-
“Upendo Alio Nao Kristo Hutulazimisha”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sehemu ya 3
“Upendo Alio Nao Kristo Hutulazimisha”
Ni nini kinachotuchochea kuendelea kumfuata Yesu? Mtume Paulo anajibu: “Upendo alio nao Kristo hutulazimisha.” (2 Wakorintho 5:14) Katika sehemu hii, tutajifunza kuhusu upendo alio nao Yesu—jinsi anavyompenda Yehova, anavyowapenda wanadamu kwa ujumla, na anavyompenda kila mmoja wetu. Kujifunza kuhusu upendo huo kutatuchochea kwelikweli. Mioyo yetu itachochewa, nasi tutaona kwamba lazima tuchukue hatua, tufanye maendeleo, na kufuata mfano wa Bwana wetu.
-
-
“Ninampenda Baba”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 13
“Ninampenda Baba”
1, 2. Mtume Yohana alifunua nini kuhusu jioni ya mwisho ambayo mitume walikuwa pamoja na Yesu?
MZEE Yohana anatia kalamu yake katika wino. Anakumbuka mambo mengi. Yeye ndiye mtume wa mwisho aliye hai kati ya mitume wote wa Yesu Kristo. Sasa Yohana ana umri wa miaka 100 hivi, naye anakumbuka yaliyotukia jioni moja isiyosahaulika miaka 70 hivi iliyopita. Hiyo ilikuwa jioni ya mwisho ambayo yeye na mitume wenzake walikuwa pamoja na Yesu kabla ya kifo Chake. Roho takatifu ya Mungu inamwezesha Yohana kukumbuka na kuandika matukio ya jioni hiyo kwa mapana na marefu.
2 Usiku huo, Yesu alitaja waziwazi kwamba muda mfupi baadaye angeuawa. Yohana tu ndiye anayefunua ni kwa nini Yesu alisema angekubali kufa kifo chenye maumivu makali: “Kusudi ulimwengu ujue kwamba ninampenda Baba, kama vile Baba amenipa amri kufanya, ndivyo ninavyofanya. Simameni, tuondoke hapa.”—Yohana 14:31.
3. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba anampenda Baba yake?
3 “Ninampenda Baba.” Hilo lilikuwa jambo kuu zaidi maishani mwa Yesu. Haimaanishi kwamba alikuwa akiyarudia-rudia maneno hayo. Katika Biblia nzima, ni andiko la Yohana 14:31 tu linalomnukuu Yesu akitaja moja kwa moja kwamba anampenda Baba yake. Hata hivyo, maisha ya Yesu yalithibitisha ukweli wa maneno hayo. Kila siku alionyesha kwamba anampenda Yehova. Uhodari, utii, na uvumilivu wa Yesu ni sifa zilizothibitisha kwamba anampenda Mungu. Huduma yake yote ilichochewa na upendo huo.
4, 5. Biblia inazungumzia sana upendo wa aina gani, nasi tunaweza kusema nini kuhusu jinsi Yesu alivyompenda Yehova?
4 Leo, huenda wengine wanafikiri kwamba kuonyesha upendo ni udhaifu. Labda wanafikiri ni upendo unaoimbwa katika mashairi na nyimbo za mapenzi au wanafikiri ni maneno ya kipuuzi ambayo nyakati nyingine yanasemwa kati ya watu wenye upendo wa kimahaba. Ni kweli kwamba Biblia inazungumzia upendo wa kimahaba, hata hivyo, inauzungumzia kwa heshima kuliko ilivyo leo. (Methali 5:15-21) Lakini, Neno la Mungu linazungumzia sana upendo mwingine. Upendo huo si msisimuko tu au hisia za muda; wala si utaalamu wa kushughulika na watu wengine bila hisia zozote, bali unatia ndani moyo na akili. Upendo huo unatoka moyoni, unaongozwa na kanuni za juu, na unaonekana kupitia matendo yenye kujenga. Si wa kipuuzi hata kidogo. Neno la Mungu linasema kwamba “upendo haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:8.
5 Kati ya wanadamu wote ambao wamepata kuishi, Yesu ndiye aliyempenda Yehova zaidi. Hakuna yeyote aliyemzidi Yesu kwa kuishi kulingana na maneno ambayo yeye mwenyewe alinukuu kuwa amri ya Mungu iliyo kuu zaidi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Yesu alikuza upendo huo jinsi gani? Alipokuwa duniani, ni nini kilichomwezesha kuendelea kumpenda Mungu sana? Nasi tunaweza kumwiga jinsi gani?
Kifungo cha Muda Mrefu Zaidi na Chenye Nguvu Zaidi cha Upendo
6, 7. Ni nini kinachoonyesha kwamba andiko la Methali 8:22-31 linamfafanua Mwana wa Mungu bali si sifa ya hekima tu?
6 Je, umewahi kufanya kazi fulani pamoja na rafiki yako na kadiri muda ulivyopita urafiki wenu ukazidi kukua? Ikiwa umewahi, unaweza kuelewa upendo uliositawi kati ya Yehova na Mwana wake mzaliwa-pekee. Tumetaja andiko la Methali 8:30 mara kadhaa, lakini acheni tuuchunguze mstari huo kwa makini zaidi tukizingatia muktadha wake. Katika mstari wa 22 mpaka 31, tunapata ufafanuzi ulioongozwa na roho wa hekima inayozungumziwa kana kwamba ni mtu. Ni nini kinachoonyesha kwamba maneno hayo yanamhusu Mwana wa Mungu?
7 Katika mstari wa 22, hekima inasema: “Yehova mwenyewe alinitokeza nikiwa mwanzo wa njia yake, nikiwa wa mapema zaidi kati ya kazi zake za zamani za kale.” Kinachozungumziwa hapa si sifa ya hekima tu, kwa sababu sifa hiyo ‘haikutokezwa.’ Haina mwanzo kwa kuwa Yehova hana mwanzo, naye amekuwa na hekima sikuzote. (Zaburi 90:2) Hata hivyo, Mwana wa Mungu ni “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” Alitokezwa, au kuumbwa; ndiye wa mapema zaidi kati ya kazi zote za Yehova. (Wakolosai 1:15) Mwana huyo alikuwako kabla ya dunia na mbingu, kama inavyosimuliwa katika kitabu cha Methali. Na kwa kuwa alikuwa Neno, Msemaji wa Mungu mwenyewe, basi angeweza kuwakilisha kabisa hekima ya Yehova.—Yohana 1:1.
8. Mwana alikuwa akifanya nini kabla ya kuja duniani, nasi tunaweza kufikiria nini tunapostaajabia uumbaji?
8 Mwana huyo alikuwa akifanya nini kwa muda mrefu sana kabla ya kuja duniani? Mstari wa 30 unatuambia kwamba alikuwa kando ya Mungu akiwa “stadi wa kazi.” Hilo linamaanisha nini? Andiko la Wakolosai 1:16 linasema: “Kwa njia yake vitu vingine vyote viliumbwa mbinguni na duniani . . . Vitu vingine vyote vimeumbwa kupitia yeye na kwa ajili yake.” Hivyo basi, Yehova, Muumba, alimtumia Mwana wake, Stadi wa Kazi, kutokeza uumbaji mwingine wote—viumbe wa roho walio mbinguni, ulimwengu mzima, dunia yenye mimea na wanyama wa aina mbalimbali, na viumbe wa hali ya juu zaidi duniani, yaani, wanadamu. Tunaweza kulinganisha uhusiano huo kati ya Baba na Mwana na ule wa mchoraji wa ramani za ujenzi na mjenzi ambaye ana ustadi wa kutokeza majengo kulingana na ubunifu wa mchoraji. Tunapostaajabia uumbaji fulani, kwa kweli tunamsifu Mchoraji wa Ramani Aliye Mkuu Zaidi. (Zaburi 19:1) Hata hivyo, hatusahau ushirikiano wa muda mrefu na wenye furaha kati ya Muumba na ‘stadi wake wa kazi.’
9, 10. (a) Ni nini kilichofanya kifungo kati ya Yehova na Mwana wake kiwe imara? (b) Ni nini kinachoweza kufanya kifungo kinachokuunganisha na Baba yako wa mbinguni kuwa imara?
9 Wanadamu wawili wasio wakamilifu wanapofanya kazi pamoja, nyakati nyingine wanaweza kukosana. Sivyo ilivyokuwa kati ya Yehova na Mwana wake! Mwana alifanya kazi kwa muda mrefu sana pamoja na Baba yake, naye ‘alifurahi mbele zake wakati wote.’ (Methali 8:30) Ndiyo, alifurahi kuwa pamoja na Baba yake, naye Baba yake alifurahi pia. Kama inavyotarajiwa, Mwana huyo alizidi kuwa kama Baba yake, akijifunza kuiga sifa za Mungu. Basi, haikosi hiyo ndiyo sababu kifungo kati ya Baba na Mwana kilikuwa imara zaidi! Kifungo hicho kinastahili kuitwa kifungo cha muda mrefu zaidi na chenye nguvu zaidi cha upendo ulimwenguni pote.
10 Hata hivyo, hilo linamaanisha nini kwetu? Labda unafikiri haiwezekani kuwa na kifungo kama hicho pamoja na Yehova. Ni kweli kwamba hakuna yeyote kati yetu aliye na cheo kikubwa kama Mwana. Lakini tuna pendeleo la pekee. Kumbuka kwamba Yesu alimkaribia Baba yake kwa kufanya kazi pamoja Naye. Kwa upendo, Yehova anatupa nafasi ya kuwa ‘wafanyakazi wenzake.’ (1 Wakorintho 3:9) Tunapofuata mfano wa Yesu katika huduma, tusisahau kwamba sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu. Hivyo, kifungo cha upendo kinachotuunganisha na Yehova kinazidi kuwa imara. Hilo ni pendeleo lisilo na kifani!
Kilichomwezesha Yesu Kuendelea Kumpenda Sana Yehova
11-13. (a) Kwa nini tuuone upendo kama kitu kilicho hai, na alipokuwa mvulana, Yesu alifanya nini ili upendo wake kwa Yehova uendelee kuwa thabiti? (b) Mwana wa Mungu alionyesha jinsi gani kwamba anapenda kujifunza kumhusu Yehova, kabla ya kuja duniani na hata baadaye akiwa mwanadamu?
11 Inafaa kuuona upendo ulio moyoni mwetu kama kitu kilicho hai. Kama vile maua mazuri kwenye bustani, upendo unahitaji kutiwa mbolea na kutunzwa ili ukue na kusitawi. Ukipuuzwa na kukosa kutunzwa, utadhoofika na kufa. Yesu hakupuuza upendo wake kwa Yehova. Aliutia nguvu na kuendelea kuukuza wakati wote alipokuwa duniani. Acheni tuone jinsi alivyofanya hivyo.
12 Fikiria tena pindi ambayo Yesu alizungumza kwa uhodari hekaluni huko Yerusalemu alipokuwa mtoto. Kumbuka jinsi alivyowaambia wazazi wake waliokuwa wamehangaika: “Kwa nini mlilazimika kunitafuta? Je, hamkujua kwamba ni lazima niwe katika nyumba ya Baba yangu?” (Luka 2:49) Alipokuwa mvulana tu, huenda bado Yesu hangeweza kukumbuka maisha yake kabla ya kuja duniani. Hata hivyo, alimpenda sana Baba yake, Yehova. Alijua kwamba angeweza kuonyesha upendo huo katika ibada. Kwa hiyo, hakuna mahali popote duniani ambapo pangempendeza Yesu kama nyumba ya Baba yake ya ibada safi. Alitamani sana kuwa humo, naye hakutaka kuondoka. Isitoshe, hakuwa mtazamaji tu. Alikuwa na hamu ya kujifunza kumhusu Yehova na kuzungumzia mambo aliyojua. Hisia hizo hazikuanza wala kuisha alipokuwa na umri wa miaka 12.
13 Kabla ya kuja duniani, Mwana huyo alikuwa amejifunza kwa makini kutoka kwa Baba yake. Unabii ulio katika Isaya 50:4-6 unaonyesha kwamba Yehova alimpa Mwana wake elimu ya pekee kuhusu daraka lake akiwa Masihi. Ijapokuwa elimu hiyo ilitia ndani kujifunza kuhusu hali fulani ngumu ambazo zingempata Mtiwa-Mafuta wa Yehova, bado Mwana huyo alikuwa na hamu ya kujifunza. Baadaye, baada ya Yesu kuja duniani na kuwa mtu mzima, aliendelea kuwa na hamu ya kwenda kwenye nyumba ya Baba yake na kushiriki katika ibada na elimu ambayo Yehova alitaka iendelezwe humo. Hivyo, Biblia inaeleza jinsi Yesu alivyokuwa na mazoea ya kwenda hekaluni na katika sinagogi. (Luka 4:16; 19:47) Ikiwa tunataka kuendelea kumpenda Yehova, tunahitaji kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, ambako tunamwabudu Yehova, tunajifunza mengi zaidi juu yake, na kuzidi kumthamini.
“Akapanda mlimani akiwa peke yake ili kusali”
14, 15. (a) Kwa nini Yesu alitafuta nafasi ya kuwa peke yake? (b) Ni kwa njia gani sala za Yesu kwa Baba yake zilionyesha heshima na uhusiano wa karibu waliokuwa nao?
14 Pia, kusali kwa ukawaida kulimwezesha Yesu kuendelea kumpenda Yehova. Ingawa alikuwa mtu mwenye urafiki, anayependa kuwa pamoja na watu, aliona faida ya kuwa peke yake. Kwa mfano, andiko la Luka 5:16 linasema: “Akaendelea kukaa faraghani katika majangwa na kusali.” Vivyo hivyo, andiko la Mathayo 14:23 linasema: “Mwishowe, baada ya kuwaruhusu umati waende zao, akapanda mlimani akiwa peke yake ili kusali. Ingawa ilikuwa jioni, alikuwa huko peke yake.” Pindi hiyo na nyinginezo, Yesu alijitenga awe peke yake si kwa sababu hakupenda kuwa na watu au alichukia ushirika wa wengine, bali kwa sababu alitaka kuwa peke yake na Yehova ili azungumze na Baba yake kwa uhuru katika sala.
15 Aliposali, nyakati nyingine Yesu alitumia maneno “Abba, Baba.” (Marko 14:36) Katika siku za Yesu, “Abba” ni neno lililotumiwa katika familia ambalo linamaanisha “baba,” nalo lilionyesha uhusiano wa karibu. Mara nyingi lilikuwa mojawapo ya maneno ya kwanza-kwanza ambayo mtoto alijifunza kutamka. Hata hivyo, lilikuwa neno la heshima. Ingawa neno hilo lilionyesha uhusiano wa karibu wa Mwana anayezungumza na Baba yake mpendwa, lilionyesha pia heshima kubwa kwa mamlaka ya Yehova akiwa baba. Tunaona uhusiano huo wa karibu na vilevile heshima katika sala zote za Yesu zilizorekodiwa. Kwa mfano, katika Yohana sura ya 17, mtume Yohana aliandika sala ndefu ya kutoka moyoni ambayo Yesu alitoa usiku Wake wa mwisho. Kuchanganua sala hiyo kunatuchochea sana, nasi tunapaswa kuiga sala hiyo, si kwa kurudia-rudia maneno ya Yesu, bali kwa kutafuta njia za kuongea na Baba yetu wa mbinguni kutoka moyoni mara nyingi iwezekanavyo. Kufanya hivyo kutatusaidia kuendelea kumpenda sana.
16, 17. (a) Maneno ya Yesu yalionyesha jinsi gani kwamba anampenda Baba yake? (b) Ni kwa njia gani Yesu alionyesha ukarimu wa Baba yake?
16 Kama tulivyoona mapema, Yesu hakurudia-rudia kusema “Ninampenda Baba.” Hata hivyo, mara nyingi maneno yake yalionyesha kwamba anampenda Baba yake. Jinsi gani? Yesu mwenyewe alisema: “Ninakusifu wewe hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia.” (Mathayo 11:25) Katika Sehemu ya 2 ya kitabu hiki, tuliona kwamba Yesu alipenda kumsifu Baba yake kwa kuwasaidia watu wamjue Yeye. Kwa mfano, alimlinganisha Yehova na baba aliyekuwa tayari sana kumsamehe mwana wake mpotevu hivi kwamba alimsubiri kijana huyo aliyetubu, na alipomwona kutoka mbali alikimbia kumlaki na kumkumbatia. (Luka 15:20) Ni nani anayeweza kusoma masimulizi hayo bila kuguswa moyo na jinsi Yesu anavyoufafanua upendo na msamaha wa Yehova?
17 Mara nyingi Yesu alimsifu Baba yake kwa ukarimu Wake. Alitumia mfano wa wazazi wasio wakamilifu kuonyesha jinsi tunavyoweza kuwa na uhakika kwamba Baba yetu atatupa roho takatifu kulingana na uhitaji wetu. (Luka 11:13) Pia, Yesu alizungumzia tumaini ambalo Baba anatoa kwa ukarimu. Yesu alizungumzia kwa hamu tumaini lake mwenyewe la kuketi tena kando ya Baba yake mbinguni. (Yohana 14:28; 17:5) Aliwaambia wafuasi wake kuhusu tumaini ambalo Yehova anawapa “kundi dogo” la Kristo—kuishi mbinguni na kutawala pamoja na Mfalme wa Kimasihi. (Luka 12:32; Yohana 14:2) Naye alimfariji mkosaji aliyekuwa akikaribia kufa kwa kumpa tumaini la kuishi katika Paradiso. (Luka 23:43) Bila shaka, kuzungumzia ukarimu mwingi wa Baba yake katika njia hizo kulimsaidia Yesu kuendelea kumpenda sana Yehova. Wafuasi wengi wa Kristo wameona kwamba kuzungumza juu ya Yehova na tumaini ambalo anawapa wale wanaompenda ndilo jambo linalowasaidia sana kumpenda na kumwamini hata zaidi.
Je, Utamwiga Yesu Katika Kumpenda Yehova?
18. Ni jambo gani kuu zaidi tunalopaswa kuiga katika Yesu, na kwa nini?
18 Hili ndilo jambo kuu zaidi tunalopaswa kuiga katika Yesu: Lazima tumpende Yehova kwa moyo, nafsi, akili, na kwa nguvu zetu zote. (Luka 10:27) Upendo huo hauonyeshwi tu kwa kuwa na hisia nyingi bali pia kwa matendo yetu. Yesu hakuridhika tu kuhisi kwamba anampenda Baba yake wala kusema tu, “Ninampenda Baba.” Alisema: “Kusudi ulimwengu ujue kwamba ninampenda Baba, kama vile Baba amenipa amri kufanya, ndivyo ninavyofanya.” (Yohana 14:31) Shetani alikuwa amedai kuwa hakuna mwanadamu anayeweza kumtumikia Yehova kwa kuchochewa na upendo usio na ubinafsi. (Ayubu 2:4, 5) Ili kutoa jibu linalofaa kwa uchongezi wa Shetani, Yesu alichukua hatua kwa uhodari na kuuonyesha ulimwengu jinsi alivyompenda Baba yake sana. Alitii hata kufikia kutoa uhai wake. Je, utamwiga Yesu? Je, utauonyesha ulimwengu kwamba unampenda Yehova Mungu kikweli?
19, 20. (a) Kwa nini tunapaswa kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida? (b) Tunapaswa kuziona jinsi gani pindi za kujifunza kibinafsi, kutafakari, na kusali?
19 Tuna uhitaji mkubwa wa kiroho wa kuonyesha upendo kama huo. Yehova amefanya mpango ili tumwabudu kwa njia ambayo upendo tulio nao kumwelekea utakuwa imara na kukuzwa. Unapohudhuria mikutano ya Kikristo, jaribu kukumbuka kwamba umeenda kumwabudu Mungu wako. Ibada hiyo inatia ndani kuungana na wengine katika sala ya kutoka moyoni, kuimba nyimbo za sifa, kusikiliza kwa makini, na kushiriki inapowezekana. Mikutano hiyo pia hukupa nafasi ya kuwatia moyo Wakristo wenzako. (Waebrania 10:24, 25) Kumwabudu Yehova kwa ukawaida kwenye mikutano ya Kikristo kutakusaidia kumpenda Mungu hata zaidi.
20 Vivyo hivyo, tutampenda Yehova hata zaidi kwa kujifunza kibinafsi, kutafakari, na kusali. Zione hizo kuwa pindi za kuwa peke yako pamoja na Yehova. Unapojifunza Neno la Mungu lililoandikwa na kulitafakari, Yehova anakujulisha mawazo yake. Unaposali, unamfunulia yaliyo moyoni mwako. Kumbuka kwamba sala si kumwomba tu Mungu akupe kitu fulani, au kukufanyia jambo fulani. Sala hukupa pia nafasi ya kumshukuru Yehova kwa baraka ambazo umepata na kumsifu kwa kazi zake za ajabu. (Zaburi 146:1) Isitoshe, kumsifu Yehova hadharani kwa shangwe na shauku ni njia nzuri ya kumshukuru Yehova na kumwonyesha kwamba unampenda.
21. Kumpenda Yehova ni jambo la maana kadiri gani, na ni nini kitakachozungumziwa katika sura kadhaa zinazofuata?
21 Kumpenda Mungu kutakuwezesha kupata furaha ya milele. Hilo tu ndilo jambo ambalo Adamu na Hawa walihitaji kufanya ili wafanikiwe, na ndilo waliloshindwa kufanya. Hilo ndilo jambo la maana zaidi unalohitaji ili kupinga na kushinda kishawishi au kuvumilia jaribu lolote la imani. Kumpenda Mungu ndio msingi wa kuwa mfuasi wa Yesu. Bila shaka, kumpenda Mungu kunatia ndani kuwapenda wanadamu wenzetu. (1 Yohana 4:20) Katika sura chache zinazofuata, tutachunguza jinsi Yesu alivyowapenda watu. Katika sura inayofuata, tutazungumzia kwa nini watu wengi sana walijisikia huru kumkaribia Yesu.
-
-
“Umati Mkubwa Ukamkaribia”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 14
“Umati Mkubwa Ukamkaribia”
“Waacheni watoto wachanga waje kwangu”
1-3. Ni nini kinachotokea wazazi wanapowaleta watoto kwa Yesu, na kisa hicho kinaonyesha nini kumhusu Yesu?
YESU anajua kwamba anakaribia sana mwisho wa maisha yake duniani. Ni majuma machache tu yanayobaki, na bado ana kazi nyingi sana! Anahubiri pamoja na mitume wake huko Perea, eneo lililo upande wa mashariki wa Mto Yordani. Wanahubiri wakielekea kusini, kuelekea Yerusalemu, ambako Yesu atahudhuria kwa mara ya mwisho Pasaka itakayomalizika kwa tukio la pekee sana.
2 Baada ya Yesu kuwa na mazungumzo mazito pamoja na viongozi fulani wa dini, kunatokea vurugu kidogo. Watu wanawaleta watoto wao wamwone. Inaonekana watoto hao wana umri mbalimbali, kwa kuwa Marko anawataja kwa kutumia neno lilelile alilotumia alipokuwa akizungumzia mtoto wa miaka 12, na Luka anatumia neno linaloweza kutafsiriwa ‘watoto wachanga.’ (Luka 18:15; Marko 5:41, 42; 10:13) Bila shaka, kwa kawaida mahali popote penye watoto huwa na kelele na hekaheka. Wanafunzi wa Yesu wanawakemea wazazi, labda wakifikiri Bwana ana shughuli nyingi mno asiweze kuwa pamoja na watoto. Yesu anafanya nini?
3 Yesu anapoona kinachoendelea, anakasirika. Ni nani wanaomkasirisha? Ni watoto? Ni wazazi? Hapana, ni wanafunzi wake! Anasema: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia, kwa maana ufalme wa Mungu ni wa wale walio kama hao. Kwa kweli ninawaambia ninyi, Yeyote yule asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mchanga hataingia kamwe ndani yake.” Kisha, Yesu ‘anawakumbatia’ watoto hao na kuwabariki. (Marko 10:13-16) Maneno ambayo Marko anatumia hapa yanadokeza kwamba Yesu anawakumbatia kwa shauku, labda hata akiwapakata watoto fulani wachanga. Ni wazi kwamba Yesu anawapenda watoto. Hata hivyo, kisa hicho kinatufundisha jambo lingine kumhusu, kwamba watu walijisikia huru kumkaribia.
4, 5. (a) Ni nini kinachotuonyesha kwamba ilikuwa rahisi kumkaribia Yesu? (b) Tutachunguza maswali gani katika sura hii?
4 Ikiwa Yesu angekuwa mtu mkali, asiye na urafiki, au mwenye kiburi, huenda watoto hao hawangevutiwa naye wala wazazi wao hawangejisikia huru kumkaribia. Hebu wazia jinsi wazazi wa watoto hao wanavyohisi mtu huyo mwenye fadhili anapowaonyesha upendo watoto wao, anapowabariki na kusema kwamba watoto hao ni wenye thamani machoni pa Mungu! Kwa kweli, ingawa Yesu alikuwa na madaraka mazito sana, watu walipenda kumkaribia zaidi kuliko mwanadamu mwingine yeyote.
5 Ni nani wengine waliojisikia huru kumkaribia Yesu? Kwa nini watu walimkaribia kwa urahisi? Nasi tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani katika jambo hilo? Hebu tuone.
Ni Nani Waliojisikia Huru Kumkaribia Yesu?
6-8. Mara nyingi Yesu alichangamana na nani, na mtazamo wake kuwaelekea watu hao ulitofautiana jinsi gani na ule wa viongozi wa dini?
6 Unaposoma masimulizi ya Injili, huenda ukashangazwa kuona jinsi watu wengi sana walivyojisikia huru kumkaribia Yesu. Kwa mfano, anapozungumziwa, mara nyingi tunasoma kuhusu “umati mkubwa.” “Umati mkubwa ukamfuata kutoka Galilaya.” “Umati mkubwa ukamkusanyikia.” “Umati mkubwa ukamkaribia.” “Umati mkubwa ulikuwa ukisafiri pamoja naye.” (Mathayo 4:25; 13:2; 15:30; Luka 14:25) Ndiyo, mara nyingi, Yesu alizungukwa na umati wa watu.
7 Kwa ujumla, hao walikuwa watu wa kawaida ambao viongozi wa dini waliwaita kwa dharau “watu wa nchi.” Mafarisayo na makuhani walisema hivi waziwazi: “Umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa.” (Yohana 7:49) Baadaye, maandishi ya marabi yalithibitisha maoni hayo. Viongozi wengi wa dini waliwaona watu hao kuwa watu wa kudharaulika, wakakataa kula nao, kununua kutoka kwao, au kushirikiana nao. Baadhi yao walisisitiza kwamba watu hao wasiojua sheria ya mdomo hawana tumaini la ufufuo! Haikosi watu wengi wa hali ya chini waliwaepuka viongozi hao badala ya kuwaomba msaada au mwongozo. Lakini Yesu alikuwa tofauti.
8 Yesu alichangamana kwa uhuru na watu wa kawaida. Alikula pamoja nao, aliwaponya, aliwafundisha, na kuwapa tumaini. Bila shaka, Yesu aliona mambo kihalisi, akitambua kwamba wengi wangekataa kumtumikia Yehova. (Mathayo 7:13, 14) Hata hivyo, alikuwa na maoni yanayofaa kuhusu kila mtu, naye alijua kwamba wengi wanaweza kutenda mema. Alikuwa tofauti kabisa na makuhani na Mafarisayo wenye mioyo migumu! Hata hivyo, inashangaza kwamba hata makuhani na Mafarisayo walimkaribia Yesu, na baadhi yao walibadili njia zao na kumfuata. (Matendo 6:7; 15:5) Pia, watu fulani waliokuwa matajiri na wenye mamlaka walijisikia huru kumkaribia Yesu.—Marko 10:17, 22.
9. Kwa nini wanawake walijisikia huru kumkaribia Yesu?
9 Wanawake walijisikia huru kumkaribia Yesu. Haikosi mara nyingi walidharauliwa sana na viongozi wa dini. Kwa kawaida marabi walidharau wazo la kuwafundisha wanawake. Wanawake hata hawakuruhusiwa kutoa ushahidi katika kesi za kisheria; walionwa kuwa mashahidi wasiotegemeka. Marabi hata walitoa sala ya kumshukuru Mungu kwamba wao si wanawake! Lakini Yesu hakuwadharau wanawake. Wengi wao walimkaribia wakitaka kujifunza. Kwa mfano, Maria, dada ya Lazaro, aliketi miguuni pa Bwana, akisikiliza kwa makini maneno ya Yesu huku dada yake, Martha, akijishughulisha na kujihangaisha sana kutayarisha chakula. Yesu alimpongeza Maria kwa kutanguliza mambo ya maana.—Luka 10:39-42.
10. Tofauti na viongozi wa dini, Yesu aliwatendea wagonjwa kwa njia gani?
10 Pia, wagonjwa wengi walimwendea Yesu ijapokuwa mara nyingi viongozi wa dini waliwaona kuwa watu wasiopaswa kuwa katika jamii. Sheria ya Musa ilisema kwamba watu wenye ukoma wanapaswa kutengwa kwa sababu za kiafya, lakini haikuruhusu watendewe kwa ukatili. (Mambo ya Walawi, sura ya 13) Hata hivyo, baadaye sheria za marabi zilisema kwamba watu wenye ukoma walikuwa wenye kuchukiza kama mavi. Viongozi fulani wa dini hata waliwarushia mawe watu wenye ukoma ili wasiwakaribie! Ni vigumu kuwazia jinsi watu waliotendewa hivyo wangeweza kuwa na uhodari wa kumkaribia mwalimu yeyote, hata hivyo, watu wenye ukoma walimkaribia Yesu. Mmoja wao alisema maneno haya yanayojulikana sana ambayo yanaonyesha imani: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” (Luka 5:12) Katika sura inayofuata, tutazungumzia jibu la Yesu. Kwa sasa, inatosha kusema kwamba huo ndio uthibitisho ulio wazi zaidi unaoonyesha kuwa watu walijisikia huru kumkaribia Yesu.
11. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba waliolemewa na hatia walijisikia huru kumkaribia Yesu, na kwa nini hilo ni jambo la maana?
11 Wale waliolemewa na hatia walijisikia huru kumkaribia Yesu. Kwa mfano, fikiria wakati ambapo Yesu alikuwa akila nyumbani kwa Farisayo fulani. Mwanamke aliyejulikana kuwa mtenda-dhambi aliingia na kupiga magoti miguuni pa Yesu, akilia kwa sababu ya hatia yake. Aliilowesha miguu ya Yesu kwa machozi na kutumia nywele zake kuyakausha. Ingawa mwenye nyumba alichukizwa na jambo hilo na kumchambua Yesu vikali kwa kumruhusu mwanamke huyo amkaribie, kwa fadhili Yesu alimpongeza mwanamke huyo kwa kutubu kikweli naye akamhakikishia kwamba Yehova amemsamehe. (Luka 7:36-50) Leo, kuliko wakati mwingine wowote, watu wanaolemewa na hatia wanahitaji kujisikia huru kuwakaribia wale wanaoweza kuwasaidia kurekebisha uhusiano wao pamoja na Mungu! Kwa nini watu walijisikia huru kumkaribia Yesu?
Kwa Nini Watu Walijisikia Huru Kumkaribia Yesu?
12. Kwa nini haishangazi kwamba watu walijisikia huru kumkaribia Yesu?
12 Kumbuka kwamba Yesu alimwiga kikamili Baba yake mpendwa wa mbinguni. (Yohana 14:9) Biblia inatukumbusha kwamba Yehova “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.” (Matendo 17:27) Akiwa “Msikiaji wa sala,” sikuzote watumishi waaminifu wa Yehova na watu wengine wowote ambao kwa unyoofu wanataka kumpata na kumtumikia wanaweza kumkaribia. (Zaburi 65:2) Hebu wazia, Mtu mwenye nguvu zaidi na aliye wa maana zaidi ndiye pia anayeweza kukaribiwa kwa urahisi zaidi! Kama Baba yake, Yesu anawapenda watu. Katika sura zinazofuata, tutazungumzia jinsi Yesu alivyokuwa na upendo mwingi sana moyoni. Hata hivyo, watu walijisikia huru kumkaribia Yesu hasa kwa sababu upendo wake kwa watu ulionekana kwa urahisi. Hebu tuchunguze baadhi ya mambo ambayo Yesu alifanya kuonyesha upendo huo.
13. Wazazi wanaweza kumwiga Yesu jinsi gani?
13 Haikuwa vigumu kwa watu kutambua kwamba Yesu anapendezwa nao binafsi. Hata alipokuwa chini ya hali ngumu hakuacha kupendezwa na watu. Kama tulivyoona, wazazi walipomletea watoto wao, Yesu alikubali wamkaribie hata alipokuwa na shughuli nyingi na madaraka mazito. Aliwawekea wazazi mfano mzuri kama nini! Si rahisi kulea watoto katika ulimwengu wa leo. Hata hivyo, watoto wanapaswa kujisikia huru wanapokuwa na wazazi wao. Ikiwa wewe ni mzazi, unajua kwamba kuna nyakati ambazo unaweza kuwa na shughuli nyingi usiweze kumpa mtoto wako uangalifu anaohitaji. Kwa nini usimwambie utatenga wakati haraka iwezekanavyo uwe pamoja naye? Ukitimiza ahadi yako, mtoto wako atajifunza faida ya kungoja. Pia, atajua kwamba wakati wowote anaweza kukueleza jambo lolote linalomhangaisha.
14-16. (a) Ni hali gani zilizomchochea Yesu afanye muujiza wake wa kwanza, na kwa nini lilikuwa tendo la ajabu? (b) Muujiza ambao Yesu alifanya huko Kana unaonyesha nini kumhusu, na wazazi wanaweza kujifunza nini?
14 Yesu alionyesha kwamba alitilia maanani mahangaiko ya watu. Kwa mfano, fikiria muujiza wa kwanza ambao Yesu alifanya. Alikuwa katika karamu ya ndoa huko Kana, mji wa Galilaya. Tatizo fulani lilitokea—divai ilikuwa imekwisha! Maria, mama ya Yesu, alimwambia mwana wake kilichokuwa kimetokea. Yesu alifanya nini? Aliwaagiza wahudumu wajaze maji katika mitungi sita mikubwa ya mawe. Msimamizi wa karamu alipopelekewa kiasi fulani aonje, ilikuwa divai tamu kama nini! Je, hayo yalikuwa mazingaombwe? Hapana, maji halisi ‘yaligeuzwa kuwa divai.’ (Yohana 2:1-11) Kwa muda mrefu, wanadamu wametamani sana kugeuza kitu kimoja kiwe kingine. Kwa karne nyingi, wataalamu fulani walijaribu kugeuza madini ya risasi yawe dhahabu. Hawakufanikiwa hata ingawa risasi na dhahabu ni madini yanayofanana sana.a Namna gani maji na divai? Maji ni mchanganyiko wa aina mbili za madini ya msingi. Nayo divai imefanyizwa kwa visehemu vipatavyo elfu moja, vingi vya visehemu hivyo vikiwa na miundo tata! Kwa nini Yesu alifanya tendo hilo la ajabu ili kutatua tatizo dogo la upungufu wa divai kwenye karamu ya ndoa?
15 Hilo halikuwa tatizo dogo kwa bwana na bibi-arusi. Zamani, katika Mashariki ya Kati, kuwaonyesha wageni ukarimu kulikuwa sifa ya maana. Kuishiwa na divai katika karamu ya ndoa kungekuwa aibu kubwa kwa wenye kufanya karamu ya ndoa, kungeitia doa siku yao ya ndoa, na jambo hilo lingekumbukwa kwa miaka mingi. Halikuwa tatizo dogo kwao wala kwa Yesu. Kwa hiyo, alichukua hatua. Je, unaona ni kwa nini watu walimwendea walipokuwa na shida?
Mwonyeshe mtoto wako kwamba anaweza kukukaribia na kwamba unamjali kikweli
16 Wazazi wanaweza kujifunza somo la maana katika kisa hicho pia. Namna gani mtoto wako akija kwako akiwa na tatizo fulani? Huenda ukaliona tatizo lake kuwa dogo. Labda hata unaweza kuliona kuwa jambo la kuchekesha. Kwa kulinganisha na matatizo yako, huenda kwa kweli tatizo la mtoto wako likaonekana kuwa dogo. Hata hivyo, kumbuka kwamba kwa mtoto wako si tatizo dogo! Ikiwa linamhangaisha mtu unayempenda sana, je, halipaswi kukuhangaisha pia? Kumwambia mtoto wako kwamba unajali mahangaiko yake kutafanya ajisikie huru kukukaribia.
17. Yesu alituwekea mfano gani wa upole, na kwa nini kuwa na sifa hiyo kunaonyesha kwamba mtu ana nguvu?
17 Kama tulivyojifunza katika Sura ya 3, Yesu alikuwa mpole na mnyenyekevu. (Mathayo 11:29) Upole ni sifa yenye kuvutia, nayo inaonyesha kwamba mtu ni mnyenyekevu moyoni. Ni sehemu ya tunda la roho ya Mungu na inahusianishwa na hekima inayotoka kwa Mungu. (Wagalatia 5:22, 23; Yakobo 3:13) Hata alipokasirishwa sana, Yesu alijizuia. Upole wake haukuwa udhaifu hata kidogo. Kulingana na mtaalamu mmoja, upole ni sifa yenye nguvu sana. Kwa kweli, mara nyingi tunahitaji nguvu ili kuzuia hasira yetu na kuwatendea wengine kwa upole. Lakini Yehova akibariki jitihada zetu, tunaweza kumwiga Yesu katika kuonyesha upole, na hivyo watu watajisikia huru kutukaribia.
18. Ni mfano gani unaoonyesha kwamba Yesu alikuwa mwenye kukubali sababu, na kwa nini unafikiri sifa hiyo inaweza kuwafanya watu wajisikie huru kumkaribia mtu?
18 Yesu alikuwa mwenye kukubali sababu. Yesu alipokuwa Tiro, mwanamke fulani alikuja kwake kwa sababu binti yake alikuwa “anasumbuliwa sana na roho mwovu.” Kwa njia tatu tofauti, Yesu alionyesha kwamba hakutaka kufanya kile ambacho mwanamke huyo alitaka. Kwanza, alinyamaza; pili, alimpa sababu kuonyesha kwa nini hakupaswa kufanya kile ambacho mwanamke huyo alitaka; tatu, alitoa mfano ili kuonyesha wazi kwa nini hangefanya jambo hilo. Hata hivyo, je, Yesu alikuwa mkaidi na asiyejali hisia za mwanamke huyo? Je, Yesu alionyesha kwamba mwanamke huyo anacheza na moto kwa kuthubutu kujibu maneno ya mtu mwenye mamlaka? Hapana, mwanamke huyo alijihisi salama. Hakuomba tu msaada, bali aliendelea kusisitiza hata ingawa Yesu alionyesha kwamba hakutaka kumsaidia. Yesu aliona imani yake kubwa iliyomchochea kusisitiza, Naye akamponya binti yake. (Mathayo 15:22-28) Bila shaka, watu walijisikia huru kumkaribia Yesu kwa sababu alikuwa mwenye kukubali sababu, alikuwa tayari kusikiliza, na kubadilika kulingana na hali!
Je, Watu Wanajisikia Huru Kukukaribia?
19. Ni kwa njia gani tunaweza kujua ikiwa kwa kweli wengine wanajisikia huru kutukaribia?
19 Kwa kawaida, watu hufikiri kwamba wengine wanajisikia huru kuwakaribia. Kwa mfano, watu fulani wenye mamlaka wanapenda kusema kwamba wanaweza kufikiwa kwa urahisi, na kwamba watu walio chini yao wako huru kuwafikia wakati wowote. Hata hivyo, Biblia inatoa onyo hili kali: “Wanadamu wengi hutangaza fadhili zao wenyewe zenye upendo, lakini ni nani anayeweza kumpata mtu mwaminifu?” (Methali 20:6) Ni rahisi kusema kwamba watu wanajisikia huru kutukaribia, lakini, je, sisi ni waaminifu kikweli katika kuiga upendo wa Yesu kwa njia hiyo? Jibu la swali hilo linategemea maoni ya wengine bali si yetu. Paulo alisema: “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.” (Wafilipi 4:5) Inafaa kila mmoja wetu ajiulize: ‘Wengine wana maoni gani kunihusu? Ninajulikana kuwa mtu wa aina gani?’
Wazee hujitahidi kuwafanya wengine wajisikie huru kuwakaribia
20. (a) Kwa nini wazee Wakristo wanapaswa kuwafanya wengine wajisikie huru kuwakaribia? (b) Kwa nini tunapaswa kuwa wenye usawaziko kuhusiana na yale tunayotarajia kutoka kwa wazee kutanikoni?
20 Wazee Wakristo hasa hujitahidi kuwafanya wengine wajisikie huru kuwakaribia. Wanatamani sana kutimiza yale yanayosemwa kwenye Isaya 32:1, 2: “Kila mmoja atakuwa kama mahali pa kujificha kutokana na upepo na mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua, kama vijito vya maji katika nchi isiyo na maji, kama kivuli cha mwamba mzito katika nchi iliyochoka.” Mzee anaweza kutoa ulinzi, burudisho, na kitulizo ikiwa tu ataendelea kuwafanya wengine wajisikie huru kumkaribia. Ni kweli kwamba kufanya hivyo si rahisi sikuzote kwa maana wazee wana madaraka mazito katika nyakati hizi ngumu. Lakini, wazee hujitahidi wasionekane kuwa wenye shughuli nyingi mno wasiweze kushughulikia mahitaji ya kondoo wa Yehova. (1 Petro 5:2) Washiriki wengine wa kutaniko wanajaribu kuwa wenye usawaziko kuhusiana na yale ambayo wanatarajia kutoka kwa wanaume hao waaminifu kwa kuonyesha roho ya unyenyekevu na ya ushirikiano.—Waebrania 13:17.
21. Wazazi wanaweza kufanya nini ili watoto wajisikie huru kuwakaribia, nasi tutazungumzia nini katika sura inayofuata?
21 Nyakati zote wazazi hujitahidi kushughulikia mahitaji ya watoto wao. Hilo ni jambo zito! Wanataka watoto wao wajue kwamba wanapaswa kujisikia huru kumweleza Baba au Mama mahangaiko yao. Hivyo, wazazi Wakristo wanajaribu kuwa wapole na wenye kukubali sababu badala ya kukasirika wakati mtoto anapoungama kosa au anapokuwa na maoni yasiyofaa. Wazazi wanapoendelea kuwazoeza watoto wao kwa subira, wao hujitahidi kuwa na mawasiliano mazuri. Kwa kweli, sote tunataka kuendelea kuwafanya wengine wajisikie huru kutukaribia, kama Yesu alivyofanya. Katika sura inayofuata, tutazungumzia jinsi Yesu alivyoonyesha huruma kutoka moyoni, mojawapo ya sifa kuu zilizofanya wengine wajisikie huru kumkaribia.
a Wanafunzi wa kemia wanajua kwamba madini ya risasi na dhahabu yanakaribiana sana katika jedwali la elementi. Kiini cha atomu ya risasi kina protoni tatu zaidi kuliko zile za dhahabu. Wanafizikia wa siku hizi hata wamefaulu kugeuza kiasi kidogo cha madini ya risasi kuwa dhahabu, lakini inagharimu sana kufanya hivyo, kwa kuwa nishati nyingi sana inahitajiwa.
-
-
“Akawasikitikia”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 15
“Akawasikitikia”
“Bwana, tunataka macho yetu yafunguliwe”
1-3. (a) Yesu anafanya nini vipofu wawili wenye kuombaomba wanapomsihi awasaidie? (b) Neno ‘sikitikia’ linamaanisha nini? (Ona maelezo ya chini.)
VIPOFU wawili wameketi kando ya barabara karibu sana na jiji la Yeriko. Kila siku wanakuja hapo na kutafuta mahali ambapo watu wengi wanapitia kisha wanaketi na kuanza kuombaomba. Hata hivyo, leo, watajionea jambo fulani ambalo litabadili kabisa maisha yao.
2 Kwa ghafula, waombaji hao wanasikia makelele. Kwa kuwa hawawezi kuona kinachoendelea, mmoja wao anauliza makelele hayo ni ya nini, naye anaambiwa: “Yesu Mnazareti anapitia hapa!” Yesu anaelekea Yerusalemu kwa mara ya mwisho. Hata hivyo, hayuko peke yake; umati mkubwa unamfuata. Baada ya kuambiwa ni nani anayepitia hapo, waombaji hao wanapaaza sauti na kusema: “Bwana, uturehemu, Mwana wa Daudi!” Umati unakasirika na kuwaambia waombaji hao wanyamaze, lakini watu hao wanahitaji sana msaada. Hawakubali kunyamazishwa.
3 Ingawa kuna makelele ya umati, Yesu anawasikia waombaji hao wakipaaza sauti. Atafanya nini? Ana mambo mengi akilini na moyoni. Juma la mwisho la maisha yake duniani linakaribia. Anajua atateswa na kuuawa kikatili Yerusalemu. Hata hivyo, hapuuzi vilio vyao vya kusihi. Anasimama na kuagiza kwamba waombaji hao waletwe kwake. Waombaji hao wanamsihi: “Bwana, tunataka macho yetu yafunguliwe.” Yesu ‘anawasikitikia,’ kisha anayagusa macho yao, nao wanaanza kuona tena.a Papo hapo, wanaanza kumfuata Yesu.—Luka 18:35-43; Mathayo 20:29-34.
4. Ni kwa njia gani Yesu alitimiza unabii uliosema kwamba “atamsikitikia mtu wa hali ya chini”?
4 Yesu hakuonyesha huruma pindi hiyo tu. Pindi nyingi na katika hali mbalimbali, Yesu alichochewa sana kuwahurumia watu. Unabii wa Biblia ulitabiri kwamba “atamsikitikia mtu wa hali ya chini.” (Zaburi 72:13) Kupatana na maneno hayo, Yesu alijali hisia za wengine. Alikuwa tayari kuwasaidia watu. Huruma yake ilimchochea kuhubiri. Hebu tuone jinsi ambavyo vitabu vya Injili vinaonyesha huruma nyororo iliyomchochea Yesu kusema na kutenda, kisha tuzungumzie jinsi tunavyoweza kumwiga.
Kujali Hisia za Wengine
5, 6. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Yesu alielewa sana hisia za wengine?
5 Yesu alijali sana jinsi wengine walivyohisi. Alielewa hisia za watu waliokuwa wakiteseka, naye akawasikitikia. Ijapokuwa hakupatwa na mambo yote yaliyowapata, alihisi kwelikweli maumivu yao moyoni mwake. (Waebrania 4:15) Alipokuwa akimponya mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu kwa miaka 12, Yesu aliutaja ugonjwa huo kuwa “wenye kuhuzunisha,” hivyo akaonyesha anatambua kwamba mwanamke huyo alikuwa ametaabika na kuteseka sana. (Marko 5:25-34) Alipomwona Maria na wale waliokuwa pamoja naye wakiombolezea kifo cha Lazaro, huzuni yao ilimgusa sana moyoni hivi kwamba akaugua rohoni. Ingawa alijua atamfufua Lazaro baada ya muda mfupi, Yesu alisikitika sana hivi kwamba machozi yalimlengalenga.—Yohana 11:33, 35.
6 Pindi nyingine, mtu fulani mwenye ukoma alimjia Yesu na kumsihi: “Ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu, mtu mkamilifu ambaye hakupata kuwa mgonjwa hata siku moja, alifanya nini? Alimhurumia sana mtu huyo. Ndiyo, ‘alimsikitikia.’ (Marko 1:40-42) Kisha akafanya jambo lisilo la kawaida. Alijua vizuri kwamba, kulingana na Sheria, wenye ukoma walionwa kuwa si safi, nao hawakupaswa kuchangamana na watu wengine. (Mambo ya Walawi 13:45, 46) Bila shaka, Yesu angeweza kumponya mtu huyo bila kumgusa. (Mathayo 8:5-13) Hata hivyo, aliamua kunyoosha mkono wake na kumgusa mtu huyo mwenye ukoma, akisema: “Ninataka. Takasika.” Mara moja ule ukoma ukamtoka. Ndiyo, Yesu alionyesha kwelikweli kwamba alielewa hisia za wengine!
Onyesha “hisia-mwenzi”
7. Ni nini kinachoweza kutusaidia kusitawisha sifa ya kuelewa hisia za wengine, nasi tunaweza kuonyesha sifa hiyo jinsi gani?
7 Tukiwa Wakristo, tunatiwa moyo kumwiga Yesu kwa kuelewa hisia za wengine. Biblia inatusihi tuwe na “hisia-mwenzi.”b (1 Petro 3:8) Huenda isiwe rahisi kuelewa hisia za wale wanaougua magonjwa ya kudumu au walioshuka moyo sana, hasa ikiwa sisi wenyewe hatujawahi kupatwa na maumivu hayo. Lakini, kumbuka kwamba si lazima mtu awe amepatwa na mambo ambayo yamewapata wengine ili aelewe jinsi wanavyohisi. Yesu alielewa hisia za wagonjwa hata ingawa yeye mwenyewe hakupata kuwa mgonjwa. Hivyo basi, tunaweza kusitawisha namna gani sifa ya kuelewa hisia za wengine? Kwa kusikiliza kwa subira wale wanaoteseka wanapotueleza matatizo yao na hisia zao. Tunaweza kujiuliza, ‘Ikiwa ningekabili hali kama yao, ningehisi namna gani?’ (1 Wakorintho 12:26) Tukijitahidi kuhisi jinsi wengine wanavyohisi, itakuwa rahisi zaidi “kuzifariji nafsi zilizohuzunika.” (1 Wathesalonike 5:14) Nyakati nyingine, tunaweza kuonyesha kwamba tunaelewa jinsi wengine wanavyohisi si kwa maneno yetu tu bali hata kwa machozi. Andiko la Waroma 12:15 linasema: “Lieni pamoja na watu wanaolia.”
8, 9. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba anajali hisia za wengine?
8 Yesu aliwajali wengine, na matendo yake yalionyesha anajali hisia zao. Kumbuka wakati mtu aliyekuwa kiziwi na mwenye kizuizi cha usemi alipoletwa mbele yake. Labda akitambua kwamba mtu huyo ana wasiwasi, Yesu alifanya jambo ambalo kwa kawaida hakulifanya alipokuwa akiwaponya wengine: ‘Alimchukua kutoka katika umati.’ Alimponya mtu huyo faraghani, mbali na umati.—Marko 7:31-35.
9 Yesu alionyesha tena kwamba anajali wakati watu walipomletea mtu aliyekuwa kipofu na kumwomba amponye. Yesu ‘alimshika mkono yule mtu aliyekuwa kipofu, akamtoa nje ya kijiji.’ Kisha, akamponya mtu huyo hatua kwa hatua. Huenda hilo liliwezesha ubongo na macho ya mtu huyo yazoee hatua kwa hatua mambo ya kustaajabisha aliyoyaona. (Marko 8:22-26) Ndiyo, Yesu alijali sana!
10. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunajali hisia za wengine?
10 Kuwa wafuasi wa Yesu kunatia ndani kujali hisia za wengine. Hivyo, tunakuwa waangalifu kuhusu yale tunayosema, tukikumbuka kwamba kutumia ulimi bila kufikiri kunaweza kuumiza hisia za wengine. (Methali 12:18; 18:21) Wakristo hawapaswi kutumia maneno makali, usemi wa dharau, na dhihaka zenye kuchoma kwa kuwa wanajali hisia za watu wengine. (Waefeso 4:31) Enyi wazee, mnaweza kuonyesha jinsi gani kwamba mnajali hisia za wengine? Mnapotoa shauri, tumieni maneno yenye fadhili yanayoonyesha kwamba mnamheshimu anayeshauriwa. (Wagalatia 6:1) Nanyi wazazi, mnaweza kuonyesha jinsi gani kwamba mnajali hisia za watoto wenu? Mnapotoa nidhamu, jitahidini kufanya hivyo bila kuwaaibisha watoto wenu.—Wakolosai 3:21.
Kuwa Tayari Kuwasaidia Wengine
11, 12. Ni visa gani katika Biblia vinavyoonyesha kwamba Yesu hakuhitaji kuombwa ili awaonyeshe wengine huruma?
11 Wakati mwingine, Yesu aliwaonyesha watu huruma bila kuombwa msaada. Huruma ni sifa inayomchochea mtu kuchukua hatua au kutenda. Basi, haishangazi kwamba Yesu alichochewa na huruma nyororo kuwasaidia wengine, bila kuombwa afanye hivyo. Kwa mfano, umati mkubwa ulipokuwa pamoja naye kwa siku tatu bila kula chochote, hakuna mtu aliyehitaji kumwambia Yesu kwamba umati una njaa au kupendekeza achukue hatua fulani. Masimulizi yanasema: “Yesu akawaita wanafunzi wake na kusema: ‘Ninausikitikia umati, kwa sababu tayari wamekaa pamoja nami siku tatu nao hawana chakula; nami sitaki kuwaacha waende zao wakiwa wamefunga. Huenda wakazimia barabarani.’” Kisha, kwa hiari yake mwenyewe, akaulisha umati huo kimuujiza.—Mathayo 15:32-38.
12 Fikiria kisa kingine. Mwaka wa 31 W.K., Yesu alipokaribia jiji la Naini, aliona kisa chenye kuhuzunisha. Msafara wa maziko ulikuwa ukiondoka jijini, labda ukielekea makaburi ya karibu yaliyokuwa milimani ili kumzika “mwana mzaliwa-pekee wa . . . mjane.” Je, unaweza kuwazia huzuni ya mama huyo? Alikuwa karibu kumzika mwana wake wa pekee, naye hakuwa na mume wa kumliwaza. Kati ya watu wote waliokuwa katika msafara huo, Yesu ‘alimwona’ mjane huyo ambaye sasa alikuwa ameachwa bila mtoto. Mambo aliyoyaona yalimgusa moyo—ndiyo, ‘alimsikitikia.’ Hakuna aliyehitaji kumwomba Yesu msaada. Huruma aliyokuwa nayo moyoni ilimchochea kuchukua hatua. Hivyo, “akakaribia na kuligusa sanduku,” naye akamfufua kijana huyo. Kisha baada ya kumfufua, Yesu hakumwomba kijana huyo ajiunge na umati mkubwa uliokuwa ukisafiri pamoja Naye. Badala yake, Yesu ‘alimkabidhi kwa mama yake,’ akiwaunganisha tena kuwa familia na kuhakikisha kwamba mjane huyo angetunzwa.—Luka 7:11-15.
Wasaidie walio na uhitaji bila kuombwa ufanye hivyo
13. Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani kwa kuchukua hatua inayofaa ili kuwasaidia wenye uhitaji?
13 Tunaweza kufuata mfano wa Yesu jinsi gani? Ni kweli kwamba hatuwezi kuwalisha watu kimuujiza wala kuwafufua wafu. Hata hivyo, tunaweza kumwiga Yesu kwa kuwasaidia wenye uhitaji, bila kuombwa msaada. Huenda mwamini mwenzetu akakabili matatizo makubwa ya kiuchumi au kupoteza kazi. (1 Yohana 3:17) Huenda nyumba ya mjane ikahitaji kurekebishwa haraka. (Yakobo 1:27) Labda tunajua familia fulani iliyofiwa ambayo inahitaji faraja au msaada fulani. (1 Wathesalonike 5:11) Wengine wanapohitaji msaada kikweli, si lazima tungoje tuombwe ili tuwasaidie. (Methali 3:27) Tutachochewa na huruma kuchukua hatua inayofaa kutoa msaada kulingana na hali zetu. Kumbuka kwamba tendo dogo tu la fadhili au maneno machache ya kufariji yanayosemwa kutoka moyoni ni njia zenye matokeo sana za kuonyesha huruma.—Wakolosai 3:12.
Huruma Ilimchochea Kuhubiri
14. Kwa nini Yesu alitanguliza kazi ya kuhubiri habari njema?
14 Kama tulivyoona katika Sehemu ya 2 ya kitabu hiki, Yesu alituwekea mfano mzuri wa kuhubiri habari njema. Alisema: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu . . . kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Kwa nini alitanguliza kazi hiyo? Hasa kwa sababu anampenda Mungu. Lakini kuna jambo lingine lililomchochea Yesu: Huruma yake ya kutoka moyoni ilimchochea kushughulikia mahitaji ya kiroho ya wengine. Kati ya njia zote ambazo alionyesha huruma, hakuna iliyokuwa ya maana zaidi kuliko kuwashughulikia waliokuwa na njaa ya kiroho. Hebu tuchunguze visa viwili vinavyoonyesha maoni ya Yesu kuhusu watu ambao aliwahubiria. Uchunguzi huo utatusaidia kuchanganua nia zetu za kuhubiri.
15, 16. Eleza visa viwili vinavyoonyesha maoni ya Yesu kuhusu watu ambao aliwahubiria.
15 Mwaka wa 31 W.K., baada ya kujikakamua katika huduma kwa miaka miwili hivi, Yesu aliongeza jitihada zake kwa “kutembelea majiji na vijiji vyote” huko Galilaya. Mambo aliyoyaona yalimgusa moyo. Mtume Mathayo anasimulia hivi: “Alipouona umati akawasikitikia, kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:35, 36) Yesu aliwahurumia watu wa kawaida. Alijua vizuri kwamba wako katika hali mbaya ya kiroho. Alifahamu kwamba walikuwa wakitendewa vibaya na kupuuzwa kabisa na viongozi wa dini ambao walipaswa kuwa wachungaji wao. Akichochewa na huruma nyingi, Yesu alijitahidi sana kuwapa watu hao ujumbe wa tumaini. Walichohitaji hasa ni habari njema ya Ufalme wa Mungu.
16 Jambo kama hilo lilitukia miezi kadhaa baadaye, karibu na Pasaka ya mwaka wa 32 W.K. Wakati huo, Yesu na mitume wake walipanda mashua na kuvuka Bahari ya Galilaya wakitafuta mahali patulivu ili wapumzike. Lakini umati wa watu ukakimbia kando ya bahari mpaka upande ule mwingine kabla ya mashua hiyo kufika. Yesu alifanya nini? “Aliposhuka, akaona umati mkubwa, lakini akawasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:31-34) Kwa mara nyingine tena, Yesu ‘alisikitika’ kwa sababu watu walikuwa katika hali mbaya ya kiroho. Kama “kondoo wasio na mchungaji,” walikuwa na njaa ya kiroho, nao hawakuwa na la kufanya ila kujitafutia chakula cha kiroho. Yesu hakuhubiri ili atimize wajibu tu bali alichochewa na huruma.
Onyesha huruma unapohubiri
17, 18. (a) Ni nini kinachotuchochea tushiriki huduma? (b) Tunaweza kufanya nini ili kukuza sifa ya kuwahurumia wengine?
17 Tukiwa wafuasi wa Yesu, ni nini kinachotuchochea tushiriki huduma? Kama tulivyoona katika Sura ya 9 ya kitabu hiki, tuna mgawo au kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:19, 20; 1 Wakorintho 9:16) Lakini hatupaswi kushiriki kazi hiyo ili tutimize wajibu tu. Kumpenda Yehova kunatuchochea kuhubiri habari njema ya Ufalme wake. Pia, tunahubiri kwa sababu tunawahurumia wale walio na imani tofauti na yetu. (Marko 12:28-31) Basi, tunaweza kufanya nini ili kukuza sifa ya kuwahurumia wengine?
18 Tunahitaji kuwaona watu kama Yesu alivyowaona, kwamba “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” Hebu wazia umempata mwana-kondoo aliyepotea. Kwa kuwa hana mchungaji wa kumwongoza malishoni na kwenye maji, kiumbe huyo mwenye kusikitisha ana njaa na kiu. Je, hungemhurumia sana mwana-kondoo huyo? Je, hungejitahidi juu chini kumpa chakula na maji? Mwana-kondoo huyo ni kama watu wengi ambao bado hawaijui habari njema. Kwa kuwa wamepuuzwa na wachungaji bandia wa dini, wana njaa na kiu ya kiroho, nao hawana tumaini la kweli la wakati ujao. Tuna kile wanachohitaji, yaani, chakula cha kiroho chenye afya na maji ya kweli yenye kuburudisha yaliyo katika Neno la Mungu. (Isaya 55:1, 2) Tunapofikiria mahitaji ya kiroho ya watu walio karibu nasi, tunawahurumia sana. Tukiwahurumia watu sana kama alivyofanya Yesu, tutajitahidi juu chini kuwaeleza tumaini la Ufalme.
19. Tunaweza kufanya nini kumchochea mwanafunzi wa Biblia anayestahili kuhubiri hadharani?
19 Tunaweza kuwasaidiaje wengine wafuate mfano wa Yesu? Tuseme tunataka kumtia moyo mwanafunzi wa Biblia ambaye anastahili kuanza kuhubiri hadharani. Au labda tunataka kumsaidia mhubiri asiyetenda aanze tena kushiriki huduma kikamili. Tunaweza kuwasaidia watu kama hao jinsi gani? Tunapaswa kuchochea mioyo yao. Kumbuka kwamba kwanza Yesu ‘aliwasikitikia’ watu, kisha akawafundisha. (Marko 6:34) Kwa hiyo, ikiwa tunaweza kuwasaidia kusitawisha sifa ya huruma, haikosi mioyo yao itawachochea kumwiga Yesu na kuwahubiria wengine habari njema. Tunaweza kuwauliza: “Ni kwa njia gani kuukubali ujumbe wa Ufalme kumefanya maisha yako yawe bora? Namna gani watu ambao bado hawajaupata ujumbe huo—je, si kweli kwamba wao pia wanahitaji habari njema? Unaweza kuwasaidia jinsi gani?” Bila shaka, kumpenda Mungu na kutaka kumtumikia ndiyo mambo yanayotuchochea zaidi kuhubiri.
20. (a) Kuwa mfuasi wa Yesu kunatia ndani nini? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?
20 Kuwa mfuasi wa Yesu kunatia ndani mengi zaidi ya kusema tu maneno aliyosema na kuiga matendo yake. Tunahitaji kuwa na ‘mtazamo wa akili’ aliokuwa nao. (Wafilipi 2:5) Hivyo, tunashukuru kama nini kwamba Biblia inatufunulia maoni na hisia zilizomchochea Yesu kusema na kutenda! Tukiielewa “akili ya Kristo,” tutakuwa wenye kujali na kuwahurumia watu kutoka moyoni, na hivyo kuwatendea wengine kama Yesu alivyowatendea watu kwa ujumla. (1 Wakorintho 2:16) Katika sura inayofuata, tutazungumzia njia mbalimbali ambazo Yesu aliwaonyesha wafuasi wake upendo.
a Inasemekana kwamba neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘sikitikia,’ ni mojawapo ya maneno ya Kigiriki yanayoonyesha kwa mkazo zaidi hisia ya huruma. Kitabu kimoja kinasema kwamba neno hilo linadokeza “si kusikitika tu unapomwona mtu akiteseka, bali pia kutaka sana kumtuliza na kumwondolea mateso yake.”
b Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “hisia-mwenzi” linamaanisha “kuteseka pamoja na.”
-
-
‘Yesu Aliwapenda Mpaka Mwisho’‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 16
‘Yesu Aliwapenda Mpaka Mwisho’
1, 2. Yesu anatumia jinsi gani usiku wake wa mwisho pamoja na mitume wake, na kwa nini saa hizo za mwisho ni za maana sana kwake?
YESU anapokutana na mitume wake katika chumba cha juu cha nyumba fulani huko Yerusalemu, anajua kwamba huo ndio usiku wa mwisho atakaokuwa pamoja nao. Wakati wa kurudi kwa Baba yake unakaribia. Baada ya muda mfupi, Yesu atakamatwa na imani yake itajaribiwa sana. Ingawa anajua kwamba anakaribia kufa, bado anawahangaikia mitume wake.
2 Ijapokuwa Yesu tayari amewaambia mitume wake kwamba atawaacha, bado ana mengi ya kuwaambia ili kuwatia nguvu kwa ajili ya wakati ujao. Hivyo, anatumia muda mfupi unaobaki akiwafundisha mambo ya maana yatakayowasaidia kuendelea kuwa waaminifu. Hayo ni baadhi ya mambo yenye kusisimua na yenye kugusa moyo zaidi ambayo amepata kuwaambia. Lakini, kwa nini Yesu anawahangaikia sana mitume wake kuliko anavyojihangaikia? Kwa nini saa hizo za mwisho pamoja nao ni za maana sana kwake? Kwa ufupi, ni kwa sababu ya upendo. Ndiyo, anawapenda sana.
3. Je, Yesu alingoja mpaka usiku wa mwisho ili kuwaonyesha wafuasi wake kwamba anawapenda? Eleza.
3 Makumi ya miaka baadaye, mtume Yohana akiongozwa na roho aliandika hivi katika utangulizi wa masimulizi yake kuhusu usiku huo: “Kwa sababu alijua kabla ya sherehe ya pasaka kwamba saa yake ya kutoka katika ulimwengu huu kwenda kwa Baba ilikuwa imefika, Yesu, akiwa amewapenda walio wake mwenyewe waliokuwa ulimwenguni, akawapenda mpaka mwisho.” (Yohana 13:1) Yesu hakungoja mpaka usiku huo ili kuonyesha kwamba anawapenda “walio wake mwenyewe.” Wakati wote wa huduma yake, na katika njia mbalimbali, alithibitisha kwamba anawapenda wanafunzi wake. Tutafaidika kwa kuchunguza baadhi ya njia ambazo alionyesha upendo, kwa sababu kwa kumwiga, tunathibitisha kwamba sisi ni wanafunzi wake wa kweli.
Kuonyesha Subira
4, 5. (a) Kwa nini Yesu alihitaji kuwa na subira alipokuwa akishughulika na wanafunzi wake? (b) Yesu alifanya nini mitume wake watatu waliposhindwa kukesha katika bustani ya Gethsemane?
4 Kuna uhusiano kati ya upendo na subira. “Upendo ni wenye ustahimilivu,” lasema andiko la 1 Wakorintho 13:4, nao ustahimilivu unatia ndani kuwavumilia wengine kwa subira. Je, Yesu alihitaji subira aliposhughulika na wanafunzi wake? Bila shaka! Kama tulivyoona katika Sura ya 3, iliwachukua mitume muda mrefu kusitawisha unyenyekevu. Walibishana mara kadhaa kuhusu ni nani aliye mkuu kati yao. Yesu alifanya nini? Je, aliudhika, akawajibu kwa hasira, na kuwafungia kinyongo? Hapana, alizungumza nao kwa subira, hata wakati “bishano kali” lilipotokea kuhusu suala hilo usiku wa mwisho aliokuwa pamoja nao!—Luka 22:24-30; Mathayo 20:20-28; Marko 9:33-37.
5 Baadaye, usiku huohuo, Yesu alipoenda katika bustani ya Gethsemane pamoja na wale mitume waaminifu 11, subira yake ilijaribiwa tena. Akiwaacha mitume wake wanane, Yesu aliwachukua Petro, Yakobo, na Yohana na kuingia nao ndani zaidi katika bustani hiyo. Ndipo Yesu akawaambia: “Nafsi yangu ina huzuni sana, kiasi cha kufa. Kaeni hapa na mwendelee kukesha pamoja nami.” Akasonga mbele kidogo, na kuanza kusali kwa bidii. Baada ya kusali kwa muda mrefu, akarudi mahali walipokuwa wale mitume watatu. Aliwakuta wakifanya nini? Saa hiyo, saa aliyokuwa akijaribiwa vikali zaidi, walikuwa wamelala fofofo! Je, aliwakemea kwa sababu hawakukesha? Hapana, aliwahimiza kwa subira. Maneno yake yenye fadhili yalionyesha kwamba alielewa uchovu waliokuwa nao na udhaifu wao mbalimbali.a Alisema: “Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” Yesu aliendelea kuwa mwenye subira jioni hiyo hata aliporudi na kuwakuta wakiwa wamelala, si mara ya kwanza tu bali pia mara ya pili na ya tatu!—Mathayo 26:36-46.
6. Tunaposhughulika na wengine tunaweza kuonyesha subira kama Yesu jinsi gani?
6 Inatia moyo kujua kwamba Yesu hakuchoshwa na mitume wake. Mwishowe, subira yake ilikuwa na matokeo mazuri, kwa kuwa wanaume hao waaminifu walijifunza faida ya kuwa wanyenyekevu na wenye kukesha. (1 Petro 3:8; 4:7) Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani tunaposhughulika na wengine? Wazee hasa wanapaswa kuwa na subira. Huenda mzee akafikiwa na waamini wenzake wakiwa na matatizo, wakati ambapo amechoka au ana mahangaiko yake mwenyewe. Wakati mwingine, wale wanaohitaji msaada huenda wasikubali shauri mara moja. Hata hivyo, wazee wenye subira watawafundisha “kwa upole” na ‘kulitendea kundi kwa wororo.’ (2 Timotheo 2:24, 25; Matendo 20:28, 29) Wazazi pia wanapaswa kumwiga Yesu kwa kuonyesha subira, kwa kuwa wakati mwingine huenda watoto wasikubali shauri au rekebisho mara moja. Ikiwa wazazi wana upendo na subira, hawatachoka kuwazoeza watoto wao. Subira hiyo inaweza kutokeza thawabu kubwa kwelikweli.—Zaburi 127:3.
Kushughulikia Mahitaji Yao
7. Yesu alishughulikia namna gani mahitaji ya kimwili ya wanafunzi wake?
7 Upendo huonyeshwa kwa matendo yasiyo ya ubinafsi. (1 Yohana 3:17, 18) “Hautafuti faida zake wenyewe.” (1 Wakorintho 13:5) Upendo ulimchochea Yesu kushughulikia mahitaji ya kimwili ya wanafunzi wake. Mara nyingi alichukua hatua hata kabla hawajamweleza mahitaji yao. Alipoona kwamba wamechoka, alipendekeza waandamane naye kwenda ‘faraghani katika mahali pasipo na watu wapumzike kidogo.’ (Marko 6:31) Alipotambua kwamba wana njaa, alichukua hatua mara moja na kuwalisha watu hao pamoja na maelfu ya watu wengine waliokuwa wamekuja kumsikiliza akifundisha.—Mathayo 14:19, 20; 15:35-37.
8, 9. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alitambua mahitaji ya kiroho ya wanafunzi wake na kuyashughulikia? (b) Alipokuwa kwenye mti wa mateso, Yesu alionyesha jinsi gani kwamba anamhangaikia sana mama yake?
8 Yesu alitambua mahitaji ya kiroho ya wanafunzi wake na kuyashughulikia. (Mathayo 4:4; 5:3) Alipokuwa akifundisha, mara nyingi aliwafikiria wao hasa. Mahubiri ya Mlimani yalitolewa hasa kwa manufaa ya wanafunzi wake. (Mathayo 5:1, 2, 13-16) Alipofundisha kwa kutumia mifano, “kwa faragha alikuwa akiwaeleza wanafunzi wake mambo yote.” (Marko 4:34) Yesu alitabiri kwamba angemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili kuhakikisha kwamba wafuasi wake wanalishwa vizuri kiroho katika kipindi cha siku za mwisho. Mtumwa huyo mwaminifu, ni kikundi kidogo cha ndugu watiwa-mafuta wa Yesu walio duniani na amekuwa akiandaa chakula cha kiroho “kwa wakati unaofaa” tangu mwaka 1919 W.K.—Mathayo 24:45.
9 Siku ya kifo chake, Yesu alionyesha kwa njia yenye kugusa moyo sana jinsi anavyohangaikia hali ya kiroho ya wale anaowapenda. Hebu wazia jinsi ilivyokuwa. Yesu alikuwa kwenye mti wa mateso, akiwa na maumivu makali sana. Ili avute pumzi, alilazimika kujiinua kwa kujisukuma kwa miguu yake. Na haikosi kufanya hivyo kulisababisha maumivu makali sana kwa kuwa uzito wa mwili wake ulizidisha majeraha ya misumari katika miguu yake huku mgongo wake uliojeruhiwa kwa mijeledi ukisuguliwa na mti. Kwa kuwa mtu anahitaji kusawazisha pumzi anapozungumza, ingekuwa vigumu kwake kuzungumza na angepata maumivu makali. Hata hivyo, kabla tu hajafa, Yesu alitaja maneno yaliyoonyesha kwamba anampenda sana mama yake, Maria. Alipomwona Maria na mtume Yohana wakiwa wamesimama karibu, Yesu alizungumza kwa sauti inayoweza kusikika na mtu aliye karibu, na kumwambia mama yake: “Mwanamke, ona! Mwana wako!” Halafu akamwambia Yohana: “Ona! Mama yako!” (Yohana 19:26, 27) Yesu alijua kwamba mtume huyo mwaminifu angemtunza Maria kimwili na kiroho vilevile.b
Wazazi wanaojali ni wenye subira na wanashughulikia mahitaji ya watoto wao
10. Wazazi wanaweza kumwiga Yesu jinsi gani wanaposhughulikia mahitaji ya watoto wao?
10 Wazazi wanaojali wanaweza kufaidika kwa kumwiga Yesu. Baba anayeipenda familia yake kikweli, ataitegemeza kimwili. (1 Timotheo 5:8) Mara kwa mara, vichwa vya familia wenye usawaziko hupanga vipindi vya pumziko na tafrija. Isitoshe, wazazi Wakristo wanashughulikia mahitaji ya kiroho ya watoto wao. Jinsi gani? Wazazi hao hupanga kuwa na funzo la Biblia kwa ukawaida, nao wanajitahidi kufanya pindi hizo za funzo ziwajenge na kuwafurahisha watoto wao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Kupitia maneno yao na mfano wao, wazazi wanawafundisha watoto wao kwamba huduma ni utendaji wa maana na kwamba kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni sehemu ya maana ya utendaji wao wa kiroho.—Waebrania 10:24, 25.
Kuwa Tayari Kusamehe
11. Yesu aliwafundisha wafuasi wake nini kuhusu kusamehe?
11 Kusamehe ni njia moja ya kuonyesha upendo. (Wakolosai 3:13, 14) Andiko la 1 Wakorintho 13:5 linasema upendo “hauweki hesabu ya ubaya.” Pindi nyingi, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake faida ya kusamehe. Aliwahimiza wawasamehe wengine “si, Mpaka mara 7, bali, Mpaka mara 77,” yaani, bila kipimo. (Mathayo 18:21, 22) Aliwafundisha kwamba mtenda-dhambi anapaswa kusamehewa iwapo baada ya kukemewa, anatubu. (Luka 17:3, 4) Hata hivyo, Yesu hakuwa kama Mafarisayo wanafiki waliofundisha kwa maneno tu; alifundisha kupitia mfano wake pia. (Mathayo 23:2-4) Hebu tuone jinsi Yesu alivyoonyesha kwamba alikuwa tayari kusamehe hata wakati rafiki aliyemtumaini sana alipotenda kinyume na matarajio yake.
12, 13. (a) Petro alifanya jambo gani lililomsikitisha Yesu usiku ambao Yesu alikamatwa? (b) Baada ya kufufuliwa, matendo ya Yesu yalionyesha jinsi gani kwamba alikuwa mwenye kusamehe kama alivyofundisha?
12 Yesu alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na mtume Petro, aliyekuwa mchangamfu na wakati mwingine alitenda bila kufikiri. Yesu alitambua sifa nzuri za Petro, naye akampa mapendeleo ya pekee. Petro, Yakobo, na Yohana walijionea miujiza fulani ambayo mitume wale wengine hawakuona. (Mathayo 17:1, 2; Luka 8:49-55) Kama tulivyotangulia kuona, Petro alikuwa mmoja wa mitume waliokuwa pamoja na Yesu alipoingia ndani zaidi ya bustani ya Gethsemane usiku ambao alikamatwa. Hata hivyo, usiku huohuo Yesu aliposalitiwa na kukamatwa, Petro na wale mitume wengine walimwacha na kutoroka. Baadaye, Petro alionyesha uhodari kwa kusimama nje huku Yesu akishtakiwa kwa uwongo. Lakini, baadaye Petro aliingiwa na woga, naye akafanya kosa zito—mara tatu alikana kwa uwongo kwamba hata hamjui Yesu! (Mathayo 26:69-75) Yesu alifanya nini? Ungefanya nini ikiwa rafiki yako wa karibu angefanya jambo kama hilo?
13 Yesu alikuwa tayari kumsamehe Petro. Alijua kwamba dhambi hiyo ilimsumbua sana Petro. Kwa kweli, mtume huyo aliyetubu ‘alianza kulia.’ (Marko 14:72) Yesu alipofufuliwa, alimtokea Petro, huenda ili kumfariji na kumtia moyo. (Luka 24:34; 1 Wakorintho 15:5) Baadaye, kabla ya miezi miwili kupita, Yesu alimkweza Petro kwa kumruhusu atoe ushahidi mbele ya umati huko Yerusalemu katika siku ya Pentekoste. (Matendo 2:14-40) Na tukumbuke pia kwamba Yesu hakuwawekea kinyongo mitume wake kwa sababu walimwacha. Badala yake, baada ya kufufuliwa, bado aliwaita “ndugu zangu.” (Mathayo 28:10) Je, si wazi kwamba mbali na kuwahimiza watu wawasamehe wengine, Yesu mwenyewe alikuwa mwenye kusamehe?
14. Kwa nini tunapaswa kujifunza kuwasamehe wengine, nasi tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tuko tayari kusamehe?
14 Tukiwa wanafunzi wa Kristo, tunahitaji kujifunza kuwasamehe wengine. Kwa nini? Tofauti na Yesu, sisi si wakamilifu, na ndivyo na wale ambao huenda wakatukosea. Mara kwa mara, sisi sote tunajikwaa katika neno na tendo. (Waroma 3:23; Yakobo 3:2) Kwa kuwasamehe wengine ikiwa kuna msingi wa kuwaonyesha rehema, tunafungua njia ili Mungu atusamehe. (Marko 11:25) Basi, tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tuko tayari kuwasamehe wale ambao huenda wakatukosea? Mara nyingi, upendo unatusaidia kuachilia makosa madogo-madogo tunayotendewa na wengine. (1 Petro 4:8) Wale waliotukosea wanapotubu kikweli, kama Petro alivyofanya, bila shaka, tungependa kumwiga Yesu kwa kuwa tayari kuwasamehe. Badala ya kuwawekea kinyongo, tunatenda kwa hekima tunapowasamehe. (Waefeso 4:32) Kwa kufanya hivyo, tunachangia amani kutanikoni, na pia amani yetu wenyewe ya akilini na moyoni.—1 Petro 3:11.
Kuwatumaini
15. Kwa nini Yesu aliwatumaini wanafunzi wake ingawa hawakuwa wakamilifu?
15 Upendo unahusianishwa na tumaini. Upendo “huamini mambo yote.”c (1 Wakorintho 13:7) Upendo wa Yesu ulimsukuma kuwatumaini wanafunzi wake ingawa hawakuwa wakamilifu. Aliwatumaini na kuamini kwamba kwa kweli wanampenda Yehova na wanataka kufanya mapenzi Yake. Hata walipokosea, Yesu hakutilia shaka nia zao. Kwa mfano, pindi moja inaonekana mitume Yakobo na Yohana walimtuma mama yao amwombe Yesu awape mitume hao pendeleo la kuketi kando yake katika Ufalme wake. Hata hivyo, Yesu hakutilia shaka ushikamanifu wao wala kuwanyang’anya pendeleo la kuwa mitume.—Mathayo 20:20-28.
16, 17. Yesu aliwapa wanafunzi wake kazi gani?
16 Yesu alionyesha kwamba anawatumaini wanafunzi wake kwa kuwapa kazi mbalimbali. Pindi mbili alipotokeza chakula kingi kimuujiza na kulisha umati wa watu, aliwapa wanafunzi wake kazi ya kugawa chakula hicho. (Mathayo 14:19; 15:36) Aliwapa Petro na Yohana mgawo wa kwenda Yerusalemu na kufanya matayarisho kwa ajili ya Pasaka yake ya mwisho. Walitafuta mwana-kondoo, divai, mkate usio na chachu, mboga chungu za majani, na vitu vingine vya maana vilivyohitajiwa. Huo haukuwa mgawo mdogo, kwa kuwa Sheria ya Musa iliagiza Pasaka iadhimishwe ifaavyo, naye Yesu alihitaji kutii Sheria hiyo. Isitoshe, baadaye usiku huo, Yesu alitumia divai hiyo na mkate huo usio na chachu kuwa mifano muhimu alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake.—Mathayo 26:17-19; Luka 22:8, 13.
17 Yesu aliwapa wanafunzi wake madaraka mazito hata zaidi. Kama tulivyoona mapema, alikikabidhi kikundi kidogo cha wafuasi wake watiwa-mafuta hapa duniani daraka zito la kutayarisha na kugawa chakula cha kiroho. (Luka 12:42-44) Pia, kumbuka kwamba aliwapa wanafunzi wake kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:18-20) Hata sasa, ingawa anatawala mbinguni na hatuwezi kumwona, Yesu amewapa watu wenye sifa za kiroho, “zawadi katika wanadamu,” daraka la kutunza kutaniko lake lililo duniani.—Waefeso 4:8, 11, 12.
18-20. (a) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunawatumaini waamini wenzetu? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kuiga mfano wa Yesu wa kuwa tayari kuwapa wengine migawo? (c) Ni nini kitakachozungumziwa katika sura inayofuata?
18 Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani tunaposhughulika na watu wengine? Kuwatumaini waamini wenzetu kunaonyesha kwamba tunawapenda. Tusisahau kwamba upendo huangalia mambo mazuri bali si mabaya. Wakati ambapo watu wengine wanatuvunja moyo, jambo ambalo mara kwa mara linatokea, upendo utatuzuia tusikate kauli mara moja kwamba nia zao ni mbovu. (Mathayo 7:1, 2) Tukiwa na maoni yanayofaa kuhusu waamini wenzetu, tutawatendea kwa njia zenye kuwajenga badala ya kuwabomoa.—1 Wathesalonike 5:11.
19 Je, tunaweza kumwiga Yesu kwa kuwa tayari kuwapa wengine mapendeleo? Ndugu walio na madaraka kutanikoni wanapaswa kuwapa wengine migawo inayowafaa na inayotimiza kusudi fulani wakiamini kwamba ndugu hao watafanya yote wanayoweza. Kwa njia hiyo, wazee wenye uzoefu wanaweza kuwazoeza vijana wanaostahili ambao ‘wanajitahidi kufikia’ mapendeleo ya kulisaidia kutaniko. (1 Timotheo 3:1; 2 Timotheo 2:2) Mazoezi hayo ni ya maana. Yehova anapoendelea kuharakisha ukuzi wa Ufalme, wanaume wanaostahili watahitaji kuzoezwa kushughulikia ongezeko hilo.—Isaya 60:22.
20 Yesu alituwekea mfano mzuri kwa kuwapenda wengine. Kati ya mambo yote tunayoweza kuiga kutoka kwa Yesu, jambo la maana zaidi ni upendo. Katika sura inayofuata, tutazungumzia njia kuu aliyotuonyesha upendo—kuwa tayari kuutoa uhai wake.
a Mbali na uchovu wa kimwili, kuna jambo lingine lililofanya mitume hao walale. Masimulizi kama hayo kwenye Luka 22:45 yanasema kwamba Yesu ‘aliwakuta wakisinzia kwa huzuni.’
b Inaonekana kufikia wakati huo Maria alikuwa mjane, na huenda bado wale watoto wake wengine hawakuwa wanafunzi wa Yesu.—Yohana 7:5.
c Bila shaka, haimaanishi kwamba upendo ni mpumbavu au unadanganyika upesi. Badala yake, inamaanisha kwamba upendo hauchambui au kuwa na shaka juu ya mambo bila sababu. Upendo huepuka kutilia shaka nia za wengine au kukata kauli kwamba hawana nia nzuri.
-
-
“Hakuna Aliye na Upendo Mkuu Kuliko Huu”‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu’
-
-
Sura ya 17
“Hakuna Aliye na Upendo Mkuu Kuliko Huu”
1-4. (a) Umati wenye hasira uliokusanyika nje ya jumba la gavana unafanya nini Pilato anapomleta Yesu? (b) Yesu anafanya nini anapoaibishwa na kuteswa, na ni maswali gani tunayopaswa kufikiria kwa uzito?
“TAZAMENI! Mwanamume!” Gavana Mroma Pontio Pilato anasema maneno hayo anapomleta Yesu Kristo kwenye umati wenye hasira uliokusanyika nje ya jumba la gavana wakati wa mapambazuko, siku ya Pasaka ya mwaka wa 33 W.K. (Yohana 19:5) Siku chache tu mapema, umati huo ulimsifu Yesu alipoingia Yerusalemu kwa shangwe ya ushindi akiwa Mfalme aliyewekwa na Mungu. Hata hivyo, usiku huu, umati huo wenye chuki unamwona kwa njia tofauti kabisa.
2 Yesu amevikwa vazi la zambarau kama la wafalme, na ana taji kichwani. Hata hivyo, kuvikwa kwake vazi hilo, linaloufunika mgongo wake unaotoka damu kwa sababu ya kupigwa mijeledi, na taji, lililotengenezwa kwa miiba na kushindiliwa kwenye kichwa chake kinachotoka damu, ni njia ya kudhihaki cheo chake cha kifalme. Watu wakiwa wamechochewa na wakuu wa makuhani, wanamkataa mwanamume aliyepigwa aliye mbele yao. Makuhani wanapaaza sauti hivi: “Mtundike mtini! Mtundike mtini!” Wakitaka sana auawe, wanapiga kelele wakisema: “Anapaswa kufa.”—Yohana 19:1-7.
3 Yesu anavumilia aibu zote hizo na mateso hayo kwa uhodari na bila kunung’unika.a Yuko tayari kabisa kufa. Baadaye, siku hiyohiyo ya Pasaka, anakubali kwa hiari kufa kifo cha kikatili kwenye mti wa mateso.—Yohana 19:17, 18, 30.
4 Kwa kuutoa uhai wake, Yesu alionyesha kwamba alikuwa rafiki wa kweli wa wafuasi wake. Alisema: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Hilo linatokeza maswali tunayopaswa kufikiria kwa uzito. Je, kweli ilikuwa lazima Yesu apatwe na mambo hayo kisha afe? Kwa nini alikubali kufa? Tukiwa “rafiki zake” na wafuasi wake, tunaweza kuiga mfano wake jinsi gani?
Kwa Nini Ilikuwa Lazima Yesu Ateseke na Kufa?
5. Yesu alijuaje mambo ambayo yangempata?
5 Akiwa Masihi aliyeahidiwa, Yesu alijua mambo ambayo yangempata. Alijua kwamba unabii mwingi ulio katika Maandiko ya Kiebrania ulitabiri kinaganaga jinsi ambavyo Masihi angeteswa na kufa. (Isaya 53:3-7, 12; Danieli 9:26) Mara kadhaa aliwatayarisha wanafunzi wake kwa ajili ya majaribu ambayo yangempata. (Marko 8:31; 9:31) Alipokuwa akielekea Yerusalemu kuadhimisha Pasaka kwa mara ya mwisho, aliwaambia mitume wake hivi waziwazi: “Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani, na waandishi, nao watamhukumia kifo na kumtia mikononi mwa watu wa mataifa, nao watamdhihaki, watamtemea mate, watampiga mijeledi na kumuua.” (Marko 10:33, 34) Hayo hayakuwa maneno matupu. Kama tulivyoona, kwa kweli Yesu alidhihakiwa, akatemewa mate, akapigwa mijeledi, na kuuawa.
6. Kwa nini ilikuwa lazima Yesu ateseke na kufa?
6 Hata hivyo, kwa nini ilikuwa lazima Yesu ateseke na kufa? Kwa sababu za maana sana. Kwanza, Yesu alithibitisha utimilifu wake na kutegemeza enzi kuu ya Yehova kwa kuendelea kuwa mshikamanifu. Kumbuka, Shetani alidai kwa uwongo kwamba wanadamu wanamtumikia Mungu kwa sababu ya ubinafsi tu. (Ayubu 2:1-5) Kwa kuendelea kuwa mwaminifu “mpaka kifo . . . juu ya mti wa mateso,” Yesu alijibu kwa njia nzuri zaidi dai la Shetani lisilo na msingi. (Wafilipi 2:8; Methali 27:11) Pili, kuteseka na kufa kwa Masihi kuliandaa upatanisho kwa ajili ya dhambi za wengine. (Isaya 53:5, 10; Danieli 9:24) Yesu alitoa “nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi,” akitufungulia njia ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. (Mathayo 20:28) Tatu, kwa kuvumilia magumu na mateso mbalimbali, Yesu ‘alijaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe.’ Kwa hiyo, yeye ni Kuhani Mkuu mwenye huruma, anayeweza “kuusikitikia udhaifu wetu.”—Waebrania 2:17, 18; 4:15.
Kwa Nini Yesu Alikubali Kuutoa Uhai Wake?
7. Yesu aliacha nini alipokuja duniani?
7 Ili kuelewa vizuri jambo ambalo Yesu alikubali kufanya, wazia hali hii: Ni mwanamume gani anayeweza kuiacha familia yake na makao yake na kuhamia nchi ya kigeni akijua kwamba wengi wa wakaaji wa nchi hiyo watamkataa, naye ataaibishwa, ateswe, na mwishowe auawe? Sasa, hebu fikiria alilofanya Yesu. Kabla ya kuja duniani, alikuwa na cheo cha pekee mbinguni kando ya Baba yake. Hata hivyo, Yesu alikubali kuacha makao yake mbinguni na kuja duniani akiwa mwanadamu. Alifanya hivyo akijua angekataliwa na wengi na kuaibishwa kikatili, kuteswa vikali, na kufa kifo cha maumivu. (Wafilipi 2:5-7) Ni nini kilichomchochea Yesu ajidhabihu kiasi hicho?
8, 9. Ni nini kilichomchochea Yesu autoe uhai wake?
8 Sababu kuu iliyomchochea Yesu kujidhabihu ni kuwa alimpenda sana Baba yake. Kuvumilia kwa Yesu kulithibitisha kwamba anampenda Yehova. Upendo huo ulimfanya Yesu ahangaikie jina na sifa ya Baba yake. (Mathayo 6:9; Yohana 17:1-6, 26) Kati ya mambo yote, Yesu alitaka kuona jina la Baba yake likiondolewa lawama. Hivyo basi, Yesu aliliona kuwa pendeleo kuteseka kwa ajili ya uadilifu kwa kuwa alijua kwamba utimilifu wake utachangia kulitakasa jina zuri la Baba yake.—1 Mambo ya Nyakati 29:13.
9 Kuna sababu nyingine iliyomchochea Yesu kutoa uhai wake—anawapenda wanadamu. Alianza kuwapenda tangu walipoumbwa. Biblia inafunua jinsi Yesu alivyohisi muda mrefu kabla ya kuja duniani inaposema: “Vitu nilivyopenda sana vilihusiana na wana wa binadamu.” (Methali 8:30, 31) Alionyesha waziwazi upendo wake alipokuwa duniani. Kama tulivyoona katika sura tatu zinazotangulia, Yesu alionyesha katika njia nyingi kwamba anawapenda wanadamu wote na hasa wafuasi wake. Lakini Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., alitoa nafsi yake kwa ajili yao. (Yohana 10:11) Kwa kweli, hiyo ndiyo njia kuu zaidi ambayo alionyesha kwamba anatupenda. Je, tunapaswa kumwiga katika njia hiyo? Ndiyo. Isitoshe, tunaagizwa tufanye hivyo.
“Mpendane; Kama Vile Ambavyo Nimewapenda Ninyi”
10, 11. Yesu aliwapa wafuasi wake amri gani mpya, nayo inatia ndani nini, na kwa nini tunapaswa kuitii?
10 Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwaambia wanafunzi wake wa karibu hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) “Mpendane”—kwa nini hiyo ni “amri mpya”? Tayari Sheria ya Musa ilikuwa imeagiza: “Mpende mwenzako [au, jirani yako] kama wewe mwenyewe.” (Mambo ya Walawi 19:18) Lakini amri hiyo mpya inatutaka tuonyeshe upendo mkubwa hata zaidi, upendo ambao utatuchochea kuutoa uhai wetu wenyewe kwa ajili ya wengine. Yesu mwenyewe alitaja hilo waziwazi aliposema: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile nilivyowapenda ninyi. Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:12, 13) Ni kana kwamba amri hiyo mpya inasema: “Wapende wengine, si kama unavyojipenda, bali kuliko unavyojipenda.” Bila shaka, Yesu alionyesha upendo huo katika maisha yake na vilevile kwa kuwa tayari kufa.
11 Kwa nini tunapaswa kutii amri hiyo mpya? Kumbuka kwamba Yesu alisema: “Kwa jambo hili [yaani, upendo wa kujidhabihu] wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu.” Ndiyo, upendo wa kujidhabihu unatutambulisha kuwa Wakristo wa kweli. Tunaweza kuufananisha upendo huo na beji ya kujitambulisha. Wajumbe ambao huhudhuria makusanyiko ya kila mwaka ya Mashahidi wa Yehova huvaa beji. Beji hiyo inamtambulisha aliyeivaa, ikionyesha jina na kutaniko lake. Upendo wa kujidhabihu kwa ajili ya wengine ni “beji” inayowatambulisha Wakristo wa kweli. Yaani, upendo tunaoonyeshana unapaswa kuonekana wazi sana hivi kwamba unakuwa ishara, au beji, inayojulisha watazamaji kwamba bila shaka sisi ni wafuasi wa kweli wa Kristo. Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza, ‘Je, “beji” yangu ya upendo wa kujidhabihu inaonekana waziwazi maishani mwangu?’
Upendo wa Kujidhabihu Unatia Ndani Nini?
12, 13. (a) Tunapaswa kujidhabihu kiasi gani kuonyesha kwamba tunapendana? (b) Kujidhabihu ni nini?
12 Tukiwa wafuasi wa Yesu tunapaswa kupendana kama vile alivyotupenda. Hilo linamaanisha kuwa tayari kujidhabihu kwa ajili ya waamini wenzetu. Tunapaswa kujidhabihu kiasi gani? Biblia inatuambia: “Kwa hili tumeujua upendo, kwa sababu huyo aliitoa nafsi yake kwa ajili yetu; na sisi tuko chini ya wajibu kuzitoa nafsi zetu kwa ajili ya ndugu zetu.” (1 Yohana 3:16) Kama Yesu, tunapaswa kuwa tayari hata kufa kwa ajili ya ndugu zetu ikihitajika. Wakati wa mateso, afadhali tufe kuliko kuwasaliti ndugu zetu wa kiroho na hivyo kuhatarisha maisha yao. Katika nchi ambazo zimegawanyika kwa sababu ya mizozo ya kikabila au kijamii, tutakuwa tayari kuhatarisha maisha yetu ili kuwalinda ndugu zetu, haidhuru jamii au kabila lao. Mataifa yanapoenda vitani, afadhali tufungwe au hata kufa kuliko kupigana na waamini wenzetu au mtu mwingine yeyote.—Yohana 17:14, 16; 1 Yohana 3:10-12.
13 Kuwa tayari kufa kwa ajili ya ndugu zetu siyo njia pekee ya kuonyesha upendo wa kujidhabihu. Kwa kweli, ni wachache kati yetu ambao huenda wakahitaji kutoa dhabihu kubwa kama hiyo. Hata hivyo, ikiwa tunawapenda ndugu zetu kiasi cha kufa kwa ajili yao, je, hatupaswi kuwa tayari kujidhabihu kwa njia ndogo-ndogo, kujitolea kuwasaidia sasa? Kujidhabihu ni kujinyima mapendezi na starehe kwa faida za wengine. Tunafanya hivyo kwa kutanguliza mahitaji yao na kuwahangaikia hata ikiwa si rahisi. (1 Wakorintho 10:24) Tunaweza kujidhabihu katika njia gani mbalimbali?
Katika Kutaniko na Katika Familia
14. (a) Wazee wanajidhabihu katika njia gani? (b) Una maoni gani kuhusu wazee wa kutaniko lenu ambao wanafanya kazi kwa bidii?
14 Wazee wa kutaniko wanajidhabihu sana ili ‘kulichunga kundi.’ (1 Petro 5:2, 3) Mbali na kutunza familia zao wenyewe, huenda wakahitaji kutumia wakati wao jioni au mwishoni mwa juma ili kushughulikia mambo ya kutaniko, kutia ndani kutayarisha migawo watakayokuwa nayo katika mikutano, kufanya ziara za uchungaji, na kushughulikia visa vya hukumu. Wazee wengi wanajidhabihu hata zaidi, wakifanya kazi kwa bidii katika makusanyiko na kutumikia wakiwa washiriki wa Halmashauri za Uhusiano na Hospitali, Vikundi vya Kuwatembelea Wagonjwa, na Halmashauri za Ujenzi za Mkoa. Ninyi wazee, msisahau kwamba mnaonyesha upendo wa kujidhabihu mnapotumikia kwa hiari mkitumia wakati wenu, nguvu zenu, na mali zenu kulichunga kundi. (2 Wakorintho 12:15) Bidii yenu isiyo na ubinafsi inathaminiwa na Yehova na vilevile kutaniko mnalochunga.—Wafilipi 2:29; Waebrania 6:10.
15. (a) Wake za wazee hujidhabihu kwa njia gani? (b) Una maoni gani kuhusu wake wanaowaunga mkono waume zao kwa kudhabihu wakati ambao wangetumia pamoja nao ili kutaniko lenu lifaidike?
15 Hata hivyo, namna gani wake za wazee? Je, si kweli kwamba dada hao wenye kuwaunga mkono wanajidhabihu pia ili waume zao walitunze kundi? Ni kweli kwamba mke hujidhabihu mume wake anapotumia wakati kwa ajili ya mambo ya kutaniko, wakati ambao angeweza kuutumia pamoja na familia yake. Wafikirie pia wake za waangalizi wanaosafiri na jinsi wanavyojidhabihu ili kusafiri pamoja na waume zao kutoka kutaniko moja kwenda lingine na kutoka mzunguko mmoja kwenda mwingine. Wao huacha makao yao wenyewe na nyakati nyingine wanalazimika kulala katika kitanda tofauti kila juma. Wake wanaotanguliza faida za kutaniko kwa hiari wanastahili pongezi kwa kuonyesha upendo wa kujidhabihu.—Wafilipi 2:3, 4.
16. Wazazi Wakristo hujidhabihu jinsi gani kwa ajili ya watoto wao?
16 Ni kwa njia gani tunaweza kuonyesha upendo wa kujidhabihu katika familia? Ninyi wazazi mnajidhabihu sana ili kutosheleza mahitaji ya watoto wenu na kuwalea “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Waefeso 6:4) Huenda mkalazimika kufanya kazi ngumu zenye kuchosha, tena kwa muda mrefu, ili kuwaandalia watoto chakula na kuhakikisha kwamba wana mavazi na makao mazuri. Huenda hata mkajinyima ili kuhakikisha kwamba mnatosheleza mahitaji ya msingi ya watoto wenu. Pia, ninyi hutia bidii sana kujifunza na watoto wenu, kwenda nao kwenye mikutano ya Kikristo, na kwenda pamoja nao katika huduma ya shambani. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Upendo wenu wa kujidhabihu unamfurahisha Mwanzilishi wa maisha ya familia na kuwawezesha watoto wenu kuwa na tumaini la uzima wa milele.—Methali 22:6; Waefeso 3:14, 15.
17. Waume Wakristo wanaweza kumwiga Yesu jinsi gani kwa kutokuwa na ubinafsi?
17 Ninyi waume, mnaweza kumwiga Yesu jinsi gani kwa kuonyesha upendo wa kujidhabihu? Biblia inajibu: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujitoa mwenyewe kwa ajili yake.” (Waefeso 5:25) Kama tulivyoona, Yesu aliwapenda wafuasi wake sana kiasi cha kufa kwa ajili yao. Mume Mkristo huiga mtazamo usio na ubinafsi alioonyesha Yesu, ambaye “hakujipendeza mwenyewe.” (Waroma 15:3) Mume kama huyo anatanguliza mahitaji na mapendezi ya mke wake kwa hiari. Hasisitizi kwa ushupavu kwamba kila kitu kifanywe anavyotaka, bali yuko tayari kukubali maoni ya mke wake ikiwa hakuna kanuni ya Kimaandiko inayohusika. Mume anayeonyesha upendo wa kujidhabihu hupata kibali cha Yehova, naye anapendwa na kuheshimiwa na mke na watoto wake.
Utafanya Nini?
18. Ni nini kinachotuchochea kutii ile amri mpya ya kupendana?
18 Si rahisi kutii ile amri mpya ya kupendana, hata hivyo, kuna jambo kuu ambalo linatuchochea kufanya hivyo. Paulo aliandika hivi: “Upendo alio nao Kristo hutulazimisha, kwa sababu hili ndilo tumehukumu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote . . . , naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.” (2 Wakorintho 5:14, 15) Kwa kuwa Yesu alikufa kwa ajili yetu, je, hatupaswi kujitahidi kuishi kwa ajili yake? Tunaweza kufanya hivyo kwa kuwaonyesha wengine upendo wa kujidhabihu kama vile alivyofanya.
19, 20. Ni zawadi gani yenye thamani kubwa ambayo Yehova ametupa, nasi tunaweza kufanya nini kuonyesha kwamba tunaikubali?
19 Yesu hakuwa akitia chumvi wakati ambapo alisema maneno haya: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Kwa kukubali kuitoa nafsi yake kwa ajili yetu, alionyesha kwa njia kuu zaidi upendo wake kwetu. Hata hivyo, kuna mwingine ambaye ametuonyesha upendo mkubwa hata zaidi. Yesu mwenyewe alieleza: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Mungu anatupenda sana hivi kwamba alimtoa Mwana wake awe fidia, na kutukomboa kutoka katika dhambi na kifo. (Waefeso 1:7) Fidia ni zawadi yenye thamani kubwa kutoka kwa Yehova, hata hivyo hatulazimishi tuikubali.
20 Lazima kila mmoja wetu afanye uamuzi wake mwenyewe ikiwa ataikubali zawadi hiyo kutoka kwa Yehova. Jinsi gani? Kwa ‘kumwamini’ Mwana wake. Hata hivyo, haitoshi tu kusema kwamba tuna imani. Lazima tuonyeshe imani yetu kwa matendo na jinsi tunavyoishi. (Yakobo 2:26) Tunaonyesha kwamba tunamwamini Yesu Kristo kwa kufuata mfano wake kila siku. Kufanya hivyo kutatuletea baraka nyingi sasa na wakati ujao, kama vile sura ya mwisho ya kitabu hiki itakavyoonyesha.
-