-
“Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
Wakati wa kipindi hicho cha harara ya utukuzo wa taifa, kongamano la makasisi lilifanywa jijini Philadelphia, katika Marekani, ambamo azimio lilipitishwa likiomba Sheria ya Ujasusi ipitiwe tena ili wakiukaji wanaoshtakiwa wajaribiwe katika mahakama ya kijeshi na kupewa adhabu ya kifo. John Lord O’Brian katibu wa pekee wa mkuu wa sheria kwa kazi ya vita, aliteuliwa kuwasilisha jambo hilo katika Bunge. Rais wa Marekani hakuruhusu mswada huo uwe sheria. Lakini Meja-Jenerali James Franklin Bell, wa jeshi la Marekani, akiwa ameghadhibika sana aliwaambia J. F. Rutherford na W. E. Van Amburgh yale yaliyokuwa yametukia kwenye kongamano hilo na kusudi la kutumia mswada huo dhidi ya maofisa wa Watch Tower Society.
Faili rasmi za serikali ya Marekani zinaonyesha kwamba angalau kuanzia Februari 21, 1918, na kuendelea, John Lord O’Brian, alihusika binafsi katika jitihada za kufanya mashtaka dhidi ya Wanafunzi wa Biblia. Rekodi ya Bunge ya Aprili 24 na Mei 4 ina hati kutoka kwa John Lord O’Brian ambayo alitoa hoja kwa nguvu kwamba ikiwa sheria iliruhusu kusemwa kwa “yale yaliyo ya kweli, kwa makusudi mema, na kwa njia zinazofaa,” kama ilivyosemwa katika ile iliyoitwa eti Sahihisho la Sheria ya Ujasusi ya Ufaransa na kama vile ilivyokuwa imekubaliwa na Bunge la Marekani, hangeweza kuwashtaki Wanafunzi wa Biblia kwa kufanikiwa.
Katika Worcester, Massachusetts, “Mwadhama” B. F. Wyland alitumia harara ya vita kwa faida yake kwa kudai kwamba Wanafunzi wa Biblia walikuwa wakiendeleza propaganda ya adui. Alichapa makala moja katika Daily Telegram ambayo alijulisha: “Mojawapo kazi za uzalendo zinazowakabili nyinyi mkiwa wananchi ni kulikandamiza Shirika la Kimataifa la Wanafunzi wa Biblia, lenye makao makuu katika Brooklyn. Chini ya kisitiri cha dini, wamekuwa wakiendeleza propaganda ya Ujerumani katika Worcester kwa kuuza kitabu chao, ‘The Finished Mystery.’” Aliwaambia wenye mamlaka waziwazi kwamba ilikuwa kazi yao kuwakamata Wanafunzi wa Biblia na kuwazuia wasifanye mikutano zaidi.
Kulikuwa na mnyanyaso wenye kuenea wa Wanafunzi wa Biblia katika masika na kiangazi cha 1918, katika Amerika Kaskazini na Ulaya pia. Miongoni mwa wachochezi mlikuwamo makasisi wa Baptisti, Methodisti, Episkopali, Luther, Katoliki ya Roma, na makanisa mengineyo. Fasihi za Biblia zilitwaliwa na maofisa bila hati ya upekuzi, na Wanafunzi wa Biblia wengi wakatiwa gerezani. Wengine walifukuzwa na wafanyaghasia, wakapigwa, wakachapwa mijeledi, wakamwagiwa lami na manyoya, au wakavunjwa mbavu au kukatwa vichwa. Wengine walilemazwa kabisa. Wanaume na wanawake Wakristo walitiwa gerezani bila kushtakiwa au bila kuhukumiwa. Visa hususa zaidi ya mia moja vya kutendwa kikatili viliripotiwa katika The Golden Age la Septemba 29, 1920.
Washtakiwa kwa Ujasusi
Kilele kilifikiwa Mei 7, 1918, wakati waranti za serikali zilipotolewa katika Marekani za kumkamata J. F. Rutherford, msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society, na washiriki wake wa karibu.
Siku iliyotangulia, mashtaka mawili yalikuwa yamefanywa dhidi ya Ndugu Rutherford na washiriki wake, katika Brooklyn, New York. Kama matokeo yaliyotakwa hayakupatikana katika kesi moja, shtaka lile jingine lingefuatiliwa. Shtaka la kwanza, lililofanywa dhidi ya idadi kubwa zaidi ya watu, lilitia ndani mashtaka manne: Mawili yaliwashtaki kwa kufanya shauri ili kukiuka Sheria ya Ujasusi ya Juni 15, 1917; na mengine mawili yaliwashtaki kwa kujaribu kufanya mipango isiyo halali au kufanya hivyo hasa. Ilidaiwa kwamba walikuwa wanafanya shauri ili kuleta maasi na kukataa kazi ya uanajeshi katika Marekani na kwamba walikuwa wanafanya shauri kuzuia kusajiliwa na kuandikishwa kwa watu kwa ajili ya utumishi huo taifa lilipokuwa vitani, pia kwamba walikuwa wamejaribu kufanya au walikuwa hasa wamefanya mambo hayo yote mawili. Shtaka lilitaja kihususa kuchapwa na kugawanywa kwa kitabu The Finished Mystery. Shtaka la pili lilionyesha kwamba kule kupelekwa kwa hundi hadi Ulaya (ambayo ingetumiwa kwa kazi ya elimu ya Biblia katika Ujerumani) kuwa ni tisho kwa masilahi ya Marekani. Wakati washtakiwa walipopelekwa mahakamani, lile shtaka la kwanza, lenye mashtaka manne, ndilo lilifuatiwa.
Shtaka jingine la C. J. Woodworth na J. F. Rutherford chini ya Sheria ya Ujasusi lilikuwako katika Scranton, Pennsylvania. Lakini, kulingana na barua kutoka kwa John Lord O’Brian ya tarehe Mei 20, 1918, washiriki wa Idara ya Sheria walihofu kwamba Hakimu Witmer wa Wilaya ya Marekani, ambaye angeamua mashtaka, hangekubali utumizi wao wa Sheria ya Ujasusi ili kukandamiza utendaji wa watu ambao, kwa sababu ya masadikisho ya kidini yaliyo manyoofu, walisema mambo ambayo wengine wangeyaona kuwa propaganda ya kupinga vita. Kwa hiyo Idara ya Sheria iliikawiza kesi ya Scranton, ikingoja matokeo ya kesi ya Brooklyn. Serikali pia iliongoza mambo hivi kwamba Hakimu Harland B. Howe, kutoka Vermont, ambaye John Lord O’Brian alijua alikubaliana na maoni yake katika mambo kama hayo, angekuwa mwamuzi wa kesi katika Mahakama ya Wilaya ya Marekani kwa Wilaya ya Mashariki ya New York. Kesi ilianza Juni 5, washtaki wakiwa Isaac R. Oeland na Charles J. Buchner wa Katoliki ya Roma. Wakati kesi ilipokuwa ikiendelea, kama vile Ndugu Rutherford alivyoona, mapadri Wakatoliki walishauriana mara kwa mara na Buchner na Oeland.
Kadiri kesi ilivyoendelea, ilionyeshwa kwamba maofisa wa Sosaiti na watungaji wa kile kitabu hawakuwa na madhumuni ya kuingilia shughuli za vita za nchi. Ushahidi uliotolewa wakati wa mashtaka ulionyesha kwamba mipango kwa ajili ya kuandikwa kwa kitabu hicho—kwa kweli, uandishi wa sehemu kubwa ya kitabu hicho—ulikuwa umefanywa kabla ya Marekani kutangaza vita (Aprili 6, 1917) na kwamba maafikiano ya kwanza ya kukichapa yalikuwa yametiwa sahihi kabla ya Marekani kupitisha sheria (mnamo Juni 15) ambayo ilisemwa walikuwa wamekiuka.
Mashtaka yalikazia nyongeza kwenye kitabu hicho iliyofanywa wakati wa Aprili na Juni wa 1917, katika shughuli za kutayarisha nakala na kusoma zile zilizokamilishwa. Hiyo ilitia ndani nukuu kutoka kwa John Haynes Holmes, kasisi aliyekuwa amejulisha kwa nguvu kwamba vita ilikuwa kukiuka Ukristo. Kama ilivyoonyeshwa na mmojawapo mawakili watetezi, maelezo hayo ya kasisi, yaliyochapwa katika kitabu chenye kichwa A Statement to My People on the Eve of War, kilikuwa bado kikiuzwa katika Marekani wakati wa kesi hiyo. Wala kasisi huyo wala mchapaji wacho hawakushtakiwa. Lakini Wanafunzi wa Biblia waliorejezea hotuba yake ndio walioshtakiwa kwa mambo yaliyosemwa ndani yacho.
Kitabu The Finished Mystery hakikuwaambia watu wa ulimwengu kwamba hawakuwa na haki ya kushiriki vitani. Lakini, katika kueleza unabii, kilinukuu madondoo kutoka matoleo ya The Watch Tower la 1915 ili kuonyesha kutopatana kwa makasisi waliodai kuwa wahudumu wa Kristo lakini walikuwa wakitenda wakiwa wajumbe wa kuandikisha majeshi ya mataifa yaliyo vitani.
Ilipofahamika kwamba serikali ilipinga kitabu hicho, Ndugu Rutherford alikuwa amepeleka telegramu mara hiyo kwa mchapaji ili aache kukitokeza, na wakati uleule, mwakilishi wa Sosaiti alikuwa ametumwa kwenye idara ya upelelezi ya Jeshi la Marekani ili kujua sababu ya wao kukipinga. Ilipojulikana kwamba kwa sababu ya vita iliyokuwa ikiendelea, kurasa 247-253 za kitabu hicho zilionwa kuwa zisizofaa, Sosaiti ilielekeza kwamba kurasa hizo ziondolewe katika nakala zote za kitabu hicho kabla ya umma kupewa. Na wakati serikali ilipojulisha mawakili wa wilaya kwamba kugawanywa kwacho zaidi kungekuwa ni kukiuka Sheria ya Ujasusi (ingawa serikali ilikataa kutoa maoni kwa Sosaiti juu ya kitabu hicho kikiwa kimebadilishwa), Sosaiti ilielekeza kwamba kugawanywa kote kwa kitabu hicho kwa umma kukomeshwe.
Kwa Nini Hukumu Kali Jinsi Hiyo?
Kujapokuwa na yote hayo, katika Juni 20, 1918, wasaidizi wa hakimu walifanya uamuzi na wakampata kila mshtakiwa kuwa na kosa kwa kila shtaka. Siku iliyofuata, sabab kati yao walihukumiwa vifungo vinne vya miaka 20 kila moja, vinavyotumika pamoja. Julai 10, yule wa nanec alihukumiwa vipindi vinne vyenye kutumika pamoja vya miaka 10. Hukumu hiyo ilikuwa kali jinsi gani? Katika barua kwa mkuu wa sheria katika Machi 12, 1919, rais wa Marekani Woodrow Wilson alikiri kwamba “vifungo hivyo kwa wazi vinapita kiasi.” Kwa kweli, yule mtu aliyefyatua risasi katika Sarajevo ambazo zilimwua maliki mwana-mfalme wa Milki ya Austria na Hungaria—jambo lililochochea matukio yaliyoingiza mataifa katika Vita ya Ulimwengu 1—hakuwa amepata hukumu kali jinsi hiyo. Hukumu yake ilikuwa miaka 20 gerezani—si vifungo vinne vya miaka 20, kama ilivyokuwa kwa Wanafunzi wa Biblia!
Ni nini kilichochea kuwekwa kwa vifungo hivyo vikali vya Wanafunzi wa Biblia? Hakimu Harland B. Howe alijulisha: “Kwa maoni ya Mahakama, propaganda ya kidini ambayo washtakiwa hawa wametetea kwa bidii na kuieneza kotekote katika taifa na miongoni mwa mataifa rafiki, ni hatari kubwa zaidi ya kikosi kimoja cha Jeshi la Ujerumani. . . . Mtu anayehubiri dini mara nyingi huwa na uvutano mwingi, na ikiwa ni mnyoofu, yeye ni mwenye matokeo hata zaidi. Hilo linazidisha badala ya kupunguza kosa walilofanya. Kwa hiyo, likiwa jambo lifaalo zaidi kufanyia watu kama hao, Mahakama imekata kauli kwamba hukumu lazima iwe kali.” Hata hivyo, inastahili kuangaliwa pia kwamba kabla ya kupitisha hukumu, Hakimu Howe alisema kwamba taarifa zilizotolewa na mawakili wa washtakiwa zilikuwa zimetia shuku na kutendea isivyofaa si maofisa wa sheria wa serikali tu bali pia “wahudumu wote wa kidini kotekote nchini.”
Baada ya uamuzi huo, rufani ilikatwa mara hiyo kwa mahakama ya mzunguko ya rufani ya Marekani. Lakini Hakimu Howe alikataa kuwaachilia kwa dhamana wakisubiri kusikizwa kwa rufani hiyo,d na katika Julai 4, kabla ya rufani ya tatu iliyokuwa ya mwisho ya kupata dhamana kusikizwa, ndugu saba wa kwanza walihamishwa upesi wakapelekwa kwenye gereza la kitaifa la Atlanta, Georgia. Baada ya hapo, ilidhihirishwa kwamba kulikuwa na makosa 130 ya kimahakama katika hukumu hiyo yenye kupendelea upande mmoja sana. Kazi ya miezi mingi ilifanywa ili kutayarisha karatasi zilizotakikana katika kusikizwa kwa rufani. Wakati uo huo, vita ilikwisha. Mnamo Februari 19, 1919, ndugu wanane walio gerezani walipeleka rufani ili wahurumiwe rasmi na rais wa Marekani, Woodrow Wilson. Barua nyinginezo zilizohimiza kuachiliwa kwa ndugu hao zilipelekwa na wananchi wengi kwa mkuu wa sheria mpya. Kisha, mnamo Machi 1, 1919, katika kujibu maulizo ya mkuu wa sheria, Hakimu Howe alipendekeza “kubadilishwa mara hiyo” kwa hukumu hiyo. Ingawa hilo lingepunguza hukumu, pia lingethibitisha kosa la washtakiwa. Kabla ya hilo kufanywa, mawakili wa akina ndugu walimpelekea wakili mkuu wa Marekani agizo la mahakama lililoleta kesi hiyo mbele ya mahakama ya rufani.
Miezi tisa baada ya Rutherford na washiriki wake kuhukumiwa—na vita ikiwa imekwisha—Machi 21, 1919, mahakama ya rufani iliagiza washtakiwa wote wanane wapate dhamana, na Machi 26, waliachiliwa katika Brooklyn kwa dhamana ya dola 10,000 kila mmoja. Katika Mei 14, 1919, mahakama ya mzunguko ya Marekani ya rufani katika New York ilikata kauli: “Washtakiwa katika kesi hii hawakupewa hukumu ya kiasi na isiyopendelea upande wowote ambayo walistahili kupewa, na kwa sababu hiyo hukumu hiyo imebatilishwa.” Kesi hiyo iliahirishwa ili ifanywe upya. Hata hivyo, Mei 5, 1920, baada ya washtakiwa kuja mahakamani, baada ya kupewa samansi, wakili wa serikali katika mahakama ya wazi katika Brooklyn, alitangaza mara tano kuondolewa kwa mashtaka.e Kwa nini? Kama ilivyofunuliwa na barua zilizohifadhiwa katika Jumba la Hati za Kitaifa la Marekani, Idara ya Sheria ilihofu kwamba ikiwa masuala hayo yangepelekwa mbele ya wasaidizi wa hakimu wasiopendelea upande wowote, huku harara ya vita ikiwa imekwisha, wangeshindwa kesi hiyo. Wakili wa Marekani aitwaye L. W. Ross alisema katika barua kwa mkuu wa sheria: “Ninafikiri ingekuwa afadhali, kwa uhusiano wetu na umma, ikiwa kwa hiari yetu wenyewe” tungesema kwamba kesi imefungwa.
Siku iyo hiyo, Mei 5, 1920, shtaka lile jingine lililokuwa limefanywa katika Mei 1918 dhidi ya J. F. Rutherford na wanne kati ya washirika wake lilifutiliwa mbali pia.
Ni Nani kwa Kweli Aliyeyachochea?
Je, yote hayo kwa kweli yalichochewa na makasisi? John Lord O’Brian alikana hilo. Lakini mambo ya hakika yalijulikana vema na wale walioishi wakati huo. Katika Machi 22, 1919, gazeti lililochapwa katika Girard, Kansas liitwalo Appeal to Reason, liliteta hivi: “Wafuasi wa Pasta Russell, Wakifuatiwa na Ukorofi wa Makasisi wa ‘Orthodoksi,’ Walihukumiwa na Kufungwa Bila Dhamana, Ingawa Walifanya Kila Jitihada Iliyowezekana ili Kushikamana na Masharti ya Sheria ya Ujasusi. . . . Tunajulisha kwamba, hata iwe au isiwe kwamba Sheria ya Ujasusi ilikuwa ya kikatiba kikweli au inayofaa kiadili, wafuasi hao wa Pasta Russell walihukumiwa isivyo haki chini ya masharti yayo. Uchunguzi wa akili iliyofunguka wa ithibati utamsadikisha yeyote upesi kwamba watu hao si kwamba tu hawakuwa na kusudi la kukiuka sheria, bali pia hawakuikiuka.”
Miaka mingi baadaye, katika kitabu Preachers Present Arms, Dakt. Ray Abrams alionelea hivi: “Ni jambo lenye kutokeza kwamba makasisi wengi walishiriki sehemu ya uchochezi katika kujaribu kuwaondolea mbali Warusselli [kama vile Wanafunzi wa Biblia walivyoitwa kwa dharau]. Mizozo ya kidini na chuki za muda mrefu, ambazo hazikushughulikiwa kwa vyovyote mahakamani katika wakati wa amani, sasa zilifika mahakamani chini ya uvutano wa harara ya wakati wa vita.” Yeye pia alisema: “Uchanganuzi wa kesi yote huongoza kwenye mkataa kwamba hapo awali makanisa na makasisi walichochea harakati ya kuwafutilia mbali Warusselli.”—Kur. 183-185.
-
-
“Vitu vya Kuchukiwa na Mataifa Yote”Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 655]
Makasisi Waonyesha Hisia Zao
Maitikio ya magazeti ya kidini baada ya kuhukumiwa kwa J. F. Rutherford na washiriki wake mwaka 1918 yanastahili kuangaliwa:
◆ “The Christian Register”: “Kile ambacho Serikali hapa inashambulia moja kwa moja kwa njia ya kufisha ni ile dhana kwamba mawazo ya kidini, hata yawe ya kichaa na yenye kudhuru jinsi gani, yanaweza kuenezwa bila hofu ya kuadhibiwa. Dhana hiyo ni uwongo wa kale, na kufikia sasa hatujakuwa waangalifu sana kulihusu. . . . Hukumu hiyo inaonekana kuwa ndiyo mwisho wa Urusselli.”
◆ “The Western Recorder,” kichapo cha Baptisti, kilisema: “Haishangazi kwamba kiongozi wa kidhehebu hicho chenye ukaidi amefungiwa katika mojawapo ya vituo vya watu wakaidi. . . . Tatizo lenye kutatanisha kwelikweli kuhusiana na jambo hilo ni ikiwa washtakiwa wangepaswa wapelekwe kwenye makao ya wenye kichaa au kwenye gereza.”
◆ “The Fortnightly Review” lilielekeza fikira kwenye maelezo katika gazeti la New York “Evening Post,” ambalo lilisema: “Tunatumaini kwamba walimu wa dini kila mahali wataona maoni ya hakimu huyu kwamba kufunza dini yoyote isipokuwa ile ambayo inapatana kabisa na sheria zilizowekwa ni hatia kubwa ambayo inafanywa kuwa kubwa zaidi, ikiwa wewe ukiwa mhudumu wa gospeli, ungali mnyoofu.”
◆ “The Continent” kwa kuwashushia heshima liliwaonyesha washtakiwa kuwa “wafuasi wa ‘Pasta’ Russell aliyekufa” na likapotoa imani zao kwa kusema kwamba waliunga mkono “kwamba watu wote wanapaswa wasipelekwe kupigana na kaiser wa Ujerumani isipokuwa wale wenye dhambi.” Lilidai kwamba kulingana na wakili mkuu katika Washington, “muda fulani uliopita serikali ya Italia ililalamikia Marekani kwamba Rutherford na washiriki wake . . . walikuwa wameeneza kiasi fulani cha propaganda ya kupinga vita katika majeshi ya Italia.”
◆ Juma moja baadaye, “The Christian Century” lilichapa sehemu kubwa ya habari iliyo juu neno kwa neno, ikionyesha kwamba walikubaliana nayo kabisa.
◆ Gazeti la Katoliki “Truth” liliripoti kifupi ile hukumu waliyopewa na kisha likaeleza hisi za wahariri walo, likisema: “Fasihi za shirika hilo zimejaa mashambulizi makali sana juu ya Kanisa Katoliki na upadri walo.” Ili kujaribu kuweka kibandiko cha “uasi” juu ya yeyote ambaye huenda akapinga hadharani maoni ya Kanisa Katoliki, liliongezea hivi: “Inazidi kuwa wazi kwamba roho ya kutovumilia inafungamanishwa kwa ukaribu na ile ya uasi.”
◆ Dakt. Ray Abrams, katika kitabu chake “Preachers Present Arms,” alionelea hivi: “Wakati habari za hukumu ya vifungo hivyo vya miaka ishirini zilipofikia wahariri wa magazeti ya kidini, karibu kila kimoja cha vichapo hivyo, kikubwa na kidogo, kilishangilia tukio hilo. Mimi nimeshindwa kupata maneno yoyote ya masikitiko katika yoyote ya majarida ya kidini yanayokubaliwa.”
-