Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Nyongeza
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • Ujumbe kwa Mhubiri Ambaye Hajabatizwa:

      Kuwa mhubiri wa kutaniko ambaye hajabatizwa ni pendeleo. Unastahili pongezi kwa sababu ya maendeleo ya kiroho uliyofanya. Umemjua Mungu kwa kujifunza Neno lake na kuamini ahadi zake.—Yoh. 17:3; Ebr. 11:6.

      Huenda ulishirikiana kwa njia fulani au hukuwa mwamini wa dini nyingine kabla ya kuanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Labda ulifanya mambo fulani yasiyopatana na kanuni za Biblia. Hata hivyo, sasa umeonyesha imani yako kwa kutubu, yaani, umesikitishwa sana na dhambi ulizofanya wakati uliopita na umegeuka, yaani, umekataa mwenendo usiofaa na umeazimia kufanya yaliyo sawa machoni pa Mungu.—Mdo. 3:19.

      Au huenda umeyajua maandishi matakatifu “tangu utoto mchanga.” Kwa sababu hiyo, umelindwa dhidi ya mwenendo usio wa Kikristo na dhambi nzito. (2 Tim. 3:15) Umejifunza kupambana na vishawishi kutoka kwa marafiki na vishawishi vingine vya kufanya mambo yanayomchukiza Yehova. Umeonyesha imani kwa kuunga mkono ibada ya kweli na kuwaeleza wengine mambo unayoamini. Umezoezwa huduma ya Kikristo. Sasa umeamua mwenyewe kumtumikia Yehova ukiwa mhubiri ambaye hajabatizwa.

      Vyovyote vile, iwe ulijifunza njia za Yehova tangu utotoni au ulimjua Yehova baadaye maishani, huenda sasa unafikiria kupiga hatua nyingine mbili katika maendeleo yako ya kiroho, yaani, kujiweka wakfu na kubatizwa. Unajiweka wakfu kwa Yehova kwa kusali na kumjulisha kwamba umeamua mwenyewe kumtumikia yeye peke yake milele. (Mt. 16:24) Kisha, unaonyesha kwamba umejiweka wakfu kwa kubatizwa katika maji. (Mt. 28:19, 20) Unapojiweka wakfu na kubatizwa, unakuwa mhudumu aliyewekwa rasmi wa Yehova Mungu. Hilo ni pendeleo kubwa!

      Hata hivyo, kama ulivyojifunza katika Biblia, huenda ukakabili changamoto mbalimbali. Kumbuka kwamba muda mfupi baada ya kubatizwa, ‘Yesu aliongozwa na roho kuingia nyikani ili kujaribiwa na Ibilisi.’ (Mt. 4:1) Baada ya kubatizwa na kuwa mwanafunzi wa Kristo, huenda ukapatwa na majaribu ya namna mbalimbali. (Yoh. 15:20) Unaweza kupingwa na watu wa familia. (Mt. 10:36) Huenda ukadhihakiwa na wanashule wenzako, wafanyakazi wenzako, au rafiki zako wa zamani. Sikuzote kumbuka maneno ya Yesu katika Marko 10:29, 30: “Kwa kweli ninawaambia, hakuna mtu aliyeacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara 100 sasa katika kipindi hiki—nyumba, ndugu, dada, mama, watoto, mashamba, pamoja na mateso—na katika mfumo wa mambo unaokuja, uzima wa milele.” Hivyo, endelea kujitahidi kukaa karibu na Yehova na kuishi kupatana na viwango vyake vya uadilifu.

      Ukitaka kubatizwa, mjulishe mratibu wa baraza la wazee. Wazee watatumia maswali yaliyo kwenye kurasa zinazofuata habari hii wanapozungumza nawe ili kuona ikiwa unastahili kubatizwa. Unaweza kuanza kupitia maswali haya katika funzo lako la kibinafsi la kawaida.

      Unapojitayarisha kwa ajili ya mazungumzo hayo, tenga wakati wa kusoma na kutafakari Maandiko yaliyotajwa au kunukuliwa. Unaweza kuandika maelezo yako katika kitabu hiki au mahali pengine. Unaweza kutumia maelezo hayo pamoja na kitabu hiki utakapokuwa ukizungumza na wazee. Ukishindwa kuelewa swali lolote, usisite kumwomba yule anayekufundisha Biblia au mzee yeyote akusaidie.

      Utakapokuwa ukizungumza na wazee, usihisi kwamba unahitaji kujibu maswali haya kwa kutoa maelezo marefu yenye mambo mengi. Jibu rahisi, la moja kwa moja na kwa maneno yako mwenyewe litafaa. Kwa maswali yaliyo mengi, ingefaa kurejelea andiko moja au mawili yanayoonyesha msingi wa Kimaandiko wa jibu lako.

      Ikiwa bado hujapata ujuzi wa kutosha wa mafundisho ya msingi ya Biblia, wazee watapanga upate msaada ili uweze kuyafahamu Maandiko vizuri na kuyaeleza kwa maneno yako mwenyewe ili ustahili kubatizwa wakati mwingine.

      [Taarifa kwa wazee wa kutaniko: Maagizo kuhusu mazungumzo pamoja na wale wanaotaka kubatizwa yanapatikana kwenye ukurasa wa 208-212.]

  • Sehemu ya 1: Mafundisho ya Kikristo
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • MASWALI KWA AJILI YA WALE WANAOTAKA KUBATIZWA

      Sehemu ya 1: Mafundisho ya Kikristo

      Kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova kumekusaidia kuijua kweli. Bila shaka, mambo uliyojifunza yamekusaidia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu na kukupatia tumaini la baraka na uzima wa wakati ujao katika dunia paradiso chini ya Ufalme wa Mungu. Imani yako katika Neno la Mungu imeimarishwa, na tayari umepata baraka nyingi kwa kushirikiana na kutaniko la Kikristo. Umejionea jinsi Yehova anavyoshughulika na watu wake leo.—Zek. 8:23.

      Unapojiandaa kwa ajili ya ubatizo, utafaidika kwa kupitia mafundisho ya msingi ya Kikristo pamoja na wazee wa kutaniko. (Ebr. 6:1-3) Yehova na aendelee kukubariki unapojitahidi kuendelea kumjua, na akupe thawabu aliyoahidi.—Yoh. 17:3.

      1. Kwa nini unataka kubatizwa?

      2. Yehova ni nani?

      • “Yehova ndiye Mungu wa kweli juu mbinguni na chini duniani. Hakuna mwingine.”—Kum. 4:39.

      • “Wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.”—Zab. 83:18.

      3. Kwa nini ni muhimu utumie jina binafsi la Mungu?

      • “Basi, salini hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.’”—Mt. 6:9.

      • “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.”—Rom. 10:13.

      4. Biblia inatumia baadhi ya maneno gani kumfafanua Yehova?

      • “Yehova, Muumba wa miisho ya dunia, ni Mungu kwa umilele wote.”—Isa. 40:28.

      • “Baba yetu uliye mbinguni.”—Mt. 6:9.

      • “Mungu ni upendo.”—1 Yoh. 4:8.

      5. Unaweza kumpa nini Yehova Mungu?

      • “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.”—Marko 12:30.

      • “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”—Luka 4:8.

      6. Kwa nini unataka kuwa mshikamanifu kwa Yehova?

      • “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie, ili niweze kumjibu yule anayenidhihaki.”—Met. 27:11.

      7. Unasali kwa nani, na kupitia kwa jina la nani?

      • “Kwa kweli ninawaambia, mkimwomba Baba jambo lolote, atawapa katika jina langu [Yesu].”—Yoh. 16:23.

      8. Unaweza kusali kuhusu mambo gani?

      • “Basi, salini hivi: ‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe. Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni. Utupatie leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii; na utusamehe madeni yetu, kama vile tunavyowasamehe wadeni wetu. Na usituingize katika majaribu, bali utukomboe kutoka kwa yule mwovu.’”—Mt. 6:9-13.

      • “Huu ndio uhakika tulio nao kwake, kwamba tukiomba chochote kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”—1 Yoh. 5:14.

      9. Ni nini kinachoweza kumfanya Yehova asisikilize sala ya mtu?

      • “Watamlilia Yehova awasaidie, lakini hatawajibu . . . kwa sababu ya matendo yao maovu.”—Mika 3:4.

      • “Macho ya Yehova yanawatazama waadilifu, na masikio yake yanasikiliza dua yao, lakini uso wa Yehova uko dhidi ya wale wanaotenda maovu.”—1 Pet. 3:12.

      10. Yesu Kristo ni nani?

      • “Simoni Petro akajibu: ‘Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.’” —Mt. 16:16.

      11. Kwa nini Yesu alikuja duniani?

      • “Mwana wa binadamu [alikuja], si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa uhai wake uwe fidia badala ya wengi.”—Mt. 20:28.

      • “Ni lazima pia nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu katika majiji mengine, kwa sababu nilitumwa [Yesu] kufanya hivyo.”—Luka 4:43.

      12. Unaweza kuonyeshaje kwamba unashukuru kwa dhabihu ambayo Yesu alitoa?

      • “Alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yule aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.”—2 Kor. 5:15.

      13. Yesu ana mamlaka gani?

      • “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”—Mt. 28:18.

      • “Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu kuliko kila jina lingine.”—Flp. 2:9.

      14. Je, unaamini kwamba Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova ni “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aliyewekwa rasmi na Yesu?

      • “Kwa kweli ni nani mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana wake alimweka rasmi asimamie watumishi wake wa nyumbani na kuwapa chakula chao kwa wakati unaofaa?”—Mt. 24:45.

      15. Je, roho takatifu ni mtu?

      • “Malaika akamjibu: ‘Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa hiyo yule atakayezaliwa ataitwa mtakatifu, Mwana wa Mungu.’”—Luka 1:35.

      • “Kwa hiyo, ingawa ninyi ni waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, je, Baba aliye mbinguni hatawapa hata zaidi roho takatifu wale wanaomwomba!”—Luka 11:13.

      16. Yehova ametumiaje roho yake takatifu?

      • “Kwa neno la Yehova mbingu ziliumbwa, na kwa roho ya kinywa chake kila kitu kilichomo kiliumbwa.”—Zab. 33:6.

      • “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Mdo. 1:8.

      • “Hakuna unabii wa Andiko unaotokana na fasiri yoyote ya kibinafsi. Kwa maana unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, bali wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.”—2 Pet. 1:20, 21.

      17. Ufalme wa Mungu ni nini?

      • “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa kamwe. Na ufalme huo hautakabidhiwa watu wengine wowote. Utazipondaponda na kuzikomesha falme hizi zote, nao pekee utasimama milele.”—Dan. 2:44.

      18. Ufalme wa Mungu utakunufaishaje?

      • “Atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufu. 21:4.

      19. Unajuaje kwamba Ufalme utaleta baraka zake hivi karibuni?

      • “Wanafunzi wakamkaribia faraghani, wakamuuliza: ‘Tuambie, mambo haya yatatukia lini, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?’ Yesu akawajibu: ‘. . . Taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali. Na hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.’”—Mt. 24:3, 4, 7, 14.

      • “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, waliojaa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu, wakionekana kama watu wanaomwogopa Mungu lakini wakizikana nguvu zake; nawe jiepushe nao.”—2 Tim. 3:1-5.

      20. Unaonyeshaje kwamba Ufalme ni jambo la muhimu kwako?

      • “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake.”—Mt. 6:33.

      • “Yesu akawaambia wanafunzi wake: ‘Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso na aendelee kunifuata.’”—Mt. 16:24.

      21. Shetani na roho waovu ni nani?

      • “Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi . . . Alikuwa muuaji alipoanza.”—Yoh. 8:44.

      • “Yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye.”—Ufu. 12:9.

      22. Ni mashtaka gani ambayo Shetani ametoa kumwelekea Yehova na watumishi wake?

      • “Mwanamke akamjibu nyoka: ‘Tunaweza kula matunda ya miti ya bustani. Lakini Mungu amesema hivi kuhusu matunda ya mti ulio katikati ya bustani: “Msiyale, wala msiyaguse; la sivyo mtakufa.”’ Ndipo nyoka akamwambia mwanamke: ‘Hakika hamtakufa. Kwa maana Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda ya mti huo, macho yenu yatafunguliwa nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.’”—Mwa. 3:2-5.

      • “Shetani akamjibu Yehova: ‘Ngozi kwa ngozi. Mtu atatoa kila kitu alicho nacho ili aokoe uhai wake.’”—Ayu. 2:4.

      23. Unaweza kuthibitishaje kwamba mashtaka ya Shetani ni ya uwongo?

      • ‘Mtumikie Mungu kwa moyo kamili.’—1 Nya. 28:9.

      • “Mpaka nitakapokufa, sitaukana utimilifu wangu!”—Ayu. 27:5.

      24. Kwa nini watu wanakufa?

      • “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, basi kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Rom. 5:12.

      25. Watu waliokufa wako katika hali gani?

      • “Walio hai wanajua kwamba watakufa, lakini waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.”—Mhu. 9:5.

      26. Kuna tumaini gani kwa watu waliokufa?

      • “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Mdo. 24:15.

      27. Ni watu wangapi wataenda mbinguni kutawala pamoja na Yesu?

      • “Tazama! Mwanakondoo amesimama juu ya Mlima Sayuni, na pamoja naye 144,000 walioandikwa jina lake na jina la Baba yake kwenye mapaji ya nyuso zao.”—Ufu. 14:1.

  • Sehemu ya 2: Maisha ya Kikristo
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • MASWALI KWA AJILI YA WALE WANAOTAKA KUBATIZWA

      Sehemu ya 2: Maisha ya Kikristo

      Kwa kujifunza Biblia, umepata ujuzi kuhusu yale ambayo Yehova anataka ufanye na jinsi ya kuishi kupatana na viwango vyake vya uadilifu. Ili uishi kupatana na mambo ambayo umejifunza, huenda ulihitaji kufanya mabadiliko kadhaa kuelekea mwenendo wako na mtazamo wako kuhusu maisha. Sasa, kwa kuwa umeazimia kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Yehova, unaweza kumtolea utumishi unaokubalika ukiwa mhudumu wa habari njema.

      Kuzungumzia maswali yafuatayo kutakusaidia kukazia akilini matakwa ya uadilifu ya Yehova na kukukumbusha baadhi ya mambo unayoweza kufanya ili uwe mtumishi wake anayekubalika. Habari hii itakazia umuhimu wa kufanya mambo yote ukiwa na dhamiri njema na kwa njia itakayomletea Yehova heshima.—2 Kor. 1:12; 1 Tim. 1:19; 1 Pet. 3:16, 21.

      Tangu ulipoanza kujifunza Biblia mpaka sasa, ni wazi kwamba una hamu ya kujitiisha chini ya utawala wa Yehova na kuwa sehemu ya tengenezo lake. Maswali na marejeo ya Maandiko yatakusaidia kuchunguza ikiwa unaelewa maana ya kujitiisha chini ya mpango uliowekwa na Yehova, iwe ni katika kutaniko, familia, au inapohusu siasa za mfumo huu wa mambo. Bila shaka, utathamini sana mipango iliyowekwa na Yehova ya kuwaelimisha na kuwaimarisha watu wake kiroho. Mipango hiyo inatia ndani mikutano ya kutaniko ambayo unapaswa kuendelea kuhudhuria na kushiriki kadiri hali zako zinavyokuruhusu.

      Kwa kuongezea, sehemu hii itazungumzia umuhimu wa kushiriki kwa ukawaida katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme ili kuwasaidia watu kumjua Yehova na mambo anayowafanyia wanadamu. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Mwishowe, sehemu hii itakusaidia kuona uzito wa wakfu wako kwa Yehova Mungu na ubatizo. Uwe na hakika kwamba Yehova anathamini utayari wako wenye unyoofu wa kukubali fadhili zisizostahiliwa anazokuonyesha.

      1. Ndoa ya Kikristo inapaswa kufuata kigezo gani? Ni nini msingi pekee wa talaka ya Kimaandiko?

      • “Je, hamkusoma kwamba yule aliyewaumba tangu mwanzo aliwaumba mwanamume na mwanamke na kusema: ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Basi wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe. . . . Yeyote anayemtaliki mke wake isipokuwa kwa sababu ya uasherati, na kumwoa mwingine, anafanya uzinzi.”—Mt. 19:4-6, 9.

      2. Kwa nini wale wanaoishi pamoja kama mume na mke wanapaswa kuwa wameoana kisheria? Ikiwa umeoa au kuolewa, je, una hakika kwamba ndoa yako imeandikishwa kisheria serikalini?

      • “Endelea kuwakumbusha wajitiishe na kuzitii serikali na mamlaka.”—Tito 3:1.

      • “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kisiwe na unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.”—Ebr. 13:4.

      3. Una jukumu gani katika familia?

      • “Mwanangu, sikiliza nidhamu ya baba yako, wala usiyaache mafundisho ya mama yako.”—Met. 1:8.

      • “Mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo alivyo kichwa cha kutaniko . .  Waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko.”—Efe. 5:23, 25.

      • “Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na maagizo ya Yehova.”—Efe. 6:4.

      • “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika kila jambo, kwa maana hilo humpendeza Bwana.”—Kol. 3:20.

      • “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu.”—1 Pet. 3:1.

      4. Kwa nini tunapaswa kuheshimu uhai?

      • “[Mungu] huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote. . . . Kupitia kwake tuko hai, tunatembea, na tunaishi.”—Mdo. 17:25, 28.

      5. Kwa nini hatupaswi kuua mtu yeyote, kutia ndani mtoto ambaye bado hajazaliwa?

      • ‘Wanaume wakipambana na kumuumiza mwanamke mwenye mimba na kifo kitokee, basi ni lazima mlipe uhai kwa uhai.’—Kut. 21:22, 23.

      • “Macho yako hata yaliniona nikiwa kiinitete; sehemu zake zote ziliandikwa katika kitabu chako kuhusiana na siku ambazo zingeumbwa, kabla sehemu yoyote haijakuwepo.”—Zab. 139:16.

      • “Yehova anachukia . . . mikono inayomwaga damu isiyo na hatia.”—Met. 6:16, 17.

      6. Sheria ya Mungu inasema nini kuhusu damu?

      • “[Endeleeni] kujiepusha . . . na damu, na vitu vilivyonyongwa.”—Mdo. 15:29.

      7. Kwa nini ni lazima tuwapende ndugu na dada zetu Wakristo?

      • “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda, nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.”—Yoh. 13:34, 35.

      8. Ili kuepuka kusambaza ugonjwa mbaya unaoambukiza: (a) Kwa nini mtu aliyeambukizwa hapaswi kuwakumbatia watu na kuwabusu? (b) Kwa nini hapaswi kukasirika ikiwa wengine hawatamkaribisha nyumbani kwao? (c) Kwa nini mtu ambaye huenda ameambukizwa na ugonjwa kama huo anapaswa kwenda kwa hiari kupima damu kabla ya kuanzisha uchumba? (d) Kwa nini mtu aliye na ugonjwa wa kuambukiza anapaswa kumwambia mratibu wa baraza la wazee kabla ya kubatizwa?

      • “Msiwe na deni lolote kwa mtu yeyote, isipokuwa kupendana. . . . ‘Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.’ Upendo haumfanyii uovu jirani.”—Rom. 13:8-10.

      • ‘Angalieni, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.’—Flp. 2:4.

      9. Kwa nini Yehova anatarajia tuwasamehe wengine?

      • “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari hata ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe kwa hiari, nanyi lazima mfanye vivyo hivyo.”—Kol. 3:13.

      10. Utafanya nini ikiwa ndugu anakuchongea au kukupunja?

      • “Ndugu yako akitenda dhambi, nenda ufunue kosa lake kati yako na yeye peke yenu. Akikusikiliza, umempata ndugu yako. Lakini asipokusikiliza, nenda pamoja na mtu mmoja au wawili, ili kwa ushahidi wa mashahidi wawili au watatu kila jambo lithibitishwe. Asipowasikiliza hao, liambie kutaniko. Asipolisikiliza kutaniko pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa na kama mkusanya kodi.”—Mt. 18:15-17.

      11. Yehova anahisije kuhusu dhambi zifuatazo:

      ▪ Uasherati

      ▪ Kutumia sanamu katika ibada

      ▪ Ngono kati ya watu wa jinsia moja

      ▪ Kuiba

      ▪ Kucheza kamari

      ▪ Ulevi

      • “Msipotoshwe. Waasherati, waabudu-sanamu, wazinzi, wanaume wanaofanya ngono na wanaume, wezi, watu wenye pupa, walevi, watukanaji, na wanyang’anyi hawataurithi Ufalme wa Mungu.”—1 Kor. 6:9, 10.

      12. Inapohusu uasherati, ambao unatia ndani matendo mbalimbali ya ngono nje ya ndoa, umeazimia kufanya nini?

      • “Ukimbieni uasherati!”—1 Kor. 6:18.

      13. Kwa nini tunapaswa kuepuka kutumia dawa zinazosababisha uraibu au zinazopumbaza akili kwa sababu isiyo ya matibabu?

      • “[Toeni] miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, na yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri. Na acheni kufinyangwa na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.”—Rom. 12:1, 2.

      14. Ni mazoea gani ya kuwasiliana na roho waovu ambayo Mungu anakataza?

      • “Asipatikane miongoni mwenu . . . mtu yeyote anayefanya uaguzi, mtu yeyote anayefanya uchawi, mtu yeyote anayetafuta ishara za ubashiri, mlozi, mtu yeyote anayewafunga wenzake kwa uchawi, mtu yeyote anayetafuta ushauri kutoka kwa watu wanaowasiliana na roho, mpiga ramli, au mtu yeyote anayetafuta habari kuhusu wafu.”—Kum. 18:10, 11.

      15. Mtu akitenda dhambi nzito na anataka kurudisha uhusiano mzuri na Yehova, anapaswa kufanya nini haraka iwezekanavyo?

      • “[Niliungama] dhambi yangu kwako; sikufunika kosa langu. Nilisema: ‘Nitaungama makosa yangu kwa Yehova.’”—Zab. 32:5.

      • “Je, kuna yeyote aliye mgonjwa kati yenu? Na awaite wazee wa kutaniko, nao wasali kwa ajili yake, wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamponya huyo mgonjwa, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.”—Yak. 5:14, 15.

      16. Ukijua kwamba Mkristo mwenzako amefanya dhambi nzito, unapaswa kufanya nini?

      • “Ikiwa mtu amesikia mwito wa hadharani wa kutoa ushahidi kuhusu jambo ambalo amejionea au kusikia au kujua, lakini amekataa kutoa habari, basi ametenda dhambi, naye atawajibika kwa sababu ya kosa lake.”—Law. 5:1.

      17. Tangazo likitolewa kwamba mtu fulani si Shahidi wa Yehova tena, tunapaswa kumtendea jinsi gani?

      • “[Acheni] kushirikiana na mtu yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au anayeabudu sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi, hata msile chakula pamoja na mtu wa namna hiyo.”—1 Kor. 5:11.

      • “Mtu yeyote akija kwenu naye haleti fundisho hili, msimpokee nyumbani mwenu wala kumsalimu.”—2 Yoh. 10.

      18. Kwa nini marafiki wako wa karibu wanapaswa kuwa watu wanaompenda Yehova?

      • “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wapumbavu ataumia.”—Met. 13:20.

      • “Msipotoshwe. Kushirikiana na watu wabaya huharibu tabia nzuri.”—1 Kor. 15:33.

      19. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na siasa?

      • “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi [Yesu] si sehemu ya ulimwengu.”—Yoh. 17:16.

      20. Kwa nini unapaswa kutii mamlaka za serikali?

      • “Kila mtu na ajitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa, kwa maana hakuna mamlaka isipokuwa kupitia Mungu; mamlaka zilizopo zimewekwa na Mungu katika vyeo vyao vya kadiri.”—Rom. 13:1.

      21. Ikiwa sheria fulani ya mwanadamu inapingana na sheria ya Mungu, utafanya nini?

      • “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.”—Mdo. 5:29.

      22. Ni maandiko gani yanayoweza kukusaidia kujitenga na ulimwengu unapochagua kazi ya kimwili?

      • “Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Mika 4:3.

      • “Tokeni kwake [Babiloni Mkubwa], watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya mapigo yake.”—Ufu. 18:4.

      23. Ni aina gani ya burudani na tafrija utakazochagua, na ni zipi utakazoepuka?

      • “Yehova . . . humchukia mtu yeyote anayependa ukatili.”—Zab. 11:5.

      • “Chukieni maovu; shikamaneni na mema.”—Rom. 12:9.

      • “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yanayopendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, mambo yoyote ya wema wa adili, na mambo yoyote yanayostahili sifa, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”—Flp. 4:8.

      24. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hawashirikiani na dini nyingine katika ibada?

      • “Hamwezi kuwa mkishiriki ‘meza ya Yehova’ na meza ya roho waovu.”—1 Kor. 10:21.

      • “‘Mjitenge,’ asema Yehova, ‘na mwache kugusa kitu kichafu’; ‘nami nitawakaribisha ndani.’”—2 Kor. 6:17.

      25. Ni kanuni zipi zitakazokusaidia kuamua ikiwa utasherehekea sherehe fulani au la?

      • “Walichangamana na mataifa hayo na kuzikubali njia zao. Waliendelea kuabudu sanamu zao, nazo zikawa mtego kwao.”—Zab. 106:35, 36.

      • “Waliokufa hawajui jambo lolote kamwe.”—Mhu. 9:5.

      • “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.”—Yoh. 17:16.

      • “Wakati uliopita uliwatosha kufanya mapenzi ya mataifa, mlipofanya vitendo vya mwenendo mpotovu, uchu, kunywa kupita kiasi, karamu zenye vurugu, mashindano ya kunywa, na ibada za sanamu zenye kuchukiza.”—1 Pet. 4:3.

      26. Masimulizi yaliyo katika Biblia yatakusaidiaje inapohusu kusheherekea siku ya kuzaliwa?

      • “Siku ya tatu ilikuwa sikukuu ya kuzaliwa kwa Farao, kwa hiyo aliwafanyia karamu watumishi wake wote, akamtoa gerezani msimamizi mkuu wa vinywaji na mwokaji mkuu, akawaleta mbele ya watumishi wake. Akamrudisha msimamizi mkuu wa vinywaji kwenye cheo chake . . . Lakini akamtundika mwokaji mkuu.”—Mwa. 40:20-22.

      • “Wakati wa sherehe ya sikukuu ya kuzaliwa kwa Herode, binti ya Herodia alicheza dansi na kumfurahisha sana Herode hivi kwamba akaahidi kwa kiapo kumpa chochote ambacho angeomba. Ndipo yule binti, akichochewa na mama yake, akasema: ‘Nipe kwenye sinia kichwa cha Yohana Mbatizaji.’ Basi akawatuma watu gerezani, nao wakamkata Yohana kichwa.”—Mt. 14:6-8, 10.

      27. Kwa nini ungependa kufuata mwongozo wa wazee?

      • “Watiini wale wanaoongoza kati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuwalinda ninyi kama wale watakaotoa hesabu, ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa huzuni, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.”—Ebr. 13:17.

      28. Kwa nini ni muhimu kwako na kwa familia yako kutenga wakati wa kusoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida?

      • “Anapendezwa na sheria ya Yehova, naye huisoma sheria Yake kwa sauti ya chini mchana na usiku. Atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, mti unaozaa matunda katika majira yake, na majani yake hayanyauki. Na kila jambo analofanya litafanikiwa.”—Zab. 1:2, 3.

      29. Kwa nini unapenda kuhudhuria na kushiriki katika mikutano?

      • “Nitalitangaza jina lako kwa ndugu zangu; katikati ya kutaniko nitakusifu.”—Zab. 22:22.

      • “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukutana pamoja, kama wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile ikikaribia.”—Ebr. 10:24, 25.

      30. Ni kazi gani muhimu zaidi ambayo Yesu ametupatia?

      • “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.”—Mt. 28:19, 20.

      31. Tunapotoa michango kwa ajili ya kazi ya Ufalme au kuwasaidia ndugu na dada zetu, ni mtazamo gani ambao humpendeza Yehova?

      • “Mheshimu Yehova kwa vitu vyako vyenye thamani.”—Met. 3:9.

      • “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”—2 Kor. 9:7.

      32. Wakristo wanatazamia kupatwa na hali zipi ngumu?

      • “Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa Ufalme wa mbinguni ni wao. Wenye furaha ni ninyi, watu wanapowashutumu na kuwatesa na kuwasingizia kila aina ya uovu kwa sababu yangu. Furahini na kushangilia sana, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni, kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwapo kabla yenu.”—Mt. 5:10-12.

      33. Kwa nini ni pendeleo la pekee kubatizwa ili kuwa Shahidi wa Yehova?

      • “Neno lako likawa furaha na shangwe ya moyo wangu, kwa maana nimeitwa kwa jina lako, Ee Yehova Mungu.”—Yer. 15:16.

  • Mazungumzo ya Kumalizia Pamoja na Wale Wanaotaka Kubatizwa
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • MASWALI KWA AJILI YA WALE WANAOTAKA KUBATIZWA

      Mazungumzo ya Kumalizia Pamoja na Wale Wanaotaka Kubatizwa

      Kwa kawaida, ubatizo hufanywa kwenye makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Mwishoni mwa hotuba ya ubatizo, msemaji atawaomba wale wanaotaka kubatizwa wasimame na kujibu maswali mawili yafuatayo kwa sauti inayosikika waziwazi:

      1. Je, umetubu dhambi zako, ukajiweka wakfu kwa Yehova, na kukubali njia yake ya wokovu kupitia Yesu Kristo?

      2. Je, unaelewa kwamba ubatizo wako unakutambulisha kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova anayeshirikiana na tengenezo la Yehova?

      Kujibu maswali hayo ni “tangazo la hadharani” la kwamba wale wanaotaka kubatizwa wana imani katika fidia na kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova kwa moyo wote. (Rom. 10:9, 10) Wale wanaotaka kubatizwa wanapaswa kusali na kufikiria kwa uzito maswali hayo mapema ili waweze kujibu kupatana na usadikisho wao.

      Je, umejiweka wakfu kwa Yehova kupitia sala, ukimwahidi kwamba utamwabudu yeye peke yake na kwamba jambo kuu zaidi maishani mwako litakuwa kufanya mapenzi yake?

      Je, unaamini kabisa kwamba unastahili kubatizwa kwenye kusanyiko lijalo?

      Ni mavazi gani yanayofaa wakati wa ubatizo? (1 Tim. 2:9, 10; Yoh. 15:19; Flp. 1:10)

      Tunapaswa kuvalia kwa “kiasi na utimamu wa akili” ili kuonyesha kwamba ‘tunamtumikia Mungu.’ Hivyo, wale wanaobatizwa hawapaswi kuvaa mavazi ya kuogelea yanayoonyesha sehemu za mwili au mavazi yenye maandishi au matangazo ya biashara. Wanapaswa kuvalia kwa njia nadhifu, safi, inayofaa, na inayoonyesha heshima kwa ajili ya pindi hiyo.

      Mtu anapaswa kujiendeshaje anapobatizwa? (Luka 3:21, 22)

      Wakristo leo wanapaswa kuiga jinsi Yesu alivyofanya alipobatizwa. Alitambua kwamba ubatizo ni hatua nzito, naye alionyesha hivyo kwa mtazamo na matendo yake. Kwa hiyo, eneo la ubatizo si mahali pa kufanyia utani, kucheza, kuogelea, au kufanya mambo mengine ambayo yanaweza kupunguza uzito wa pindi hiyo; wala Mkristo mpya hapaswi kusisimuka kana kwamba amepata ushindi mkubwa. Ijapokuwa ubatizo ni pindi ya shangwe, shangwe hiyo inapaswa kuonyeshwa kwa heshima.

      Kuhudhuria mikutano na kushirikiana kwa ukawaida na kutaniko kutakusaidiaje kutimiza wakfu wako kwa Yehova?

      Baada ya kubatizwa, kwa nini ni muhimu kudumisha ratiba nzuri ya kujifunza kibinafsi na kushiriki kwa ukawaida katika huduma?

      MAAGIZO KWA WAZEE WA KUTANIKO

      Mhubiri ambaye hajabatizwa anaposema kwamba anataka kubatizwa, anapaswa kutiwa moyo apitie kwa makini “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa,” yaliyo kwenye ukurasa wa 185-207 wa kitabu hiki. Anapaswa kuelekezwa kwenye sehemu yenye kichwa, “Ujumbe kwa Mhubiri Ambaye Hajabatizwa,” kuanzia ukurasa wa 182, inayoeleza jinsi anavyoweza kujitayarisha kwa ajili ya mazungumzo hayo pamoja na wazee. Yule anayetaka kubatizwa anaweza kutumia maandishi aliyoandika mahali pengine na anaweza pia kufungua kitabu hiki wakati wa mazungumzo hayo. Hata hivyo, hakuna haja ya mtu mwingine kupitia maswali hayo pamoja naye kabla ya kukutana na wazee.

      Yeyote anayetaka kubatizwa anapaswa kumjulisha mratibu wa baraza la wazee. Baada ya mtu anayetaka kubatizwa kupitia “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa,” mratibu wa baraza la wazee atamuuliza ikiwa amejiweka wakfu kwa Yehova kupitia sala ili kufanya mapenzi Yake. Ikiwa mtu huyo amejiweka wakfu, mratibu wa baraza la wazee atapanga wazee wawili wazungumzie pamoja naye “Maswali kwa Ajili ya Wale Wanaotaka Kubatizwa.” Kila sehemu itashughulikiwa na mzee mmoja. Si lazima kusubiri mpaka tarehe ya kusanyiko itangazwe ndipo mazungumzo hayo yafanywe.

      Kwa kawaida, sehemu hizo mbili zinaweza kuzungumziwa katika vikao viwili vya saa moja hivi kila kimoja, ingawa si vibaya kutumia muda zaidi ikiwa inahitajika. Kila sehemu inapaswa kuanza na kumalizika kwa sala. Yule anayetaka kubatizwa wala wazee hawapaswi kuwa na haraka wanapopitia maswali hayo. Wazee waliopewa mgawo huo wanapaswa kuhakikisha kwamba mazungumzo hayo yanapewa kipaumbele katika ratiba zao.

      Kwa kawaida, ingefaa kupitia maswali pamoja na kila mtu anayetaka kubatizwa akiwa peke yake, wala si wakiwa kikundi. Anayetaka kubatizwa akitoa maelezo katika kila swali, wazee wataelewa vizuri kina cha ufahamu wake, na kuhakikisha kabisa ikiwa anastahili kubatizwa. Pia, huenda yule anayeomba kubatizwa akawa huru zaidi kutoa maelezo akiwa peke yake. Mume na mke wanaweza kupitia maswali hayo pamoja.

      Ikiwa yule anayetaka kubatizwa ni dada, mazungumzo hayo yanapaswa kufanywa mahali ambapo mzee na dada huyo hawatakuwa peke yao. Ikiwa ni muhimu kwenda na mtu mwingine, itafaa awe mzee au mtumishi wa huduma, ikitegemea sehemu wanayopitia kama inavyoonyeshwa katika fungu linalofuata.

      Katika makutaniko ambayo hakuna wazee wa kutosha, watumishi wa huduma wanaostahili wenye utambuzi na uwezo wa kufanya uamuzi mzuri wanaweza kutumiwa kupitia maswali ya ubatizo katika “Sehemu ya 1: Mafundisho ya Kikristo.” Ni wazee tu wanaopaswa kushughulikia “Sehemu ya 2: Maisha ya Kikristo.” Ikiwa kutaniko halina ndugu wa kutosha wanaostahili, mnaweza kuwasiliana na mwangalizi wa mzunguko ili aamue ikiwa wazee wa kutaniko la karibu wanaweza kusaidia.

      Ikiwa anayetaka kubatizwa ni mtoto, mzazi au wazazi wake ambao ni Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuwepo wakati wa mazungumzo ya maswali ya ubatizo. Ikiwa mzazi au wazazi hawataweza kuhudhuria, wazee wawili (au mzee na mtumishi wa huduma, ikitegemea sehemu wanayozungumzia) wanapaswa kuwepo katika kila sehemu ya mazungumzo hayo.

      Wazee watahakikisha kwamba mtu anayetaka kubatizwa anaelewa vya kutosha mafundisho ya msingi ya Biblia. Pia, watajitahidi kuthibitisha ikiwa mtu anayetaka kubatizwa anaithamini sana kweli na anaheshimu ifaavyo tengenezo la Yehova. Ikiwa mtu huyo haelewi mafundisho ya msingi ya Biblia, wazee watapanga asaidiwe kibinafsi ili astahili kubatizwa wakati mwingine. Huenda wengine wakahitaji kupewa wakati zaidi ili wathamini zaidi utumishi wa shambani au waonyeshe ujitiisho chini ya mipango ya kitengenezo. Wazee watatumia hekima kuamua jinsi watakavyotumia muda huo wa saa moja hivi katika kila sehemu ili wajue vizuri ikiwa mtu huyo yuko tayari kwa ajili ya ubatizo. Ingawa muda zaidi unaweza kutumiwa katika maswali fulani na maswali mengine yakachukua muda mfupi, maswali yote yanapaswa kuzungumziwa.

      Wazee waliopewa mgawo wa kupitia maswali na anayetaka kubatizwa watakutana baada ya kikao cha pili na kuamua ikiwa mtu huyo anapaswa kubatizwa au la. Wazee wanapaswa kuzingatia malezi, uwezo, na hali nyingine za kila mmoja anayetaka kubatizwa. Tunapendezwa hasa na wale ambao wameanza kusitawisha upendo kumwelekea Yehova na wanaoelewa kweli za msingi za Biblia. Mkiwasaidia kwa upendo, wale wanaobatizwa watakuwa wametayarishwa vya kutosha ili watimize mgawo wao muhimu wakiwa wahudumu wa habari njema.

      Baadaye, mzee mmoja au wote wawili waliopewa mgawo wa kuzungumza naye wanapaswa kukutana na mtu huyo na kumjulisha ikiwa anastahili kubatizwa au la. Ikiwa anastahili kubatizwa, wazee watapitia pamoja naye habari yenye kichwa “Mazungumzo ya Kumalizia Pamoja na Wale Wanaotaka Kubatizwa,” iliyo kwenye ukurasa wa 206-207. Ikiwa hajamaliza kujifunza kitabu Furahia Maisha Milele!, wazee wamtie moyo kumalizia baada ya ubatizo. Watamwambia yule anayetaka kubatizwa kwamba tarehe yake ya ubatizo itaandikwa kwenye Rekodi ya Kutaniko ya Mhubiri iliyo na jina lake. Watamkumbusha kwamba wazee hukusanya taarifa hizo za kibinafsi kutoka kwa mhubiri ili tengenezo liweze kushughulikia utendaji wa kidini wa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote na ili mhubiri ashiriki katika shughuli za kiroho na kupokea msaada wa kiroho. Zaidi ya hilo, wazee wanaweza kuwakumbusha wahubiri wapya kwamba taarifa zozote za kibinafsi hushughulikiwa kulingana na Sera ya Mashahidi wa Yehova ya Kulinda Taarifa Ulimwenguni Pote inayopatikana kwenye tovuti ya jw.org. Mazungumzo hayo yasizidi dakika kumi.

      Mwaka mmoja baada ya mhubiri kubatizwa, wazee wawili wanapaswa kukutana naye ili kumtia moyo na kumpa mapendekezo yatakayomsaidia. Mzee mmoja anapaswa kuwa mwangalizi wa kikundi cha utumishi cha mhubiri huyo. Ikiwa mhubiri huyo ni mtoto, wazazi au mzazi wake Mkristo anapaswa kuwepo. Kikao hicho kinapaswa kuwa chenye uchangamfu na kujenga. Wazee watazungumzia maendeleo yake ya kiroho na kumpa madokezo ya jinsi anavyoweza kuendelea kuwa na ratiba nzuri ya funzo la kibinafsi na usomaji wa Biblia kila siku, ibada ya familia ya kila juma, kuhudhuria na kushiriki mikutano kwa uaminifu, na kushiriki utumishi wa shambani kila juma. (Efe. 5:15, 16) Ikiwa hajamaliza kujifunza kitabu Furahia Maisha Milele! wazee wanapaswa kufanya mipango ili mhubiri fulani amsaidie kumalizia. Wazee wanapaswa kumpongeza kwa upendo. Kwa kawaida, shauri au pendekezo moja au mawili yanatosha.

  • Fahirisi
    Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
    • Fahirisi

      Zingatia: Marejeo mengi yaliyo hapa chini yameonyeshwa kwa namba ya sura ikifuatwa na namba ya fungu. Kwa mfano, rejeo la kwanza chini ya “Baraza Linaloongoza” ni “kulitambua: 3:1-6.” Hii inamaanisha kwamba habari zinazohusu kulitambua Baraza Linaloongoza zinapatikana katika Sura ya 3, fungu la 1 hadi la 6.

      Baraza Linaloongoza

      kulitambua: 3:1-6

      kulitumaini: 3:12-15

      sababu za kufuata mwongozo wa: 3:9-11; 4:9-11

      Dada

      ikiwa hakuna ndugu anayestahili: 6:9; 7:23

      kujitolea kwa ajili ya ujenzi: 10:21

      shule za kitheokrasi: 10:17-18

      Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo: 7:14-18

      Eneo

      la kikundi na la kibinafsi: 9:31-34

      lenye lugha nyingi: 9:36-38

      rekodi: 9:31

      Funzo la Mnara wa Mlinzi: 7:11-13

      Halmashauri

      ya Hukumu: 14:21-28, 34-37

      ya Nchi: 5:53

      ya Tawi: 4:13; 5:51-54

      ya Uendeshaji wa Jumba la Ufalme: 11:8

      ya Uhusiano na Hospitali: 5:40

      ya Utumishi ya Kutaniko: 5:35

      Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali na Vikundi vya Kuwatembelea Wagonjwa: 5:40

      Halmashauri ya utumishi

      (Ona Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko)

      Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko: 5:35

      Halmashauri za hukumu: 14:21-28, 34-37

      Harusi: 11:10-11

      Hotuba ya watu wote: 7:5-10

      Jumba la Ufalme

      gharama: 11:6; 12:5-6

      maktaba: 7:19

      makutaniko kadhaa: 11:8-9

      matumizi ya pekee: 11:10-11

      ujenzi: 10:21-23; 11:4-5, 15-17

      usafi na udumishaji: 11:7-8

      wakfu: 11:4

      JW.ORG: 9:24-25

      Karipio: 14:4, 23-24

      Kazi ya kimwili: 13:25-26

      Kazi za shuleni: 13:22-24

      Kuhubiri habari njema

      eneo: 9:30-34

      hadharani: 9:11-12

      isivyo rasmi: 9:26-29

      karne ya kwanza: 8:1-2; 9:1, 4

      kuongoza: 5:3, 17, 29-33; 6:4

      kuripoti: 8:19-29, 31-36

      kusimamiwa na mwangalizi wa utumishi: 5:28

      kustahili: 8:6-9, 13-15

      kutumia Tovuti ya jw.org: 9:24-25

      kuwatia moyo wanafunzi wa Biblia kutoa ushahidi isivyo rasmi: 8:5

      machapisho: 9:22-23

      maeneo yenye lugha nyingi: 9:35-44

      mahubiri ya vikundi: 9:45-46

      mapambo, mwenendo: 13:12

      mkutano kwa ajili ya utumishi wa shambani: 7:20-21

      msaada wa kibinafsi: 5:28-29, 33; 7:21; 9:7, 15, 19

      nyumba kwa nyumba: 9:3-9

      umuhimu: 9:5-8; 10:1-2

      utume kutoka kwa Mungu: 8:2

      vijana: 8:13-15

      wakati wa marufuku: 17:13-18

      ziara za kurudia: 9:14-15

      Kujitenga na ushirika: 14:30-33

      Kujitiisha

      (Ona Ukichwa)

      Kujitolea kwa ajili ya ujenzi: 10:21-23

      Kikundi cha Ujenzi: 10:23

      mjitoleaji wa Idara ya Usanifu-Majengo na Ujenzi: 10:23

      mjitoleaji wa ujenzi: 10:23

      mtumishi wa ujenzi: 10:23

      mtumishi wa ujenzi kutoka nchi nyingine: 10:23

      Kurudishwa: 14:34-36

      Kusanyiko la mzunguko

      gharama: 12:8-11

      mahali: 11:18

      tengenezo: 5:49

      Kutaniko

      (Ona pia Jumba la Ufalme; Mikutano)

      jipya na dogo: 7:22-23

      umoja: 13:28-30

      yamepangwa kitheokrasi: 1:3; 4:4-11

      Kutenga na ushirika: 14:25-29

      Kutoelewana

      makosa mazito: 14:13-20

      tofauti ndogo-ndogo: 14:5-6

      Kutumikia mahali penye uhitaji: 10:6-9

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki