Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Wakati Maneno Yanapokuwa Silaha
    Amkeni!—1996 | Oktoba 22
    • Wakati Maneno Yanapokuwa Silaha

      “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga.”—MITHALI 12:18.

      “MNAMO majuma machache baada ya arusi, mambo yakaanza,” asema Elaine.a “Maneno yasiyo na fadhili, maneno yenye kushusha, na jitihada za kunifedhehesha. Sikuweza kushindana na mume wangu. Akili yake yenye kufahamu mambo upesi na ulimi wake wa haraka vingeweza kugeuza na kupotosha kila kitu nilichosema.”

      Katika ndoa yake yote Elaine amekuwa chini ya aina ya udhia wenye athari inayoongezeka ambayo haiachi makovu na ambayo haionewi huruma. Kwa kuhuzunisha, hali yake haijaboreka kadiri wakati upitavyo. “Tumeoana kwa zaidi ya miaka 12 sasa,” yeye asema. “Hakuna siku ipitayo bila yeye kuwa mwenye kunichambua na mwenye kunikejeli, akitumia usemi wenye kudhulumu, ulio mchafu.”

      Biblia haitii chumvi inaposema kwamba ulimi waweza kuwa “kitu kisichotawalika chenye ubaya, . . . umejaa sumu yenye kuleta kifo.” (Yakobo 3:8, NW; linganisha Zaburi 140:3.) Hili ni kweli hasa katika ndoa. “Yeyote yule aliyesema ‘vijiti na mawe vyaweza kuvunja mifupa yangu lakini maneno hayawezi kamwe kuniumiza’ alikosea vibaya sana,” asema mke mmoja aitwaye Lisa.—Mithali 15:4.

      Waume pia waweza kuwa shabaha ya ukatili wa maneno. “Je, unajua jinsi ilivyo kuishi na mwanamke ambaye daima hukuita mwongo, mjinga au maneno mabaya hata zaidi?” auliza Mike, ambaye ndoa yake ya miaka minne pamoja na Tracy yaelekea kwenye talaka. “Siwezi hata kurudia mambo aniambiayo mbele ya waandamani wenye kuheshimika. Hiyo ndiyo sababu siwezi kuzungumza naye na inayofanya nibaki kazini hadi kuchelewa mno. Kuna amani nyingi zaidi kazini kuliko kuja nyumbani.”—Mithali 27:15.

      Akiwa na sababu yenye msingi mzuri, mtume Paulo alionya Wakristo hivi: “Acheni . . . kupiga kelele na usemi wenye kuudhi viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31, NW) Lakini “usemi wenye kuudhi” ni nini? Paulo autofautisha na “kupiga kelele” (Kigiriki, krau·geʹ), ambako humaanisha kupaaza sauti tu. “Usemi wenye kuudhi” (Kigiriki, bla·sphe·miʹa) hurejezea zaidi yaliyo katika ujumbe. Ikiwa huo ni wa kukandamiza, wenye nia ya kudhuru, wenye kuharibia heshima, au wenye kutukana, basi huo ni usemi wenye kuudhi—iwe waja kwa njia ya mpaazo wa sauti au kwa mnong’ono.

      Majeraha ya Maneno

      Tabia ya usemi mkali yaweza kudhoofisha ndoa, kama tu vile mawimbi ya bahari yamomonyoavyo mwamba mgumu. “Kadiri yanavyozidi kuwa mazito na yenye kuendelea,” aandika Dakt. Daniel Goleman, “ndivyo hatari iwavyo kubwa. . . . Mazoea ya kuchambua na kudharau au kuchukizwa ni ishara za hatari kwa sababu huonyesha kwamba mume au mke kwa ukimya tayari amemhukumu mwenzi kuwa mbaya.” Upendo unapopungua, mume na mke wanakuwa, kama kitabu kimoja kisemavyo, “wameoana kisheria, bali si kihisia-moyo.” Baada ya muda, ndoa yao haitaendelea tena.

      Hata hivyo, usemi wenye kukemea-kemea waweza kuathiri mtu hata kuliko kuathiri ndoa yenyewe. Mithali ya Biblia husema: “Kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.” (Mithali 15:13) Mkazo unaotokana na mashambulio ya daima ya maneno yenye kuumiza waweza kuharibu sana afya ya mtu. Kwa kielelezo, uchunguzi mmoja uliofanywa na Chuo Kikuu cha Washington (Marekani) ulifunua kwamba mwanamke ambaye hutukanwa-tukanwa anaweza kupatwa zaidi na homa, matatizo ya kibofu cha mkojo, maambukizo ya Candidiasis (ambayo huathiri uke), na matatizo ya tumbo.

      Wake wengi ambao wamevumilia kutendwa vibaya kwa maneno na kupigwa kimwili husema kwamba maneno yanaweza kuumiza zaidi kuliko ngumi. “Michubuo itokanayo na makofi itapona na kwisha hatimaye,” asema Beverly, “lakini sitasahau kamwe mambo mabaya aliyosema kuhusu sura yangu, jinsi ninavyopika, jinsi ninavyotunza watoto.” Julia ahisi vivyohivyo. “Najua inasikika kama kichaa,” yeye asema, “lakini afadhali anipige na mambo yaishe kuliko kuendelea kuteswa kiakili.”

      Lakini kwa nini watu wengine huchambua na kukemea-kemea yule ambaye walidai kumpenda? Makala ifuatayo itashughulikia swali hili.

  • Kufunua Visababishi vya Usemi Wenye Kuudhi
    Amkeni!—1996 | Oktoba 22
    • Kufunua Visababishi vya Usemi Wenye Kuudhi

      “Kinywa cha mtu hunena yaujazayo moyo wake.”—MATHAYO 12:34.

      MILEANI mbili hivi zilizopita, Yesu Kristo alitaarifu maneno yaliyo juu. Ndiyo, maneno ya mtu mara nyingi huonyesha hisia zake za ndani na nia zake. Hayo huenda yakawa yenye kustahili sifa. (Mithali 16:23) Kwa upande ule mwingine, huenda yakawa yenye hila.—Mathayo 15:19.

      Mwanamke mmoja alisema hivi kuhusu mwenzi wake: “Yeye huelekea kukasirika ghafula, na kuishi naye mara nyingi ni kama kutembea katika eneo lililo na mabomu ya kutegwa ardhini—hujui kamwe ni nini kitakachochochea mlipuko.” Richard afafanua hali sawa na hiyo kuhusu mke wake. “Lydia sikuzote yuko tayari kwa vita,” yeye asema. “Yeye hazungumzi tu; yeye hushambulia kwa maneno kwa njia ya kivita, akinielekezea kidole kana kwamba mimi ni mtoto.”

      Bila shaka, mabishano yaweza kuzuka hata katika ndoa bora zaidi, na wote waume na wake husema mambo ambayo baadaye hughairi. (Yakobo 3:2) Lakini usemi wenye kuudhi katika ndoa ni zaidi ya hilo; huo hutia ndani usemi wenye kushushia heshima na wenye kuchambua ambao unanuiwa kutawala, au kudhibiti mwenzi. Nyakati fulani, usemi wenye kudhuru hujificha katika mwonekano wenye kudanganya wa upole. Kwa kielelezo, mtunga-zaburi Daudi alimfafanua mtu ambaye alikuwa mpole, lakini ndani ni mwovu: “Kinywa chake ni laini kuliko siagi, bali moyo wake ni vita. Maneno yake ni mororo kuliko mafuta, bali hayo ni panga wazi.” (Zaburi 55:21; Mithali 26:24, 25) Uwe ni wenye kudhuru au uliofichika, usemi mkali waweza kuharibu ndoa.

      Jinsi Unavyoanza

      Ni nini kimfanyacho mtu atumie usemi wenye kuudhi? Kwa ujumla, utumizi wa usemi kama huo waweza kufuatiwa kwenye kile ambacho mtu huona na kusikia. Katika mabara mengi kukejeli, matukano, na maneno ya kuaibisha mtu hukubaliwa na hata kuonwa kuwa yenye ucheshi.a Waume hasa huenda wakaathiriwa na vyombo vya habari, ambavyo huonyesha wanaume “kamili” kuwa wenye kutawala na wakali.

      Vivyo hivyo, wengi ambao hutumia usemi wenye kushusha heshima walilelewa katika nyumba ambamo hasira, chuki, na ugomvi wa mzazi ulitokea kwa ukawaida. Hivyo, tangu umri mchanga, walifahamu kwamba namna hii ya mwenendo ni ya kawaida.

      Mtoto aliyelelewa katika mazingira kama hayo huenda akajifunza zaidi ya tabia hiyo ya usemi; yeye aweza pia kuingiza akilini maoni yaliyopotoka kujihusu na kuhusu wengine. Kwa kielelezo, ikiwa usemi mkali unaelekezewa mtoto, huenda akakua akihisi kuwa bure, hata kuchochewa kuwa mwenye hasira. Lakini namna gani ikiwa mtoto asikia tu kwa mbali baba yake akimshambulia mama yake kwa maneno? Hata kama mtoto huyo ni mchanga sana, yeye aweza kuweka akilini madharau ya baba yake kwa wanawake. Mvulana aweza kujifunza kutokana na mwenendo wa baba yake kwamba mwanamume ahitaji kudhibiti wanawake na kwamba njia ya kuwadhibiti ni kuwatisha au kuwaumiza.

      Mzazi mwenye hasira huenda akamlea mtoto mwenye hasira, ambaye hatimaye atakua na kuwa “bwana mkubwa wa hasira” ambaye hutenda “makosa mengi sana.” (Mithali 29:22, NW, kielezi-chini) Hivyo matokeo ya usemi wenye kuumiza yaweza kupitishwa kutoka kizazi kimoja hadi kifuatacho. Akiwa na sababu nzuri, Paulo aliwashauri akina baba: “Msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike.” (Wakolosai 3:21, NW) Ni jambo la maana kwamba neno la Kigiriki lililotafsiriwa “kuchochea ili kukasirika,” kulingana na Theological Lexicon of the New Testament, laweza kuwa na maana ya “kutayarisha na kuchochea kwa ajili ya pambano.”

      Bila shaka, uvutano wa kimzazi hauvumilii kushambulia wengine, kwa maneno au vingine; lakini husaidia kueleza jinsi mwelekeo wa usemi wenye kudhulumu uwezavyo kuwa wa kina kirefu. Mwanamume kijana huenda asimtendee vibaya mke wake kimwili, lakini je, yeye humtendea vibaya kwa maneno yake na hisia zake za moyo zenye kubadilika-badilika? Kujichunguza huenda kukamfunulia mtu kwamba ameingiwa akilini na dharau la baba yake kwa wanawake.

      Kwa wazi, kanuni zilizo juu zaweza pia kutumika kwa wanawake. Ikiwa mama anamtendea vibaya mume wake kwa maneno, huenda binti akamtendea mume wake kwa njia hiyo hiyo anapoolewa. Mithali ya Biblia yasema: “Ni bora kuwa ukiishi katika bara lililo ukiwa, kuliko na mwanamke mwenye ulimi-mchungu na mwenye hasira.” (Mithali 21:19, The Bible in Basic English) Hata hivyo, mwanamume apaswa kutahadhari hasa kuhusu jambo hili. Kwa nini?

      Uwezo wa Wakandamizaji

      Kwa kawaida mume huwa na uwezo zaidi katika ndoa kuliko mke. Sikuzote yaelekea yeye ni mwenye nguvu zaidi kimwili, ikifanya vitisho vya madhara ya kimwili viwe vyenye kuhofisha hata zaidi.b Kwa kuongezea, mara nyingi mwanamume ana stadi nzuri zaidi za kazi, stadi nyingi zaidi za kujiruzuku bila kutegemea wengine, na faida kubwa zaidi za kifedha. Kwa sababu ya hili, yaelekea mwanamke mwenye kushambuliwa kwa maneno atahisi amenaswa katika mtego na akiwa mpweke. Huenda akakubaliana na taarifa ya Mfalme Sulemani mwenye hekima: “Nikarudi na kuona madhalimu yote yanayotendeka chini ya jua; na tazama, machozi yao waliodhulumiwa, ambao walikuwa hawana mfariji; na upande wa wale waliowadhulumu kulikuwa na uwezo, walakini wale walikuwa hawana mfariji.”—Mhubiri 4:1.

      Huenda mke akavurugika ikiwa mume wake hubadilika-badilika sana—mwenye fadhili dakika moja, mwenye kuchambua dakika ifuatayo. (Linganisha Yakobo 3:10.) Na zaidi, ikiwa mume wake anaandaa vizuri kimwili, mke ambaye ni shabaha ya usemi mkali huenda akahisi kuwa mwenye hatia kwa kufikiri kwamba kuna jambo baya katika ndoa. Huenda hata akajilaumu kwa mwenendo wa mume wake. “Kama tu mke mwenye kupigwa kimwili,” aungama mwanamke mmoja, “mimi sikuzote nilikuwa nikijifikiria kuwa kisababishi.” Mke mwingine asema: “Nilifanywa niamini kwamba ikiwa ningejaribu zaidi tu kumfahamu na ‘kuwa mwenye subira’ naye ningepata amani.” Kwa kuhuzunisha, mara nyingi kutendwa vibaya huendelea.

      Kwa kweli ni jambo lenye kuhuzunisha kwamba waume wengi hutumia vibaya uwezo wao kwa kumtawala mwanamke ambaye huenda walitoa nadhiri kumpenda na kumtunza. (Mwanzo 3:16) Lakini ni nini kiwezacho kufanywa kuhusu hali kama hiyo? “Sitaki kuondoka,” asema mke mmoja, “Nataka tu aache kunitenda vibaya.” Baada ya miaka tisa ya ndoa, mume mmoja akiri hivi: “Natambua kwamba niko katika uhusiano wenye maneno yenye kuudhi na kwamba mimi ndiye mwenye kuudhi. Bila shaka nataka kubadilika, si kuondoka.”

      Kuna msaada kwa wale ambao ndoa zao zimepatwa na usemi wenye kuumiza, kama makala ifuatayo itakavyoonyesha.

      [Foonotes]

      a Kwa wazi, ndivyo ilivyokuwa katika karne ya kwanza. The New International Dictionary of New Testament Theology hutaja kwamba “kwa Wagiriki ulikuwa mmojapo usanii wa maisha kujua jinsi ya kutukana wengine au kustahimili matukano.”

      b Ukatili wa maneno waweza kuwa jiwe la kukanyagia kuelekea jeuri ya nyumbani. (Linganisha Kutoka 21:18.) Asema mshauri mmoja wa wanawake wenye kupigwa: “Kila mwanamke anayekuja ili kupata amri ya kisheria ya ulinzi dhidi ya kupigwa, kudungwa kisu, au kusongwa pumzi ambako kwahatarisha uhai wake amekuwa, kwa kuongezea, na historia ndefu yenye maumivu ya kuudhiwa kusiko kwa kimwili.”

  • Kutoka Maneno Yaumizayo Hadi Maneno Yaponyayo
    Amkeni!—1996 | Oktoba 22
    • Kutoka Maneno Yaumizayo Hadi Maneno Yaponyayo

      “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.”—MITHALI 18:21.

      UTUKANAJI—zoea la kimakusudi la kutumia usemi wenye kutusi na kuudhi—hushutumiwa waziwazi katika Biblia. Chini ya Sheria ya Kimusa, mtu ambaye angewatukana wazazi wake angepata adhabu ya kifo. (Kutoka 21:17) Hivyo, Yehova Mungu hachukui jambo hilo kwa wepesi. Neno lake, Biblia, haliungi mkono wazo la kwamba chochote kitendekacho ‘katika usiri wa nyumba ya mtu’ hakina maana mradi mtu adai kumtumikia Mungu. Biblia hutaarifu hivi: “Mtu akidhani ya kuwa anayo dini, wala hauzuii ulimi wake kwa hatamu, hali akijidanganya moyo wake, dini yake mtu huyo haifai.” (Yakobo 1:26; Zaburi 15:1, 3) Kwa hiyo ikiwa mwanamume amuudhi mke wake kwa maneno, kazi zake nyinginezo zote za Kikristo zaweza kuonwa kuwa bure machoni pa Mungu.a—1 Wakorintho 13:1-3.

      Isitoshe, Mkristo ambaye ni mtukanaji aweza kuondoshwa kutanikoni. Aweza hata kupoteza baraka za Ufalme wa Mungu. (1 Wakorintho 5:11; 6:9, 10) Kwa wazi, mtu ambaye ni mwenye kuumiza kwa maneno yake ahitaji kufanya badiliko kubwa. Lakini hilo laweza kutimizwaje?

      Kulifunua Hilo Tatizo

      Kwa wazi, mkosaji hatabadilika isipokuwa afahamu waziwazi kwamba ana tatizo zito. Kwa kuhuzunisha, kama mshauri mmoja alivyoonelea, wanaume wengi ambao hutumia usemi wenye kuudhi “hawaoni mwenendo wao kuwa wenye kuudhi hata kidogo. Kwa wanaume hawa, vitendo kama hivyo ni vya kawaida kabisa navyo ni njia ‘asilia’ ambayo waume na wake huchangamana.” Hivyo, wengi hawataona uhitaji wa kubadilika hadi waonyeshwe hali hiyo moja kwa moja.

      Mara nyingi, baada ya kuchanganua hali yake kwa mwelekeo wa sala, mke atasukumwa kusema kwa ujasiri—kwa ajili ya hali-bora yake mwenyewe na ile ya watoto wake na kwa sababu ya kuhangaikia msimamo wa mume wake pamoja na Mungu. Ni kweli, sikuzote kuna uwezekano kwamba kusema kwa ujasiri kwaweza kufanya mambo yawe mabaya zaidi na kwamba maneno yake huenda yakakabili mlipuko wa kujitetea. Labda mke aweza kuiweza hali hiyo kwa kufikiri kwa uangalifu kimbele jinsi atakavyotokeza habari hiyo. “Neno linenwalo wakati wa kufaa. Ni kama machungwa katika vyano vya fedha,” yasema Biblia. (Mithali 25:11) Mfikio wenye fadhili lakini wa waziwazi katika wakati mtulivu huenda ukaufikia moyo wake.—Mithali 15:1.

      Badala ya kutokeza mashtaka, mke apaswa kujaribu kujieleza kulingana na jinsi usemi wenye kuumiza unavyomwathiri. Taarifa za “Mimi” mara nyingi hufanya kazi vyema. Kwa kielelezo, ‘Mimi nahisi kuumizwa kwa sababu . . .’ au ‘Mimi nahisi kupondeka unaponiambia . . .’ Taarifa kama hizo zitaelekea zaidi kuufikia moyo, kwa kuwa hushambulia tatizo badala ya mtu.—Linganisha Mwanzo 27:46–28:1.

      Mwingilio wa mke ulio imara lakini wenye busara waweza kuwa na matokeo mazuri. (Linganisha Zaburi 141:5.) Mwanamume tutakayemwita Steven aliona ndivyo ilivyo. “Mke wangu alitambua mtazamo wa kuudhi ndani yangu ambao sikuutambua, naye alikuwa na ujasiri wa kunieleza kuuhusu,” yeye asema.

      Kupata Msaada

      Lakini mke aweza kufanya nini ikiwa mume wake akataa kukubali tatizo hilo? Kufikia hatua hii wake fulani hutafuta msaada wa nje. Katika nyakati za taabu hizo, Mashahidi wa Yehova waweza kuwaendea wazee wao wa kutaniko. Biblia huwahimiza wanaume hawa wawe wenye kuonyesha upendo na fadhili wakati wanapochunga kundi la kiroho la Mungu na, kwa wakati huohuo, ‘kuwaonya watu wenye kupinga’ mafundisho yenye mafaa ya Neno la Mungu. (Tito 1:9; 1 Petro 5:1-3) Ingawa hawapaswi kuingilia mambo ya kibinafsi ya waume na wake, wazee wana haki ya kuhangaika wakati mwenzi mmoja anateswa kwa usemi mkali wa yule mwingine. (Mithali 21:13) Wakitii kwa ukaribu viwango vya Biblia, wanaume hawa hawaachilii au kupunguza uzito wa usemi wenye kuudhi.b

      Huenda wazee wakaweza kurahisisha mawasiliano kati ya mume na mke. Kwa kielelezo, mzee mmoja alifikiwa na mwanamke aliyemweleza juu ya miaka mingi ya kupigwa kwa maneno na mume wake, mwabudu mwenzake. Mzee huyo alipanga kukutana nao wawili. Kila mmoja alipokuwa akisema, yeye alimwomba yule mwingine asikilize bila kukatiza. Ilipokuwa zamu ya mke, yeye alisema kwamba hangeweza tena kustahimili hasira yenye kulipuka ya mume wake. Kwa miaka mingi, yeye akaeleza, alikuwa na hofu sana mwishoni mwa kila siku, akiwa hajui kamwe ikiwa mume wake angekuwa amekasirika alipokuja nyumbani. Alipolipuka, alikuwa akisema mambo yenye kushushia heshima familia ya mke, marafiki wake, na mke mwenyewe.

      Mzee huyo alimuuliza mke huyo aeleze jinsi maneno ya mume wake yalivyomfanya ahisi. “Nilihisi kama kwamba nilikuwa mtu mbaya ambaye hakuna mtu angeweza kumpenda,” yeye akajibu. “Nyakati nyingine nilikuwa nikimuuliza mama yangu, ‘Mama, je, mimi ni mtu mgumu sana kuishi naye? Je, mimi ni mtu asiyeweza kupendeka?’” Alipokuwa akifafanua jinsi maneno ya mume wake yalivyomfanya ahisi, mume wake alianza kulia. Kwa mara ya kwanza, aliweza kuona jinsi alivyokuwa akimuumiza sana mke wake kwa maneno yake.

      Wewe Waweza Kubadilika

      Wakristo fulani katika karne ya pili walikuwa na tatizo na usemi wenye kuudhi. Mtume Mkristo Paulo aliwaonya waweke mbali “hasira, na ghadhabu, na uovu, na matukano, na matusi.” (Wakolosai 3:8) Hata hivyo, usemi mkali ni tatizo la moyo hasa kuliko la ulimi. (Luka 6:45) Hiyo ndiyo sababu Paulo aliongeza: ‘Uvueni kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake, na mvae utu mpya.’ (Wakolosai 3:9, 10) Kwa hiyo badiliko huhusisha si tu kuzungumza kwa njia tofauti bali pia kuhisi tofauti.

      Mume atumiaye usemi wenye kuumiza huenda akahitaji msaada ili kupambanua ni nini hasa kichocheacho mwenendo wake.c Yeye atataka kuwa na mtazamo wa mtunga-zaburi: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu. Uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu.” (Zaburi 139:23, 24) Kwa kielelezo: Kwa nini yeye ahisi uhitaji wa kumtawala, au kumdhibiti, mwenzi wake? Ni nini kianzishacho udhia wa maneno? Je, mashambulizi yake ni dalili za chuki yenye kina? (Mithali 15:18) Je, ana hisia za kwamba yeye hafai kitu, labda zikitokana na kulelewa kwake ambako kulikuwa na usemi wa kuchambuliwa? Maswali kama hayo yaweza kumsaidia mwanamume agundue chanzo cha mwenendo wake.

      Ingawa hivyo, usemi wenye kuudhi ni mgumu kung’oa, hasa ikiwa umekazwa kikiki na wazazi ambao wenyewe walikuwa wenye kukejeli kwa maneno au kwa utamaduni ambao huchochea mwenendo wa kutawala. Lakini chochote ajifunzacho mtu—kwa wakati na jitihada—chaweza kutanguliwa. Biblia ndio msaada mkubwa zaidi kuhusu jambo hili. Yaweza kumsaidia mtu kutangua hata mwenendo uliotia mzizi sana. (Linganisha 2 Wakorintho 10:4, 5.) Jinsi gani?

      Maoni Yafaayo Kuhusu Mafungu ya Kupewa na Mungu

      Mara nyingi, wanaume ambao ni wenye kuumiza kwa maneno wana maoni yaliyopotoka kuhusu mafungu ya kupewa na Mungu kwa waume na wake. Kwa kielelezo, mwandikaji wa Biblia Paulo ataarifu kwamba wake wapaswa ‘kutii waume zao’ na kwamba “mume ni kichwa cha mkewe.” (Waefeso 5:22, 23) Huenda mume akahisi kwamba ukichwa humpatia mamlaka ya kuwa na udhibiti kamili. Lakini sivyo ilivyo. Mke wake, ingawa yuko chini ya ujitiisho, si mtumwa wake. Yeye ni ‘msaidiaji’ na ‘kikamilisho.’ (Mwanzo 2:18, NW) Hivyo, Paulo aongeza: “Imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea kanisa.”—Waefeso 5:28, 29.

      Akiwa kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu hakuwakemea-kemea wanafunzi wake, akiwafanya wawe na wasiwasi ni wakati gani tena mlipuko ufuatao wa uchambuzi utakapotokea. Badala ya hivyo, yeye alikuwa mwororo, hivyo akidumisha hadhi yao. “Nitawapumzisha,” akawaahidi. “Mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo.” (Mathayo 11:28, 29) Kutafakari kwa mwelekeo wa sala juu ya jinsi Yesu alidhihirisha ukichwa wake kwaweza kumsaidia mume aone ukichwa wake kwa maoni yaliyosawazika zaidi.

      Mikazo Inapozuka

      Ni rahisi kujua kanuni za Biblia; kuzitumia ukiwa chini ya mkazo ndilo jambo gumu zaidi. Mikazo inapozuka, mume anaweza kuepukaje kurudia kitabia cha usemi wenye kudhulumu?

      Si ishara ya uanamume kwa mume kuwa mkali kwa maneno anapokasirika. Biblia hutaarifu: “Asiye mwepesi wa hasira ni mwema kuliko shujaa; na mtu aitawalaye roho yake kuliko mtu atekaye mji.” (Mithali 16:32) Mwanamume halisi hudhibiti roho yake. Yeye huonyesha hisia-mwenzi kwa kufikiria: ‘Maneno yangu yanamwathirije mke wangu? Mimi ningehisije kama ningekuwa mahali pake?’—Linganisha Mathayo 7:12.

      Ingawa hivyo, Biblia hukubali kwamba hali fulani zaweza kuchochea hasira. Kuhusu hali kama hizo mtunga-zaburi aliandika hivi: “Kasirikani, lakini msitende dhambi: Semezanani kila mtu na moyo wakwe, vile alivyo mwakwe kitandani, mnganyamaa kimya.” (Zaburi 4:4, The Old Testament In Swahili [Mombasa]) Pia imesemwa hivi: “Hakuna kosa lolote kukasirika, lakini ni kosa kushambulia kwa maneno kwa kuwa mwenye kukejeli, mwenye kuaibisha au mwenye kushusha heshima.”

      Ikiwa mume ahisi kwamba anapoteza udhibiti wa usemi wake, yeye aweza kujifunza kujiondokea. Labda lingekuwa jambo la hekima kuondoka chumbani, kwenda kutembea, au kutafuta mahali pa faragha ili apoe. Mithali 17:14 (NW) yasema: “Kabla magombano hayajalipuka, jiondokee.” Rudieni mazungumzo baada ya hasira kupoa.

      Bila shaka, hakuna aliye mkamilifu. Mume ambaye amekuwa na tatizo la usemi mkali aweza kuangukia tena hali hiyo. Hili linapotukia, apaswa kuomba radhi. Kuvaa “utu mpya” ni utaratibu wenye kuendelea, lakini ule ambao huvuna thawabu kubwa.—Wakolosai 3:10.

      Maneno Yaponyayo

      Ndiyo, “Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.” (Mithali 18:21) Usemi wenye kuumiza lazima ubadilishwe na maneno yajengayo na yenye kuimarisha ndoa. Methali ya Biblia hutaarifu: “Maneno yapendezayo ni kama sega la asali; ni tamu nafsini, na afya mifupani.”—Mithali 16:24.

      Miaka fulani iliyopita, uchunguzi ulifanywa ili kujua ni mambo gani yaliyosababisha familia zenye nguvu kufanya kazi kwa matokeo. “Uchunguzi huo ulipata kwamba washiriki wa familia walipendana, na waliendelea kuambiana kwamba wanapendana,” aripoti mtaalamu wa ndoa David R. Mace. “Kila mmoja alihakikishiwa kwamba anakubaliwa, wakaonyeshana kwamba kila mmoja astahili, na kuchukua kila fursa ifaayo kuzungumza na kutenda kwa upendo. Tokeo, kiasili, lilikuwa kwamba walifurahi kuwa pamoja na kuimarishana kwa njia ambazo zilifanya mahusiano yao yaridhishe.”

      Hakuna mume mwenye kumhofu Mungu awezaye kusema kwa kweli kwamba ampenda mke wake ikiwa amuumiza kimakusudi kwa maneno yake. (Wakolosai 3:19) Bila shaka, ndivyo ilivyo kwa mke ambaye humpiga mume wake kwa maneno. Kwa kweli, ni wajibu wa wenzi wote kufuata onyo la Paulo kwa Waefeso: “Neno lo lote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji, ili liwape neema wanaosikia.”—Waefeso 4:29.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ingawa twamrejezea mkosaji kuwa mwanamume, kanuni zilizopo hapa zatumika sawasawa kwa wanawake.

      b Ili kustahili kutumikia au kuendelea kutumikia akiwa mzee, mwanamume hapaswi kuwa mpiganaji. Hawezi kuwa yule ambaye apiga watu kimwili au kuwadhulumu kwa maneno yenye kuumiza. Wazee na watumishi wa huduma wanapaswa kusimamia nyumba zao kwa njia nzuri. Haidhuru hata atende kwa fadhili namna gani katika hali nyinginezo, mwanamume hastahili ikiwa yeye ni mtawala mkatili nyumbani.—1 Timotheo 3:2-4, 12.

      c Iwe Mkristo atatafuta tiba ya mwenendo wenye kuudhi au la ni uamuzi wa kibinafsi. Hata hivyo, apaswa kuhakikisha kwamba tiba yoyote apokeayo haipingani na kanuni za Biblia.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki