-
Yehova Hubariki Ibada SafiUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Sura Ya Ishirini Na Saba
Yehova Hubariki Ibada Safi
1. Ni vichwa gani vinavyokaziwa katika sura ya mwisho ya Isaya, na ni maswali gani yanayojibiwa?
KATIKA sura ya mwisho ya Isaya, baadhi ya vichwa vikuu vya kitabu hiki cha kiunabii vinafikishwa kwenye upeo wenye mkazo mwingi, na maswali kadhaa muhimu yanajibiwa. Miongoni mwa vichwa vinavyokaziwa ni kutukuka kwa Yehova, chuki yake kuelekea unafiki, azimio lake la kuwaadhibu waovu, na upendo na hangaiko lake kuwaelekea waaminifu. Isitoshe, maswali yafuatayo yanajibiwa: Ni nini hutofautisha ibada ya kweli na ile ya uwongo? Tunaweza kuwaje na uhakika kwamba Yehova atawalipa wanafiki adhabu yao kwa sababu wanasingizia kuwa watakatifu huku wakiwakandamiza watu wa Mungu? Na Yehova atawabarikije wale wanaobaki wakiwa waaminifu kwake?
Ufunguo wa Ibada Safi
2. Yehova anatoa tamko gani kuhusu fahari yake, lakini tamko hilo halina maana gani?
2 Kwanza, unabii unakazia fahari ya Yehova: “BWANA asema hivi, Mbingu ni kiti changu cha enzi, na dunia ni mahali [“kibago,” “NW”] pa kuweka miguu yangu; mtanijengea nyumba ya namna gani? na mahali pangu pa kupumzikia ni mahali gani?” (Isaya 66:1) Watu fulani wanaamini kwamba nabii anawavunja moyo Wayahudi wasimjengee Yehova hekalu tena wakati taifa litakaporudishwa kwenye nchi yao. Lakini si hivyo; Yehova mwenyewe atatoa amri hekalu lijengwe upya. (Ezra 1:1-6; Isaya 60:13; Hagai 1:7, 8) Basi je, kifungu hicho kina maana gani?
3. Kwa nini inafaa kwamba dunia inaelezewa kuwa “kibago” cha Yehova?
3 Kwanza, ingefaa tufikirie ni kwa nini dunia inatajwa kuwa “kibago” cha Yehova. Huo si usemi wa madharau. Kati ya yale mabilioni ya nyota na maumbo mengine yaliyo katika ulimwengu mzima, ni dunia tu inayopewa jina hilo la kipekee. Sayari yetu itabaki milele bila nyingine ya kufanana nayo, kwa maana hapa ndipo Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova alipolipia ile fidia, na hapa ndipo Yehova atakapotetea ustahili wa enzi yake kuu kupitia Ufalme wake wa Kimesiya. Inafaa kama nini kwamba dunia inaitwa kibago cha Yehova! Huenda mfalme akatumia kibago kama kikanyagio cha kupanda kiti chake kilichoinuka, na baada ya hapo akitumie kupumzisha miguu juu yake.
4. (a) Kwa nini haiwezekani jengo lolote duniani liwe mahali pa kupumzikia pa Yehova Mungu? (b) Maneno “vitu hivi vyote” yana maana gani, na ni lazima tukate kauli gani juu ya ibada ya Yehova?
4 Bila shaka, mfalme hafanyi makao yake juu ya kibago chake, wala makao ya Yehova hayako katika dunia hii. Kwani, hata mbingu halisi zilizotandaa sana hazimtoshi! Sembuse jengo la kawaida tu hapa duniani kumtosha Yehova kiasi cha kuweza kuwa nyumba yake. (1 Wafalme 8:27) Kiti cha ufalme cha Yehova na mahali pake pa kupumzikia zimo katika makao ya roho, na hiyo ndiyo maana ya neno “mbingu” lililotumiwa kwenye Isaya 66:1. Mstari unaofuata unaeleza linalomaanishwa hasa: “Maana mkono wangu ndio uliofanya hivi vyote, vitu hivi vyote vikapata kutokea, asema BWANA.” (Isaya 66:2a) Ebu wazia Yehova akinyoosha mkono kwa ishara ya mapana ili kuonyesha “vitu hivi vyote,” maana yake kila kitu mbinguni na duniani. (Isaya 40:26; Ufunuo 10:6) Kwa kuwa yeye ndiye Muumba Mkuu wa ulimwengu mzima, anastahili kufanyiwa mambo mengi kuliko kutoa jengo moja tu liwe lake. Anastahili mengi kuliko kuabudiwa kijuu-juu tu.
5. Tunaonyeshaje kwamba sisi ni ‘wenye kuteseka na wenye roho iliyopondeka’?
5 Ni ibada ya aina gani inayomfaa Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Mzima? Yeye mwenyewe anatuambia hivi: “Lakini, mtu huyu ndiye nitakayemwangalia, mtu aliye mnyonge [“mwenye kuteseka,” “NW”], mwenye roho iliyopondeka, atetemekaye asikiapo neno langu.” (Isaya 66:2b) Ndiyo, ni muhimu mwabudu awe na mtazamo wa moyoni unaofaa ili ibada yake iweze kuwa safi. (Ufunuo 4:11) Mwabudu wa Yehova ni lazima ‘awe mwenye kuteseka na mwenye roho iliyopondeka.’ Je, inamaanisha kwamba Yehova anataka tukose furaha? La, yeye ndiye “Mungu mwenye furaha,” na anataka waabudu wake wawe na shangwe pia. (1 Timotheo 1:11; Wafilipi 4:4) Hata hivyo, sisi sote hutenda dhambi mara nyingi, na tusizione dhambi zetu kama mchezo tu. Tunapaswa ‘kuteswa’ nazo, kuhuzunika kwamba tumeikosa shabaha ya viwango vya Yehova vya uadilifu. (Zaburi 51:17) Tunahitaji kuonyesha kwamba ‘tuna roho iliyopondeka’ kwa kutubu, kupigana na maelekeo yetu yenye dhambi, na kumtolea Yehova sala ya kuomba msamaha.—Luka 11:4; 1 Yohana 1:8-10.
6. Ni katika maana gani waabudu wa kweli wanapaswa ‘kutetemeka wasikiapo neno la Mungu’?
6 Kwa kuongezea, Yehova huwatafuta wale ‘watetemekao wasikiapo neno lake.’ Je, hii inamaanisha kwamba anataka tutikisike kwa hofu kila tunaposikia matamko yake? Sivyo, bali anatutaka tuyaone maneno yake kwa kicho na staha nyingi. Tunatafuta shauri lake kwa moyo mweupe, tukilitumia ili litupe mwongozo katika shughuli zote za maisha. (Zaburi 119:105) Tunaweza pia ‘kutetemeka’ katika maana ya kuhofu tusije tukakosa kumtii Mungu, kuichafua kweli yake kwa mapokeo ya kibinadamu, au kuiona kama mchezo tu. Mtazamo huo wa unyenyekevu ni muhimu katika ibada safi—lakini inahuzunisha kwamba ni watu wachache walio na mtazamo huo katika ulimwengu wa leo.
Yehova Anachukia Ibada ya Kiunafiki
7, 8. Yehova anaionaje ibada ya kidesturi ya wanafiki wa kidini?
7 Wakati Isaya anapotafakari juu ya watu walioishi wakati mmoja naye, anajua sana kwamba ni wachache wenye mwelekeo ambao Yehova huutafuta katika waabudu wake. Kwa sababu hiyo, Yerusalemu lenye uasi-imani linaistahili ile hukumu inayokaribia kulipata. Angalia jinsi Yehova anavyoiona ibada inayoendelea ndani ya jiji hilo: “Yeye achinjaye ng’ombe ni kama yeye amwuaye mtu; na yeye atoaye dhabihu ya mwana-kondoo ni kama yeye avunjaye shingo ya mbwa; na yeye atoaye matoleo ni kama yeye atoaye damu ya nguruwe; na yeye afukizaye uvumba ni kama yeye abarikiye sanamu; naam, wamezichagua njia zao wenyewe, na nafsi zao zafurahia machukizo yao.”—Isaya 66:3.
8 Maneno haya yanatukumbusha maneno ya Yehova yaliyoandikwa katika sura ya kwanza ya Isaya. Hapo Yehova aliwaambia watu wake wapotovu kwamba, licha ya yeye kutopendezwa na vitendo vyao vya kufuata desturi rasmi tu ya ibada, kwa kweli vitendo hivyo vilizidisha pia hasira yake ya uadilifu kwa sababu waabudu hao walikuwa wanafiki. (Isaya 1:11-17) Vivyo hivyo, sasa Yehova anafananisha matoleo yao na vitendo vya uhalifu mbaya sana. Hawawezi kuutuliza moyo wa Yehova kwa kumtolea dhabihu ya ng’ombe dume wa bei kubwa, kama vile tu wasivyoweza kuutuliza kwa kuua binadamu kimakusudi! Dhabihu nyingine zinafananishwa na kutoa toleo la mbwa au nguruwe, wanyama wachafu chini ya Sheria ya Kimusa, tena wasiofaa kamwe kutolewa kama dhabihu. (Mambo ya Walawi 11:7, 27) Je, Yehova anauachilia unafiki huo wa kidini bila kutoa adhabu?
9. Wayahudi walio wengi wameitikiaje vikumbusha vya Yehova kupitia Isaya, na kutakuwa na matokeo gani yasiyoepukika?
9 Sasa Yehova anasema hivi: “Mimi nami nitachagua mapigo yao, nitaleta hofu zao juu yao; kwa sababu nilipoita, hawakuitika;na niliponena,hawakusikia; bali walifanyayaliyo maovu machoni pangu, na kuyachagua nisiyoyafurahia.” (Isaya 66:4) Bila shaka Isaya anaweza kuyatamka maneno haya kwa usadikisho wa moyoni. Kwa muda wa miaka mingi amekuwa chombo cha Yehova, huku ‘akiita’ watu Wake na ‘kunena’ nao. Nabii anajua sana kwamba, kwa ujumla hakuna mtu amekuwa akisikiliza. Kwa sababu wameendelea kutenda mabaya, hawawezi kukosa adhabu. Kweli Yehova atachagua adhabu yao na kuwaletea watu wake waasi-imani matukio yenye kutisha.
10. Shughuli za Yehova na Yuda zinatuonyesha kwamba yeye ana maoni gani kuhusu Jumuiya ya Wakristo?
10 Vivyo hivyo, Jumuiya ya Wakristo ya kisasa imefanya mambo ambayo Yehova hayafurahii. Ibada ya sanamu inasitawi katika makanisa yake. Falsafa na mapokeo yasiyo ya Kimaandiko yanatukuzwa kwenye vijukwaa vya makanisa. Na jumuiya hiyo imeng’ang’ania kupata mamlaka ya kisiasa, na kwa njia hiyo ikadidimia hata zaidi katika uhusiano wa kuzini na mataifa ya ulimwengu. (Marko 7:13; Ufunuo 18:4, 5, 9) Kama vile ilivyokuwa kwa habari ya Yerusalemu la kale, Jumuiya ya Wakristo itapatwa na kitu cha kutia “hofu,” yaani malipo ya adhabu yaliyo haki yake, ipende isipende. Mojawapo ya sababu zitakazofanya ipate adhabu hakika ni jinsi imewatendea watu wa Mungu.
11. (a) Ni nini kinachoongezea dhambi ya waasi-imani katika siku za Isaya? (b) Watu wanaoishi wakati mmoja na Isaya wanawatupaje waaminifu ‘kwa ajili ya jina la Mungu’?
11 Isaya anaendelea kusema hivi: “Lisikilizeni neno la BWANA, ninyi mtetemekao kwa sababu ya neno lake; Ndugu zenu wawachukiao ninyi, waliowatupa kwa ajili ya jina langu, wamesema, Na atukuzwe BWANA, tupate kuiona furaha yenu; lakini watatahayarika.” (Isaya 66:5) “Ndugu” za Isaya, ambao ni wananchi wenzake hasa, ndio wanaopaswa kubeba daraka walilopewa na Mungu la kumwakilisha Yehova Mungu na kutii enzi yake kuu. Wameshindwa kufanya hivyo wakawa na dhambi nzito kweli kweli. Lakini kinachoongezea dhambi yao ni kwamba wanawachukia wanaume walio waaminifu na wanyenyekevu, kama vile Isaya. Waasi-imani hao wanawachukia waaminifu na kuwatupa kwa sababu wanamwakilisha Yehova Mungu kwa njia ya kweli. Ni katika maana hiyo kwamba waaminifu hao wanatupwa ‘kwa ajili ya jina la Mungu.’ Wakati huo huo, watumishi hawa wa Yehova wasio wa kweli wanadai kumwakilisha, wakijifanya eti wanamcha Mungu sana kwa kutumia maneno yanayosikika kama ya kidini, kama vile ‘Yehova na atukuzwe!’a
12. Ni baadhi ya mifano gani inayoonyesha jinsi wanafiki wa kidini wanavyonyanyasa watumishi waaminifu wa Yehova?
12 Chuki ambayo dini ya uwongo inayo kuelekea wale wanaoshikamana na ibada safi haikuanza sasa hivi. Chuki hiyo inazidi tu kutimiza unabii ulio kwenye Mwanzo 3:15, uliotabiri uadui wa muda mrefu kati ya mbegu ya Shetani na Mbegu ya mwanamke wa Mungu. Yesu aliwaambia wafuasi wake watiwa-mafuta katika karne ya kwanza kwamba wao pia wangeteseka mikononi mwa wananchi wenzao—watupwe nje ya masinagogi na kunyanyaswa hadi kifo. (Yohana 16:2) Namna gani nyakati za kisasa? “Siku za mwisho” zilipokuwa zikianza, watu wa Mungu waliona kwamba mnyanyaso kama huo ungetokea siku za usoni. (2 Timotheo 3:1) Huko nyuma mwaka wa 1914, gazeti Mnara wa Mlinzi lilinukuu Isaya 66:5, likisema hivi: “Karibu minyanyaso yote ambayo imewapata watu wa Mungu imetoka kwa watu wanaodai eti ni Wakristo.” Makala hiyo hiyo ilisema hivi: “Hatujui watafika wapi na mambo hayo, kwani huenda hata wakaruka mipaka katika siku zetu—kutuangamiza katika mambo ya kijamii, kutuangamiza kidini, na labda hata kutuangamiza kimwili.” Maneno hayo yalikuwa kweli kama nini! Muda mfupi baada ya maneno hayo kuchapishwa, mnyanyaso wenye kuchochewa na makasisi uliwaka kweli kweli wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza. Lakini Jumuiya ya Wakristo ikaaibishwa, kama ilivyotabiriwa. Jinsi gani?
Kurudishwa Upesi Sana na kwa Ghafula
13. “Sauti ya fujo” ni nini katika utimizo wa kwanza?
13 Isaya anatoa unabii hivi: “Sauti ya fujo itokayo mjini! Sauti itokayo hekaluni! Sauti ya BWANA awalipaye adui zake adhabu!” (Isaya 66:6) Katika utimizo wa kwanza wa maneno hayo, ‘mji’ ni Yerusalemu, ambamo mna hekalu la Yehova. “Sauti ya fujo” inaleta wazo la msukosuko wa vita, unaosikiwa katika jiji wakati majeshi ya Babiloni yanapovamia mji huo na kuushambulia mwaka wa 607 K.W.K. Namna gani utimizo wa kisasa?
14. (a) Malaki alitabiri nini kuhusu kuja kwa Yehova kwenye hekalu Lake? (b) Kulingana na unabii wa Ezekieli, matokeo yalikuwa nini Yehova alipokuja kwenye hekalu lake? (c) Yehova na Yesu walilichunguza hekalu la kiroho wakati gani, na matokeo yakawa nini kwa wenye kudai eti wanawakilisha ibada safi?
14 Maneno haya katika Isaya yanapatana na matamko mengine mawili ya kiunabii. Tamko moja ni lile lililoandikwa kwenye Ezekieli 43:4, 6-9 na lile jingine liko kwenye Malaki 3:1-5. Ezekieli na hata Malaki wanautabiri wakati ambao Yehova Mungu anakuja kwenye hekalu lake. Unabii wa Malaki unaonyesha kwamba Yehova anakuja kuchunguza nyumba yake ya ibada safi na kutenda kama Mtakasaji, akiwakataa wale wanaomwakilisha vibaya. Njozi ya Ezekieli inaonyesha Yehova akiingia katika hekalu na kudai kwamba alama zote za ukosefu wa adili na za ibada ya sanamu ziondolewe.b Katika utimizo wa kisasa wa unabii huo mbalimbali, jambo muhimu la kiroho lilitokea mwaka wa 1918 kuhusiana na ibada ya Yehova. Ushuhuda unaonyesha kwamba Yehova na Yesu waliwachunguza wale wote wale waliodai kuwakilisha ibada safi. Matokeo ya uchunguzi huo ni kwamba, mwishowe Jumuiya ya Wakristo yenye ufisadi ilitupiliwa mbali. Uchunguzi huo ulitokeza kipindi kifupi cha kuwatakasa watiwa-mafuta wa Kristo, kisha wakarudishiwa upesi sana hali nzuri ya kiroho mwaka wa 1919.—1 Petro 4:17.
15. Ni uzazi gani unaotabiriwa, na unatimizwaje mwaka wa 537 K.W.K.?
15 Hali hiyo ya kurudishwa inaonyeshwa kwa kufaa sana katika mistari ifuatayo ya Isaya: “Kabla hajaona utungu alizaa; kabla maumivu yake hayajampata, alizaa mtoto mwanamume. Ni nani aliyesikia neno kama hili? Ni nani aliyeona mambo kama haya? Je! nchi yaweza kuzaliwa siku moja? Taifa laweza kuzaliwa mara? Maana Sayuni, mara alipoona utungu, alizaa watoto wake.” (Isaya 66:7, 8) Maneno haya yanatimizwa mara ya kwanza kwa njia ya kusisimua kuhusiana na Wayahudi wahamishwa walioko Babiloni. Sayuni, au Yerusalemu, anaonyeshwa tena kuwa mwanamke anayezaa. Lakini huo ni uzazi wa kushangaza kama nini! Unafanyika upesi sana, ghafula sana, hata kabla ya utungu kuanza! Maelezo ya tukio hilo yanafaa sana. Kuzaliwa kwa watu wa Mungu mwaka wa 537 K.W.K. wakiwa taifa la kipekee kunatukia upesi sana, ghafula sana, hivi kwamba kunaonekana kama mwujiza. Kwani, muda unaopita kuanzia wakati ambao Koreshi anawaweka huru Wayahudi watoke utekwani hadi wakati ambao mabaki waaminifu wanakuwa wamerudia nchi yao, ni miezi michache tu! Hali hiyo inatofautiana kama nini na matukio yaliyotangulia kuzaliwa kwa taifa la Israeli mara ya kwanza! Mwaka wa 537 K.W.K., hakuna haja ya kumwomba mtawala mpinzani atoe uhuru wa kuondoka, hakuna haja ya kukimbia jeshi lenye uadui, hakuna haja ya kukaa-kaa jangwani muda wa miaka 40.
16. Katika utimizo wa kisasa wa Isaya 66:7, 8, Sayuni inafananisha nini, na wazao wake wamezaliwaje upya?
16 Katika utimizo wa kisasa, Sayuni inawakilisha “mwanamke” wa kimbingu wa Yehova, yaani tengenezo lake la kimbingu la viumbe-roho. Mwaka wa 1919 “mwanamke” huyu alishangilia kuona kuzaliwa kwa wana wake watiwa-mafuta duniani ili wawe watu waliopangwa kitengenezo, maana yake “taifa.” Tukio hilo la kuzaliwa upya lilifanyika upesi sana, tena kwa ghafula.c Katika muda wa miezi michache tu, watiwa-mafuta wakiwa kikundi walitoka katika hali ya kutotenda iliyo kama kifo, wakaanza maisha ya utendaji wa kujibidiisha sana katika “nchi” yao, yale makao yao ya utendaji wa kiroho waliyopewa na Mungu. (Ufunuo 11:8-12) Kufikia miezi ya mwishoni mwa mwaka wa 1919, hata walitangaza kuchapishwa kwa gazeti jipya la kukamilishana na Mnara wa Mlinzi. Kichapo hicho kipya kiliitwa The Golden Age (sasa Amkeni!), na kilikuwa ushuhuda wa kwamba watu wa Mungu wametiwa nguvu mpya, wakiwa wamepangwa tena kuwa tengenezo kwa ajili ya utumishi.
17. Yehova anawahakikishiaje watu wake kwamba hakuna cha kumzuia asitimize kusudi lake kuhusiana na Israeli wa kiroho?
17 Katika ulimwengu mzima hakuna nguvu yoyote ambayo ingeweza kuzuia uzaliwa huo mpya. Mstari unaofuata unasema lilo hilo: “Je! mimi nilete wana karibu na kuzaliwa, nisizalishe? asema BWANA; mimi nizalishaye, je! nilifunge tumbo? asema Mungu wako.” (Isaya 66:9) Sawa na vile hatua za kuzaa mtoto zisivyoweza kuepukwa zikiisha kuanza, ndivyo kuzaliwa upya kwa Israeli wa kiroho hakungeweza kuzuiliwa baada ya kuanza. Ni kweli kwamba upinzani ulikuwako, na yaelekea kwamba kutakuwako upinzani zaidi wakati ujao. Lakini ni Yehova peke yake aliye na uwezo wa kukomesha kitu anachokianzisha. Hata hivyo, yeye hafanyi hivyo kamwe! Ingawa hivyo, Yehova anawatendeaje watu wake waliotiwa nguvu mpya?
Utunzaji Mwororo wa Yehova
18, 19. (a) Yehova anatumia mfano gani wenye kugusa moyo, nao unatumikaje kuwahusu watu wake walio uhamishoni? (b) Leo mabaki watiwa-mafuta wamefaidikaje na lishe na utunzaji wenye upendo?
18 Mistari minne inayofuata inaufafanua utunzaji mwororo wa Yehova kwa njia ya kuvutia. Kwanza, Isaya anasema hivi: “Furahini pamoja na Yerusalemu, shangilieni kwa ajili yake, ninyi nyote mmpendao; furahini pamoja naye kwa furaha, ninyi nyote mliao kwa ajili yake; mpate kunyonya, na kushibishwa kwa maziwa ya faraja zake, mpate kukama, na kufurahiwa kwa wingi wa utukufu wake.” (Isaya 66:10, 11) Hapa Yehova anatumia mfano wa mwanamke anayenyonyesha kitoto chake kichanga. Mtoto mchanga anapoumwa na njaa, kazi yake ni kulia-lia tu. Lakini anapoletwa karibu na matiti ya mama yake anyonye, sasa yeye huacha kihoro chake na kutosheka akiwa na furaha kamili. Vivyo hivyo, mabaki ya Wayahudi waaminifu walioko Babiloni watatolewa haraka haraka katika hali ya kuomboleza waingie katika hali ya furaha na uradhi ufikapo wakati wao wa kukombolewa na kurudishwa. Watakuwa na shangwe. Yerusalemu litapewa utukufu tena, huku likijengwa upya na kukaliwa upya. Na utukufu wa jiji hilo utaenea uangaze juu ya wakaaji wake wote waaminifu. Kwa mara nyingine, watalishwa kiroho kupitia ukuhani wenye utendaji wa bidii.—Ezekieli 44:15, 23.
19 Israeli wa kiroho pia alibarikiwa kwa lishe tele baada ya kurudishwa mwaka wa 1919. Tangu wakati huo, chakula cha kiroho kinachotolewa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” kimekuwa kikitiririka kwa ukawaida. (Mathayo 24:45-47) Kweli huu umekuwa wakati wa faraja na shangwe kwa mabaki watiwa-mafuta. Lakini kumekuwako na baraka nyingine nyingi.
20. Yerusalemu limebarikiwaje kwa “kijito kifurikacho,” nyakati za kale na za kisasa pia?
20 Unabii unaendelea kusema hivi: “BWANA asema hivi, Tazama, nitamwelekezea amani kama mto, na utukufu wa mataifa kama kijito kifurikacho, nanyi mtapata kunyonya; mtabebwa [“ubavuni,” “NW”]; na juu ya magoti mtabembelezwa.” (Isaya 66:12) Hapa mfano wa kunyonyesha umeunganishwa na wazo la mtiririko wa baraka nyingi, yaani “mto” na “kijito kifurikacho.” Licha ya kubarikiwa kwa amani tele kutoka kwa Yehova, Yerusalemu litabarikiwa pia kwa “utukufu wa mataifa,” unaowatiririkia watu wa Mungu na kuwabariki. Hii inamaanisha kwamba watu wa mataifa watafurika kuwaendea watu wa Yehova. (Hagai 2:7) Katika utimizo wa kale, ni kweli kwamba watu kadhaa wa mataifa mbalimbali walijiunga na Israeli wakawa waongofu Wayahudi. Hata hivyo, utimizo mkubwa zaidi umetukia wakati wetu wenyewe ambapo “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha”—ambao kwa kweli ni miminiko kubwa sana la wanadamu—wamejiunga na mabaki ya Wayahudi wa kiroho.—Ufunuo 7:9; Zekaria 8:23.
21. Ni faraja ya aina gani inayotabiriwa kwa maneno ya ufananisho yenye kuvutia?
21 Andiko la Isaya 66:12 pia linataja semi zitumiwazo na mama-mzazi kuonyesha upendo. Semi hizo zinahusu kubembeleza mtoto kwa kumpakata magotini na kumbeba kwa kumweka ubavuni. Katika mstari unaofuata, wazo la namna hiyo linaelezwa kwa maoni tofauti yanayostahili kufikiriwa. “Mfano wa mtu ambaye mama yake amfariji, ndivyo nitakavyowafariji ninyi; nanyi mtafarijiwa katika Yerusalemu.” (Isaya 66:13) Sasa mtoto huyo ni “mtu,” mtu mzima. Lakini mama yake hajaacha kutamani kumfariji wakati wa msononeko.
22. Yehova anaonyeshaje wororo na uthabiti wa upendo wake?
22 Kwa njia hiyo ya kuvutia, Yehova anaonyesha jinsi anavyowapenda watu wake kwa uthabiti na wororo mwingi. Hata upendo imara kabisa wa mama-mzazi unakuwa kitu kidogo sana unapolinganishwa na upendo wa kina kirefu ambao Yehova huwaonyesha watu wake waaminifu. (Isaya 49:15) Ni muhimu kama nini Wakristo wote waonyeshe sifa hiyo ya Baba yao wa kimbingu! Mtume Paulo aliionyesha, na hivyo akawaachia wazee wa kutaniko la Kikristo mfano mzuri. (1 Wathesalonike 2:7) Yesu alisema kwamba upendo wa kidugu ndio ungekuwa alama kuu ya kutambulisha wafuasi wake.—Yohana 13:34, 35.
23. Simulia hali yenye furaha ya watu wa Yehova waliorudishwa.
23 Yehova huonyesha upendo wake kwa matendo. Hivyo, yeye anaendelea kusema hivi: “Nanyi mtaona, na mioyo yenu itafurahi, na mifupa yenu itasitawi kama majani mabichi; na mkono wa BWANA utajulikana, uwaelekeao watumishi wake, naye atawaonea adui zake ghadhabu.” (Isaya 66:14) Mtaalamu fulani wa sarufi ya Kiebrania anadokeza kwamba usemi “nanyi mtaona” una wazo la kwamba popote pale ambapo wahamishwa wanaorudi wanatazama katika nchi yao iliyorudishwa, “sasa macho yao yanaona shangwe tupu.” Watashangilia vilivyo, wasisimuke hata midomo ibaki wazi kwa kuona kwamba wamerudishwa kwenye nchi yao kipenzi. Watahisi kurudishiwa nguvu za ujana, kana kwamba mifupa yao imeanza kuimarika tena, wapate nguvu mpya kama nyasi wakati wa masika. Watu wote watajua kwamba hali hii yenye baraka haikutokea kwa jitihada ya mwanadamu yeyote, bali kwamba imesababishwa na ‘mkono wa Yehova.’
24. (a) Wewe unakata kauli gani unapoyafikiria matukio yanayowahusu watu wa Yehova leo? (b) Tunapaswa kufanya azimio gani?
24 Je, wewe unatambua wakati mkono wa Yehova unapofanya kazi miongoni mwa watu wake leo? Hakuna mwanadamu yeyote yule ambaye angaliweza kuirudisha ibada safi. Hakuna mwanadamu angaliweza hata kidogo kusababisha mamilioni ya watu wa thamani kubwa wamiminike kutoka katika mataifa yote kujiunga na mabaki waaminifu katika nchi yao ya kiroho. Ni Yehova Mungu peke yake awezaye kufanya hayo. Maonyesho hayo ya upendo wa Yehova yanatupa sisi sababu ya kuwa na shangwe nyingi sana. Tusithubutu kamwe kuuchezea-chezea upendo wa Yehova. Na tuendelee ‘kutetemeka tusikiapo neno lake.’ Na tuazimie kuishi kwa kufuata kanuni za Biblia na kufurahia kumtumikia Yehova.
[Maelezo ya Chini]
a Leo watu wengi katika Jumuiya ya Wakristo wanakataa kulitumia jina la Mungu la kibinafsi, na hata wanaliondoa katika tafsiri nyingi sana za Biblia. Wengine huwadhihaki vikali watu wa Mungu kwa sababu wanatumia jina lake la kibinafsi. Na bado, watu mmoja-mmoja kati yao hujionyesha kuwa wanadini wanaomcha Mungu kwa kutumia neno “Haleluya,” maana yake “Sifuni Yah.”
b Usemi “mizoga ya wafalme wao,” uliotumiwa kwenye Ezekieli 43:7, 9, humaanisha sanamu. Viongozi na watu wa Yerusalemu walio waasi walikuwa wamelichafua hekalu la Mungu kwa sanamu na, kwa njia hiyo wakazifanya kuwa wafalme.
c Uzaliwa unaotajwa hapa kwa njia ya unabii sio ule ule unaoelezwa kwenye Ufunuo 12:1, 2, 5. Katika sura hiyo ya Ufunuo, “mwana, wa kiume,” anafananisha Ufalme wa Kimesiya, ulioanza kazi mwaka wa 1914. Hata hivyo, “mwanamke” wa unabii anayetajwa katika maandiko hayo mawili ni yule yule.
-
-
Nuru kwa MataifaUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
Sura Ya Ishirini Na Nane
Nuru kwa Mataifa
1, 2. Kwa nini nuru ni muhimu, na leo ni giza la namna gani linaloifunika dunia?
YEHOVA ndiye Chanzo cha nuru, yule “awapaye watu jua, ili kuwa nuru wakati wa mchana, na amri za mwezi na nyota, ili kuwa nuru wakati wa usiku.” (Yeremia 31:35) Sababu hiyo peke yake inatosha kufanya Yehova astahili kutambuliwa kuwa ndiye Chanzo cha uhai, kwani hakuna uhai bila nuru. Kama dunia haingepashwa joto na nuru ya jua daima, haingewezekana tuendelee kuwa hai. Sayari yetu dunia ingekuwa isiyokalika.
2 Kwa hiyo, inatupasa tuhangaishwe sana na wazo la kwamba, Yehova alipotazama mbele kwenye siku zetu, alitabiri wakati wa giza wala si wa nuru. Isaya alipuliziwa kuandika hivi: “Tazama, giza litaifunika dunia, na giza kuu litazifunika kabila za watu.” (Isaya 60:2) Bila shaka, maneno hayo yalihusiana na giza la kiroho, wala si giza halisi, lakini yana uzito usiopasa kupuuzwa. Hatimaye, inakuwa haiwezekani kwa wale wasio na nuru ya kiroho kuendelea kuwa hai, sawa na vile inavyokuwa kwa wale wasioweza kupata nuru ya jua.
3. Tunaweza kupata nuru wapi nyakati hizi za giza?
3 Nyakati hizi za giza, tusithubutu kamwe kuipuuza nuru ya kiroho ambayo Yehova ametupatia leo. Ni muhimu tutegemee Neno la Mungu ili lituangazie njia yetu, tukiisoma Biblia kila siku ikiwezekana. (Zaburi 119:105) Mikutano ya Kikristo inatuandalia nafasi za kutiana moyo ili tubaki katika “njia ya wenye haki.” (Mithali 4:18; Waebrania 10:23-25) Nguvu tunazopata kwa kujifunza Biblia na kutokana na ushirika mzuri wa Kikristo hutusaidia tuepuke kupotelea ndani ya giza la hizi “siku za mwisho,” ambalo litafikia upeo katika ‘siku ya hasira ya Yehova.’ (2 Timotheo 3:1; Sefania 2:3) Siku hiyo inakuja mbio-mbio! Hakika itakuja, sawasawa na vile siku nyingine kama hiyo ilivyowajilia wakaaji wa Yerusalemu la kale.
Yehova ‘Ateta’
4, 5. (a) Yehova anavamia Yerusalemu jinsi gani? (b) Kwa nini tunaweza kukata kauli kwamba ni idadi ndogo tu kwa kulinganishwa ambayo itauokoka uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K.? (Ona kielezi-chini.)
4 Katika mistari ile inayoumalizia unabii wa Isaya wenye kusisimua, Yehova anatoa maelezo dhahiri sana kuhusu matukio yatakayoelekeza kwenye siku ya hasira yake. Tunasoma hivi: “BWANA atakuja na moto, na magari yake ya vita kama upepo wa kisulisuli; ili atoe malipo ya ghadhabu yake kwa moto uwakao, na maonyo yake kwa miali ya moto. Kwa maana BWANA atateta na wote wenye mwili, kwa moto na kwa upanga wake; nao watakaouawa na BWANA watakuwa wengi.”—Isaya 66:15, 16.
5 Maneno hayo yanapasa kuwasaidia watu wa siku za Isaya wautambue uzito wa hali yao. Wakati unakaribia ambapo Wababiloni wenye kuleta hukumu ya Yehova watavamia Yerusalemu, huku magari yao ya kivita yakitifua vumbi kwa fujo kana kwamba ni upepo wa kisulisuli. Hicho kitakuwa kivumbi cha kutisha wee! Yehova atatumia wavamizi hao kutimiza hukumu zake mwenyewe zilizo motomoto juu ya Wayahudi “wote wenye mwili” wasio waaminifu. Itakuwa kana kwamba Yehova mwenyewe anapigana na watu wake. “Ghadhabu” yake haitarudi nyuma. Wayahudi wengi wataanguka wakiwa ‘wameuawa na Yehova.’ Mwaka wa 607 K.W.K., unabii huo unatimizwa.a
6. Ni mazoea gani yenye hatia yanayotukia katika Yuda?
6 Je, Yehova ana haki ya ‘kuteta’ kwa kuwapinga watu wake? Tena sana! Katika mazungumzo yetu ya kitabu cha Isaya, tumeona mara nyingi kwamba Wayahudi wameingilia sana ibada ya uwongo, huku ikidhaniwa kwamba eti wamejiweka wakfu kwa Yehova. Na Yehova hajawa kipofu muda huo, asiweze kuyaona matendo yao. Tunaona hivyo tena katika maneno yafuatayo ya unabii: “Watu wale wajitakasao, na kujisafisha katika bustani, nyuma yake aliye katikati; wakila nyama ya nguruwe, na machukizo, na panya; watakoma pamoja, asema BWANA.” (Isaya 66:17) Je, Wayahudi hao ‘wanajitakasa na kujisafisha’ ili wajitayarishe kwa ajili ya ibada safi? La, hasha. Badala ya hivyo, wanajihusisha katika desturi za utakaso wa kipagani katika bustani za pekee. Kisha wanakula kwa pupa nyama ya nguruwe na viumbe wengine walioonwa kuwa wachafu chini ya Sheria ya Kimusa.—Mambo ya Walawi 11:7, 21-23.
7. Jumuiya ya Wakristo inafananaje na Yuda yenye kuabudu sanamu?
7 Ni chukizo kama nini kwamba jambo hilo linatendwa na taifa lililo katika uhusiano wa agano pamoja na yule Mungu wa pekee wa kweli! Lakini ebu fikiri: Leo kuna hali ya kuchukiza jinsi hiyo katika dini za Jumuiya ya Wakristo. Dini hizo pia hudai kwamba zinamtumikia Mungu, na wengi wa viongozi wake hujifanya eti wanamcha Mungu sana. Hata hivyo, wanajitia unajisi kwa mafundisho na mapokeo ya kipagani, jambo linalothibitisha kuwa wamo katika giza la kiroho. Giza tititi!—Mathayo 6:23; Yohana 3:19, 20.
“Watauona Utukufu Wangu”
8. (a) Yuda na hata Jumuiya ya Wakristo zitapatwa na jambo gani? (b) Mataifa ‘yatauona utukufu wa Yehova’ jinsi gani?
8 Je, Yehova anaziona hatia za Jumuiya ya Wakristo na mafundisho yake ya uwongo? Ebu yasome maneno ya Yehova yafuatayo, kama yalivyoandikwa na Isaya, uone utakata kauli gani: “Nami nayajua matendo yao na mawazo yao; wakati unakuja nitakapokusanya mataifa yote na lugha zote; nao watakuja, nao watauona utukufu wangu.” (Isaya 66:18) Licha ya kujua na kuwa tayari kuhukumu matendo ya wale wanaodai kuwa watumishi wake, anayajua hata mawazo yao na atayahukumu hayo pia. Yuda anadai kuwa anamwamini Yehova, lakini matendo yake ya kuabudu sanamu na mazoea ya kipagani yanakanusha dai lake. Raia zake ‘wanajitakasa’ bure kulingana na desturi za kipagani. Taifa hilo litafyekwa, tena peupe mbele ya jirani zake wanaoabudu sanamu. Majirani hao ‘watauona utukufu wa Yehova’ kwa maana ya kwamba watashuhudia matukio hayo kwa macho yao wenyewe na kulazimika kukubali kwamba neno la Yehova limetimia. Yote hayo yanatumikaje kuhusu Jumuiya ya Wakristo? Wakati jumuiya hiyo itakapofikia mwisho wake, wengi wa wale waliokuwa rafiki zake na waliofanya biashara pamoja naye watalazimika kusimama kando tu na kutazama wakiwa hoi wakati neno la Yehova linapotimizwa.—Yeremia 25:31-33; Ufunuo 17:15-18; 18:9-19.
9. Yehova anatangaza habari njema zipi?
9 Je, kuharibiwa kwa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. kunamaanisha kwamba Yehova hatakuwa tena na mashahidi duniani? Sivyo. Watu walio na uaminifu-maadili wenye kutokeza, kama vile Danieli na waandamani wake watatu, wataendelea kumtumikia Yehova hata wakiwa wahamishwa Babiloni. (Danieli 1:6, 7) Naam, ule mfuatano wa mashahidi wengi waaminifu wa Yehova utabaki hivyo hivyo, na mwishoni mwa miaka 70, wanaume na wanawake waaminifu wataondoka Babiloni kurudi Yuda ili kuirudisha ibada safi huko. Hilo ndilo jambo ambalo sasa Yehova anagusia: “Nami nitaweka ishara kati yao, nami nitawatuma hao waliookoka kwa mataifa, Tarshishi, na Puli, na Ludi, wavutao upinde, kwa Tubali na Yavani, visiwa vilivyo mbali; watu wasioisikia habari yangu, wala kuuona utukufu wangu; nao watahubiri utukufu wangu katika mataifa.”—Isaya 66:19.
10. (a) Wayahudi waaminifu waliokombolewa Babiloni watakuwaje ishara? (b) Ni nani leo wanaokuwa ishara?
10 Kundi la wanaume na wanawake waaminifu wanaorudi Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. litatumika likiwa ishara ya kugutusha, ushuhuda wa kwamba Yehova amewakomboa watu wake. Ni nani angaliwaza kwamba siku moja Wayahudi mateka wangekuwa huru ili kufuatia ibada safi kwenye hekalu la Yehova? Hali kadhalika, katika karne ya kwanza Wakristo watiwa-mafuta ndio waliokuwa “ishara na ajabu,” nao walimiminikiwa na watu watiifu waliotaka kumtumikia Yehova. (Isaya 8:18; Waebrania 2:13) Leo Wakristo watiwa-mafuta, wanaopata ufanisi katika nchi yao iliyorudishiwa hali nzuri, wanakuwa kama ishara ya kugutusha duniani. (Isaya 66:8) Wao ni ushuhuda halisi wa kuonyesha kwamba roho ya Yehova ina nguvu za kuvuta watu watiifu wanaosukumwa na mioyo yao kumtumikia Yehova.
11. (a) Baada ya kurudishwa, itakuwaje kwamba watu wa mataifa watakuja kujifunza habari za Yehova? (b) Andiko la Zekaria 8:23 lilitimizwaje mara ya kwanza?
11 Lakini, baada ya kurudishwa mwaka wa 537 K.W.K., watu wa mataifa ambao hawajawahi kuisikia habari za Yehova watamjuaje? Si Wayahudi wote waaminifu watakaorudi Yerusalemu mwishoni mwa utekwa wa Kibabiloni. Wengine, kama vile Danieli, watabaki Babiloni. Na wengine zaidi watatawanyika hadi pembe nne za dunia. Kufikia karne ya tano K.W.K., sehemu zote za Milki ya Uajemi zilikuwa na Wayahudi. (Esta 1:1; 3:8) Bila shaka wengine wao waliwaeleza majirani zao wapagani habari za Yehova, kwa maana wengi kutoka mataifa hayo walikuja kuwa waongofu Wayahudi. Inaonekana hata yule towashi Mwethiopia aliyehubiriwa na Filipo mwanafunzi Mkristo katika karne ya kwanza alikuwa mwongofu. (Matendo 8:26-40) Yote hayo yalitukia yakiwa utimizo wa kwanza wa maneno ya nabii Zekaria: “Siku hizo watu kumi, wa lugha zote za mataifa, wataushika upindo wa nguo yake yeye aliye Myahudi; naam, wataushika wakisema, Tutakwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yu pamoja nanyi.” (Zekaria 8:23) Kwa kweli, Yehova aliyapelekea mataifa nuru!—Zaburi 43:3.
‘Kumletea Yehova Zawadi’
12, 13. Kuanzia mwaka wa 537 K.W.K., “ndugu” wataletwa Yerusalemu kwa njia gani?
12 Baada ya Yerusalemu kujengwa upya, Wayahudi waliotawanyika mbali sana na nchi yao wataelekeza fikira na mtazamo wao kwenye jiji hilo pamoja na ukuhani wake uliorudishwa likiwa kituo cha ibada safi. Wengi wao watasafiri mbali kuhudhuria sherehe za kila mwaka huko. Isaya anaandika hivi kwa kupuliziwa: “Nao watawaleta ndugu zenu wote kutoka mataifa yote, kuwa sadaka [“zawadi,” “NW”] kwa BWANA, juu ya farasi, na katika magari, na katika machela, na juu ya nyumbu, na juu ya wanyama wepesi, mpaka mlima wangu mtakatifu Yerusalemu, asema BWANA; kama vile wana wa Israeli waletavyo sadaka [“zawadi,” “NW”] yao nyumbani kwa BWANA katika chombo safi. Na baadhi ya hao nitawatwaa kuwa makuhani na Walawi.”—Isaya 66:20, 21.
13 Wengine wa hao ‘ndugu kutoka mataifa yote’ walikuwako siku ya Pentekoste wakati roho takatifu ilipomiminwa juu ya wanafunzi wa Yesu. Masimulizi hayo yanasema hivi: “Kulikuwa na Wayahudi wakikaa katika Yerusalemu, wanaume wenye kumhofu Mungu, kutoka kila taifa la yale yaliyo chini ya mbingu.” (Matendo 2:5) Walikuja Yerusalemu kuabudu kulingana na desturi ya Kiyahudi, lakini walipozisikia habari njema juu ya Yesu Kristo, wengi walionyesha wazi kwamba wanamwamini kisha wakabatizwa.
14, 15. (a) Wakristo watiwa-mafuta waliwakusanyaje wengi wa “ndugu” zao wa kiroho baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, nao waliletwaje kwa Yehova wakiwa ‘zawadi katika chombo safi’? (b) Yehova ‘alitwaa baadhi ya hao kuwa makuhani’ jinsi gani? (c) Ni akina nani waliokuwa baadhi ya Wakristo watiwa-mafuta waliohusika katika kukusanya ndugu zao wa kiroho? (Ona sanduku katika ukurasa huu.)
14 Je, unabii huu una utimizo wa kisasa? Tena sana. Baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, watumishi watiwa-mafuta wa Yehova walitambua kutokana na Maandiko kwamba Ufalme wa Mungu ulikuwa umeanzishwa mbinguni mwaka wa 1914. Kupitia funzo la uangalifu la Biblia, walijifunza kwamba warithi wa ziada wa Ufalme, au akina “ndugu,” walipasa kukusanywa. Wahudumu hodari walisafiri “hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia,” wakitumia usafiri wa kila namna ili kuwatafuta wale waliotazamiwa kuwa washirika wa mabaki-watiwa mafuta, wengi wao wakitoka kwenye makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Walipopatikana, waliletwa wawe zawadi kwa Yehova.—Matendo 1:8.
15 Watiwa-mafuta waliokusanywa miaka ya mapema hawakumtazamia Yehova awakubali wakiwa na hali waliyokuwa nayo kabla ya kuujua ukweli wa Biblia. Walichukua hatua za kujisafisha uchafu wa kiroho na wa kiadili ili waweze kutolewa wawe ‘zawadi katika chombo safi,’ au kama ilivyotajwa na mtume Paulo, wawe “bikira safi kiadili kwa Kristo.” (2 Wakorintho 11:2) Zaidi ya kukataa kosa la kimafundisho, watiwa-mafuta walilazimika kujifunza jinsi ya kudumisha msimamo wa kutokuwamo kabisa katika mambo ya kisiasa ya ulimwengu huu. Mwaka wa 1931, watumishi wake walipokuwa wamesafishwa kwa kiasi kinachofaa, Yehova aliwaonyesha neema kwa kuwapa pendeleo la kubeba jina lake wakiwa Mashahidi wa Yehova. (Isaya 43:10-12) Ingawa hivyo, Yehova ‘aliwatwaa baadhi yao kuwa makuhani’ jinsi gani? Wakiwa kikundi, watiwa-mafuta hawa wanakuwa sehemu ya “ukuhani wa kifalme, taifa takatifu,” wakimtolea Mungu dhabihu za sifa.—1 Petro 2:9; Isaya 54:1; Waebrania 13:15.
Ukusanyaji Waendelea
16, 17. Ni nani wale wanaoitwa “uzao wenu” baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu?
16 Idadi kamili ya huo “ukuhani wa kifalme” ni 144,000, na baada ya muda, kazi ya kuwakusanya ilimalizika. (Ufunuo 7:1-8; 14:1) Je, huo ulikuwa mwisho wa kazi ya kukusanya? Sivyo. Unabii wa Isaya unaendelea kusema hivi: “Kama vile mbingu mpya na nchi mpya, nitakazofanya, zitakavyokaa mbele zangu, asema BWANA, ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyokaa.” (Isaya 66:22) Katika utimizo wa kwanza wa maneno hayo, Wayahudi wanaorudi kutoka kwenye utekwa wa Babiloni wataanza kulea watoto. Kwa njia hiyo, mabaki ya Wayahudi waliorudishwa, yaani ile “dunia mpya,” wakiwa chini ya usimamizi mpya wa Kiyahudi, yaani “mbingu mpya,” wataimarika sana. Hata hivyo, unabii huo umekuwa na utimizo wenye kutokeza sana katika siku zetu.
17 “Uzao” ambao taifa la ndugu za kiroho wanautokeza ni “umati mkubwa,” walio na tumaini la uhai wa milele duniani. Wao ‘hutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha,’ na husimama “mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwana-Kondoo.” “Wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” (Ufunuo 7:9-14; 22:17) Leo wale walio “umati mkubwa” wanaepuka giza la kiroho na kuja kwenye nuru ambayo Yehova huandaa. Wanaonyesha imani katika Yesu Kristo, na wanajitahidi kubaki wakiwa safi kiroho na kiadili kama ndugu na dada zao watiwa-mafuta. Wakiwa kikundi, wanaendelea kutumikia chini ya mwelekezo wa Kristo na ‘watakaa’ milele!—Zaburi 37:11, 29.
18. (a) Washirika wa umati mkubwa wameenenda kama ndugu zao watiwa-mafuta jinsi gani? (b) Watiwa-mafuta na waandamani wao humwabudu Yehova “mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato” jinsi gani?
18 Wanaume na wanawake hawa wenye bidii walio na tumaini la kidunia wanajua kwamba ingawa ni muhimu kubaki safi kiadili na kiroho, mengi zaidi yanahusika ili kumfurahisha Yehova. Kazi ya ukusanyaji inavuma, nao wanataka kuishiriki. Kitabu cha Ufunuo kinatoa unabii huu kuwahusu: “Wako mbele ya hicho kiti cha ufalme cha Mungu; nao wanamtolea utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufunuo 7:15) Maneno hayo yanatukumbusha mstari wa pili kutoka mwisho wa unabii wa Isaya: “Na itakuwa, mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato, wanadamu wote watakuja kuabudu mbele zangu, asema BWANA.” (Isaya 66:23) Jambo hilo linatendeka leo. “Mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato,” yaani, kwa ukawaida, kila juma la kila mwezi, Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao, yaani ule umati mkubwa, hukutanika kumwabudu Yehova. Njia mojawapo ambayo wanafanya hivyo ni kuhudhuria mikutano ya Kikristo na kushiriki katika huduma ya peupe. Je, wewe ni mmoja wa wale ‘wanaokuja kuabudu mbele za Yehova’? Watu wa Yehova wanapata shangwe kubwa wanapofanya hivyo, na wale wa umati mkubwa wanautazamia wakati ambao “wanadamu wote,” watamtumikia Yehova “mwezi mpya hata mwezi mpya, na sabato hata sabato” kwa umilele wote.
Mwisho Kamili wa Adui za Mungu
19, 20. Gehena ilitumika kwa kusudi gani nyakati za Biblia, na inafananisha nini?
19 Mstari mmoja unabaki katika funzo letu la unabii wa Isaya. Kitabu kinafikia mwisho kwa kusema hivi: “Watatoka nje na kuitazama mizoga ya watu walioniasi; maana funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika nao watakuwa chukizo machoni pa wote wenye mwili.” (Isaya 66:24) Inaelekea kwamba Yesu Kristo alikuwa akiufikiria unabii huu alipowahimiza wanafunzi wake kurahisisha maisha yao na kuweka masilahi ya Ufalme kwanza. Alisema hivi: “Ikiwa jicho lako lakufanya ukwazike, litupilie mbali; ni bora zaidi kwako kuingia katika ufalme wa Mungu ukiwa na jicho moja kuliko kutupwa ndani ya Gehena ukiwa na macho mawili, mahali ambapo funza wao hafi na ule moto hauzimwi.”—Marko 9:47, 48; Mathayo 5:29, 30; 6:33.
20 Ni mahali gani hapa panapoitwa Gehena? Karne nyingi zilizopita, msomi Myahudi David Kimhi aliandika hivi: “Hapo ni mahali . . . ambapo pamepakana na Yerusalemu, tena ni mahali pa kuchukiza sana, na watu hutupa humo vitu vichafu na mizoga. Vilevile, humo mlikuwa na moto ulioendelea kuwaka ili kuchoma vitu vichafu na mifupa ya mizoga. Kwa hiyo, hukumu ya waovu huitwa Gehinnom kwa njia ya mfano.” Ikiwa, kama vile msomi huyu Myahudi anavyodokeza, Gehena ilitumiwa kama mahali pa kutupia takataka na mizoga ya wale walioonwa hawastahili kuzikwa, basi moto ungekuwa kitu kinachofaa cha kumaliza takataka hizo. Kisichoteketezwa na moto, kingeliwa na funza. Hiyo inaonyesha vizuri kama nini mwisho kamili utakaowapata adui za Mungu!b
21. Kitabu cha Isaya kinafikia mwisho mzuri kuhusiana na akina nani, na kwa nini?
21 Kwa sababu ya kutaja maiti, moto, na funza, je, si kweli kwamba unabii wenye kusisimua wa Isaya unamalizika kwa njia ya kutisha? Hakuna shaka kwamba maadui sugu wa Mungu watafikiri hivyo. Lakini uharibifu wa milele wa waovu ni kitia-moyo kweli kweli kwa marafiki wa Mungu. Watu wa Yehova wanahitaji uhakikisho huo kwamba sasa adui zao hawatawaweza tena. Maadui hao, ambao wamewatesa sana watu wa Mungu na kuliletea jina lake suto kubwa, wataharibiwa milele. Halafu, “mateso hayatainuka mara ya pili.”—Nahumu 1:9.
-
-
Nuru kwa MataifaUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 409]
Zawadi Zilizotiwa Mafuta za Kumpa Yehova Kutoka Katika Mataifa Yote
Mwaka wa 1920, Juan Muñiz aliondoka Marekani kwenda Hispania kisha akasonga mbele na safari yake hadi Argentina, ambako aliyapanga kitengenezo makutaniko ya watiwa-mafuta. Kuanzia mwaka wa 1923 na kuendelea, nuru ya kweli iling’aa juu ya wenye mioyo minyoofu katika Afrika Magharibi wakati mishonari William R. Brown (ambaye mara nyingi aliitwa Bible Brown) aliposhika njia kwenda kuhubiri ujumbe wa Ufalme katika sehemu kama vile Sierra Leone, Ghana, Liberia, Gambia, na Nigeria. Mwaka huo huo George Young wa Kanada aliteremka Brazil, kisha akasonga mbele kwenda Argentina, Costa Rica, Panama, Venezuela, na hata Muungano wa Sovieti. Karibu na wakati huo huo, Edwin Skinner alisafiri baharini kutoka Uingereza hadi India, na huko akajikakamua muda wa miaka mingi katika kazi ya mavuno.
[Picha katika ukurasa wa 411]
Wayahudi fulani waliokuwa kwenye Pentekoste walikuwa ‘ndugu kutoka mataifa yote’
[Picha ya ukurasa mzima katika ukurasa wa 413]
-
-
Nuru kwa MataifaUnabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
a Kuhusu hali iliyokuwako baada ya Yerusalemu kuangushwa na Wababiloni, andiko la Yeremia 52:15 linataja “baadhi ya watu waliokuwa maskini, na mabaki ya watu walioachwa katika mji.” Kichapo Insight on the Scriptures, katika Buku la 1, ukurasa wa 415, kinaeleza jambo hilo hivi: “Inaonekana kwamba kusema ‘mabaki ya watu walioachwa katika mji’ ni kuonyesha kwamba watu wengi walikuwa wamekufa kwa njaa, magonjwa, au moto, au sivyo walichinjwa katika vita hiyo.”
b Kwa kuwa kinachoteketezwa na moto katika Gehena ni mizoga, wala si watu walio hai, mahali hapo hapafananishi mateso ya milele.
-