Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Haiwezi Kuwa Kweli!”
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • “Haiwezi Kuwa Kweli!”

      MTU fulani kutoka New York (Marekani) asimulia hivi: “Mwanangu Jonathan alikuwa akiwatembelea marafiki umbali wa kilometa chache. Mke wangu, Valentina, hakupenda aende huko. Sikuzote alikuwa akiogopa mwendo wa magari. Lakini mwana wetu alipenda sana shughuli za kielektroniki, na marafiki zake walikuwa na duka la ufundi alimoweza kupata ustadi wenye kutumika. Nilikuwa nyumbani katika Manhattan magharibi, New York. Mke wangu alikuwa akitembelea familia yake katika Puerto Riko. ‘Jonathan atarudi karibuni,’ nikafikiri. Kisha kengele ya mlango ikalia. ‘Bila shaka ndiye huyo.’ Hakuwa huyo. Hao walikuwa polisi na wafanya-kazi wa tiba. ‘Je! watambua leseni (cheti) hii ya udereva?’ ofisa wa polisi akauliza. ‘Ndiyo, hiyo ni ya mwanangu, Jonathan.’ ‘Tumekuletea habari mbaya. Kumekuwa na aksidenti, na . . . mwana wako, . . . mwana wako ameuawa.’ Itikio langu la kwanza lilikuwa, ‘Haiwezi kuwa kweli!’ Tukio hilo la kushtua lilisababisha umivu mioyoni mwetu ambalo bado linapona, hata miaka kadhaa baadaye.”

      Baba fulani katika Barcelona (Hispania) aandika hivi: “Huko nyuma katika Hispania miaka ya 1960, sisi tulikuwa familia yenye furaha. Kulikuwa na María, mke wangu, na watoto wetu watatu, David wa miaka 13, Paquito wa miaka 11, na Isabel wa miaka 9.

      “Siku moja katika Machi 1963, Paquito alirudi nyumbani kutoka shuleni akilalamika juu ya maumivu makali ya kichwani. Tulitatanika kuhusu ni nini kingeweza kuwa chanzo chayo—lakini si kwa muda mrefu. Muda wa saa tatu baadaye yeye alikuwa amekufa. Kuvuja kwa damu ubongoni kulikuwa kumekomesha uhai wake kwa ghafula.

      “Kifo cha Paquito kilitukia zaidi ya miaka 30 iliyopita. Hata hivyo, umivu lenye kina kirefu kutokana na kifo hicho labaki nasi hadi siku hii. Hakuna njia yoyote ambayo wazazi waweza kufiwa na mtoto na wasihisi kwamba wamepoteza sehemu fulani ya wao wenyewe—haidhuru ni muda gani wa wakati upitao au ni watoto wengine wangapi huenda wakapata.”

      Maono haya mawili, ambayo katika hayo wazazi walifiwa na watoto, yaonyesha jinsi umivu lisababishwalo wakati mtoto anapokufa lilivyo lenye kina na lenye kudumu. Ni ya kweli kama nini yale maneno ya daktari fulani aliyeandika hivi: “Kwa kawaida kifo cha mtoto ni msiba nacho ni umivu kali la kimoyoni zaidi ya kifo cha mtu mwenye umri mkubwa zaidi kwa sababu mtoto ni mshiriki wa familia asiyetazamiwa kufa. . . . Kifo cha mtoto yeyote huwakilisha kupotezwa kwa ndoto za wakati ujao, watu wa ukoo [mwana, binti-mkwe, wajukuu], maono . . . ambayo bado hayajafurahiwa.” Na hisi hii ya kupoteza mengi sana yaweza kumhusu pia mwanamke yeyote aliyempoteza mtoto mchanga kupitia mimba iliyoharibika.

      Mke fulani aliyefiwa aeleza hivi: “Mume wangu, Russell, alikuwa ametumikia akiwa msaidizi wa kitiba katika eneo la mapigano la Pasifiki wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Alikuwa ameona na kuokoka mapigano fulani yaliyo mabaya sana. Yeye alirudi Marekani kwenye maisha matulivu zaidi. Baadaye alitumikia akiwa mhudumu wa Neno la Mungu. Mwanzoni-mwanzoni mwa miaka yake ya 60 alianza kuwa na dalili za matatizo ya moyo. Alijaribu kuwa na maisha yenye utendaji mwingi. Halafu, siku moja katika Julai 1988, alipatwa kwa ghafula na ugonjwa mbaya sana wa moyo, akafa. Kifo chake kilihuzunisha sana. Sikupata kamwe hata nafasi ya kuagana. Yeye hakuwa mume wangu tu. Alikuwa rafiki yangu aliye bora zaidi ya wote. Tulikuwa tumeshiriki miaka 40 ya maisha pamoja. Sasa ilionekana kwamba ilinilazimu kukabili upweke usio wa kawaida.”

      Haya ni machache tu kati ya yale maelfu ya misiba ambayo huathiri vibaya familia nyingi kotekote ulimwenguni kila siku. Kama vile watu wengi wanaohuzunika watakavyokuambia, kifo kimchukuapo mtoto wako, mume wako, mke wako, mzazi wako, rafiki yako, kwa kweli huwa kile ambacho mwandikaji Mkristo Paulo alikiita, “adui wa mwisho.” Mara nyingi itikio la kwanza la asili kwa habari hiyo yenye kuhofisha laweza kuwa kukana, “Haiwezi kuwa kweli! Siamini hilo.” Mara nyingi maitikio mengine hufuata, kama tutakavyoona.—1 Wakorintho 15:25, 26, New World Translation.

      Hata hivyo, kabla ya sisi kuchunguza hisia za huzuni, acheni tujibu baadhi ya maswali ya maana. Je! kifo humaanisha mwisho wa mtu huyo? Je! kuna tumaini lolote kwamba twaweza kuwaona wapendwa wetu tena?

      Kuna Tumaini Halisi

      Mwandikaji wa Biblia Paulo alitoa tumaini la kitulizo kutoka kwa yule “adui wa mwisho,” kifo. Aliandika hivi: “Kifo kitafanywa kuwa si kitu.” “Adui wa mwisho kufutiliwa mbali ni kifo.” (1 Wakorintho 15:26, The New English Bible) Kwa nini Paulo angeweza kuwa na uhakika hivyo juu ya jambo hilo? Kwa sababu alikuwa amefundishwa na Yesu Kristo, mmoja aliyekuwa ameinuliwa kutoka kwa wafu. (Matendo 9:3-19) Hiyo ndiyo sababu pia Paulo angeweza kuandika hivi: “Kwa kuwa kifo ni kupitia mtu [Adamu], ufufuo wa wafu pia ni kupitia mtu [Yesu Kristo]. Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, ndivyo pia katika yule Kristo wote watafanywa kuwa hai.”—1 Wakorintho 15:21,22, NW.

      Yesu alihuzunika sana alipokutana na mjane fulani wa Naini na kumwona mwana wake mfu. Simulizi la Biblia latuambia hivi: “[Yesu] alipokaribia lango la jiji [Naini], kumbe! tazama! kulikuwa na mtu mfu akiwa anapelekwa nje, mwana mzaliwa-pekee wa mama yake. Mbali na hilo, alikuwa ni mjane. Pia umati mkubwa kutoka kwenye jiji ulikuwa pamoja naye. Na Bwana alipomwona akamsikitikia, naye akamwambia: ‘Koma kutoa machozi.’ Ndipo akakaribia na kuligusa jeneza, na wachukuzi wakasimama tuli, naye akasema: ‘Mwanamume kijana, nakuambia, Inuka!’ Na huyo mtu mfu akaketi na kuanza kusema, naye akampa huyo kwa mama yake. Basi hofu ikawashika wote, nao wakaanza kumtukuza Mungu, wakisema: ‘Nabii mkubwa ameinuliwa miongoni mwetu,’ na, ‘Mungu ameelekeza uangalifu wake kwa watu wake.’” Ona jinsi Yesu alivyosikitika sana, hivi kwamba akamfufua mwana wa mjane huyo! Ebu wazia ni nini ambacho tukio hilo laonyesha kuhusu wakati ujao!—Luka 7:12-16, NW.

      Hapo, akiwa mbele ya mashahidi wenye kujionea kwa macho yao wenyewe, Yesu alifanya ufufuo usiosahaulika. Ilikuwa dalili ya ule ufufuo aliokuwa tayari ametabiri juu yao wakati fulani kabla ya tukio hili, kurudishwa kwa uhai duniani chini ya “mbingu mpya.” Kwenye pindi hiyo Yesu alikuwa amesema hivi: “Msistaajabie hili, kwa sababu saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti yake na kutoka.”—Ufunuo 21:1, 3, 4; Yohana 5:28, 29; 2 Petro 3:13, NW.

      Mashahidi wengine wenye kujionea ufufuo kwa macho yao wenyewe ni kutia ndani Petro, pamoja na wengine wa wale 12 walioandamana na Yesu kwenye safari zake. Kwa kweli wao walimsikia Yesu aliyefufuka akisema akiwa kando ya Bahari ya Galilaya. Simulizi hilo latuambia hivi: “Yesu akawaambia: ‘Njoni, twaeni kifungua-kinywa chenu.’ Hakuna hata mmoja kati ya wanafunzi aliyekuwa na moyo wa kuulizia habari kwake: ‘Wewe ni nani?’ kwa sababu walijua alikuwa Bwana. Yesu akaja na kuchukua ule mkate na kuwapa, na samaki hivyohivyo. Sasa hiyo ilikuwa ni mara ya tatu ambayo Yesu alionekana kwa wanafunzi baada ya kuinuliwa kwake kutoka kwa wafu.”—Yohana 21:12-14, NW.

      Kwa hiyo, Petro angeweza kuandika hivi akiwa na usadikisho kamili: “Mbarikiwa awe yule Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alitupa sisi uzaliwa mpya kwenye tumaini lililo hai kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu.”—1 Petro 1:3, NW.

      Mtume Paulo alionyesha tumaini lake hakika aliposema hivi: “Naamini mambo yote yaliyoelezwa katika ile Sheria na kuandikwa katika Manabii; nami nina tumaini kuelekea Mungu, tumaini ambalo watu hawa wenyewe hulishikilia, kwamba kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:14, 15, NW.

      Kwa hiyo mamilioni ya watu waweza kuwa na tumaini thabiti la kuona wapendwa wao wakiwa hai tena hapa duniani lakini chini ya hali zilizo tofauti sana. Hali hizo zitakuwa nini? Habari zaidi juu ya lile tumaini lenye msingi wa Biblia kwa wapendwa wetu waliokufa itazungumziwa katika sehemu ya mwisho ya broshua hii, yenye kichwa “Tumaini Hakika kwa Wafu.”

      Lakini acheni kwanza tufikirie maswali ambayo huenda unayo ikiwa unahuzunika kwa sababu ya kifo cha mpendwa: Je! ni kawaida kuhuzunika hivi? Naweza kuishije nikiwa na huzuni yangu? Wengine waweza kufanya nini kunisaidia nishughulike na hali hii? Naweza kuwasaidiaje wengine walio na huzuni? Na hasa, Biblia husema nini juu ya tumaini hakika kwa wafu? Je! nitapata kuwaona wapendwa wangu tena? Na nitawaona wapi?

  • Je! Ni Kawaida Kuhisi Hivi?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • Je! Ni Kawaida Kuhisi Hivi?

      MTU fulani aliyefiwa aandika hivi: “Nilipokuwa mtoto katika Uingereza, nilifunzwa nisionyeshe hisia zangu hadharani. Naweza kukumbuka babangu, aliyekuwa mwanajeshi hapo awali, akiniambia hivi akiwa ameyakaza sana meno yake kwa ukali, ‘Usilie!’ wakati jambo fulani lilipokuwa limeniumiza. Siwezi kukumbuka kama mamangu alipata wakati wowote kubusu au kukumbatia yeyote kati ya sisi watoto (tulikuwa wanne). Nilikuwa na miaka 56 nilipomwona babangu akifa. Nilihisi nimepatwa na hasara kubwa mno. Hata hivyo, mwanzoni, sikuweza kutoa machozi.”

      Katika tamaduni fulani-fulani, watu huonyesha hisia zao waziwazi. Iwe wana furaha au huzuni, wengine wanajua jinsi wanavyohisi. Kwa upande mwingine, katika sehemu nyinginezo za ulimwengu, hasa katika kaskazini mwa Ulaya na Uingereza, watu, hasa wanaume, wamezoezwa kuficha hisia zao, kuzuia hisiamoyo zao, kubaki watulivu bila kuonyesha hisia zao waziwazi. Lakini wakati umefiwa na mpendwa, je, ni vibaya kwa njia fulani kuonyesha huzuni yako? Biblia husema nini?

      Wale Katika Biblia Waliotoa Machozi

      Biblia iliandikwa na Waebrania wa mkoa wa mashariki mwa Mediterania, waliokuwa watu walioonyesha hisia zao waziwazi. Hutoa vielelezo vingi vya watu mmoja-mmoja walioonyesha huzuni yao waziwazi. Mfalme Daudi aliomboleza kifo cha mwana wake Amnoni aliyeuawa kimakusudi. Kwa kweli, alitoa machozi kwa “kilio kikubwa mno.” (2 Samweli 13:28-39) Yeye hata alihuzunika alipofiwa na mwana wake mwenye hila Absalomu, aliyekuwa amejaribu kutwaa utawala kwa nguvu. Simulizi la Biblia latuambia hivi: “Naye mfalme [Daudi] akataabika sana, akapanda juu, akaingia kile chumba kilichokuwa juu ya lango, akalia; na katika kwenda kwake alisema hivi, Mwanangu Absalomu! Ee mwanangu! mwanangu Absalomu! laiti ningalikufa badala yako, Absalomu, mwanangu, mwanangu!” (2 Samweli 18:33) Daudi aliomboleza sawa na baba yeyote wa kawaida. Na ni mara nyingi jinsi gani wazazi wametamani wangalikufa badala ya watoto wao! Laonekana kutokuwa jambo la asili hata kidogo kwa mtoto kufa kabla ya mzazi.

      Yesu aliitikiaje kifo cha rafiki yake Lazaro? Yeye alitoa machozi alipokaribia kaburi lake. (Yohana 11:30-38) Baadaye, Maria Magdalene alitoa machozi alipokaribia kaburi la Yesu. (Yohana 20:11-16) Ni kweli, Mkristo mwenye uelewevu wa tumaini la ufufuo la Biblia hahuzuniki bila kufarijika, kama vile wengine hufanya ambao imani zao kuhusu hali ya wafu hazina msingi wa Biblia ulio dhahiri. Lakini akiwa binadamu mwenye hisia za kawaida, Mkristo wa kweli, hata aliye na tumaini la ufufuo, huhuzunikia na kuombolezea kifo cha mpendwa yeyote.—1 Wathesalonike 4:13, 14.

      Kutoa Machozi au Kutotoa Machozi

      Namna gani maitikio yetu leo? Je! wewe waona kwamba kuonyesha hisia zako ni jambo gumu au linaloaibisha? Washauri hupendekeza nini? Mara nyingi maoni yao ya kisasa hurudia tu ile hekima ya kale ya Biblia iliyopuliziwa. Wao husema kwamba twapaswa kuonyesha huzuni yetu, si kuizuia. Hili latukumbusha wanaume waaminifu wa kale, kama vile Ayubu, Daudi, na Yeremia, ambao maneno yao ya huzuni yanapatikana katika Biblia. Kwa hakika hawakuzizuia hisia zao. Kwa hiyo, si jambo la hekima kujitenga na watu. (Mithali 18:1) Bila shaka, kuomboleza kunaonyeshwa kwa njia tofauti-tofauti katika tamaduni tofauti-tofauti, pia kunategemea imani za kidini zilizoenea.a

      Namna gani ikiwa wahisi kutaka kutoa machozi? Kutoa machozi ni sehemu ya asili ya binadamu. Kumbuka tena ile pindi ya kifo cha Lazaro, wakati Yesu ‘alipopiga kite katika roho na kutokwa na machozi.’ (Yohana 11:33, 35, NW) Hivyo akaonyesha kwamba kutoa machozi ni itikio la kawaida kwa kifo cha mpendwa.

      Hili laungwa mkono na kisa cha mama fulani, Anne, aliyekuwa amefiwa na mtoto wake mchanga Rachel kutokana na SIDS (Ugonjwa wa Kifo cha Ghafula cha Kitoto). Mume wake alieleza hivi: “Jambo la kushangaza ni kwamba wala Anne wala mimi hatukulia kwenye maziko. Wengine wote walikuwa wakitoa machozi.” Anne aliitikia hilo hivi: “Ndiyo, lakini nimelia vya kutosha sana kwa ajili ya sote wawili. Nafikiri niliathiriwa kwelikweli majuma machache baada ya msiba huo, siku moja nilipokuwa peke yangu nyumbani hatimaye. Nililia siku nzima. Lakini naamini hilo lilinisaidia. Nilisikia nafuu kwa kufanya hivyo. Nililazimika kuomboleza kifo cha mtoto wangu mchanga. Naamimi kwelikweli kwamba wapaswa kuacha watu wanaohuzunika watoe machozi. Ingawa ni itikio la asili kwa wengine kusema, ‘Usilie,’ kwa kweli hilo halisaidii.”

      Jinsi Wengine Huitikia

      Wengine wameitikiaje wanapohuzunishwa na kifo cha mpendwa? Kwa kielelezo, fikiria Juanita. Yeye ajua zinavyokuwa hisia wakati wa kufiwa na mtoto mchanga. Yeye alikuwa ameharibikiwa mimba mara tano. Sasa akawa mjamzito tena. Basi wakati aksidenti ya gari ilipomlazimisha alazwe hospitalini, ni wazi yeye alikuwa na wasiwasi. Majuma mawili baadaye alipatwa na utungu wa kuzaa—kabla ya wakati wake. Muda mfupi baadaye Vanessa mdogo akazaliwa—mwenye uzani zaidi kidogo ya gramu mia tisa. “Nilisisimuka sana,” Juanita akumbuka. “Hatimaye nikawa mama!”

      Lakini furaha yake ilikuwa ya muda mfupi tu. Siku nne baadaye Vanessa alikufa. Juanita akumbuka hivi: “Nilihisi utupu sana. Nilitwaliwa hali yangu ya kuwa mama. Nilihisi kutokuwa kamili. Iliumiza sana kuja nyumbani kwenye chumba tulichokuwa tumemtayarishia Vanessa na kuona zile shati ndogo za kuvaliwa ndani nilizokuwa nimemnunulia. Kwa miezi kadhaa iliyofuata, nilikumbuka upya ile siku ya kuzaliwa kwake. Sikutaka kushirikiana na yeyote yule.”

      Je! hilo ni itikio la kupita kiasi? Huenda ikawa vigumu kwa wengine kuelewa, lakini wale ambao, kama vile Juanita, wamepitia hali hiyo wanaeleza kwamba walihuzunikia mtoto wao mchanga sawa na vile ambavyo wangehuzunikia mtu fulani aliyekuwa ameishi kwa muda fulani. Wanasema kwamba, muda mrefu kabla ya mtoto kuzaliwa, huyo huwa anapendwa na wazazi wake. Kuna kifungo cha pekee pamoja na mama. Mtoto huyo mchanga anapokufa, mama huhisi kwamba mtu halisi amekufa. Na hilo ndilo jambo ambalo wengine wanahitaji kuelewa.

      Jinsi Kasirani na Kuhisi Una Hatia Kwaweza Kukuathiri

      Mama mwingine alionyesha hisia zake alipoambiwa kwamba mwana wake wa miaka sita alikuwa amekufa ghafula kwa sababu ya tatizo la moyo alilozaliwa nalo. “Nilipatwa na mfululizo wa maitikio—ganzi, kutoamini, kuhisi una hatia, na kasirani kuelekea mume wangu na daktari kwa ajili ya kutong’amua jinsi hali yake ilivyokuwa mbaya sana.”

      Kasirani yaweza kuwa dalili nyingine ya huzuni. Huenda ikawa ni kasirani kuelekea madaktari na wauguzi, ukihisi kwamba wangalipaswa kufanya zaidi ili wamshughulikie yule mfu. Au huenda ikawa ni kasirani kuelekea marafiki na watu wa ukoo ambao, yaonekana, wanasema au kufanya jambo lisilofaa. Wengine humkasirikia yule mfu kwa sababu ya kupuuza afya yake. Stella akumbuka hivi: “Nakumbuka nikiwa nimemkasirikia mume wangu kwa sababu nilijua hali ingalikuwa tofauti. Yeye alikuwa amekuwa mgonjwa sana, lakini alikuwa amepuuza maonyo ya madaktari.” Na nyakati nyingine kuna kasirani kuelekea yule mfu kwa sababu ya mizigo yenye kulemea ambayo kifo chake chamletea yule anayebaki.

      Wengine wanahisi wana hatia kwa sababu ya kuwa na kasirani—yaani, huenda wakajilaumu kwa sababu wanahisi kasirani. Wengine wanajilaumu kwa ajili ya kifo cha mpendwa wao. “Yeye asingalikufa,” wao wanajisadikisha, “laiti tu ningalimfanya aende kwa daktari mapema zaidi” au “ningalimfanya amwone daktari mwingine” au “ningalimfanya atunze afya yake vema zaidi.”

      Kwa wengine kuhisi wana hatia kunafikia hatua nyingine zaidi, hasa ikiwa mpendwa wao alikufa ghafula, bila kutazamiwa. Wanaanza kukumbuka nyakati walizokuwa wamemkasirikia yule mfu au walikuwa wamebishana naye. Au huenda wakahisi kwamba kwa kweli hawakuwa kabisa vile wangalipaswa kuwa kuelekea yule mfu.

      Ile kawaida ya kuhuzunika kwa muda mrefu ya akina mama wengi huunga mkono yale ambayo wastadi wengi husema, kwamba kifo cha mtoto huacha pengo la daima maishani mwa wazazi, hasa mama.

      Unapofiwa na Mwenzi wa Ndoa

      Kufiwa na mwenzi wa ndoa ni aina nyingine ya umivu kali la kimoyoni, hasa ikiwa wote wawili waliishi maisha yenye utendaji mwingi wakiwa pamoja. Hilo laweza kumaanisha mwisho wa mtindo-maisha mzima walioshiriki pamoja, mwisho wa kusafiri, wa kufanya kazi, wa kuwa na vitumbuizo, na wa kutegemeana.

      Eunice aeleza yale yaliyotendeka wakati mume wake alipokufa ghafula kutokana na ugonjwa wa moyo. “Kwa juma la kwanza, nilikuwa katika hali ya kutohisi lolote kihisiamoyo, kana kwamba mwili wangu haukuwa ukifanya kazi tena. Hata sikuweza kuonja wala kunusa. Hata hivyo, hisi yangu ya kufikiri vizuri iliendelea ikiwa imejitenga. Kwa sababu nilikuwa nimekuwa na mume wangu walipokuwa wakijaribu kusawazisha hali yake kwa kutumia CPR (utaratibu wa kumhuisha mtu ili aanze kupumua kikawaida) pamoja na madawa, sikupatwa na zile dalili za kawaida za kukana. Hata hivyo, nilihisi kukata tamaa sana, kana kwamba nilikuwa nikitazama gari likianguka kutoka gengeni (mteremko wa ghafula) nami singeweza kufanya lolote juu yalo.”

      Je! alitoa machozi? “Bila shaka nilifanya hivyo, hasa niliposoma yale mamia ya kadi za kusikitikia nilizokuwa nimepokea. Nililia kwa kila moja. Hilo lilinisaidia kujiweza hadi sehemu iliyobaki ya siku. Lakini hakuna chochote ambacho kingeweza kusaidia nilipoulizwa mara kwa mara jinsi nilivyohisi. Bila shaka, nilikuwa katika hali ya kuhuzunika sana.”

      Ni nini kilichomsaidia Eunice avumilie huzuni yake? “Bila kung’amua, niliamua kuendelea na maisha yangu bila kujua,” yeye asema. “Hata hivyo, jambo liniumizalo bado ni wakati nikumbukapo kwamba mume wangu, aliyependa uhai sana, hayupo hapa kuufurahia.”

      “Usiruhusu Wengine Wakuamulie . . . ”

      Watunga-vitabu wa Leavetaking—When and How to Say Goodbye washauri hivi: “Usiruhusu wengine wakuamulie jinsi upaswavyo kutenda au kuhisi. Kawaida ya kuhuzunika huwa tofauti kwa kila mtu. Huenda wengine wakafikiri—na wakakujulisha kwamba wao wanafikiri—una huzuni nyingi mno au huna huzuni ya kutosha. Wasamehe na usahau hilo. Kwa kujaribu kujilazimisha kuwa jinsi wengine watakavyo au jamii ya watu kwa ujumla itakavyo, unazuia ukuzi wako wa kurudia afya nzuri ya kihisiamoyo.”

      Bila shaka, watu tofauti hushughulikia huzuni yao kwa njia tofauti-tofauti. Sisi hatujaribu kudokeza kwamba njia moja kwa lazima ndiyo iliyo bora zaidi ya nyingine kwa kila mtu. Hata hivyo, hatari hutokea wakati mtu aliye na huzuni akwamapo katika hali fulani, wakati hawezi kujipatanisha na uhalisi wa hali. Hapo ndipo huenda msaada ukahitajika kutoka kwa marafiki wenye huruma. Biblia husema: “Rafiki [“wa kweli,” NW] hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Kwa hiyo usiogope kutafuta msaada, kuongea, na kutoa machozi.—Mithali 17:17.

      Huzuni ni itikio la kawaida la kufiwa, na si vibaya huzuni yako kuonekana waziwazi kwa wengine. Lakini maswali mengine yahitaji majibu: ‘Naweza kuishije nikiwa na huzuni yangu? Je! ni kawaida kupatwa na hisia za kuwa na hatia na kasirani? Napaswa kushughulikaje kwa kufaa na maitikio hayo? Ni nini kiwezacho kunisaidia nivumilie kifo na huzuni hii?’ Sehemu ifuatayo itajibu maswali hayo na mengine.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa kielelezo, Wayoruba wa Nigeria wana imani ya kimapokeo ya nafsi kuzaliwa upya katika mwili mwingine. Kwa hiyo mama anapofiwa na mtoto, kuna huzuni nyingi lakini ni kwa kipindi kifupi tu, kwani kama vile kibwagizo (kiitikio) fulani cha Kiyoruba kisemacho: “Maji ndiyo yamemwagika. Kibuyu hakijavunjika.” Kulingana na Wayoruba, hicho chamaanisha kwamba kile kibuyu kibebacho maji, yaani mama, aweza kuzaa mtoto mwingine—labda nafsi iliyozaliwa upya ya yule aliyekufa. Mashahidi wa Yehova hawafuati mapokeo yoyote yenye msingi wa ushirikina mbalimbali unaotokana na mawazo bandia juu ya kutokufa kwa nafsi na kuzaliwa upya katika mwili mwingine, ambayo hayana msingi katika Biblia.—Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4, 20.

      [Sanduku katika ukurasa wa 13]

      Maswali ya Kufikiriwa Sana

      Huzuni ya watu wengine huathiriwaje na utamaduni wao?

      Tuna vielelezo vipi katika Biblia vya wale walioonyesha huzuni waziwazi?

      Wengine wameitikiaje kifo cha mpendwa? Wewe umeitikiaje katika hali zinazofanana na hizo?

      Ni nini kifanyacho kifo cha mwenzi wa ndoa kiwe ono la aina tofauti?

      Kawaida ya kuhuzunika huwaje? Je! ni vibaya kuhuzunika?

      Ni nini baadhi ya mambo ya kawaida ya kuhuzunika? (Ona kisanduku kwenye ukurasa wa 9.)

      Ni hali zipi za pekee huathiri wazazi katika kifo cha ghafula cha kitoto? (Ona kisanduku kwenye ukurasa wa 12.)

      Akina mama wengi wanaathiriwaje na hali ya kuharibikiwa mimba au kuzaa mtoto mfu? (Ona kisanduku kwenye ukurasa wa 10.)

      [Sanduku katika ukurasa wa 9]

      Kawaida ya Kuhuzunika

      Neno “kawaida” halidokezi kwamba huzuni ina ratiba au programu yoyote iliyo imara. Maitikio ya huzuni yaweza kupitana na kuchukua urefu mbalimbali wa wakati, ikitegemea mtu mmoja-mmoja. Orodha hii si kamili. Maitikio mengine yaweza kudhihirishwa pia. Zifuatazo ni baadhi ya dalili za huzuni ambazo huenda mtu akapatwa nazo.

      Maitikio ya mapema: Mshtuko wa kwanza; kutoamini, kukana; ganzi ya kihisiamoyo; hisia za kuwa na hatia; kasirani.

      Huzuni nyingi sana yaweza kutia ndani: Kusahau-sahau na kutoweza kulala usingizi; uchovu wa kupita kiasi; mabadiliko ya ghafula ya hali ya moyoni; kuamua na kufikiri kwa njia isiyofaa; vipindi vya kulia-lia; mabadiliko katika hamu ya kula chakula, kukiwa na matokeo ya kupoteza uzani na kuongeza uzani; ishara mbalimbali za afya iliyoathiriwa; kusinzia-sinzia isivyo kawaida; uwezo uliopungua wa kufanya kazi; kuona-ona njozi—kuhisi, kusikia, kumwona yule mfu; katika hali ya kufiwa na mtoto, kuchukizwa na mwenzi wako wa ndoa bila sababu nzuri.

      Kipindi cha kupata usawaziko: Huzuni pamoja na kukumbuka kwa kutamani sana wakati uliopita; kukumbuka mambo yenye kupendeza zaidi juu ya yule mfu, hata kutia ndani yale yenye kuchekesha.

      [Sanduku katika ukurasa wa 10]

      Kuharibikiwa Mimba na Kuzaa Mtoto Mfu—Huzuni ya Mama

      Ingawa alikuwa na watoto wengine tayari, Monna alikuwa akitazamia kwa hamu kuzaliwa kwa mtoto wake mwingine. Hata kabla ya yeye kuzaliwa, alikuwa mtoto mchanga “aliyecheza naye, kuongea naye, na kuotea ndoto.”

      Ile kawaida ya kupata kifungo kati ya mama na mtoto asiyezaliwa ilikuwa yenye nguvu. Yeye aendelea hivi: “Rachel Anne alikuwa mtoto mchanga aliyepiga teke vitabu kutoka tumboni pangu [akiwa bado hajazaliwa], alifanya nikose usingizi usiku. Ningali naweza kukumbuka yale mateke madogo ya kwanza, kama vile midukuo ya upendo, yenye uanana. Kila wakati aliposonga, nilijawa na upendo mwingi. Nilimjua vizuri sana hivi kwamba nilijua alipokuwa akiumwa, alipokuwa mgonjwa.”

      Monna aendelea na simulizi lake hivi: “Daktari hakuniamini mpaka kulipokuwa kumechelewa mno. Aliniambia niache kuwa na wasiwasi. Naamini nilihisi alipokufa. Yeye aligeuka tu ghafula na kwa nguvu. Siku iliyofuata alikuwa amekufa.”

      Ono la Monna si tukio lisilo la kawaida. Kulingana na watunga-vitabu Friedman na Gradstein, katika kitabu chao Surviving Pregnancy Loss, karibu wanawake milioni moja kwa mwaka katika Marekani pekee huharibikiwa mimba. Bila shaka, hesabu ya ulimwenguni pote ni wengi zaidi.

      Mara nyingi watu hukosa kung’amua kwamba kuharibikiwa mimba au kuzaa mtoto mfu ni msiba kwa mwanamke na ni mmoja akumbukao—labda muda wote wa maisha yake. Kwa kielelezo, Veronica, ambaye amezeeka sasa, akumbuka kuharibikiwa kwake mimba mara kadhaa na hasa akumbuka yule mtoto mchanga mfu aliyemzaa, aliyekuwa hai hadi mwezi wa tisa na kuzaliwa akiwa na uzani wa kilo sita. Alimbeba akiwa amekufa ndani yake kwa yale majuma mawili ya mwisho. Alisema hivi: “Kumzaa mtoto mfu ni jambo mbaya sana kwa mama.”

      Maitikio ya akina mama hawa waliokata tamaa hayaeleweki sikuzote, hata na wanawake wengine. Mwanamke fulani aliyekuwa amepoteza mtoto wake kupitia mimba iliyoharibika aliandika hivi: “Yale ambayo nimejifunza kwa njia yenye maumivu sana ni kwamba kabla ya hilo kunipata, kwa kweli sikuwa na wazo lolote kuhusu yale ambayo marafiki zangu walilazimika kuvumilia. Sikugusika moyo upesi wala kuelewa vema hali yao kama vile nionavyo kwamba watu hawagusiki moyo wala kuelewa vema hali yangu.”

      Tatizo jingine kwa mama anayehuzunika ni kuona kwamba mume wake hahisi jinsi yeye anavyohisi juu ya hasara hiyo. Mke mmoja alieleza jambo hilo hivi: “Nilikatishwa tamaa kabisa na mume wangu wakati huo. Kulingana na maoni yake, kwa kweli hakukuwa na mimba yoyote. Hakuweza kuhisi ile huzuni niliyokuwa nikihisi. Alikuwa mwenye kusikitikia sana hofu zangu lakini si mwenye kusikitikia huzuni yangu.”

      Labda itikio hilo ni la asili kwa mume—yeye hawi na kifungo kilekile cha kimwili na cha kihisiamoyo (pamoja na kijusi) kama vile mke wake mjamzito huwa nacho. Hata hivyo, anahisi hasara fulani. Na ni muhimu kwamba mume na mke wang’amue kwamba wanateseka pamoja, ingawa ni kwa njia tofauti-tofauti. Wao wapaswa washiriki huzuni yao pamoja. Mume akificha huzuni yake, huenda mke wake akafikiri kwamba yeye hakugusika moyo upesi na hali hiyo. Kwa hiyo shirikini pamoja machozi, mawazo, na makumbatio yenu. Onyesheni kwamba mnahitajiana zaidi ya wakati mwingine wowote. Ndiyo, waume, onyesheni hisia-mwenzi yenu.

      [Sanduku katika ukurasa wa 12]

      Ugonjwa wa Kifo cha Ghafula cha Kitoto—Kukabili Hiyo Huzuni

      Kifo cha ghafula cha mtoto mchanga ni msiba wenye kufadhaisha. Siku moja mtoto mchanga aonekanaye kuwa wa kawaida, mwenye afya nzuri ashindwa kuamka. Hilo halitazamiwi hata kidogo, kwani ni nani awaziaye kwamba kitoto au mtoto yeyote atakufa kabla ya wazazi wake? Mtoto mchanga ambaye amekuja kupendwa sana na mamake kwa ghafula awa chanzo cha huzuni kubwa.

      Hisia za kuwa na hatia zaanza kuja kwa wingi. Huenda wazazi wakahisi wao ndio wa kulaumiwa kwa ajili ya kifo hicho, kana kwamba kilisababishwa na uzembe fulani. Wanajiuliza, ‘Tungaliweza kufanya nini ili kukizuia?’b Katika hali nyingine, huenda mume, bila msingi wowote, akamlaumu mke wake bila kujua. Alipoenda kazini, yule mtoto mchanga alikuwa hai na mwenye afya nzuri. Alipofika nyumbani, mtoto huyo mchanga alikuwa amekufa kitandani mwake! Mke wake alikuwa akifanya nini? Yeye alikuwa wapi wakati huo? Ni lazima maswali hayo yenye kusumbua yajibiwe ili yasisababishe mkazo juu ya ndoa.

      Hali zisizotazamiwa na zisizoweza kuonwa kimbele zilisababisha msiba huo. Biblia husema: “Nikarudi, na kuona chini ya jua, ya kwamba si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” NW] huwapata wote.”—Mhubiri 9:11.

      Wengine wanaweza kusaidiaje wakati familia inapofiwa na mtoto mchanga? Mama mmoja aliyefiwa aliitikia hivi: “Rafiki mmoja alikuja akaisafisha nyumba bila mimi kusema neno lolote. Wengine walitupikia chakula. Baadhi yao walisaidia kwa kunikumbatia tu—bila kusema maneno yoyote, kumbatio tu. Sikutaka kuongea juu yalo. Sikutaka kueleza tena na tena juu ya kile kilichotendeka. Sikuhitaji maswali ya kupeleleza, kana kwamba nilikuwa nimekosa kufanya jambo fulani. Nilikuwa ndiye mama [yake]; ningalifanya jambo lolote lile kumwokoa mtoto wangu mchanga.”

      [Maelezo ya Chini]

      b Sudden Infant Death Syndrome (SIDS, Ugonjwa wa Kifo cha Ghafula cha Kitoto), ambao kwa kawaida huwapata watoto wachanga wenye umri wa mwezi mmoja hadi sita, ndilo jina linalotumiwa wakati watoto wachanga wenye afya nzuri wanapokufa ghafula bila sababu yoyote yenye kuelezeka. Katika hali nyingine inaaminiwa kwamba uwezekano huo waweza kuepukwa ikiwa mtoto mchanga analazwa chali (kwa mgongo) au upande mmoja lakini si kifudifudi. Hata hivyo, hakuna njia ya kulala itakayozuia kila kisa cha Ugonjwa wa Kifo cha Ghafula cha Kitoto.

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Ni kawaida kuhuzunika na kutoa machozi wakati mpendwa anapokufa

      [Picha katika ukurasa wa 11]

      Kufiwa na mtoto ni umivu kali sana la kimoyoni—sikitikio na hisia-mwenzi ya kweli yaweza kuwasaidia wazazi

  • Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • Naweza Kuishije Nikiwa na Huzuni Yangu?

      “NILIHISI kusongwa sana nizuie hisia zangu,” aeleza Mike alipokumbuka kifo cha baba yake. Kwa Mike, kuzuia huzuni yake lilikuwa jambo la kiume kufanya. Hata hivyo baadaye aling’amua kwamba alikuwa amekosea. Kwa hiyo rafikiye Mike alipofiwa na babu yake, Mike alijua jambo la kufanya. Yeye asema hivi: “Miaka michache iliyopita, ningalimpigapiga begani na kusema ‘Uwe mwanamume.’ Sasa niligusa mkono wake na kusema, ‘Hisi vile utakavyo kuhisi. Hilo litakusaidia ushughulike vya kufaa na hali hii. Ikiwa wataka niende, nitaenda. Ikiwa wataka nikae, nitakaa. Lakini usiogope kuhisi.’”

      MaryAnne pia alihisi kusongwa azuie hisia zake wakati mume wake alipokufa. “Nilihangaikia sana kuwekea wengine kielelezo chema,” yeye akumbuka, “hivi kwamba sikujiruhusu nionyeshe hisia za kawaida. Lakini hatimaye nilijifunza kwamba kujaribu kuwa nguzo ya imara kwa ajili ya wengine hakukuwa kunanisaidia. Nilianza kuchanganua hali yangu na kusema, ‘Lia ikiwa ni lazima ulie. Usijaribu kuwa imara mno. Onyesha hisia zako zote kabisa.’”

      Kwa hiyo Mike na pia MaryAnne wanapendekeza hivi: Jiruhusu uhuzunike! Nao wasema kweli. Kwa nini? Kwa sababu kuhuzunika ni ondoleo la kihisiamoyo linalohitajika. Kuondosha hisia zako kwaweza kutuliza ule msongo unaokabili. Wonyesho wa asili wa hisiamoyo, pamoja na uelewevu na habari sahihi, unakuruhusu uzionyeshe hisia zako ifaavyo.

      Bila shaka, si kila mtu aonyeshaye huzuni kwa njia ileile. Na mambo kama ya kwamba mpendwa alikufa ghafula au kwamba kifo kilikuja baada ya ugonjwa wa muda mrefu huenda yakaathiri itikio la kihisiamoyo la wale wanaobaki. Lakini kuna jambo moja lionekanalo kuwa hakika: Kuzuia hisia zako kwaweza kukudhuru kimwili na kihisiamoyo pia. Ni bora zaidi kwa afya ukiondosha huzuni yako. Jinsi gani? Maandiko yana shauri lenye kutumika.

      Kuondosha Huzuni—Jinsi Gani?

      Kuongea kwaweza kuwa njia yenye kusaidia kuondosha huzuni. Baada ya kifo cha watoto wake wote kumi, pamoja na misiba mingine ya kibinafsi, Ayubu yule mzee wa ukoo wa kale alisema hivi: “Hakika nafsi yangu yahisi kukirihi kuelekea maisha yangu. Nitatoa [Kiebrania, “nitaachilia”] hangaiko langu kuhusu mwenyewe. Nitasema katika uchungu wa nafsi yangu!” (Ayubu 1:2, 18, 19; 10:1, NW) Ayubu hakuweza tena kuzuia hangaiko lake. Alilazimika kuliachilia; alihitaji ‘kunena.’ Vivyo hivyo, mtunga-drama Mwingereza Shakespeare aliandika hivi katika drama iitwayo Macbeth: “Onyesha majonzi; huzuni isiyosema manong’ono hulemea moyo nayo huupasua.”

      Kwa hiyo kuongea juu ya hisia zako pamoja na “rafiki wa kweli” atakayesikiliza kwa saburi na kwa kusikitikia kwaweza kuleta kadiri fulani ya kitulizo. (Mithali 17:17, NW) Mara nyingi kueleza maono na hisia hufanya iwe rahisi zaidi kuzielewa na kushughulika nazo kwa kufaa. Na ikiwa msikilizaji ni mtu mwingine aliyefiwa ambaye ameshughulika vya kufaa na hasara yake mwenyewe kwa mafanikio, huenda ukapata madokezo yenye kutumika juu ya jinsi ya kushughulika vya kufaa na hali yako. Mtoto wake alipokufa, mama mmoja alieleza kwa nini ilisaidia kuongea na mwanamke mwingine aliyekuwa amepatwa na hasara hiyohiyo: “Kujua kwamba mtu mwingine alikuwa amepatwa na jambo lilo hilo, alikuwa angali na afya nzuri ya kiakili na ya kihisiamoyo, na kwamba alikuwa angali anaendelea kuishi na kuwa na utaratibu fulani maishani mwake tena kuliniimarisha sana.”

      Namna gani ikiwa huhisi starehe kuongea juu ya hisia zako? Baada ya kifo cha Sauli na Yonathani, Daudi alitunga wimbo wa maombolezo ambao katika huo alimwaga huzuni yake yote. Hatimaye wimbo huo wa maombolezo ukawa sehemu ya maandishi ya kitabu cha Biblia cha Samweli wa Pili. (2 Samweli 1:17-27; 2 Mambo ya Nyakati 35:25) Vivyo hivyo, wengine huona ni rahisi zaidi kujieleza kwa kuandika. Mjane mmoja aliripoti kwamba yeye alikuwa akiandika hisia zake kisha siku kadhaa baadaye alikuwa akisoma yale aliyokuwa ameandika. Aliona hiyo kuwa njia yenye kusaidia kuondosha huzuni.

      Iwe ni kwa kuongea au kwa kuandika, kuwasilisha hisia zako kwaweza kukusaidia uondoshe huzuni yako. Kwaweza pia kuondolea mbali kutoelewana. Mama mmoja aliyefiwa aeleza hivi: “Mume wangu nami tulisikia juu ya waume na wake wengine waliotalikana baada ya kufiwa na mtoto, nasi hatukutaka hilo litupate. Kwa hiyo wakati wowote tulipokasirika, tukitaka kulaumiana, tulikuwa tukiongea juu yalo. Nafikiri tulikaribiana sana kwa kufanya hivyo.” Hivyo, kujulisha hisia zenu kwaweza kuwasaidia mwelewe kwamba hata ingawa huenda ikawa mnashiriki pamoja hasara ile ile, wengine waweza kuhuzunika kwa njia tofauti—kwa mwendo wao wenyewe na kwa njia yao wenyewe.

      Jambo jingine liwezalo kurahisisha ondoleo la huzuni ni kulia. Kuna “wakati wa kulia,” Biblia husema. (Mhubiri 3:1, 4, NW) Kwa hakika kifo cha mtu fulani tumpendaye huleta wakati wa jinsi hiyo. Kulia machozi ya huzuni kwaonekana kuwa sehemu ya lazima ya kawaida ya kupona.

      Mwanamke mmoja mchanga aeleza jinsi rafiki wa karibu alivyomsaidia ashughulike vya kufaa na hali wakati mama yake alipokufa. Yeye akumbuka hivi: “Sikuzote rafiki yangu alikuwapo kwa ajili yangu. Alilia pamoja nami. Aliongea nami. Niliweza tu kuonyesha hisiamoyo zangu waziwazi sana, na hilo lilikuwa jambo la maana kwangu. Sikuhitaji kuaibika kwa sababu ya kulia.” (Ona Warumi 12:15.) Wewe pia hupaswi kuaibika kwa sababu ya machozi yako. Kama vile tumeona, Biblia imejaa vielelezo vya wanaume na wanawake wa imani—kutia na Yesu Kristo—waliolia machozi ya huzuni waziwazi bila kuonekana kuwa na aibu.—Mwanzo 50:3; 2 Samweli 1:11, 12; Yohana 11:33, 35.

      Huenda ukaona kwamba kwa wakati fulani hisiamoyo zako zitatokea bila kutazamiwa. Huenda machozi yakatiririka bila ya wewe kujua kimbele. Mjane mmoja aliona kwamba kununua vitu kwenye duka kubwa (jambo alilokuwa amefanya mara nyingi pamoja na mume wake) kuliweza kumfanya alie, hasa wakati, kwa sababu ya kuzoea, alipofikia ili achukue vyakula vilivyopendwa sana na mume wake. Jionyeshe saburi. Na usihisi kwamba ni lazima uyazuie machozi yasitoke. Kumbuka, hiyo ni sehemu ya asili na ya lazima ya kuhuzunika.

      Kushughulika vya Kufaa na Hali ya Kuhisi Una Hatia

      Kama ilivyoonyeshwa kimbele, wengine wana hisia za kuwa na hatia baada ya kufiwa na mpendwa. Hilo huenda likasaidia kueleza sababu ya ile huzuni nyingi ya yule mwanamume mwaminifu Yakobo alipofanywa aamini kwamba mwana wake Yusufu alikuwa ameuawa na “hayawani-mwitu mkali.” Yakobo mwenyewe alikuwa amemtuma Yusufu aende akachunguze hali njema ya ndugu zake. Kwa hiyo yaelekea Yakobo alisumbuliwa na hisia za kuwa na hatia, kama vile ‘Kwa nini nilimtuma Yusufu akiwa peke yake? Kwa nini nilimtuma kwenye eneo ambalo limejaa mahayawani-mwitu?’—Mwanzo 37:33-35, NW.

      Labda wewe wahisi kwamba uzembe fulani upande wako ulichangia kifo cha mpendwa wako. Kung’amua kwamba kuhisi una hatia—iliyo halisi au ya kuwaziwa tu—ni itikio la kawaida la huzuni kwenyewe kwaweza kusaidia. Hapa tena, usihisi kwamba hupaswi kuonyesha hisia hizo. Kuongea juu ya jinsi uhisivyo kwamba una hatia kwaweza kuandaa ondoleo kubwa linalohitajiwa la huzuni.

      Ingawa hivyo, ng’amua kwamba haidhuru ni kadiri gani tumpendavyo mtu mwingine, sisi hatuwezi kudhibiti maisha yake, wala hatuwezi kuzuia “wakati na tukio lisilotazamiwa” lisiwapate wale tuwapendao. (Mhubiri 9:11, NW) Ingawaje, bila shaka madhumuni yako hayakuwa mabaya. Kwa kielelezo, kwa kutofanya mpango wa kumwona daktari mapema zaidi, je, wewe ulikusudia mpendwa wako awe mgonjwa na kufa? Bila shaka sivyo! Basi, je, una hatia kwelikweli ya kusababisha kifo cha mtu huyo? La.

      Mama mmoja alijifunza kushughulika vya kufaa na hali ya kuhisi ana hatia baada ya binti yake kufa katika aksidenti ya gari. Yeye aeleza hivi: “Nilihisi nina hatia kwa sababu ya kumtuma. Lakini nikaja kung’amua kwamba kuhisi hivyo lilikuwa jambo la upuuzi. Kumtuma aende na baba yake afanye kazi fulani hakukuwa kosa. Hiyo ilikuwa aksidenti tu iliyo mbaya sana.”

      ‘Lakini kuna mambo mengi sana ambayo laiti ningalisema au kufanya,’ huenda ukasema. Ni kweli, lakini ni nani kati yetu awezaye kusema kwamba sisi tumekuwa baba, mama, au mtoto mkamilifu? Biblia hutukumbusha hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyu ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2; Warumi 5:12, NW) Kwa hiyo kubali uhakika wa kwamba wewe si mkamilifu. Kuendelea kufikiri-fikiri ati “laiti tu ningalifanya hivi au vile” hakutabadili chochote, lakini huenda kwaweza kukawiza kupata kwako nafuu.

      Ikiwa una sababu nzuri za kuamini kwamba hatia yako ni halisi, isiyowaziwa tu, basi fikiria lile jambo la maana zaidi ya yote katika kutuliza hisia ya kuwa na hatia—msamaha wa Mungu. Biblia hututia moyo hivi: “BWANA, kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama? Lakini kwako kuna msamaha.” (Zaburi 130:3, 4) Huwezi kurudia wakati uliopita na kubadili chochote. Lakini, waweza kumwomba Mungu msamaha kwa makosa ya wakati uliopita. Kisha nini? Ikiwa Mungu anaahidi kufuta kabisa makosa yako, je, wewe hupaswi pia kujisamehe?—Mithali 28:13; 1 Yohana 1:9.

      Kushughulika vya Kufaa na Kasirani

      Je! wahisi kasirani pia, labda kuelekea madaktari, wauguzi, marafiki, au hata yule mfu? Ng’amua kwamba hilo pia ni itikio la kawaida la kufiwa. Labda kasirani yako yaandamana kwa asili na uchungu unaohisi. Mwandikaji mmoja alisema: “Ni kwa kuja kutambua kukasirika kwako tu—si kwa kutenda kulingana nayo bali kwa kujua unahisi hivyo—ndipo uwezapo kuwa huru na matokeo yayo yenye uharibifu.”

      Huenda pia ikasaidia kueleza au kushiriki kasirani hiyo na mwingine. Jinsi gani? Kwa hakika si kwa mifoko isiyodhibitiwa. Biblia huonya kwamba kasirani yenye kudumu muda mrefu ni hatari. (Mithali 14:29, 30) Lakini huenda ukapata faraja katika kuongea juu yayo pamoja na rafiki mwenye kuelewa. Na wengine huona kwamba mazoezi yenye nguvu wanapokuwa wamekasirika ni njia yenye kusaidia ya kuondosha kasirani.—Ona pia Waefeso 4:25, 26.

      Ingawa ni jambo la maana kuonyesha hisia zako waziwazi na kwa haki, onyo lafaa kutolewa hapa. Kuna tofauti kubwa kati ya kuonyesha hisia zako na kuwafokea wengine. Hakuna haja ya kuwalaumu wengine kwa sababu ya kasirani na kukatishwa tamaa kwako. Kwa hiyo uwe mwangalifu juu ya kueleza hisia zako, lakini si kwa njia yenye uhasama. (Mithali 18:21) Kuna msaada mmoja muhimu sana katika kushughulika vya kufaa na huzuni, na tutauzungumzia sasa.

      Msaada Kutoka kwa Mungu

      Biblia hututia moyo hivi: “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” (Zaburi 34:18) Ndiyo, zaidi ya jambo jingine lolote, uhusiano na Mungu waweza kukusaidia ushughulike vya kufaa na kifo cha mtu fulani umpendaye. Jinsi gani? Madokezo yote yenye kutumika ambayo yametolewa hadi sasa yametegemea au yanapatana na Neno la Mungu, Biblia. Kuzitumia kwaweza kukusaidia ushughulike vya kufaa na hali.

      Kwa kuongezea, usipunguze umaana wa thamani ya sala. Biblia hutusihi hivi: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Ikiwa kumweleza rafiki mwenye kusikitikia hisia zako kwaweza kusaidia, basi kummwagia “Mungu wa faraja yote” yaliyomo moyoni mwako kwaweza kukusaidia hata zaidi kama nini!—2 Wakorintho 1:3, NW.

      Si kwamba sala hutufanya tuhisi vizuri zaidi tu. “Msikiaji wa sala” anaahidi kuwatolea roho takatifu watumishi wake waiombao kwa moyo mweupe. (Zaburi 65:2; Luka 11:13, NW) Na roho takatifu, au kani ya utendaji ya Mungu, yaweza kukupa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili uendelee kuishi siku moja baada ya nyingine. (2 Wakorintho 4:7, NW) Kumbuka: Mungu aweza kuwasaidia watumishi wake waaminifu wavumilie tatizo lolote lile ambalo huenda wakakabili.

      Mwanamke mmoja aliyefiwa na mtoto wake akumbuka jinsi nguvu ya sala ilivyomsaidia yeye na mume wake wakati wa hasara yao. “Ikiwa tulikuwa nyumbani usiku na huzuni ikazidi, tulikuwa tukisali pamoja kwa sauti kubwa,” yeye aeleza. “Mara ya kwanza tulilazimika kufanya lolote bila yeye—mkutano wa kutaniko wa kwanza tuliokwenda, mkusanyiko wa kwanza tuliohudhuria—tulikuwa tukisali ili kupata imara. Tulipoamka asubuhi na ikaonekana hatuwezi kuvumilia uhalisi wa hali hiyo, tulikuwa tukisali kwa Yehova atusaidie. Kwa sababu fulani, nilikuwa na umivu kali kwelikweli la kimoyoni kuingia nyumbani nikiwa peke yangu. Kwa hiyo kila wakati nilipokuja nyumbani nikiwa peke yangu, nilikuwa tu nikimwomba Yehova tafadhali anisaidie kudumisha kadiri fulani ya utulivu.” Mwanamke huyo mwaminifu aamini kwa uthabiti na ifaavyo kwamba sala hizo zilifanya hali iwe tofauti. Wewe pia waweza kuona kwamba likiwa tokeo la sala zako zenye udumifu, ‘amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda moyo wako na nguvu zako za akili.’—Wafilipi 4:6, 7; Warumi 12:12, NW.

      Kwa kweli ule msaada ambao Mungu huandaa hufanya hali iwe tofauti. Mtume Mkristo Paulo alisema kwamba Mungu “hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tupate kuweza kufariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki.” Ni kweli, msaada wa kimungu hauondoi umivu, lakini waweza kufanya hali iwe rahisi zaidi kuvumilia. Hilo halimaanishi kwamba hutalia tena au utamsahau mpendwa wako. Lakini waweza kupata nafuu. Na upatapo nafuu, yale ambayo umepatwa nayo yaweza kukufanya uwe mwenye kuelewa na mwenye kusikitikia zaidi katika kuwasaidia wengine washughulike vya kufaa na hasara hiyohiyo.—2 Wakorintho 1:4, NW.

      [Sanduku katika ukurasa wa 19]

      Maswali ya Kufikiriwa Sana

      Kwa nini ni jambo la maana kujiruhusu uhuzunike?

      Waweza kuondoshaje huzuni yako?

      Maandiko yaweza kukusaidiaje ushughulike vya kufaa na hisia za kuwa na hatia na kasirani?

      Uhusiano na Mungu waweza kukusaidia kwa njia gani ushughulike vya kufaa na kifo cha mpendwa?

      Ni nini baadhi ya madokezo yenye kutumika ya kushughulika vya kufaa na huzuni?

      [Sanduku katika ukurasa wa 18]

      Baadhi ya Madokezo Yenye Kutumika

      Tegemea marafiki: Usisite kuwaruhusu wengine wasaidie ikiwa wanajitolea kufanya hivyo na kwa kweli wahitaji msaada huo. Elewa ya kwamba huenda hiyo ikawa njia yao ya kukuonyesha jinsi wahisivyo; labda hiyo ndiyo njia rahisi zaidi kwao kufanya hivyo kuliko kueleza hisia hizo kwa maneno.—Mithali 18:24.

      Tunza afya yako: Kuhuzunika kwaweza kukudhoofisha, hasa mwanzoni. Mwili wako wahitaji pumziko la kutosha, mazoezi yenye afya, na lishe ifaayo kuliko wakati mwingine wowote. Kuchunguzwa pindi kwa pindi na daktari wa familia yako kwaweza kuwa jambo zuri.

      Ahirisha maamuzi makubwa: Ikiwezekana, ngoja angalau muda fulani mpaka unapoanza kufikiria kwa wazi zaidi kabla ya kuamua mambo kama vile kuuza nyumba yako au kubadili kazi yako. (Mithali 21:5) Mjane mmoja alikumbuka kwamba siku kadhaa baada ya mume wake kufa, yeye aliwapa wengine vitu vingi vya kibinafsi vya mume wake. Baadaye, aling’amua kwamba alikuwa amewapa vikumbusha vidogo-vidogo alivyohazini.

      Jionyeshe saburi: Mara nyingi huzuni huendelea muda mrefu zaidi ya vile watu kwa ujumla hung’amua. Vikumbusha vya kila mwaka vya mpendwa aliyekufa vyaweza kurudisha umivu kali. Picha za pekee, nyimbo, au hata harufu zaweza kutokeza machozi. Uchunguzi mmoja wa kisayansi juu ya kufiwa ulieleza yafuatayo kuhusu kawaida ya kuhuzunika: “Huenda yule aliyefiwa akabadilika-badilika upesi na kwa njia yenye kutokeza kutoka hali moja ya hisia hadi nyingine, na hali ya kuepuka vikumbusha vya yule mfu yaweza kubadilishana na hali ya ukuzaji wa kumbukumbu hiyo kimakusudi kwa kipindi fulani cha wakati.” Kumbuka ahadi za Yehova zenye thamani kubwa.—Wafilipi 4:8, 9.

      Wape wengine nafasi: Jaribu kuwa mwenye saburi kuelekea wengine. Ng’amua kwamba hali ni ngumu kwao. Kwa sababu ya kutojua la kusema, huenda bila kufikiri wakasema jambo lisilofaa.—Wakolosai 3:12, 13.

      Epuka kutumia madawa au kileo ili kushughulika na huzuni yako: Kitulizo chochote kinachotolewa na madawa au kileo ni cha muda tu. Madawa yapaswa kutumiwa chini ya usimamizi wa daktari tu. Lakini uwe mwangalifu; madawa mengi ni yenye kutia uraibu (uzoevu). Kwa kuongezea, huenda hayo yakakawiza kawaida ya kuhuzunika. Tabibu fulani aonya hivi: “Lazima msiba huo uvumiliwe, uonwe na hatimaye usawazishwe na kukawiza hatua hizo bila sababu nzuri kwa kumlevya kabisa [mtu] huyo kwa madawa kwaweza kurefusha au kupotosha kawaida hiyo.” Kitulizo cha kudumu kitakuja kupitia njia ya kutafakari juu ya makusudi matukufu ya Yehova.—Zaburi 1:2; 119:97.

      Rudia ratiba ya kawaida: Huenda ukahitaji kujilazimisha mwanzoni kwenda kazini, kwenda kununua vitu dukani, au kushughulika na madaraka mengine. Lakini huenda ukaona kwamba muundo wa ratiba yako ya kawaida utakunufaisha sana. Uwe mwenye shughuli katika utendaji wa Kikristo.—Linganisha 1 Wakorintho 15:58.

      Usiogope kuacha kuhuzunika sana: Ingawa huenda ikaonekana kuwa jambo la ajabu, wengine waliofiwa huogopa kuacha kuhuzunika sana, wakiamini kwamba hiyo huenda ikaonyesha kwamba kumpenda kwao yule mfu kunapungua. Sivyo hata kidogo. Kuacha kuwa na umivu hufungulia njia kumbukumbu zenye kuhaziniwa ambazo bila shaka utaendelea kuwa nazo sikuzote.—Mhubiri 3:1, 4.

      Usihangaike bila sababu nzuri: Huenda ukajipata ukihangaika hivi, ‘Hali yangu itakuwaje sasa?’ Biblia hushauri tushughulikie siku moja-moja. “Kushughulikia siku moja-moja hunisaidia kwelikweli,” aeleza mjane mmoja. Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Msihangaike wakati wowote juu ya siku ifuatayo, kwa maana siku ifuatayo itakuwa na mahangaiko yayo yenyewe.”—Mathayo 6:25-34, NW.

      [Picha katika ukurasa wa 15]

      Vielelezo vya Biblia huonyesha kwamba kuandika hisia zako kwaweza kukusaidia uonyeshe huzuni yako

      [Picha katika ukurasa wa 16]

      Katika kila utamaduni, watu wanaohuzunika huthamini kupokea faraja

  • Wengine Waweza Kusaidiaje?
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • Wengine Waweza Kusaidiaje?

      “IKIWA kuna lolote niwezalo kufanya, nijulishe tu.” Hivyo ndivyo wengi wetu humwambia rafiki au mtu wa ukoo aliyefiwa karibuni. Oh, twamaanisha hivyo kwa moyo mweupe. Tungefanya jambo lolote ili kusaidia. Lakini je, huyo aliyefiwa hutuita na kusema: “Nimefikiria lile uwezalo kufanya ili kunisaidia”? Kwa kawaida sivyo. Kwa wazi, huenda tukahitaji kuchukua hatua fulani ya kwanza ikiwa kwa kweli tutamsaidia na kumfariji mtu anayehuzunika.

      Mithali moja ya Biblia husema hivi: “Neno linenwalo wakati wa kufaa. Ni kama machungwa katika vyano vya fedha.” (Mithali 15:23; 25:11) Kuna hekima katika kujua la kusema na lisilopasa kusemwa, la kufanya na lisilopasa kufanywa. Hapa pana madokezo machache ya Kimaandiko ambayo baadhi ya wale waliofiwa wameona kuwa yenye msaada.

      La Kufanya . . .

      Sikiliza: Uwe “mwepesi sana juu ya kusikia,” husema Yakobo 1:19, NW. Mojapo mambo yenye kusaidia zaidi uwezalo kufanya ni kushiriki umivu la yule aliyefiwa kwa kusikiliza. Wengine waliofiwa huenda wakahitaji kuongea juu ya mpendwa wao ambaye amekufa, juu ya aksidenti au ugonjwa uliosababisha kifo hicho, au juu ya hisia zao tangu kifo hicho kitokee. Kwa hiyo uliza hivi: “Je! ungependa kuongea juu yalo?” Acha wao waamue. Akikumbuka wakati baba yake alipokufa, kijana mmoja alisema hivi: “Ilinisaidia sana wakati wengine walipouliza lile lililotukia kisha wakasikiliza kwelikweli.” Sikiliza kwa saburi na kwa kusikitikia bila ya kuhitaji kuhisi kwamba ni lazima uandae majibu au masuluhisho. Waruhusu waeleze lolote lile watakalo kushiriki.

      Andaa kitia-moyo: Wahakikishie kwamba walifanya yote yaliyowezekana (au lolote jingine ujualo kuwa kweli na hakika). Watie moyo wajue kwamba lile wanalohisi—huzuni, kasirani, hatia, au hisiamoyo nyingine—ni jambo la kawaida tu. Waambie juu ya wengine uwajuao waliopata nafuu kwa mafanikio kutokana na hasara iyo hiyo. “Maneno [hayo] yapendezayo” ni “afya mifupani,” yasema Mithali 16:24.—1 Wathesalonike 5:11, 14, NW.

      Uwe mwenye kupatikana: Jifanye mwenyewe kupatikana, si kwa zile siku chache za kwanza tu wakati marafiki na watu wa ukoo wengi wapo, bali hata miezi kadhaa baadaye wakati wengine wamerudia kawaida yao ya maisha. Kwa njia hiyo unakuwa ‘rafiki wa kweli,’ yule anayekuwapo pamoja na rafiki wakati wa “taabu.” (Mithali 17:17) “Rafiki zetu walihakikisha kwamba jioni zetu zilikuwa na shughuli nyingi sana hivi kwamba hatukuhitaji kutumia wakati mwingi mno tukiwa nyumbani peke yetu,” aeleza Teresea, ambaye mtoto wake alikufa katika aksidenti ya gari. “Hilo lilitusaidia tushughulike vya kufaa na ile hisia ya utupu tuliyokuwa nayo.” Kwa miaka kadhaa baadaye, tarehe za matukio fulani zinapokuja kila mwaka, kama vile tarehe ya harusi au tarehe ya kifo, huo waweza kuwa wakati wenye mkazo kwa wale wanaobaki. Kwa nini usitie alama tarehe hizo kwenye kalenda yako ili zinapofika, waweza kujifanya mwenyewe kupatikana, ikiwa lazima, ili kutoa utegemezo wenye kusikitikia?

      Chukua hatua ya kwanza ifaayo: Je! kuna kazi ndogo-ndogo zinazohitaji kushughulikiwa? Je! mtu anahitajika kuwatunza watoto? Je! marafiki na watu wa ukoo wanaotembelea wanahitaji mahali pa kukaa? Mara nyingi watu waliofiwa karibuni huwa wameduwaa sana hivi kwamba hawajui hata lile wahitajilo kufanya, achia mbali kuwaambia wengine jinsi wawezavyo kusaidia. Kwa hiyo ukitambua uhitaji wa kweli, usingoje kuulizwa; chukua hatua ya kwanza. (1 Wakorintho 10:24; linganisha 1 Yohana 3:17, 18.) Mwanamke mmoja aliyekuwa amefiwa na mume wake alikumbuka hivi: “Wengi walisema, ‘Ikiwa kuna lolote niwezalo kufanya, nijulishe.’ Lakini rafiki mmoja hakuuliza. Yeye aliingia moja kwa moja katika chumba cha kulala, akaondoa shuka zote za kitanda zilizokuwa zimechafuka kutokana na kifo chake, na kuzifua. Mwingine alichukua ndoo, maji, na sabuni akasafisha mkeka mdogo ambao mume wake alikuwa ametapikia. Majuma machache baadaye, mmoja wa wazee wa kutaniko alikuja akiwa amevaa mavazi ya kufanyia kazi na pia akiwa na vyombo vyake vya kufanyia kazi akasema hivi, ‘Najua kuna kitu fulani kinachohitaji kurekebishwa. Ni kitu gani?’ Huyo mwanamume ni mpendwa kama nini moyoni mwangu kwa kurekebisha mlango uliokuwa umeng’oka kwenye bawaba moja na kurekebisha chombo fulani kitumiacho umeme!”—Linganisha Yakobo 1:27, NW.

      Uwe mkaribishaji-wageni: “Msisahau ukaribishaji-wageni,” Biblia hutukumbusha. (Waebrania 13:2, NW) Twapaswa hasa kukumbuka kuwa wakaribishaji-wageni kwa wale wanaohuzunika. Badala ya mwaliko wa “kuja wakati wowote,” weka tarehe na wakati fulani. Wakikataa, usikate tamaa kwa urahisi mno. Kitia-moyo chenye uanana huenda kikahitajika. Labda walikataa mwaliko wako kwa sababu waliogopa kupoteza udhibiti wa hisiamoyo zao mbele ya wengine. Au huenda wakahisi kuwa wenye hatia juu ya kufurahia mlo na ushirika kwa wakati huu. Kumbuka yule mwanamke mkaribishaji-wageni Lidia atajwaye katika Biblia. Baada ya kualikwa nyumbani mwake, Luka asema, “Naye akatushurutisha kwelikweli tuje.”—Matendo 16:15, NW.

      Uwe mwenye saburi na mwenye uelewevu: Usishangazwe mno na yale ambayo waliofiwa huenda wakasema mwanzoni. Kumbuka, huenda wakawa wanahisi kasirani na kuwa wenye hatia. Ikiwa mishindo ya kihisiamoyo imeelekezwa kwako, huenda ufahamu wenye kina na saburi zikahitajika kwa upande wako ili usiitikie kwa njia ya kuudhika. “Jivikeni wenyewe shauku zenye wororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu,” Biblia hupendekeza.—Wakolosai 3:12, 13, NW.

      Andika barua: Mara nyingi jambo linalopuuzwa ni thamani ya barua ya kutoa rambirambi au kadi ya kusikitikia. Faida yavyo ni nini? Cindy, aliyefiwa na mama yake kwa sababu ya kansa, ajibu hivi: “Rafiki mmoja aliniandikia barua nzuri. Hilo lilinisaidia kwelikweli kwa sababu niliweza kuisoma tena na tena.” Barua au kadi ya jinsi hiyo yenye kitia-moyo yaweza kutungwa “kwa maneno machache,” lakini yapaswa ionyeshe yaliyomo moyoni mwako. (Waebrania 13:22, NW) Yaweza kusema kwamba wajali na kwamba washiriki kumbukumbu ya pekee juu ya yule mfu, au yaweza kuonyesha jinsi maisha yako yalivyoguswa na yule mtu aliyekufa.

      Sali pamoja nao: Usipunguze umaana wa thamani ya sala zako pamoja na kwa ajili ya wale waliofiwa. Biblia husema hivi: “Dua ya mtu mwadilifu . . . ina kani nyingi.” (Yakobo 5:16, NW) Kwa kielelezo, kukusikia ukisali kwa ajili yao kwaweza kuondosha hisia zisizofaa kama vile hatia.—Linganisha Yakobo 5:13-15.

      Lisilopasa Kufanywa . . .

      Usikae mbali nao kwa sababu hujui la kusema au la kufanya: ‘Nina hakika wanahitaji kuwa pekee yao kwa sasa,’ huenda tukajiambia. Lakini labda ukweli ni kwamba tunakaa mbali nao kwa sababu tunaogopa kusema au kufanya jambo lisilofaa. Hata hivyo, kuepukwa na marafiki, watu wa ukoo, au waamini wenzake huenda tu kukamfanya yule aliyefiwa ahisi upweke mwingi zaidi, na kuongeza umivu. Kumbuka kwamba mara nyingi, maneno na vitendo vyenye fadhili zaidi ni vile vilivyo sahili zaidi. (Waefeso 4:32) Kuwapo kwako pekee kwaweza kuwa chanzo cha kitia-moyo. (Linganisha Matendo 28:15.) Akikumbuka ile siku binti yake alipokufa, Teresea asema: “Katika muda wa saa moja, ukumbi wa hospitali ulikuwa umejaa marafiki zetu; wazee wote na wake zao walikuwako. Baadhi ya wanawake walikuwa na vile vijidude vya kukunjia nywele kichwani pao, wengine walikuwa na mavazi yao ya kufanyia kazi. Waliacha tu kila kitu wakaja. Wengi wao walituambia kwamba hawakujua la kusema, lakini hiyo haikuwa kitu kwa sababu kitu tu ni kwamba walikuwapo.”

      Usiwakaze waache kuhuzunika: ‘Basi, basi, sasa, usilie,’ huenda tukataka kusema. Lakini huenda ikafaa zaidi kuruhusu machozi yatiririke. “Nafikiri ni jambo la maana kuruhusu waliofiwa waonyeshe hisiamoyo zao na kuziondosha kabisa,” asema Katherine, akikumbuka kifo cha mume wake. Kinza mwelekeo wa kuwaambia wengine jinsi wapaswavyo kuhisi. Na usidhani kwamba ni lazima ufiche hisia zako ili kulinda zao. Badala ya hivyo, “toeni machozi pamoja na watu watoao machozi,” Biblia hupendekeza.—Warumi 12:15, NW.

      Usiwe mwepesi wa kuwashauri waondolee mbali mavazi au vitu vingine vya kibinafsi vya yule mfu kabla hawajawa tayari: Huenda tukahisi kwamba ingefaa zaidi kwao kuondolea mbali vitu vyenye kuchochea kumbukumbu kwa sababu hivyo vitu hurefusha huzuni kwa njia fulani. Lakini usemi “Kisichoonekana hakifikiriwi” huenda usihusike hapa. Huenda mtu aliyefiwa akahitaji kumwacha yule mfu kwa njia ya polepole. Kumbuka simulizi la Biblia kuhusu itikio la mzee wa ukoo Yakobo alipofanywa aamini kwamba mwana wake mchanga Yusufu alikuwa ameuawa na hayawani-mwitu. Baada ya Yakobo kuonyeshwa vazi refu la Yusufu lenye mawaa ya damu, yeye ‘alimlilia mwanawe siku nyingi. Wanawe wote, na binti zake wote, wakaondoka wamtulize, lakini akakataa kutulizwa.’—Mwanzo 37:31-35.

      Usiseme, ‘Waweza kuzaa mtoto mwingine’: “Nilichukia kuambiwa na watu kwamba ningeweza kuzaa mtoto mwingine,” akumbuka mama mmoja aliyefiwa na mtoto. Huenda wakawa na madhumuni mazuri, lakini kwa mzazi anayehuzunika, maneno yaonyeshayo kwamba mtoto mwingine aweza kuwa mahali pa mtoto aliyekufa yaweza ‘kuchoma kama upanga.’ (Mithali 12:18) Mtoto mmoja hawezi kamwe kuwa mahali pa mtoto mwingine. Kwa nini? Kwa sababu kila mmoja ni wa aina yake.

      Usiepuke kwa lazima kumtaja yule aliyekufa: “Watu wengi hawakuwa wakitaja hata jina la mwana wangu Jimmy wala kuongea juu yake,” akumbuka mama mmoja. “Ni lazima nikiri kwamba nilihisi kuumia kidogo wengine walipofanya hivyo.” Kwa hiyo usibadili habari kwa lazima wakati jina la mfu linapotajwa. Muulize mtu huyo kama ahitaji kuongea juu ya mpendwa wake. (Linganisha Ayubu 1:18, 19 na 10:1.) Watu wengine waliofiwa wanathamini kusikia marafiki wakisema juu ya sifa za pekee zilizompendekeza yule aliyekufa kwao.—Linganisha Matendo 9:36-39.

      Usiwe mwepesi sana kusema, ‘Ilifaa iwe hivyo’: Kujaribu kupata jambo fulani la hakika kuhusu kifo hicho ‘hakuliwazi sikuzote nafsi zilizoshuka moyo’ zinazohuzunika. (1 Wathesalonike 5:14, NW) Akikumbuka wakati mama yake alipokufa, mwanamke mmoja mchanga alisema: “Wengine walikuwa wakisema, ‘Yeye hateseki’ au, ‘Angalau ana amani.’ Lakini sikutaka kusikia hivyo.” Maelezo ya jinsi hiyo yaweza kudokeza kwa wale wanaobaki kwamba hawapaswi kuhisi huzuni au kwamba hasara haikuwa kubwa sana. Hata hivyo, huenda wakawa wanahisi huzuni sana kwa sababu wanamkosa sana mpendwa wao.

      Huenda ikawa bora zaidi kutosema, ‘Najua uhisivyo’: Je! wajua kwelikweli? Kwa kielelezo, waweza kwa kweli kujua jinsi mzazi ahisivyo wakati mtoto anapokufa ikiwa hujapatwa na hasara hiyo mwenyewe? Na hata kama umepatwa nayo, ng’amua kwamba huenda wengine wasihisi sawasawa na vile ulivyohisi. (Linganisha Maombolezo 1:12.) Kwa upande mwingine, ikionekana yafaa, huenda kukawa na manufaa ya kusema jinsi ulivyopata nafuu kutokana na kifo cha mpendwa wako. Mwanamke mmoja ambaye binti yake alikuwa ameuawa aliona yatia moyo wakati mama wa msichana mwingine aliyekuwa amekufa alipoongea juu ya kurudia kwake maisha ya kawaida. Yeye alisema: “Mama wa huyo msichana mfu hakuanza simulizi lake kwa [kusema] ‘Najua uhisivyo.’ Aliniambia tu jinsi mambo yalivyokuwa kwake akaniacha nijihusianishe nayo.”

      Kumsaidia mtu aliyefiwa kwataka huruma, ufahamu, na upendo mwingi kwa upande wako. Usimngojee yule aliyefiwa aje kwako. Usiseme tu, “Ikiwa kuna lolote niwezalo kufanya . . . ” Tafuta “lolote” hilo wewe mwenyewe, na uchukue hatua ya kwanza ifaayo.

      Maswali machache yabaki: Namna gani tumaini litolewalo na Biblia juu ya ufufuo? Hilo laweza kumaanisha nini kwako na kwa mpendwa wako aliyekufa? Twaweza kuwaje na uhakika kwamba tumaini hilo ni lenye kutegemeka?

      [Sanduku katika ukurasa wa 24]

      Maswali ya Kufikiriwa Sana

      Kwa nini kushiriki umivu la yule aliyefiwa kwa kusikiliza kunasaidia?

      Ni nini baadhi ya mambo tuwezayo kufanya ili kumfariji mtu anayehuzunika?

      Twapaswa kuepuka kusema au kufanya nini kwa mtu fulani anayeomboleza?

      [Sanduku katika ukurasa wa 25]

      Kusaidia Watoto Washughulike na Kifo

      Mara nyingi kifo kipatapo familia, wazazi pamoja na watu wa ukoo na marafiki huwa hawajui la kusema wala la kufanya ili kuwasaidia watoto washughulike vya kufaa na jambo ambalo limetukia. Hata hivyo, watoto wanahitaji watu wazima wawasaidie washughulike na kifo. Fikiria baadhi ya maswali ambayo huulizwa kwa kawaida juu ya kuwasaidia watoto waelewe kifo.

      Utawaelezaje watoto maana ya kifo? Ni jambo la maana kueleza mambo kwa maneno sahili. Pia eleza mambo yenye ukweli. Usisite kutumia maneno halisi, kama vile “kufa” na “kifo.” Kwa kielelezo, waweza kuketi na mtoto, umchukue mikononi mwako, na kusema: “Jambo la kuhuzunisha sana, sana, limetukia. Baba alipatwa na ugonjwa mbaya sana ambao watu wengi hawapatwi nao [au lolote lile ujualo kuwa ni kweli], naye akafa. Hakufa kwa sababu ya kosa la mtu yeyote. Tutamkosa sana kwa sababu tulimpenda, naye alitupenda sisi.” Hata hivyo, huenda ikasaidia kueleza kwamba haielekei kwamba mtoto huyo au mzazi anayebaki atakufa kwa sababu tu yeye huwa mgonjwa nyakati nyingine.

      Watie moyo waulize maswali. ‘Kifo ni nini?’ huenda wakauliza. Waweza kujibu hivi: “‘Kufa’ kwamaanisha kwamba mwili umekoma kufanya kazi na hauwezi kufanya yoyote ya mambo uliyokuwa ukifanya—hauwezi kuongea, kuona, au kusikia, na hauwezi kuhisi lolote.” Mzazi aaminiye ahadi ya Biblia juu ya ufufuo aweza kutumia fursa hii kueleza kwamba Yehova Mungu anamkumbuka yule aliyekufa na aweza kumrudisha kwenye uhai katika Paradiso ya kidunia ya wakati ujao. (Luka 23:43; Yohana 5:28, 29)—Ona sehemu “Tumaini Hakika kwa Wafu.”

      Je! kuna lolote ambalo hupaswi kusema? Haisaidii kusema kwamba yule mfu amesafiri mbali sana. Hofu ya kuachwa ni hangaiko kubwa la mtoto, hasa wakati mzazi amekufa. Kuambiwa kwamba yule mfu amesafiri huenda tu kukaimarisha hisia ya mtoto ya kuachwa na huenda akasababu hivi: ‘Nyanya aliondoka, naye hata hakutuaga!’ Uwe mwangalifu na watoto wachanga pia, kuhusu kusema kwamba yule aliyekufa ameenda kulala usingizi. Watoto huelekea kuelewa mambo kihalisi sana. Mtoto akilinganisha kulala usingizi na kufa, tokeo laweza kuwa atahofu kwenda kitandani usiku.

      Je! watoto wahudhurie maziko? Wazazi wanapaswa wafikirie hisia za watoto. Ikiwa hawataki kwenda, msiwalazimishe au kuwafanya kwa njia yoyote wahisi wana hatia kwa sababu ya kutokwenda. Ikiwa wanataka kwenda, wasimulie yale yote yatakayotukia, kutia na kama kutakuwa na jeneza (sanduku) na kama litakuwa wazi au litakuwa limefungwa. Eleza pia, kwamba huenda wakaona watu wengi wakilia kwa sababu wana huzuni. Tena, waruhusu waulize maswali. Na watie moyo kwamba wanaweza kuondoka ikiwa wanahitaji kufanya hivyo.

      Watoto huitikiaje kifo? Mara nyingi watoto huhisi kwamba wao ndio wa kulaumiwa juu ya kifo cha mpendwa. Kwa sababu huenda ikawa wakati mmoja au mwingine mtoto alihisi kasirani kuelekea yule aliyekufa, mtoto huyo aweza kuja kuamini kwamba mawazo au maneno ya kasirani ndiyo yaliyosababisha kifo hicho. Huenda ukahitaji kutoa faraja hivi: ‘Mawazo na maneno yako hayafanyi watu wawe wagonjwa, nayo hayafanyi watu wafe.’ Huenda mtoto mchanga akahitaji kutiwa moyo hivyo mara kwa mara.

      Je! uwafiche watoto huzuni yako? Kulia mbele ya watoto ni jambo la kawaida na lenye afya pia. Mbali na hilo, ni vigumu sana kuwaficha watoto hisia zako kabisa; wao huelekea kuwa wenye kufahamu sana na mara nyingi wanaweza kuhisi kwamba mambo si mazuri. Kuonyesha huzuni yako wazi huwajulisha kwamba kuhuzunika na kuonyesha hisia zako nyakati nyingine ni jambo la kawaida.

      [Picha katika ukurasa wa 21]

      Ukitambua uhitaji wa kweli, usingojee kuulizwa—chukua hatua ya kwanza ifaayo

      [Picha katika ukurasa wa 23]

      Kuwapo kwako hospitalini kwaweza kuwatia moyo waliofiwa

  • Tumaini Hakika kwa Wafu
    Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa
    • [Picha katika ukurasa wa 26]

      [Picha katika ukurasa wa 31]

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki