae, nitakaa. Lakini usiogope kuhisi.’”

      MaryAnne pia alihisi kusongwa azuie hisia zake wakati mume wake alipokufa. “Nilihangaikia sana kuwekea wengine kielelezo chema,” yeye akumbuka, “hivi kwamba sikujiruhusu nionyeshe hisia za kawaida. Lakini hatimaye nilijifunza kwamba kujaribu kuwa nguzo ya imara kwa ajili ya wengine hakukuwa kunanisaidia. Nilianza kuchanganua hali yangu na kusema, ‘Lia ikiwa ni lazima ulie. Usijaribu kuwa imara mno. Onyesha hisia zako zote kabisa.’”

      Kwa hiyo Mike na pia MaryAnne wanapendekeza hivi: Jiruhusu uhuzunike! Nao wasema kweli. Kwa nini? Kwa sababu kuhuzunika ni ondoleo la kihisiamoyo linalohitajika. Kuondosha hisia zako kwaweza kutuliza ule msongo unaokabili. Wonyesho wa asili wa hisiamoyo, pamoja na uelewevu na habari sahihi, unakuruhusu uzionyeshe hisia zako ifaavyo.

      Bila shaka, si kila mtu aonyeshaye huzuni kwa njia ileile. Na mambo kama ya kwamba mpendwa alikufa ghafula au kwamba kifo kilikuja baada ya ugonjwa wa muda mrefu huenda yakaathiri itikio la kihisiamoyo la wale wanaobaki. Lakini kuna jambo moja lionekanalo kuwa hakika: Kuzuia hisia zako kwaweza kukudhuru kimwili na kihisiamoyo pia. Ni bora zaidi kwa afya ukiondosha huzuni yako. Jinsi gani? Maandiko yana shauri lenye kutumika.

      Kuondosha Huzuni—Jinsi Gani?

      Kuongea kwaweza kuwa njia yenye kusaidia kuondosha huzuni. Baada ya kifo cha watoto wake wote kumi, pamoja na misiba mingine ya kibinafsi, Ayubu yule mzee wa ukoo wa kale alisema hivi: “Hakika nafsi yangu yahisi kukirihi kuelekea maisha yangu. Nitatoa [Kiebrania, “nitaachilia”] hangaiko langu kuhusu mwenyewe. Nitasema katika uchungu wa nafsi yangu!” (Ayubu 1:2, 18, 19; 10:1, NW) Ayubu hakuweza tena kuzuia hangaiko lake. Alilazimika kuliachilia; alihitaji ‘kunena.’ Vivyo hivyo, mtunga-drama Mwingereza Shakespeare aliandika hivi katika drama iitwayo Macbeth: “Onyesha majonzi; huzuni isiyosema manong’ono hulemea moyo nayo huupasua.”

      Kwa hiyo kuongea juu ya hisia zako pamoja na “rafiki wa kweli” atakayesikiliza kwa saburi na kwa kusikitikia kwaweza kuleta kadiri fulani ya kitulizo. (Mithali 17:17, NW) Mara nyingi kueleza maono na hisia hufanya iwe rahisi zaidi kuzielewa na kushughulika nazo kwa kufaa. Na ikiwa msikilizaji ni mtu mwingine aliyefiwa ambaye ameshughulika vya kufaa na hasara yake mwenyewe kwa mafanikio, huenda ukapata madokezo yenye kutumika juu ya jinsi ya kushughulika vya kufaa na hali yako. Mtoto wake alipokufa, mama mmoja alieleza kwa nini ilisaidia kuongea na mwanamke mwingine aliyekuwa amepatwa na hasara hiyohiyo: “Kujua kwamba mtu mwingine alikuwa amepatwa na jambo lilo hilo, alikuwa angali na afya nzuri ya kiakili na ya kihisiamoyo, na kwamba alikuwa angali anaendelea kuishi na kuwa na utaratibu fulani maishani mwake tena kuliniimarisha sana.”

      Namna gani ikiwa huhisi starehe kuongea juu ya hisia zako? Baada ya kifo cha Sauli na Yonathani, Daudi alitunga wimbo wa maombolezo ambao katika huo alimwaga huzuni yake yote. Hatimaye wimbo huo wa maombolezo ukawa sehemu ya maandishi ya kitabu cha Biblia cha Samweli wa Pili. (2 Samweli 1:17-27; 2 Mambo ya Nyakati 35:25) Vivyo hivyo, wengine huona ni rahisi zaidi kujieleza kwa kuandika. Mjane mmoja aliripoti kwamba yeye alikuwa akiandika hisia zake kisha siku kadhaa baadaye alikuwa akisoma yale aliyokuwa ameandika. Aliona hiyo kuwa njia yenye kusaidia kuondosha huzuni.

      Iwe ni kwa kuongea au kwa kuandika, kuwasilisha hisia zako kwaweza kukusaidia uondoshe huzuni yako. Kwaweza pia kuondolea mbali kutoelewana. Mama mmoja aliyefiwa aeleza hivi: “Mume wangu nami tulisikia juu ya waume na wake wengine waliotalikana baada ya kufiwa na mtoto, nasi hatukutaka hilo litupate. Kwa hiyo wakati wowote tulipokasirika, tukitaka kulaumiana, tulikuwa tukiongea juu yalo. Nafikiri tulikaribiana sana kwa kufanya hivyo.” Hivyo, kujulisha hisia zenu kwaweza kuwasaidia mwelewe kwamba hata ingawa huenda ikawa mnashiriki pamoja hasara ile ile, wengine waweza kuhuzunika kwa njia tofauti—kwa mwendo wao wenyewe na kwa njia yao wenyewe.

      Jambo jingine liwezalo kurahisisha ondoleo la huzuni ni kulia. Kuna “wakati wa kulia,” Biblia husema. (Mhubiri 3:1, 4, NW) Kwa hakika kifo cha mtu fulani tumpendaye huleta wakati wa jinsi hiyo. Kulia machozi ya huzuni kwaonekana kuwa sehemu ya lazima ya kawaida ya kupona.

      Mwanamke mmoja mchanga aeleza jinsi rafiki wa karibu alivyomsaidia ashughulike vya kufaa na hali wakati mama yake alipokufa. Yeye akumbuka hivi: “Sikuzote rafiki yangu alikuwapo kwa ajili yangu. Alilia pamoja nami. Aliongea nami. Niliweza tu kuonyesha hisiamoyo zangu waziwazi sana, na hilo lilikuwa jambo la maana kwangu. Sikuhitaji kuaibika kwa sababu ya kulia.” (Ona Warumi 12:15.) Wewe pia hupaswi kuaibika kwa sababu ya machozi yako. Kama vile tumeona, Biblia imejaa vielelezo vya wanaume na wanawake wa imani—kutia na Yesu Kristo—waliolia machozi ya huzuni waziwazi bila kuonekana kuwa na aibu.—Mwanzo 50:3; 2 Samweli 1:11, 12; Yohana 11:33, 35.

      Huenda ukaona kwamba kwa wakati fulani hisiamoyo zako zitatokea bila kutazamiwa. Huenda machozi yakatiririka bila ya wewe kujua kimbele. Mjane mmoja aliona kwamba kununua vitu kwenye duka kubwa (jambo alilokuwa amefanya mara nyingi pamoja na mume wake) kuliweza kumfanya alie, hasa wakati, kwa sababu ya kuzoea, alipofikia ili achukue vyakula vilivyopendwa sana na mume wake. Jionyeshe saburi. Na usihisi kwamba ni lazima uyazuie machozi yasitoke. Kumbuka, hiyo ni sehemu ya asili na ya lazima ya kuhuzunika.

      Kushughulika vya Kufaa na Hali ya Kuhisi Una Hatia

      Kama ilivyoonyeshwa kimbele, wengine wana hisia za kuwa na hatia baada ya kufiwa na mpendwa. Hilo huenda likasaidia kueleza sababu ya ile huzuni nyingi ya yule mwanamume mwaminifu Yakobo alipofanywa aamini kwamba mwana wake Yusufu alikuwa ameuawa na “hayawani-mwitu mkali.” Yakobo mwenyewe alikuwa amemtuma Yusufu aende akachunguze hali njema ya ndugu zake. Kwa hiyo yaelekea Yakobo alisumbuliwa na hisia za kuwa na hatia, kama vile ‘Kwa nini nilimtuma Yusufu akiwa peke yake? Kwa nini nilimtuma kwenye eneo ambalo limejaa mahayawani-mwitu?’—Mwanzo 37:33-35, NW.

      Labda wewe wahisi kwamba uzembe fulani upande wako ulichangia kifo cha mpendwa wako. Kung’amua kwamba kuhisi una hatia—iliyo halisi au ya kuwaziwa tu—ni itikio la kawaida la huzuni kwenyewe kwaweza kusaidia. Hapa tena, usihisi kwamba hupaswi kuonyesha hisia hizo. Kuongea juu ya jinsi uhisivyo kwamba una hatia kwaweza kuandaa ondoleo kubwa linalohitajiwa la huzuni.

      Ingawa hivyo, ng’amua kwamba haidhuru ni kadiri gani tumpendavyo mtu mwingine, sisi hatuwezi kudhibiti maisha yake, wala hatuwezi kuzuia “wakati na tukio lisilotazamiwa” lisiwapate wale tuwapendao. (Mhubiri 9:11, NW) Ingawaje, bila shaka madhumuni yako hayakuwa mabaya. Kwa kielelezo, kwa kutofanya mpango wa kumwona daktari mapema zaidi, je, wewe ulikusudia mpendwa wako awe mgonjwa na kufa? Bila shaka sivyo! Basi, je, una hatia kwelikweli ya kusababisha kifo cha mtu huyo? La.

      Mama mmoja alijifunza kushughulika vya kufaa na hali ya kuhisi ana hatia baada ya binti yake kufa katika aksidenti ya gari. Yeye aeleza hivi: “Nilihisi nina hatia kwa sababu ya kumtuma. Lakini nikaja kung’amua kwamba kuhisi hivyo lilikuwa jambo la upuuzi. Kumtuma aende na baba yake afanye kazi fulani hakukuwa kosa. Hiyo ilikuwa aksidenti tu iliyo mbaya sana.”

      ‘Lakini kuna mambo mengi sana ambayo laiti ningalisema au kufanya,’ huenda ukasema. Ni kweli, lakini ni nani kati yetu awezaye kusema kwamba sisi tumekuwa baba, mama, au mtoto mkamilifu? Biblia hutukumbusha hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2; Warumi 5:12, NW) Kwa hiyo kubali uhakika wa kwamba wewe si mkamilifu. Kuendelea kufikiri-fikiri ati “laiti tu ningalifanya hivi au vile” hakutabadili chochote, lakini huenda kwaweza kukawiza kupata kwako nafuu.

      Ikiwa una sababu nzuri za kuamini kwamba hatia yako ni halisi, isiyowaziwa tu, basi fikiria lile jambo la maana zaidi ya yote katika kutuliza hisia ya kuwa na hatia—msamaha wa Mungu. Biblia hututia moyo hivi: “BWANA, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha.” (Zaburi 130:3, 4) Huwezi kurudia wakati uliopita na kubadili chochote. Lakini, waweza kumwomba Mungu msamaha kwa makosa ya wakati uliopita. Kisha nini? Ikiwa Mungu anaahidi kufuta kabisa makosa yako, je, wewe hupaswi pia kujisamehe?—Mithali 28:13; 1 Yohana 1:9.

      Kushughulika vya Kufaa na Kasirani

      Je! wahisi kasirani pia, labda kuelekea madaktari, wauguzi, marafiki, au hata yule mfu? Ng’amua kwamba hilo pia ni itikio la kawaida la kufiwa. Labda kasirani yako yaandamana kwa asili na uchungu unaohisi. Mwandikaji mmoja alisema: “Ni kwa kuja kutambua kukasirika kwako tu—si kwa kutenda kulingana nayo bali kwa kujua unahisi hivyo—ndipo uwezapo kuwa huru na matokeo yayo yenye uharibifu.”

      Huenda pia ikasaidia kueleza au kushiriki kasirani hiyo na mwingine. Jinsi gani? Kwa hakika si kwa mifoko isiyodhibitiwa. Biblia huonya kwamba kasirani yenye kudumu muda mrefu ni hatari. (Mithali 14:29, 30) Lakini huenda ukapata faraja katika kuongea juu yayo pamoja na rafiki mwenye kuelewa. Na wengine huona kwamba mazoezi yenye nguvu wanapokuwa wamekasirika ni njia yenye kusaidia ya kuondosha kasirani.—Ona pia Waefeso 4:25, 26.

      Ingawa ni jambo la maana kuonyesha hisia zako waziwazi na kwa haki, onyo lafaa kutolewa hapa. Kuna tofauti kubwa kati ya kuonyesha hisia zako na kuwafokea wengine. Hakuna haja ya kuwalaumu wengine kwa sababu ya kasirani na kukatishwa tamaa kwako. Kwa hiyo uwe mwangalifu juu ya kueleza hisia zako, lakini si kwa njia yenye uhasama. (Mithali 18:21) Kuna msaada mmoja muhimu sana katika kushughulika vya kufaa na huzuni, na tutauzungumzia sasa.

      Msaada Kutoka kwa Mungu

      Biblia hututia moyo hivi: “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:18) Ndiyo, zaidi ya jambo jingine lolote, uhusiano na Mungu waweza kukusaidia ushughulike vya kufaa na kifo cha mtu fulani umpendaye. Jinsi gani? Madokezo yote yenye kutumika ambayo yametolewa hadi sasa yametegemea au yanapatana na Neno la Mungu, Biblia. Kuzitumia kwaweza kukusaidia ushughulike vya kufaa na hali.

      Kwa kuongezea, usipunguze umaana wa thamani ya sala. Biblia hutusihi hivi: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Ikiwa kumweleza rafiki mwenye kusikitikia hisia zako kwaweza kusaidia, basi kummwagia “Mungu wa faraja yote” yaliyomo moyoni mwako kwaweza kukusaidia hata zaidi kama nini!—2 Wakorintho 1:3, NW.

      Si kwamba sala hutufanya tuhisi vizuri zaidi tu. “Msikiaji wa sala” anaahidi kuwatolea roho takatifu watumishi wake waiombao kwa moyo mweupe. (Zaburi 65:2; Luka 11:13, NW) Na roho takatifu, au kani ya utendaji ya Mungu, yaweza kukupa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili uendelee kuishi siku moja baada ya nyingine. (2 Wakorintho 4:7, NW) Kumbuka: Mungu aweza kuwasaidia watumishi wake waaminifu wavumilie tatizo lolote lile ambalo huenda wakakabili.

      Mwanamke mmoja aliyefiwa na mtoto wake akumbuka jinsi nguvu ya sala ilivyomsaidia yeye na mume wake wakati wa hasara yao. “Ikiwa tulikuwa nyumbani usiku na huzuni ikazidi, tulikuwa tukisali pamoja kwa sauti kubwa,” yeye aeleza. “Mara ya kwanza tulilazimika kufanya lolote bila yeye—mkutano wa kutaniko wa kwanza tuliokwenda, mkusanyiko wa kwanza tuliohudhuria—tulikuwa tukisali ili kupata imara. Tulipoamka asubuhi na ikaonekana hatuwezi kuvumilia uhalisi wa hali hiyo, tulikuwa tukisali kwa Yehova atusaidie. Kwa sababu fulani, nilikuwa na umivu kali kwelikweli la kimoyoni kuingia nyumbani nikiwa peke yangu. Kwa hiyo kila wakati nilipokuja nyumbani nikiwa peke yangu, nilikuwa tu nikimwomba Yehova tafadhali anisaidie kudumisha kadiri fulani ya utulivu.” Mwanamke huyo mwaminifu aamini kwa uthabiti na ifaavyo kwamba sala hizo zilifanya hali iwe tofauti. Wewe pia waweza kuona kwamba likiwa tokeo la sala zako zenye udumifu, ‘amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda moyo wako na nguvu zako za akili.’—Wafilipi 4:6, 7; Warumi 12:12, NW.

      Kwa kweli ule msaada ambao Mungu huandaa hufanya hali iwe tofauti. Mtume Mkristo Paulo alisema kwamba Mungu “hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tupate kuweza kufariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki.” Ni kweli, msaada wa kimungu hauondoi umivu, lakini waweza kufanya hali iwe rahisi zaidi kuvumilia. Hilo halimaanishi kwamba hutalia tena au utamsahau mpendwa wako. Lakini waweza kupata nafuu. Na upatapo nafuu, yale ambayo umepatwa nayo yaweza kukufanya uwe mwenye kuelewa na mwenye kusikitikia zaidi katika kuwasaidia wengine washughulike vya kufaa na hasara hiyohiyo.—2 Wakorintho 1:4, NW.

      [Sanduku katika ukurasa wa 19]

      Maswali ya Kufikiriwa Sana

      Kwa nini ni jambo la maana kujiruhusu uhuzunike?

      Waweza kuondoshaje huzuni yako?

      Maandiko yaweza kukusaidiaje ushughulike vya kufaa na hisia za kuwa na hatia na kasirani?

      Uhusiano na Mungu waweza kukusaidia kwa njia gani ushughulike vya kufaa na kifo cha mpendwa?

      Ni nini baadhi ya madokezo yenye kutumika ya kushughulika vya kufaa na huzuni?

      [Sanduku katika ukurasa wa 18]

      Baadhi ya Madokezo Yenye Kutumika

      Tegemea marafiki: Usisite kuwaruhusu wengine wasaidie ikiwa wanajitolea kufanya hivyo na kwa kweli wahitaji msaada huo. Elewa ya kwamba huenda hiyo ikawa njia yao ya kukuonyesha jinsi wahisivyo; labda hiyo ndiyo njia rahisi zaidi kwao kufanya hivyo kuliko kueleza hisia hizo kwa maneno.—Mithali 18:24.

      Tunza afya yako: Kuhuzunika kwaweza kukudhoofisha, hasa mwanzoni. Mwili wako wahitaji pumziko la kutosha, mazoezi yenye afya, na lishe ifaayo kuliko wakati mwingine wowote. Kuchunguzwa pindi kwa pindi na daktari wa familia yako kwaweza kuwa jambo zuri.

      Ahirisha maamuzi makubwa: Ikiwezekana, ngoja angalau muda fulani mpaka unapoanza kufikiria kwa wazi zaidi kabla ya kuamua mambo kama vile kuuza nyumba yako au kubadili kazi yako. (Mithali 21:5) Mjane mmoja alikumbuka kwamba siku kadhaa baada ya mume wake kufa, yeye aliwapa wengine vitu vingi vya kibinafsi vya mume wake. Baadaye, aling’amua kwamba alikuwa amewapa vikumbusha vidogo-vidogo alivyohazini.

      Jionyeshe saburi: Mara nyingi huzuni huendelea muda mrefu zaidi ya vile watu kwa ujumla hung’amua. Vikumbusha vya kila mwaka vya mpendwa aliyekufa vyaweza kurudisha umivu kali. Picha za pekee, nyimbo, au hata harufu zaweza kutokeza machozi. Uchunguzi mmoja wa kisayansi juu ya kufiwa ulieleza yafuatayo kuhusu kawaida ya kuhuzunika: “Huenda yule aliyefiwa akabadilika-badilika upesi na kwa njia yenye kutokeza kutoka hali moja ya hisia hadi nyingine, na hali ya kuepuka vikumbusha vya yule mfu yaweza kubadilishana na hali ya ukuzaji wa kumbukumbu hiyo kimakusudi kwa kipindi fulani cha wakati.” Kumbuka ahadi za Yehova zenye thamani kubwa.—Wafilipi 4:8, 9.

      Wape wengine nafasi: Jaribu kuwa mwenye saburi kuelekea wengine. Ng’amua kwamba hali ni ngumu kwao. Kwa sababu ya kutojua la kusema, huenda bila kufikiri wakasema jambo lisilofaa.—Wakolosai 3:12, 13.

      Epuka kutumia madawa au kileo ili kushughulika na huzuni yako: Kitulizo chochote kinachotolewa na madawa au kileo ni cha muda tu. Madawa yapaswa kutumiwa chini ya usimamizi wa daktari tu. Lakini uwe mwangalifu; madawa mengi ni yenye kutia uraibu (uzoevu). Kwa kuongezea, huenda hayo yakakawiza kawaida ya kuhuzunika. Tabibu fulani aonya hivi: “Lazima msiba huo uvumiliwe, uonwe na hatimaye usawazishwe na kukawiza hatua hizo bila sababu nzuri kwa kumlevya kabisa [mtu] huyo kwa madawa kwaweza kurefusha au kupotosha kawaida hiyo.” Kitulizo cha kudumu kitakuja kupitia njia ya kutafakari juu ya makusudi matukufu ya Yehova.—Zaburi 1:2; 119:97.

      Rudia ratiba ya kawaida: Huenda ukahitaji kujilazimisha mwanzoni kwenda kazini, kwenda kununua vitu dukani, au kushughulika na madaraka mengine. Lakini huenda ukaona kwamba muundo wa ratiba yako ya kawaida utakunufaisha sana. Uwe mwenye shughuli katika utendaji wa Kikristo.—Linganisha 1 Wakorintho 15:58.

      Usiogope kuacha kuhuzunika sana: Ingawa huenda ikaonekana kuwa jambo la ajabu, wengine waliofiwa huogopa kuacha kuhuzunika sana, wakiamini kwamba hiyo huenda ikaonyesha kwamba kumpenda kwao yule mfu kunapungua. Sivyo hata kidogo. Kuacha kuwa na umivu hufungulia njia kumbukumbu zenye kuhaziniwa ambazo bila shaka utaendelea kuwa nazo sikuzote.—Mhubiri 3:1, 4.

      Usihangaike bila sababu nzuri: Huenda ukajipata ukihangaika hivi, ‘Hali yangu itakuwaje sasa?’ Biblia hushauri tushughulikie siku moja-moja. “Kushughulikia siku moja-moja hunisaidia kwelikweli,” aeleza mjane mmoja. Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Msihangaike wakati wowote juu ya siku ifuatayo, kwa maana siku ifuatayo itakuwa na mahangaiko yayo yenyewe.”—Mathayo 6:25-34, NW.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki