-
Muumba Aweza Kufanya Maisha Yako Yawe na Maana ZaidiMnara wa Mlinzi—1999 | Juni 15
-
-
Muumba Aweza Kufanya Maisha Yako Yawe na Maana Zaidi
“Na vilisifu jina la BWANA, kwa maana aliamuru, vikaumbwa.” —ZABURI 148:5.
1, 2. (a) Twapaswa kufikiria swali gani? (b) Uumbaji wahusikaje katika swali la Isaya?
“JE, HUJAPATA kujua?” Huenda swali hilo likasikika kama swali linalochochea wengi waulize, ‘Kujua nini?’ Lakini hilo ni swali zito. Na twaweza kuelewa jibu lake vizuri zaidi tukijua muktadha wake—sura ya 40 ya kitabu cha Biblia cha Isaya. Isaya, ambaye ni Mwebrania wa kale, ndiye aliyekiandika na kwa hiyo hilo ni swali la kale. Hata hivyo, swali hilo ni la kisasa sana nalo lahusu kiini cha maana ya maisha yako.
2 Kwa kuwa swali lililo katika Isaya 40:28, (NW), ni muhimu sana, linahitaji tulifikirie kwa uzito: “Je, hujapata kujua au hujapata kusikia? Yehova, Muumba wa miisho ya dunia, ni Mungu wa milele.” Basi kule ‘kupata kujua’ kulihusu Muumba wa dunia, na muktadha waonyesha kwamba mbali na dunia kuna mambo mengi zaidi yanayohusika. Katika mistari miwili inayotangulia, Isaya aliandika hivi kuhusu nyota: “Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; . . . kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake.”
3. Hata kama unajua mengi juu ya Muumba, kwa nini inafaa utake kujua zaidi?
3 Basi, lile swali, “Je, hujapata kujua?” hasa lahusu Muumba wa ulimwengu. Huenda wewe binafsi unasadiki kwamba Yehova Mungu ndiye “Muumba wa miisho ya dunia.” Huenda pia unajua mambo mengi kuhusu utu wake na njia zake. Lakini namna gani ukikutana na mwanamume au mwanamke ambaye anatilia shaka kuwapo kwa Muumba, na ambaye kwa wazi hajui jinsi alivyo? Usishangae ukikutana na mtu kama huyo kwa sababu kuna mamilioni ya watu wasiomjua Muumba na wasio na imani katika yeye.—Zaburi 14:1; 53:1.
4. (a) Kwa nini inafaa kufikiria Muumba wakati huu? (b) Sayansi haiwezi kujibu maswali gani?
4 Shule huendelea kutokeza watu wengi wenye kutilia shaka ambao huhisi kwamba sayansi ina majibu (au itapata majibu) ya maswali yanayohusu chanzo cha ulimwengu na uhai. Katika kichapo The Origin of Life (Kilichoitwa kwa Kifaransa Aux Origenes de la Vie), watungaji Hagene na Lenay wataarifu hivi: “Chanzo cha uhai kingali kinajadiliwa katika mwanzo wa karne ya ishirini na moja. Tatizo hili, ambalo ni gumu sana kutatuliwa, lahitaji kufanyiwa utafiti katika nyanja zote, kuanzia anga kubwa ajabu hadi mata ndogo sana isiyoweza kukadiriwa.” Ingawa hivyo, sura ya mwisho, “Swali Bado Lipo,” yakiri hivi: “Tumechunguza majibu fulani ya kisayansi kuhusu swali hili, Ni jinsi gani uhai ulitokea duniani? Lakini sayansi haiwezi kujibu maswali haya, Kwa nini uhai ulitokea? Je, uhai una kusudi? . Hiyo huchunguza tu ‘jinsi’ vitu vilivyotokea. ‘Jinsi’ na ‘kwa nini’ ni maswali mawili yanayotofautiana kabisa. . . . Kuhusu swali la ‘kwa nini,’ ni lazima falsafa, dini, na—zaidi ya yote—kila mmoja wetu atafute jibu.”
Kupata Majibu na Maana
5. Ni watu wa aina gani ambao wanaweza kunufaika hasa kwa kujua mengi kuhusu Muumba?
5 Naam, twataka kuelewa kwa nini kuna uhai—na hasa sababu ya kuwapo kwetu. Na zaidi, twapasa kupendezwa na watu ambao hawajakata kauli juu ya kama kweli Muumba yupo na ambao kwa hakika hawajui njia zake. Au fikiria wale watu ambao malezi yao yamwona Mungu kwa njia tofauti kabisa na vile Biblia inavyotaja. Mabilioni ya watu wamelelewa katika nchi za Mashariki au katika sehemu ambazo watu wengi hawamfikirii Mungu kuwa mtu halisi na mwenye utu wa kupendeza. Kwa maoni yao neno “mungu” huenda likamaanisha kani fulani isiyoeleweka vizuri au kisababishi fulani cha kuwaziwa tu. ‘Hawajapata kumjua Muumba’ au njia zake. Ikiwa wao, au mamilioni ya wengine wenye maoni kama hayo, wangesadiki kwamba kuna Muumba, wangepata thawabu iliyoje, kutia ndani matazamio ya milele! Pia wanaweza kupata kitu ambacho ni nadra sana kupatikana—umaana halisi, kusudi halisi na amani ya akili, maishani.
6. Maisha ya wengi leo yanafananaje na maisha ya Paul Gauguin na mojawapo ya michoro yake?
6 Kwa mfano: Mwaka wa 1891, mchoraji Mfaransa Paul Gauguin alienda kutafuta maisha yenye kuridhisha katika Polinesia ya Ufaransa, iliyokuwa tu kama paradiso. Lakini upesi maisha yake ya zamani ya kuponda raha na anasa yalimletea yeye na wengine maradhi. Alipohisi kwamba alikuwa anakaribia kufa, alichora picha kubwa na kwenye picha hiyo ilionekana alikuwa ‘akionyesha kwamba maisha yalikuwa fumbo kubwa.’ Je, wajua Gauguin aliuitaje mchoro huo? Aliuita “Twatoka Wapi? Sisi Ni Nini? Twaelekea Wapi?” Huenda ikawa umesikia wengine wakiuliza maswali kama hayo. Watu wengi huyauliza. Lakini wasipopata majibu yenye kuridhisha—na kukosa kusudi halisi maishani—wao waweza kufanya nini? Wanaweza kukata kauli ya kwamba maisha yao hayana tofauti na yale ya wanyama.—2 Petro 2:12.a
7, 8. Kwa nini uchunguzi wenyewe wa sayansi hautoshi?
7 Basi unaweza kuelewa sababu inayomfanya mtu kama profesa wa fizikia Freeman Dyson aandike: “Mawazo yangu yanapatana na mawazo ya watu wengi wenye kuheshimika ninapouliza tena maswali ambayo Yobu aliuliza. Kwa nini tunateseka? Kwa nini ulimwengu hauna haki? Ni nini kusudi la maumivu na msiba?” (Ayubu 3:20, 21; 10:2, 18; 21:7) Kama ilivyotajwa, watu wengi hugeukia sayansi ili wapate majibu badala ya kumgeukia Mungu. Wataalamu wa biolojia, wataalamu wa bahari na wengine wanaongeza ujuzi wetu juu ya dunia yetu na uhai uliomo. Wakitafuta majibu kwingineko, wataalamu wa nyota na wa fizikia wanajifunza mengi zaidi kuhusu mfumo wetu wa jua, nyota, na hata makundi ya mbali ya nyota. (Linganisha Mwanzo 11:6.) Mambo hayo yaweza kufikia kauli gani yenye kupatana na akili?
8 Wanasayansi fulani husema juu ya “akili” ya Mungu au “kazi” yake ambayo imefunuliwa katika ulimwengu. Lakini je, wamekosea? Gazeti Science lilisema: “Watafiti wasemapo kwamba ulimwengu wafunua ‘akili’ au ‘kazi’ za Mungu, wao wamsifu Mungu kwa mambo ambayo si muhimu sana ulimwenguni —yaani muundo wake uonekanao.” Hata mtaalamu wa fizikia aliye pia mshindi wa tuzo la Nobeli Steven Weinberg aliandika: “Kadiri ulimwengu uonekanavyo kuwa wenye kueleweka zaidi, ndivyo inavyozidi kuonekana kuwa hatuelewi ni kwa nini ulimwengu upo.”
9. Ni uthibitisho gani uwezao kutusaidia na kuwasaidia wengine wajifunze juu ya Muumba?
9 Lakini bado huenda ikawa wewe ni baadhi ya mamilioni ya watu ambao wamechunguza jambo hilo kwa uzito na ambao wanafahamu kwamba umaana halisi wa maisha wahusisha kumjua Muumba. Kumbuka maneno ambayo mtume Paulo aliandika: “Watu hawawezi kusema kwamba hawajui mambo ya Mungu. Tangu mwanzo wa ulimwengu, watu wanaweza kuona vile Mungu alivyo kupitia vitu ambavyo Yeye amefanya. Hilo laonyesha Uweza wake udumuo milele. Laonyesha kwamba Yeye ni Mungu.” (Waroma 1:20, Holy Bible, New Life Version) Ndiyo, kuna mambo yanayohusu ulimwengu wetu na yanayotuhusu ambayo yanaweza kusaidia watu wamtambue Muumba na kupata umaana kuhusiana naye. Fikiria mambo matatu kuhusu jambo hilo: ulimwengu ambao umetuzunguka, chanzo cha uhai, na uwezo wetu wenyewe wa akili.
Sababu Zinazotufanya Tuamini
10. Kwa nini twapaswa kufikiria kuwapo kwa ‘mwanzo’? (Mwanzo 1:1; Zaburi 111:10)
10 Ulimwengu wetu ulipataje kuwapo? Huenda umejua kutokana na ripoti za darubini za angani na uvumbuzi wa angani kwamba wanasayansi wengi hutambua kwamba ulimwengu wetu haukuwapo wakati wote. Ulikuwa na mwanzo nao unaendelea kupanuka. Hilo laonyesha nini? Ebu msikilize mtaalamu wa nyota Sir Bernard Lovell: “Ikiwa wakati fulani uliopita, Ulimwengu ulikuwa kitu kidogo sana kisichoweza kuwazika na chenye uzito usioweza kuwazika, ni lazima tuulize ni nini kilichokuwapo hapo awali . . . Ni lazima tukabili suala la kuwapo kwa [Mwanzo].”
11. (a) Ulimwengu ni mkubwa kadiri gani? (b) Vipimo sahihi katika ulimwengu vyaonyesha nini?
11 Mfanyizo wa ulimwengu, kutia ndani dunia yetu, waonyesha vipimo sahihi vya kushangaza sana. Kwa mfano, sifa mbili zenye kutokeza za jua letu na nyota nyinginezo ni kwamba hizo ni thabiti na zina uwezo wa kutenda kwa muda mrefu. Kwa sasa inakadiriwa kwamba kuna makundi ya nyota baina ya bilioni 50 (50,000,000,000) na bilioni 125 katika ulimwengu uonekanao. Na kundi letu la nyota liitwalo Kilimia lina mabilioni ya nyota ndani yake. Sasa fikiria: Twajua kwamba injini ya gari huhitaji usawaziko mzuri wa mafuta na hewa. Ikiwa una gari, unaweza kumwomba mekanika anayestahili arekebishe injini yake ili gari lako liende vizuri. Kwa mfano, ikiwa vipimo hivyo vya mafuta na hewa ni muhimu kwa injini tu, vipi jua “lenye kuwaka” kwa njia bora? Kwa wazi, zile kani kuu zinazohusika zimepimwa kwa usahihi kabisa ili uhai uwepo duniani. Je, jambo hilo lilitukia lenyewe tu? Yobu wa kale aliulizwa: “Je, ulizitangaza kanuni zinazoongoza mbingu, au kujua sheria za asili zilizo duniani?” (Ayubu 38: 33, The New English Bible) Hakuna mwanadamu aliyepata kufanya hivyo. Basi ni nani aliyeviweka vipimo hivyo vilivyo sahihi?—Zaburi 19:1.
12. Kwa nini ni jambo linalopatana na akili kufikiri kwamba uumbaji ulianzishwa na Mtu fulani mwenye nguvu na mwenye akili nyingi?
12 Je, yawezekana kwamba vipimo hivyo viliwekwa na kitu fulani au Mtu fulani ambaye hatuwezi kumwona kwa macho ya kibinadamu? Ebu fikiria swali hili kwa kuzingatia sayansi ya kisasa. Wataalamu wengi wa nyota sasa hukubali kwamba kuna magimba ya kimbingu yenye nguvu sana yaitwayo mashimo meusi. Mashimo hayo meusi hayawezi kuonekana, lakini wataalamu wamesadiki kwamba yapo. Kwa kulinganisha, Biblia yaripoti kwamba katika makao mengine mna viumbe wenye nguvu ambao hawawezi kuonekana—viumbe wa roho. Ikiwa kuna viumbe wenye nguvu wasioweza kuonekana, je, si jambo linalopatana na akili kwamba vipimo sahihi vinavyofunuliwa kote katika ulimwengu viliwekwa na Mtu mwenye nguvu na mwenye akili nyingi?—Nehemia 9:6.
13, 14. (a) Sayansi imethibitisha nini hasa juu ya chanzo cha uhai? (b) Kuwapo kwa uhai duniani kwaonyesha nini?
13 Uthibitisho wa pili ambao unaweza kusaidia watu wakubali kwamba kuna Muumba wahusu chanzo cha uhai. Tangu majaribio ya Louis Pasteur, imekubalika kwamba uhai hautokani na kitu kisicho na uhai. Basi uhai wa dunia ulianzaje? Katika miaka ya 1950, wanasayansi walijaribu kuthibitisha kwamba huenda uhai ulianza polepole katika bahari fulani ya awali wakati ambapo anga la awali lilipokuwa likipigwa na radi daima. Lakini, uthibitisho wa karibuni zaidi waonyesha kwamba haiwezekani kuwa uhai duniani ulianza hivyo kwa sababu aina hiyo ya anga haikuwapo kamwe. Kwa hiyo, wanasayansi fulani wanatafuta maelezo ambayo hayana kasoro sana. Lakini, je, hata hao hawajafahamu jambo kuu?
14 Mwanasayansi Mwingereza Sir Fred Hoyle alisema hivi baada ya kuchunguza kwa miongo mingi ulimwengu na uhai uliomo: “Badala ya kukubali uwezekano mdogo kabisa wa kwamba uhai ulitokana na nguvu za asili zisizoongozwa, inaonekana kuwa afadhali kufikiri kwamba uhai ulianzishwa kwa tendo lililopangwa na mtu mwenye akili.” Ndiyo, kadiri tujifunzavyo maajabu ya uhai, ndivyo inavyokuwa wazi kwamba uhai ulitokana na Chanzo chenye akili.—Ayubu 33:4; Zaburi 8:3, 4; 36:9; Matendo 17:28.
15. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba wewe ni mtu wa kipekee?
15 Basi jambo la kwanza lahusu ulimwengu, na la pili, chanzo cha uhai duniani. Sasa ona jambo la tatu—hali yetu ya kipekee. Wanadamu wote ni wa kipekee kwa njia nyingi, kumaanisha kwamba hata wewe ni wa kipekee. Kwa jinsi gani? Labda umesikia ubongo ukilinganishwa na kompyuta yenye nguvu. Lakini, kwa kweli mambo yaliyogunduliwa karibuni yaonyesha kwamba haifai hata kidogo kufanya ulinganishi huo. Mwanasayansi mmoja katika Taasisi ya Tekinolojia ya Massachusetts alisema: “Kompyuta za leo hata hazifikii mwanadamu mwenye umri wa miaka 4 kwa uwezo wa kuona, kuzungumza, kusonga, au kutumia akili. . . . Imekadiriwa kwamba uwezo wa kuchanganua habari wa hata kompyuta yenye nguvu zaidi unatoshana na uwezo wa mfumo wa neva wa konokono—sehemu kidogo sana ya uwezo wa kompyuta bora zaidi iliyo katika kichwa [chako].”
16. Uwezo wako wa kufahamu lugha waonyesha nini?
16 Lugha ni mojawapo ya uwezo ulio nao kwa sababu ya ubongo wako. Ingawa watu fulani husema lugha mbili, tatu, au zaidi, uwezo wa kusema hata lugha moja watufanya tuwe wa kipekee. (Isaya 36:11; Matendo 21:37-40) Maprofesa R. S. na D. H. Fouts waliuliza: “Je, ni mwanadamu tu . . . aliye na uwezo wa kuwasiliana kwa lugha? . . . Wanyama wote wa hali ya juu huwasiliana kwa . . . ishara, harufu, miito, milio na nyimbo, na hata kucheza dansi kama vile nyuki. Lakini inaonekana kwamba mbali na mwanadamu, wanyama hawana lugha yenye kufuata sarufi. Na jambo ambalo huenda likawa muhimu zaidi ni kwamba wanyama hawachori picha za kuwakilisha mambo wanayotaka kuwasilisha. Hawawezi kufanya chochote zaidi ya kuchora tu vitu visivyo na maana.” Kwa kweli, ni wanadamu tu wawezao kutumia ubongo kusema lugha na kuchora picha zenye maana.—Linganisha Isaya 8:1; 30:8; Luka 1:3.
17. Kuna tofauti gani ya msingi kati ya mnyama atazamaye kwenye kioo na binadamu atazamaye kwenye kioo?
17 Isitoshe, unajifahamu; unajitambua. (Mithali 14:10) Je, umepata kutazama ndege, mbwa, au paka akitazama kioo kisha agogota, anguruma, au kukishambulia? Yeye hufikiri ameona mnyama mwingine, hajitambui. Kwa kutofautisha, utazamapo kioo, unajua ya kwamba ni wewe unayejiona. (Yakobo 1:23, 24) Huenda ukachunguza sura yako au ukajiuliza utafananaje miaka michache ijayo. Wanyama hawafanyi hivyo. Ndiyo, ubongo wako wakufanya uwe wa kipekee. Ni nani astahiliye kupata sifa? Ubongo wako ulipataje kuwapo, kama haukutokana na Mungu?
18. Ni uwezo gani wa akili unaokufanya uwe tofauti na wanyama?
18 Ubongo wako pia hukufanya uthamini sanaa na muziki na vilevile kuwa na maadili. (Kutoka 15:20; Waamuzi 11:34; 1 Wafalme 6:1, 29-35; Mathayo 11:16, 17) Kwa nini iwe ni wewe na si wanyama? Wanyama hutumia ubongo hasa kwa kushughulikia mahitaji yao ya sasa—kupata chakula, kupata mwenzi, au kufanyiza kiota. Ni wanadamu pekee hufikiria zaidi ya mambo ya sasa tu. Watu wengine hata hufikiria jinsi matendo yao yatakavyoathiri mazingira au kuathiri wazao wao miaka mingi baadaye. Kwa nini? Andiko la Mhubiri 3:11 lasema hivi juu ya wanadamu: “[Muumba] ameiweka hiyo milele ndani ya mioyo yao.” Ndiyo, uwezo wako wa kufikiria umaana wa umilele au wa kuwazia uhai wa milele ni wa kipekee sana.
Muumba na Aongeze Umaana
19. Ni njia ipi ya kusababu yenye sehemu tatu ambayo unaweza kutumia kuwasaidia wengine wafikirie Muumba?
19 Tumetaja maeneo matatu tu: vipimo sahihi vinavyoonekana katika ulimwengu mkubwa, chanzo cha uhai duniani, na hali isiyotilika shaka ya upekee wa ubongo wa binadamu pamoja na uwezo wake mbalimbali. Mambo hayo matatu yanaonyesha nini? Hapa pana njia moja ya kusababu ambayo unaweza kutumia unapowasaidia wengine wafikie uamuzi. Kwanza unaweza kuuliza: Je, ulimwengu ulikuwa na mwanzo? Wengi watakubali. Kisha uliza: Je, mwanzo huo ulitokea wenyewe tu, au ulitokezwa? Watu wengi hutambua kwamba mwanzo wa ulimwengu ulitokezwa. Hilo latokeza swali la mwisho: Je, mwanzo huo ulitokezwa na kitu fulani cha milele au na Mtu fulani wa milele? Hoja zikitolewa kwa njia hiyo ya wazi na yenye kupatana na akili, wengi waweza kusaidiwa wafikie uamuzi huu: Ni lazima iwe kuna Muumba! Basi, je, si inawezekana kwamba maisha yana maana?
20, 21. Kwa nini kumjua Muumba ni muhimu ili maisha yetu yawe na maana?
20 Kuwapo kwetu, kutia ndani maadili yetu na maadili yenyewe yapaswa kuhusianishwa na Muumba. Pindi moja Dakt. Rollo May aliandika hivi: “Mfumo wa pekee unaofaa wa maadili ni ule unaotegemea umaana wa msingi wa maisha.” Huo unapatikana wapi? Aliendelea kusema: “Mfumo huo wa msingi ndio utu wa Mungu. Kanuni za Mungu ndizo kanuni zinazoongoza maisha tangu mwanzo wa uumbaji hadi mwisho.”
21 Basi, twaweza kuelewa ni kwa nini mtunga-zaburi alikuwa akionyesha unyenyekevu na hekima alipomwomba Muumba hivi: “Ee BWANA, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako, uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha. Maana wewe ndiwe Mungu wa wokovu wangu.” (Zaburi 25:4, 5) Kadiri alivyopata kumjua Muumba vizuri, ndivyo kwa hakika maisha ya mtunga-zaburi yangepata umaana, kusudi, na mwelekezo zaidi. Ndivyo inavyoweza kuwa kwa kila mmoja wetu.—Kutoka 33:13.
22. Ni nini kinachohusika katika kupata kujua njia za Muumba?
22 Kupata kujua ‘njia za’ Muumba kwahusisha kujua vizuri zaidi jinsi alivyo, utu wake na njia zake. Lakini kwa kuwa Muumba haonekani naye ana nguvu nyingi sana, tunawezaje kumjua vizuri? Makala ifuatayo itazungumzia jambo hili.
[Maelezo ya Chini]
a Akirejezea mambo yaliyompata katika kambi za mateso za Nazi, Dakt. Viktor E. Frankl alitambua hivi: “Hali ya binadamu ya kutafuta maana ni nguvu ya msingi katika maisha yake wala si ‘kufikiri tu’ kunakoongozwa na silika,” kama wanyama. Pia alisema kwamba miaka mingi baada ya vita ya pili ya ulimwengu, uchunguzi uliofanywa nchini Ufaransa “ulionyesha kuwa asilimia 89 ya watu waliohojiwa walikubali kwamba binadamu ahitaji ‘kitu’ cha kumpa kusudi maishani.”
-
-
Muumba Wako—Jifunze Jinsi AlivyoMnara wa Mlinzi—1999 | Juni 15
-
-
Muumba Wako—Jifunze Jinsi Alivyo
“Nitapitisha wema wangu wote mbele yako, nami nitalitangaza jina la BWANA mbele yako.”—KUTOKA 33:19.
1. Kwa nini Muumba astahili kuheshimiwa?
MTUME Yohana, aliyeandika kitabu cha mwisho cha Biblia, alirekodi tangazo hili kuu kuhusu Muumba: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.” (Ufunuo 4:11) Kama makala iliyotangulia ilivyoonyesha, magunduzi ya sayansi ya kisasa mara nyingi huongezea sababu za kuamini kuwepo kwa Muumba wa vitu vyote.
2, 3. (a) Watu wanahitaji nini ili kujifunza juu ya Muumba? (b) Kwa nini si jambo linalopatana na akili kukutana na Muumba binafsi?
2 Japo ni muhimu kukubali kwamba kuna Muumba, ni muhimu vilevile kujifunza jinsi alivyo—kwamba yeye ni mtu halisi, mwenye utu na njia ambazo zinavuta watu kwake. Kwa kadiri ambavyo umefanya hivyo, je, halingenufaisha kupata kumjua zaidi? Hilo halimaanishi kwamba ukutane na yeye binafsi, kwa jinsi ambavyo binadamu hukutana.
3 Yehova ndiye Chanzo cha hata nyota, jua letu likiwa tu nyota yenye ukubwa wa kadiri. Je, ungewazia kujaribu kukaribia jua? Hata kidogo! Watu wengi hata hawataki kulitazama tu kifupi au hata kukaa kwenye mwangaza wake wenye nguvu kwa muda mrefu bila kujifunika. Kiini chake kina joto lipatalo digrii 15,000,000 Selsiasi. Kwa kila sekunde, tanuri hiyo yenye kutokeza nguvu za nyuklia hugeuza tani milioni nne za masi kuwa nishati. Ni sehemu kidogo tu ya nishati hiyo inayofikia dunia ikiwa joto na nuru, lakini kiasi hicho kinadumisha viumbe vyote duniani. Mambo hayo ya msingi yapasa kutustaajabisha juu ya nguvu nyingi sana za Muumba. Kwa kufaa Isaya angeweza kuandika kuhusu ‘ukuu wa uweza wa Muumba, na kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake.’—Isaya 40:26.
4. Musa aliomba nini, na Yehova aliitikiaje?
4 Lakini, je, ulijua kwamba miezi kadhaa baada ya Waisraeli kuondoka Misri mwaka wa 1513 K.W.K., Musa alimwomba Muumba hivi: “Nakusihi unionyeshe utukufu wako.” (Kutoka 33:18) Ukikumbuka kwamba Mungu ndiye Chanzo cha hata jua, unaweza kuelewa ni kwa nini alimwambia Musa: “Huwezi kuniona uso wangu, maana mwanadamu hataniona akaishi.” Muumba alimruhusu Musa ajifiche mahali fulani kwenye Mlima Sinai Alipokuwa ‘akipita.’ Kisha Musa akaona “nyuma” ya Mungu, kitamathali, yaani mng’ao fulani uliobaki wa utukufu wa Muumba, au kuwapo kwake.—Kutoka 33:20-23; Yohana 1:18.
5. Muumba aliridhisha ombi la Musa kwa njia gani, akithibitisha nini?
5 Tamaa ya Musa ya kutaka kumjua Muumba vizuri iliridhishwa. Kwa wazi akisema kupitia malaika, Mungu alipita karibu na Musa na kutangaza: “BWANA, Mungu mwingi wa huruma, mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema na kweli; mwenye kuwaonea huruma watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.” (Kutoka 34:6, 7) Jambo hilo laonyesha kwamba kupata kumjua Muumba vizuri zaidi hakuhusishi kutazama umbo lake halisi bali kufahamu zaidi jinsi alivyo, utu wake na sifa zake.
6. Mfumo wetu wa kinga wastaajabisha kwa njia gani?
6 Njia moja tunayoweza kumfahamu Mungu ni kwa kutambua sifa zake kutokana na uumbaji wake. Fikiria mfumo wako wa kinga ya mwili. Toleo moja la Scientific American lililohusu mfumo wa kinga lilisema hivi: “Tokea wakati wa kabla ya kuzaliwa hadi kifo, mfumo wa kinga huwa chonjo nyakati zote. Molekuli na chembe nyingi tofauti-tofauti . . . hutukinga dhidi ya vimelea na viini. Bila kinga hizo, wanadamu hawawezi kuishi.” Mfumo huo ulianzaje? Makala moja katika gazeti hilo ilisema hivi: “Chembe nyingi tofauti-tofauti zinazoshirikiana kwa ustadi sana, ambazo hukinga mwili dhidi ya mashambulizi ya viini na virusi, hutokana na chembe za awali ambazo hutokea majuma tisa hivi baada ya mimba kutungwa.” Mwanamke aliye mja-mzito hupitishia kijusu chake kinachokua mfumo fulani wa kinga. Baadaye, kupitia maziwa ya matiti, yeye pia huandalia mtoto wake chembe za kinga na kemikali zenye manufaa.
7. Tunaweza kufikiria nini kuhusu mfumo wetu wa kinga, jambo linalotufanya tufikie uamuzi gani?
7 Kuna sababu nzuri ya kufikia uamuzi wa kwamba mfumo wako wa kinga unashinda kitu kingine chochote ambacho tiba ya kisasa inaweza kuandaa. Basi, jiulize, ‘Jambo hilo ladokeza nini juu ya Mwanzilishi na Mwandaaji wa mfumo huo?’ Mfumo huo, ambao ‘hutokea kwa mara ya kwanza majuma tisa hivi baada ya mimba kutungwa’ na ambao upo tayari kulinda mtoto ambaye ametoka kuzaliwa, kwa kweli waonyesha hekima na hali ya kufikiria kimbele. Lakini je, tunaweza kujifunza hata mengi zaidi kuhusu Muumba kutokana na mfumo huu wa kinga? Wengi wetu hukata kauli gani kuhusu Albert Schweitzer na wengine ambao walitoa maisha zao ili wawatibu maskini? Kwa kawaida watu kama hao wenye huruma nyororo ya kusaidia wenye uhitaji huonwa kuwa wema. Kwa kulinganisha, twaweza kukata kauli gani juu ya Muumba, ambaye amewapa matajiri kwa maskini mfumo wa kinga? Ni wazi kwamba yeye ni mwenye upendo, asiye na ubaguzi, mwenye huruma nyororo, na mwenye haki. Je, jambo hilo halipatani na ufafanuzi wa Muumba ambao Musa alisikia?
Ajifunua Jinsi Alivyo
8. Yehova hujifunua kwetu kwa njia gani ya kipekee?
8 Lakini, kuna njia nyingine ya kupata kumjua Muumba wetu vizuri zaidi—kupitia Biblia. Hilo ni jambo muhimu hasa kwa sababu kuna mambo yanayomhusu ambayo wala sayansi wala ulimwengu hauwezi kamwe kufunua na mambo mengine yaliyo wazi sana katika Biblia. Mfano mmoja wa jambo ambalo wala sayansi wala ulimwengu hauwezi kufunua ni jina binafsi la Muumba. Ni Biblia tu inayotaja jina la Muumba na umaana wa jina hilo. Katika hati-kunjo za Kiebrania za Biblia, jina lake latokea mara 7,000 hivi likiwa limeandikwa kwa konsonanti nne ambazo zaweza kuandikwa YHWH au JHVH, nalo kwa kawaida hutamkwa Yehova kwa Kiswahili.—Kutoka 3:15; 6:3.
9. Jina binafsi la Muumba linamaanisha nini, na tunaweza kufikia uamuzi gani juu ya jambo hili?
9 Ili tumjue Muumba vizuri, twahitaji kutambua kwamba yeye si “Kianzilishi tu cha Kwanza” wala “MIMI NIKO” asiyeeleweka. Jina lake binafsi laonyesha jambo hilo. Jina hilo ni namna ya kitenzi cha Kiebrania kinachomaanisha “kuwa” au “thibitika kuwa.”a (Linganisha Mwanzo 27:29; Mhubiri 11:3, NW.) Jina la Mungu lamaanisha “Yeye Husababisha Iwe” nalo lakazia kwamba yeye hukusudia na kuchukua hatua. Kwa kujua jina hilo na kulitumia, tunaweza kufahamu vema zaidi kwamba yeye hutimiza ahadi zake na kutekeleza makusudi yake.
10. Tunaweza kupata ufahamu gani muhimu katika rekodi ya kitabu cha Mwanzo?
10 Biblia ndiyo iwezayo kutoa ujuzi juu ya makusudi na utu wa Mungu. Rekodi ya kitabu cha Mwanzo yafunua kwamba pindi moja wanadamu walikuwa na amani na Mungu, nao walikuwa na tazamio la maisha marefu yenye umaana. (Mwanzo 1:28; 2:7-9) Kwa kupatana na umaana wa jina lake, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atamaliza kuteseka na mfadhaiko ambao wanadamu wamekabili kwa muda mrefu. Twasoma hivi juu ya kutimiza kusudi lake: “Ulimwengu halisi ulifadhaishwa, si kwa tamaa yake, bali kwa mapenzi ya Muumba, ambaye kwa kuufanya hivyo, aliupa tumaini ya kwamba huenda siku moja upate . . . kufanywa ushiriki uhuru mtakatifu wa watoto wa Mungu.” —Waroma 8:20, 21, The New Testament Letters, cha J. W. C. Wand.
11. Kwa nini tunaweza kufikiria masimulizi ya Biblia, na mojawapo ya masimulizi hayo yana mambo gani?
11 Biblia inaweza kutusaidia pia kumjua Muumba vizuri zaidi kwa sababu inafunua matendo yake alipokuwa akishughulika na Israeli la kale. Fikiria mfano unaohusu Elisha na Naamani, aliyekuwa mkuu wa jeshi la Wasiria wenye uhasama. Usomapo simulizi hilo kwenye 2 Wafalme sura ya 5, utaona kwamba msichana Mwisraeli aliyetekwa alisisitiza kwamba Naamani angeweza kuponywa ukoma wake kwa msaada wa Elisha katika Israeli. Naamani alienda huko akidhani kwamba Elisha atapunga mikono kwa kufuatia mafumbo fulani ya kuponesha. Badala yake, Elisha alimwambia Msiria huyo akaoge ndani ya Mto Yordani. Ingawa ilibidi watumishi wa Naamani wamsadikishe akubali kufanya hivyo, alipooga aliponywa. Naamani alitoa zawadi zenye thamani, naye Elisha akazikataa. Baadaye mshiriki mmoja wa Elisha akamwendea Naamani kisirisiri na kwa kutumia udanganyifu akapata baadhi ya zawadi hizo zenye thamani. Akapigwa kwa ukoma kwa sababu ya kutofuatia haki. Hili ni simulizi lenye kuvutia la kuonyesha hali ya kibinadamu, ambalo linaweza kutufundisha.
12. Tunaweza kufikia uamuzi gani kuhusu Muumba katika simulizi la Elisha na Naamani?
12 Kwa njia yenye kuvutia, simulizi hilo laonyesha kwamba Muumba Mtukufu wa ulimwengu hakujiona kuwa wa maana sana asiweze kumpendelea msichana mdogo, sifa iliyo tofauti kabisa na desturi za tamaduni nyingi leo. Pia linathibitisha kwamba Muumba haonyeshi upendeleo kwa jamii moja au taifa moja. (Matendo 10:34, 35) Kwa kupendeza, badala ya kutarajia watu watumie ujanja—ambalo ni jambo la kawaida kwa “waponyaji” fulani wa wakati uliopita na wa sasa—Muumba alionyesha hekima ya ajabu sana. Alijua namna ya kuponya ukoma. Pia alionyesha ufahamu na haki kwa kutoruhusu udanganyifu wowote ufaulu. Je, jambo hili vilevile halipatani na utu wa Yehova ambao Musa alisikia? Japo simulizi hilo la Biblia ni fupi, tunaweza kuona kwa kadiri kubwa kama nini jinsi Muumba alivyo!—Zaburi 33:5; 37:28.
13. Toa kielelezo cha jinsi tuwezavyo kupata masomo muhimu katika masimulizi ya Biblia.
13 Masimulizi mengine kuhusu matendo ya Waisraeli yasiyoonyesha shukrani na jinsi Mungu alivyotenda yanathibitisha kwamba kwa kweli Yehova anajali. Biblia yasema kwamba Waisraeli walimjaribu Yehova tena na tena, wakimhuzunisha na kumtia uchungu. (Zaburi 78:40, 41) Kwa hiyo, Muumba ana hisia, naye anajali kile ambacho wanadamu wanafanya. Pia kuna mengi ya kujifunza katika masimulizi ya watu mmoja-mmoja walio mashuhuri. Daudi alipochaguliwa kuwa mfalme wa Israeli, Mungu alimwambia Samweli: “Wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Ndiyo, Muumba hutazama jinsi tulivyo kwa ndani, si sura tu ya nje. Jambo hilo laridhisha kama nini!
14. Tusomapo Maandiko ya Kiebrania, tunaweza kunufaika kwa kufanya nini?
14 Vitabu 39 vya Biblia viliandikwa kabla ya wakati wa Yesu, na yafaa tuvisome. Kusudi halipasi kuwa kujifunza tu masimulizi ya Biblia au historia. Kama kweli tunataka kujifunza jinsi Muumba wetu alivyo, tunapaswa kutafakari masimulizi hayo, labda kwa kufikiria, ‘Tukio hili lafunua nini kuhusu utu wake? Ni sifa zake zipi zinazodhihirika hapa?’b Kufanya hivyo kwaweza hata kuwasaidia wenye kutilia shaka waone kwamba ni lazima Biblia iwe imetokana na Mungu, jambo ambalo linawawekea msingi wa kupata kumjua Mtungaji wake mwenye upendo vizuri zaidi.
Mwalimu Mkuu Atusaidia Kumjua Muumba
15. Kwa nini matendo ya Yesu na mafundisho yake yawe yenye kufundisha?
15 Ni kweli kwamba watu ambao hutilia shaka kuwapo kwa Muumba au ambao humwona Mungu kuwa kitu kisicho dhahiri huenda wakawa hawaijui Biblia vizuri. Labda umekutana na watu ambao hawajui kama Musa aliishi kabla ya Mathayo au baada yake na ambao hawajui matendo na mafundisho ya Yesu. Jambo hilo lahuzunisha sana kwa sababu mtu aweza kujifunza mengi sana kuhusu Muumba kutokana na Mwalimu Mkuu, Yesu. Kwa kuwa alikuwa na uhusiano wa karibu na Mungu, yeye angeweza kufunua jinsi Muumba wetu alivyo. (Yohana 1:18; 2 Wakorintho 4:6; Waebrania 1:3) Naye alifanya hivyo. Hata pindi moja alisema: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yohana 14:9.
16. Mazungumzo ya Yesu pamoja na mwanamke Msamaria yatoa kielelezo cha nini?
16 Fikiria mfano huu. Pindi moja Yesu alipokuwa amechoka kwa sababu ya kusafiri, aliongea na mwanamke Msamaria karibu na Sikari. Alimweleza kweli za ndani, akikazia uhitaji wa ‘kumwabudu Baba kwa roho na kweli.’ Wayahudi wa wakati huo waliepukana na Wasamaria. Tofauti na hivyo, Yesu alionyesha utayari wa Yehova wa kukubali wanaume na wanawake wenye mioyo myeupe wa mataifa yote, kama tulivyoona katika kisa cha Elisha na Naamani. Tunapaswa kufarijika kwamba Yehova hana uhasama wa kishupavu wa kidini ambao umejaa ulimwenguni leo. Pia twaweza kuona kwamba Yesu alikuwa tayari kumfundisha mwanamke, na katika kisa hiki mwanamke aliyekuwa akiishi na mwanamume asiye mume wake. Badala ya kumshutumu, Yesu alimtendea kwa adhama, kwa njia ambayo kwa kweli ingeweza kumsaidia. Baadaye, Wasamaria wengine walimsikiliza Yesu na kukata kauli hivi: “Twajua kwamba mtu huyu kwa hakika ndiye mwokozi wa ulimwengu.”—Yohana 4:2-30, 39-42; 1 Wafalme 8:41-43; Mathayo 9:10-13.
17. Simulizi la ufufuo wa Lazaro laonyesha nini?
17 Ebu tufikirie kielelezo kingine cha jinsi tunavyoweza kujifunza kuhusu Muumba kwa kufahamu matendo na mafundisho ya Yesu. Fikiria pindi ile ambapo rafiki ya Yesu, Lazaro, alipokufa. Awali Yesu alikuwa amethibitisha uwezo wake wa kuwafufua wafu. (Luka 7:11-17; 8:40-56) Lakini, alitendaje alipomwona dada ya Lazaro, Maria, akiomboleza? Yesu “akapiga kite katika roho na kuwa mwenye kutaabika.” Yeye alijali na hakujitenga; “akatokwa na machozi.” (Yohana 11:33-35) Na hilo halikuwa wonyesho tu wa hisia. Yesu alisukumwa kuchukua hatua nzuri—akamfufua Lazaro. Unaweza kuwazia jinsi jambo hilo lilivyowasaidia mitume wafahamu hisia na matendo ya Muumba. Linapasa kutusaidia na kusaidia wengine pia kuelewa utu wa Muumba na njia zake.
18. Watu wanapaswa kuhisije juu ya kujifunza Biblia?
18 Hakuna sababu ya kuaibika kusoma Biblia na kujifunza zaidi kuhusu Muumba wetu. Biblia si kitabu kisichotumika. Yohana aliisoma akawa mshiriki wa karibu wa Yesu. Baadaye aliandika: “Twajua kwamba Mwana wa Mungu amekuja, na yeye ametupa sisi uwezo wa akili ili tupate ujuzi juu ya aliye wa kweli. Na sisi tumo katika muungano na aliye wa kweli, kwa njia ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli na uhai udumuo milele.” (1 Yohana 5:20) Ona kwamba kutumia “uwezo wa akili” ili kupata ujuzi wa “aliye wa kweli,” Muumba, kwaweza kutuongoza kwenye “uhai udumuo milele.”
Unaweza Kuwasaidiaje Wengine Wajifunze Kumhusu?
19. Ni hatua zipi ambazo zimechukuliwa ili kuwasaidia watu wenye kutilia shaka?
19 Watu wengine wanahitaji kujua mengi zaidi ndipo waamini kwamba kuna Muumba mwenye huruma anayetujali ndipo watambue jinsi alivyo. Kuna mamilioni ya watu ambao bado wanatilia shaka kuhusu Muumba au ambao maoni yao juu yake hayapatani na yale yanayopatikana katika Biblia. Unaweza kuwasaidiaje? Kwenye mikusanyiko ya wilaya na ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova iliyofanywa katika kipindi cha 1998/1999, chombo kipya chenye kufaa kilitolewa katika lugha nyingi—kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?
20, 21. (a) Kitabu cha Muumba kinaweza kutumiwaje kwa mafanikio? (b) Simulia mambo yaliyoonwa ya jinsi ambavyo kitabu Muumba tayari kimethibitika kuwa chenye matokeo.
20 Hicho ni kichapo ambacho kitaimarisha imani yako mwenyewe juu ya Muumba wetu na uthamini wako juu ya utu wake na njia zake. Kwa nini hili ni jambo la hakika? Kwa sababu kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? kimetayarishwa hasa kwa malengo hayo. Jambo kuu linalokaziwa katika kitabu hicho chote ni “Ni Nini Kinachoweza Kufanya Maisha Yako Yawe na Maana Zaidi?” Habari hii imeandaliwa kwa njia ya kwamba hata watu wenye elimu nyingi sana watapata ikiwa yenye kuvutia. Lakini, habari hiyo inagusia tamaa ambazo sisi sote tunazo. Kuna habari zenye kuvutia na zenye kushawishi wasomaji wanaotilia shaka kuwapo kwa Muumba. Kitabu hicho hakichukulii kwamba msomaji anaamini kuna Muumba. Wenye kutilia shaka kuhusu kuwapo kwa Muumba watavutiwa na uvumbuzi na hoja za kisayansi za karibuni. Mambo hayo yataimarisha pia imani ya wale wanaoamini Mungu.
21 Unapojifunza kitabu hiki kipya, itaonekana kwamba sehemu zake zinatoa pitio la historia ya Biblia kwa njia inayokazia sehemu mbalimbali za utu wa Mungu, kikisaidia wasomaji wamjue Mungu vizuri zaidi. Wengi ambao tayari wamekisoma wameeleza jinsi ambavyo wameona ukweli wa jambo hilo. (Ona makala ifuatayo, ukurasa wa 25-26.) Na iwe hivyo kwako pia unapokisoma kitabu hicho na kukitumia kuwasaidia wengine kupata kumjua Muumba wao vizuri zaidi.
[Maelezo ya Chini]
a Alipokuwa mhariri mkuu wa The Catholic Biblical Quarterly, msomi mmoja Myesuiti M. J. Gruenthaner alisema kwamba kitenzi hiki kinahusishwa na maneno yanayohusu kitenzi kinachofanana nacho, ya kwamba “hakidokezi kamwe wazo la kuwapo kwa njia ya kuwaziwa tu bali sikuzote kitenzi hicho humaanisha kuwapo halisi au kufahamiwa, yaani kujidhihirisha kwa njia thabiti.”
b Wazazi wasimuliapo watoto wao masimulizi ya Biblia, wao waweza kuwasaidia kwa kutokeza maswali kama hayo. Kwa njia hiyo vijana wanaweza kumfahamu Mungu, na vilevile kujifunza kutafakari Neno lake.
-