-
Kwa Nini Tuongozwe na Roho ya Mungu?Mnara wa Mlinzi—2011 | Desemba 15
-
-
Kwa Nini Tuongozwe na Roho ya Mungu?
“Wewe ni Mungu wangu. Roho yako ni nzuri; na iniongoze.”—ZAB. 143:10.
1. Toa mfano wa jinsi nguvu isiyoonekana inavyoweza kumwongoza mtu.
JE, UMEWAHI kutumia dira ili kujua mahali unapoelekea? Dira ni kifaa rahisi kilicho tu na sehemu moja inayozunguka-zunguka, yaani, mshale wenye sumaku unaoelekeza upande wa kaskazini. Nguvu isiyoonekana inayoitwa nguvu ya sumaku ndiyo inayouwezesha mshale huo wa dira kuzunguka. Kwa karne nyingi, wagunduzi na wasafiri wametumia dira ili iwaongoze katika safari zao za nchi kavu na za baharini.
2, 3. (a) Yehova alitumia nguvu gani nyingi miaka mingi iliyopita? (b) Kwa nini tunapaswa kutarajia nguvu ya utendaji ya Mungu isiyoonekana iongoze maisha yetu leo?
2 Kuna nguvu nyingine isiyoonekana ambayo ni muhimu hata zaidi ili kutuongoza. Ni nguvu gani hiyo? Ni ile inayozungumziwa katika mistari ya kwanza ya Biblia. Kitabu cha Mwanzo kinasema hivi kuhusu yale ambayo Yehova alitimiza miaka mingi iliyopita: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Tunajua kwamba Mungu alitumia nguvu nyingi ili kuumba vitu kwa sababu simulizi la uumbaji linaongeza hivi: “Nguvu za utendaji za Mungu zilikuwa zikienda huku na huku.” (Mwa. 1:1, 2) Mungu alitumia nguvu gani? Roho takatifu, nguvu yake yenye msukumo aliyotumia katika uumbaji. Tunashukuru kwamba Yehova alitumia roho hiyo ili kutupatia uhai na kuumba vitu vingine vyote.—Ayu. 33:4; Zab. 104:30.
3 Tukiwa wanadamu hai wanaopumua, je, hatungetarajia nguvu ya utendaji ya Mungu iwe na uvutano zaidi katika maisha yetu? Mwana wa Mungu alijua kwamba tungepaswa kutarajia hilo, kwa kuwa Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Roho . . . atawaongoza ninyi ndani ya kweli yote.” (Yoh. 16:13) Roho hiyo ni nini, na kwa nini tutake ituongoze?
Roho Takatifu Ni Nini?
4, 5. (a) Wale wanaoamini fundisho la Utatu wana maoni gani yenye makosa kuhusu roho takatifu? (b) Eleza roho takatifu ni nini hasa.
4 Inaelekea, baadhi ya watu unaokutana nao katika huduma wanaamini kile ambacho tafsiri ya King James Version na tafsiri nyingine za Biblia zinaita Roho Mtakatifu (Holy Ghost). Wale wanaoamini fundisho la Utatu wanafikiri kimakosa kwamba roho hiyo ni mtu aliye sawa na Mungu Baba. (1 Kor. 8:6) Hata hivyo, inapendeza kujua kwamba mtungaji wa kamusi Mmarekani Noah Webster, katika tafsiri yote ya The Webster Bible, ambayo ilitegemea tafsiri iliyorekebishwa ya King James Version, ambayo ilichapishwa kwanza mwaka wa 1833, alitumia maneno “Roho Takatifu” badala ya “Roho Mtakatifu.” Webster alifanya hivyo kwa sababu alijua kwamba katika Maandiko maneno hayo hayakumaanisha “mzuka,” (apparition, ghost).a
5 Hivyo basi, roho takatifu ni nini hasa? Biblia ya Marejeo (New World Translation of the Holy Scriptures—With References) inasema hivi katika maelezo ya chini ya andiko la Mwanzo 1:2: “Zaidi ya kutafsiri neno ruʹach [Kiebrania] kuwa ‘roho,’ neno hilo linatafsiriwa pia kuwa ‘upepo’ na linatafsiriwa kwa maneno mengine ambayo yanamaanisha nguvu ya utendaji isiyoonekana.” (Linganisha na maelezo ya chini ya Mwanzo 3:8; 8:1.) Hata ingawa hatuwezi kuona upepo, tunaweza kuona yale unayofanya. Vivyo hivyo, roho takatifu haionekani wala si mtu, lakini tunaweza kuona matokeo ya kazi inayofanya. Roho hiyo ni nishati kutoka kwa Mungu inayotumiwa kutenda juu ya watu au vitu ili kutimiza mapenzi yake. Je, ni vigumu kuamini kwamba nguvu hizo za ajabu zinatoka kwa Chanzo kitakatifu, yaani, Mungu Mweza-Yote? Hapana!—Soma Isaya 40:12, 13.
6. Ni jambo gani muhimu sana ambalo Daudi alimsihi Yehova?
6 Je, Yehova anaweza kuendelea kutumia roho yake kutuongoza katika maisha yetu yote? Alimwahidi mtunga-zaburi Daudi hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea.” (Zab. 32:8) Je, Daudi alitaka kuongozwa na Mungu? Naam, kwa sababu alimsihi Yehova hivi: “Unifundishe kufanya mapenzi yako, kwa maana wewe ni Mungu wangu. Roho yako ni nzuri; na iniongoze.” (Zab. 143:10) Sisi pia tunapaswa kuwa na tamaa kama hiyo na kuwa tayari kuongozwa na roho ya Mungu. Kwa nini? Chunguza sababu nne.
Hatuna Uwezo wa Kujiongoza Wenyewe
7, 8. (a) Kwa nini hatuwezi kujiongoza wenyewe bila kumtegemea Mungu? (b) Ni mfano gani unaotusaidia kuelewa kwa nini hatupaswi kujaribu kujiongoza wenyewe katika mfumo huu mwovu?
7 Kwanza, tunapaswa kuwa na tamaa ya kutaka kuongozwa na roho ya Mungu kwa sababu hatuna uwezo wa kujiongoza wenyewe. Kumwongoza mtu kunamaanisha kumwonyesha njia inayofaa kufuata. Hata hivyo, Yehova hakutuumba tukiwa na uwezo wa kujiongoza sisi wenyewe, hasa tukiwa katika hali yetu ya kutokamilika. Nabii wake Yeremia aliandika hivi: “Ee Bwana, najua kwamba njia ya mwanadamu haimo ndani yake mwenyewe: mwanadamu hana uwezo wa kuongoza hatua zake.” (Yer. 10:23, The Bible in Basic English) Kwa nini? Mungu alituambia kupitia Yeremia kwa nini hatuwezi kujiongoza wenyewe. Yehova alisema hivi kuhusu mtu tuliye kwa ndani: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?”—Yer. 17:9; Mt. 15:19.
8 Je, halingekuwa jambo la upumbavu kwa mtu asiye na uzoefu kutembea peke yake kupitia eneo fulani hatari kama vile msituni au nyikani bila dira au ramani? Ikiwa mtu huyo hajui jinsi ya kuishi katika eneo kama hilo na hajui jinsi ya kupata njia iliyo salama, angekuwa akihatarisha maisha yake. Vivyo hivyo, mtu anayefikiri kwamba anaweza kujiongoza mwenyewe katika ulimwengu huu mwovu bila kukubali Mungu amwonyeshe njia inayofaa, anahatarisha maisha yake. Uwezekano pekee tulionao wa kupita kwa mafanikio katika mfumo huu wa mambo ni kumwomba Yehova hivi kama alivyofanya Daudi: “Hatua zangu na zishike njia zako, ambamo hatua za miguu yangu hakika hazitatikiswa.” (Zab. 17:5; 23:3) Tunawezaje kupata mwongozo huo?
9. Kama inavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 17, roho ya Mungu inaweza kutuongoza kwa uhakika jinsi gani?
9 Ikiwa sisi ni wanyenyekevu na tuko tayari kumtegemea Yehova, atatupatia roho yake takatifu ili iongoze hatua zetu kwa uhakika. Nguvu hiyo ya utendaji itatusaidia jinsi gani? Yesu aliwaeleza hivi wanafunzi wake: “Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba atatuma katika jina langu, hiyo itawafundisha ninyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” (Yoh. 14:26) Tukisali na kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu, kutia ndani maneno yote ya Kristo, roho takatifu itatusaidia kuelewa zaidi hekima yenye kina ya Yehova ili tuweze kumtii. (1 Kor. 2:10) Isitoshe, mambo fulani yasiyotarajiwa yanapotokea katika maisha yetu, roho ya Mungu itatuonyesha njia ya kufuata. Itatukumbusha kanuni za Biblia ambazo tayari tumejifunza na itatusaidia kuelewa jinsi tunavyoweza kufanya maamuzi mazuri.
Yesu Aliongozwa na Roho ya Mungu
10, 11. Ni matarajio gani ambayo Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alikuwa nayo kuhusiana na roho takatifu, na roho takatifu ilimsaidiaje?
10 Sababu ya pili ya kutaka tuongozwe na roho takatifu ni kwamba Mungu alimwongoza Mwanawe kupitia roho hiyo. Kabla ya kuja duniani, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alijua unabii huu: “Roho ya Yehova itatua juu yake, roho ya hekima na ya uelewaji, roho ya shauri na ya nguvu, roho ya ujuzi na ya kumwogopa Yehova.” (Isa. 11:2) Hebu fikiria jinsi Yesu alivyokuwa na hamu kubwa ya kupokea msaada wa roho ya Mungu ili kukabiliana na matatizo hapa duniani.
11 Maneno ya Yehova yalitimia. Simulizi la Injili linasema mambo yaliyotukia mara tu baada ya ubatizo wa Yesu: “Basi Yesu, akiwa amejaa roho takatifu, akarudi kutoka Yordani, naye akaongozwa na roho huku na huku nyikani.” (Luka 4:1) Huko nyikani, Yesu alipokuwa akifunga, kusali, na kutafakari, inaelekea Yehova alimpa maagizo na kumtayarisha Mwanawe kwa ajili ya mambo ambayo yangempata baadaye. Nguvu ya utendaji ya Mungu ilikuwa na uvutano juu ya akili na moyo wa Yesu, ikiongoza fikira na maamuzi yake. Kwa sababu hiyo, Yesu alijua jambo la kufanya katika kila hali, na alifanya sawasawa na yale ambayo Baba yake alitaka afanye.
12. Kwa nini ni muhimu kuomba roho ya Mungu ituongoze?
12 Akijua thamani ya uvutano mzuri wa roho ya Mungu katika maisha yake, Yesu alikazia umuhimu wa wanafunzi wake kuomba wapewe roho takatifu na pia umuhimu wa kuongozwa na roho hiyo. (Soma Luka 11:9-13.) Kwa nini hilo ni jambo muhimu sana kwetu? Kwa sababu roho ya Mungu inaweza kubadili kufikiri kwetu na kutusaidia kuwa na akili ya Kristo. (Rom. 12:2; 1 Kor. 2:16) Kwa kuiruhusu roho ya Mungu iongoze maisha yetu, tunaweza kufikiri kama Kristo na kuiga mfano wake.—1 Pet. 2:21.
Roho ya Ulimwengu Itatuongoza Vibaya
13. Roho ya ulimwengu ni nini, na inatokeza nini?
13 Sababu ya tatu ya kutaka tuongozwe na roho ya Mungu ni kwamba bila roho hiyo tungeongozwa vibaya na roho ya ulimwengu isiyo takatifu ambayo inaongoza maisha ya watu wengi leo. Hiyo ni roho yenye nguvu ambayo inawachochea watu kutenda tofauti kabisa na yale ambayo roho takatifu inatuongoza kutenda. Badala ya kuwasaidia watu kuwa na akili ya Kristo, roho hiyo ya ulimwengu inawachochea watu kufikiri na kutenda kama mtawala wa ulimwengu, Shetani. (Soma Waefeso 2:1-3; Tito 3:3.) Mtu anaporuhusu roho ya ulimwengu imwongoze na kuanza kutenda matendo ya mwili, kunakuwa na matokeo mabaya, ambayo yatamzuia kurithi Ufalme wa Mungu.—Gal. 5:19-21.
14, 15. Tunaweza kufaulu jinsi gani kuipinga roho ya ulimwengu?
14 Yehova ametupatia kila kitu tunachohitaji ili kuipinga roho ya ulimwengu. Mtume Paulo alisema kwamba ‘uendelee kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake ili uweze kupinga katika ile siku ya uovu.’ (Efe. 6:10, 13) Kupitia roho yake, Yehova anatuimarisha ili tupinge jitihada za Shetani za kutupotosha. (Ufu. 12:9) Roho ya ulimwengu ni yenye nguvu, na hatuwezi kuiepuka kabisa. Hata hivyo, tunaweza kuipinga. Roho takatifu ni yenye nguvu hata zaidi, na itatusaidia!
15 Mtume Petro alisema hivi kuhusu wale walioacha Ukristo katika karne ya kwanza: “Wameiacha njia iliyo nyoofu, wamepotoshwa.” (2 Pet. 2:15) Tunaweza kuwa wenye shukrani kama nini kwamba tumepokea “si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu”! (1 Kor. 2:12) Kwa kuiruhusu roho takatifu ituongoze na kwa kutumia maandalizi yote ambayo Yehova anatupatia ili kuendelea kuimarisha uhusiano wetu pamoja naye, tunaweza kufaulu kuipinga roho ya kishetani ya ulimwengu huu mwovu.—Gal. 5:16.
Roho Takatifu Inatokeza Tunda Zuri
16. Roho takatifu inaweza kutokeza ndani yetu tunda gani?
16 Sababu ya nne ya kutaka kuongozwa na roho ya Mungu ni kwamba inatokeza tunda zuri katika maisha ya wale ambao wanaongozwa nayo. (Soma Wagalatia 5:22, 23.) Ni nani miongoni mwetu ambaye hangetaka kuwa mwenye upendo, shangwe, na amani zaidi? Ni nani miongoni mwetu ambaye hangetaka kuwa na ustahimilivu, fadhili, na wema zaidi? Ni nani miongoni mwetu ambaye hangefaidika kwa kusitawisha zaidi sifa ya imani, upole, na kujizuia? Roho ya Mungu inatokeza ndani yetu sifa nzuri ambazo zinatunufaisha na kuwanufaisha wale tunaoishi nao na kutumika nao. Kwa kuwa hakuna mwisho wa kusitawisha tunda la roho kwa kadiri ambayo tunahitaji na kwa kadiri ambayo tunaruhusiwa kusitawisha, tunapaswa kujitahidi sana kuendelea kusitawisha tunda hilo.
17. Tunaweza kusitawishaje sifa fulani ya tunda la roho kwa kadiri kubwa zaidi?
17 Ni jambo la hekima tuhakikishe kwamba maneno na matendo yetu yanathibitisha kuwa tunaongozwa na roho takatifu na tunazaa tunda lake. (2 Kor. 13:5a; Gal. 5:25) Ikiwa tunaona kwamba tunahitaji kusitawisha sifa fulani za tunda la roho, tunaweza kushirikiana na roho takatifu kwa kadiri kubwa ili tusitawishe sifa hizo. Tunafanya hivyo kwa kujifunza kila sifa kama inavyofunuliwa katika Biblia na kuzungumziwa katika machapisho yetu ya Kikristo. Hivyo tunaweza kutambua jinsi tunavyopaswa kuonyesha tunda la roho katika maisha yetu ya kila siku na kisha kulisitawisha kwa kadiri kubwa zaidi.b Tunapoona matokeo ya utendaji wa roho ya Mungu katika maisha yetu wenyewe na pia katika maisha ya Wakristo wenzetu, tunaona waziwazi kwa nini ni lazima tuongozwe na roho hiyo.
Je, Unairuhusu Roho ya Mungu Ikuongoze?
18. Yesu alituwekeaje kielelezo kwa kukubali roho ya Mungu imwongoze?
18 Akiwa “stadi wa kazi” wa Mungu katika uumbaji wa ulimwengu, Yesu alijua kila kitu kuhusu nguvu za sumaku za dunia ambazo wanadamu wanatumia ili kusafiri duniani. (Met. 8:30; Yoh. 1:3) Hata hivyo, hakuna uthibitisho katika Biblia unaoonyesha kwamba Yesu aliwahi kutumia nguvu hizo ili kuongoza hatua zake alipokuwa duniani. Biblia inasema kwamba akiwa mwanadamu, Yesu alijionea jinsi roho takatifu ya Mungu ilivyotenda kwa nguvu sana katika maisha yake. Alikubali uvutano wa roho hiyo, na ilipomchochea, aliiruhusu imwongoze naye akatenda kulingana nayo. (Marko 1:12, 13; Luka 4:14) Je, wewe unairuhusu roho ya Mungu ikuongoze kama alivyofanya Yesu?
19. Ni lazima tufanye nini ili roho takatifu iwe nguvu yenye kutuongoza maishani?
19 Bado nguvu ya utendaji ya Mungu inatenda kazi juu ya akili na mioyo ili kuwachochea na kuwaongoza wale wanaoikubali. Unawezaje kuiruhusu roho ya Mungu itende kazi juu yako na kukuongoza upande unaofaa? Sali daima kwa Yehova ili akupe roho yake na kukusaidia kukubali mwongozo wake. (Soma Waefeso 3:14-16.) Tenda kulingana na sala zako kwa kutafuta mashauri katika Neno la Mungu lililoandikwa, Biblia, ambalo liliandikwa chini ya mwongozo wa roho takatifu. (2 Tim. 3:16, 17) Tii maagizo yenye hekima yanayotolewa na Biblia na kisha uwe tayari kukubali mwongozo wa roho takatifu. Onyesha una imani kwamba Yehova ana uwezo wa kukuongoza ifaavyo maishani katika ulimwengu huu mwovu.
[Maelezo ya Chini]
a Katika utangulizi wa Biblia yake, Webster aliandika hivi: “Wakati wowote maneno yanapoeleweka kwa njia tofauti na jinsi yalivyoeleweka mwanzoni, na kwa maana tofauti na ile ya lugha za awali, hayamsaidii msomaji kuelewa Neno la Mungu kwa usahihi.”
b Kwa maelezo zaidi kuhusu kila sifa ya tunda la roho, ona kichwa ‘Tunda la Roho ya Mungu’ na orodha ya kila sifa ya tunda hilo katika Fahirisi.
-
-
Waaminifu wa Zamani Waliongozwa na Roho ya MunguMnara wa Mlinzi—2011 | Desemba 15
-
-
Waaminifu wa Zamani Waliongozwa na Roho ya Mungu
“Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amenituma, ndiyo, roho yake.”—ISA. 48:16.
1, 2. Ni nini kinachohitajiwa ili kuonyesha imani, na tutatiwa moyo jinsi gani tukichunguza watumishi waaminifu wa kale?
INGAWA watu wengi wameonyesha imani tangu siku za Abeli, Biblia inasema kwamba “imani si mali ya watu wote.” (2 The. 3:2) Basi mtu anawezaje kuwa na imani, na ni nini kinachomwezesha kuwa mwaminifu? Kwa kadiri kubwa, imani inafuata mambo yanayosikiwa kutoka katika Neno la Mungu. (Rom. 10:17) Ni sehemu ya tunda la roho takatifu ya Mungu. (Gal. 5:22, 23) Kwa hiyo, ili tuwe na imani na kuionyesha kwa matendo tunahitaji roho takatifu.
2 Ni kosa kukata kauli kwamba wanaume na wanawake wenye imani wanazaliwa wakiwa na imani, yaani, ni sifa ya asili. Watumishi walioweka mfano mzuri ambao tunasoma kuwahusu katika Biblia walikuwa watu ‘wenye hisia kama zetu.’ (Yak. 5:17) Walikuwa na shaka, wasiwasi, na udhaifu mbalimbali lakini “wakafanywa kuwa wenye nguvu” na roho ya Mungu ili waweze kukabiliana na hali ngumu. (Ebr. 11:34) Tukichunguza jinsi roho ya Yehova ilivyowasaidia watumishi hao, tunaweza kutiwa moyo kuendelea kuwa waaminifu leo, kwa kuwa tunaishi wakati ambapo imani yetu inashambuliwa.
Roho ya Mungu Ilimtia Nguvu Musa
3-5. (a) Tunajuaje kwamba Musa alitimiza majukumu yake kwa msaada wa roho takatifu? (b) Mfano wa Musa unatufundisha nini kuhusu jinsi Yehova anavyotupatia roho yake?
3 Musa “alikuwa mpole zaidi” kuliko wanadamu wote waliokuwa hai katika mwaka wa 1513 K.W.K. (Hes. 12:3) Mtumishi huyo mwenye tabia-pole alikabidhiwa daraka zito sana katika taifa la Israeli. Roho ya Mungu ilimtia nguvu Musa ili atoe unabii, ahukumu, aandike, aongoze, na afanye miujiza. (Soma Isaya 63:11-14.) Hata hivyo, pindi moja, Musa alilalamika kwamba mzigo aliobeba ulikuwa mzito sana. (Hes. 11:14, 15) Hivyo, Yehova aliondoa “sehemu ya roho” iliyokuwa juu ya Musa na kuiweka juu ya watu wengine 70 ili wamsaidie kuubeba mzigo huo. (Hes. 11:16, 17) Ingawa mzigo wa Musa ulionekana kuwa mzito sana, kwa kweli, hakuwa akiubeba peke yake, na wale 70 pia waliowekwa rasmi ili wamsaidie hawangeubeba peke yao.
4 Musa alikuwa amepewa roho takatifu ya kutosha ili kutimiza kazi hiyo. Baada ya badiliko hilo, bado Musa alikuwa na roho yote aliyohitaji. Musa hakuwa na kiasi kidogo sana cha roho, na wale wanaume wazee 70 hawakuwa na roho nyingi sana. Yehova anatupatia kiasi tunachohitaji cha roho yake, kulingana na hali zetu. ‘Hatoi roho kwa kipimo’ lakini anatoa “kutokana na wingi alio nao.”—Yoh. 1:16; 3:34.
5 Je, unavumilia majaribu? Je, majukumu yako yanaongezeka na yanazidi kuchukua wakati wako mwingi zaidi? Je, unajitahidi kuiandalia familia yako mahitaji yake ya kiroho na ya kimwili huku ukikabiliana na gharama zinazozidi kuongezeka au mahangaiko kuhusu afya? Je, unabeba majukumu mazito katika kutaniko? Uwe na hakika kwamba kupitia roho yake, Mungu anaweza kukupa nguvu unazohitaji ili ukabiliane na hali yoyote.—Rom. 15:13.
Roho Takatifu Ilimfanya Bezaleli Astahili
6-8. (a) Roho ya Mungu iliwawezesha Bezaleli na Oholiabu kufanya nini? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Bezaleli na Oholiabu waliongozwa na roho ya Mungu? (c) Kwa nini simulizi la Bezaleli linatia moyo sana?
6 Simulizi la Bezaleli aliyeishi siku za Musa linafunua mengi kuhusu jinsi roho ya Mungu inavyofanya kazi. (Soma Kutoka 35:30-35.) Bezaleli aliwekwa rasmi ili aongoze katika kutengeneza vifaa muhimu vya maskani. Je, alikuwa na ujuzi wa kazi ya ufundi kabla ya mradi huo mkubwa? Labda, lakini kuna uwezekano mkubwa sana kwamba kazi ya mwisho aliyofanya kabla ya mradi huo ilikuwa kazi ya kuwatengenezea Wamisri matofali. (Kut. 1:13, 14) Basi Bezaleli angetimizaje kazi yake ngumu? Yehova “akamjaza roho ya Mungu katika hekima, katika uelewaji na katika ujuzi na katika kila aina ya ufundi na kwa ajili ya kubuni vyombo . . . ili kufanya vifaa sanifu vya kila namna.” Roho takatifu ilizidisha kipawa chochote cha asili ambacho huenda Bezaleli alikuwa nacho. Ndivyo ilivyokuwa na Oholiabu. Ni wazi kwamba Bezaleli na Oholiabu walijifunza vyema kazi yao, kwa kuwa hawakutimiza tu kazi yao bali pia waliwafundisha wengine mambo ya kufanya. Ndiyo, Mungu alitia hekima moyoni mwao ili wawafundishe wengine.
7 Pia, tunajua kwamba Bezaleli na Oholiabu waliongozwa na roho ya Mungu kwa sababu vitu walivyotengeneza vilidumu kwa muda mrefu sana. Vitu walivyotengeneza bado vilikuwa vikitumiwa miaka 500 baadaye. (2 Nya. 1:2-6) Tofauti na watu wanaotengeneza bidhaa leo, Bezaleli na Oholiabu hawakuwa na nia ya kuandika jina lao juu ya vitu walivyotengeneza ili kujiletea sifa. Sifa zote zilimwendea Yehova kwa sababu ya kazi walizotimiza.—Kut. 36:1, 2.
8 Leo, huenda tukawa na kazi ngumu zinazohitaji ustadi wa pekee, kama vile kujenga, kuchapisha, kupanga makusanyiko ya wilaya, kutoa misaada wakati wa misiba, na kuwasiliana na madaktari na wafanyakazi wa hospitali kuhusiana na msimamo wetu wa Kimaandiko unaohusu matumizi ya damu. Nyakati nyingine, kazi hizo zinafanywa na wafanyakazi wenye ustadi, lakini mara nyingi zinafanywa na wajitoleaji ambao hawana uzoefu katika kazi hususa. Roho ya Mungu inafanya jitihada zao zifanikiwe. Je, unasitasita kukubali mgawo katika utumishi wa Yehova, na kuhisi kwamba wengine wanastahili zaidi kuliko wewe? Kumbuka kwamba roho ya Yehova inaweza kuongeza ujuzi na uwezo wako na kukusaidia kutimiza mgawo wowote ambao anakupa.
Yoshua Alifanikiwa kwa Msaada wa Roho ya Mungu
9. Waisraeli walijikuta katika hali gani baada ya kutoka Misri, na ni swali gani lililozuka?
9 Roho ya Mungu ilimwongoza pia mtu mwingine aliyeishi katika siku za Musa na Bezaleli. Muda mfupi baada ya Waisraeli kutoka Misri, Waamaleki waliwashambulia watu wa Mungu bila sababu yoyote. Wakati ulifika wa Waisraeli kukabiliana na tishio hilo. Ingawa Waisraeli hawakuwa wamezoea kamwe kupigana vita, walilazimika kushiriki katika pambano la kwanza la kijeshi wakiwa watu waliowekwa huru. (Kut. 13:17; 17:8) Mtu fulani alihitajiwa ili kuongoza jeshi hilo katika vita. Ni nani angewaongoza?
10. Kwa nini Waisraeli walishinda vita chini ya uongozi wa Yoshua?
10 Yoshua alichaguliwa. Ikiwa angehitaji kutaja kazi ambayo alikuwa na uzoefu wa kufanya ili astahili kupata mgawo huo, angetaja kazi gani? Je, angesema kwamba amewahi kufanya kazi akiwa mtumwa? Kazi ya kuchanganya nyasi za kutengeneza matofali? Kukusanya mana? Ni kweli kwamba Elishama, babu ya Yoshua, alikuwa mkuu wa kabila la Efraimu na ni wazi kwamba aliongoza wanaume 108,100 waliokuwa katika mgawanyo mmoja kati ya migawanyo ya makabila matatu ya Israeli. (Hes. 2:18, 24; 1 Nya. 7:26, 27) Hata hivyo, Yehova aliagiza kupitia Musa kwamba Yoshua ndiye aliyepaswa kuongoza jeshi ambalo lingemwangamiza adui, hakumchagua Elishama au Nuni, mwana wake. Vita hivyo viliendelea kwa karibu siku nzima. Waisraeli walishinda kwa sababu Yoshua alitii kikamili na kuthamini kwa moyo wote mwongozo wa roho takatifu ya Mungu.—Kut. 17:9-13.
11. Tunaweza kufanikiwa jinsi gani katika utumishi mtakatifu kama Yoshua?
11 Baadaye, Yoshua, ‘akiwa amejaa roho ya hekima,’ alichukua mahali pa Musa. (Kum. 34:9) Roho takatifu haikumpa uwezo wa kutoa unabii au kufanya miujiza kama Musa, lakini ilimwezesha Yoshua kuwaongoza Waisraeli katika mapambano mengi ya kijeshi ambayo yaliwasaidia kushinda na kuichukua nchi ya Kanaani. Leo, huenda tukahisi kwamba hatuna uzoefu au hatustahili kutimiza migawo fulani katika utumishi wetu mtakatifu. Hata hivyo, kama Yoshua, tuna hakika kwamba tutafanikiwa ikiwa tutafuata kwa ukaribu maagizo kutoka kwa Mungu.—Yos. 1:7-9.
‘Roho ya Yehova Ilimfunika Gideoni’
12-14. (a) Ushindi wa wanaume 300 Waisraeli waliopigana na jeshi kubwa sana la Wamidiani unaonyesha nini? (b) Yehova alimpa Gideoni uhakikisho gani? (c) Mungu anatuhakikishia nini leo?
12 Baada ya kifo cha Yoshua, Yehova aliendelea kuonyesha jinsi nguvu zake zinavyoweza kuwaimarisha watu waaminifu. Kitabu cha Waamuzi kina masimulizi mengi kuhusu wanadamu ambao ‘kutoka hali ya udhaifu walifanywa kuwa wenye nguvu.’ (Ebr. 11:34) Kupitia roho takatifu, Mungu alimchochea Gideoni apigane kwa niaba ya watu Wake. (Amu. 6:34) Hata hivyo, jeshi ambalo Gideoni alikusanya lilikuwa dogo sana likilinganishwa na jeshi la Wamidiani. Kulikuwa na askari-jeshi wanne Wamidiani kwa kila askari-jeshi mmoja wa Israeli. Machoni pa Yehova, jeshi hilo dogo sana la Waisraeli lilikuwa kubwa sana. Mara mbili Yehova alimwagiza Gideoni apunguze jeshi lake kufikia askari-jeshi 1 Mwisraeli kwa askari-jeshi 450 wa adui. (Amu. 7:2-8; 8:10) Yehova alikubali idadi hiyo. Ikiwa wangepata ushindi mkubwa, ni nani angejigamba kwamba walishinda kwa sababu ya jitihada au hekima ya wanadamu?
13 Gideoni na askari-jeshi wake walikuwa tayari. Kama ungekuwa katika jeshi hilo dogo, je, ungejihisi salama kujua kwamba wale ambao waliogopa au wale ambao hawakuwa macho kuona hatari waliambiwa warudi nyumbani? Au ungeogopa ikiwa ungefikiria matokeo ya vita hivyo? Tuna hakika kwamba Gideoni alimtegemea Mungu. Alifanya mambo aliyoambiwa afanye! (Soma Waamuzi 7:9-14.) Yehova hakumshutumu Gideoni alipoomba ishara ya kuthibitisha kwamba Mungu angekuwa pamoja naye. (Amu. 6:36-40) Badala yake, Mungu aliimarisha imani ya Gideoni.
14 Nguvu za Yehova za kuokoa hazina mipaka. Anaweza kuwakomboa watu wake kutoka katika hali yoyote ngumu, hata anaweza kuwakomboa akitumia watu ambao wanaonekana kuwa dhaifu au wasio na uwezo. Huenda nyakati nyingine tukahisi kwamba maadui wetu ni wengi mno au tunakabili hali ngumu sana. Hatutazamii Mungu atuonyeshe ishara za kimuujiza kama alizomwonyesha Gideoni, lakini tunaweza kupata mwongozo na uhakikisho mwingi kutoka katika Neno la Mungu na kupitia kutaniko lake ambalo linaongozwa na roho yake. (Rom. 8:31, 32) Ahadi za Yehova zenye upendo zinaimarisha imani yetu na kutusadikisha kwamba kwa kweli yeye ni Msaidiaji wetu!
“Sasa Roho ya Yehova Ikaja Juu ya Yeftha”
15, 16. Kwa nini binti ya Yeftha alikuwa na mtazamo mzuri, na hilo linawatiaje moyo wazazi?
15 Fikiria mfano mwingine. Waisraeli walipolazimika kupigana na Waamoni, roho ya Yehova ‘ilikuja juu ya Yeftha.’ Akiwa na hamu kubwa ya kushinda vita hivyo na kumletea Yehova sifa, Yeftha aliweka nadhiri ambayo ilimgharimu sana. Yeftha aliweka nadhiri kwamba ikiwa Mungu angewatia Waamoni mikononi mwake, mtu ambaye angetoka kwanza nje ya mlango na kumpokea anaporudi nyumbani, angekuwa wa Yehova. Yeftha aliporudi baada ya kuwashinda Waamoni, binti yake alikuja mbio kumlaki. (Amu. 11:29-31, 34) Je, Yeftha alishangazwa na jambo hilo? Inaelekea kwamba halikumshangaza kwa sababu alikuwa na mtoto mmoja tu. Alitimiza nadhiri yake kwa kumtoa binti yake kwa ajili ya utumishi wa pekee katika patakatifu pa Yehova huko Shilo. Akiwa mwabudu mshikamanifu wa Yehova, binti ya Yeftha alisadiki kwamba nadhiri ya baba yake ilipaswa kutimizwa. (Soma Waamuzi 11:36.) Roho ya Yehova iliwapa wote wawili nguvu walizohitaji.
16 Binti ya Yeftha alisitawishaje roho hiyo ya kujidhabihu? Hapana shaka kwamba imani yake ilijengwa alipoona bidii ya baba yake ya kujitoa kwa Mungu. Wazazi, watoto wenu wanaona mfano wenu. Maamuzi yenu yanaonyesha kwamba mnaamini mambo mnayosema. Watoto wenu wanasikiliza sala zenu za unyoofu, wanasikiliza kwa makini mafundisho yenu, na kuona jitihada zenu zote za kumtumikia Yehova kwa moyo kamili. Watoto wenu wanapofanya hivyo, inaelekea kwamba watasitawisha tamaa yenye nguvu ya kujitoa ili wamtumikie Yehova. Jambo hilo litawaletea shangwe.
“Roho ya Yehova Ikaanza Kutenda Kazi Juu” ya Samsoni
17. Samsoni alifanya nini kupitia roho ya Mungu?
17 Fikiria mfano mwingine. Waisraeli walipotekwa nyara na Wafilisti, ‘baada ya muda roho ya Yehova ilianza kumchochea’ Samsoni ili awakomboe Waisraeli. (Amu. 13:24, 25) Samsoni alipewa nguvu za kutenda mambo ya kustaajabisha na yaliyohitaji uwezo usio na kifani. Wafilisti walipowashawishi Waisraeli wengine wamkamate Samsoni, “roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu yake, na zile kamba zilizokuwa kwenye mikono yake zikawa kama nyuzi za kitani ambazo zimeunguzwa kwa moto, nazo pingu zake zikayeyuka kutoka kwenye mikono yake.” (Amu. 15:14) Hata katika hali ya udhaifu iliyosababishwa na uamuzi wake mbaya, Samsoni alifanywa kuwa mwenye nguvu “kupitia imani.” (Ebr. 11:32-34; Amu. 16:18-21, 28-30) Roho ya Yehova ilitenda kazi juu ya Samsoni kwa njia ya pekee kwa sababu ya hali zisizo za kawaida. Hata hivyo, matukio hayo ya kihistoria yanatutia moyo sana. Jinsi gani?
18, 19. (a) Kisa cha Samsoni kinatuhakikishia nini? (b) Umefaidikaje kwa kuchunguza mifano ya watu waaminifu ambao wamezungumziwa katika makala hii?
18 Tunategemea roho takatifu ileile ambayo Samsoni alitegemea. Tunafanya hivyo tunapotimiza kazi ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake, yaani, ‘kuwahubiria watu na kutoa ushahidi kamili.’ (Mdo. 10:42) Mgawo huo unahitaji ustadi ambao huenda hatukuzaliwa nao. Tunashukuru kama nini kwamba Yehova anatumia roho yake kutuwezesha kutimiza kazi mbalimbali ambazo tumekabidhiwa! Hivyo, tunapotimiza mgawo wetu, tunaweza kusema hivi kama nabii Isaya: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova mwenyewe amenituma, ndiyo, roho yake.” (Isa. 48:16) Naam, ni roho ya Mungu ambayo imetutuma! Tunatimiza kazi hiyo kwa moyo wetu wote tukiwa na hakika kwamba Yehova atatufanya tustahili zaidi kama Musa, Bezaleli, na Yoshua. Tunauchukua “upanga wa roho, yaani, neno la Mungu,” tukiwa na hakika kwamba atatutia nguvu kama alivyomtia nguvu Gideoni, Yeftha, na Samsoni. (Efe. 6:17, 18) Tukimtegemea Yehova ili atusaidie kushinda vizuizi, tunaweza kuwa na nguvu nyingi za kiroho kama Samsoni alivyokuwa na nguvu nyingi za kimwili.
19 Ni wazi kwamba Yehova anawabariki wale ambao wanaunga mkono kwa ujasiri ibada ya kweli. Tunapofuata mwongozo wa roho takatifu ya Mungu, imani yetu inaongezeka. Kwa hiyo, tutafurahi pia kuchunguza baadhi ya matukio yenye kusisimua yaliyoandikwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kufanya hivyo kutafunua jinsi roho ya Yehova ilivyotenda kazi juu ya watumishi wake waaminifu katika karne ya kwanza, kabla na baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Masimulizi hayo yatazungumziwa katika makala inayofuata.
-
-
Kuongozwa na Roho ya Mungu Katika Karne ya Kwanza na LeoMnara wa Mlinzi—2011 | Desemba 15
-
-
Kuongozwa na Roho ya Mungu Katika Karne ya Kwanza na Leo
‘Roho ileile moja inafanya utendaji huu wote.’—1 KOR. 12:11.
1. Tutazungumzia mambo gani katika funzo hili?
PENTEKOSTE. Neno hilo moja linatukumbusha matukio yenye kusisimua sana! (Mdo. 2:1-4) Kumiminwa kwa roho takatifu wakati huo katika karne ya kwanza kulibadili kabisa jinsi Mungu alivyoshughulika na watumishi wake. Katika makala iliyotangulia, tulichunguza baadhi ya njia ambazo roho ya Mungu iliwawezesha watu waaminifu walioishi zamani kutimiza migawo migumu na yenye maagizo mengi. Lakini kuna tofauti gani kati ya jinsi roho ya Mungu ilivyotenda kazi kabla ya nyakati za Ukristo na jinsi ilivyotenda kazi katika karne ya kwanza? Na Wakristo watafaidikaje kutokana na utendaji wa roho takatifu ya Mungu leo? Acheni tuone.
“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”
2. Maria aliona utendaji wa roho takatifu jinsi gani?
2 Maria alikuwa katika chumba kikubwa cha juu huko Yerusalemu wakati roho takatifu iliyoahidiwa ilipomiminwa. (Mdo. 1:13, 14) Hata hivyo, kwa zaidi ya miongo mitatu kabla ya tukio hilo, Maria alikuwa ameona utendaji wa roho ya Yehova kwa njia za ajabu. Yehova alikuwa amehamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni hadi duniani, na kutunga mimba katika tumbo la uzazi la Maria alipokuwa angali bikira. Mimba aliyokuwa nayo ‘ilitokana na roho takatifu.’—Mt. 1:20.
3, 4. Maria alionyesha mtazamo gani, na tunaweza kumwiga jinsi gani?
3 Kwa nini Maria alipewa pendeleo hilo lisilo na kifani? Baada ya malaika kumweleza mapenzi ya Yehova kumhusu, Maria alisema hivi: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.” (Luka 1:38) Maria aliposema hivyo, alionyesha mtazamo wa moyo ambao Mungu alikuwa tayari ameona. Jinsi alivyoitikia haraka habari hizo ilionyesha kwamba alikuwa tayari kukubali mapenzi ya Mungu katika jambo hilo. Hakuuliza swali lolote kuhusu jinsi ambavyo watu katika jamii wangeona ujauzito wake au ingekuwaje kwa uhusiano wake na mchumba wake. Kwa kusema kwamba yeye ni mtumishi wa hali ya chini kabisa, Maria alionyesha kwamba alimtegemea kikamili Yehova akiwa Bwana wake.
4 Je, nyakati fulani umehisi kwamba umelemewa na mambo fulani magumu au majukumu katika utumishi wa Mungu? Ni vizuri kila mmoja wetu ajiulize hivi: ‘Je, ninamtegemea Yehova kikamili ili aongoze mambo kupatana na mapenzi yake? Je, kweli ninaonyesha kwamba nina roho ya kujitoa kwa hiari?’ Uwe na hakika kwamba Mungu anawapa roho yake watu ambao wanamtegemea kwa moyo wao wote na kutambua mapenzi yake akiwa mwenye enzi kuu.—Mdo. 5:32.
Petro Alisaidiwa na Roho Takatifu
5. Petro aliona roho takatifu ikitenda kazi kwa njia zipi kabla ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.?
5 Kama Maria, mtume Petro alijionea utendaji wenye nguvu wa roho takatifu ya Mungu kabla ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Yesu alikuwa amempa yeye na mitume wengine mamlaka ya kuwafukuza roho waovu. (Marko 3:14-16) Na ingawa Maandiko hayasemi mambo mengi, inaelekea kwamba Petro alitumia mamlaka hayo. Nguvu za Mungu zilionekana pia wakati Yesu alipomruhusu Petro atembee juu ya Bahari ya Galilaya kumwelekea, na Petro akafanya hivyo. (Soma Mathayo 14:25-29.) Ni wazi kwamba Petro aliitegemea roho takatifu ili imsaidie kufanya matendo yenye nguvu. Punde si punde, roho hiyo ingetenda kazi juu ya Petro na wanafunzi wenzake kwa njia mpya.
6. Petro alifanya nini kupitia roho ya Mungu wakati na baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.?
6 Kwenye Sherehe ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Petro na wengine walipewa uwezo wa kimuujiza wa kuzungumza lugha zilizotumiwa na wakaaji wa muda waliotembelea Yerusalemu. Baadaye, Petro aliongoza katika kuhutubia kusanyiko hilo. (Mdo. 2:14-36) Ndiyo, mwanamume huyo ambaye pindi fulani aliogopa au kutenda bila kufikiri alipewa ujasiri wa kutoa ushahidi ingawa alikabili vitisho na mateso. (Mdo. 4:18-20, 31) Mungu alimpa ujuzi kupitia ufunuo. (Mdo. 5:8, 9) Na hata alipewa nguvu za kufufua.—Mdo. 9:40.
7. Ni mafundisho gani ya Yesu ambayo Petro alielewa baada tu ya kutiwa mafuta?
7 Hata kabla ya Pentekoste, Petro alielewa kweli nyingi ambazo Yesu alifundisha. (Mt. 16:16, 17; Yoh. 6:68) Lakini kulikuwa na mambo fulani aliyofundisha Yesu ambayo Petro hakuelewa vizuri kabla ya Pentekoste. Kwa mfano, Petro hakuwa ametambua kwamba siku ya tatu Kristo angefufuliwa akiwa kiumbe wa roho na pia hakuelewa kwamba Ufalme ungekuwa mbinguni. (Yoh. 20:6-10; Mdo. 1:6) Wazo la kwamba wanadamu wangekuwa viumbe wa roho na kutawala katika Ufalme wa mbinguni lilikuwa jipya kwa Petro. Mara tu baada ya yeye mwenyewe kubatizwa kwa roho takatifu na kupewa tumaini la kimbingu, ndipo angeweza kuelewa mafundisho ya Yesu kuhusu mambo hayo.
8. Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wanapata ujuzi gani?
8 Mambo ambayo wanafunzi wa Yesu hawakuelewa mwanzoni walianza kuyaelewa baada ya roho takatifu kumiminwa. Kwa mwongozo wa roho takatifu, waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo waliandika kwa faida yetu mambo mbalimbali ya kustaajabisha yanayohusiana na kusudi la Yehova. (Efe. 3:8-11, 18) Leo, Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wanakula chakula kilekile cha kiroho na kuelewa kweli zilezile. (Yoh. 10:16) Je, unathamini ujuzi na uelewaji wa Neno la Mungu ambao roho takatifu inakuwezesha kupata?
Paulo ‘Alijaa Roho Takatifu’
9. Paulo aliweza kutimiza nini kwa uwezo wa roho takatifu?
9 Mwaka mmoja hivi baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., mtu mwingine alipewa na Mungu zawadi ya roho takatifu. Mtu huyo ni Sauli, ambaye baadaye aliitwa Paulo. Roho ilitenda kazi juu yake kwa njia ambazo zinatunufaisha leo. Mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika vitabu 14 vya Biblia. Na kama ilivyokuwa kuhusiana na Petro, roho ya Mungu ilimwezesha Paulo kuelewa na kuandika kwa njia ya wazi kuhusu tumaini la kupata uhai wa mbinguni usioweza kufa na usioharibika. Roho takatifu ilimwezesha Paulo kuponya, kufukuza roho waovu, na hata kuwafufua wafu! Hata hivyo, nguvu alizopokea kupitia roho takatifu zilitimiza kusudi muhimu zaidi, kusudi ambalo watumishi wote wa Mungu leo wanapata, hata ingawa si kwa njia ya kimuujiza.
10. Roho takatifu iliboreshaje uwezo wa Paulo wa kusema?
10 Paulo, ambaye alikuwa “amejaa roho takatifu,” alimshutumu kwa ujasiri mlozi fulani. Jambo hilo lilikuwa na matokeo makubwa sana juu ya ofisa mkuu wa Saiprasi, ambaye alikuwa akisikiliza mazungumzo hayo yote! Liwali huyo alikubali kweli, ‘alipostaajabishwa na fundisho la Yehova.’ (Mdo. 13:8-12) Ni wazi kwamba Paulo alijua vizuri umuhimu wa roho takatifu ya Mungu inapohusu kusema kweli. (Mt. 10:20) Baadaye alilisihi kutaniko la Efeso litoe dua kwa ajili yake ili apewe “uwezo wa kusema.”—Efe. 6:18-20.
11. Paulo aliongozwaje na roho ya Mungu?
11 Roho takatifu haikumwezesha tu Paulo kusema bali pia, nyakati nyingine, ilimkataza kusema katika maeneo fulani. Alipoanza safari zake za umishonari, Paulo aliongozwa na roho ya Mungu. (Mdo. 13:2; soma Matendo 16:6-10.) Bado Yehova anaongoza kazi ya kuhubiri kupitia roho yake. Kama Paulo, watumishi wote watiifu wa Yehova wanajitahidi kutangaza kweli kwa ujasiri na bidii. Hata ingawa mwongozo wa Mungu hauonekani moja kwa moja leo kama ilivyokuwa katika siku za Paulo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anatumia roho yake takatifu kuhakikisha kwamba watu wanaostahili wanasikia kweli.—Yoh. 6:44.
“Utendaji wa Namna Mbalimbali”
12-14. Je, roho ya Mungu inatenda juu ya watumishi wake wote kwa njia ileile? Eleza.
12 Je, masimulizi yanayoonyesha jinsi Yehova alivyolibariki kutaniko la karne ya kwanza la watiwa-mafuta, yanawatia moyo sana watumishi waliojiweka wakfu kwa Mungu leo? Bila shaka! Kumbuka maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho ambayo aliandikia kutaniko la Korintho kuhusu zawadi za kimuujiza za roho katika siku zake: “Basi kuna zawadi za namna mbalimbali, lakini kuna roho ileile; na kuna huduma za namna mbalimbali, na bado kuna Bwana yuleyule; na kuna utendaji wa namna mbalimbali, na bado ni Mungu yuleyule anayefanya utendaji wote katika watu wote.” (1 Kor. 12:4-6, 11) Ndiyo, roho takatifu inaweza kutenda kazi kwa njia tofauti-tofauti juu ya watumishi mbalimbali wa Mungu kwa kusudi fulani. Kwa kweli, roho takatifu inaweza kutenda juu ya “kundi dogo” na “kondoo wengine” wa Kristo. (Luka 12:32; Yoh. 10:16) Hata hivyo, sikuzote haitendi kwa njia ileile juu ya kila mshiriki wa kutaniko.
13 Kwa mfano, wazee wanawekwa rasmi na roho takatifu. (Mdo. 20:28) Lakini si watiwa-mafuta wote wanaotumikia wakiwa waangalizi katika kutaniko. Tunapaswa kukata kauli gani kuhusu jambo hilo? Kwa ufupi ni kwamba roho ya Mungu inatenda kazi kwa njia mbalimbali juu ya washiriki wa kutaniko.
14 Roho ambayo inatia ndani ya watiwa-mafuta “roho ya kufanywa kuwa wana,” au hisia ya kuwa wana, ndiyo roho ileile ambayo Yehova alitumia kumfufua kutoka kwa wafu Mwana wake mzaliwa-pekee na kumpa uhai usioweza kufa mbinguni. (Soma Waroma 8:11, 15.) Ni roho hiyohiyo ambayo Yehova alitumia kuumba ulimwengu wote. (Mwa. 1:1-3) Kwa roho hiyohiyo takatifu, Yehova alimwezesha Bezaleli astahili kufanya kazi ya pekee katika maskani, alimtia nguvu Samsoni afanye matendo yaliyohitaji nguvu nyingi sana, na kumwezesha Petro kutembea juu ya maji. Kwa hiyo, acheni tusifikiri kwamba kuwa na roho ya Mungu ni sawa na kutiwa mafuta na roho ya Mungu, kwa kuwa kutiwa mafuta ni utendaji mmoja tu wa pekee wa roho. Kutiwa mafuta kwa roho kunategemea uamuzi wa Mungu.
15. Je, watu wataendelea kubatizwa kwa roho takatifu milele? Eleza.
15 Nguvu takatifu ya utendaji ya Mungu imekuwa ikitenda kazi kwa njia mbalimbali juu ya watumishi wake waaminifu muda wote, ndiyo, kwa maelfu ya miaka kabla watu hawajaanza kutiwa mafuta kwa roho. Katika Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., utendaji huo mpya ulianza, lakini hautaendelea milele. Kubatizwa kwa roho kutakoma, lakini roho takatifu itaendelea kutenda kazi juu ya watu wa Mungu ili wafanye mapenzi yake kwa umilele wote.
16. Watumishi wa Mungu wanafanya nini sasa kwa msaada wa roho yake?
16 Ni nini hasa kinachotukia duniani sasa kwa uwezo wa roho takatifu ya Yehova? Andiko la Ufunuo 22:17 linajibu hivi: “Na roho na bibi-arusi huendelea kusema: ‘Njoo!’ Na yeyote anayesikia na aseme: ‘Njoo!’ Na yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.” Wakichochewa na roho ya Mungu, leo Wakristo wanampa mwaliko wa Yehova unaookoa uhai, mtu “yeyote anayetaka” kukubali maji ya uzima. Wakristo watiwa-mafuta wanaongoza katika kufanya hivyo. Hata hivyo, washiriki wa kondoo wengine wanajiunga nao katika kutoa mwaliko huo. Jamii zote mbili zinashirikiana na roho ileile takatifu kutimiza kazi hiyo. Washiriki wa jamii zote mbili wameonyesha wakfu wao kwa Yehova kwa kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mt. 28:19) Na wote wanatii mwongozo wa roho ya Mungu katika maisha yao, na kuiruhusu itokeze ndani yao tunda lake. (Gal. 5:22, 23) Kama watiwa-mafuta, kondoo wengine wanaruhusu roho ya Mungu iwasaidie. Kwa msaada wa roho hiyo, wanafanya yote wanayoweza kutimiza matakwa ya Yehova ya utakatifu.—2 Kor. 7:1; Ufu. 7:9, 14.
Endelea Kuomba ili Upewe Roho Takatifu
17. Tunaweza kuthibitishaje kwamba tuna roho ya Mungu?
17 Kwa hiyo, hata kama una tumaini kutoka kwa Mungu la kuishi milele mbinguni au duniani, Yehova anaweza kukupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili uweze kudumisha utimilifu wako na kupokea thawabu yako. (2 Kor. 4:7) Huenda ukadhihakiwa kwa sababu ya kuendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme. Lakini kumbuka kwamba ‘ikiwa unashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, wewe ni mwenye furaha, kwa sababu ile roho ya utukufu, yaani roho ya Mungu, inatulia juu yako.’—1 Pet. 4:14.
18, 19. Yehova atakusaidiaje kupitia roho yake takatifu, na umeazimia kufanya nini kuhusiana na hilo?
18 Roho takatifu ni zawadi ya bure ambayo Mungu anawapa wale ambao wanaitafuta kwa unyoofu. Inaweza kuzidisha si uwezo wako tu bali pia tamaa yako ya kufanya yote unayoweza katika utumishi wake. “Mungu ndiye ambaye, kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” Zawadi hiyo ya roho takatifu ambayo ni yenye thamani, pamoja na jitihada zetu nyingi za kuendelea “kulishika sana neno la uzima,” zitatuwezesha ‘kuendelea kuufanyia kazi wokovu wetu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.’—Flp. 2:12, 13, 16.
19 Basi, ukiwa na uhakika kamili katika roho ya Mungu, timiza kila mgawo kwa moyo wako wote, uwe stadi katika mgawo unaopewa, na umtegemee Yehova ili akusaidie. (Yak. 1:5) Atakupa msaada unaohitaji ili uelewe Neno lake, ukabiliane na matatizo ya maisha, na kuhubiri habari njema. ‘Endelea kuomba, nawe utapewa; endelea kutafuta, nawe utapata; endelea kupiga hodi, nawe utafunguliwa,’ na hilo linatia ndani kupokea roho takatifu. (Luka 11:9, 13) Kwa kweli, endelea kutoa dua kwa Yehova ili uwe kama watumishi waaminifu wa leo na wa kale ambao waliongozwa na roho takatifu ya Mungu.
-