Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Maumivu ya Kuwaacha Waende
    Amkeni!—1998 | Januari 22
    • Maumivu ya Kuwaacha Waende

      “Mume wangu alikuwa amenionya siku ambayo mtoto wetu wa kwanza alizaliwa—‘Kulea watoto, mpenzi, ni utaratibu mrefu wa kuwaacha waende.’”—Ourselves and Our Children—A Book by and for Parents.

      WAZAZI wengi wanafurahi—hata wanasisimka—mtoto wao wa kwanza anapozaliwa. Yajapokuwa magumu yote, mabishano, maumivu, kukatishwa tamaa, na mahangaiko yaletwayo na uzazi, watoto waweza kuwa chanzo cha shangwe kubwa. Kama miaka elfu tatu hivi iliyopita, Biblia ilijulisha wazi hivi: “Watoto ni zawadi kutoka kwa BWANA; wao ni baraka kwelikweli.”—Zaburi 127:3, Today’s English Version.

      Hata hivyo, Biblia hutoa utabiri huu wenye kufanya mtu afikiri: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Kwa sababu tofauti-tofauti watoto walio watu wazima kwa kawaida huondoka nyumbani—kuendeleza masomo au kazi-maisha, kupanua huduma yao ya Kikristo, kuoa au kuolewa. Lakini kwa wazazi fulani, uhalisi huu ni wenye kuumiza sana. Wanaruhusu kushindania uhuru kwa watoto wao kwa asili kuwafanye—kama mwandikaji moja alivyosema—“wahisi kutukanwa, kutendwa kwa njia mbaya, kuaibishwa, kutishwa au kukataliwa.” Hii kwa kawaida huongoza kwenye zogo na uvutano wa kifamilia usiokwisha. Kukataa kuikabili siku ambayo watoto wao wataondoka nyumbani, wazazi fulani hukosa kuwatayarisha kwa ajili ya utu mzima. Matokeo ya kupuuza kama huko yaweza kuwa yenye kuogofya: kwaweza kutokeza watu wazima ambao hawako tayari kusimamia nyumba, kutunza familia, au hata kupata na kubaki katika kazi ya kuajiriwa.

      Maumivu ya kutengana yaweza kuwa mabaya zaidi katika familia za mzazi aliye pekee. Mmoja aliye mzazi pekee aitwaye Karen asema: “Binti yangu nami tuna ukaribu sana; tumesitawisha muungano halisi wa urafiki. Kila nilikokwenda, nilienda naye.” Uhusiano wa karibu kati ya mzazi na mtoto ni wa kawaida katika nyumba zenye mzazi aliye pekee. Kwa kueleweka, wazo la kupoteza ukaribu huo laweza kuwa lenye kuangamiza kabisa.

      Hata hivyo, kitabu Traits of a Healthy Family chawakumbusha wazazi hivi: “Hili ndilo lahusika katika maisha ya familia: kumtunza mtoto mchanga mwenye kuwategemea kabisa hadi awapo mtu mzima anayejitegemea.” Kisha chaonya: “Matatizo mengi katika familia hutokea kwa sababu wazazi hawawaachi watoto waende.”

      Namna gani wewe? Je, wewe ni mzazi? Ikiwa ndivyo, je, umejitayarisha kwa ajili ya siku ambayo utawaacha watoto wako waende? Na namna gani watoto wako? Je, unawatayarisha ili waweze kujitegemea?

  • Kujifunza Kuwaacha Waende
    Amkeni!—1998 | Januari 22
    • Kujifunza Kuwaacha Waende

      “KAMA mishale mkononi mwa shujaa, ndivyo walivyo wana wa ujanani,” akaandika mtunga-zaburi wa Biblia. (Zaburi 127:4) Mshale haufikii shabaha yake kwa aksidenti. Lazima ulengwe kwa uangalifu. Kwa njia hiyohiyo, watoto hawawezi kufikia lengo la kuwa watu wazima wenye madaraka bila mwongozo wa wazazi. “Mlee mtoto katika njia impasayo,” Biblia yahimiza, “naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”—Mithali 22:6.

      Badiliko la kutoka kuwa mtoto mwenye kutegemea wazazi hadi kuwa mtu mzima mwenye kujitegemea haliwezi kufanywa usiku mmoja. Kwa hiyo wazazi wapaswa kuanza lini kuwazoeza watoto wao kuwa wenye kujitegemea? Mtume Paulo alimkumbusha mwanamume kijana aliyeitwa Timotheo hivi: “Tangu utoto sana umeyajua maandishi matakatifu, yawezayo kukufanya uwe mwenye hekima kwa ajili ya wokovu kupitia imani kuhusiana na Kristo Yesu.” (2 Timotheo 3:15) Wazia, mama ya Timotheo alianza kumpa mazoezi ya kiroho akiwa angali mtoto mchanga sana!

      Sasa, ikiwa watoto wachanga sana waweza kufaidika kutokana na mazoezi ya kiroho, je, si jambo lenye ukubalifu kuwapatia mazoezi kwa ajili ya utu mzima mapema iwezekanavyo? Njia moja ya kufanya hivyo ni kuwafunza kuchukua mambo kwa uzito, kufanya maamuzi yao wenyewe.

      Kuwafunza Watoto Wawe Wenye Madaraka

      Waweza kuwatiaje moyo watoto wako wawe wenye madaraka? Wenzi waliooana waitwao Jack na Nora wakumbuka kuhusiana na binti yao: “Kabla hajaweza kutembea kabisa, alijifunza kubeba soksi au vitu vidogo kupeleka kwenye chumba chake cha kulala na kuviweka katika mtoto wa meza anayefaa. Pia alijifunza kuweka vichezeo na vitabu mahali panapofaa.” Hii ni mianzo midogo, lakini tayari mtoto alikuwa akijifunza kufanya maamuzi yenye madaraka.

      Kadiri mtoto aendeleavyo kuwa mkubwa, yeye aweza kukabidhiwa madaraka mazito zaidi. Hivyo Abra na Anita walimruhusu binti yao awe na mbwa kama mnyama-rafiki. Kijana huyo alikuwa na daraka kuelekea utunzaji wa mbwa huyo na hata alitoa pesa kutoka katika ruzuku yake kwa ajili ya gharama za kumtunza. Kuwazoeza watoto kuishi kulingana na madaraka yao kwahitaji subira. Lakini ni kwenye kufaa na kwachangia ukuzi wao wa kihisia-moyo.

      Kazi za kila siku za nyumbani zatoa fursa nyingine ya kufunza watoto kuwa wenye madaraka. Wazazi wengine kwa kweli huwaachilia watoto wao kutokana na wajibu wa familia, wakiona kujihusisha kwao kuwa usumbufu kuliko kuwa msaada. Wengine hukata kauli kwamba watoto wapaswa ‘kuishi maisha bora zaidi kuliko waliyokuwa nayo wakiwa watoto.’ Huku ni kufikiri kwenye kasoro. Maandiko yasema “Ikiwa mtu anamwendekeza mtumishi wake tangu ujana na kuendelea, katika maisha yake ya baadaye atakuwa hata asiye na shukrani.” (Mithali 29:21, NW) Kanuni ya andiko hili bila shaka yatumika kwa watoto. Inahuzunisha wakati kijana afikiapo utu mzima akiwa si “asiye na shukrani” tu bali pia akiwa hawezi kushughulikia hata kazi rahisi kabisa za nyumbani.

      Vijana katika nyakati za Biblia kwa kawaida waligawiwa kazi za kila siku za nyumbani. Kwa kielelezo, katika umri mchanga wa miaka 17, Yusufu mchanga alishiriki katika madaraka ya kutunza mifugo ya familia. (Mwanzo 37:2) Huu haukuwa mgawo mdogo kwani, mifugo ya baba yake ilikuwa mingi sana. (Mwanzo 32:13-15) Kwa kufikiria uhakika wa kwamba Yusufu alikua akawa kiongozi mwenye nguvu, yawezekana kuwa mazoezi yake ya mapema yalikuwa na sehemu kubwa katika kufanyiza tabia yake kwa njia chanya. Mfalme wa baadaye wa Israeli Daudi vilevile alipewa mifugo ya familia yake ili awatunze akiwa angali kijana.—1 Samweli 16:11.

      Somo ni nini kwa wazazi leo? Wagawieni watoto wenu migawo ya kazi za kila siku za nyumbani zenye umaana. Kwa wakati, nishati, na subira, waweza kuwafunza wachanga kushiriki kusafisha, kupika, kutunza uwanja, na kurekebisha nyumba na gari. Ni kweli kuwa mengi yategemea umri na uwezo wa mtoto. Lakini hata watoto wadogo waweza kuwa na sehemu katika ‘kumsaidia Baba kurekebisha gari’ au katika ‘kumsaidia Mama kupika chakula.’

      Kufunza kazi za kawaida za nyumbani pia kwahitaji wazazi wawape watoto zawadi ya thamani sana—wakati wao. Wenzi fulani waliooana, wazazi wa watoto wawili, waliulizwa siri ya kufaulu kuwazoeza watoto. Walijibu: “Wakati, wakati, wakati!”

      Rekebisho Lenye Upendo

      Watoto wafanyapo kazi yao vizuri, au angalau wawekapo jitihada kuifanya, watie moyo kwa sifa zenye ukarimu na za moyo mweupe! (Linganisha Mathayo 25:21.) Bila shaka, ni nadra kwa watoto kufanya mambo kwa uhodari wa watu wazima. Na wakati watoto wakubaliwapo kufanya maamuzi yao wenyewe, mara nyingi wao watafanya makosa. Lakini jihadhari usitende kupita kiasi! Je, hujafanya makosa ukiwa mtu mzima? Kwa hiyo, kwa nini usionyeshe subira mtoto wako akoseapo? (Linganisha Zaburi 103:13.) Acha nafasi kwa ajili ya makosa. Yaone kama sehemu ya hatua za kujifunza.

      Watungaji Michael Schulman na Eva Mekler waonelea: “Watoto wanaotendewa kwa njia yenye urafiki hawaogopi kuwa wataadhibiwa kwa kufanya tendo la kujisimamia wenyewe.” Hata hivyo, “watoto walio na wazazi wasio na shauku au walio wakali wanaogopa kufanya tendo lolote la kujianzia, kutia ndani yawezayo kusaidia, kwa kuogopa kuwa wazazi wao watapata kosa katika yale ambayo wamefanya na kuwachambua au kuwaadhibu.” Elezo hili lapatana na onyo la Biblia kwa wazazi: “Msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike, ili wasishuke moyo.” (Wakolosai 3:21) Kwa hiyo wakati jitihada za mtoto hazifikii yaliyotarajiwa, kwa nini usimsifu kwa kuwa angalau alijaribu? Mtie moyo afanye vizuri zaidi wakati ujao. Mwache ajue kwamba maendeleo yake yanakuletea furaha. Mhakikishie upendo wako.

      Bila shaka, wakati mwingine rekebisho lahitajika. Hili laweza kuwa wazi hasa katika miaka ya ubalehe, wakati ambapo vijana hupigania utambulisho wao, ili wakubalike wakiwa watu binafsi walio na haki zao. Wazazi wanakuwa wenye hekima waonapo jitihada hizo kwa uelewevu badala ya kila mara kuzifasiri kuwa uasi.

      Kweli, vijana wana mwelekeo wa kufanya mambo kwa msukumo au kujiruhusu kuathiriwa na “tamaa zenye kutukia ujanani.” (2 Timotheo 2:22) Kwa hiyo kukosa kuwekea mipaka tabia ya kijana kwaweza kumharibu mtoto kihisia-moyo; atakosa kujifunza kujidhibiti na hatakuwa na nidhamu ya kibinafsi. Biblia yaonya: “Mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.” (Mithali 29:15) Lakini nidhamu inayofaa, ikitolewa kwa upendo, ni yenye manufaa na humtayarisha kijana kwa ajili ya madai na misongo ya utu mzima. Biblia yahimiza hivi: “Yeye asiyetumia fimbo yake humchukia mwanawe; bali yeye ampendaye humrudi mapema.” (Mithali 13:24) Hata hivyo, kumbuka kwamba, kiini cha nidhamu ni kufunza na kuzoeza—si kuadhibu. Hapa “fimbo” yaelekea yarejezea fimbo iliyotumiwa na wachungaji kuwaelekeza mifugo yao. (Zaburi 23:4) Ni ishara ya mwongozo wenye upendo—si unyama wenye kudhulumu.

      Elimu kwa Ajili ya Uhai

      Mwongozo wa wazazi wahitajika hasa elimu ya mtoto inapohusika. Pendezwa na elimu ya mtoto wako. Msaidie kuchagua masomo ya shuleni yanayofaa na uchukue daraka la kuamua ikiwa elimu yoyote ya ziada itahitajika.a

      Bila shaka, elimu ya maana zaidi ya zote ni elimu ya kiroho. (Isaya 54:13) Watoto watahitaji kanuni za kimungu ili kuokoka katika ulimwengu wa utu mzima. “Nguvu zao za ufahamu” lazima zizoezwe. (Waebrania 5:14) Wazazi waweza kufanya mengi ili kuwasaidia watoto wao katika hili. Familia miongoni mwa Mashahidi wa Yehova zinatiwa moyo kuwa na funzo la Biblia la kawaida pamoja na watoto wao. Wakifuata kielelezo cha mama ya Timotheo, ambaye alimfunza Maandiko tangu utoto mchanga sana, wazazi Mashahidi vivyo hivyo huwafunza watoto wao wadogo.

      Mzazi aliye pekee aitwaye Barbara hufanya funzo la familia la Biblia kuwa pindi yenye kupendeza zaidi kwa watoto wake. “Jioni hiyo nahakikisha kuwa nawapa watoto chakula kizuri, kamili na kitindamlo wanachofurahia. Nacheza kanda za Kingdom Melodies ili kufanyiza mandhari nzuri. Kisha, baada ya kufungua kwa sala, kwa kawaida sisi hujifunza gazeti Mnara wa Mlinzi. Lakini kukiwa na uhitaji maalumu, naweza kutumia vichapo kama vile Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi.”b Kulingana na Barbara, kujifunza Biblia huwasaidia watoto wake “kupata maoni ya Yehova kuhusu mambo.”

      Ndiyo, hakuna zawadi kubwa kuliko ujuzi na uelewevu wa Neno la Mungu Biblia, ambayo mtoto aweza kupewa. Huo waweza kuwapa “wajinga werevu, na kijana maarifa na hadhari.” (Mithali 1:4) Hivyo, akiwa amejihami, kijana aingia utu mzima akiwa na uwezo wa kukabili misongo na hali mpya.

      Hata hivyo, watoto wanapoondoka nyumbani, hilo husababisha badiliko kubwa katika mtindo-maisha wa wazazi wengi. Jinsi wawezavyo kukabiliana na kuondoka kwa watoto nyumbani kwazungumziwa katika makala yetu ifuatayo.

  • Kuishi kwa Furaha Katika Nyumba Isiyo na Watoto
    Amkeni!—1998 | Januari 22
    • Kuishi kwa Furaha Katika Nyumba Isiyo na Watoto

      “KWA wengi wetu,” akakiri mzazi mmoja, “kutengana kwa mwisho huleta mshtuko hata tuwe tumejitayarisha vema kadiri gani.” Ndiyo, kadiri kuondoka kwa mtoto kusivyoweza kuepukika, kunapotukia kwa hakika, kushughulika nako kwaweza kuwa vigumu. Baba mmoja aeleza kuhusu itikio lake mwenyewe baada ya kumwambia mwana wake kwaheri: “Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu . . . , nililia tu, na kulia na kulia.”

      Kwa wazazi wengi kuondoka kwa watoto wao huacha utupu katika maisha yao—kidonda kilicho wazi. Kwa kunyimwa uhusiano wa kila siku na watoto wao, wengine hupatwa na hisia nyingi za upweke, maumivu, na hasara. Na huenda ikawa si wazazi peke yao wanaopata wakati mgumu wa kujirekebisha. Wenzi waitwao Edward na Avril watukumbusha: “Ikiwa bado kuna watoto wengine nyumbani, wao pia watahisi hasara.” Shauri la wenzi hawa ni nini? “Wapeni watoto walio nyumbani upendo na uelewevu wenu. Hili litawasaidia kujirekebisha.”

      Ndiyo, maisha yaendelea. Ikiwa utawatunza watoto waliobaki—vilevile kazi yako ya kimwili au wajibu wa nyumbani—huwezi kujiruhusu ukwame kwa huzuni. Kwa hiyo, acheni tuangalie njia fulani uwezazo kupata furaha watoto wako waondokapo nyumbani.

      Tazama Yaliyo Chanya

      Bila shaka, ikiwa wahisi huzuni au mpweke na wataka kulia au kuzungumza kuhusu hisia zako na rafiki mwenye kukusikitikia, kwa vyovyote fanya hivyo. Biblia husema: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha; bali neno jema huufurahisha.” (Mithali 12:25) Nyakati nyingine wengine waweza kukupatia mtazamo mpya wa akilini. Kwa kielelezo, wenzi waitwao Waldemar na Marianne washauri hivi: “Ona jambo hilo, si kama kupoteza, bali kama mafanikio ya mradi.” Njia chanya kama nini ya kuona mambo! “Tunafurahi kwamba tuliweza kuwalea wavulana wetu kuwa watu wazima wenye madaraka,” wasema wenzi waitwao Rudolf na Hilde.

      Je, umejitahidi sana kumlea mtoto wako “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova”? (Waefeso 6:4) Hata kama umefanya hivyo, waweza bado kuwa na hangaiko kuhusu kuondoka kwake. Lakini kwa wale wanaomzoeza mtoto wao hivyo, hakikishio la Biblia ni kwamba “hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Je, hairidhishi kuona kwamba mtoto wako ameitikia mazoezi yako? Mtume Yohana alisema hivi kuhusu familia yake ya kiroho: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 4) Labda waweza kusema maneno kama hayo kuhusiana na mtoto wako.

      Ni kweli kwamba si watoto wote wanaoitikia mazoezi ya Kikristo. Ikiwa yatokea hivi kwa mtoto wako aliye mtu mzima, haimaanishi kuwa umeshindwa ukiwa mzazi. Usijishushe isivyofaa ikiwa umefanya yote uwezayo ili kumlea katika njia ya kimungu. Tambua kwamba akiwa mtu mzima mtoto wako anachukua mzigo wake mwenyewe wa daraka mbele ya Mungu. (Wagalatia 6:5) Dumisha tumaini kwamba huenda baada ya wakati aweza kufikiria tena machaguo yake na kwamba hatimaye “mshale” utaenda ulipolengwa.—Zaburi 127:4.

      Ungali Mzazi!

      Huku kuondoka kwa mtoto wako kukitangaza badiliko, hakumaanishi kuwa kazi yako kama mzazi imekwisha. Mwanasaikolojia Howard Halpern asema: “Wewe ndiye mzazi hadi siku utakayokufa, lakini kutoa na kutunza lazima kufanyizwe upya.”

      Zamani Biblia ilikiri kwamba uzazi haukwishi kwa sababu mtoto amekuwa mtu mzima. Mithali 23:22 husema: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee.” Ndiyo, hata wakati wazazi ‘wamekuwa wazee’ na watoto wao ni watu wazima, wazazi wanaweza bado kuwa na uvutano fulani katika maisha ya watoto wao. Bila shaka, marekebisho fulani yahitaji kufanywa. Lakini mahusiano yote yahitaji kurekebishwa mara kwa mara ili yabaki yakiwa mapya na yenye kuridhisha. Sasa kwa vile watoto wako wamekua, fanyia kazi kuufanya uhusiano wenu kuwa na msingi wa utu mzima zaidi. Kwa kupendeza, uchunguzi waonyesha kwamba uhusiano kati ya mzazi na mtoto mara nyingi huboreka mara watoto waondokapo nyumbani! Watoto waonapo misongo inayohusiana na mahangaiko ya kila siku, mara nyingi wao huanza kuwaona wazazi wao kwa njia tofauti. Mwanamume Mjerumani aitwaye Hartmut asema: “Sasa nawaelewa wazazi wangu vizuri zaidi na natambua kwa nini walifanya mambo jinsi walivyofanya.”

      Epuka Kujiingiza

      Ikiwa wajiingiza katika maisha ya kibinafsi ya mtoto wako aliye mtu mzima, madhara mengi yaweza kutokea. (Linganisha 1 Timotheo 5:13.) Mwanamke mmoja aliyeolewa ambaye anapatwa na mkazo kutoka kwa wakwe zake aomboleza hivi: “Twawapenda, lakini twataka tu kuishi maisha yetu wenyewe na kufanya maamuzi yetu wenyewe.” Bila shaka, hakuna mzazi yeyote mwenye kujali ambaye atakaa kitako tu wakati mtoto wake aliye mtu mzima aingiapo katika msiba. Lakini kwa kawaida ni vizuri zaidi kutotoa shauri la kimzazi bila kuombwa, hata liwe ni lenye hekima jinsi gani au liwe la nia njema jinsi gani. Hili ni kweli hasa baada ya mtoto kuoa au kuolewa.

      Amkeni! lilitoa shauri hili katika mwaka wa 1983: “Kubali daraka lako lililobadilika. Unaacha kumtendea mtoto wako kama mtoto mchanga sana anayenyonya wakati aanzapo kutembea. Vivyo hivyo, lazima ubadilishane daraka la kuwa mtunzaji na daraka la kuwa mshauri. Kufanya maamuzi kwa ajili ya mtoto wako katika wakati huu wa maisha kungekuwa kusikofaa kama tu vile kumtoa hewa au kumnyonyesha akiwa mtu mzima. Ukiwa mshauri, una mipaka dhahiri. Huwezi tena kufanya amri yako ukiwa mzazi itumike kwa matokeo. (‘Fanya hivyo kwa sababu nimesema.’) Lazima kuwe na staha kwa hadhi ya mtoto wako ya utu mzima.”a

      Huenda usikubaliane na maamuzi yote ambayo mtoto wako na mwenzi wake wafanya. Lakini staha kwa utakatifu wa ndoa itakusaidia kupima mahangaiko yako na kuepuka kuingilia isivyo lazima. Ukweli ni kwamba, kwa kawaida ni vizuri zaidi kwa wazazi kuwaacha wenzi wachanga kutatua matatizo yao wenyewe. Kama sivyo, wajihatarisha kupatwa na kabiliano lisilo la lazima unapotoa shauri lisilohitajika kwa mwana au binti-mkwe ambaye, katika hali ya ndoa iliyo rahisi kuvunjika, aweza kuwa mwenye hisia nyepesi kuelekea uchambuzi. Amkeni! lililotajwa hapo juu lilitoa shauri hili la ziada: “Vunja tamaa ya kutoa mashauri yasiyo na mwisho, yasiyoombwa, ambayo yaweza kumfanya mwana-mkwe au binti-mkwe awe adui.” Uwe mwenye tegemezo—usiwe mwenye kuongoza kwa hila. Kwa kudumisha uhusiano mzuri, unafanya iwe rahisi kwa mtoto wako kukujia ikiwa shauri lahitajiwa kikweli.

      Fanyeni Upya Vifungo Vyenu vya Ndoa

      Kwa wenzi wengi, kuondoka kwa watoto nyumbani kwaweza pia kufungulia uwezekano wa kuongezeka kwa furaha katika ndoa. Wakati na jitihada inayotumika katika uzazi wenye matokeo zaweza kuwa nyingi mno hivi kwamba wenzi wanapuuza uhusiano wao wenyewe. Mke mmoja asema: “Sasa kwa vile watoto wameenda, Konrad nami twajaribu kujuana upya tena.”

      Kwa kuwekwa huru kutokana na madaraka ya kila siku ya uzazi, sasa mwaweza kuwa na wakati mwingi zaidi wa kuwa pamoja. Mzazi mmoja alionelea: “Wakati huu mpya usiopangiwa mambo . . . waturuhusu kuelekeza uangalifu zaidi juu ya sisi ni nani, kukazia fikira kujifunza mengi kuhusu mahusiano yetu, na kuanza kujihusisha katika utendaji unaojazia mahitaji yetu.” Yeye aongezea: “Ni wakati wa kujifunza kupya na ukuzi wa ajabu, na ingawa nyakati kama hizo zaweza kuwa zisizo na utulivu, ni zenye kuchangamsha pia.”

      Wenzi fulani pia wana uhuru zaidi wa kifedha. Hobi na kazi-maisha ambazo zilikuwa zimewekwa kando sasa zaweza kufuatiwa. Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, wenzi wengi hutumia uhuru wao walioupata upya kufuatia mapendezi ya kiroho. Baba aitwaye Hermann aeleza kwamba baada ya watoto wake kuondoka nyumbani, yeye na mke wake mara moja waligeuzia uangalifu wao kurudia utumishi wa wakati wote.

      Wazazi Walio Pekee Wakiwaacha Waende

      Kujipatanisha na hali baada ya watoto kuondoka nyumbani kwaweza kuwa vigumu hata zaidi kwa wazazi walio pekee. Rebecca, mama aliye mzazi pekee wa watoto wawili aeleza: “Watoto wetu waondokapo, hatuna mume wa kutupatia ushirika na upendo.” Mama aliye mzazi pekee huenda akawaona watoto wake kuwa chanzo cha tegemezo la kihisia-moyo. Na ikiwa walikuwa wanachangia fedha za nyumbani, kuondoka kwao kwaweza pia kuleta ugumu wa kiuchumi.

      Wengine huweza kuboresha hali yao ya kiuchumi kwa kujiunga na programu za kuzoeza kikazi au kuchukua mitaala ya muda mfupi katika shule. Lakini mmoja hujaziaje utupu wa upweke? Mzazi aliye pekee asema: “Kile ambacho hufanya kazi kwangu ni kuwa na jambo la kufanya kila wakati. Yaweza kuwa ni kusoma Biblia, kusafisha nyumba yangu, au kwenda tu matembezi au kukimbia. Lakini njia yenye kuridhisha zaidi kwangu ni kuzungumza na rafiki wa kiroho.” Ndiyo, ‘panuka,’ na utafute marafiki wapya wenye kuridhisha. (2 Wakorintho 6:13) ‘Dumu katika dua na sala’ unapohisi mpweke kabisa. (1 Timotheo 5:5) Uwe na uhakika kuwa Yehova atakupa nguvu na kukutegemeza katika kipindi hiki kigumu cha kujirekebisha.

      Kuwaacha Waende kwa Furaha

      Hata hali yako iweje, tambua kwamba maisha hayaishi wakati watoto wako waondokapo nyumbani. Wala vifungo vya familia havivunjiki. Upendo halisi unaoelezwa katika Biblia ni wenye nguvu za kutosha kuwaunganisha watu pamoja, hata wakiwa wako mbali. Mtume Paulo atukumbusha kwamba upendo “huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.” (1 Wakorintho 13:7, 8) Upendo usio na ubinafsi ambao umekuza katika familia yako hautashindwa kwa sababu tu watoto wako wameondoka nyumbani.

      Kwa kupendeza, wakati watoto waondokapo nyumbani na kuanza kukabiliana na maumivu ya kutengana na kukosa nyumbani au wakati waanzapo kuhisi msongo wa kiuchumi, mara nyingi wao ndio huwa wa kwanza kurudisha upya uhusiano. Hans na Ingrid washauri hivi: “Waache watoto wajue kwamba wanakaribishwa nyumbani wakati wowote.” Ziara za kawaida, barua, au simu za mara fulani-fulani zitasaidia kudumisha uhusiano. “Pendezwa na wanayofanya bila kuingilia mambo yao,” hivyo ndivyo Jack na Nora walivyoeleza.

      Watoto waondokapo nyumbani, maisha hubadilika. Lakini maisha katika nyumba isiyo na watoto yaweza kuwa yenye shughuli nyingi, yenye utendaji, na yenye kuridhisha. Pia, uhusiano wako na watoto wako hubadilika. Lakini, uhusiano wenu waweza kuwa wenye furaha na wenye kupendeza. “Kusitawisha uhuru kutoka kwa wazazi,” wasema Maprofesa Geoffrey Leigh na Gary Peterson, “hakudokezi kukosa upendo, uaminifu-mshikamanifu, au staha kwa wazazi. . . . Kwa kweli, vifungo vyenye nguvu vya familia huendelea muda wote wa duru ya maisha.” Ndiyo, hutaacha kamwe kuwapenda watoto wako, na hutaacha kamwe kuwa mzazi wao. Na kwa sababu umewapenda watoto wako kiasi cha kwamba umewaruhusu waende, kwa kweli hujawapoteza.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki