Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 11/8 kur. 10-13
  • Nilijifunza Lugha Nyingine Ili Kuwasiliana na Mtoto Wangu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nilijifunza Lugha Nyingine Ili Kuwasiliana na Mtoto Wangu
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Nilihisi Vibaya Sana
  • Kitu Gani Kingekuwa Bora kwa Spencer?
  • Badiliko Kubwa Sana Kwangu
  • Wakati wa Kuhama
  • “Twaweza Kuongea Jambo Lolote”
  • Lugha Ambayo Waiona!
    Amkeni!—1998
  • Jinsi Mungu Anavyowajali Viziwi
    Habari Zaidi
  • Nilipata Usalama Nijapokuwa Kiziwi na Kipofu
    Amkeni!—2001
  • Wathamini Ndugu na Dada Zako Viziwi!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 11/8 kur. 10-13

Nilijifunza Lugha Nyingine Ili Kuwasiliana na Mtoto Wangu

KUZALIWA kwa mwana wetu, Spencer, katika Agosti 1982 kulikuwa moja ya matukio ya furaha zaidi katika maisha yetu. Alikuwa mtoto mwenye afya nzuri! Mume wangu nami tulipanga kipindi cha miaka mitano ya kungoja kabla ya kupata mtoto wetu wa kwanza. Kadiri miezi ilivyopita baada ya kuzaliwa kwake, ndivyo tulivyozidi kupata shangwe kumwona akikua! Matokeo ya kupimwa kwake kwa ukawaida katika ofisi ya daktari yalikuwa mazuri sikuzote. Nilimshukuru Yehova kwa zawadi ya ajabu namna hii.

Lakini, Spencer alipofika umri wa miezi tisa, nilianza kuhisi kwamba kulikuwa na kasoro fulani. Hakuwa akiitikia sauti au milio fulani. Ili kujaribu kusikia kwake nilikaa mahali ambapo asingeniona kisha ningepiga sufuria au vitu vingine. Mara nyingine aligeuka, lakini haikuwa hivyo nyakati zote. Alipopimwa akiwa na umri wa miezi tisa, nilizungumza na daktari wake kuhusu wasiwasi wangu, lakini alinihakikishia kwamba mwana wangu alikuwa mzima na kwamba hamna haja ya kuwa na wasiwasi. Lakini, miezi ilipozidi kupita, bado hakuwa akisikia au kutoa sauti ya kusikika.

Alipopimwa akiwa na umri wa mwaka mmoja, nilieleza wasiwasi wangu tena kwa daktari. Kwa mara nyingine hakugundua tatizo lolote lakini alituelekeza kwa mtaalamu wa sikio. Nilimpeleka Spencer huko akapimwe, lakini bado matokeo hayakuwa kamili. Nilirudi kwa mara ya pili na ya tatu, niliambiwa tu kwamba matokeo yalikuwa bado si kamili. Daktari huyo alihisi kwamba kadiri Spencer alipozidi kukua, angeonyesha matokeo bora zaidi baada ya kupimwa. Miaka mitatu ya kwanza ya mtoto ni muhimu kwa maendeleo ya lugha. Niliendelea kuwa mwenye wasiwasi sana. Niliendelea kumuuliza mtaalamu wa sikio kuhusu upimaji ambao ungeonyesha matokeo kamili. Hatimaye aliniambia kuhusu upimaji fulani wa sikio wa shina la ubongo upatikanao Hospitali ya Macho na Masikio ya Massachusetts.

Nilihisi Vibaya Sana

Juma lililofuata tulienda kwenye hiyo hospitali katika Boston. Nilisali kwa Yehova anipe nguvu kukabiliana na matokeo, yawe ni yapi. Katika moyo wangu nilihisi kwamba Spencer alikuwa na ugumu wa kusikia na kwamba kifaa cha kusaidia kusikia kitakuwa ndicho kitu pekee kilichohitajiwa. Nilikosea kama nini! Baada ya kupimwa, huyo fundisanifu alituita katika ofisi yake. Matokeo yalikuwa kamili: Spencer alikuwa na kasoro kubwa katika mishipa ya kusikia. Nilipouliza hilo lilimaanisha nini hasa, alieleza kwamba mtoto wangu hakuwa na uwezo wa kusikia usemi na sauti nyinginezo nyingi. Sikutarajia kusikia hilo, nilihisi vibaya sana.

Mara moja, nilijiuliza, ‘Hili lilitukiaje? Ni nini kilicholisababisha?’ Nilifikiria wakati wa mimba na kujifungua. Kila kitu kilikuwa kimeenda vizuri. Kamwe Spencer hakupata kushikwa na ambukizo la sikio au homa yoyote kali. Nililemewa na hisia moyo! Nilipaswa kufanya nini sasa? Niliwapigia simu familia yangu na marafiki wachache na kuwaambia matokeo ya kupimwa kwake. Rafiki mmoja Shahidi alinitia moyo kuiona hali hii kuwa mwito wa ushindani; nilipaswa tu kumfundisha Spencer katika njia tofauti. Nilishukuru Yehova kwa nguvu iliyohitajiwa.

Kitu Gani Kingekuwa Bora kwa Spencer?

Sikujua lolote kuhusu kumlea mtoto kiziwi au kilichomaanishwa na kuwa kiziwi. Ningeweza kumleaje mwana wangu na kuwasiliana naye vizuri? Nikawa na mawazo mengi na wasiwasi mwingi.

Juma lililofuata tulirudi hospitali, na huyo fundisanifu alizungumzia mambo tuwezayo kufanya. Alieleza kwamba njia moja, njia ya mdomo, ilikazia maendeleo ya usemi na ustadi wa kusoma mdomo. Njia nyingine ilikuwa kutumia lugha ya ishara, ambayo ni lugha ya viziwi. Kulikuwa na programu ambayo iliandaa maagizo katika lugha ya ishara na baadaye ingetia ndani ustadi wa kusoma mdomo na usemi. Huyo fundisanifu pia alishauri kutumia vifaa vya kusaidia kusikia ili kukuza uwezo mdogo wa mwana wangu wa kusikia. Kisha tulimtembelea mtaalamu wa sikio wa eneo letu ambaye alimwagiza Spencer atumie ear molds na vifaa vya kusaidia kusikia. Wakati wa ziara yetu mtaalamu huyo wa sikio alishauri kwamba Spencer angefaa sana kufundishwa njia ya mdomo.

Kitu gani kingekuwa bora kwa Spencer? Nilifikiria kile ambacho kilikuwa cha maana sana. Yehova atutaka kuwasiliana na watoto wetu, hili ni jambo la maana sana ikiwa twataka kuwa na maisha ya familia yenye mafanikio. Twaweza kuendelea na njia ya mdomo na kukazia juu ya maendeleo ya usemi na ustadi wa kusoma mdomo. Iliwezekana kwamba Spencer angeendeleza ustadi wake wa usemi kufikia mahali ambapo wengine wangemwelewa. Lakini isingejulikana kwa miaka mingi kama angefanikiwa! Tulipaswa kufanya nini sasa? Tuliamua kutumia lugha ya ishara.

Mwezi uliofuata Spencer aliandikishwa katika ile iliyoitwa wakati huo programu ya uwasiliano kamili. Sote wawili Spencer nami tulikuwa tunajifunza masomo ya msingi ya lugha ya ishara, na Spencer alipewa maagizo katika Kiingereza kinachosemwa na pia katika kusoma mdomo. Nilionyeshwa namna ningemfundisha mwana wangu. Miezi ilipita, na Spencer alikuwa akifanya maendeleo sana. Hata hivyo, bado kulikuwa na nyakati ambazo nilihisi nimelemewa sana. Nilikatishwa tamaa nilipoona watoto wengine wakisema “Mama” au wakijifunza jinsi ya kusema “Yehova.” Lakini baadaye nilijiuliza mwenyewe, ‘Kwa nini nahisi hivi? Mwana wangu ni mwenye furaha na ana afya nzuri.’ Nilisali kwa Yehova ili anisaidie nithamini pendeleo la kuwa na mtoto mzuri namna hiyo.

Spencer alipokuwa na umri wa miaka miwili, tulifanya mipango ili kuhudhuria mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova ambapo programu ingetafsiriwa katika Lugha ya Ishara ya Kimarekani (ASL). Nilizungumzia hisia zangu za kuvunjika moyo na wenzi ambao walikuwa wamefanya kazi na Mashahidi viziwi kwa miaka mingi. Walinieleza juu ya mkutano wa Mashahidi wa Yehova wa ASL unaofanyika kila mwezi katika Massachusetts na walinitia moyo niende.

Nilifuata shauri lao, sote wawili Spencer na mimi tulianza kuhudhuria. Hapo tulikuwa na nafasi ya kukutana na kuchocheana na viziwi walio watu wazima. Katika kutaniko letu la Kiingereza, Spencer hakufaidika na mikutano. Angeshikamana nami, kwani nilikuwa mtu pekee ambaye angeweza kuwasiliana naye. Kukatishwa tamaa kwake katika mikutano kama hiyo kuliongezeka kadiri alivyokua, na tabia yake ikaanza kuzorota. Hata hivyo, tulipohudhuria mikutano iliyofanywa katika lugha ya ishara, hali haikuwa hivyo. Aliweza kuchangamana kwa uhuru na kila mtu bila kuhitaji kupitia kwa mama yake akiwa mkalimani. Alikuza uhusiano wenye thamani sana na watu katika kutaniko. Sote wawili tulikuza matumizi ya lugha ya ishara, na nilijifunza jinsi ya kuwa mwalimu mzuri wa funzo letu la Biblia nyumbani. Ilipendeza kama nini! Sasa kwa mara ya kwanza, katika mkutano ningeweza kuwa na mwana na kuwa tu MAMA yake badala ya mkalimani wake!

Badiliko Kubwa Sana Kwangu

Kwa kibali cha mume wangu, Spencer alipofikia umri wa miaka mitatu, nilimwandikisha katika programu ya watoto viziwi na walio na ugumu wa kusikia iliyokuwa katika shule moja ya umma. Mikutano ya vikundi iliandaliwa ili kuwaelimisha wazazi, na nilijifaidi na nafasi hii kujifunza zaidi. Katika mkutano mmojawapo kikundi cha wasemaji kilichoundwa na viziwi walio na umri mkubwa na matineja kilihutubia kikundi. Wasemaji walieleza kwamba walikuwa na mawasiliano kidogo au walikosa kabisa mawasiliano na wazazi au familia zao. Nilipowauliza kwa nini, walijibu kwamba wazazi wao hawakupata kujifunza lugha ya ishara, hivyo hawakuweza kamwe kuzungumza kikamili na wazazi wao kuhusu maisha, hisia zao, au mapendezi yao. Ilionekana kwamba hawakujisikia kuwa sehemu ya familia zao.

Hili lilikuwa badiliko kubwa sana kwangu. Nilimfikiria mwana wangu. Sikuweza kuvumilia kufikiria akikua bila kuwa na uhusiano kamwe na wazazi wake. Niliazimia kuliko wakati mwingine wowote kuendelea kukuza stadi zangu katika lugha ya ishara. Kadiri wakati ulivyopita, ndivyo nilivyozidi kutambua kwamba uamuzi wa kutumia lugha ya ishara ulikuwa bora kwa upande wetu. Lugha yake ya ishara iliendelea kukua, na tungeweza kuzungumza jambo lolote, kama vile, “Tutaenda wapi wakati wa likizo?” au “Utakapokuwa mkubwa, ungependa kufanya kazi gani?” Nilitambua jinsi ningekosa mambo mengi kama ningejaribu kutegemea mawasiliano ya mdomo.

Alipokuwa na umri wa miaka mitano, Spencer aliwekwa katika masomo ya kawaida ya shule akiwa na watoto wanaosikia na mwalimu ambaye alijua kutoa ishara. Alidumu na programu hii kwa miaka mitatu ambayo ilikuwa mingi sana kwetu. Alichukia shule, na haikuwa rahisi kumwona akipitia magumu makubwa kama hayo. Kwa uzuri, niliweza kuwasiliana naye kadiri tulivyojaribu njia tofauti za kukabiliana na kukata tamaa kwake. Lakini, mwishowe, niliamua kwamba programu kama hii katika shule ya umma haikuwa nzuri kwa hadhi yake binafsi au kwa maendeleo yake ya kielimu.

Katika mwaka 1989 ndoa yangu ilivunjika. Sasa nilikuwa mzazi mmoja wa mwana aliye na umri wa miaka sita ambaye uwezo wake wa lugha ya ishara ulikuwa unaongezeka haraka. Ingawa niliweza kuwasiliana naye, nilijua nilihitaji kukuza stadi zangu katika ASL ili kudumisha na kuimarisha mawasiliano kati yetu.

Wakati wa Kuhama

Nilichunguza programu kadhaa kwa ajili ya watoto viziwi katika majimbo kadhaa na niligundua shule moja katika Massachusetts ambapo ASL na Kiingereza kilitumiwa katika ule uliofikiriwa kuwa mfikio wa lugha mbili. Kwa kuongezea, niliambiwa kwamba karibuni kungekuwa na kutaniko la ASL la Mashahidi wa Yehova katika eneo la Boston, na rafiki yangu mmoja alipendekeza tuhamie huko. Nikiwa mzazi mmoja, wazo la kuhama nyumbani kwetu na familia na marafiki katika eneo la mashambani la New Hampshire kwenda katika eneo la mji lilikuwa gumu kulikubali. Spencer pia alifurahia kuishi mashambani. Hata hivyo, kulikuwa na mambo mawili ambayo nilipaswa kuyafikiria. Spencer alipaswa kuwa katika shule ambayo walimu na wanafunzi wote wangewasiliana kwa uhuru katika lugha ya ishara, na nilihisi ingekuwa bora kuwa katika kutaniko pamoja na Mashahidi viziwi.

Tulihama miaka minne iliyopita, Spencer alipokuwa na umri wa miaka tisa. Muda mfupi baadaye, Kutaniko la Lugha ya Ishara katika Malden, Massachusetts, lilianzishwa, na tangu wakati huo, Spencer amefanya maendeleo makubwa sana. Tabia yake imekuwa bora zaidi, naye hufurahia kuwapo katika mikutano. Napata shangwe sana kumwona akiwasiliana na kufanya urafiki na wengine. Ndugu na dada viziwi katika kutaniko ni mifano ya kuigwa kwelikweli kwa mwana wangu, wakimsaidia atambue kwamba yeye pia aweza kufikia miradi ya kiroho. Na amefanya hivyo. Sasa yeye hutoa hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na anatumikia akiwa mhubiri asiyebatizwa. Ameonyesha tamaa yake ya kutaka kubatizwa.

Nina furaha kama nini katika huduma, kumwona akieleza imani yake kwa viziwi wengine, katika lugha ya ishara! Kujiheshimu kwake kumekua sana. Spencer ameniambia jinsi anavyohisi kuhusu kutaniko. Alisema: “Twapaswa kuwa hapa. Ndugu na dada waweza kuwasiliana nami.” Mwana wangu hanisihi tena tuondoke mara tu baada ya mikutano. Sasa ninalazimika kumwambia ni wakati wa kuondoka Jumba la Ufalme!

Katika shule yake ya sasa, Spencer aweza kuwasiliana kwa urahisi na watoto wengine viziwi. Mazungumzo yake pamoja nao yamemsaidia kuona tofauti kati ya maoni ya ulimwengu kuelekea watoto na maoni ya Yehova kuwaelekea. Spencer nami huwasiliana kwa uhuru na kuwa na uhusiano wa karibu, kulingana na kanuni za Biblia. Arudipo nyumbani alasiri, sisi hufanya mgawo wake wa masomo ya nyumbani pamoja. Sisi huenda katika mikutano yetu na katika huduma ya nyumba hadi nyumba pamoja. Lakini, Spencer aweza kuona kwamba si watoto wote shuleni ambao wana uhusiano huu wa ukaribu na wazazi wao.—Wakolosai 3:20, 21.

“Twaweza Kuongea Jambo Lolote”

Karibu mwaka mmoja uliopita, niligundua Spencer akiniangalia kana kwamba alitaka kuniambia jambo fulani. Nilimuuliza ikiwa alihitaji kitu chochote. “Hapana,” alijibu. Nilimuuliza maswali machache jinsi kila kitu kilivyokuwa shuleni na kadhalika. Nilitambua kwamba kulikuwa na kitu fulani alitaka kuniambia. Kisha, wakati wa funzo letu la jamaa la Mnara wa Mlinzi, alisema, “Je, ulijua kwamba baadhi ya wazazi wa wanafunzi katika shule yetu hawajui lugha ya ishara?” Nilimtazama kwa mshangao. “Kweli nakuambia,” alisema. “Kuna wazazi ambao hawawezi kuwasiliana na watoto wao.” Alieleza kwamba baadhi ya wazazi walikuwa wametembelea shule hiyo na kwamba amewaona katika jitihada ya kuwasiliana na watoto wao, wakiashiria kwa mikono na kuigiza mambo yale waliyokuwa wanataka kusema. “Nina pendeleo sana kwamba ulijifunza lugha ya ishara. Twaweza kuwasiliana. Wewe hutoi ishara tu za mkono; twaweza kuongea jambo lolote.”

Hili liligusa moyo wangu kama nini! Wengi wetu hatuthamini jitihada za wazazi wetu mpaka tukuapo. Lakini ona, akiwa na umri wa miaka 12, mwana wangu alikuwa akinieleza jinsi alivyokuwa mwenye shukrani kwamba twaweza kufurahia mawasiliano yenye maana.

Mmojawapo miradi yangu nikiwa mama ilikuwa kuwa na uhusiano mzuri na mwana wangu na kuwa karibu naye. Hilo labda lisingetokea ikiwa nisingejifunza lugha ya ishara. Wakfu wangu kwa Yehova umenisukuma kufikiria kwa uzito wajibu wangu nikiwa mzazi; huo ulifanya kuwe rahisi kufanya maamuzi muhimu. Sote wawili tumefaidika kiroho kwa sababu ya tokeo la maamuzi haya. Ni muhimu jinsi gani maneno katika Kumbukumbu la Torati 6:7, ambapo wazazi wanaamriwa kuwasilisha amri za Yehova kwa watoto wao ‘waketipo katika nyumba zao, na watembeapo njiani, na walalapo na waondokapo.’ Mimi ni mwenye shukrani sana kwamba Spencer na mimi twaweza kuwasiliana kwa uhuru kuhusu “matendo makuu ya Mungu.” (Matendo 2:11)—Kama ilivyosimuliwa na Cindy Adams.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

‘Sikuweza kuvumilia kufikiria akikua bila kuwa na uhusiano kamwe na wazazi wake’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki