Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ni Nini Huwafanya Watu Wavutiwe na Uchawi?
    Amkeni!—2011 | Februari
    • Ni Nini Huwafanya Watu Wavutiwe na Uchawi?

      HUENDA jibu la swali hilo likategemea kwa kiasi kikubwa mahali mtu anapoishi, na pia imani yake ya kidini pamoja na malezi. Ni nini huwafanya watu katika eneo lenu wavutiwe na uchawi? Huenda wakavutiwa na moja ya sababu zifuatazo.

      ● Udadisi Wanadamu wamezaliwa wakiwa wadadisi, na uchawi ni moja kati ya mambo yanayochochea udadisi wao. Kwa hiyo, watu fulani wangependa kujua ikiwa kuna nguvu iliyofichika inayoongoza uchawi. Wengine huwaendea wachawi ili wajue ni nani wanaowaloga na wengine husimama barabarani kuwatazama watu wanaofanya miujiza. Huenda hata wengine wakahudhuria mkutano wa kuwasiliana na pepo.

      ● Burudani Katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na ongezeko la ghafula katika burudani—vitabu, sinema, na michezo ya kompyuta—kuhusu uchawi na ushirikina wa dini za kipagani za kale. Pia, baadhi ya burudani hizo huonyesha jeuri na ngono waziwazi.

      ● Mahangaiko kuhusu wakati ujao Biblia ilitabiri hivi: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Kwa kweli tunaishi katika siku za mwisho, na watu wengi wanawatembelea watu wanaofanya mambo ya uchawi—kama vile, viongozi wa kidini wanaodai kuzungumza na Mungu na wachawi wanaodai kuwa wanaweza kufanya uaguzi—ili kupata mwongozo. Mtu fulani ambaye husoma akili za watu alisema: “Hii ni moja kati ya biashara chache ambazo haziathiriwi na kuporomoka kwa uchumi. Kwa kawaida watu hawaji kukuona wanapokuwa na furaha.” Mbashiri mmoja huko Kanada alisema: “Siku hizi mimi hupigiwa simu na wafanyabiashara mashuhuri ambao hupendelea kuzungumza kupitia simu zao za kibinafsi kazini au kupitia simu zao za mkononi nao hunong’oneza wanapozungumza wakiwa nje ya ofisi zao.” Pia aliongeza hivi: “Hawa ni watu ambao, awali walikuwa na shaka kuhusu kumwendea mtu anayesoma akili za watu.”

      ● Magonjwa Mara nyingi katika nchi fulani wagonjwa wengi wanaougua sana huacha matibabu ya hospitali na kutafuta msaada kutoka kwa waganga wa kienyeji wanaotumia uchawi. Huenda wakaambiwa kuwa wao ni wagonjwa kwa sababu wamelogwa. Ili kumsaidia mtu aliyelogwa, huenda marafiki au watu wa familia wakatafuta msaada kutoka kwa mchawi ambaye huenda akawaambia walipe kiasi kikubwa cha pesa.

      ● Kutafuta ulinzi na bahati njema Katika maeneo fulani ya Afrika, wanakijiji hutafuta “nabii” wa kanisa lenye uvutano mkubwa au mchawi ili afukuze roho waovu kutoka katika jamii. Desturi hizo hutia ndani kunywa michanganyiko fulani na “maji matakatifu.” Kwingineko pia watu hutumia wachawi ili kuleta bahati katika nyumba mpya au kaburi kwa kuwa inaaminiwa kwamba roho za wafu zinaweza kuwaletea bahati.

      ● Kuwalinda watoto Huko Papua New Guinea, huenda mama akakataa kutoka nje usiku akiwa na mtoto wake mchanga. Kwa nini? Anahofu kwamba huenda roho waovu wakamdhuru mtoto wake. Huko Uganda, ni kawaida kwa akina mama kuwafunga watoto wao hirizi mikononi na miguuni, ambazo wakati mwingine huwa zimetengenezwa kwa makoa na shanga, ili kuwalinda kutokana na madhara.

      ● Kifo cha mpendwa Mwandikaji Mwingereza Sir Arthur Conan Doyle aliwapoteza mwana, kaka, ndugu-mkwe, na mpwa wake wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Akiwa amehuzunika sana, Doyle pamoja na mke wake walienda kwenye mikutano ya kuwasiliana na pepo wakiwa na matumaini ya kuzungumza na mwana wao aliyekufa. Leo pia, watu wengi huwaendea watu wanaowasiliana na pepo wakiwa na matumaini ya kuzungumza na wapendwa wao waliokufa. Katika nchi fulani, dini za kienyeji pamoja na zile zinazodai kuwa za Kikristo hufundisha kwamba kifo husababishwa na roho waovu waliokasirika. Makanisa hayo hudai kwamba lazima watu wafanye matambiko fulani ambayo hugharimu pesa nyingi sana ili watu zaidi katika jamii wasife.

      ● Kuwahofu wafu Imani kuhusu kifo na wafu imewaathiri sana wanadamu. Kwa hiyo, katika nchi nyingi watu hufanya matambiko ya kila aina yanayotia ndani kuwa na karamu mwaka mmoja baada ya mtu kufa, kufagia boma lote la aliyekufa, kunyoa nywele zote, na pia kujiumiza, ili wawafurahishe wafu au “kuthibitisha” kwamba wanawapenda. Jamii fulani katika visiwa vya Pasifiki huwalazimisha wajane kuvaa mavazi meusi na kuomboleza kwa miezi mingi, wakiwa wamejifungia ndani ya nyumba na bila kula vyakula ambavyo mpendwa wao aliyekufa alipenda sana. Watu wanaojihusisha na desturi hiyo wanaweza kushuka moyo au kupata magonjwa yanayoletwa na njaa au hata kufa.

      Ni wazi kwamba kuna mambo mengi yanayowavutia watu kufanya uchawi. Hivyo, ni jambo la maana tuelewe chanzo halisi cha mafundisho kuhusu uchawi! Acheni sasa tuchunguze Biblia, kwa sababu ndicho kitabu pekee kinachoeleza wazi kuhusu uchawi.

  • Ni Nani Chanzo Halisi cha Uchawi?
    Amkeni!—2011 | Februari
    • Ni Nani Chanzo Halisi cha Uchawi?

      BIBLIA inasema hivi kumhusu Muumba wetu: “Mungu ni nuru na hakuna giza kamwe katika muungano na yeye.” (1 Yohana 1:5) Hilo ni kweli hasa kuhusu mambo ya kiroho. Kwa hiyo, je, Mungu wa kweli anaweza kuwa ndiye chanzo cha uchawi? Au je, kuna nguvu fulani ya uovu inayoongoza uchawi?

      Baadhi ya mazoea ya kiuchawi ambayo watu hujihusisha sana nayo ni uaguzi na kuwasiliana na pepo kutia ndani unajimu, ubashiri wa kutumia namba, usomaji wa viganja, kuwasiliana na “wafu” na vilevile ulozi. Mazoea hayo yana historia ndefu, kwani mengi kati yake yalianzia Babiloni la kale, ambalo magofu yake yanapatikana huko Iraki. (Isaya 47:1, 12, 13) Kutoka Babiloni, mazoea ya uchawi yalienea kote katika ulimwengu wa kale na kutia mizizi katika tamaduni na jamii nyingi.

      Fikiria tukio lililotokea katika jiji la Filipi lililokuwa katika Makedonia ya kale. Kikundi kidogo cha wahudumu Wakristo, kilichotia ndani mtume Paulo na daktari Luka, kilikutana na msichana aliyekuwa na nguvu za kufanya uchawi. Ona jinsi Luka, mwandikaji wa Biblia, alivyofunua chanzo cha nguvu hizo. Aliandika hivi: “Kijakazi fulani mwenye roho, roho mwovu wa uaguzi, akakutana nasi. Yeye alikuwa akiwapatia mabwana zake faida nyingi kwa kufanya ufundi wa kubashiri.”—Matendo 16:16-18.

      Naam, msichana huyo hakupata nguvu hizo kutoka kwa Mungu wa kweli, Yehova, bali kutoka kwa roho mwovu. Hiyo ndiyo sababu Paulo pamoja na waandamani wake walikataa kumsikiliza. Huenda unajiuliza hivi: ‘Roho waovu ni nani? Nao walitoka wapi?’ Hebu ona majibu ya Biblia.

      Roho Waovu Ni Nani?

      Mapema kabla ya kuwaumba wanadamu, Yehova aliumba ‘wana wa Mungu’ wa roho huko mbinguni, wenye akili na walio wengi sana. (Ayubu 38:4, 7) Kama wanadamu, wao pia wana uhuru wa kuchagua, na kwa muda mrefu walikuwa washikamanifu kwa Mungu. Lakini kwa ghafula hali hiyo ya furaha ilikatizwa. Jinsi gani?

      Baada ya Mungu kuwaumba wanadamu, kiumbe mmoja wa roho alianza kutamani kitu ambacho hakikuwa chake —ibada. Kama vile mtu mwenye ustadi anavyoweza kufanya ionekane kana kwamba sauti inatoka katika mwanasesere, malaika huyo mwovu alitumia nyoka kumshawishi mwanamke wa kwanza, Hawa, asimtii Muumba wake. (Mwanzo 3:1-6) Biblia inamtaja malaika huyo mwasi kuwa “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani.” (Ufunuo 12:9) Yesu alimtaja kuwa “muuaji” ambaye “hakusimama imara katika kweli,” halafu akaongeza hivi: “Anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.”—Yohana 8:44.

      Baadaye, ‘wana wengine wa roho wa Mungu wa kweli’ walijiunga katika uasi huo wa Shetani. (Mwanzo 6:1, 2) Wanajulikana kama “wale malaika waliofanya dhambi” na wale “malaika ambao hawakubaki mahali pao pa kwanza bali wakayaacha makao yao wenyewe yanayofaa,” au mahali pao walipogawiwa huko mbinguni. (2 Petro 2:4; Yuda 6) Wakaja kujulikana kama roho waovu. (Yakobo 2:19) Zaidi ya hilo, wameazimia kuwaondoa watu wengi iwezekanavyo kutoka kwenye ibada ya kweli, kama vile tu walivyowafanya Waisraeli katika nyakati za Biblia. (Kumbukumbu la Torati 32:16, 17) Vivyo hivyo leo pia, kama vile ilivyokuwa nyakati zilizopita, Shetani pamoja na roho waovu hutumia ujanja kufundisha uwongo wa kidini.—2 Wakorintho 11:14, 15.

      Jilinde!

      Hata ingawa roho waovu wana nguvu zinazopita zile za wanadamu, kupitia msaada wa Mungu, tunaweza ‘kuchukua msimamo kuwapinga’ na kuwa washindi. (1 Petro 5:9) Hata hivyo, ili kupata msaada huo, tunahitaji kujifunza yale ambayo Mungu anataka tufanye na kutenda kupatana nayo. Akizungumza kuhusu Wakristo walioishi wakati wake, mtume Paulo aliandika hivi: “Sisi . . . hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba kwamba mjazwe ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na utambuzi wa kiroho, ili mtembee kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili.”—Wakolosai 1:9, 10.

      Wale ambao walipata ‘ujuzi huo sahihi’ walitia ndani watu kadhaa kutoka jiji la Efeso ambao walifanya uchawi. Ona jinsi ujuzi kuhusu kweli ulivyowasaidia. Biblia inasema hivi: “Hesabu kubwa ya wale waliozoea kufanya ufundi wa uchawi wakaleta pamoja vitabu vyao wakaviteketeza mbele ya kila mtu.” Vitabu hivyo vilikuwa na thamani ya “vipande 50,000 vya fedha,” na hizo zilikuwa pesa nyingi sana! (Matendo 19:17-19) Mfano huo wa ujasiri ulirekodiwa kwa faida yetu.—2 Timotheo 3:16.

      Kanuni Zitakazokulinda

      Kuna mambo mengine tunayoweza kufanya ambayo yatatulinda kutokana na roho waovu. Hebu chunguza kanuni za Biblia zifuatazo.

      “Msiamini kila neno lililoongozwa na roho, lakini yajaribuni maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu.” (1 Yohana 4:1) Huenda mambo fulani yanayosemwa na wanajimu, watu wanaosoma akili za watu, watu wanaowasiliana na pepo, na wachawi yakawa ya kweli. Kwa mfano, yule msichana kutoka Filipi aliyekuwa na roho mwovu, alisema ukweli aliposema hivi kumhusu Paulo na waandamani wake: “Watu hawa ni watumwa wa Mungu Aliye Juu Zaidi, wanaowatangazia ninyi njia ya wokovu.” (Matendo 16:17) Hata hivyo, Paulo na waandamani wake hawakukubali awafuate. Badala yake, Paulo aliamuru roho huyo mwovu atoke ndani yake. Chunguza mambo ambayo dini zinasema na uyalinganishe na yale ambayo Biblia inasema.—Matendo 17:11.

      “Basi, jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.” (Yakobo 4:7) Roho waovu ni adui wa Mungu na wako pia. Usijaribu hata kidogo kuwa mdadisi kuhusu mambo yao yaliyofichika. Badala yake, jitiishe kwa Mungu kwa kutii amri zake zenye upendo, ambazo si zenye kulemea. (1 Yohana 5:3) Kwa mfano, Mungu aliliambia hivi taifa la kale la Israeli: “Asipatikane ndani yako yeyote . . . anayefanya uaguzi, mwenye kufanya uchawi au yeyote anayetafuta ishara za bahati au mlozi, au anayefunga wengine kwa kuwatakia maovu au yeyote anayetafuta shauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo au mjuzi wa kubashiri matukio au yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu. Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Maoni ya Mungu hayajabadilika.—Wagalatia 5:19, 20.

      “Hakuna apizo lolote la bahati mbaya juu ya [watumishi wa Yehova].” (Hesabu 23:23) Wale wote ambao wanataka kumpendeza Mungu hawapaswi kuwaogopa roho waovu. Kwa kweli, roho hao waovu hata “hutetemeka” mbele za Mungu, kwa sababu wanajua kwamba yeye ana nguvu nyingi, ambazo atatumia kuwaharibu. (Yakobo 2:19) Mungu ataonyesha “nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye,” na ‘hatamwacha mwadilifu atikisike kamwe.’—2 Mambo ya Nyakati 16:9; Zaburi 55:22.

      “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Neno la Mungu linafundisha kwamba mtu akifa, amekufa! Hatupaswi kuwaogopa, kwa sababu hawawezi kumdhuru mtu yeyote. (Isaya 26:14) Ili wawadanganye watu, wakati mwingine roho waovu hujifanya kuwa roho za wafu, na hilo linaweza kueleza kwa nini “roho” anayewatokea ni tofauti kabisa na mtu halisi walimjua.

      “Hamwezi kuwa mkishiriki ‘meza ya Yehova’ na meza ya roho waovu.” (1 Wakorintho 10:21, 22) Wale wote wanaompenda Yehova kikweli wataepuka kabisa vitabu, sinema, na michezo ya kompyuta iliyo na mambo ya uchawi au inayochochea mazoea na imani zinazohusiana na uchawi.a Zaburi 101:3 inasema: “Sitaweka mbele ya macho yangu kitu chochote kisichofaa.” Zaidi ya hilo, mara nyingi burudani zinazohusisha uchawi hutukuza jeuri na mwenendo mpotovu, ambao ‘wale wanaompenda Yehova’ wanapaswa kukataa kabisa.—Zaburi 97:10.

      Roho waovu wamejitahidi sana kuficha utu wao kutoka kwa wanadamu. Lakini hawajafaulu kabisa kufanya hivyo. Kupitia Biblia, Yehova amefunua kabisa jinsi walivyo—waongo wabaya sana na adui hatari wa wanadamu. Wao ni tofauti sana na Muumba wetu, Yehova Mungu! Kama vile habari ifuatayo inavyoonyesha, yeye anatupenda, sikuzote yeye hutueleza ukweli, na anataka tuishi milele kwa furaha.—Yohana 3:16; 17:17.

      [Maelezo ya Chini]

      a Dhamiri za watu hutofautiana, ikitegemea malezi ya kidini na pia ukomavu wa kiroho. Jambo kuu ni kwamba kila mtu anapaswa kudumisha dhamiri safi mbele za Mungu na asisumbue dhamiri za watu wengine kutia ndani watu wa familia. Waroma 14:10, 12 linasema kwamba “sisi sote tutasimama mbele ya kiti cha hukumu cha Mungu.”

  • Chanzo cha Kweli cha Mwongozo na Tumaini
    Amkeni!—2011 | Februari
    • Chanzo cha Kweli cha Mwongozo na Tumaini

      TOFAUTI na roho waovu, Yehova Mungu ni mwenye hekima yote na nguvu zote. Pia, yeye ndiye mfano bora zaidi wa upendo. (1 Yohana 4:8) Shauri lake ni zuri wakati wote, naye hutushauri bila malipo, kwa sababu anatujali sana. Mashauri yake ni tofauti kama nini na yale ya wabashiri na watu wanaosoma akili za watu! Mungu anasema: “Haya, ninyi nyote mlio na kiu [ya kiroho]! Njooni kwenye maji. Na wale wasio na pesa! Njooni, mnunue mle. Ndiyo, njooni, mnunue divai na maziwa bila pesa na bila bei. Kwa nini mnaendelea kulipa pesa kwa ajili ya kitu ambacho si mkate, na kwa nini kazi yenu ni kwa ajili ya kitu ambacho hakishibishi? Nisikilizeni kwa makini, na mle yaliyo mema, na nafsi yenu ipate furaha tele katika unono.”—Isaya 55:1, 2.

      Kwa sababu Biblia iliandikwa chini ya mwongozo wa Muumba wetu mwenye upendo, inatupatia tumaini, ulinzi wa kiroho, kusudi maishani, na kanuni bora zaidi za kutuongoza. Hebu chunguza maswali yafuatayo pamoja na maandiko ya Biblia yaliyoonyeshwa.

      [Sanduku katika ukurasa wa 7]

      ● Ninaweza kupata amani ya kweli ya moyoni kwa njia gani? Biblia inasema hivi: “Yehova, Mkombozi wako, Mtakatifu wa Israeli, amesema hivi: ‘Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake. Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.’”—Isaya 48:17, 18.

      ● Je, uovu utaendelea milele? “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.” (Methali 2:21, 22) Ndiyo, wanadamu waovu, pamoja na malaika waovu, wataharibiwa milele, kana kwamba kwa moto.—Ufunuo 20:10, 14.

      ● Je, magonjwa na kuteseka kutaisha? “Tazama! Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani [matatizo mengi ya sasa] yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.

      Tofauti na roho waovu, Mungu hasemi uwongo kamwe. Kwa kweli ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Zaidi ya hilo, kama vile habari ya mwisho katika mfululizo huu itakavyoonyesha, kweli yake huwaweka watu huru na kuwapa uhai.—Yohana 8:32; 17:3.

  • Kweli ya Biblia Iliwaweka Huru
    Amkeni!—2011 | Februari
    • Kweli ya Biblia Iliwaweka Huru

      YESU KRISTO aliwaambia hivi watu waliokuwa wakimsikiliza: “Mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:32) Kama vile mifano ifuatayo inavyoonyesha, uhuru huo unatia ndani kuwa huru kutokana na roho waovu, ambao ndio wanasema uwongo na kuwadanganya watu wakitumia uchawi.—Yohana 8:44.

      Kila moja ya masimulizi haya inaonyesha jinsi kweli ya Biblia ina nguvu za kuweka watu huru. Naam, hiyo pekee ndiyo inayowaweka watu huru. Mbona usijichunguzie Biblia uone. Hutakatishwa tamaa.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

      Picha hizi zimeigizwa

      ● Susanna alikuwa kuhani wa kike katika dini moja huko Brazili. Alitaka kutumia nguvu zake zisizo za kawaida kuwasaidia watu wenye uhitaji. Pia, alifurahia sana “kuzungumza na mama yake aliyekuwa amekufa.” Hata hivyo, baada ya muda, “mama” yake alimsihi sana ajiue ili waishi pamoja katika ulimwengu wa roho. Jambo hilo lilimsumbua sana Susanna na hata aliota ndoto mbaya. Kisha Susanna na mume wake wakaanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Walijitahidi sana ‘kumpinga Ibilisi,’ na mwishowe ‘aliwakimbia.’ (Yakobo 4:7) Sasa wanaishi kwa amani, na Susanna haoti ndoto mbaya. Alisema, “Nina sababu nyingi sana za kumshukuru Yehova, lakini ninashukuru hata zaidi kwamba alitutoa kwenye giza la kiroho.”

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

      ● Timothy, anayeishi Afrika Magharibi, ni kiziwi na bubu.a Kwa sababu madaktari wa kawaida hawakuweza kumsaidia, aliwaendea waponyaji wa kimuujiza, lakini wao pia walishindwa. Aliandika, “Nilivunjika moyo sana kutokana na uwongo nilioambiwa.” Baadaye Timothy alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, ambao walimweleza kusudi la Mungu la kuondoa magonjwa na ulemavu wote. Timothy anasema, “Ninasubiri kwa hamu siku ambayo katika ulimwengu mpya wa Mungu ‘masikio ya viziwi yatazibuliwa . . . na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.’” (Isaya 35:1-6) Kwa sasa, yeye hufurahia kutumia mashini ndogo ya DVD kuwahubiria kweli za Biblia watu wengine walio na matatizo ya kusikia, na kuwasaidia kupata uhuru wa kweli.

      [Maelezo ya Chini]

      a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

      ● Evelyn anayeishi nchini Estonia, alikuwa amejiingiza sana katika uchawi. Kwa sababu Yesu aliwaponya watu, yeye pia alitaka kufanya hivyo. Alitaka hasa kumsaidia mama yake aliyekuwa na ugonjwa wa kudumu. Hivyo, ili atambue na kutibu magonjwa mabaya alijifunza kutumia pinduli. Baada ya muda, alianza kuchunguza Biblia. Matokeo? Alisema, “Nilitambua kwamba nilikuwa nimedanganywa sana. Kwa hiyo, niliteketeza vitabu na pinduli zangu za uchawi.” Sasa anafundisha kweli za Biblia zinazowaweka watu huru.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

      ● Mary alilelewa katika mojawapo ya visiwa vya Papua New Guinea ambako watu wanawahofu sana wafu. Iwapo mtu angekufa katika kijiji chake, Mary angelala chini ya kitanda cha mtu mwingine, kwani alihofu kuwa roho ya huyo mfu ingemsumbua akiwa peke yake. Kisha akajifunza kutoka katika Biblia kwamba wafu wamelala—kwamba wako kaburini wakisubiri kufufuliwa waishi katika Paradiso duniani. (Luka 23:43; Yohana 11:11-14) Tangu wakati huo, Mary hahofu wafu tena.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

      ● Alicia, aliyelelewa na wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova huko Marekani, alianza kusoma vitabu na kutazama sinema za kichawi. Kisha akaanza kufikiri kwa uzito kuhusu kweli za Biblia alizokuwa amejifunza. Alipotambua kwamba alikuwa akijaribu ‘kushiriki meza ya Yehova na meza ya roho waovu,’ alibadili njia zake na sasa anafurahia kuwa na dhamiri safi mbele za Mungu.—1 Wakorintho 10:21.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki