-
Uhai Wako—Kusudi Lao ni Nini?Mnara wa Mlinzi—1997 | Februari 15
-
-
Uhai Wako—Kusudi Lao ni Nini?
“Moyo wangu . . . ukiniongoza kwa hekima . . . hata niyaone yaliyo mema ya kuwafaa wanadamu . . . siku zote za maisha yao.” —MHUBIRI 2:3.
1, 2. Kwa nini hakuna ubaya katika kujipenda kwa kiasi?
WEWE wajipenda sivyo? Hilo ni jambo la kawaida. Hivyo twala kila siku, twalala usingizi tunapochoka, na twapenda kuwa pamoja na marafiki na wapendwa. Nyakati nyingine twacheza michezo, twaogelea, au kufanya mambo mengine tunayofurahia, tukionyesha hali ya kujipenda yenye usawaziko.
2 Kujipenda huko kwapatana na yale ambayo Mungu alimsukuma Solomoni kuandika: “Mwanadamu hapati jema kupita kula na kunywa, na kuiburudisha roho yake kwa mema katika kazi yake.” Kwa msingi wa mambo aliyoona, Solomoni aliongeza hivi: “Hayo nayo naliona ya kwamba hutoka mkononi mwa Mungu. Kwa maana ni nani awezaye kula au kujiburudisha kuliko mimi?”—Mhubiri 2:24, 25.
3. Ni maswali gani ya kutatanisha yanayoonwa na watu wengi kuwa yasiyojibika?
3 Hata hivyo wajua kwamba maisha hayahusishi tu kula, kunywa, kulala usingizi, na kufanya mambo fulani yaliyo mema. Twapatwa na maumivu, hali za kutamausha, na mahangaiko. Na yaonekana kuwa sisi ni wenye shughuli mno kupata kufikiria maana ya uhai wetu. Je, sivyo ilivyo na wewe? Vermont Royster, mhariri wa zamani wa jarida The Wall Street Journal, baada ya kuonyesha ujuzi na stadi za wanadamu zilizoongezeka, aliandika hivi: “Hapa pana jambo la kusisimua. Tufikiriapo mwanadamu mwenyewe, hali zake za kutatanisha, mahali pake katika ulimwengu wote mzima, hatujui mengi kuliko wakati uhai ulipoanza. Bado tunabaki na maswali juu ya sisi ni nani na kwa nini tupo hapa na ni wapi tunakoelekea.”
4. Kwa nini kila mmoja wetu apaswa kutaka kuweza kujibu maswali yanayotuhusu?
4 Ungejibuje maswali: Sisi ni nani? Ni kwa nini tupo hapa? Na twaelekea wapi? Mwezi wa Julai uliopita, Bw. Royster alikufa. Je, wadhani kwamba kufikia wakati huo alikuwa amepata majibu ya kuridhisha? Kwa kufaa zaidi, Je, kuna njia ambayo wewe waweza kuyapata? Na kuyapata kwaweza kukusaidiaje ufurahie maisha yenye furaha zaidi, yaliyo na maana zaidi? Acheni tuone.
Chanzo Kikuu cha Ufahamu Wenye Kina
5. Kwa nini twapaswa kumtegemea Mungu tunapotafuta ufahamu wenye kina katika maswali juu ya maana ya uhai?
5 Ikiwa sisi mmoja-mmoja tungejitafutia kusudi la uhai wetu, huenda tusingefanikiwa sana au hata kidogo, kama ambavyo imekuwa kwa habari ya wanaume na wanawake walio wengi, hata wale wenye elimu na uzoefu mwingi sana. Lakini hatukuachwa bila msaada. Muumba wetu ameandaa msaada. Ufikiriapo jambo hilo, je, yeye si Chanzo kikuu cha ufahamu wenye kina na hekima, akiwa wa “tangu milele hata milele” na mwenye ujuzi kamili juu ya ulimwengu wote mzima na juu ya historia? (Zaburi 90:1, 2) Aliwaumba wanadamu na ameona hali zote za binadamu, kwa hiyo yeye ndiye yule Mmoja ambaye twapaswa kumtegemea ili kupata ufahamu wenye kina, wala si wanadamu wasio wakamilifu, wakiwa na ujuzi wao na maoni yao yaliyo na mipaka.—Zaburi 14:1-3; Waroma 3:10-12.
6. (a) Muumba ameandaaje ufahamu wenye kina unaohitajiwa? (b) Solomoni anahusikaje?
6 Ingawa hatuwezi kumtarajia Muumba awasiliane nasi kibinafsi juu ya ufunuo wa maana ya uhai, yeye ameandaa chanzo cha ufahamu wenye kina—Neno lake lililopuliziwa. (Zaburi 32:8; 111:10) Kitabu cha Mhubiri ni chenye thamani hasa kwa habari hii. Mungu alimpulizia mwandikaji wacho, hivi kwamba, “hekima ya Sulemani [“Solomoni,” NW] ikapita hekima ya wana wote wa mashariki.” (1 Wafalme 3:6-12; 4:30-34) ‘Hekima ya Solomoni’ ilimvutia sana mtawala fulani wa kifalme aliyekuwa akimtembelea hivi kwamba alisema hakuwa amesimuliwa hata nusu ya habari yote na kwamba wale waliosikiliza hekima ya Solomoni wangekuwa wenye furaha kikweli.a (1 Wafalme 10:4-8) Sisi pia twaweza kupata ufahamu wenye kina na furaha kutokana na hekima ya kimungu ambayo Muumba wetu aliandaa kupitia Solomoni.
7. (a) Solomoni alifikia mkataa gani juu ya utendaji ulio mwingi chini ya mbingu? (b) Ni nini kitoacho kielezi cha makadirio ya kihalisi ya Solomoni?
7 Kitabu cha Mhubiri huonyesha hekima yenye kupewa na Mungu, iliyoathiri moyo na ubongo wa Solomoni. Kwa sababu ya kuwa na wakati, mali, na ufahamu wenye kina wa kufanya hivyo, Solomoni alichunguza ‘yote yaliyokuwa yametendeka chini ya mbingu.’ Aliona kwamba mengi yayo “[yalikuwa] ubatili na kujilisha upepo,” ambalo ni kadirio lililopuliziwa tunalopaswa kukumbuka tunapofikiria kusudi letu maishani. (Mhubiri 1:13, 14, 16) Solomoni alikuwa akisema mambo kwa unyoofu, kihalisi. Kwa kielelezo, fikiria maneno yake yapatikanayo kwenye Mhubiri 1:15, 18. Wajua kwamba katika karne zote ambazo zimepita wanadamu wamejaribu namna mbalimbali za serikali, nyakati nyingine wakijaribu kwa moyo mweupe kusuluhisha matatizo na kuboresha hali ya maisha ya watu. Lakini je, serikali zozote zimenyoosha mambo yote “yaliyo kombo” ya mfumo huu usio mkamilifu? Na huenda ukawa umeona kwamba kadiri mtu alivyo na ujuzi zaidi ndivyo ang’amuavyo vyepesi zaidi kwamba katika muda mfupi wa maisha, haiwezekani kusahihisha mambo kikamili. Ufahamu huo huwaletea wengi hali ya kutamauka, lakini si lazima iwe hivyo kwetu.
8. Ni duru zipi ambazo zimekuwako kwa muda mrefu?
8 Jambo jingine la kufikiria ni zile duru (kawaida) za kurudiarudia zinazotuathiri, kama vile kupanda na kushuka kwa jua au misogeo ya upepo na maji. Zilikuwako katika siku za Musa, Solomoni, Napoléon, na baba wazazi wa babu zetu. Nazo zaendelea. Vivyo hivyo, “kizazi huenda, kizazi huja.” (Mhubiri 1:4-7) Kutokana na maoni ya kibinadamu, mambo machache yamebadilika. Watu wa kale na wa kisasa wamekuwa na utendaji mbalimbali, matumaini, tamaa za makuu, na utimizo mbalimbali unaofanana. Hata ingawa katika njia ya kibinadamu, mtu mmoja-mmoja amejifanyia jina mashuhuri au alikuwa mwenye kutokeza katika uzuri au uwezo, mtu huyo yu wapi sasa? Amekufa na labda amesahauliwa. Maoni hayo si ya kuhuzunisha. Watu walio wengi hata hawajui majina ya wazazi wa nyanya na babu zao wala hawajui ni wapi hao walipozaliwa na kuzikwa. Waweza kuona ni kwa nini Solomoni aliona kwa uhalisi ubatili katika shughuli na jitihada za kibinadamu.—Mhubiri 1:9-11.
9. Twaweza kusaidiwaje kwa kupata ufahamu halisi wenye kina wa juu ya hali ya wanadamu?
9 Badala ya kututamausha, ufahamu huo wa kimungu wenye kina juu ya hali ya msingi ya wanadamu waweza kuwa na tokeo lenye manufaa, ukitusukuma tuepuke kupatia thamani zisizo haki miradi au ufuatiaji mbalimbali utakaotoweka na kusahauliwa upesi. Wapaswa kutusaidia tupime thamani ya yale tunayopata maishani na yale tunayojaribu kutimiza. Kwa kutoa kielezi, badala ya kuwa wenye kujinyima raha, twaweza kupata shangwe katika kula na kunywa kwa njia ya usawaziko. (Mhubiri 2:24) Na kama tutakavyoona, Solomoni afikia mkataa ulio chanya na wenye matazamio mazuri sana. Kwa ufupi, huo ni kwamba twapaswa kuthamini sana uhusiano wetu pamoja na Muumba wetu, awezaye kutusaidia kuwa na wakati ujao wenye furaha ya milele, na wenye kusudi. Solomoni alikazia hivi: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhubiri 12:13.
Kusudi la Uhai Baada ya Kufikiria Duru za Maisha
10. Solomoni aliwalinganisha wanyama na wanadamu katika njia ipi?
10 Hekima ya kimungu inayoonyeshwa katika Mhubiri yaweza kutusaidia zaidi katika kufikiria kusudi letu maishani. Jinsi gani? Kwa habari ya kwamba Solomoni alikazia kwa uhalisi kweli nyingine ambazo huenda tusizifikirie mara nyingi. Moja yahusisha ufanano kati ya wanadamu na wanyama. Yesu aliwafananisha wafuasi wake na kondoo, hata hivyo watu kwa kawaida hawafurahii kulinganishwa na wanyama. (Yohana 10:11-16) Hata hivyo Solomoni alitokeza mambo fulani ya hakika yasiyokanushika: “Mungu awajaribu [wana wa wanadamu], nao waone ya kuwa wao wenyewe wafanana na wanyama. Kwa maana linalowatukia wanadamu linawatukia wanyama; jambo moja lawatukia; anavyokufa huyu ndivyo anavyokufa huyu; . . . wala mwanadamu hana kitu cha kumpita mnyama; kwa maana yote ni ubatili. . . . Wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.”—Mhubiri 3:18-20.
11. (a) Duru halisi ya maisha ya mnyama yaweza kufafanuliwaje? (b) Wewe wahisije juu ya mchanganuo huo?
11 Ebu fikiria mnyama ambaye wapenda kumtazama, labda wibari au sungura. (Kumbukumbu la Torati 14:7; Zaburi 104:18; Mithali 30:26) Au labda huenda ukawazia kindi; kuna zaidi ya aina 300 kotekote ulimwenguni. Ni nini duru yake ya maisha? Baada ya kuzaliwa, mama yake humtunza kwa majuma kadhaa. Upesi anakuwa na manyoya na aweza kutoka kiotani. Huenda ukamwona akikimbia huku na huku akijifunza kutafuta chakula. Lakini mara nyingi aonekana kuwa anacheza tu, akifurahia ujana wake. Baada ya kukua kwa muda wa mwaka mmoja hivi, anapata mwenzi. Kisha ni lazima ajenge kiota au kitundu na kuwatunza wazao. Familia ya kindi ikipata beri, kokwa, na mbegu za kutosha, yaweza kunenepa na kuwa na wakati wa kupanua makao yayo. Lakini katika miaka michache tu, huyo mnyama azeeka na kuelekea zaidi kupatwa na aksidenti na ugonjwa. Yeye hufa akiwa na miaka ipatayo kumi. Hiyo kwa ujumla ndiyo duru ya maisha yake, kukiwa na tofauti ndogo-ndogo kati ya kindi wa aina mbalimbali.
12. (a) Kwa uhalisi, kwa nini duru ya maisha ya wanadamu wengi ni kama ile ya mnyama wa kawaida? (b) Wakati mwingine tumwonapo mnyama tuliyemfikiria, twaweza kufikiria nini?
12 Watu walio wengi wangeiona duru hiyo kuwa yamfaa mnyama, nao wasingemtazamia kindi awe na kusudi lenye maana maishani. Hata hivyo, maisha ya wanadamu wengi hayako tofauti sana na ya kindi, sivyo? Wanazaliwa na kutunzwa wakiwa watoto wachanga. Wanakula, wanakua, na kucheza wakiwa vijana. Punde si punde wanakuwa watu wazima, wanapata mwenzi, na kutafuta mahali pa kuishi na njia ya kuandaa chakula. Wakifanikiwa, wananenepa na kupanua makao yao (kiota chao) ambamo wanalea wazao. Lakini miongo ya miaka inapita upesi, nao wanazeeka. Ikiwa hawafi kimbele, huenda wakafa baada ya miaka 70 au 80 ikiwa imejawa na “taabu na ubatili.” (Zaburi 90:9, 10, 12) Wakati mwingine umwonapo kindi (au mnyama mwingine uliyemfikiria), waweza kuyafikiria mambo hayo ya hakika yenye uzito.
13. Ni tokeo gani linalothibitika kuwa kweli kwa habari ya wanyama na pia wanadamu?
13 Waweza kuona ni kwa nini Solomoni alilinganisha maisha za watu na zile za wanyama. Aliandika hivi: “Kwa kila jambo kuna majira yake, . . . wakati wa kuzaliwa, na wakati wa kufa.” Tukio hilo la mwisho, kifo, liko sawa kwa habari ya wanadamu na hayawani, “anavyokufa huyu ndivyo anavyokufa huyu.” Aliongeza hivi: “Wote hutoka katika mavumbi; na hata mavumbini hurudi tena.”—Mhubiri 3:1, 2, 19, 20.
14. Wanadamu fulani hujaribu kuibadilije duru ya maisha ya kawaida, lakini kukiwa na tokeo jipi?
14 Hatupaswi kuona kadirio hilo la kihalisi kuwa lenye kuvunja moyo. Ni kweli, watu fulani hujaribu kuibadili hali, kama vile kufanya kazi ya ziada ili kuifanya hali yao ya kimwili iwe bora kuliko ile ambayo wazazi wao walikuwa nayo. Huenda wakafuatia miaka mingi zaidi ya elimu ili kuandaa kiwango bora zaidi cha riziki, huku wakijaribu kupanua uelewevu wao juu ya maisha. Au huenda wakakazia mazoezi au taratibu za ulaji ili kupata afya bora na maisha yaliyo marefu zaidi kidogo. Na huenda jitihada hizo zikaleta manufaa fulani. Lakini ni nani awezaye kuwa na hakika kwamba jitihada hizo zitathibitika kuwa zenye mafanikio? Hata zikiwa na mafanikio, hiyo itakuwa kwa muda gani?
15. Ni kadirio gani la unyoofu juu ya maisha za watu walio wengi lililo halali?
15 Solomoni aliuliza hivi: “Kwa kuwa kuna mambo mengi yaongezayo ubatili, mwanadamu hufaidiwa nini? Kwa maana ni nani ajuaye yaliyo mema ya mwanadamu katika maisha yake, siku zote za maisha yake ya ubatili, anayoishi kama kivuli? Kwa maana ni nani awezaye kumweleza mwanadamu mambo yatakayofuata baada yake?” (Mhubiri 6:11, 12) Kwa kuwa kifo huzikomesha jitihada za mtu upesi kwa kadiri fulani, je, kwa kweli kuna faida nyingi ya kung’ang’ana ili kupata vitu vingi zaidi vya kimwili au ya kufuatia miaka mingi ya elimu kwa kusudi hasa la kupata mali nyingi zaidi? Na kwa kuwa maisha ni mafupi sana, yakipita kama kivuli, wengi huona kwamba hakuna wakati wa kutosha kuelekeza upya jitihada kwenye mradi mwingine wa kibinadamu wanapohisi wameshindwa kutimiza mradi wao; wala mtu hawezi kuwa na uhakika ni jambo gani litakalowapata watoto wake “baada yake.”
Wakati wa Kufanya Jina Jema
16. (a) Twapaswa kufanya nini ambacho wanyama hawawezi kufanya? (b) Ni kweli gani nyingine ipaswayo kuathiri kufikiri kwetu?
16 Tofauti na wanyama, sisi wanadamu tuna uwezo wa kutafakari, ‘Ni nini maana ya kuwako kwangu? Je, ni duru tu iliyowekwa imara, ikiwa na wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa?’ Kwa habari hiyo, kumbuka ile kweli ya maneno ya Solomoni juu ya mwanadamu na hayawani: ‘Wote hurudi mavumbini tena.’ Je, hilo lamaanisha kwamba kifo hukomesha kabisa kuwako kwa mtu? Biblia huonyesha kwamba wanadamu hawana nafsi isiyoweza kufa inayoendelea kuishi mbali na mwili. Wanadamu ni nafsi, na nafsi itendayo dhambi inakufa. (Ezekieli 18:4, 20, NW) Solomoni aliongezea hivi: “Walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, wala hawana ijara tena; maana kumbukumbu lao limesahauliwa. Lo lote mkono wako utakalolipata kulifanya, ulifanye kwa nguvu zako; kwa kuwa hakuna kazi, wala shauri, wala maarifa, wala hekima, huko kuzimu uendako wewe.”—Mhubiri 9:5, 10.
17. Mhubiri 7:1, 2 lapaswa kufanya tutafakari nini?
17 Kwa sababu ya jambo hilo la hakika lisiloepukika, fikiria taarifa hii: “Heri sifa njema [“jina ni bora,” NW] kuliko marhamu nzuri; na siku ya kufa kuliko siku ya kuzaliwa. Heri kuiendea nyumba ya matanga, kuliko kuiendea nyumba ya karamu. Kwa maana huo ndio mwisho wa wanadamu wote, naye aliye hai atautia moyoni mwake.” (Mhubiri 7:1, 2) Ni lazima tukubali kwamba kifo kimekuwa “mwisho wa wanadamu wote.” Hakuna binadamu ambaye ameweza kunywa kinywaji chochote cha kurefusha maisha, kula mchanganyiko wowote wa vitamini, kufuata utaratibu wowote wa ulaji, wala kushiriki katika mazoezi yoyote yanayotokeza uhai wa milele. Na kwa kawaida “kumbukumbu lao limesahauliwa” muda mfupi baada ya kifo chao. Basi kwa nini jina ‘ni bora kuliko marhamu nzuri, na siku ya kufa kuliko siku ya kuzaliwa’?
18. Kwa nini twaweza kuwa na hakika kwamba Solomoni aliamini katika ufufuo?
18 Kama ilivyoonyeshwa, Solomoni alikuwa mwenye kutaja mambo kihalisi. Alijua juu ya wazazi wake wa kale waliokufa Abrahamu, Isaka, na Yakobo, ambao kwa hakika walikuwa wamefanya jina jema pamoja na Muumba wetu. Kwa sababu ya kumjua Abrahamu vizuri, Yehova Mungu aliahidi kumbariki yeye na mbegu yake. (Mwanzo 18:18, 19; 22:17) Ndiyo, Abrahamu alikuwa na jina jema pamoja na Mungu, akawa rafiki yake. (2 Mambo ya Nyakati 20:7; Isaya 41:8; Yakobo 2:23) Abrahamu alijua kwamba uhai wake na ule wa mwana wake haukuwa sehemu tu ya duru isiyokoma kamwe ya kuzaliwa na ya kufa. Pasipo shaka kulikuwa na kusudi kubwa kuliko kuishi miaka michache tu na kufa. Walikuwa na tazamio lililohakikishiwa la kuishi tena, si kwa sababu walikuwa na nafsi isiyoweza kufa, bali kwa sababu wangefufuliwa. Abrahamu alisadikishwa kwamba “Mungu alikuwa aweza kumfufua hata kutoka kwa wafu.”—Waebrania 11:17-19.
19. Twaweza kupata ufahamu gani wenye kina kutoka kwa Ayubu kuhusu maana ya Mhubiri 7:1?
19 Huo ni ufunguo wa kuelewa jinsi ‘jina ni bora kuliko marhamu nzuri, na siku ya kufa kuliko siku ya kuzaliwa.’ Kama vile Ayubu kabla yake, Solomoni alisadikishwa kwamba Yule aliyeumba uhai wa kibinadamu aweza kuurudisha. Aweza kuwarudisha kwenye uhai wanadamu ambao wamekufa. (Ayubu 14:7-14) Ayubu mwaminifu alisema hivi: “Wewe [Yehova] ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:15) Ebu fikiria hilo! Muumba wetu ana “tamaa” ya kuwaona watumishi wake waaminifu-washikamanifu ambao wamekufa. (“Ungetaka kuona tena kazi ya mikono yako.”—The Jerusalem Bible) Kwa kutumia dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo, Muumba aweza kuwafufua wanadamu. (Yohana 3:16; Matendo 24:15) Kwa wazi, wanadamu waweza kuwa tofauti na wanyama tu wanaokufa.
20. (a) Ni wakati gani ambapo siku ya kifo ni bora kuliko siku ya kuzaliwa? (b) Ni lazima ufufuo wa Lazaro uliwaathirije watu wengi?
20 Hilo lamaanisha kwamba siku ya kifo yaweza kuwa bora kuliko siku ya kuzaliwa kwa mtu, ikiwa kufikia wakati huo mtu amesitawisha jina jema pamoja na Yehova, awezaye kuwafufua waaminifu wanaokufa. Solomoni Mkubwa Zaidi, Yesu Kristo, alithibitisha hilo. Kwa kielelezo, alimrudisha kwenye uhai yule mwanamume mwaminifu Lazaro. (Luka 11:31; Yohana 11:1-44) Kama uwezavyo kuwazia, wengi wa wale waliojionea wenyewe kurudi kwa Lazaro kwenye uhai waliathiriwa sana, wakaweka imani katika Mwana wa Mungu. (Yohana 11:45) Je, wafikiri walihisi kuwa hawana kusudi maishani, kutojua hata kidogo wao ni nani na ni wapi wanakoelekea? La hasha, waliweza kuona kwamba hawakuhitaji kuwa wanyama tu wanaozaliwa, waishi muda fulani, kisha kufa. Kusudi lao maishani lilifungamanishwa moja kwa moja na kwa ukaribu na kumjua Babaye Yesu na kufanya mapenzi Yake. Namna gani wewe? Je, mazungumzo haya yamekusaidia uone, au kuona kwa wazi zaidi, jinsi uhai wako uwezavyo na upaswavyo kuwa na kusudi halisi?
21. Ni sehemu gani ya kupata maana katika uhai wetu tunayotaka kuchunguza bado?
21 Hata hivyo, kuwa na kusudi la kweli na lenye maana katika kuishi kwamaanisha mengi kuliko kufikiria kifo na kuishi tena baadaye. Kwahusisha yale tunayofanya na maisha zetu kila siku. Solomoni alielewesha wazi jambo hilo pia katika Mhubiri, kama vile tutakavyoona katika makala ifuatayo.
-
-
“Kwa Jumla Ndiyo Impasayo Mtu”Mnara wa Mlinzi—1997 | Februari 15
-
-
“Kwa Jumla Ndiyo Impasayo Mtu”
“Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—MHUBIRI 12:13.
1, 2. Kwa nini yafaa tuchunguze wajibu wetu kwa Mungu?
“BWANA anataka nini kwako?” Nabii wa kale alizusha swali hilo. Kisha akataja mahususi yale ambayo Yehova alitaka—kudhihirisha haki, kupenda fadhili, na kutembea kwa kiasi pamoja na Mungu.—Mika 6:8.
2 Katika siku hizi za ubinafsi na hali ya kujitegemea, wengi husumbuliwa na wazo la kwamba Mungu ataka wafanye mambo fulani. Hawataki kuwa na wajibu. Lakini namna gani ule mkataa alioufikia Solomoni katika Mhubiri? “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu.”—Mhubiri 12:13.
3. Kwa nini tufikirie kwa uzito kitabu cha Mhubiri?
3 Hali zetu na maoni yetu juu ya uhai hata yawe nini, twaweza kunufaishwa sana tukichunguza mambo yaliyoongoza kwenye mkataa huo. Mfalme Solomoni, mwandikaji wa kitabu hicho kilichopuliziwa, alichunguza baadhi ya mambo yenyewe yaliyo sehemu ya maisha yetu ya kila siku. Huenda watu fulani wakakata maneno upesi kwamba kwa msingi mchanganuo wake ni wenye kuvunja moyo. Hata hivyo ulipuliziwa kimungu na waweza kutusaidia tukadirie thamani ya utendaji wetu mbalimbali na mambo tunayotanguliza, tokeo likiwa shangwe iliyoongezeka.
Kutimiza Mahangaiko Makuu ya Maisha
4. Solomoni alichunguza na kuzungumza nini katika Mhubiri?
4 Solomoni alichunguza kwa kina ‘shughuli za wana wa wanadamu.’ (NW) “Nikatia moyo wangu ili kuyatafuta yote yanayotendeka chini ya mbingu.” Kwa kutumia neno “shughuli” Solomoni hakumaanisha kwa lazima kibarua, au kazi ya kuajiriwa, bali alimaanisha mambo yote ambayo wanaume na wanawake hushughulikia muda wote wa maisha zao. (Mhubiri 1:13) Ebu tuchunguze baadhi ya mahangaiko makuu, au shughuli mbalimbali, kisha tulinganishe utendaji wetu mbalimbali na mambo ambayo sisi wenyewe hutanguliza.
5. Ni nini mojawapo ya shughuli kuu za wanadamu?
5 Kwa hakika fedha ndizo kiini cha mahangaiko na utendaji mwingi wa kibinadamu. Hakuna awezaye kusema kwa haki kwamba Solomoni alikuwa na maoni ya uzembe kuelekea fedha ambayo ndiyo maoni ya matajiri fulani. Alikiri kwa utayari uhitaji wa kuwa na kiasi fulani cha fedha; kuwa na fedha za kutosha ni bora kuliko kulazimika kuishi maisha yasiyo na raha wala anasa au kuishi katika umaskini. (Mhubiri 7:11, 12) Lakini yamkini umeona kwamba fedha, pamoja na mali ambazo hizo zanunua, zaweza kuwa mradi mkuu maishani—kwa maskini na kwa matajiri vilevile.
6. Twaweza kujifunza nini juu ya fedha kutokana na mojawapo ya vielezi vya Yesu na kutokana na yale ambayo Solomoni mwenyewe aliyaona?
6 Kumbuka kielezi cha Yesu juu ya tajiri ambaye, kwa sababu ya kutoridhika kamwe, alijitahidi kujipatia mengi zaidi. Mungu alimhukumu kuwa mtu mwenye kukosa akili. Kwa nini? Kwa sababu ‘uhai wetu hautokani na vitu tulivyo navyo.’ (Luka 12:15-21) Mambo aliyoyaona Solomoni—labda yenye kuenea zaidi kuliko yale ambayo tumeyaona—yathibitisha maneno ya Yesu. Soma ufafanuzi kwenye Mhubiri 2:4-9. Kwa wakati fulani Solomoni alijishughulisha katika kujipatia mali. Alijenga makao na bustani nyingi sana. Alikuwa na uwezo wa kujipatia naye alijipatia waandamani warembo wa kike. Je, mali na mambo ambayo mali hizo zilimwezesha kufanya zilimletea uradhi wenye kina, hisi ya utimizo wa kweli, na maana maishani mwake? Alijibu hivi kwa unyoofu: “Kisha nikaziangalia kazi zote zilizofanywa kwa mikono yangu, na taabu yote niliyotaabika katika kuzitenda; na tazama, yote ni ubatili na kujilisha upepo, wala faida hakuna chini ya jua.”—Mhubiri 2:11; 4:8.
7. (a) Mambo yaliyoonwa huthibitisha nini kwa habari ya thamani ya fedha? (b) Wewe binafsi umeona nini kithibitishacho mkataa wa Solomoni?
7 Hilo ni jambo la kihalisi, kweli iliyothibitishwa katika maisha za watu wengi. Ni lazima tukiri kwamba kuwa na fedha nyingi hakusuluhishi matatizo yote. Kuwa nazo kungeweza kusuluhisha baadhi ya matatizo, kama vile kufanya iwe rahisi zaidi kujipatia chakula na nguo. Lakini mtu aweza kuvaa nguo moja tu kwa wakati mmoja na kufurahia kiasi fulani tu cha chakula na kinywaji. Na umesoma juu ya matajiri ambao maisha zao zimekumbwa na talaka, kutumia vibaya alkoholi au madawa, na uhasama wa kudumu kati ya jamaa. Tajiri mwenye mamilioni mengi ya dola J. P. Getty alisema hivi: “Si lazima fedha zihusiane na furaha. Labda zahusiana na kukosa furaha.” Kwa sababu nzuri, Solomoni aliainisha upendo wa fedha na ubatili. Linganisha jambo hilo la hakika na jambo hili ambalo Solomoni alionelea: “Usingizi wake kibarua ni mtamu, kwamba amekula kidogo, au kwamba amekula kingi; lakini kushiba kwake tajiri hakumwachi kulala usingizi.”—Mhubiri 5:10-12.
8. Kuna sababu gani ya kutokadiria umaana wa fedha kupita kiasi?
8 Fedha na mali hazileti pia hisi ya uradhi kwa habari ya wakati ujao. Ikiwa ungekuwa na fedha na mali nyingi, yawezekana kwamba ungekuwa na hangaiko la ziada juu ya namna ya kuzihami, na bado usingejua jinsi mambo yangekuwa kesho. Je, ungeweza kuzipoteza zote, pamoja na uhai wako? (Mhubiri 5:13-17; 9:11, 12) Kwa sababu hazileti uradhi, haipaswi kuwa vigumu kuona ni kwa nini uhai wetu, au shughuli zetu, zapaswa kuwa zenye umaana wa juu zaidi, udumuo zaidi kuliko fedha na mali.
Familia, Umaarufu, na Mamlaka
9. Kwa nini maisha ya familia yalitokea kwa kufaa katika uchunguzi wa Solomoni?
9 Mchanganuo wa Solomoni juu ya uhai ulihusisha jambo la kushughulikia familia kupita kiasi. Biblia hukazia maisha ya familia, kutia ndani shangwe ya kuwa na watoto na kuwalea. (Mwanzo 2:22-24; Zaburi 127:3-5; Mithali 5:15, 18-20; 6:20; Marko 10:6-9; Waefeso 5:22-33) Lakini, je, hiyo ndiyo sehemu kuu ya maisha? Yaonekana kwamba watu wengi huona hivyo, hasa tufikiriapo jinsi ambavyo tamaduni fulani hukazia ndoa, watoto na mahusiano ya familia. Hata hivyo Mhubiri 6:3 huonyesha kwamba hata kuwa na watoto mia moja si ufunguo wa kupata uradhi maishani. Ebu wazia jinsi ambavyo wazazi wengi wamejidhabihu kwa ajili ya watoto wao ili kuwapa mwanzo mzuri maishani na kufanya maisha yao yawe rahisi zaidi. Hata ingawa kujidhabihu huko ni jambo bora kama nini, kwa hakika Muumba wetu hakutaka kwamba kusudi kuu la kuwako kwetu liwe kupitisha tu uhai kwa kizazi kifuatacho, kama vile wanyama hufanya kisilika ili kuziendeleza spishi.
10. Kwa nini kukazia familia isivyostahili kwaweza kuthibitika kuwa ubatili?
10 Solomoni alitokeza kwa ufahamu mambo fulani halisi juu ya maisha ya familia. Kwa kielelezo, huenda mwanamume akakazia uangalifu kuandalia watoto na wajukuu wake. Lakini je, wao watathibitika kuwa wenye hekima? Au watatumia kwa upumbavu vitu ambavyo amejitahidi kuwakusanyia? Jambo la pili kutajwa likitokea, lingekuwa ‘ubatili na baa kuu’ kama nini!—Mhubiri 2:18-21; 1 Wafalme 12:8; 2 Mambo ya Nyakati 12:1-4, 9.
11, 12. (a) Watu fulani wamekazia uangalifu ufuatiaji upi mbalimbali maishani? (b) Kwa nini yaweza kusemwa kwamba kutafuta umashuhuri ni “kujilisha upepo”?
11 Kwa upande ule mwingine kabisa, watu wengi wameona maisha ya familia ya kawaida kuwa yenye umaana kidogo kuliko azimio lao la kuwa na umaarufu au mamlaka juu ya watu wengine. Huenda hilo likawa kosa la kawaida miongoni mwa watu wa kiume. Je, umeona mwelekeo huo katika wanashule wenzako, wafanyakazi wenzako, au majirani wako? Watu wengi hung’ang’ana sana ili wapate kujulikana, kuwa mashuhuri, au kuwa na mamlaka juu ya wengine. Lakini hilo kwa kweli ni lenye maana jinsi gani?
12 Ebu fikiria jinsi watu fulani hung’ang’ana kuwa maarufu, iwe ni kwa kiwango kidogo au kikubwa. Twaona mwelekeo huo shuleni, katika ujirani wetu, na katika vikundi mbalimbali vya kijamii. Hiyo pia ni kani ya kuchochea katika wale wanaotaka kujulikana katika ufundi mbalimbali, vitumbuizo, na siasa. Lakini je, kung’ang’ana huko si jitihada ya ubatili kwa msingi? Solomoni alikuita kwa usahihi “kujilisha upepo.” (Mhubiri 4:4) Hata ikiwa kijana alipata kuwa mashuhuri katika klabu fulani, katika timu ya michezo, au katika kikundi cha muziki—au mwanamume au mwanamke fulani alipata sifa njema katika kampuni au jumuiya fulani—ni wangapi kwa kweli wajuao juu ya umashuhuri huo? Je, watu walio wengi kwenye upande ule mwingine wa tufe (au hata wa nchi hiyohiyo) wajua kwamba mtu huyo yu hai? Au wao waendelea tu na maisha bila kujua kabisa ule umaarufu kidogo ambao mtu huyo anao? Na hayohayo yaweza kusemwa kuhusu nguvu au mamlaka yoyote ambayo mtu apata kazini, mjini, au miongoni mwa kikundi fulani.
13. (a) Mhubiri 9:4, 5 hutusaidiaje tuwe na maoni yafaayo juu ya kujitahidi kupata umashuhuri au mamlaka? (b) Twapaswa kukabili mambo gani ya hakika ikiwa uhai ndio uu huu tu? (Ona kielezi-chini.)
13 Umashuhuri au mamlaka hiyo ina tokeo gani hatimaye? Kizazi kimoja kipitapo na kingine kuja, watu mashuhuri au wenye mamlaka wanakufa na kusahauliwa. Ndivyo ilivyo kwa habari ya wajenzi, wanamuziki, na mafundi wengine, wanamapinduzi wa kijamii, na kadhalika, jinsi ilivyo kweli kwa habari ya wanasiasa walio wengi na viongozi wa kijeshi. Kati ya shughuli hizo, unajua watu wangapi hususa walioishi kati ya mwaka wa 1700 na wa 1800? Solomoni alikadiria mambo ifaavyo, akisema hivi: “Ni afadhali mbwa aliye hai kuliko simba aliyekufa; kwa sababu walio hai wanajua ya kwamba watakufa; lakini wafu hawajui neno lo lote, . . . kumbukumbu lao limesahauliwa.” (Mhubiri 9:4, 5) Na ikiwa uhai ndio uu huu tu, basi kujitahidi ili kupata umashuhuri au mamlaka ni ubatili kikweli.a
Jambo Tunalokazia Uangalifu na Wajibu Wetu
14. Kwa nini kitabu cha Mhubiri chapaswa kutusaidia kibinafsi?
14 Solomoni hakueleza juu ya utendaji mwingi, miradi, na raha mbalimbali ambazo wanadamu hukazia uangalifu maishani mwao. Hata hivyo, yale aliyoandika yanatosha. Kuchunguza kwetu hicho kitabu hakupaswi kuonekana kuwa jambo la kushusha moyo au lisilofaa, kwa kuwa tumepitia kwa uhalisi kitabu cha Biblia ambacho Yehova Mungu alipulizia kwa kusudi kwa manufaa yetu. Chaweza kusaidia kila mmoja wetu turekebishe mtazamo wetu juu ya uhai na yale mambo tunayokazia uangalifu. (Mhubiri 7:2; 2 Timotheo 3:16, 17) Ndivyo ilivyo hasa tuchunguzapo mikataa ambayo Yehova alimsaidia Solomoni afikie.
15, 16. (a) Solomoni alikuwa na maoni gani juu ya kufurahia uhai? (b) Solomoni alisema nini kwa kufaa ni cha lazima ili kufurahia uhai?
15 Jambo moja alilotokeza Solomoni kwa kurudiarudia lilikuwa kwamba watumishi wa Mungu wa kweli wapaswa kupata shangwe katika utendaji wao mbalimbali mbele Yake. “Mwanadamu hapati jema kupita kula na kunywa, na kuiburudisha roho yake kwa mema katika kazi yake. Hayo nayo naliona ya kwamba hutoka mkononi mwa Mungu.” (Mhubiri 2:24; 3:12, 13; 5:18; 8:15) Ona kwamba Solomoni hakuwa akitia moyo sherehe zenye kelele za ulevi na ulafi; wala hakupendekeza mtazamo wa ‘Acheni tule na tunywe, na kufurahi, kwa maana kesho tutakufa.’ (1 Wakorintho 15:14, 32-34) Alimaanisha kwamba twapaswa kupata ufurahio katika raha za kawaida, kama vile kula na kunywa, huku ‘tufanyapo mema maishani mwetu.’ Hilo kwa wazi lafanya maisha yetu yakaziwe kule kufanya mapenzi ya Muumba, aamuaye yaliyo mema kikweli.—Zaburi 25:8; Mhubiri 9:1; Marko 10:17, 18; Waroma 12:2.
16 Solomoni aliandika hivi: “Enenda zako, ule chakula chako kwa furaha, unywe mvinyo yako kwa moyo wa kuchangamka, kwa kuwa Mungu amekwisha kuzikubali kazi zako.” (Mhubiri 9:7-9) Ndiyo, mwanamume au mwanamke ambaye kwa kweli ana maisha mazuri na yenye utimilizo ni mwenye utendaji katika kazi ambazo Yehova hufurahia. Hilo lataka tumfikirie daima. Mtazamo huo ni tofauti kama nini na ule wa watu walio wengi, wanaoishi kwa kufuata njia ya kusababu ya kibinadamu!
17, 18. (a) Watu wengi huitikiaje uhalisi mbalimbali wa maisha? (b) Twapaswa kukumbuka tokeo gani sikuzote?
17 Ingawa dini fulani hufundisha kuhusu uhai baada ya kifo, watu wengi huamini kwamba waweza kwa kweli kuwa na hakika juu ya uhai huu tu. Huenda ukawa umewaona wakiitikia jinsi alivyofafanua Solomoni: “Kwa sababu hukumu juu ya tendo baya haitekelezwi upesi, mioyo ya wanadamu huthibitishwa ndani yao ili kutenda mabaya.” (Mhubiri 8:11) Hata wale ambao hawajihusishi katika vitendo vibaya huonyesha kwamba wanahangaikia hasa wakati uliopo, wa sasa. Hiyo ndiyo sababu moja inayofanya fedha, mali, umashuhuri, mamlaka juu ya watu wengine, familia, au upendezi mwingine mbalimbali wa jinsi hiyo uwe wenye umaana wa kupita kiasi kwao. Hata hivyo, Solomoni hakumalizia mambo hapo. Aliongezea hivi: “Ajapokuwa mwenye dhambi amefanya maovu mara mia, akazidisha siku zake; lakini hata hivyo najua hakika ya kwamba itakuwa heri [“bora,” NW] kwao wamchao [“wamhofuo,” NW] Mungu, wenye kicho mbele zake; walakini haitakuwa heri kwa mwovu, wala hatazidisha siku zake, zilizo kama kivuli, kwa sababu hana kicho mbele za Mungu.” (Mhubiri 8:12, 13) Kwa wazi, Solomoni alisadikishwa kwamba itakuwa bora kwetu ‘tukimhofu Mungu wa kweli.’ Bora jinsi gani? Twaweza kulipata jibu katika zile hali alizolinganisha. Yehova ‘aweza kuzidisha siku zetu.’
18 Wale wangali vijana wapaswa kutafakari hasa lile jambo la hakika kabisa lenye kutegemeka kwamba itakuwa bora kwao wakimhofu Mungu. Kama vile ambavyo huenda ukawa umeona kibinafsi, mpiga-mbio aliye kasi kupita wote huenda akajikwaa na kutoshinda shindano la mbio. Jeshi lenye nguvu huenda likashindwa na jingine. Mwanabiashara mwerevu huenda akajipata akiwa katika hali ya umaskini. Na hali nyingine nyingi zisizo na uhakika hufanya maisha yasiweze kutabirika hata kidogo. Lakini waweza kuwa na uhakika kamili juu ya jambo hili: Mwendo wenye hekima na wenye hakika zaidi ni kufurahia uhai huku ufanyapo mema kulingana na sheria za kiadili za Mungu na kulingana na mapenzi yake. (Mhubiri 9:11) Hilo latia ndani mtu kujifunza kutokana na Biblia mapenzi ya Mungu ni nini, kuweka wakfu maisha yake kwa Mungu, na kuwa Mkristo aliyebatizwa.—Mathayo 28:19, 20.
19. Vijana waweza kutumiaje uhai wao, lakini mwendo wenye hekima ni upi?
19 Muumba hatawalazimisha vijana wala watu wengine wafuate mwongozo wake. Wanaweza kujihusisha sana na elimu, labda hata kuwa wanafunzi wa vitabu vingi vyenye elimu ya kibinadamu muda wote wa maisha yao. Hilo hatimaye litathibitika kuwa lenye kuuchosha mwili. Au wao waweza kutembea katika njia za moyo wao wa kibinadamu usio mkamilifu au kufuata kile kinachoyavutia macho. Hilo bila shaka litaleta majonzi, na uhai utumiwavyo hivyo utathibitika kuwa wa ubatili tu hatimaye. (Mhubiri 11:9–12:12; 1 Yohana 2:15-17) Kwa hiyo Solomoni awatolea vijana ombi—ombi ambalo twapaswa kufikiria kwa uzito, hata tuwe wa umri gani: “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku zilizo mbaya, wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo.”—Mhubiri 12:1.
20. Ni nini maoni yenye usawaziko juu ya ujumbe uliomo katika Mhubiri?
20 Tufikie mkataa gani, basi? Namna gani ule mkataa alioufikia Solomoni? Aliona, au alichunguza, “kazi zote zifanywazo chini ya jua; na, tazama, mambo yote ni ubatili na kujilisha upepo.” (Mhubiri 1:14) Katika kitabu cha Mhubiri hatupati maneno ya mtu mwenye dharau au ya mtu asiyeridhika. Hayo ni sehemu ya Neno la Mungu lililopuliziwa na yastahili uchunguzi wetu.
21, 22. (a) Ni sehemu zipi za maisha alizofikiria Solomoni? (b) Alifikia mkataa upi wenye hekima? (c) Kuchunguza yaliyomo katika Mhubiri kumekuathirije?
21 Solomoni alichunguza kutaabika, kung’ang’ana, na kutamani makuu kwa kibinadamu. Alifikiria matokeo ya mwendo wa kawaida wa mambo, yale matokeo yenye kutamausha na yaliyo matupu ambayo huwapata wanadamu wengi. Alichunguza uhalisi wa kutokamilika kwa kibinadamu na kifo kinachokuwa tokeo. Alifikiria na kutia ndani ule ujuzi wenye kupewa na Mungu juu ya hali ya wafu na matazamio yoyote ya uhai wa wakati ujao. Yote hayo yalikadiriwa na mwanamume aliyekuwa na hekima iliyoongezwa na Mungu, ndiyo, mmoja wa wanadamu wenye hekima zaidi aliyepata kuishi. Kisha mkataa alioufikia ukatiwa ndani ya Maandiko Matakatifu kwa manufaa ya wote watakao uhai wenye maana kikweli. Je, hatupaswi kukubali?
22 “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu. Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.”—Mhubiri 12:13, 14.
-