-
Misaada Yatolewa Kotekote DunianiAmkeni!—2001 | Julai 22
-
-
Misaada Yatolewa Kotekote Duniani
BAXTER, mwanafunzi wa shule ya sekondari mwenye umri wa miaka 15, anafanya jambo lisilo la kawaida kila Jumamosi alasiri. Huwa anatembelea kikundi cha wazee kwenye makao yao, na kupiga muziki na kuimba pamoja nao. Mwalimu wa Baxter asema hivi: “Yeye huwachekesha wakazi hao, na kuwaletea burudani na furaha ya maisha.” Lucille, aliye na umri wa miaka 78, anafanya matendo mema kama ya Baxter. Yeye huwagawia wenye uhitaji chakula na kuwatembelea wagonjwa walio wapweke hospitalini. Rafiki mmoja wa Lucille asema hivi juu yake: “Ikiwa kuna mtu mwenye uhitaji na yeye anaweza kusaidia, atakwenda kumsaidia.”
Maana ya Kujitolea
Mamilioni ya watu kotekote duniani wana mtazamo huu—‘Niko tayari kusaidia wakati wa uhitaji.’ Wanasaidia kwenye ujenzi na ofisi mbalimbali, viwanda, makao ya wazee, hospitali za wagonjwa wenye magonjwa yasiyotibika, kambi za wakimbizi, mahali ambapo wasio na makao hutunzwa kwa muda, idara za zimamoto, vituo vya kutoa ushauri, sehemu za kutunzia wanyama waliopotea au wasio na wenyewe, na penginepo. Wako kila mahali! Wanatumia stadi zao katika shughuli tofauti-tofauti kama vile kujenga vibanda, kuchangisha pesa, kukumbatia watoto wachanga walioachwa, na kufariji wale wenye magonjwa yasiyotibika. Wale wanaofanya matendo hayo ni wafanyakazi wa kujitolea—watu wanaofaidi sana wale wenye uhitaji.
Kazi ya kujitolea imefafanuliwa kuwa “tendo linalochochewa na roho isiyo na ubinafsi.” Hiyo yatia ndani mambo kama kujihusisha kutetea haki fulani, roho ya kujidhabihu, kutotarajia malipo, na kufikiria hali bora ya watu wengine. Watu wawili ambao wamefanya kazi ya kujitolea kwa muda mrefu wasema hivi: “Tunajitoa wenyewe: tunatoa wakati wetu, mikono na miguu yetu, mawazo yetu, uwezo wetu wa kusaidia mtu mwingine, ustadi wetu wa kutatua matatizo na stadi zetu za kazi.” Jambo la kufurahisha ni kwamba, kujitoa kwa aina hiyo hunufaisha wale wanaojitolea pia.—Soma sanduku “Wanaojitolea Wanafaidika Pia.”
Wafanyakazi wa Kujitolea Waongezeka Huku Uhitaji Ukizidi
Huko Marekani, watu milioni 100 hufanya kazi ya kujitolea—na idadi yao inaongezeka. Hivi majuzi, Kathleen Behrens, aliye mkurugenzi mtendaji wa shirika la wafanyakazi wa kujitolea linaloitwa New York Cares (New York Hujali), alimweleza mwandishi wa Amkeni! hivi: ‘Shirika letu huongezeka kwa haraka sana. Mwaka uliopita watu wapya 5,000 walijiunga na programu yetu.” Wafanyakazi wa kujitolea huko Ulaya wanaongezeka vivyo hivyo. Kwa mfano, idadi yao imekuwa ikiongezeka kwa asilimia 6 kila mwaka katika kipindi cha miaka 20 iliyopita nchini Ufaransa. Hata hivyo, wafanyakazi wa kujitolea wengi zaidi wanahitajika. Wakala la Wafanyakazi wa Kujitolea wa Umoja wa Mataifa lasema kwamba, “kuna uhitaji mkubwa wa watu wanaojitolea kufanya kazi leo kuliko wakati wowote mwingine” kotekote duniani. Msimamizi wa jumba moja la ukumbusho asema hivi: “Hatungeweza kuendesha shughuli za jumba hili la ukumbusho endapo watu wasingejitolea kusaidia kazi.”
Hata hivyo, jambo moja linashangaza. Ijapokuwa wakurugenzi, mameneja, na wasimamizi wengi wanahisi kwamba wafanyakazi waliojitolea ni watu wa “maana sana,” bado hawaonyeshi uthamini kwa kazi wanayofanya. Ili kubadili hali hiyo, shirika la Umoja wa Mataifa liliamua kutilia mkazo umuhimu wa wafanyakazi wa kujitolea katika mwaka huu wa 2001. Sanduku “Mwaka wa Kimataifa wa Wafanyakazi wa Kujitolea” laonyesha malengo mbalimbali ambayo shirika la Umoja wa Mataifa latazamia kutimiza.
Kwa sasa, mabadiliko mengi yanayotokea ni mwito wa ushindani kwa wafanyakazi wa kujitolea na wale wanaoongoza kazi yao. Hata hivyo, bado kuna watu wengi ulimwenguni walio tayari kujitolea kusaidia wengine. Wanasukumwa na nini kufanya hivyo? Wana matokeo gani? Na wanaweza kubadilije maisha yako?
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 4]
Wanaojitolea Wanafaidika Pia
Michael anayefanya kazi ya kujitolea mara kwa mara asema hivi: “Kujitolea ili kuwasaidia wengine kumeniridhisha kwelikweli kwa njia ambayo singaliweza kuridhishwa ikiwa ningalifanya kazi yangu ya biashara tu.” Si Michael pekee anayehisi hivyo. Sharon Capeling-Alakija aliye mratibu mtendaji wa wakala la Wafanyakazi wa Kujitolea wa Umoja wa Mataifa, asema hivi: “Kotekote duniani watu ambao . . . wanajitolea wanatambua kabisa jinsi wanavyofaidika kwa kufanya kazi hiyo.” Dakt. Douglas M. Lawson, aliye mtaalamu wa kazi ya kujitolea, anasema kwamba watafiti wameona kwamba “mara nyingi kufanya kazi ya kujitolea kwa muda wa saa chache tu hufanya mwenendo wa mtu na hali yake ya akili ziboreke sana, hivi kwamba hali hiyo imeitwa ‘Raha ya Aliyejitolea.’” Na hiyo “raha ya aliyejitolea” si ya muda tu. Watafiti kwenye Chuo Kikuu cha Cornell huko Marekani walichunguza kikundi cha watu kwa muda wa zaidi ya miaka 30 na wakapata kwamba “wale waliojitolea walikuwa wenye furaha na afya nzuri kuliko wale wasiojitolea.” Kwa kupendeza, Biblia yasema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35; Mithali 11:25.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]
Mwaka wa Kimataifa wa Wafanyakazi wa Kujitolea
Katika Novemba 20, 1997, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilitangaza mwaka wa 2001 kuwa “Mwaka wa Kimataifa wa Wafanyakazi wa Kujitolea.” Shirika la Umoja wa Mataifa lataka malengo manne yatimizwe mwaka huu.
Kutoa shukrani Serikali zinahimizwa zitambue umuhimu wa wafanyakazi wa kujitolea kwa kuchunguza na kurekodi kile wanachotimiza na kutoa tuzo kwa utendaji wao bora.
Kutunga sheria zinazoendeleza kazi ya kujitolea Serikali zinahimizwa zichochee watu kujitolea, kwa mfano, kwa kukubali watu wafanye kazi ya kujitolea badala ya kufanya utumishi wa kijeshi au kuwapunguzia kodi fulani zinazotozwa na serikali.
Kutumia vyombo vya habari Vyombo vya habari vimekaribishwa kusaidia kuchapisha na kutangaza habari za miradi iliyofanikiwa ya kazi ya kujitolea. Kwa njia hiyo wengine wangeweza kuiga miradi hiyo iliyofanikiwa, na “jumuiya nyingine hazingehitaji kutumia muda mrefu na kujitahidi kuunda miradi yake yenyewe.”
Kutangaza faida zake Mashirika ya wafanyakazi wa kujitolea yanahimizwa yapange maonyesho ili kujulisha watu juu ya jinsi ambavyo jamii hunufaika kwa kazi ya kujitolea.
Shirika la Umoja wa Mataifa latumaini kwamba watu wengi zaidi watatiwa moyo kuomba msaada wa wale waliojitolea na watu wengi zaidi watajitolea kufanya kazi katika mwaka wa 2001, ambao ni Mwaka wa Kimataifa wa Wafanyakazi wa Kujitolea. Mbali na hayo, ili mashirika ya wafanyakazi wa kujitolea yaweze kushughulikia mahitaji yanayoongezeka ya jamii, mahali pengi zaidi pa kufanyia kazi huhitajika na vilevile fedha nyingi zaidi. Serikali 123 zimekubali kugharimia malengo ya azimio hilo la Umoja wa Mataifa.
-
-
Wafanyakazi wa Kujitolea KaziniAmkeni!—2001 | Julai 22
-
-
Wafanyakazi wa Kujitolea Kazini
KILA Ijumaa alasiri, Sirley, mwanamke wa makamo huko Brazili, hugeuza sebule yake kuwa darasa. Amélia, mmoja wa wanafunzi wake, huwasili saa nane hivi. Hakosi kamwe kufika na tayari anajua kusoma vizuri kuliko vijana wengi wa shule ya sekondari. Amélia ana umri wa miaka 82.
Amélia anafuata mfano wa wazee zaidi ya 60 ambao wamehitimu madarasa ambayo Sirley hufunza katika mji wa kwao bila malipo. Hivi majuzi, gazeti la Jornal do Sudoeste la Brazili lilikuwa na habari ya kindani juu ya kazi ya kujitolea ya Sirley. Baada ya kutaja kwamba “amesaidia sana watu wa jumuiya hii,” gazeti hilo lilisema kwamba njia ambayo Sirley hutumia kufundisha wazee ni yenye mafanikio hivi kwamba “baada ya kufundishwa kwa muda wa saa 120 tu, wanafunzi wanajua kuandika barua, kusoma magazeti, kufanya hesabu sahili, na kushughulikia mambo mengine ya kila siku.” Gazeti hilo laongeza kusema kwamba kitabu cha masomo ambacho Sirley hutumia darasani ni kijitabu kiitwacho Kujifunza Kusoma na Kuandika, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.a
Kuacha Kuaibika na Kuanza Maisha Yenye Heshima
Dona Luzia, mwanafunzi mwingine wa Sirley aliye na umri wa miaka 68, anaeleza kwamba kabla ya kujua kusoma na kuandika aliona haya kuongea na watu. Hata aliona vigumu kwenda dukani kununua vitu. “Sasa huwa ninawaandikia watu wa ukoo wanaoishi katika miji mingine barua, na ninashughulikia fedha zangu mwenyewe. Hakuna anayeweza kunidanganya tena kwa kunirudishia hela chache,” anasema akitabasamu. Maria, aliye na umri wa miaka 68 pia, akumbuka jinsi alivyokuwa akiaibika alipotia sahihi hundi ya malipo ya uzeeni kwa kuweka alama ya kidole-gumba. “Nilihisi kana kwamba nilikuwa mlemavu,” anasema. Lakini, sasa, kwa kuwa anajua kusoma na kuandika Maria anafurahia kutia sahihi kwa kuandika jina lake.
Wanafunzi na wahitimu wamesifu darasa ambalo Sirley hufunza bila malipo hivi kwamba sebule yake imekuwa ndogo. Hivi punde darasa hilo litahamishwa mahali pakubwa zaidi.
Programu Iliyotuzwa
Sirley ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Bila shaka unajua kwamba Mashahidi wa Yehova hujitolea kuwafundisha watu Biblia. Kuna wengi ambao wamefanikiwa kama Sirley. Watu zaidi ya 22,000 wamefundishwa kusoma na kuandika katika madarasa yanayofanywa katika mamia ya Majumba ya Ufalme kotekote nchini Brazili.
Madarasa kama hayo ya Mashahidi wa Yehova yamefanikiwa katika sehemu nyingine duniani vilevile. Kwa mfano, katika nchi ya Afrika ya Burundi, maofisa wa Idara ya Taifa ya Kufundisha Watu Wazima Kusoma na Kuandika (idara ya Wizara ya Elimu) walipendezwa sana na matokeo ya madarasa ya kusoma na kuandika ya Mashahidi hivi kwamba waliwapa walimu wanne tuzo kwa sababu ya “jitihada nyingi za kufundisha wengine kusoma.” Maofisa wa Serikali wanavutiwa hasa kuona kwamba asilimia 75 za wale waliojifunza kusoma na kuandika walikuwa wanawake—ambao kwa kawaida husitasita kuhudhuria madarasa kama hayo.
Wanafunzi 4,000 wanahudhuria madarasa ya kujifunza kusoma na kuandika ya Mashahidi nchini Msumbiji, na wanafunzi zaidi ya 5,000 wamejifunza kusoma na kuandika katika muda wa miaka minne iliyopita. Mhitimu mmoja aliandika hivi: “Ninataka kutoa shukrani zangu za moyoni. Ninajua kusoma na kuandika kwa sababu ya shule hiyo.”
Misaada Ambayo Ni “Halisi, Wala Si ya Kijuujuu Tu”
Kutoa msaada ni kazi nyingine ya kujitolea ambayo Mashahidi wa Yehova hufanya. Hivi majuzi, kulikuwa na shughuli nyingi katika bohari moja huko Paris, Ufaransa. Watu 400 hivi walijitolea kutumia mwisho-juma wao kufunga chakula, nguo, na dawa katika masanduku. Kufikia mwishoni mwa mwisho-juma huo, makontena tisa makubwa, yaliyojaa vitu hivyo vyenye thamani ya dola za Marekani milioni moja, yalikuwa tayari kusafirishwa. Muda mfupi baadaye, vitu hivyo vilifika nchi za Afrika ya Kati zilizokumbwa na vita, ambapo Mashahidi waliojitolea waliwagawia wenye uhitaji bila kuchelewa. Karibu vitu vyote vilichangwa na Mashahidi vilevile.
Gazeti moja la Kongo (Kinshasa) lilisifu misaada ambayo Mashahidi wa Yehova hutoa, kuwa misaada ambayo ni “halisi, wala si ya kijuujuu tu.” Maofisa wa Tume ya Umoja wa Mataifa Inayoshughulikia Wakimbizi (UNHCR) vilevile wamesifu jitihada hizo. Ofisa mmoja wa UNHCR huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo alivutiwa sana na jinsi Mashahidi walivyofanya kazi hiyo kwa utaratibu sana hivi kwamba aliwapa waliojitolea ruhusa ya kutumia gari lake. Wenyeji pia wanavutiwa. Watazamaji walipoona jinsi vifaa hivyo vilivyogawiwa wenye uhitaji bila kuchelewa, wengine waliuliza hivi kwa mshangao: “Nyinyi mna mpango gani unaowawezesha kuwafikia watu wote wenye uhitaji?”
Kutoa misaada na kufundisha watu kusoma na kuandika ni baadhi tu ya utumishi mbalimbali ambao Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakifanya kotekote duniani kwa miaka mingi. Hata hivyo, Mashahidi wanafanya kazi nyingine ya kujitolea pia—utumishi unaowaletea wengine faida ya kudumu. Sehemu inayofuata itazungumzia habari hiyo.
[Maelezo ya Chini]
a Kijitabu Kujifunza Kusoma na Kuandika (kimetafsiriwa katika lugha 6) na kijitabu kipya Jitahidi Kusoma na Kuandika (kimetafsiriwa katika lugha 29). Vyote viwili vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova. Ukitaka nakala yako ya bila malipo, nenda kwenye Jumba la Ufalme katika eneo lenu au uwaandikie wachapishaji wa gazeti hili.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6, 7]
Hali Inabadilika
Julie anajitahidi kujitolea mara kwa mara kufanya kazi mbalimbali—kwa muda wa saa chache au siku nzima—huku akisafiri kotekote duniani kwa ajili ya biashara yake. Hivi majuzi alipokuwa Amerika Kusini, alitumia alasiri moja kusaidia kazi kwenye makao ya mayatima karibu na Santiago, nchini Chile. Anasema kwamba safari zake humwezesha kujitolea kufanya ‘kazi nyingi tofauti-tofauti.’
Idadi ya watu wanaotoa wakati wao kusaidia wengine huzidi kuongezeka, lakini muda ambao wanatoa huzidi kuwa mfupi. Sara Meléndez, aliye msimamizi wa kikundi cha watafiti wanaokusanya habari kuhusu kazi ya kujitolea, asema hivi: ‘Huo ni mwelekeo mpya. Watu wanajitolea, lakini wanapofanya hivyo, wanajitolea ili watimize mradi mmoja tu kwa muda mfupi.’ Kwa hiyo, ni vigumu kwa wanaosimamia miradi mbalimbali kupata wafanyakazi wa kutosha, na wanalalamikia ‘upungufu wa wafanyakazi wa kujitolea,’ kwa miradi yao.
“Kujitolea Kulingana na Hali”
Baadhi ya wasimamizi wanahisi kwamba mwelekeo huo mpya—yaani, kujitolea kwa muda mfupi tu—husababishwa na mtazamo mpya kwa upande wa wale waliojitolea. Susan Ellis, aliye mshauri wa vikundi vya wafanyakazi wa kujitolea, asema hivi: “Siku hizi husikii tena wale wanaojitolea wakisema: ‘Niko hapa kwa muda wote ninaohitajika.’ Watu hawataki kujifunga.” Mwandishi Eileen Daspin anakubaliana naye. Baada ya kuhoji wakurugenzi kadhaa wa vikundi vya wafanyakazi wa kujitolea kuhusu upungufu wa watu wanaotaka kujitolea, yeye alikata kauli kwamba “watu huogopa kujifunga, na jambo hilo limeathiri kazi ya kujitolea.”
Hata hivyo, Kathleen Behrens, mkurugenzi wa shirika la New York Cares aliyetajwa mapema katika mfululizo huu wa habari, anahisi kwamba wale wanaojitolea kwa muda mfupi tu, hufanya hivyo, si kwa sababu wanaogopa kujiwekea masharti, bali kwa sababu hawana wakati. Watu wanaofanya kazi ya kuajiriwa kwa muda wa saa 50 kila juma, na pia wana watoto na wazazi wazee wanaohitaji kutunzwa hawawezi kujitolea kwa ukawaida kufanya kazi ya ziada. ‘Hata hivyo, wanafanya utumishi wa jumuiya kuwa sehemu ya maisha yao, licha ya kuwa na shughuli nyingi hivyo. Jambo hilo laonyesha kwamba wanataka sana kujitolea, wala hawaogopi kujifunga,’ Kathleen Behrens asema.
Watu hao wenye shughuli nyingi ‘wanajitolea kulingana na hali,’ Behrens anasema. Siku hizi mashirika mengi ya wafanyakazi wa kujitolea huwaalika watu kufanya kazi kwenye miradi ya siku moja tu. “Jambo hilo huwapa watu fursa ya kujitolea kufanya kazi muhimu bila kujifunga kwa ukawaida.”
Watu wengi hujitolea pia kwa kutumia kompyuta yao nyumbani ili kufanya kazi kama kuingiza habari na tarakimu kwenye kompyuta au kufanya utafiti. Gazeti la The Wall Street Journal lasema hivi: ‘Kujitolea kufanya kazi kwa kutumia kompyuta ni njia moja isiyo ya kawaida ya “kujitolea kulingana na hali,” na baadhi ya watu husema ni njia yenye matokeo mazuri zaidi.’
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]
Kutoa Msaada Huko Kobe!
Tetemeko la ardhi lilipokumba jiji lenye kusitawi la Kobe huko Japani, Januari 1995, lilisababisha uharibifu mkubwa sana. Watu zaidi ya 5,000 walikufa. Hilo lilikuwa tetemeko la ardhi lenye kusababisha vifo vingi zaidi tangu lile lililotukia mwaka wa 1923 huko Japani. Mara moja Mashahidi wa Yehova huko Japani na kotekote ulimwenguni walianza kusaidia walioathiriwa. Katika siku tatu tu dola za Marekani zaidi ya milioni moja zilichangwa. Vitu vingi vya aina yote vilichangwa na kusafirishwa mpaka Kobe.
Mzee mmoja Mkristo aliyeshughulikia kazi ya kutoa msaada alipata kwamba vitu vilivyochangwa kwenye Jumba la Ufalme la kwao vilikuwa vingi mno. Wangefanya nini na vitu hivyo vyote? Alidokeza vichangwe kwa hospitali moja ya karibu. Mashahidi walijaza vifaa hivyo kwenye gari la kubeba mizigo na kuvisafirisha. Safari hiyo ilichukua muda wa saa kadhaa badala ya dakika chache kama kawaida kwa sababu ya vifusi. Walipofika hospitalini walimpa daktari mkuu vitu hivyo vilivyotia ndani mablanketi, magodoro, nepi, matunda, na madawa yasiyohitaji maagizo ya daktari. Daktari alifurahi sana na kuwaambia kwamba wangefurahi sana kupokea chochote kile ambacho Mashahidi wangetoa. Hasa matunda yalithaminiwa sana kwa kuwa hakukuwapo chakula cha kutosha kwa wagonjwa wote.
Mashahidi walipoteremsha vitu hivyo, yule daktari—ijapokuwa alikuwa na kazi nyingi ya kufanya—alisimama kando na kutazama tu. Kisha aliinama kwa unyenyekevu na kuwashukuru. Walipoondoka aliendelea kusimama papo hapo ili kuonyesha uthamini wake. Mzee aliyeshughulikia jambo hili alisema kwamba baadaye madaktari katika hospitali hiyo walikubali kwa utayari zaidi kutibu wagonjwa walio Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
Kazi ya Kujitolea Huleta Faida
Kikundi cha wafanyakazi waliojitolea katika kijiji cha Kabezi cha Burundi walipotaka kujenga Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, ofisa wa sehemu hiyo aliwaomba jambo lisilo la kawaida. Aliwaomba Mashahidi waitengeneze barabara inayopita mahali walipotaka kujenga Jumba la Ufalme. Mashahidi walikubali kwa furaha kutengeneza barabara hiyo iliyoharibika, nao walifanya kazi yote kwa mikono. Wafanyakazi hao waliojitolea waliitengeneza vizuri sana hivi kwamba maofisa wa sehemu hiyo waliwashukuru kwa kazi yao na roho yao ya kujitolea. Baadaye, watu hao waliojitolea walijenga Jumba lao la Ufalme, linaloonekana juu. Sasa wana jumba zuri ambalo litaweza kuwasaidia kwa miaka mingi kuendeleza elimu ya Biblia. Naam, kazi ya kujitolea yaweza kuleta faida kubwa.
[Picha katika ukurasa wa 6, 7]
Sirley huridhika anapowafundisha wengine kusoma
[Hisani]
Nelson P. Duarte-Jornal do Sudoeste
-
-
Kazi ya Kujitolea Yenye Faida ya KudumuAmkeni!—2001 | Julai 22
-
-
Kazi ya Kujitolea Yenye Faida ya Kudumu
YESU KRISTO alikuwa akitenda mema na kusaidia wenye uhitaji kwa ukawaida. Kwa mfano, alilisha wenye njaa na kuponya wagonjwa. (Mathayo 14:14-21) Lakini, alitanguliza kazi gani? Tutapata jibu tukichunguza tukio moja lililotukia mapema katika huduma ya Yesu. Tukio hilo linasimuliwa katika sura ya kwanza ya Injili ya Marko.
Yesu alipokuwa Kapernaumu, karibu na Bahari ya Galilaya, alipelekwa kwenye nyumba ya Simoni, au Petro. “Mama-mkwe wa Simoni alikuwa amelala chini akiwa mgonjwa wa homa,” na Yesu akamponya. (Marko 1:29-31) Baadaye, watu wengi kutia ndani wale “waliokuwa na magonjwa ya namna mbalimbali” walianza kukusanyika mlangoni pa nyumba ya Petro, na Yesu akawaponya pia. (Marko 1:32-34) Kisha usiku ukafika na wote wakalala.
Asubuhi iliyofuata “kulipokuwa bado kuna giza,” Yesu aliamka polepole na kutoka katika nyumba, “akaenda mahali pa upweke, na huko akaanza kusali.” Punde si punde, wanafunzi wakaamka pia, wakachungulia nje, na kuona watu wengi sana waliongoja mlangoni. Lakini wafanye nini? Yesu hakuwapo! Mara moja Petro na wenzake walikwenda kumtafuta Yesu, wakampata na kumwambia hivi: “Wote wanakutafuta wewe.” (Marko 1:35-37; Luka 4:42) Ni kana kwamba walimwambia Yesu hivi: ‘Unafanya nini hapa? Jana usiku ulifanikiwa sana kuponya wagonjwa. Leo una fursa nyingine ya kufanya vivyo hivyo!’
Lakini zingatia maneno ambayo Yesu aliwaambia: “Acheni twende mahali pengine, katika miji ya vijiji iliyo karibu, ili nipate kuhubiri huko pia.” Jibu hilo ni la maana. Yesu hakurudi kwenye nyumba ya Petro ili aponye wengine. Alieleza sababu hakufanya hivyo aliposema hivi: “Kwa sababu kwa ajili ya hili [yaani, kuhubiri] nilitumwa.” (Marko 1:38, 39; Luka 4:43) Yesu alimaanisha nini? Kufanya matendo mema kulikuwa muhimu kwake, lakini kuhubiri na kufundisha neno la Mungu kulikuwa kazi kuu ya Yesu.—Marko 1:14.
Kwa kuwa Biblia yasihi Wakristo ‘wafuate hatua za Yesu kwa ukaribu,’ Wakristo wa kweli wana mwongozo ulio wazi inapohusu kazi ya kujitolea ambayo inapasa kutangulizwa. (1 Petro 2:21) Kama Yesu, wao wanasaidia watu wenye uhitaji—jinsi ilivyosimuliwa hapo awali. Vilevile kama Yesu, wao wanatanguliza kazi ya kufundisha ujumbe wa Biblia juu ya habari njema za Ufalme wa Mungu.a (Mathayo 5:14-16; 24:14; 28:19, 20) Lakini, kwa nini tutangulize kazi ya kufundisha ujumbe wa Biblia mbele ya kazi nyingine muhimu za kujitolea?
Kinachofanya Elimu ya Biblia Iwe Yenye Faida
Mithali moja ya Asia yajibu kwa kusema hivi: “Ukipanga kwa mwaka mmoja, panda mbegu. Ukipanga kwa miaka kumi, panda miti. Ukipanga kwa miaka mia moja, elimisha watu.” Naam, ili kuandaa masuluhisho yenye faida ya kudumu, elimu ni muhimu sana, kwa kuwa inakuza uwezo wa mtu wa kufanya maamuzi yatakayoboresha maisha yake. Kwa hiyo, wafanyakazi wa kujitolea zaidi ya milioni sita hutumia wakati, nguvu, na mali zao kuwafundisha watu Biblia bila malipo. Baadhi yao wanafanya kazi hiyo mara kwa mara na wengine wanaifanya wakati wote. Kazi hiyo ambayo Mashahidi wa Yehova wamefanya kwa miaka mingi inanufaisha jumuiya mbalimbali kotekote duniani. Vipi?
Watu wanaposaidiwa kuelewa na kufuata ushauri wa Biblia, wanaelewa vizuri zaidi jinsi ya kukabiliana na matatizo ya maisha. Wanapata nguvu za maadili zinazohitajika kushinda mazoea mabaya. Nelson, kijana mmoja huko Brazili, anaonyesha faida nyingine ya elimu ya Biblia anaposema hivi: “Tangu nianze kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, nimekuwa na furaha kwa sababu sasa nina kusudi maishani mwangu.” (Mhubiri 12:13) Mamia ya maelfu ya watu—vijana kwa wazee—ambao wameanza kujifunza Neno la Mungu hivi majuzi wana maoni kama ya Nelson. Mbali na kuwasaidia wanafunzi kupata kusudi linaloridhisha maishani, ujumbe juu ya Ufalme wa Mungu huwapa tumaini la wakati ujao lenye kutia moyo—tumaini linalofanya maisha yawe yenye maana, haidhuru hali iwe ngumu kadiri gani. (1 Timotheo 4:8)—Soma sanduku “Faida Ambazo Ufalme wa Mungu Utaleta.”
Wanapofundisha Biblia, Mashahidi wa Yehova wanafanya kazi ya kujitolea yenye faida za kudumu. Zitadumu kwa muda gani? Neno la Mungu lasema hivi: ‘Hii yamaanisha uhai udumuo milele, wao kuendelea kutwaa ujuzi juu yako wewe, Mungu pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Ebu wazia, unaweza kushiriki kazi inayoleta faida za milele—hiyo ndiyo kazi ya kujitolea yenye faida kwelikweli! Je, ungependa kujua zaidi kuhusu kazi hiyo? Ikiwa ndivyo, ongea na Mashahidi wa Yehova wanaoishi katika eneo lenu. Hutajuta kamwe ukiamua kukubali mwaliko huu.
[Maelezo ya Chini]
a Mashahidi wa Yehova huiona kazi yao ya kuhubiri kuwa ya lazima kwa Wakristo wa kweli—kama alivyofanya mtume Paulo. Yeye alisema hivi: “Ikiwa, sasa, ninatangaza habari njema, hiyo si sababu ya mimi kujisifu, kwa maana nimewekewa sharti.” (1 Wakorintho 9:16) Hata hivyo, kazi yao ya kuhubiri ni kazi ya kujitolea kwa sababu wamechagua kwa hiari kuwa wanafunzi wa Kristo, wakijua kabisa madaraka yanayoambatana na pendeleo hilo.
[Blabu katika ukurasa wa 11]
“Ukipanga kwa mwaka mmoja, panda mbegu. Ukipanga kwa miaka kumi, panda miti. Ukipanga kwa miaka mia moja, elimisha watu”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]
Anawapa Msaada na Tumaini
Nadine, mwuguzi Mfaransa mwenye umri wa miaka 43 aliye stadi kutibu magonjwa ya nchi za joto, ni mmojawapo wa wale ambao walikuwa wamejitolea kufanya kazi huko Afrika ya Kati. Alipohojiwa hivi majuzi alisema hivi: ‘Watu huniuliza ni kwa nini ninafanya kazi hii. Ninamwamini Mungu, ninapenda watu, na ninataka kujitolea. Na kwa sababu mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova ninasukumwa kutibu wagonjwa na kuwapa wanaoteseka tumaini.’ Kazi ya kujitolea ya Nadine huku Afrika yatia ndani kutoa misaada na kushiriki kazi ya kufundisha Biblia pamoja na Mashahidi wenyeji.
[Picha]
Nadine akiwa Afrika
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
Faida Ambazo Ufalme wa Mungu Utaleta
Tafadhali soma maandiko haya katika Biblia yako mwenyewe, ukaone jinsi Mungu anavyoahidi kutimiza mahitaji yafuatayo ya wanadamu:
Afya “Atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4; Isaya 33:24; 35:5, 6.
Elimu “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9; Habakuki 2:14.
Kazi “Watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine . . . Hawatajitaabisha kwa kazi bure.”—Isaya 65:21-23.
Chakula “Nchi imetoa mazao yake MUNGU, Mungu wetu, ametubariki.”—Zaburi 67:6; 72:16; Isaya 25:6.
Hali ya Jamii “BWANA amelivunja gongo la wabaya . . . Dunia yote inastarehe na kutulia.”—Isaya 14:5, 7.
Haki “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu.”—Isaya 11:3-5; 32:1, 2.
-